Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 6/15 kur. 10-22
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WANADAMU HAWAKUUMBWA WATAWALE WANADAMU
  • MAMBO AMBAYO MTAWALA WA ULIMWENGU ANATAKIWA KUWA NAYO
  • KWA SABABU GANI UFALME WA MUNGU UMEKAWIA SANA?
  • KUWEKA MSINGI ULIO IMARA
  • SHERIA YA UFALME
  • KUONYESHA MATUNDA YA ROHO
  • KUPATA FAIDA ZA UFALME LEO
  • UMOJA WA UFALME
  • FAIDA ZENYE KUDUMU ZA UFALME
  • Ufalme wa Mungu Watawala
    Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele
  • Ufalme “Ambao Hautaangamizwa Milele”
    Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli
  • Mungu Amekuwa Akifanya Nini?
    Amani na Usalama wa Kweli—Wewe Unaweza Kuupataje?
  • Serikali ltakayoleta Amani Duniani Pote
    Furaha​—Namna ya Kuipata
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 6/15 kur. 10-22

Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe

“[Yehova] huwalinda wasio na hila . . . Nimrudishie [Yehova] nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?”​—Zab. 116:6, 12.

1. (a) Kusudi la serikali linapaswa kuwa nini? (b) Kwa sababu gani serikali Inahitajiwa kabisa?

JE! KUSUDI la serikali halipaswi kuwa kuwafaidi raia zake? Mwamerika ajulikanaye sana, George Washington, alisema kwamba “lengo la serikali zote ni kufurahisha jamii ya watu, na ikiwa hazina lengo hilo zinapaswa kuwa nalo.” Karne zilizopita wanadamu wameishi wakitawalwa na mamia ya serikali za namna mbali-mbali. Hakuna serikali yo yote iliyotimiza kabisa mahitaji ya watu wote. Lakini, hata kuwe kumetokea malalamiko ya namna gani, ni wazi kwamba ni afadhali kuwa na serikali ya namna fulani badala ya kuwa bila. Bila serikali kungekuwa na fujo; ingekuwa kama kwamba watu wenye ghasia wanatawala. Ikiwa wewe umeona watu wakifanya ghasia, unajua jinsi mambo yangekuwa​—kwa maana kunapokuwa na ghasia watu wanatumia nafasi hizo kufanya mambo ya chuki, pupa na ukatili mwingi, wakidhani hawawezi kuonekana wakati huo na kuadhibiwa.

2. (a) Ni kwa kadiri gani serikali za kibinadamu zimefaidi watu? (b) Ni mipango gani kutoka kwa Mungu imesaidia wanadamu kwa habari ya serikali?

2 Mungu wa mbinguni anajua hivyo. Na kwa kuwa ni afadhali kuwa na serikali ya mwanadamu badala ya kuwa na mchafuko wa utawala, Mungu ameruhusu serikali za dunia ziwepo maelfu ya miaka. Sana-sana, kuwapo kwa serikali kumefaidi watu kwa kuwapa usalama, ulinzi na utaratibu wa kadiri, na nafasi ya kujipatia riziki. Mungu alimfanya mwanadamu akiwa na tamaa ya kutaka utaratibu na dhamiri ya kutofautisha mema na mabaya. Vilevile ametumia Biblia kujulisha watu kanuni zake za haki, kwa hiyo mataifa mengi ya dunia yameweka nyingine za kanuni hizo katika katiba (constitution) zao. Katika kitabu cha Biblia cha Warumi, sura ya pili, mistari 14 na 15, tunasoma hivi: “Watu wa Mataifa wasio na sheria [yaani, sheria itokayo kwa Mungu moja kwa moja] wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia.”

3. (a) Serikali nyingi zimeonyeshaje kwamba zina kusudi zuri? (b) Lakini Biblia inasema nini juu ya tumaini halisi la kupata usalama? (Mt. 6:10)

3 Ndiyo sababu serikali nyingi zimeanza zikiwa na kusudi zuri. Zimejaribu kufaidi watu. Zimeandika katiba zenye sheria na kanuni nzuri. Lakini, hata ikiwa zimefanikiwa kwa njia fulani, serikali za kila mahali leo zinakubali kwamba taifa la wanadamu limeshindwa sana kupata usalama na amani ulimwenguni. Kwa sababu gani? Neno la Mungu, Biblia, linatoa jibu na ahadi ya kwamba maisha yenye furaha ya ulimwengu wenye umoja yataletwa bila shaka na ufalme wa Mungu, yaani, serikali yake itakayotawala wanadamu wote.

WANADAMU HAWAKUUMBWA WATAWALE WANADAMU

4. Kwa sababu gani leo hatuoni ulimwengu wenye raha? (Mit. 20:24)

4 Baada ya mwanadamu kuwako maelfu ya miaka, mbona hatuuoni ulimwengu wenye amani, ufanisi na furaha, unaotaminiwa na watu kila mahali? Unyenyekevu, matukio ya kweli ya maisha na unyofu unatulazimisha kukubali kwamba ni kwa sababu wanadamu wote si wakamilifu. Kosa si la watawala peke yao, bali watawalwa wana kosa pia. Ndiyo sababu jitihada za mwanadamu za kufanya dunia hii iwe makao yenye furaha kwa wanadamu wote zinapungukiwa sana zikilinganishwa na mambo ambayo Mungu ameahidi kufanya kwa kutumia utawala wake mwenyewe. Katika unabii wa Yeremia, sura ya 10, mstari wa 23, Biblia inasema hivi juu ya jambo hilo: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”

5. Ni geuzi gani la utawala lililoletea Israeli magumu?

5 Mumo humo ndani ya Biblia, usemi huo unahakikishwa na historia inayotoa juu ya serikali ya taifa la kale la Israeli. Taifa hilo lilikuwa na sheria kamilifu, waliyopewa na Mungu mwenyewe. (Rum. 7:12) Kwanza taifa hilo lilitawalwa na Mungu tu, akiwa Mfalme asiyeonekana, naye aliwakilishwa mbele ya watu na manabii na waamuzi. Lakini baadaye watu walitaka mfalme wa kibinadamu, mfalme ambaye wangeweza kumwona awape utukufu machoni pa mataifa mengine. Mungu aliwajulisha wazi kwamba jambo hilo lingewaletea matatizo mengi, pamoja na ukosefu mwingi wa uhuru. Ndivyo ilivyotukia. (1 Sam. 8:9-18) Hata mmoja wa wafalme wa Israeli yenyewe, mtu aliyechunguza maisha na matatizo yake bila mchezo, alisema “mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.”​—Mhu. 8:9.

6. Mungu aliwakusudia wanadamu wawe na utawala gani, na matokeo yamekuwa nini kwa sababu ya wanadamu kuruka mpaka huo?

6 Mbona inakuwa hivyo? Biblia inaonyesha ni kwa sababu hapo mwanzo Mungu hakukusudia wanadamu watawale wanadamu wenzao. Katika kitabu cha kwanza cha Biblia, Mwanzo, sura ya kwanza na mstari wa 28, Mungu aliambia wanadamu wawili wa kwanza ‘wazae, wakaongezeke, wakaijaze nchi, na kuitiisha; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.’ Mwanadamu alipaswa kutawala wanyama peke yao. Lakini wanadamu waliuruka mpaka huo wakajitwalia utawala juu ya wanadamu wenzao. Migogoro, uvunjaji sheria na vita vimetokea kwa sababu hiyo, huku pande zote mbili zikipingania utawala.

7, 8. Ni kwa njia gani Waisraeli ni kielelezo cha kuonyesha matokeo ya utawala wa wanadamu? (Mik. 7:2, 3)

7 Taifa la kale la Israeli ni kielelezo cha kufundisha wanadamu kwamba utawala wa mwanadamu hauwezi kamwe kuleta maisha yanayotafutwa na watu kila mahali. Katika taifa hilo watawala walitawala vizuri kwa muda. Lakini wakati ulipoendelea kupita na magumu makubwa yakatokea, watawala hao walianza kutegemea mambo mengine yawape hekima badala ya kumtegemea Mungu, wakaipuza sheria aliyokuwa amewapa waitumie kumaliza magumu yao. Walianza kutegemea hekima yao wenyewe na kusikiliza wanadamu wenye hekima ya kibinadamu tu. Mara nyingi watu hao walikuwa wakitaka kujifaidi wenyewe tu, tena walishauri watawala vibaya na kuwadanganya. Hawakuwaeleza mambo yalivyokuwa hasa. Watawala walipotaka kufanya mambo, washauri hao waliwakubalia tu wakisema “ndiyo-ndiyo, ndiyo-ndiyo,” kwa sababu ya kutaka kujipendekeza au kwa sababu ya woga. Wengine hata walifanya hila wapindue mtawala wao.​—Linganisha 1 Wafalme 12:8-19.

8 Kwa hiyo kutawala wanadamu kulilemea mno mwanadamu ye yote au baraza ya wanadamu, ingawa watu hao walikuwa na sheria kamilifu ya Mungu. Watawala walianza kusahau kufaidi watu. Watawala wachache tu ndio waliokuwa wanyofu wakajaribu kuleta mabadiliko mazuri. Lakini hawakuweza kuondoa matatizo kabisa.

9. Ni mageuzo gani yametukia ulimwenguni, nayo Mhubiri 1:15 inatumikaje leo?

9 Leo, tunaona hali gani? Njia za haraka sana za kuwasiliana na kusafiri zimefanya ulimwengu uonekane mdogo, kwa hiyo mataifa yanaelezana mapendezi yao, wala hakuna taifa linaloweza kujitenga kabisa, liwe peke yake. Mambo yanayotukia mahali pamoja yanawapata watu wa mahali penginepo. Serikali zinaweza kuchukua hatua ndogo-ndogo kugeuza mambo na kufanya hali zipendeze watu kidogo. Lakini msaada huo unakuwa wa kijuu-juu na wa muda mfupi tu. Mmojawapo watawala wenye hekima zaidi waliopata kuishi, yaani Mfalme Sulemani, alisema hivi katika Mhubiri 1:15: “Yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa, wala yasiyokuwapo [yanayokosekana, New World] hayahesabiki.” Ni kweli kwamba kuna magumu ya namna nyingi sana, na mawazo na mapendezi mengi yenye kupingana, tena kuna matukio mengi yasiyotazamiwa yanayofanya kusiwe na tengenezo la kibinadamu linaloweza kunyosha magumu ya ulimwengu, hata liwe na unyofu wa namna gani.

MAMBO AMBAYO MTAWALA WA ULIMWENGU ANATAKIWA KUWA NAYO

10. Ni nini kinachohitajiwa ili kuwe na serikali nzuri kabisa? (Mit. 29:2)

10 Basi, kuna tumaini gani la kupata serikali nzuri kabisa, yenye haki? Ili iweko, ni mambo gani yanayotakiwa? Kwanza, mtawala wake angepaswa kuwa na mamlaka kamili, bila kulazimika kupatanisha mawazo yanayopingana ya baraza ya wanadamu wasio wakamilifu. Angepaswa kuwa na sheria kamilifu, yenye haki kabisa. Hekima na upendo zingehitajiwa ili kufuata sheria na kuitumia kufaidi kila mtu. Ni mwanadamu gani leo anayeweza kutimiza matakwa hayo?

11. Mtawala mwenye kufanikiwa angehitaji kuwa na maarifa na mapendezi gani?

11 Mtawala mwenye kufaulu angehitaji pia maarifa kamili juu ya kila jambo, si juu ya mambo ya kibinadamu tu pamoja na hali zao na magumu yao, bali pia juu ya uumbaji wote. Kwa sababu gani? Kwa sababu mengine ya magumu yaliyo makubwa zaidi yasumbuayo watu yanahusu mazao ya dunia, uchafu na mazingira ya viumbe. Mtawala mwema angepaswa kufikiria kila mtu na kutaka kumwona akiwa na hali njema.

12. Kwa sababu gani ni jambo la maana sana mtawala ajue mambo yaliyo katika akili na mioyo ya watu? (Mat. 3:3. 4)

12 Tena, ili usimamizi wake ulete furaha na kutimiza mambo, mtawala angepaswa kujua mambo yaliyo katika akili na mioyo ya watu, kwa sababu ingempasa kuvuta mioyo yao ili wakubaliane naye kabisa. Sababu pia ni kwamba mapendezi ya watu mmoja mmoja ndiyo yanayokuwa mapendezi ya watu wote, na serikali haiwezi kuleta hali ya kutosheka wala furaha watu wote wasipofanya mambo kwa mapatano. (Mit. 14:28) Ili serikali iwe na amani, lazima kuwe na amani na umoja kati ya watu mmoja mmoja. Je! si ni wazi kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kuwa na maarifa yote na uwezo unaohitajiwa kutimiza mambo hayo?

13. (a) Ni nani peke yake anayeweza kuleta serikali ya kupendeza, na kwa sababu gani? (Zab. 127:1) (b) Ni jambo gani linaloonyesha kwamba Mungu anamfikiria sana kila mwanadamu na kupendezwa naye? (Mt. 6:26)

13 Basi, ni hakika kwamba Mtu mwenye uweza wote, yaani Muumba, Yehova Mungu, ndiye peke yake anayeweza kuleta serikali inayohitajiwa na wanadamu. Kwa habari ya maarifa ya Mungu juu ya jinsi mwanadamu alivyoumbwa, mtunga zaburi aliandika hivi katika Zaburi 139:3, 4, 16: “Umeelewa na njia zangu zote. Maana hamna neno ulimini mwangu usilolijua kabisa, [Yehova]. Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; chuoni mwako ziliandikwa zote pia, siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado.” Muumba peke yake ndiye anayejua akili na mioyo ya wanadamu. “[Yehova] huutazama moyo.” (1 Sam. 16:7) Mungu anamfikiria kila mmoja wetu na kupendezwa naye. Mithali iliyoongozwa na Mungu inasema, “Macho ya [Yehova] yako kila mahali; yakimchunguza mbaya na mwema.” (Mit. 15:3) Anafikiria watu kadiri gani? Yesu Kristo alisema: “Je! mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu; lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”​—Mt. 10:29-31.

14. Mungu anaonyeshaje anapendezwa na mambo ya dunia? (Matendo 17:26, 27)

14 Lakini huenda mtu akasema, ‘Kwa kuwa Mungu anauendesha ulimwengu huu ulio mkubwa ajabu, ambao dunia ni chembe yake, atakujaje karibu apendezwe na wanadamu vya kutosha hata aondoe magumu yote na kuleta mambo ambayo kila mwanadamu anahitaji?’ Jibu ni kwamba, Yeye anaweza kufanya hivyo kwa kutumia Ufalme utakaosimamiwa na Masihi wake, Yesu Kristo. Namna gani? Biblia inatusaidia kufahamu.

15. (a) Hapo mwanzo, Mungu alitawalaje? (b) Mungu atatumia njia gani kurudishia wanadamu serikali nzuri? (Dan. 4:17)

15 Hapo kwanza, Mungu ndiye aliyekuwa akitawala wanadamu moja kwa moja. Adamu alimwabudu Mungu wakiwa na ushirika kama wa Baba na mwanawe. (Luka 3:38) Adamu hakuhitaji hekalu lo lote duniani ili kumwabudu Mungu. Wala hakuhitaji mpatanishi ili apitie kwake anaposema na Mungu. Kwa kuwa alikuwa mwana wa Mungu, alikuwa na ushirika mwingi Naye, na bila shaka aliongea naye kila siku. (Mwa. 3:8) Lakini mwanadamu huyo aliasi akawa mchafu, akawa hafai kuwa mshiriki wa jamaa ya Mungu, basi akafukuzwa katika bustani aliyokuwa akikaa. Jambo hilo lilitenganisha wanadamu na Mungu. Lakini, Mungu hakuishiwa na nguvu za kuondoa hali hiyo mbaya. Alichagua kuanza mpango wa pekee wa kuwakilishwa na Ufalme. Ufalme huo ungerudisha ushirika wake na wanadamu na kuwarudishia hali inayowafaa katika serikali yake ya ulimwengu wote, wawe kama walivyokuwa mwanzoni.

KWA SABABU GANI UFALME WA MUNGU UMEKAWIA SANA?

16. (a) Ni maulizo gani yamefanya Ufalme ukawie sana? (b) Kwa sababu gani Mungu halazimishi watu wafuate ufalme wake kwa kutumia nguvu nyingi kama zile zinazotumiwa wakati wa mapinduzi ya haraka? (2Pe. 3:9)

16 Je! wo wote kati yetu wanashindwa kungoja na kuuliza, ‘Lakini mbona Mungu amekawia sana kutimiza kusudi lake?’ Ili kujibu inatupasa tuulize maulizo yanayofanana na hilo: Ingechukua muda gani kusimamisha serikali ambayo ingetawala dunia kwa haki kabisa? Ingechukua muda gani kuchagua watawala wa serikali hiyo na kuwazoeza? Tena, watu wangejulishwaje kwamba ufalme huo ni serikali yenye haki itokayo kwa Mungu? Watu wangepewaje ushuhuda wa kutosha hata waiamini serikali hiyo​—waone kwamba hali yake na kanuni zake zote zitawafaa​—waache iongoze maisha yao? Biblia inaonyesha kwamba Mungu halazimishi watu kufuata ufalme wake kwa kutumia uwezo mwingi sana kama ule unaotumiwa kupindua serikali kwa haraka nyingi sana. Bali Mungu anayafikiria maoni na haki za raia zake, kwa hiyo anawafundisha kwanza wafuate njia yake, akiwaongezea imani juu ya utawala wake wenye haki.

17. Kupatana na Mwanzo 3:15, kwa sababu gani haiwezi kusemwa kwamba Mungu amejikalia kitako bila jambo la kufanya?

17 Ndiyo sababu muda mwingi umepita kabla ufalme wa Mungu haujaletwa. Yehova Mungu hakuwa akijikalia kitako tu kama wengine wanavyodhani, bali amekuwa akichukua hatua moja moja tangu mwanadamu alipoasi mara ya kwanza, ili kuusimamisha kabisa ufalme huo. (Mwa. 3:15) Sasa anakaribia kumaliza matayarisho hayo. Fikiria mambo haya:

18. Kwa sababu gani wakati mwingi umepita kabla Mungu hajaleta amani?

18 Yehova ameahidi kwamba atasimamia dunia yote, alete amani na umoja. Lakini hatatawala watu kwa kutumia nguvu. Kusudi lake ni kufundisha watu wamjue na kunyenyekea usimamizi wake kwa moyo wa kupenda. Kwa hiyo, muda mwingi umehitajiwa ili kuweka msingi wa ulimwengu mzima wa wanadamu watakaoishi chini ya utawala wake wa Ufalme. Mungu anaonyesha neema kutujulisha kanuni za usimamizi wake wenye haki na jinsi unavyofanya kazi.​—Yohana 17:3.

19. Mungu asiyeonekana amejifunuaje kwa wanadamu? (Zab. 145:3-5)

19 Lakini Yehova ni Mungu asiyeonekana. (1 Tim. 1:17) Kwa hiyo, angetumia njia gani kuwapa wanadamu wenye nyama na damu ufahamu? Hangeonyesha tu uweza wake kwa kutoa sauti za kuogofya akiwa mbinguni. Bali, Mungu angetumia wakati kufunua kanuni na sifa zake kwa kufanya shughuli pamoja na watu. Inajenga, inasadikisha na kupendeza zaidi kusikia na kusoma habari za matangazo ya Mungu, na kuona katika maandishi ya kweli ya Biblia uhakikisho wa kwamba yeye anatimiza kwa haki mambo anayosema.

KUWEKA MSINGI ULIO IMARA

20. (a) Yehova ametufaidl kufanya mambo gani ya lazima? (b) Baada ya wanadamu kutawala maelfu ya miaka, ni jambo gani limehakikishwa waziwazi?

20 Hivyo, ili kuweka msingi wa serikali yake itakayotawala dunia yote, Yehova ametufaidi kwanza kwa kufanya mambo haya ya lazima: (1) kuweka msingi imara wa kuamini usimamizi ambao angeleta, (2) kutujulisha kanuni za serikali yake, (3) kutuonyesha sifa zake kama Mtawala wa ulimwengu wote na (4) kutambulisha Masihi ni nani kwa uhakika kabisa, ambaye ndiye angekuwa Mkombozi wa wanadamu na Mfalme mwenye kutawala kwa jina la Yehova. (Gal. 3:24) Wakati uo huo, kulinganishwa kwa matokeo ya utawala huo na utawala wa wanadamu muda wa maelfu ya miaka kumehakikisha kwamba utawala wa Mungu ni bora, unastahili na ni mnyofu.

21. Katika kuweka msingi, Mungu alitumia Israeli kwa kusudi gani?

21 Mungu alitumia njia gani kuweka msingi huo? Kwanza, alichagua taifa moja, wazao wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, yaani, taifa la Israeli wa kale. Yehova alijifunua akaonyesha sifa zake nzuri za haki na hekima alipoadhibu Israeli kwa sababu ya dhambi zao. (Rum. 10:21) Lakini aliwaonyesha pia sifa zake za upendo, rehema na ustahimilivu wakati wo wote walipotubu.

22. (a) Yehova alitimiza nini kwa kushughulika sana na Israeli? (b) Hata mataifa yenye Upinzani yangefaidikaje?

22 Historia ya Biblia inatuambia kwamba Mungu alishughulika na taifa la Israeli tu muda wa karne nyingi. Wao walikuwa na sheria yake; kisha walikuwa na kanuni za ibada ya kweli ya Yehova. Kwa kushughulika na Israeli karibu-karibu aliwaunganisha akahifadhi kweli yake duniani, huku mataifa mengine yakifuata njia yao wenyewe, yakifuata imani za uongo na ushirikina wa namna zote. Mungu alimtokeza pia mtu wa kuonyesha kwa maisha yake kwamba kanuni za serikali yake ni zenye haki, akaweka msingi ili Mfalme wa serikali hiyo atokee, yaani, Masihi. Wakati huo hakushughulika na mataifa yale mengine, isipokuwa walipojiingiza katika mambo ya taifa lake teule kwa njia fulani. Mengi ya mataifa hayo yalipinga vikali ibada ya Mungu na taifa la Israeli. Hawakujua kwamba Mungu alikuwa akitumia Israeli ili mwishowe wao wenyewe wapate hali njema, na kwamba katika wakati wake angeanza kushughulika nao pia.

23. Kuja kwa Masihi kulihakikishaje kwamba Mungu hakuwa amepoteza wakati?

23 Ndipo Masihi alipokuja, yule ambaye Mungu angemtumia aongoze utawala wa Ufalme. Yeye hakujitokeza mwenyewe duniani akijitangaza kwamba ndiye Masihi. Bali, Maandiko ya Kiebrania yalionyesha waziwazi kabisa kwamba Mwana wa Mungu ndiye aliyepaswa kuja akiwa Nabii mkuu na Mfalme wa Yehova. Kwa kuwa wanadamu walitakiwa kuwa na imani, vithibitisho vya maandiko hayo vilihitajiwa vionyeshe kwamba ndiye, kwa kutegemea shughuli za Mungu na wanadamu, tangu unabii wake wa kwanza katika Edeni na muda wote wa miaka 1,500 ya historia ya Israeli. Basi Mungu hakuwa amepoteza wakati bure. Maisha ya Yesu duniani yalihakikisha kwamba alitoka kwa Mungu. Ufufuo wake ulihakikisha kwamba alitukuzwa mbinguni, ili achukue mamlaka ya Ufalme katika wakati wake.

24. Kwa sababu gani imechukua wakati mwingi kuchagua wafalme wenzi wa Kristo?

24 Lakini Mungu alikusudia kuwe na watawala wengi katika Ufalme. Kristo ndiye angekuwa na mamlaka kamili, lakini Biblia inaonyesha katika Ufunuo 14:1-3, kwamba Mungu alikusudia watu wengine 144,000 wawe wafalme na wasimamizi pamoja na Kristo. Kama vile mtawala ye yote anavyofikiria sana watakaoshirikiana naye katika utawala kabla hajaanza kutawala, ndivyo Yesu alivyochagua mitume wake kwa uangalifu, watakaokuwa misingi midogo ya hiyo serikali mpya. Aliwatumia watu hao kuuhubiri ufalme wa Mungu katika Israeli yote, na baada ya kufa na kufufuliwa kwake ukahubiriwa kwa mataifa yote. Mpaka sasa, kwa muda mrefu uliopita Mungu amekuwa akichagua watu hao 144,000 watakaokuwa wafalme pamoja na Mwanawe. Lazima watu hao wawe na sifa bora kabisa kama Ufunuo 14:4, 5 unavyosema: “Hao ndio wamfuatao Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] kila aendako. Hawa wamenunuliwa katika wanadamu, malimbuko kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo. Na katika vinywa vyao haukuonekana uongo. Maana hawana mawaa.”

25. (a) Tunaona matokeo gani kwa sababu ya subira (uvumilivu) ya Mungu? (b) Ni faida gani zinazofurahiwa na mamilioni ya waliomo katika “mkutano mkubwa”?

25 Basi tunaona matokeo gani? Leo, tunaona habari njema za Ufalme zikitangazwa katika karibu pembe zote za dunia, tena tunaona watu wengi zaidi ya 144,000, naam, watu zaidi ya milioni mbili wakikusanyika pamoja kwa amani na umoja katika ibada ya kweli ya Mungu. Watu hao wanatangazia wengine wengi “habari njema.” Wana cheo gani katika kusudi la Mungu? Biblia inatuambia kwamba wao ni “mkutano mkubwa” watakaookoka wakati serikali za dunia zitakapopondwa na Ufalme uliofananishwa na “jiwe” lililotajwa na Danieli, wawe msingi wa “nchi mpya.” (Dan. 2:34, 35, 44) Wao ndio watakaokuwa wa kwanza kufurahia utawala wa Ufalme juu ya dunia, tena watakuwapo wakati wa utawala wa Kristo wa miaka 1,000 kukaribisha mamilioni ya wafu watakaofufuliwa na kuwasaidia wajifunze ibada ya kweli ya Mungu na kuifuata.​—Ufu. 7:9-17.

26. Mfano mdogo uliotajwa unatufaidije katika imani? (Yuda 20, 21)

26 Hata mfano huo mdogo wa matayarisho ambayo Mungu amefanya hatua kwa hatua ili kuwe na utawala wenye haki duniani unaonyesha kwamba Mungu hakuwa akijikalia kitako tu, bali amejenga serikali yake juu ya misingi imara na kuonyesha wanadamu mambo ya kutosha ili waweze kuijua serikali hiyo na kuiamini. Lakini tunapata ufahamu zaidi wa jambo hilo tunapozidi kuichunguza Biblia. Ni faida gani zinazofanya watu wawe raia za ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Yesu Kristo, kwa moyo wa kupenda?

SHERIA YA UFALME

27. Ni maulizo gani yanayotokea juu ya sheria ya Ufalme?

27 Serikali ya mbinguni inafanya kazi kwa kufuata sheria kama serikali zote. Lakini, sheria ya ufalme huo ni tofauti sana na sheria zenye kuonea watu ambazo zimetumiwa katika falme nyingi za kibinadamu muda wote wa historia. Watu wasio na maarifa huenda wakaogopa wakidhani kwamba sheria ya Ufalme huo itanyima watu uhuru wa kufanya mambo fulani. Lakini je! Ufalme huo utatunga sheria ya kunyima raia zake furaha za maisha? Je! utawawekea vizuizi vyenye kuwalemea, au watafurahi kikweli watakapokuwa wakiutii utawala wake?

28. (a) Yesu alionyeshaje kwamba hiyo ni sheria ya upendo? (b) Yesu aliwapa watu wa Mungu amri gani, na je! zinawawekea vizuizi?

28 Wakati Mfalme, Kristo Yesu, alipokuwa hapa duniani, alionyesha kwa maneno na matendo yake kwamba sheria ya Ufalme ingekuwa sheria ya upendo. Alihakikisha kwamba alikuwa na sifa zote ambazo mtu anayeweza kupewa mamlaka kamili anastahili kuwa nazo. Yesu alionyesha wazi kwamba Mungu ‘alimtoa Mwanawe pekee’ aje duniani kwa sababu Yeye “aliupenda ulimwengu [wa wanadamu].” (Yohana 3:16) Alisema hivi alipokuwa akinena habari za dhabihu aliyotoa mwenyewe kwa ajili ya wanadamu: “Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Aliwatia wanafunzi wake moyo wasitawishe sifa iyo hiyo ya upendo wa kujinyima. (Yohana 13:34, 35) Yesu alimwambia hivi mtu mmoja aliyemwuliza ulizo: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa [nafsi] yako yote, na kwa akili zako zote. Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. Na ya pili yafanana nayo, nayo ni hii, Mpende jirani yako kama nafsi yako. Katika amri hizi mbili hutegemea torati yote.” (Mt. 22:37-40) Je! amri hizo zinatuwekea vizuizi? Bila shaka, zinaweza kuzuia watu wa Mungu wasiumize au wasitaabishe wenzao, na bas! Faida zenye kuchangamsha moyo zitapatikana kwa kutii sheria hiyo ya Ufalme!

29. Tofauti na mataifa, kwa sababu gani Ufalme hautoi orodha yenye sheria nyingi? (Linganisha Warumi 6:14).

29 Roho hiyo ya upendo wa kujinyima imekwisha kuwapo kwa wingi kati ya Wakristo wa kweli, nayo inawaonyesha kuwa wanafunzi wa Yesu. Inafanya isiwe lazima kuwe na sheria nyingi za kuwazuia wasiruke mpaka. Sheria ya upendo inajenga na kufaidi watu, Itofautishe na maelfu ya sheria zilizo katika vitabu vya mataifa, zinazotumiwa kuzuia raia wakaidi. Sheria hizo zinatokeza ulizo kama lile lililowekwa katika jalada ya gazeti Newsweek mapema mwaka huu: Je! kuna “Sheria Nyingi Mno?”

KUONYESHA MATUNDA YA ROHO

30. (a) Kwa sababu gani Wakristo wa kweli wanasemwa kuwa raia (wananchi) wenye kutii sheria kuliko watu wengine wote’? (b) Mika anaonyesha nini juu ya matakwa ya Yehova?

30 Leo, Mashahidi wa Yehova wamekwisha anza kujitahidi sana kutumia sheria ya upendo kama wawezavyo katika hali yao ya kutokamilika. Hiyo si kusema kwamba hawatii sheria za mataifa wanamoishi. Sivyo hata kidogo! Kwa kweli, mahali pengi wamesemekana kuwa raia ‘wenye kutii sheria kuliko watu wengine wote.’ Kwa sababu gani? Kwa sababu sheria Ufalme, sheria ya upendo, imeandikwa juu ya mioyo yao. Kwa ajili ya dhamiri zao wanaheshimu na kutii “mamlaka iliyo kuu” ya mataifa na sheria zao, lakini wanaitii zaidi sana mamlaka iliyo kuu kupita zote, yaani, ya Yehova Mungu na ufalme wake unaosimamiwa na Kristo Yesu. Ufalme wa Mungu hauwalemei kwa kuwawekea sheria na vizuizi vyenye kuwalemea, kwa maana nabii Mika anaandika hivi akimthamini Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”​—Mik. 1:2; 6:8.

31. (a) Kwa sababu gani wazee wa ukoo hawakuhitaji orodha yenye sheria zilizoandikwa? (b) Je! watazihitaji sheria hizo watakapofufuliwa?

31 Maneno hayo yanatukumbusha juu ya wanaume waaminifu waliotembea na Mungu wa kweli nyakati za kale​—Habili, Henoko na Nuhu. (Ebr. 11:4-7; Mwa. 4:4; 5:22; 6:9) Waebrania sura ya kumi na moja inaonyesha kwamba walimpendeza Mungu kwa imani yao. Baadaye, Ibrahimu, Isaka na Yakobo walipewa sheria juu ya utakatifu wa damu na juu ya tohara. (Mwa. 9:4; 17:9-14) Lakini imani waliyoonyesha kwa kutii amri za Mungu ndiyo iliyoonyesha walistahili kupewa nafasi ya kuwa raia za Ufalme. (Mwa. 18:18, 19) Mtume Paulo anatuambia hivi: “Kwa imani Ibrahimu . . . aliitika . . . akikaa katika hema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ile ile. Maana alikuwa akiutazamia mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu.” (Ebr. 11:8-10) Wazee hao wa ukoo hawakuhitaji sheria nyingi zenye kuwazuia walipokuwa duniani miaka zaidi ya 3,500 iliyopita, wala hawatazihitaji kamwe ili kuhakikisha kwamba ni wenye imani watakapofufuliwa watumikie kama “wakuu” katika dunia itakayokuwa paradiso.​—Zab. 45:16.

32. Ni kwa njia gani utawala wa Mungu una faida kuliko utawala wa wanadamu?

32 Kutokana na yote hayo tunaweza kuona tofauti kubwa kati ya utawala wa Mungu na utawala wa mwanadamu. Utawala wa ufalme wa Mungu unasihi watu wafuate tabia njema, nao wanaokubali wanautii kwa sababu ya kumpenda Mungu na jirani zao. Huo ni utawala wenye kuunganisha watu. Kunakuwa na matokeo mazuri sana kati ya wale wanaoutii sana ufalme huo wa mbinguni. Ni ufalme wenye faida. Unaweza kuona hivyo kwa kutazama jinsi kusanyiko la Mashahidi Wakristo wa Yehova linavyopatana kwa upendo. Kwa upande mwingine, utawala wa mwanadamu unategemea sheria nyingi zenye kuzuia watu, ambazo huenda zikawa na faida fulani lakini watu wanazitii kwa kunung’unika au kwa sababu ya kuogopa adhabu, wala si kwa kupenda. Watu wengi wakiona wanaweza kuponyoka wanadharau sheria, na miaka ya majuzi wakuu wa serikali wamekuwa kati ya wenye kufanya hivyo​—watu wale wale wanaopaswa kuwa wa kwanza kutii sheria.

33. Ulimwengu umezionaje faida wanazopata watu wa Mungu kwa kuitii sheria ya ufalme wa Mungu? Taja mifano yo yote.

33 Watu wa ulimwengu wamestaajabishwa mara nyingi na faida ambazo Mashahidi wa Yehova wanapata kwa sababu ya kutii sheria ya ufalme wa Mungu. Kwa mfano, makala moja iliyokuwa katika gazeti Des Moines Register, Iowa, ilieleza habari za “Utumishi Mtakatifu” Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova lililofanywa katika mji huo kiangazi cha mwaka 1976, ikasema hivi:

“Mtazamaji aliyekuwa na maoni mabaya juu ya [Mashahidi wa Yehova] maisha yake yote alihudhuria kusanyiko la majuzi lenye Mashahidi karibu 8,000 katika jumba Veterans Auditorium ambako watu hawakuwa wakiruhusiwa kwenda zamani.

“Alistaajabishwa na matukio kama haya:

“● Usawa wa mataifa yote na ushirika wa Watu wa namna zote za maisha.

“● Urafiki na uchangamfu wa Mashahidi ambao walitumia upendo kujaribu kusadikisha watu badala ya kuwalaumu, ingawa wanasadiki wao peke yao ndio wenye ile kweli.

“● Mipango mizuri ya kusanyiko, lenye watu karibu 2,200 waliojitolea kufanya kazi mbalimbali, kuanzia kazi ya kusugua sakafu mpaka ya kupika vyakula. . . . Wao wana usemi mzuri unaosema, ‘Sikuzote sisi tunajaribu kuacha jumba likiwa katika hali bora kuliko tulivyolikuta.’

“● Kuwapo kwa mamia ya watoto wa umri mbalimbali walioketi kwa unyamavu mpaka mwisho wa mikutano mirefu sana, huku wazazi​—walioshika Biblia na vijitabu vya kuandikia​—wakisikiliza sana . . . hotuba.”

34. Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova wanafurahia umoja mwingi sana, na huo ni mfano mdogo wa nini?

34 Umoja huo wenye kustaajabisha, unaoonekana duniani pote kati ya Mashahidi wa Yehova peke yao, ni mojawapo faida wanazopata kwa sababu ya kutii ufalme wa Mungu kwanza na kuifuata sheria ya upendo ya ufalme huo. Huo ni mfano mdogo wa mapatano na upendo utakaositawi kati ya ulimwengu mzima wa wanadamu watakaokuwa chini ya utawala wa ufalme wa mbinguni.

35. Uumbaji wote utakujaje kuitegemea kabisa enzi kuu ya Yehova? (Ufu. 4:11)

35 Wakati ufalme huo wa Kimasihi wa miaka elfu utakapokwisha timiza kusudi lake la kukamilisha wanadamu katika paradiso ya dunia yote, ndipo maneno haya yanayohusu Kristo yatakapotimizwa: “Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake . . . ili kwamba Mungu awe yote katika wote.” (1 Kor. 15:24-28) Ndipo viumbe vyote vitakapotegemea kutii Utawala Mkuu wa Mfalme wa milele ili viendelee kuishi.

KUPATA FAIDA ZA UFALME LEO

36. Imeonyeshwaje kwamba ufalme wa Mungu unaweza kuunganisha watu katika upendo? (Rum. 13:10)

36 Hata sasa, kabla ya kuitawala dunia miaka elfu, ufalme wa mbinguni unawapa faida nyingi sana wafuasi wake washikamanifu, wanaomkubali Yesu kuwa Mfalme wao. Wao hawana migawanyiko tena kwa sababu ya kujivunia mataifa yao wala kwa sababu ya chuki. Waliacha zamani ugomvi na chuki za kikabila. Kisa kilichotukia katika vijiji viwili vya Mexico kinaonyesha namna sheria ya Ufalme inavyofanya kazi. Miaka kadha iliyopita wanavijiji walikuwa na bastola na bunduki za kutumia nyakati za ugomvi kati ya makabila, na watu walikuwa wakiuawa-uawa. Mapolisi walishindwa kuzuia mambo hayo. Ndipo jamaa moja ilipokubali kujifunza Biblia na mhudumu wa Mashahidi wa Yehova aliyekuwa akiwatembelea. Mwishowe, karibu kila mtu kijijini alianza kujifunza akazikubali kweli za Biblia. Baada ya muda mfupi hali za ukatili zilikwisha kukawa na hali za urafiki. Wanakijiji waliuza silaha zao wakatumia pesa walizopata kununua Biblia. Kwa njia hiyo waliungana kwa upendo wakiwa chini ya ufalme wa Mungu.

37. Hasa katika karne hii, faida za umoja wa Kikristo zimeonyeshwaje?

37 Umoja wa kweli wa Kikristo unaonekana waziwazi pamoja na faida zake, huku mataifa ya dunia yakiuana ndugu na ndugu. Katika mapigano yaliyobarikiwa na viongozi wa dini karne hii ya 20, mara nyingi Wakatoliki waliua Wakatoliki wenzao, Waprotestanti wakaua Waprotestanti wenzao, na wafuasi wa Buddha wakaua wafuasi wenzao wa Buddha. Lakini sivyo Mashahidi wa Yehova. Umoja wao umekuwa halisi, nao umehakikisha kwamba ufalme wa Mungu ndiyo serikali ya pekee inayoweza kuunganisha watu wa mataifa na makabila yote.​—⁠Isa. 2:2-4.

38. Ufalme umewafaidije wale waliokuwa watumwa wa Babeli Mkuu hapo kwanza?

38 Ufalme huo umekomboa pia umati mkubwa wa watu wenye mioyo minyofu katika utumwa wa dini za Kibabeli na mafundisho yake. Tunaposema dini za Kibabeli tunamaanisha dini zote duniani ambazo mafundisho na desturi zake zilianza katika Babeli ya kale, iliyokuwa chanzo cha dini zote za uongo. Mafumbo na ushirikina ulio katika dini nyingi za leo zenye madhehebu mbalimbali, pamoja na Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani, yalitoka Babeli. Lakini sasa ‘Babeli Mkuu,’ yaani, milki ya kisasa ya dini ya uongo ulimwenguni pote, inaelekeana na uharibifu. Mungu anawapa amri hii wale wampendao: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” (Ufu. 18:2, 4) Ufalme wa mbinguni unatusaidia tuache dini za uongo kabla Mungu hajaleta hukumu juu ya taratibu nzima ya Kibabeli.

39. Yesu alipendekeza Wakristo wawe na lengo gani, nasi tutaepushwaje na utafutaji wa mali tukilifuata shauri lake?

39 Ufalme unatusaidia pia tujitenge na mtego wa kutafuta sana mali. Unatusaidiaje? Katika Mahubiri yake juu ya Mlima yajulikanayo sana, Yesu alitaja ‘mambo ambayo Mataifa huyatafuta’ kwa bidii. Alisema kwamba sikuzote maulizo wanayofikiria ni “Tule nini? au Tunywe nini? au Tuvae nini?” Lakini je! hayo ndiyo mambo ya maana zaidi? Hapana, kwa maana Yesu aliendelea kusema: “Utafuteni kwanza ufalme [wa Mungu], na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mt. 6:31-33) Kwa hiyo, lengo letu likiwa kuendelea kuutafuta Ufalme​—kwa kuchunguza habari zake, kwa kuutii sana na kutumikia faida zake​—Baba wa mbinguni atahakikisha kwamba tumepata riziki yetu.​—1 Tim. 6:6-8.

40. Mafundisho ya Ufalme yanatulindaje kwa habari ya tabia na afya?

40 Faida nyingine tunazoweza kuletewa na Ufalme ni ulinzi wa tabia na wa kimwili. Wale wanaoishi kulingana na “habari njema” wanajiangalia waendelee kuwa na tabia safi. Ama sivyo hawawezi ‘kuurithi ufalme wa Mungu.’ (1 Kor. 6:9-11) Hivyo wanalindwa wasiwe na anasa zenye madhara wala magonjwa yenye kuogofya ya kaswende na kisonono yanayopatikana kwa kulalana na watu ovyo-ovyo, tena wanaepuka maumivu ya moyo na ya dhamiri yanayotokana na kuvunja sheria ya Mungu. Kwa kufuata amri ya mitume ya ‘kuendelea kujiepusha na damu’ wanaendelea kuwa na dhamiri njema mbele za Mpaji-Uzima Mkuu, na kulindwa wasiambukiwe na ugonjwa wa kufura ini na magonjwa mengine ambayo watu wanapata wanapotiwa damu mishipani.​—Matendo 15:20, 28, 29.

41. Kutumia kanuni za Ufalme katika maisha ya jamaa kunasaidiaje?

41 Kwa kuacha kanuni za Ufalme ziongoze maisha yao ya jamaa, watumishi wa Yehova wanaepuka masikitiko mengi yanayotokea jamaa zinapoharibika katika ulimwengu huu wa ki-siku-hizi. Biblia inatia jamaa moyo zikae pamoja, zipashane habari, zifurahie maisha zikiwa pamoja, zimtumikie Mungu zikiwa pamoja. (Kol, 3:14, 18-21) Inazionyesha vizuri jinsi zinavyoweza kufanya hivyo. Ingawa United States iliandikisha talaka milioni moja mwaka 1976, na ingawa uasi wa watoto na magumu mengine ya jamaa yaliongezeka sana, jamaa nyingi za Mashahidi wa Yehova ziliweza kuepuka magumu hayo. Kwa sababu gani? Kwa sababu wanatumia sheria ya Ufalme katika maisha yao.

42. Taja mifano yo yote kuonyesha namna ujumbe wa Ufalme unavyosaidia katika magumu ya maisha.

42 Mara nyingi wapya wanaojifunza kweli za Ufalme wamefaidika pia kwa kupata uongozi unaofaa juu ya jinsi ya kutatua magumu ya maisha. Mwanamke aliyepata talaka kabla ya kujifunza habari za ufalme wa Mungu, kisha akawa na kazi ngumu ya kulea vivulana wawili katika ulimwengu usio na huruma, anaandika habari zifuatazo juu ya namna ujumbe wa Ufalme ulivyomfaidi:

“Nilitaka tu kuwajulisha kwamba nashukuru sana kuwa katika kundi la Yehova. Ningependa sana watu wengine waliotalikiana ulimwenguni wamjue Yehova na kufahamu kwamba kuna mtu anayeweza kuwapenda mara elfu zaidi wakimpenda yeye, anayempa mtu sababu ya kutaka kuendelea kuishi. Hakuna mahali penginepo ulimwenguni unapoweza kupata watu wenye upendo kama katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Nami namshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya kumwongoza dada aliyekuja mlangoni kwangu miaka saba iliyopita, kwa sababu ya kuruhusu kazi ya kuhubiri iendelee, na kwa sababu ya kutoleta dhiki kubwa upesi. Unamshukuruje mtu kwa sababu ya kuokoa uhai wako?”

UMOJA WA UFALME

43. Umoja wa jamaa au kundi zima unaletaje faida?

43 Kuwa na umoja katika jamaa na katika kundi la Kikristo kunaweza kuleta faida kwa njia nyingi. Huko nyuma siku zilizotangulia gharika, je! Nuhu alifanya kazi akiwa peke yake? Hapana, jamaa nzima ilifanya kazi pamoja, ikaokoka pamoja na kumshukuru Yehova pamoja. (Mwa. 8:18, 20) Wakati Musa alipotenganisha maji ya Bahari ya Shamu, je! alivuka peke yake? Hapana, kundi zima la Israeli lilikuwa likisafiri pamoja naye; nalo lilivuka bahari pamoja likiwa chini ya ulinzi wa Yehova. (Kut. 14:29-31) Faida kama hizo zinaweza kupatikana leo jamaa na makundi yakiwa na umoja katika ushirika wenye upendo ambao Neno la Mungu linatutia moyo tuwe nao.​—Linganisha Matendo 2:46, 47.

44. Tunaweza kupata faida gani za pekee kwa kuendelea kukusanyika pamoja wakati wa hatari?

44 Wakati wa hatari au mateso, umoja huo unaleta faida za pekee. Mfano mmoja ni huu: Wakati wa vita kati ya vyama Lebanoni, Mashahidi wa Yehova wa nchi hiyo walikaa pamoja wakaona maajabu. Wakati wa kusanyiko la wilaya, Mashahidi 117 walikusanyika katika nyumba ya mtu fulani. Mara tu baada ya dada wa mwisho kuingia, kombora lilianguka hapo hapo mlangoni Lakini wote walisalimika. Wakati wote wa mkutano, makombora na risasi zilimiminwa karibu na nyumba hiyo kama maji, zikang’oa vigingi vya umeme na kuponda-ponda majengo yaliyokuwa karibu, lakini hakuna hata moja iliyogonga nyumba walimokusanyika. Wakati mwingine, nyumba za jamaa mbili za Mashahidi wa Yehova zilikuwa katika eneo lililokuwa likimiminiwa makombora. Walizungumza waone kama watajihatirisha waende mkutanoni, lakini wakaamua ‘kutoacha kukusanyika pamoja.’ (Ebr. 10:25) Waliporudi nyumbani walikuta nyumba moja ikiwa imeharibiwa kabisa na kombora, na ile nyingine ikiwa imeharibiwa sana na risasi zenye kulipua marisaa hivi kwamba asingaliokoka mtu kama angalikuwa ndani. Walipoteza mali zao zote, lakini wee, waliponya maisha yao!

45. Tunawezaje kufaidika kutokana na ushirika sasa na wakati wa “dhiki kubwa?”

45 Je! hiyo maana yake ni kwamba Mashahidi wa Yehova watalindwa kimwili sikuzote, chini ya hali zote? Si lazima iwe hivyo. Mashahidi wa Yehova wasiopungua wawili waliuawa na mwoteaji mwenye bunduki katika Lebanoni, na nyakati nyingine wengine wao wamekufa katika misiba kama ya matetemeko ya ardhi. Lakini, kwa ujumla, mambo yaliyowafaidi ni kumtegemea Yehova katika sala, umoja wao katika kundi na kutulia wanapokuwa katika mikazo. (Flp. 4:5-7) Huo umekuwa mfano mdogo wa ulinzi ambao Mungu anaahidi kuwapa watu wake wakati wa “dhiki kubwa,” wakati Ufalme utakapochukua hatua ya kuharibu mataifa yenye upinzani.​—Mt. 24:21, 22; Dan. 2:44.

46. Watu, wa Mungu kwa ujumla wanaweza kutazamia ulinzi gani wakati Yehova atakapoleta hukumu, na kwa sababu gani? (Sef. 2:3; 3:8)

46 Mpaka sasa hatujui jinsi Ufalme utakavyofanya mwujiza huo wa kutulinda. Lakini manabii wa Mungu wanahakikishia watu wake watii kwamba watafaidika milele kwa kumtumaini Yehova kabisa. Hivyo Yehova anamtumia nabii wake Isaya kutoa ukaribishaji huu: “Njoni, watu wangu, ingia wewe ndani ya vyumba vyako, ukafunge mlango nyuma yako ujifiche kitambo kidogo, mpaka ghadhabu hii itakapopita. Kwa maana, tazama, [Yehova] anakuja kutoka mahali pake, ili kuwaadhibu wakaao duniani, kwa sababu ya uovu wao; ardhi nayo itafunua damu yake, wala haitawafunika tena watu wake waliouawa.” (Isa. 26:20, 21) Bila shaka Yehova ataleta hukumu zake na kuokoa watu wake.​—Zab. 119:155, 156.

FAIDA ZENYE KUDUMU ZA UFALME

47. Kupatana na Isaya 48:17, sasa watu wa Mungu wanafurahia faida gani zilizoahidiwa?

47 Sasa “mkutano mkubwa” wa watu wanamkubali Yesu Kristo kuwa Mfalme wao. Amewaonyesha jinsi ya kuishi maisha safi na kuwa wafanya kazi wenye furaha katika faida za ufalme wa Baba yake. Amewaingiza katika ushirika bora sana pamoja na Baba yake, anayewaambia hivi: “Mimi ni [Yehova] Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.” (Isa. 48:17) Yehova anatumia Neno lake la unabii kuonyesha watu wake jinsi wanavyoweza kutembea kwa usalama siku hizi zinazoitangulia “dhiki kubwa.”

48. (a) Ni jambo gani ambalo watu wa Mungu leo wanahitajiwa wafanye kwa haraka? (b) Inatupasa sasa tulithamini onyo gani la Yesu, na kwa sababu gani?

48 Watu wote wanaomtafuta Mungu wanapaswa kufanya haraka waikimbie taratibu mbovu ya mambo ya leo, kisha wakae mbali nayo! Ingawa bado hatuwezi kujitenga nayo kimwili, tunaweza kuonyesha tumejitenga kwa kuepuka njia za maisha ya kujifaidi wenyewe tu na ya kutafuta sana mali. Ili tuokoke ni lazima tufanye hivyo. Anapomalizia unabii wake, Yesu anatuonya hivi kulingana na masimulizi ya Luka: “Jiangalieni, mioyo yenu isije ikalemewa na ulafi, na ulevi, na masumbufu ya maisha haya; siku ile ikawajia ghafula, kama mtego unasavyo; kwa kuwa ndivyo itakavyowajilia watu wote wakaao juu ya uso wa dunia nzima. Basi, kesheni ninyi kila wakati, mkiomba, ili mpate kuokoka katika hayo yote yatakayotokea, na kusimama mbele za Mwana wa Adamu.”​—Luka 21:34-36.

49. Masimulizi ya Marko na Mathayo yanakaziaje onyo la Yesu?

49 Masimulizi ya Marko ya unabii wa Yesu yanataja maneno haya ya mwisho: “Kesheni, . . . asije akawasili ghafula akawakuta mmelala. Na hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.” (Marko 13:35-37) Nayo ripoti ya Mathayo inasema hivi: “Jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja.”​—Mt. 24:44.

50. Kwa sababu gani inatupasa ‘tuinue vichwa vyetu juu’ hata nyakati zenye wasiwasi?

50 “Mwana wa Adamu,” Kristo Yesu, anasema kwamba katika wakati ambao mataifa yatakuwa na hofu nyingi na huzuni kuu, watamwona Mwana wa Adamu akija katika mawingu, akiwa na mamlaka na utukufu mwingi. Anatuambia hivi: “Mambo hayo yaanzapo kutokea, changamkeni, mkaviinue vichwa vyenu, kwa kuwa ukombozi wenu umekaribia.” (Luka 21:28) Naam, tutakombolewa na ufalme wa Mungu tutoke katika hii taratibu mbovu ya mambo! Tutakombolewa na ufalme wa Mungu tuingie katika paradiso duniani​—ambamo Ufalme utamininia wanadamu baraka muda wa miaka elfu! Nayo matokeo ya baraka hizo za Ufalme yatadumu mpaka kale na kale.

51. Ni ushirika gani uliokuwa kati ya Mungu na wanadamu utakaorudishwa?

51 Lakini Biblia inasema kwamba kusudi la Mungu ni kurudisha utawala wake wa asili, wa moja kwa moja, juu ya wanadamu. Inaonyesha kwamba “jiwe” linalotajwa na Danieli, linalofananisha Ufalme, “lilichongwa” likatoka katika “mlima,” ambao ni enzi kuu ya Mungu, kwa kusudi la kutetea enzi yake kuu ya ulimwengu wote na kuuanza tena huo uhusiano mwingi sana wa asili, juu ya dunia. Basi, jambo hilo litatukiaje? Wanadamu wote watakuwaje tena kama Adamu​—wawe wana wa Mungu, waweze kusema naye moja kwa moja, bila kupitia kwa mpatanishi ye yote?

52. Ni matumaini gani wanayopewa watu wa Mungu kama yanavyoonyeshwa na 1 Wakorintho 15:24-28?

52 Katika 1 Wakorintho 15:24-28, Neno la Mungu linaonyesha kwamba Ufalme utakapokwisha tetea enzi kuu ya Mungu juu ya dunia na kuonyesha kwamba ulimwengu wote ni wenye haki, ndipo Kristo atakapomrudishia Yehova Ufalme huo, ili kwamba “Mungu awe yote katika wote.” Ndipo Yehova atakapompa Yesu na wenzake 144,000 utumishi mwingine. Wakaaji wa dunia watakaolipita jaribu la mwisho watamheshimu Yesu milele kama wakili mkuu wa Mungu wa kuirudishia dunia cheo kinachoifaa katika ulimwengu wote, huku wakimtumikia Yehova Mungu katika ibada safi yenye kutakata.

53. (a) Lazima tuseme nini juu ya faida ambazo zitaletwa na ufalme wa Mungu? (b) Tunatiwa moyo tuchukue msimamo gani, na tuna tumaini gani lililo zuri sana?

53 Kwa kutazama maajabu hayo yote yatakayotimizwa, je! unadhani kuna kitu kingine kinachoweza kukufaidi zaidi ya ufalme wa Mungu? Hakika inakupasa sana umshukuru Yehova kwa sababu ya mpango huo wenye upendo mwingi. Unaombwa usimame sasa upande wa ufalme wa Mungu unaosimamiwa na Yesu Kristo, kwa imara na ushikamanifu, uzipate faida zake mpaka kale na kale!

​—Kutoka The Watchtower, January 15, 1978

[Picha katika ukurasa wa 14]

Katika Japan, katika Ujeremani, katika Nigeria​—ndiyo, kote kote katika dunia hii​—ufalme wa Mungu unatangazwa

[Picha katika ukurasa wa 18]

Zaidi ya kuwa na faida za sasa zinazoletwa na Ufalme, kuna tumaini la kuwa na maisha yenye utulivu katika taratibu mpya ya Mungu

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki