“Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”
1-4. (a) Wewe ungefurahia kushiriki sehemu gani za picha ya jalada letu? (b) Unatolewa hapa taraja gani lenye utukufu? (c) Ni maandiko gani machache ya Biblia yanayothibitisha tumaini hilo?
ONA watu wenye furaha juu ya jalada la broshua hii. Je! wewe, ungependa kuwa mmoja wao? ‘Ndiyo,’ unasema. Kwa maana hapa pana amani na upatano ambao wanadamu wote wanatamani. Watu wa jamii zote—weusi, weupe, wa kimanjano—wote wanachanganyika kama jamaa moja. Loo! furaha! Loo! umoja! Bila shaka watu hawa hawahangaishwi na makombora ya nyukilia wala na ogofyo la kiharamia. Ndege za kivita haziharibu anga zenye utulivu zilizo juu ya bustani hii nzuri. Hakuna askari wa vita, hakuna vifaru, hakuna bunduki. Wala virungu vya polisi havihitajiwi kutumiwa ili kutunza utaratibu. Vita na uvunjaji wa sheria hakuna. Na wala hakuna upungufu wa nyumba, kwa sababu kila mtu ana makao yake mwenyewe yaliyo mazuri.
2 Ebu waangalie watoto hao! Ni furaha kutazama wanavyocheza. Loo! kuna wanyama wa kucheza nao! Hakuna haja ya pao za vyuma katika bustani hii, kwa sababu wanyama wote wanakaa kwa amani na wanadamu na hata kati yao wenyewe. Hata simba na mwana-kondoo wamekuwa marafiki. Tazama wale ndege wenye rangi nzuri wakiruka huku na huku, tena sikia nyimbo zao nzuri zinapoungana na vicheko vya watoto kuijaa hewa. Ala! Hakuna vizimba (matundu)? Hakuna, kwa sababu ni uhuru kwa wote na furaha isiyozuiliwa katika makao haya. Ebu sikia manukato ya maua yale. Sikiliza mlio wa kijito. Sikia msisimuko wa joto la jua. Lo! mwonjo wa matunda katika kapu lile, maana ndiyo matunda bora ambayo nchi yaweza kuzaa, yaliyo bora sana sana, kama vitu vyote vinavyoweza kuonekana na kufurahiwa katika sehemu hii iliyo kama bustani.
3 ‘Lakini, ebu ngoja,’ mtu fulani asema, ‘wazee wako wapi? Je! hawapaswi kushiriki shangwe ya watu hawa wenye furaha?’ Kwa hakika wazee wapo apo hapo, lakini wanageuka kuwa vijana. Katika bustani hii hakuna mtu anayekufa kwa uzee. Sasa vijana wanakuwa watu wazima lakini hawazeeki. Hata kwamba, umri wao ni miaka 20 au miaka 200 kila mmoja wa mamilioni ya watu wanaoishi katika bustani hii anafurahia hali ya maisha yake ya ujana, akiwa na afya kamilifu. Mamilioni, unasema? Ndiyo, mamilioni, kwa maana bustani hii inapanuka kufika kila nchi. Itajawa na uhai, amani, na uzuri mpaka miisho yenyewe ya dunia yetu, kutoka Fuji mpaka Andes, kutoka Hong Kong mpaka Bahari ya Mediterania. Kwa maana dunia yote inageuzwa kuwa bustani ya paradiso. Itakuwa paradiso itakayorudishwa ulimwenguni pote.
4 ‘Haisadikiki,’ ukasema? Kwanza, ingawaje, fikiria mambo ya hakika yanayothibitisha. Inawezekana kwako wewe pamoja na jamaa yako kuokolewa wakati wa kupita huu mfumo wa mambo wenye taabu na kuingia katika Paradiso inayofananishwa katika jalada letu.a
Kitabu Kinachoeleza Paradiso
5. (a) Ni kitabu gani kinachoeleza mambo hayo? (b) Ni kitabu chenye kutokeza kwa njia zipi?
5 Mambo yote hayo ya utukufu, na uhakika wayo yanaelezwa katika kitabu, kitabu cha ajabu kabisa kilichopata kuandikwa. Kinaitwa Biblia. Ni kitabu cha kale sana, sehemu zacho ziliandikwa miaka kama 3,500 iliyopita. Kwa wakati ule ule hicho ndicho kitabu cha kisasa sana kwa kueleza mambo yanayohusu maisha ya siku hizi. Unabii wacho unaamsha tumaini zuri kwa wakati ujao. Katika historia yote, kimekuwa ndicho kitabu chenye kuuzwa zaidi sana. Nakala za Biblia nzima au sehemu zayo kubwa-kubwa zaidi ya 2,000,000,000 zimeenezwa katika lugha fulani fulani 1,810.
6. Ni nini kinachoitofautisha Biblia na maandishi mengine yanayoonwa kuwa matakatifu?
6 Hakuna kitabu kitakatifu ambacho kimepata kuenezwa sana mahali pote kama hicho, na karibu vingine vyote havina umri ulio karibu nacho. Korani ya Waislamu ina umri mdogo kuliko miaka 1,400. Buddha na Konfusho waliishi miaka kama 2,500 iliyopita, na tarehe ya maandishi yao inaanza wakati huo. Maandishi ya Shinto yalikusanywa katika umbo layo miaka 1,200 iliyopita. Kitabu cha Mormon kina umri wa miaka 160 tu. Hakuna hata kimoja cha vitabu hivyo vitakatifu kiwezacho kufuatia historia ya kibinadamu kurudi nyuma miaka 6,000, kama Biblia. Kwa hiyo, ili tufahamu dini ya kwanza-kwanza, ni lazima tuiendee Biblia. Ndicho kitabu peke yake kilicho na ujumbe wa ulimwengu mzima kwa wanadamu wote.
7. Watu wenye kufikiri wamesema nini juu ya Biblia?
7 Hekima na uzuri wa ujumbe ulioandikwa katika Biblia imesifiwa sana na watu wenye kufikiri kutoka mataifa yote na kutoka namna zote za maisha. Bwana Isaac Newton, mwanasayansi mwenye kujulikana sana na mvumbuzi wa kanuni ya uvutano, alisema hivi: “Hakuna mambo ya sayansi yanayoshuhudiwa vizuri zaidi ya Biblia.” Patrick Henry, Mwamerika kiongozi wa mageuzi mwenye sifa sana ya maneno haya “Nipe uhuru, au nipe kifo,” alitangaza hivi: “Biblia ni yenye kufaa sana kuliko vitabu vingine vyote ambavyo vimepata kuchapwa.” Hata Mohandas K. Gandhi, Mhindu mkuu mwenye akili sana wakati mmoja alimwambia kaimu wa mfalme wa Uingereza katika India hivi: “Wakati nchi yako na yangu zitakapopatana juu ya mafundisho yaliyowekwa na Kristo katika haya Mahubiri ya Mlimani, hatutakuwa tumetatua matatizo ya nchi zetu tu bali pia yale ya ulimwengu mzima.” Gandhi alikuwa akizungumza juu ya Mathayo sura ya 5 na 7, katika Biblia. Jisomee mwenyewe sura hizo uone kama husisimuliwi na ujumbe wazo wenye nguvu.
Biblia—Kitabu Kilichoandikwa Katika Nchi za Esia
8, 9. (a) Kwa nini ni kosa kuiita Biblia kitabu cha Wazungu? (b) Biblia iliandikwaje, na kwa muda gani? (c) Sababu gani Biblia inaweza kuitwa maktaba? (d) Ni watu wangapi waliotumiwa kuandika Biblia? (e) Ni ushuhuda gani ambao wengine kati ya watu hao walitoa juu ya Chanzo cha Biblia?
8 Tofauti na imani ya watu wengi, Biblia si zao la ustaarabu wa nchi za Wazungu, wala haitukuzi ustaarabu huo. Karibu Biblia nzima iliandikwa katika nchi za Esia. Watu walioiandika walikuwa wote Waesia. Miaka elfu moja kabla ya Buddha, katika mwaka wa 1513 K.W.K., Musa, aliyeishi katika Mashariki ya Kati, aliongozwa na Mungu aandike kitabu cha kwanza cha Biblia, kiitwacho Mwanzo. Kutoka mwanzo huo, Biblia inafuata moja kwa moja kichwa kimoja chenye kupatana mpaka kitabu chayo cha mwisho cha Ufunuo. Biblia ilikamilika mwaka wa 98 W.K., kama miaka 600 baada ya Buddha. Je! ulijua kwamba Biblia ina vitabu tofauti-tofauti 66? Ndiyo, Biblia yenyewe ni maktaba!
9 Hivyo, zaidi ya kipindi cha miaka 1,600 tangu wakati wa Musa, watu kama 40 walishiriki kuandika habari ya Biblia yenye kupatana. Wanashuhudia kwamba maandishi yao yaliongozwa na uwezo wa juu kuliko ule wa mwanadamu anayekufa. Paulo, mtume Mkristo aliandika hivi: “Andiko lote liliongozwa na Mungu na ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”b (1 Timotheo 3:16, NW) Naye mtume Petro alieleza hivi: “Hakuna unabii wa Andiko unaotokana na fasiri yo yote ya mtu binafsi. Kwa maana unabii haukuletwa wakati wo wote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu wakati walipoongozwa kwa roho takatifu.”—2 Petro 1:20, 21, NW; 2 Samweli 23:2; Luka 1:70.
10. (a) Biblia ilifikaje kwenye siku yetu hii? (b) Kwa sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba tungali tuna maandishi ya awali ya Biblia yaliyoongozwa na Mungu?
10 Jambo la kustaajabisha zaidi pia, ni njia ambayo Biblia imeweza kufika kwenye siku hii ya leo. Kwa maelfu ya miaka, nakala za Biblia zilipasa ziandikwe kwa mkono mpaka mashine za kuchapia zilipovumbuliwa miaka kama 500 iliyopita. Hakuna kitabu kingine cha nyakati za kale kilichonakiliwa na kurudia kunakiliwa kwa makini sana kama Biblia. Kilinakiliwa tena na tena, lakini nyakati zote kwa uangalifu mkubwa. Wenye kunakili walifanya makosa machache tu, na kuyalinganisha hayo kumethibitisha maandishi ya awali kuwa yaliongozwa na Mungu. Sir Frederic Kenyon, mtaalamu wa hati za Biblia anasema hivi: “Msingi wa mwisho wa kuwa na shaka lo lote kwamba Maandiko yametufikia sisi kama yalivyoandikwa sasa umeondolewa.” Leo, kungali kuna nakala za Biblia au sehemu yake 16,000 zilizoandikwa kwa mkono. Nyingine hata zimeendelea tangu karne ya pili kabla ya Kristo. Tena, tafsiri sahihi zimefanywa katika karibu lugha zote za dunia kutokana na lugha ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki ilimoandikwa Biblia hapo awali.
11. Ni mavumbuzi gani ya kisasa yanayopatana na maandishi ya Biblia?
11 Watu fulani wamejaribu kuipuuza Biblia kwa kusema ati si sahihi. Hata hivyo, katika miaka ya juzijuzi wachimbuzi wa mambo ya kale wamechimbua magofu ya miji ya kale katika nchi za Biblia, nao wamepata michoro na ushahidi mwingine unaothibitisha kikamili kwamba kulikuwako hakika watu na mahali panapotajwa hata katika maandishi ya Biblia yaliyo ya kale zaidi sana. Wamefukua ushahidi mwingi wenye kuelekeza kwenye gharika ya dunia yote, ambayo Biblia inasema ilitukia siku za Noa miaka zaidi ya 4,000 iliyopita. Juu ya jambo hilo, Mikasa, Mwana-mfalme, mtaalamu wa mambo ya kale mwenye kujulikana sana, alieleza hivi: “Je! kweli kulikuwako Gharika? . . . Uhakika wa kwamba gharika ilitukia hasa umethibitishwa kwa njia yenye kusadikisha.”c
Mungu wa Biblia
12. (a) Wadhihaki fulani wanasema nini juu ya Mungu? (b) Kwa sababu gani Biblia inarejeza kwa Mungu kuwa Baba? (c) Biblia inaonyesha Mungu anaitwa jina gani?
12 Kama vile watu fulani wameidhihaki Biblia, wengine wamedhihaki kuwako kwa Mungu Mwenye Nguvu Zote. (2 Petro 3:3-5) Wanasema, “Nimwaminije Mungu, hali siwezi kumwona? Je! kuna ushuhuda wa kwamba kuna Muumba asiyeonekana, ambaye yuko juu kuliko wanadamu? Je! Mungu hakai katika kila kitu?” Wengine wanasema: ‘Hakuna Mungu wala Buddha.’ Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba kama vile sisi sote tulivyopokea uhai kutoka kwa baba wa kidunia, vivyo hivyo wazazi wetu wa kwanza walipata uhai kutoka kwa Baba wa kimbingu au Muumba, ambaye jina lake kibinafsi ni Yehova.—Zaburi 83:18; 100:3; Isaya 12:2; 26:4.
13. Yehova amejifunua mwenyewe kwa wanadamu kwa njia gani mbili?
13 Yehova amejifunua kwa wanadamu katika njia mbili zenye kutokeza. Njia iliyo kuu ni kupitia Biblia, inayojulisha ukweli wake na makusudi yake ya milele. (Yohana 17:17; 1 Petro 1:24, 25) Njia nyingine ni kupitia uumbaji wake. Kwa kutazama vitu vya ajabu vinavyowazunguka, watu wengi wamepata kuthamini kwamba bila shaka kuna Mungu-Muumba ambaye utu wake wenye fahari unaonekana katika kazi zake.—Ufunuo 15:3, 4.
14. Biblia inatuambia nini juu ya Yehova?
14 Yehova ndiye Mtunga Biblia. Yeye ni Roho Kuu aliyeko katika umilele wote. (Yohana 4:24; Zaburi 90:1, 2) Jina lake “Yehova” linavuta fikira kwenye kusudi lake kuelekea viumbe vyake. Ni kusudi lake kutetea jina hilo kuu kwa kuwaharibu waovu na kuwaokoa wanaompenda ili waweze kuishi katika dunia-paradiso. (Kutoka 6:2-8; Isaya 35:1, 2) Yeye akiwa Mungu Mwenye Nguvu Zote, anao uwezo wa kufanya hivyo. Akiwa Muumba wa ulimwengu mzima, yeye yuko juu sana kuliko miungu na sanamu za kawaida za mataifa.—Isaya 42:5, 8; Zaburi 115:1, 4-8.
15. Uchunguzi juu ya uumbaji ambao umefanywa na watu wenye akili umeongoza kwenye maamuzi gani?
15 Katika karne za karibuni, watu wa sayansi wametumia wakati mwingi wakijifunza kazi za uumbaji. Wamekata shauri gani? Mmoja wa wavumbuzi wa umeme, Lord Kelvin, yule mwanafizikia Mwingereza mwenye kujulikana sana, alitangaza hivi: “Naamini kwamba kadiri sayansi inavyochunguzwa kikamili ndivyo inavyotupeleka mbali na jambo lo lote linalolinganishwa na wazo la kwamba hakuna Mungu.” Albert Einstein, mwanasayansi mzaliwa-Ulaya, ingawa yeye ni mtu anayejulikana sana kuwa asiyeamini kuwako kwa Mungu, aliungama hivi: “Imenitosha . . . kufikiria muundo wa ajabu wa ulimwengu mzima, tunaoweza kufahamu kidogo, na kujaribu kwa unyenyekevu kuelewa hata sehemu ndogo sana ya akili inayoonekana katika asili.” Arthur Holly Compton, mwanasayansi na mshindi wa zawadi ya Nobeli, alisema: “Ulimwengu mzima wenye utaratibu unaofunuka unashuhudia ukweli wa maneno yenye utukufu zaidi yaliyopata kusemwa kwamba ‘Mwanzoni Mungu.’” Alikuwa akinakili maneno ya kwanza ya Biblia.
16. Ulimwengu mzima unatukuzaje hekima na uwezo wa Mungu wa kuumba vitu?
16 Watawala wa mataifa yenye nguvu wamejivunia akili yao na mambo ambayo wametimiza katika kushinda anga ya juu zaidi. Lakini setilaiti zao za angani ni ndogo kama nini zinapolinganishwa na mwezi ambao unaizunguka dunia na sayari nyingine zinazolizunguka jua! Matimizo ya watu hao wawezao kufa, ni madogo kama nini, yakilinganishwa na uumbaji wa Yehova wa mabilioni ya makundi ya nyota mbinguni, kila kundi la nyota likiwa na majua kama jua letu wenyewe, na ameyakusanya na kuyaweka angani kwa wakati usiopimika. (Zaburi 19:1, 2; Ayubu 26:7, 14) Si ajabu kwamba Yehova anawaona watu kama panzi, na mataifa yenye nguvu “kama si kitu.”—Isaya 40:13-18, 22.
17. Sababu gani ni jambo la akili kuamini kuna Muumba?
17 Je! wewe unaishi ndani ya nyumba? Labda hukuijenga nyumba hiyo wewe mwenyewe, wala hujui mtu aliyeijenga. Hata hivyo, uhakika wa kwamba humjui mjenzi huyo haungekuzuia kukubali ukweli wa kwamba mtu fulani mwenye akili aliijenga. Kufikiri kwamba nyumba hiyo ilijijenga yenyewe kungeonekana kuwa upumbavu sana! Kwa kuwa ulimwengu mzima ulio mkubwa, na kila kitu kilichomo, ulitaka akili kubwa zaidi isiyo na mwisho ili ujengwe, je! si jambo la akili kukata shauri kwamba bila shaka kuna Muumba Mwenye Akili? Kweli kweli, ni mtu asiye na akili peke yake ndiye angesema moyoni mwake, “Hakuna Yehova.”—Zaburi 14:1, NW; Waebrania 3:4.
18. Ni nini kinachoonyesha kwamba Mungu ni mtu, na anastahili kusifiwa?
18 Yale maajabu yenye utukufu yanayotuzunguka—maua, ndege, na wanyama, uumbaji wa ajabu unaoitwa wanadamu, ile miujiza ya uhai na uzawa—yote hayo yanashuhudia kwamba kuna Mtaalamu Mwenye Akili asiyeonekana aliyeyafanyiza. (Warumi 1:20) Palipo na fikira, pana akili. Palipo na akili, pana mtu. Fikira kuu ni ile ya Mtu Mkuu, Muumba wa vitu vyote vilivyo hai, aliye chemchemi yenyewe ya uhai. (Zaburi 36:9) Ndiyo, Muumba anastahili sifa na ibada yote.—Zaburi 104:24; Ufunuo 4:11.
19. (a) Sababu gani hakuna taifa leo linaloweza kudai linapewa na Mungu kushinda vita? (b) Sababu gani Mungu hahusiki na vita vya mataifa?
19 Kuna watu fulani ambao imani yao katika Mungu ilitikiswa na taabu za Vita ya Ulimwengu ya Pili. Wakati huo kila nchi iliomba “Mungu” wayo, kwamba ni wa dini za Kikatoliki ama wa Kiprotestanti ama wa dini za nchi za Esia. Je! ingeweza kusemwa kwamba “Mungu” aliyapa mataifa fulani ushindi kisha akaruhusu mengine yashindwe? Biblia inaonyesha kwamba hakuna moja la mataifa hayo lililokuwa likimwomba Mungu wa kweli. Yehova Mungu, Muumba wa mbingu na dunia, siye mwenye kuleta fujo hiyo na vita kati ya mataifa. (1 Wakorintho 14:33) Mawazo yake yako juu sana kuliko yale ya mataifa ya kisiasa na ya kivita ya dunia hii. (Isaya 55:8, 9) Vilevile, dini na ibada ya kweli ya Yehova haina sehemu katika vita vya mataifa. Yehova yuko juu sana kuliko miungu ya mataifa. Yeye ni wa pekee katika kuwa ndiye Mungu wa wanaume na wanawake wanaopenda amani katika mataifa yote. Ni kama Biblia inavyosema: “Mungu hana ubaguzi. Mtu wa taifa lo lote anayemcha Mungu na kutenda yaliyo haki anapokelewa naye.” (Matendo 10:34, 35, Habari Njema kwa Watu Wote) Watu wenye maelekeo ya kupenda uadilifu katika mataifa yote sasa wanajifunza Biblia na wanaikubali kwa moyo ibada ya “Mungu [wa kweli] wa amani,” yule Muumba wa wanadamu wote.—Warumi 16:20; Matendo 17:24-27.
20. Ni nini kinachoonyesha kwamba Jumuiya ya Wakristo iko kinyume cha Ukristo na inapinga Mungu?
20 Watu fulani wanaelekeza kwenye migawanyiko na unafiki uliomo katika dini za Jumuiya ya Wakristo, dini zinazodai ati zinaifuata Biblia. Wao pia wanasema, ‘Niaminije Mungu wa Biblia, na hali mataifa yaliyo na Biblia yamo kati ya yale yanayorundika kabambe silaha za nyukilia?’ Uhakika ni kwamba, ingawa nyakati zote Biblia ni ya kweli, mataifa ya Jumuiya ya Wakristo yamejiondoa mbali sana na Ukristo wa Biblia kama vile Ncha ya Kaskazini ya dunia ilivyo mbali na Ncha ya Kusini. Wao ni wanafiki katika kujidai kuwa na Ukristo. Wanayo Biblia, lakini hawatii mafundisho yayo. Ili kuongoza watu katika hatari hii ya ulimwengu, wakati mmoja Rais Mwamerika aliyeamuru kombora la kwanza la atomi liangushwe juu ya Hiroshima, alipaaza sauti hivi: “O, kwa kuunga mkono Isaya au Mtakatifu Paulo!” Kama angalikubaliana na Isaya wa Biblia, hangaliangusha kamwe kombora la atomi, kwani Isaya aliunga mkono ‘kufua panga kuwa majembe na mikuki kuwa miundu.’ Tena, ni Paulo wa Biblia aliyetangaza hivi: “Sisi hatufanyi vita kulingana na tulivyo katika mwili. Kwa maana silaha za vita yetu si za kimwili.” (Isaya 2:4, UV; 2 Wakorintho 10:3, 4, NW) Hata hivyo, badala ya kufuata shauri hilo la Biblia lenye hekima, mataifa ya Jumuiya ya Wakristo yamehusika katika mashindano ya kuunda silaha za kujiangamiza. Madai yao yo yote ya kwamba wao ni Wakristo wenye kutii Biblia si ya kweli. Ni lazima wahukumiwe na Mungu kwa kushindwa kufanya mapenzi yake.—Mathayo 7:18-23; Sefania 1:17, 18.
Maumbaji ya Yehova na Miujiza
21. Sababu gani ni jambo la akili kutotia shaka juu ya miujiza ya Mungu?
21 Yehova anaumba, na anafanya miujiza. Umepata kustaajabia kugeuzwa kwa maji kuwa damu, kutengwa kwa Bahari Nyekundu, jinsi Yesu alivyozaliwa na bikira, na miujiza mingine iliyoandikwa katika Biblia? Kwa kuwa mwanadamu ni mwenye uwezo wa akili ndogo, yaelekea hatafahamu kamwe jinsi mingine kati ya miujiza hiyo ilivyotukia. Ni kama asivyoweza kufahamu kikamili muujiza wa kutokea kwa jua na kushuka kwalo kila siku. Kuumbwa kwa mwanadamu kulikuwa ni muujiza. Mwanadamu wa kisasa hakuona muujiza huo, lakini anajua ulitukia, kwa maana yuko hai leo ili kuthibitisha hilo. Ndiyo, uhai wote na ulimwengu mzima ni muujiza mmoja wa daima. Hivyo, je! tutie shaka wakati Biblia, Neno la Mungu linaposema kwamba yeye alifanya miujiza nyakati zilizo dhahiri, hata ingawa hakuna uhitaji wa kufanya miujiza ile ile leo?
22. Ebu simulia uumbaji wa kwanza wa Mungu.
22 Uumbaji wote wa Yehova ni wa kimuujiza na ni wa ajabu! Hata hivyo, uumbaji wake wenyewe wa kwanza ulikuwa wa kimuujiza kuliko yote. Ulikuwa kuumbwa kwa Mwana wa kiroho, “mzaliwa wa kwanza” wake. (Wakolosai 1:15) Mwana huyo wa kimbingu aliitwa “Neno.” Vilipopita vipindi vya wakati visivyohesabika baada ya kuumbwa kwake, akaja kwenye dunia hii akaitwa “Mwanadamu Kristo Yesu.” (1 Timotheo 2:5) Ndipo iliposemwa juu yake hivi: “Hivyo Neno akawa mwili na akakaa kati yetu, nasi tuliona utukufu wake, utukufu kama wa mwana mzaliwa-pekee kutoka kwa baba; naye alikuwa mwenye kujaa fadhili zisizostahilika na ukweli.”—Yohana 1:14, NW.
23. (a) Uhusiano kati ya Mungu na Mwanaye unaweza kuelezwaje? (b) Yehova aliumba nini kupitia Mwanaye?
23 Uhusiano wa Yehova na Mwanaye unaweza kulinganishwa na uhusiano wa meneja mwenye mali na mwanaye katika kiwanda cha kazi, ambamo mwana huyo anasaidia kufanyiza vitu vinavyobuniwa na baba yake. Kupitia Mwanaye mzaliwa wa kwanza na mfanya kazi mwenziye, Yehova aliumba viumbe wengine wengi wa kiroho, wana wa Mungu. Baadaye, wana hao walishangilia kuona Mwana wa Yehova, Mfanya Kazi Stadi wake, akitokeza mbingu zenye kuonekana na dunia tunayoishi juu yake. Je! unatilia shaka kuumbwa kwa vitu hivyo? Maelfu ya miaka iliyofuata, Yehova alimwuliza mtu mwaminifu hivi: “Wewe ulipata kuwa wapi nilipoweka msingi wa dunia? Ebu niambie, ikiwa unajua ufahamu. Nyota za asubuhi zilipolia kwa sauti pamoja kwa shangwe, na wana wa Mungu wote walipoanza kupaaza sauti kwa vifijo?”—Ayubu 38:4, 7, NW; Yohana 1:3.
24. (a) Ni uumbaji gani wa kidunia wa Yehova ulio wa kutokeza sana, na katika mambo gani? (b) Sababu gani ni jambo lisilo la akili kusema mtu alipanda ngazi kwa kugeuka-geuka kutokana na wanyama?
24 Kadiri wakati ulivyosonga, Yehova akaumba vitu vilivyo hai, vinavyoonekana hapa duniani, mimea, miti, maua, samaki, ndege, na wanyama. (Mwanzo 1:11-13, 20-25) Kisha Mungu akasema hivi kwa Mfanya Kazi Stadi wake: “Na tufanye mtu kwa mfano wetu . . . Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwanzo 1:26, 27) Akiwa ameumbwa kwa mfano na sura ya Mungu, akiwa na sifa kuu za upendo, hekima, haki, na uwezo, mtu wa kwanza alikuwa bora kuwapita wanyama. Mtu yumo katika aina iliyo mbali na wanyama kwa kuwa yeye aweza kufikiri na kutoa sababu, aweza kupangia wakati ujao, na ana uwezo wa kumwabudu Mungu. Wanyama hawana akili ya kufikiri na kutoa sababu, ila wanaishi kwa silika. Ni upumbavu kama nini kusema kwamba hakuna Muumba, lakini kusema kwamba kiumbe mwanadamu mwenye sifa na akili nyingi alipanda ngazi ya juu kwa kugeuka-geuka kutoka wanyama wa chini wasio na akili!—Zaburi 92:6, 7; 139:14.
25, 26. (a) Ni taraja gani zuri ajabu lililowekwa mbele ya mtu? (b) Sababu gani hakungekuwako tatizo la dunia kusongamana watu?
25 Mungu akamweka mtu katika “bustani upande wa mashariki wa Edeni.” Ilikuwa bustani ya furaha, kama bustani ile kwenye jalada letu, ingawa bado walikuwa ndio watu wawili pekee, yaani, Adamu na mke wake. Paradiso hiyo ya kwanza haipo tena. Iliharibiwa na Gharika ya siku za Noa. Lakini inaonekana kama ilikuwa kule Mashariki ya Kati, kwa sababu mito fulani inayotajwa majina katika Biblia iliyokuwa ikitiririka ndani yake, ipo mpaka leo hii. (Mwanzo 2:7-14) Mtu alikuwa na nafasi bora ya kutumia bustani hiyo kuwa mahali ambapo toka hapo angesambaa na kuilima dunia nzima, aifanye kuwa paradiso mahali pote.—Isaya 45:12, 18.
26 Kwa vile Mungu na Mwanaye ni wafanya kazi, hivyo pia Mungu alimpa mtu kazi ya kufanya hapa duniani. (Yohana 5:17) Alisema hivi, kwa Adamu na Hawa, yule mwanamume na mwanamke wa kwanza: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze [dunia], na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya [dunia].” (Mwanzo 1:28) Je! hiyo ilikuwa na maana kwamba mtu alipaswa kuongezeka, aijaze dunia, kisha azidi kuongezeka mpaka dunia ijae sana hata kufurika? Sivyo. Mtu akikuambia ujaze kikombe chai, huzidi kumwaga chai katika kikombe mpaka kikombe kinapofurika chai na kumwagikia meza yote. Unakijaza kikombe tu na kuacha. Hali moja na hiyo, amri ya Yehova aliyompa mtu ‘aijaze dunia,’ ilionyesha kusudi lake la kutaka mtu aijaze dunia bila kusongamana, kisha kuzaa aina ya watu hapa duniani kungekoma. Jambo hilo halingetokeza tatizo katika jamii kamilifu ya kibinadamu. Kusongamana watu kunatokeza tatizo katika ulimwengu wa leo tu wenye wanadamu wasiokamilika.
Mambo Mabaya—Sababu Gani Mungu Anayaruhusu?
27. Ni maswali gani yanayotaka jibu sasa?
27 Ikiwa kusudi la Mungu ni kujenga dunia-paradiso, ikoje kwamba leo dunia imejaa sana uovu, kuteseka, na huzuni? Ikiwa Mungu ni Mwenye Nguvu Zote, sababu gani ameruhusu hali hizo kwa muda mrefu sana? Je! kuna tumaini la mwisho wa taabu zetu zote? Biblia inasema nini?
28. Uasi uliingiaje katika bustani ya Paradiso?
28 Biblia inaonyesha kwamba taabu za wanadamu zilianza wakati mmoja wa wana wa Mungu alipoasi enzi kuu ya Yehova, au utawala. (Warumi 1:20; Zaburi 103:22, maelezo ya chini katika NW Ref. Bi.) Bila shaka malaika huyo alikuwa kati ya wale waliokuwa wameshangilia kuona uumbaji wa mtu. Lakini ndipo tamaa mbaya na kiburi vikawa na mizizi katika moyo wake, akavutwa na tamaa ya kutaka Adamu na Hawa wamwabudu yeye badala ya kuabudu Muumba wao, Yehova. Akisema kwa kutumia nyoka, kama vile mtu mwenye ujuzi wa kusema anavyofanya ionekane kama kwamba ni kisanamu kinachosema, malaika huyo alimshawishi Hawa akose kumtii Mungu Mwenye Nguvu Zote. Ndipo Adamu, mume wake, akamfuata katika kutokutii.—Mwanzo 2:15-17; 3:1-6; Yakobo 1:14, 15.
29. (a) Ni masuala gani ya kuamuliwa yaliyotokea? (b) Mungu ameshughulikaje na dai hilo? (c) Wewe unaweza kushirikije kutoa jibu kwenye laumu la Shetani?
29 Malaika mwasi huyo akaja kujulikana kuwa “nyoka wa zamani.” (Ufunuo 12:9; 2 Wakorintho 11:3) Pia anaitwa jina Shetani, maana yake “Mpingaji,” na Ibilisi, maana yake “Mchongezi.” Alitilia shaka kufaa na uadilifu wa utawala wa Yehova juu ya dunia, akampinga Mungu kwa kusema kwamba sasa yeye, yaani Shetani, angeweza kuondoa wanadamu wote katika ibada ya kweli. Mungu ameruhusu Shetani awe na miaka kama 6,000 hivi ili ajaribu kuthibitisha dai lake, ili suala juu ya enzi kuu ya Yehova lipate kumalizwa kwa umilele wote. Utawala wa mwanadamu usiomtegemea Mungu umeshindwa kwa jinsi ya kusikitisha. Lakini wanaume na wanawake wenye imani, ambao kati yao Yesu ndiye mfano wenye kutokeza sana, wameshika ukamilifu kwa Mungu chini ya majaribu makali zaidi sana, wakimtetea Yehova na kumthibitisha Ibilisi kuwa mwongo. (Luka 4:1-13; Ayubu 1:7-12; 2:1-6; 27:5) Wewe, pia, unaweza kuwa mshika ukamilifu. (Mithali 27:11) Lakini Shetani siye adui pekee anayetusumbua. Kuna adui gani mwingine?
Adui—Kifo
30. Maandiko yanasema nini juu ya adhabu iliyotokea kwa mtu kwa sababu ya kutokutii?
30 Mungu alikuwa amesema adhabu ya kutokutii ingekuwa kifo. Alipokuwa akitoa hukumu ya kwanza juu ya mwanamke wa kwanza, Yehova alisema: “Nitakuzidishia uchungu wako, na kuzaa kwako; kwa utungu utazaa watoto; na tamaa yako itakuwa kwa mumeo, naye atakutawala.” Kwa mwanamume Adamu, alisema: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:16-19) Watu wawili wasiotii wakafukuzwa katika Paradiso ya furaha, wakaingia katika dunia isiyolimwa. Wakati uliposonga wakafa.—Mwanzo 5:5.
31. Dhambi ni nini, na matokeo yake yamekuwa nini kwa wanadamu?
31 Ikawa walipokwisha shindwa kufikia ile alama ya ukamilifu ndipo Adamu na Hawa wakaanza kuzaa watoto. Wanadamu wote leo ni wazao wao wasiokamilika, na kwa sababu hiyo wote wanakufa. Mwandikaji mmoja wa Biblia anaeleza hali hiyo kwa maneno haya: “Kwa njia ya mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, nayo ikasababisha kifo. Hivyo kifo kimeenea katika jumuiya yote ya binadamu, kwa maana wote wametenda dhambi.” “Dhambi” hiyo ni nini? Ni kushindwa kufikia alama ya ukamilifu. Yehova Mungu hakubali wala hahifadhi hai kitu cho chote kisichokamilika. Kwa kuwa watu wote wamerithi dhambi na kutokamilika kutoka kwa mtu wa kwanza Adamu, kifo ‘kiliwatawala’ wao. (Waroma 5:12, 14, HNWW) Mwanadamu mkosaji anakufa, kwa njia ile ile wanavyokufa wanyama.—Mhubiri 3:19-21.
32. Biblia inasimuliaje kifo ambacho tumerithi?
32 “Kifo” ni nini? Kifo ni kinyume cha uhai. Mungu alikuwa ameweka mbele ya mtu taraja la uzima usio na mwisho hapa duniani kama angetii. Hata hivyo, yeye alikosa kutii, na adhabu ikawa kifo, hali ya bila fahamu, kutokuwako. Mungu hakuwa amesema lo lote juu ya kuhamisha uhai wa mtu kuupeleka kwenye makao ya kiroho wala kwenye mahali pa moto kama angekosa kutii na kufa. Yeye alikuwa amemwonya mtu hivi: “Hakika utakufa.” Ni Ibilisi mwuaji wa watu aliyekuwa amesema uwongo hivi: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 2:17; 3:4; Yohana 8:44) Kitu ambacho wanadamu wote wamerithi kutoka kwa Adamu ni kifo cha mfano wa mavumbi.—Mhubiri 9:5, 10; Zaburi 115:17; 146:4.
33. (a) Ni wakati ujao gani mtukufu unaowangoja wanadamu na dunia hii? (b) Ni mambo gani matatu ambayo Yehova anatimiza kupitia Mwanaye?
33 Basi, je! hakuna wakati ujao kwa mtu anayekufa? Kuna wakati mzuri ajabu! Biblia inaonyesha kwamba kusudi la Mungu la kuwa na dunia-paradiso kwa wanadamu wote, kutia na wale ambao sasa wamekufa, halitakosa kutimizwa. Asema Yehova hivi: “Mbingu ni kiti changu cha enzi na dunia ni mahali pa kuweka miguu yangu.” “Nitapatukuza mahali pa miguu yangu.” (Isaya 66:1; 60:13) Kwa wingi wa upendo wake, Yehova alimtuma Mwanaye, Neno, kwenye dunia hii, ili ulimwengu wa wanadamu upate kupokea uzima kupitia yeye. (Yohana 3:16; 1 Yohana 4:9) Kuna mambo ya maana matatu ambayo ni lazima tuzungumze sasa na ambayo Yehova anatimiza kupitia Mwanaye, yaani, (1) kuandaa kufunguliwa katika nguvu za kifo; (2) kuwarudisha hasa wafu kwenye uzima; na (3) kusimamisha serikali kamilifu juu ya wanadamu wote.
Kufunguliwa Katika Kifo
34, 35. (a) Ni kwa njia gani pekee mtu angeweza kukombolewa kutoka kifo? (b) Ukombozi ni nini?
34 Tangu nyakati za kale, manabii wa Mungu wameonyesha uhakika wao, si katika kutokufa kwa mtu, bali katika tumaini la kwamba Mungu ‘angewakomboa’ katika kifo. (Hosea 13:14) Lakini mtu angeweza kufunguliwa katika vifungo vya kifo namna gani? Haki kamilifu ya Yehova ilitaka ‘nafsi kwa nafsi, jicho kwa jicho, jino kwa jino.’ (Kumbukumbu la Torati 19:21, NW) Hivyo, kwa kuwa Adamu aliletea wanadamu wote kifo kilichorithiwa kwa sababu ya kutokumtii Mungu makusudi na hivyo akapoteza ukamilifu wa uhai wa kibinadamu, binadamu mkamilifu mwingine alipaswa awe badala ya Adamu katika kulipa uhai wake mkamilifu, ili anunue na kurudisha kile ambacho Adamu alikuwa amepoteza.
35 Kanuni hiyo ya haki ya kulipa ‘sawa kwa sawa’ imekubaliwa kote kote katika historia yote. Usemi unaotumiwa na wengi ni “kulipa ukombozi.” Ukombozi ni nini? Ni “bei inayolipwa kuokoa mtu au kitu kutoka kwa mwingine anayemzuia mtu huyo au kitu kilichotekwa nyara. Kwa sababu hiyo mateka wa vita au watumwa wanasemwa kuwa wamekombolewa wakati wanapoachwa huru kwa kubadilishwa na kitu chenye thamani. . . . Cho chote kinachotolewa badala ya kingine au kutolewa ili kufidia mtu huyo ni ukombozi wake.”d Tangu Adamu atende dhambi, wanadamu wote wamekuwa kama mateka wa vita au watumwa, wamefungwa na kutokamilika na kifo. Ili kuwafungua, ilikuwa lazima ukombozi utolewe. Ili kuepuka ugomvi wo wote sasa au baadaye juu ya kufaa kwa bei ya ukombozi, ingekuwa lazima kutoa uhai wa kibinadamu mmoja ulio mkamilifu, yaani, kiasi kinacholingana barabara na Adamu.
36. Yehova aliandaaje uhai mkamilifu wa kibinadamu uwe ukombozi?
36 Hata hivyo, uhai mkamilifu huo wa kibinadamu ungeweza kupatikana wapi? Watu wote, wakiwa wazao wa Adamu asiyekamilika, wamezaliwa wakiwa wasiokamilika. “Hakuna mmoja wao anayeweza kwa njia yo yote kukomboa hata ndugu, wala kumpa Mungu ukombozi kwa ajili yake.” (Zaburi 49:7, NW) Katika kuitikia uhitaji huo, kwa hakika Yehova, akisukumwa na upendo wake wenye kina kirefu kwa ajili ya wanadamu, alimwandaa Mwanaye “mzaliwa wa kwanza” mwenye bei kubwa awe dhabihu iliyokuwa ikihitajiwa. Yeye alihamisha uhai mkamilifu wa Mwana huyo wa kiroho, yaani, Neno, akaupeleka katika tumbo la uzazi la Mariamu, bikira wa Kiyahudi. Mwanamke huyo kijana akachukua mimba, na kwa wakati unaofaa akazaa mwana, aliyeitwa jina “Yesu.” (Mathayo 1:18-25) Kwa kufaa Muumba wa uhai angeweza kufanya muujiza huo wa ajabu.
37. Yesu alionyeshaje upendo wake kwa wanadamu wote wanaotamani uzima?
37 Yesu alikua akawa mtu mzima. Akajitokeza kwa Yehova, akabatizwa. Kisha Mungu akamwagiza afanye mapenzi Yake. (Mathayo 3:13, 16, 17) Kwa kuwa uhai wa kidunia wa Yesu ulitoka mbinguni, naye alikuwa mkamilifu, yeye angeweza kutoa uhai mkamilifu huo wa kibinadamu, akiutumia kufungua wanadamu katika kifo. (Warumi 6:23; 5:18, 19) Ni kama alivyosema: “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.” “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 10:10; 15:13) Shetani alipopanga Yesu auawe kwenye mti wa mateso, Yesu alijitoa afe kifo hicho cha ukatili, akijua kwamba wanadamu wenye kuzoea imani wangepata uzima kupitia ukombozi huo.—Mathayo 20:28; 1 Timotheo 2:5, 6.
Kurudishwa Kwenye Uzima
38. Mwana wa Mungu alirudishwaje kwenye uzima, na ni nini kinachohakikisha hilo?
38 Hata ajapouawa na adui zake, Mwana wa Mungu hakupoteza kamwe haki yake ya kwenye uhai mkamilifu wa kibinadamu, kwa maana alikuwa ameshika ukamilifu kwa Mungu. Lakini, kwa kuwa mfu katika kaburi, Yesu angewezaje kukitumia kitu hicho chenye thamani, yaani, haki ya kwenye uhai wa kibinadamu, kwa ajili ya wanadamu? Hapo ndipo Yehova alipofanya muujiza mwingine, ulio wa kwanza wa aina yake. Siku ya tatu ya kuwa kwa Yesu katika kaburi, Yehova alimwinua kutoka kifo akiwa kiumbe wa kiroho, asiyeweza kufa. (Warumi 6:9; 1 Petro 3:18) Ili kuimarisha imani katika ufufuo, Yesu alifanyiza miili ya kibinadamu katika pindi tofauti-tofauti na kujitokeza kwa wanafunzi wake. Wakati mmoja alijitokeza kwa wanafunzi kati yao 500 na zaidi. Hakuna ye yote wa hao aliyekuwa na sababu yo yote ya kutilia shaka muujiza wa kufufuliwa kwake, wala mtume Paulo ambaye baadaye alipofushwa kwa kutokewa na Yesu aliyetukuzwa.—1 Wakorintho 15:3-8; Matendo 9:1-9.
39. (a) Yesu anatumiaje bei ya dhabihu yake, na kwanza kwa faida ya nani? (b) Yesu alisema juu ya muujiza gani mwingine ulio mkubwa?
39 Baada ya siku 40 Yesu aliyefufuliwa alipanda kuingia mahali alipo Mungu mwenyewe katika mbingu, ili akatoe huko bei ya dhabihu yake kamilifu ya kibinadamu ikiwa kitu cha kufungua wanadamu. “Lakini huyu, alipokwisha kutoa kwa ajili ya dhambi dhabihu moja idumuyo hata milele, aliketi mkono wa kuume wa Mungu; tangu hapo akingojea hata adui zake wawekwe kuwa chini ya miguu yake.” (Waebrania 10:12, 13) Wa kwanza kutazamia kufunguliwa kupitia ukombozi huo ni “kundi dogo” la Wakristo waaminifu “walio wake Kristo.” (Luka 12:32; 1 Wakorintho 15:22, 23) Hao “wamenunuliwa katika wanadamu,” na kwa sababu hiyo wanapofufuliwa, wanakuwa washiriki wa kiroho wa Kristo katika mbingu. (Ufunuo 14:1-5) Hata hivyo, namna gani wale wa halaiki kubwa za wanadamu ambao sasa wangali ni wafu katika makaburi yao? Yesu alipokuwa hapa duniani, alisema kwamba Baba yake amempa mamlaka ya kuhukumu na kutoa uhai. Aliongeza hivi: “Msione hili kuwa ajabu, kwa sababu ile saa inakuja ambayo katika hiyo wale wote walio katika makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake watoke, . . . kwenye ufufuo.” (Yohana 5:26-29, NW) Atawarudisha hao kwenye uzima katika dunia-Paradiso.
40, 41. (a) Eleza hasa maana ya “ufufuo.” (b) Sababu gani tunaweza kuiamini ahadi ya Mungu ya ufufuo?
40 Angalia maneno haya ya Yesu, “Msione hili kuwa ajabu.” Hata hivyo, mtu aliyekufa zamani sana anaweza kufunguliwaje kutoka kifo na kurudishwa kwenye uzima? Je! mwili wake haukurudia mavumbi? Sehemu fulani zilizokuwa za mwili huo labda hata zimeingia katika vitu vingine vilivyo hai, kama vile mimea na wanyama. Hata hivyo, ufufuo haumaanishi kukusanya pamoja tena mchanganyiko wa vitu vile vile vya asili. Unamaanisha kwamba Mungu anaumba upya mtu yule yule, akiwa na utu ule ule. Yeye anatokeza mwili mpya katika vitu vya asili vya dunia, na anaweka katika mwili huo tabia zile zile, sifa zile zile zenye kutokeza, kumbukumbu ile ile, kiolezo kile kile cha maisha ambacho mtu huyo alikuwa amejenga kufikia wakati wa kifo chake.
41 Labda umepata kuona nyumba yako uliyopenda sana sana ikiteketea moto. Hata hivyo, ungeweza kujengesha kwa urahisi nyumba ile ile, kwa maana kiolezo cha mambo yake yote uliyopenda kimo katika kumbukumbu yako. Bila shaka, basi, Mungu ambaye ndiye Asili ya kumbukumbu anaweza kuumba upya watu ambao ametunza katika kumbukumbu yake kwa sababu anawapenda. (Isaya 64:8) Hiyo ndiyo sababu Biblia inatumia usemi huu “makaburi ya ukumbusho.” Utakapokuwa wakati wake Mungu wa kuleta wafu kwenye uhai tena, yeye atafanya muujiza huo, kama alivyofanya muujiza wa kuumba mtu wa kwanza, isipokuwa kwamba wakati huu ataufanya mara nyingi-nyingi.—Mwanzo 2:7; Matendo 24:15.
42. Sababu gani uzima wa milele duniani unawezekana na ni hakika?
42 Mungu atarudisha wanadamu kwenye uzima, wawe na tumaini la kutokufa tena hapa duniani. Lakini uzima wa milele duniani unawezekanaje? Unawezekana na ni hakika kwa sababu ndiyo mapenzi na kusudi la kimungu (Yohana 6:37-40; Mathayo 6:10) Sababu moja tu inayofanya mtu afe na kuondoka duniani leo ni kwamba yeye alirithi kifo kutoka kwa Adamu. Hata hivyo, tufikiriapo vitu vya namna namna vya ajabu visivyo na mwisho hapa dunia ambavyo mtu alikusudiwa avifurahie, muda mfupi wa kuishi ambao haufikii hata miaka 100, ni mfupi mno mno! Katika kuwapa watoto wa wanadamu dunia hii, Mungu alikusudia mtu aendelee kuishi ili afurahie fahari za uumbaji Wake, si kwa muda wa miaka 100 tu, wala hata miaka 1,000, bali milele na milele!—Zaburi 115:16; 133:3.
Serikali Iliyo Kamilifu ya Amani
43. (a) Kuna uhitaji gani wa kuwa na serikali kamilifu? (b) Yehova anakusudia nini katika jambo hili?
43 Kwa sababu wazazi wetu wa kwanza walikataa sheria ya Mungu, serikali ya kibinadamu ikaja kuwa chini ya uongozi wa Shetani. Kwa kufaa Biblia inamwita Shetani “mungu wa huu mfumo wa mambo.” (2 Wakorintho 4:4, NW) Vita, matendo ya unyama, ufisadi, na ukosefu wa imara ya serikali za wanadamu, yote hayo yanathibitisha yeye yuko hivyo. Ule Ushirika wa Mataifa na Umoja wa Mataifa umeshindwa kutokeza amani katika mvurugo. Wanadamu wanalia wakitaka serikali ya amani. Je! si jambo la akili kwamba Muumba, anayekusudia kurudisha Paradiso kwenye dunia hii, angetoa pia serikali kamilifu itawale Paradiso hiyo? Hivyo ndivyo Yehova amekusudia kufanya hasa. Yule Mfalme anayemwakilisha Yeye katika serikali hiyo ni “Mwana-Mfalme” wake, Kristo Yesu, na “kwa wingi wa utawala wa mwana-mfalme na kwa amani hakutakuwa na mwisho.”—Isaya 9:6, 7, NW.
44. (a) Serikali hiyo itakuwa wapi? (b) Nani watakuwa watawala?
44 Biblia inaonyesha kwamba serikali hiyo kamilifu itakuwa mbinguni. Akiwa huko, Mfalme Yesu Kristo ataitawala kwa kufaa dunia yote kwa uadilifu. Zaidi ya hayo, yeye atakuwa na watawala wa kushirikiana naye katika serikali hiyo ya kimbingu isiyoonekana. Hao wanachaguliwa kutoka wanadamu waaminifu, wafuasi wa Yesu walioshikamana naye katika majaribu yote na ambao anaambia hivi: “Mimi nafanya agano pamoja nanyi, kama vile Baba yangu amefanya agano pamoja na mimi, kwa ajili ya ufalme.” (Luka 22:28, 29, NW) Ni wachache tu kutoka wanadamu wanaochukuliwa waende mbinguni wakatawale pamoja na Kristo Yesu. Ni sawa yalivyo mataifa leo, yanayochagua watu wachache tu wawe mawaziri au wabunge wa serikali. Biblia inaonyesha kwamba Yesu Kristo atakuwa na watu 144,000 tu watakaoshiriki naye kuwa watawala. Hivyo, Ufalme wa Mungu, au serikali ya kimbingu, ina Kristo Yesu na watu 144,000 waliochukuliwa kutoka dunia waende mbinguni. (Ufunuo 14:1-4; 5:9, 10) Na namna gani dunia hii? Zaburi 45:16, NW, inataja kwamba Mfalme huyo ataweka “wana-wafalme katika dunia yote.” Kuwekwa rasmi kwa “wana-wafalme” wa kibinadamu, au waangalizi wa kiserikali, kutatoka mbinguni kwa sababu ya kufuata kwao sana kanuni za uadilifu.—Linganisha Isaya 32:1.
45, 46. (a) Ni nini kilichokuwa kichwa kikuu cha mahubiri ya Yesu duniani? (b) Sababu gani serikali hiyo kamilifu haikusimamishwa mara hiyo? (c) Ni kwa njia gani mwaka 1914 ulikuwa wenye kutokeza sana katika unabii na katika matukio ya ulimwengu?
45 Serikali kamilifu hiyo inasimamishwa wakati gani na jinsi gani? Yesu alipokuwa duniani Ufalme huo ulikuwa ndio kichwa kikuu cha mahubiri yake. (Mathayo 4:17; Luka 8:1) Hata hivyo, yeye hakusimamisha Ufalme huo wakati huo, wala wakati wa kufufuliwa kwake. (Matendo 1:6-8) Hata alipopanda kuingia katika mbingu, alipaswa kungojea wakati uliowekwa wa Yehova. (Zaburi 110:1, 2; Waebrania 1:13) Unabii wa Biblia waonyesha kwamba wakati huo uliowekwa ulikuja mwaka wa 1914. Hata hivyo, mtu atauliza hivi, ‘Je! mwaka wa 1914 haukuweka alama ya mwanzo wa ongezeko la ole za ulimwengu, badala ya serikali kamilifu?’ Ndiyo maana yake hasa! Kuna uhusiano wa karibu sana kati ya kuja kwa Ufalme wa Mungu na matukio yenye hasara nyingi ya miaka ya karibuni, kama tutakavyoona sasa.
46 Kwa miaka kama 35 iliyokuwa imetangulia mwaka wa 1914, Mnara wa Mlinzi (sasa likiwa ndilo gazeti la kidini lenye kuenezwa zaidi kote kote duniani) limekuwa likivuta fikira kwenye mwaka 1914 kuwa mwaka uliotiwa alama na unabii wa Biblia. Matabiri hayo yalianza kutimizwa kwa njia yenye kutokeza sana katika mwaka wa 1914. Mojapo matabiri hayo ni unabii wa Yesu mwenyewe, uliotamkwa miaka 1,900 iliyopita, kuhusu “ishara” ambayo ingeonekana kwenye mwisho wa mfumo wa mambo na ambayo ingethibitisha kwamba yeye angekuwa amekuwapo bila kuonekana katika uwezo wa kifalme. Kwa kujibu swali la wanafunzi wake juu ya “ishara” hiyo, alisema: “Taifa litainuka juu ya taifa na ufalme juu ya ufalme, na kutakuwako upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi mahali hapa na mahali hapa. Mambo hayo yote ni mwanzo wa maumivu makali ya ghafula ya taabu.” (Mathayo 24:3, 7, 8, NW) Kwa utimizo wenye kuvuta fikira za watu, ya kwanza ya vita vya ulimwengu ikaanza mwaka wa 1914, ikileta uharibifu mkubwa sana mara saba kuliko vita vyote 900 vya miaka 2,500 iliyotangulia! Maumivu makali ya taabu yameendelea tangu wakati huo. Je! wewe umepata kuona uharibifu wenye kuletwa na vita, upungufu wa chakula, au lo lote la matetemeko makubwa ya ardhi ambayo yameisumbua dunia tangu mwaka wa 1914? Ikiwa ndivyo, umekuwa shahidi mwenye kujionea “ishara” ya “wakati wa mwisho” wa huu mfumo wa mambo.—Danieli 12:4.
47. Matukio yenye kutimiza “ishara” yameongezekaje katika miaka ya karibuni?
47 “Maumivu makali ya ghafula ya taabu” yameongezeka wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, iliyoleta uharibifu mkubwa mara nne kuliko Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, mpaka kuingia kipindi cha nyukilia, yakitimiza unabii zaidi wa Yesu: “Duniani huzuni kuu ya mataifa, wasijue njia ya kutokea . . . , huku wanadamu wakizimia kwa sababu ya hofu na kwa kutazamia mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa na watu.” (Luka 21:25, 26, NW) Ongezeko la uhalifu na uovu, kutokutii na watoto kuwa waasi, pia ongezeko la kukana kuwako kwa Mungu na la ukosefu wa adili—matukio hayo yenye kuogopesha yalitabiriwa pia kuwa alama ya “siku za mwisho” za mfumo huu wenye uovu.—2 Timotheo 3:1-5; Mathayo 24:12.
48. Ni nani mwenye kuleta ole mwingi ulio duniani, na kwa nini ole huo umeongezeka tangu mwaka wa 1914?
48 Hata hivyo, ikiwa serikali ya kimbingu ilisimamishwa mwaka wa 1914, sababu gani kuna taabu yote hii duniani? Mwenye kuileta ni Shetani Ibilisi. Kristo alipopokea uwezo wa Ufalme, hatua yake ya kwanza ilikuwa ni kupiga vita juu ya Shetani katika mbingu zisizoonekana. Matokeo ni kwamba, Shetani, “audanganyaye ulimwengu wote,” alivurumishwa chini pamoja na malaika zake kwenye ujirani wa dunia. Kwa kujua kwamba kuangamizwa kwake kunakaribia, anachochea matata makubwa duniani. Ni “ole . . . kwa dunia na bahari! Kwani yule Diabolo ameshuka kwenu mwenye gazabu nyingi kwa sababu anajua ana wakati mfupi tu.”—Ufunuo 12:7-9, 12, Zaire Swahili Bible.
49. (a) Ni nini litakalowapata wale “wanaoangamiza dunia”? (b) Yehova atatekelezaje “uamuzi wa hukumu” yake juu ya mataifa?
49 Je! kutakuwa na mwisho wa ole hizo? Ndiyo!—ni wakati serikali yenyewe ya mbingu, Ufalme wa Mungu Mwenye Nguvu Zote, utakapochukua hatua ya “kuwaangamiza wale wanaoangamiza dunia.” (Ufunuo 11:18, HNWW; Danieli 2:44) Mungu hataruhusu kamwe serikali za kisiasa, Wakristo wasio wa kweli, wala mtu mwingineye yote aharibu kazi yake ya mikono, yaani, dunia, kwa vyombo vya kinyukilia. Badala ya kufanya hivyo, yeye anatangaza hivi: “[Uamuzi wa hukumu yangu ni, NW] kuwakusanya mataifa, ili nizikutanishe falme, nipate kuwamwagia ghadhabu yangu; naam, ukali wote wa hasira yangu.” (Sefania 3:8) Kupitia Kristo wake, Yehova atatumia kani zote anazoongoza katika ulimwengu mzima wote katika kuleta uangamivu mkubwa sana kwa wote wanaomfuata Shetani duniani. Huo utapata dunia nzima, na utakuwa uangamivu ulio mkubwa kama vile Gharika ya siku za Noa.—Yeremia 25:31-34; 2 Petro 3:5-7, 10.
50. (a) “Har–Magedoni” ni nini? (b) Ni nani tu watakaookolewa katika Har–Magedoni?
50 Uangamivu huo unaitwa katika Biblia pigano la Mungu la Har–Magedoni. (Ufunuo 16:14-16) Watu wapole, wale tu wanaotafuta Yehova na uadilifu, ndio huenda wakaokolewa katika Har–Magedoni waingie Utaratibu Mpya wa Mungu wenye amani. (Sefania 2:3; Isaya 26:20, 21) Biblia inasema hivi kuhusu hao: “Wenye upole watairithi [dunia], watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) Hapo ndipo kazi tukufu na iliyo kubwa mno ya kurudisha Paradiso kwenye dunia hii itakapoanza!
Elimu ya Kuingia Katika Paradiso
51. Sababu gani ni lazima kwako uchukue hatua sasa?
51 Je! ungependa kuishi katika Paradiso? Ikiwa jibu lako ni ‘Ndiyo,’ utafurahi sana kujua kwamba Yesu aliposema juu ya mfumo wa leo wenye taabu na juu ya “ishara” ya kukaribia kwa uharibifu utakaoupata, aliongeza hivi, “Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” Angalau, watu fulani wa kizazi kilichoona “mwanzo wa utungu” mwaka wa 1914 wataishi waje waone Paradiso ikirudishwa duniani. (Mathayo 24:3-8, 34) Hata hivyo, ni uhakika wenye huzuni kwamba watu walio wengi leo wamo katika barabara pana inayoongoza kwenye uharibifu. (Mathayo 7:13, 14) Wanabaki na wakati mchache wa kubadilika. Unaweza kuwa mwenye shukrani kama nini kwa vile Yehova ametoa onyo mapema! Kwa sababu Yehova anataka wewe uje upate uzima, atakusaidia uchukue hatua zinazofaa.—2 Petro 3:9; Ezekieli 18:23.
52. Unahitaji nini ili uchague dini kwa hekima?
52 Jambo ambalo sasa unahitaji haraka ni maarifa sahihi. (1 Timotheo 2:4; Yohana 17:3, NW) Unaweza kuyapata wapi? Je! yanaweza kupatikana katika dini yo yote? Watu fulani wanasema dini zote zinaongoza kwenye mradi mmoja, kama vile njia zote za kupandia mlima fulani zinavyoongoza kwenye kilele. Wamekosea kama nini! Ili kupata njia inayofaa, wapanda-milima wanatumia ramani, na wanaajiri watu wa kuwaongoza. Hali kadhalika, kuna dini moja tu ya ukweli inayoongoza kwenye uzima wa milele, na mwongozo wahitajiwa ili kuiona.—Matendo 8:26-31.
53. (a) Ili uje upate uzima wa milele, ni lazima uendelee kufanya nini? (b) Huenda ukahitaji kushinda vishawishi gani kutoka kwa Shetani?
53 Broshua hii imetolewa na Mashahidi wa Yehova ikusaidie wewe. Imekwisha kusaidia wewe ufahamu kweli fulani za msingi za Biblia, sivyo? Bila shaka umejihakikishia mwenyewe kwamba kila jambo linategemea Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho yake. Sasa, ili ufanye maendeleo kuelekea mradi wako, ni lazima uendelee kujifunza. Kama vile elimu ya kilimwengu inayofaa ilivyo ya lazima ili imweke mtu mahali panapofaa katika jamii ya watu ya kila siku, vivyo hivyo elimu inayofaa ya Biblia ni ya lazima ili imweke mtu tayari kuingia katika jamii ya watu itakayookolewa iishi katika dunia ya Paradiso. (2 Timotheo 3:16, 17) Huenda Shetani akajaribu kuvuta fikira zako kando kwa kutumia washiriki wa karibu sana wakupinge au kwa kukushawishi uingie katika njia za kichoyo za kufuatia vitu vya kimwili au njia zisizo za adili. Usimkubalie Shetani. Usalama wako na wakati ujao wako wote na wa jamaa yako wategemea kujifunza kwako zaidi Biblia.—Mathayo 10:36; 1 Yohana 2:15-17.
54. Ni uandalizi gani zaidi wa kupata elimu ambao Yehova amefanya katika ujirani wako?
54 Zaidi ya kuendeleza funzo lako la Biblia, kuna njia nyingine ya kujifunza. Watu walio katika ujirani wako wanaopendezwa na elimu ya Biblia wanahudhuria kwa ukawaida mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Wote wanaohudhuria wanakuwa huko ili watwae mafundisho kutoka Biblia na wanajaribu kwa moyo mweupe wawe watu bora. Wanakaribisha kwa utayari wapya, wakisema, “Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova, mahali pake pa ibada] . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” (Isaya 2:3) Sababu nzuri za kuhudhuria mikutano ya Biblia zinaelezwa katika Waebrania 10:24, 25, panaposomwa hivi: “Tukaangaliane sisi kwa sisi na kuhimizana katika upendo na kazi nzuri; wala tusiache kukusanyika pamoja, kama ilivyo desturi ya wengine; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia.”
55. (a) Tengenezo la Yehova ni tofauti na mengine kwa njia zipi? (b) Ni kwa namna gani Mashahidi wa Yehova wana umoja kuliko watu wengine?
55 Unaposhirikiana na tengenezo la Yehova, utaona kwamba hali ni tofauti sana na ile ya mahekalu na makanisa. Hakuna kuomba-omba fedha, hakuna kusengenyana wala kugombana, na hakuna kubaguana kwa sababu ya hali ya jamaa au msimamo wa kifedha. Sifa iliyo yenye kutokeza kuliko zote kati ya Mashahidi wa Yehova ni upendo. Kwanza, wanampenda Yehova, na pili, wanapenda watu wengine. Hizo ni alama za kutambulisha walio Wakristo wa kweli. (Mathayo 22:37-39; Yohana 13:35) Imekupasa uhudhurie mikutano yao na kujihakikishia mwenyewe jambo hilo. Bila shaka utavutiwa na umoja wao. Ulimwenguni pote katika nchi zaidi ya 200, kuna Mashahidi zaidi ya milioni tatu. Hata hivyo, Mashahidi katika dunia yote wanafuata programu moja kwenye mikutano yao. Na kwa sababu ya uchapaji wa habari ile ile yenye kutokea wakati mmoja katika lugha nyingi, wengi wa Mashahidi wa Yehova katika ulimwengu wote wanajifunza kwenye mikutano yao ya kila juma masomo ya Kimaandiko yale yale katika muda wa saa chache baada ya wengine. Umoja wa tengenezo la Yehova ni muujiza wa kisasa katika ulimwengu uliogawanyika.
56. (a) Ni faida gani ambazo unaweza kupokea kwa kushirikiana na tengenezo la Yehova? (b) Matatizo yanapotokea, imekupasa utende namna gani? (c) Sababu gani ni jambo la maana kwako uweke maisha yako wakfu kwa Yehova?
56 Unaposhirikiana kwa ukawaida pamoja na watu wa Yehova, utahitaji ujivike “utu mpya” na kusitawisha tunda la roho ya Mungu—“upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” (Wakolosai 3:10, 12-14, UV; Wagalatia 5:22, 23, NW) Jambo hilo litakuletea uradhi wenye kina kirefu. Huenda mara kwa mara ukawa na matatizo unayohitaji kushinda kwa sababu unaishi katika ulimwengu wenye upotovu na pia kwa sababu ya kutokamilika kwako. Lakini Yehova atakusaidia. Neno lake linawahakikishia hivi, wale wanaojaribu kumpendeza kwa moyo mweupe: “Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu. Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Utavutwa na upendo wa Yehova, hata utataka umtumikie. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukuonyesha jinsi uwezavyo kuweka maisha yako wakfu kwa Mungu huyu mwenye upendo na kuwa mmoja wa mashahidi wake wenye kupendelewa. (Zaburi 104:33; Luka 9:23) Ndiyo, ni pendeleo. Ebu fikiria! Ukiwa mwabudu wa Yehova, unaweza kuufikia mradi wa uzima wa milele katika paradiso apa hapa duniani.—Sefania 2:3; Isaya 25:6, 8.
57. (a) Katika Utaratibu Mpya, ni uhusiano gani wa karibu sana utakaokuwapo kati ya Mungu na wanadamu? (b) Ni zipi kati ya baraka ambazo huenda ukaja kuzifurahia wakati huo?
57 Basi, endelea kujifunza na kukua katika upendo na uthamini wa Yehova Mungu, Mwanaye, na serikali ya kimbingu ya uadilifu. Katika kueleza habari za serikali ya Mungu na baraka ambazo itamiminia wanadamu, unabii wa Biblia unasema hivi: “Tazama, hema ya Mungu ni pamoja na watu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake, na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao.” “Mungu mwenyewe,” ambaye yuko juu sana kupita utawala wa leo wenye choyo, na wenye kuharibu mambo ya wanadamu, atakuwa karibu sana akiwa Baba mwenye fadhili kwa wote wale wanaopenda na kumwabudu yeye katika ule Utaratibu Mpya. Ndiyo, kutakuwako ile dini moja tu, ile ibada ya kweli ya Yehova Mungu, na waabudu wake watafurahia uhusiano wa karibu sana wa wana na Baba. Loo! jinsi atakavyojionyesha kuwa Baba mwenye upendo! “Naye atapanguza kila chozi katika macho yao; wala mauti haitakuwa tena; wala maombolezo, wala kilio, wala uchungu hautakuwa tena; kwa maana maneno ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4, ZSB.
58. Unaweza kuhakikishiwaje kwamba Yehova ‘atafanya vitu vyote kuwa vipya’?
58 Hivyo ndivyo utakavyokuwa umetimizwa ule muujiza mkubwa wa kusimamisha dunia-paradiso chini ya serikali kamilifu ya kimbingu. Ni hakika kama ulivyo uhakika wa kwamba jua litatokea na kushuka kesho. Kwa maana ahadi za Yehova Mungu, Muumba wa mbingu na dunia, ni “ya uaminifu na ya kweli.” Ndiye anayetangaza hivi, akiwa katika kiti chake cha ufalme mbinguni: “Tazama! mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.”—Ufunuo 21:5, NW.
Kwa kurudia broshua hii, wewe ungejibuje maulizo yafuatayo?
Biblia ni yenye kutokeza katika njia zipi?
Ulijifunza nini juu ya Mungu?
Yesu Kristo ni nani?
Shetani Ibilisi ni nani?
Sababu gani Mungu ameruhusu uovu?
Sababu gani mtu anakufa?
Wafu wamo katika hali gani?
Ukombozi ni nini?
Ufufuo utatokea wapi, na jinsi gani?
Ufalme ni nini, na utatimiza nini?
Ni nini iliyo “ishara” ya “umalizio wa mfumo wa mambo”?
Unaweza kujitayarishaje kuja kupata uzima wa milele katika Paradiso?
[Maelezo ya Chini]
a Marejezo ya Biblia yanayothibitisha mafungu yaliyo juu: (1) Matendo 17:26; Zaburi 46:9; Mika 4:3, 4; Isaya 65:21-23; (2) Isaya 65:25; 11:6-9; 55:12, 13; Zaburi 67:6, 7; (3) Ayubu 33:25; Isaya 35:5, 6; 33:24; Zaburi 104:24; (4) Isaya 55:11.
b Isipokuwa iwe imeonyeshwa vingine, nakili za Maandiko katika kichapo hiki zinatokana na Biblia ya Kiswahili ya Union Version.
c Monarchs and Tombs and Peoples—The Dawn of the Orient, ukurasa 25.
d Cyclopedia of Biblical, Theological, and Ecclesiastical Literature, cha J. McClintock na J. Strong, Buku la 8, ukurasa 908.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Akiwa uumbaji, mwanadamu ni bora kuwapita wanyama
[Picha katika ukurasa wa 18]
Yesu alilingana na Adamu mtu mkamilifu