Sura 6
Mungu Amekuwa Akifanya Nini?
1. Watu wengi leo wanaamini nini juu ya Mungu, lakini je! ni kweli?
WATU wengi leo wanaamini kwamba Mungu hapendezwi na dunia kwa vitendo au kwamba hafanyi lo lote juu ya matatizo yanayowasumbua wanadamu. Lakini ukweli ni kwamba Mungu anajali sana. Kweli, labda hakufanya yale ambayo wanadamu walimtazamia kufanya. Lakini hiyo haimaanishi kwamba hakuna lo lote amefanya. Kwa kweli, tangu mwanzo wa historia ya kibinadamu mpaka wakati huu wa sasa yeye amekuwa akiwafanyia wanadamu mambo.
2. Ufupi wa muda wa maisha ya watu unaweza ukawafanya waoneje juu ya jambo hilo?
2 Sababu moja inayowafanya watu wengine waone kwamba Mungu hafanyi lo lote ni muda wao wenyewe wa maisha ulio mfupi. Jambo hilo lawafanya wakose subira na kutaka mambo yafanyike katika muda wao mfupi ambao maisha yanawaruhusu. Kwa hiyo tamaa ya kuona mabadiliko katika muda wa maisha yao wenyewe inatawala kufikiri kwao. Basi, elekeo lao linakuwa kumhukumu Mungu kwa msingi wa ujuzi huo wa kibinadamu wenye mapungufu mengi sana.
3. Urefu wa maisha ya Yehova unahusuje uwezo wake wa kushughulika na hali katika wakati unaofaa zaidi?
3 Kwa upande mwingine, Yehova anaishi milele. (Zaburi 90:2, 4; Isaya 44:6) Akiwa mahali pake pa kutazamia mambo, yeye anaweza kuona ni wapi hasa katika mkondo wa wakati ambapo vitendo vyake vitatimiza faida iliyo kubwa zaidi kwa kila mtu anayehusika na vilevile vilikuze kusudi lake kwa matokeo yaliyo makubwa zaidi. (Isaya 40:22; 2 Petro 3:8, 9) Hivyo barabara ndivyo Mungu amekuwa akifanya.
Namna Mungu Amejifunua Mwenyewe
4. Yehova ametangaza kusudi lake kuwa nini, na kwa hiyo ni maarifa gani ambayo ameandalia wanadamu?
4 Kusudi la Yehova ni kuandalia uumbaji wote usimamizi wenye uadilifu utakaounganisha wanadamu katika amani na umoja, wakifurahia usalama kamili. (Waefeso 1:9, 10; Mithali 1:33) Hata hivyo, Mungu halazimishi mtu ye yote aje chini ya usimamizi wake. Ni wale tu wanaomtumikia na kupenda njia ya utawala wake wanaokaribishwa. Ili kuweka msingi kwa ajili ya ulimwengu mzima ambao ungeishi kulingana na viwango vyake vya uadilifu, Mungu ameandalia wanadamu maarifa ya viwango hivyo na ya namna usimamizi wake unavyotenda kazi. Wakati uo huo Mungu amekuwa akiwawezesha wanadamu wapate maarifa yaliyo muhimu juu yake mwenyewe na sifa zake za kibinafsi.—Yohana 17:3.
5. Twaweza kujifunza nini juu ya Mungu kutokana na kazi za uumbaji?
5 Kwa kuwa Yehova ni roho, bila shaka yeye hawezi kuonekana na wanadamu. Kwa hiyo, yeye angewafanya wanadamu wenye mwili na damu wayafahamuje mambo hayo? Kwanza, mambo mengi yaweza kujulikana juu ya sifa za Muumba kutokana na kazi ya mikono yake. (Warumi 1:20) Mahusiano mazuri ajabu yaliyo miongoni mwa vitu vilivyo hai na sheria zinazoongoza vitu vyote vyenye maumbo yanashuhudia hekima yake. Uwezo mwingi ajabu unaodhihirika katika zile bahari kuu, katika hali ya hewa, na katika nishati ya nyota unatoa ushahidi wa kwamba yeye ni mwenye nguvu zote. (Ayubu 38:8-11, 22-33; 40:2) Na namna mbalimbali za vyakula vya kulipendeza kaakaa la kinywa, uzuri wa maua, ndege, kucha na kuchwa, na tabia zenye kupendeza za wanyama—vyote vinasimulia juu ya upendo wa Muumba kwa wanadamu na kutamani kwake tuone furaha katika maisha. Hata hivyo kujifunua kwa Mungu mwenyewe hakukomi kwa mambo hayo.
6. (a) Ni kwa njia gani Mungu ameandaa mafunuo ya wazi juu ya mapenzi yake? (b) Ni kwa njia gani nyingine Mungu amefunulia mwanadamu kanuni na sifa zake?
6 Katika vipindi mbalimbali yeye mwenyewe amesema pia kutoka kwenye mbingu. Mara nyingine alifanya hivyo yeye binafsi. Mara nyingine alisema kupitia malaika, kama alivyofanya katika Mlima Sinai katika Peninsula ya Uarabu, ambako aliwapa mamilioni ya Waisraeli sheria yake. (Kutoka 20:22; Waebrania 2:2) Ndipo, kupitia manabii wake akawasiliana na wanadamu kwa muda wa karne nyingi, na akawaagiza waandike mafunuo ya mapenzi yake. (2 Petro 1:21) Hivyo, Yehova amewajulisha wanadamu pole kwa pole viwango Vyake vya uadilifu na mapenzi Yake. Upande mmoja wa maana kuhusu jambo hilo ni njia ambayo amezifunua kanuni na sifa zake kupitia shughuli zake na wanadamu. Jambo hilo limefanya Neno lake la maandishi livutie zaidi kwa kuwa na matukio yanayolingana na maisha halisi ya kibinadamu. Lo! jinsi kuwamo katika maandishi ya Biblia mifano iliyo hai inayotusaidia kufahamu mapenzi yake vizuri zaidi kunatufundisha na kutusadikisha zaidi ya kusoma matangazo ya kusudi la Mungu! (1 Wakorintho 10:11) Na maandishi hayo yanafunua nini?
7. (a) Mungu ameonyeshaje kwamba yeye havumilii ukosefu wa uadilifu milele? (b) Tunapojua namna Mungu anavyouona mwenendo kama huo, imetupasa tufanye nini?
7 Yanaandaa ushahidi wa kwamba Mungu havumilii ukosefu wa uadilifu milele. Kweli, yeye aliwaacha wazao wa Adamu na Hawa wafuate njia yao wenyewe, wakijenga kumbukumbu lisiloepukika la kutoweza kwa mwanadamu kujitawala mwenyewe kwa mafanikio. Lakini Mungu hakuwaacha wanadamu pasipo ushahidi wa hukumu Yake dhidi ya njia zao za ukosefu wa uadilifu. Hivyo alileta gharika katika siku za Noa kwa sababu ‘dunia ilikuwa imejaa jeuri.’ (Mwanzo 6:11-13, NW) Aliiangamiza miji ya Sodoma na Gomora yenye kushusha maadili. (Mwanzo 19:24, 25; Yuda 7) Aliliacha taifa la Israeli, lililojidai kumtumikia, liingie katika uhamisho kwa sababu walizoea dini ya uwongo. (Yeremia 13:19, 25) Tunapojua namna Mungu anavyoutazama mwenendo huo, tunakuwa na nafasi ya kufanya mabadiliko katika maisha zetu kuonyesha upendo wetu kuelekea mambo yanayofaa. Je! tutafanya hivyo?
8. Mungu anapoleta uharibifu, je! wanakuwako waokokaji wo wote? Toa mfano.
8 Maandishi ya Biblia yanafunua pia kwamba Mungu anatofautisha kati ya waadilifu na waovu. Katika ile Gharika ya duniani pote, Mungu hakumwangamiza Noa, aliyekuwa “mhubiri wa uadilifu,” bali alimwachilia yeye na wengine saba. (2 Petro 2:5, NW) Na, kabla moto na kiberiti havijanyeshea Sodoma, njia ya kuokokea ilifanywa iwezekane kwa Loti mwenye uadilifu na watu wa nyumba yake.—Mwanzo 19:15-17; 2 Petro 2:7.
9. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Israeli wa kale?
9 Wakati watu wa Israeli, waliokuwa wameapa kutumikia Mungu, walipothibitika kuwa si waaminifu, yeye hakuwatupilia mbali mara hiyo. Kama alivyowaambia: “Nimewatuma watumishi wangu wote manabii kwenu ninyi, nikiamka mapema kila siku, na kuwatuma.” Lakini hawakusikiliza. (Yeremia 7:25, 26) Hata wakati wa kuuharibu Yerusalemu ulipokaribia, Yehova alisema: “Je! mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? . . . si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi? . . . Basi ghairini, mkaishi.”—Ezekieli 18:23, 32.
10. Zaidi ya kuwa mwenye subira, ni mambo gani mengine ambayo masimulizi hayo ya Biblia yanatufundisha juu ya Mungu?
10 Basi, twaona nini? Kwamba katika njia inayovuta sana moyo wa watu wenye elekeo la uadilifu, Yehova ameonyesha wazi subira kuu aliyo nayo kwa wanadamu. Wakati uo huo, shughuli zake pia zinakazia kwa nguvu sana juu yetu kwamba anapenda uadilifu na ni jambo la maana tuishi kupatana na matakwa yake.
11. (a) Ni usemi gani wenye kusudi ambao Yehova alifanya katika Edeni? (b) Tangu wakati huo Mungu amekuwa akifanya nini?
11 Jambo jingine, la msingi sana, linatokeza waziwazi. Tangu mwanzo inakuwa wazi kwamba Mungu amekuwa na kusudi fulani la wazi katika kila jambo ambalo amefanya. Naye hajashindwa hata kidogo kutenda wakati utimizo wa kusudi lake ulipotaka kitendo kifanywe. Kusudi hilo la msingi lilisemwa mle mle Edeni. Alipokuwa akipitisha hukumu juu ya Shetani, Yehova alitabiri kwamba Shetani angekuwa na nafasi ya kutokeza “uzao,” wale ambao wangeonyesha tabia zake na kumuunga mkono. Pia alitabiri kutokezwa kwa “uzao” mwingine, mkombozi mwenye uadilifu. Mmoja huyu angemtia jeraha la kifo “nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani,” hivyo awafungue wanadamu kutoka utawala wake wenye kuharibu. (Mwanzo 3:15; Ufunuo 12:9) Baada ya kutangaza rasmi hiyo taarifa ya kusudi, Yehova alianza kufanya matayarisho halisi ya usimamizi wa hatimaye juu ya dunia chini ya “uzao” ulioahidiwa. Kama tutakavyoona, kazi hii ya kutayarisha ingechukua wakati.
Sababu Gani Alishughulika na Israeli wa Kale Peke Yao
12, 13. (a) Kwa sababu gani Mungu alichagua Israeli na akalipa taifa hilo moja tu sheria zake? (b) Kwa hiyo, twaweza kujifunza nini kutokana na historia ya Israeli na kutokana na ile ya mataifa mengine?
12 Muda mrefu kabla ya kuwako mataifa ya leo, Mungu alichagua taifa moja ambalo alilitumia kwa mamia ya miaka kama watu wake mwenyewe. Kwa sababu gani? Ili aandae wonyesho ulio hai wa utendaji wa kanuni zake za uadilifu. Taifa hilo, Israeli wa kale, lilikuwa la wazao wa Abrahamu, mtu aliyekuwa ameonyesha imani kuu katika Muumba. Yehova aliwaambia hivi: “[Yehova, NW] hakuwapenda ninyi, wala hakuwachagua ninyi, kwa sababu mlikuwa wengi kuliko mataifa yote, maana mlikuwa wachache kuliko watu wote; bali kwa sababu [Yehova, NW] anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu.”—Kumbukumbu 7:7, 8; 2 Wafalme 13:23.
13 Alipokwisha kuwakomboa kutoka utumwani katika Misri, Yehova aliwatolea nafasi ya kuwaingiza ndani ya uhusiano wa pekee pamoja naye, nao wakajibu hivi: “Hayo yote aliyoyasema [Yehova, NW] tutayatenda.” (Kutoka 19:8) Ndipo Yehova alipowapa marekebisho yake, hivyo akawatenga kando na mataifa mengine yote na kuwaandalia habari zenye maelezo mengi kuhusu viwango vyake vya uadilifu. (Kumbukumbu 4:5-8) Kwa hiyo, historia ya Israeli wa kale inaandaa maandishi ya jambo linalotukia wakati sheria za Mungu za uadilifu zinapotiiwa au zisipotiiwa. Wakati uo huo, historia ya mataifa mengine inafunua matokeo yanayowapata wale wanaoishi bila sheria ya Mungu.
14. (a) Je! Mungu aliyakosea mataifa yasiyo ya Kiisraeli kwa kutokuingilia mambo yao? (b) Hata hivyo, yalipataje manufaa kutokana na fadhili zisizostahilika za Mungu?
14 Namna gani mataifa hayo mengine? Yalifuata njia yao wenyewe, yakijichagulia namna zao wenyewe za serikali. Watu wao hawakuachwa kabisa bila wema wo wote katika maisha zao. Bado walikuwa na uwezo wa dhamiri, na nyakati nyingine hiyo iliwaongoza wawatendee wanadamu wenzao kwa huruma. (Warumi 2:14; Matendo 28:1, 2) Lakini dhambi yao ya kurithi na kukataa kwao mwongozo wa kimungu iliwafanya wafuatie mwendo wa kujitafutia mambo ya kibinafsi, hilo liliongoza kwenye vita vyenye ukatili na mazoea yenye kushusha maadili. (Waefeso 4:17-19) Hakika Mungu hangeweza kuonwa kuwa mwenye daraka juu ya ole mwingi ulioletwa na mwendo wa maisha waliojichagulia wenyewe. Nyakati zile tu Mungu alipoingilia mambo ni wakati ambapo utendaji wa kibinadamu ulipingana na hatua za kutimizwa kwa makusudi yake. Kwa wakati uliokuwapo, Mungu aliwaruhusu kwa fadhili wawe na ushiriki katika furaha ya kuishi, katika mazuri ya uumbaji na mazao ya dunia.—Matendo 14:16, 17.
15. Ni mipango gani ya kuwabariki hatimaye watu wa mataifa hayo ambayo Mungu alikuwa anaendelea kutayarisha?
15 Wala Yehova hakuwazuia watu wa mataifa hayo wasipokee hatimaye manufaa zilizoahidiwa kupitia “uzao” wa Abrahamu. Yehova alisema hivi juu ya “uzao” huo ambao ungekuja kupitia ukoo wa jamaa ya Abrahamu: “Katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:18) Kwa hiyo ingawa Yehova alikuwa akishughulika na Israeli peke yao, bila upendeleo alikuwa anaendelea kutayarisha kusudi lake ili awabariki mataifa mengine wakati ujao, ingawa hawakujua jambo hilo.—Matendo 10:34, 35.
16. (a) Wakati wote huo, Mungu alikuwa akifanya nini kwa habari ya ahadi juu ya ule Uzao? (b) Uzao huo wa ahadi ulithibitika kuwa nani?
16 Kwa muda ambao Yehova alikuwa akishughulika na Israeli wa kale, yeye aliandaa mambo mengi ya unabii yaliyojaza uhitaji muhimu kwa watu wenye imani—jinsi ya kutambua Uzao wa Abrahamu ulioahidiwa wakati alipofika hatimaye. Hata ukoo wake, kupitia kabila la Yuda na nyumba ya Daudi, ulionyeshwa wazi. (Mwanzo 49:10; Zaburi 89:35, 36) Mahali pa kuzaliwa kwake, Bethlehemu, palitajwa kwa jina. (Mika 5:2) Mwaka ule ule wenyewe ambapo angepakwa mafuta awe Masihi ulionyeshwa karne nyingi mapema. (Danieli 9:24-27) Utumishi wake wa kikuhani kwa ajili ya wanadamu ulionyeshwa kimbele. Ndivyo na kujidhabihu kwake mwenyewe kulikowafungulia watu wa mataifa yote nafasi ya kupata uzima wa milele. (Waebrania 9:23-28) Hivyo, wakati uliowekwa rasmi ulipofika, bila kukosea kila kitu kilionyesha kwamba Yesu Kristo ndiye Uzao wa ahadi ambaye kupitia kwake baraka zingewajia wanadamu wote hatimaye.—Wagalatia 3:16, 24; 2 Wakorintho 1:19, 20.
Kutayarisha Watawala kwa Ajili ya Wanadamu
17. Mungu alikuwa akifanya mpango wa kutokeza nini kupitia Yesu, na hili lilitiliwaje mkazo wakati wa kuzaliwa kwake?
17 Kabla ya kuzaliwa kwa Yesu, Mariamu mama yake alikuwa ameambiwa na malaika wa Mungu kwamba mwana wake angepewa ufalme wa milele. Wachungaji karibu na Bethlehemu walijulishwa juu ya kuzaliwa kwake, kisha wakasikia kundi la majeshi ya mbinguni likimsifu Mungu likisema: “Utukufu katika vimo vya juu kwa Mungu, na duniani amani miongoni mwa watu wa nia njema.”—Luka 1:31-33; 2:10-14, NW.
18. (a) Ni katika njia gani mambo yaliyompata duniani yalimtayarisha kwa vyeo vya kuwa mfalme na kuhani? (b) Kifo chake kilikuwa na matokeo gani juu ya kupata amani?
18 Fikiria manufaa za kwamba Mfalme huyo wa kimbingu wa wakati ujao alipata kuishi duniani. Akiwa mwanadamu alikuja kuyajua na kuyafahamu matatizo ya wanadamu. Aliishi na akafanya kazi pamoja nao, akishiriki kihoro chao na mwenyewe akipatwa na ugumu. Alithibitisha ushikamanifu wake kwa Yehova na upendo wake kwa uadilifu akiwa chini ya majaribu yaliyo makali zaidi ya yote. Kwa njia hiyo Mungu alikuwa akimtayarisha Yesu awe Mfalme mwenye ufahamu na vilevile Kuhani Mkuu ili atoe kwa wanadamu manufaa zenye kupa uzima. (Waebrania 1:9; 4:15; 5:8-10) Zaidi ya hilo, kwa kudhabihu uhai wake mwenyewe, Yesu Kristo aliwafungulia wanadamu njia ya kupata tena mahusiano yenye amani pamoja na Mungu.—1 Petro 3:18.
19. (a) Twajuaje kwamba Yesu alifufuliwa na akapaa mbinguni? (b) Kwa habari ya ufalme wake, alifanya nini alipokwisha kurudi mbinguni?
19 Baada ya kifo cha Yesu, Mungu alimwinua kwenye uzima tena, na akaonekana na mashahidi wa kibinadamu zaidi ya 500 ambao wangeweza kutoa ushuhuda wa kwamba ufufuo ulikuwa umetukia kweli. (1 Wakorintho 15:3-8) Siku 40 baada ya Yesu kuinuliwa, yeye alipaa kuelekea mbinguni na akatoweka kutoka kwenye macho ya wanafunzi wake wenye kutazama. (Matendo 1:9) Alianza kutumia ufalme wake kuelekea wafuasi wake mwenyewe waaminifu akiwa mbinguni, na manufaa za utawala wake ziliwatofautisha wazi na wanadamu wengine wote. Lakini je! sasa ulikuwa wakati wake kuanza kuyatawala mataifa? Hapana, kwa maana mambo mengine katika programu yenye fahari ya Mungu yalitakwa yaangaliwe.—Waebrania 10:12, 13.
20. Ni kazi gani mpya ambayo Yesu alikuwa ameanzishia wanafunzi wake duniani?
20 Kazi kubwa ilibaki kufanywa duniani pote. Kabla ya kufa na kufufuliwa kwa Yesu, hakuna Waisraeli waliokuwa wametoka kama wahubiri kwenda kuwageuza watu wa mataifa mengine. Lakini wo wote waliotamani kuikubali ibada ya Yehova wangeweza kushiriki manufaa pamoja na Israeli. (1 Wafalme 8:41-43) Hata hivyo, kuja kwa Ukristo kulifungua shughuli mpya kubwa. Yesu Kristo mwenyewe aliuweka mfano na kuwaachia wanafunzi wake kama wasia, akiwaambia hivi kabla ya kupaa kwake mbinguni: “Mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Yerusalemu na katika Yudea yote na Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8, NW.
21. Badala ya kugeuza ulimwengu, Mungu alikuwa akitimiza nini kwa njia ya kazi hiyo ya kutoa ushuhuda?
21 Je! lengo lilikuwa kuugeuza ulimwengu? Hapana. Badala yake, Yesu alionyesha kwamba wakati wa kipindi hicho mpaka moja kwa moja ndani ya “umalizio wa mfumo wa mambo” kungekuwa kukusanywa kwanza kwa “wana wa ufalme.” Ndiyo, ilikuwa lazima washiriki wale wengine wa serikali ya Ufalme inayokuja wachaguliwe. (Mathayo 13:24-30, 36-43, NW) Ye yote anayesoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo aweza kuona kwa utayari kwamba kuanzia Pentekoste ya 33 W.K., wengine walikuwa wakialikwa kushiriki pamoja na Yesu Kristo katika utawala wake wa Ufalme wa kimbingu.—2 Timotheo 2:12; Waebrania 3:1; 1 Petro 1:3, 4.
22. (a) Ni sifa gani ambazo Mungu alitaka kwa hao wanaotazamiwa kuwa warithi wa Ufalme wa kimbingu? (b) Kwa hiyo, je! uchaguzi huo ulifanywa kwa haraka-haraka?
22 Kuchagua hao watawala-wenzi watakaokuwa juu ya wanadamu wakati ujao kungechukua wakati. Kwa sababu gani? Kwanza, nafasi hiyo ilipasa kutolewa kwa watu wa mataifa yote. Na, ingawa wengi walidai kuwa waliishika, wachache ndio waliothibitika kikweli kuwa wafuasi waaminifu wa Mwana wa Mungu. (Mathayo 22:14) Ilikuwa lazima viwango vya juu vitimizwe. Ingawa Wakristo hawajaishi kama taifa lililotengwa kando na watu wengine kama Waisraeli wa kale, wao wameonwa kuwa kama wageni, wakifuata njia nyingine ya maisha. (1 Petro 2:11, 12) Ni lazima wadumishe usafi wa kujitenga na mazoea yasiyo ya adili na yenye ufisadi ya ulimwengu unaowazunguka. (1 Wakorintho 6:9, 10) Ili wawe “wana wa Mungu” kweli kweli, inawapasa wajionyeshe wenyewe kuwa ‘wenye kuamanika,’ wasishiriki katika vita vya mataifa wala kulipa kisasi wakati wanapoteswa kwa sababu ya imani yao. (Mathayo 5:9; 26:52; Warumi 12:18, 19) Ni lazima waonyeshe ushikamanifu kwa utawala wa Mungu, kwa kukataa kujionyesha kama wenye kuziunga mkono serikali za kisiasa za wanadamu, ambazo katika Biblia zinaonyeshwa kuwa kama ‘wanyama.’ (Ufunuo 20:4, 6) Kwa sababu ya yote hayo, na kwa sababu wamelifuata sana jina la Yesu Kristo katika jukumu lake akiwa Mfalme mpakwa mafuta wa Mungu, wao wamekuwa “vitu vya kuchukiwa na mataifa yote.” (Mathayo 24:9, NW) Kwa hiyo, wale watakaokuwa watawala wa kimbingu wa wanadamu pamoja na Kristo hawakuchaguliwa kwa haraka-haraka.
23. (a) Ni wangapi watakaokuwa katika hilo baraza la usimamizi la kimbingu pamoja na Kristo? (b) Wamechaguliwa kutoka kati ya nani, na kwa sababu gani?
23 Sababu ambayo imefanya kuchaguliwa kwao kuchukue muda mrefu sana si kwamba hesabu yenye kuchaguliwa ingekuwa kubwa. Kulingana na Maandiko, Mungu aliweka kikomo cha hesabu ya hilo baraza chaguliwa la usimamizi lililo chini ya Yesu Kristo liwe na watu 144,000 tu. (Ufunuo 14:1-3) Lakini Mungu amewachagua kwa uangalifu. Wamechukuliwa kutoka “kila kabila na lugha na jamaa na taifa.” (Ufunuo 5:9, 10) Miongoni mwao mna watu wa namna zote za maisha, wanaume na wanawake, watu ambao wameshiriki matatizo yote mbalimbali ya wanadamu. Hakuna hata tatizo moja ambalo halijapata wengine kati yao na wakalishinda wakati wa kuuvaa utu mpya wa Kikristo. (Waefeso 4:22-24; 1 Wakorintho 10:13) Lo! tunaweza kufurahia jambo hilo kama nini! Kwa sababu gani? Kwa sababu linatupa sisi uhakikisho wa kwamba watakuwa wafalme na makuhani wenye huruma na rehema, wawezao kuwasaidia wanaume na wanawake wa aina zote wapate manufaa kutokana na uandalizi wa Mungu wa uzima wa milele.
24. Namna gani mamilioni ya watu wengine walioishi na wakafa wakati wa muda huo, wengi kati yao wakiwa hawana habari juu ya Biblia?
24 Namna gani wanadamu walio nje ya mpango huo? Wakati wa muda huu wote, Mungu hakuziingilia serikali mbalimbali. Aliwaacha wanadamu wafuate njia ambayo walichagua. Bila shaka, mamilioni ya watu waliishi na wakafa, wengi kati yao wasisikie hata kidogo juu ya Biblia au juu ya Ufalme wa Mungu. Hata hivyo Mungu hakuwa amewasahau. Yeye alikuwa akitayarisha kwa ajili ya wakati uliosemwa na mtume Paulo: “Nina tumaini kuelekea Mungu . . . kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15, NW) Ndipo, chini ya hali zenye kufaa za Mfumo Mpya wa Mungu, wangepewa nafasi kamili ya kujifunza njia za Yehova. Kwa kutegemea hilo, wangeweza kuchukua msimamo wa kibinafsi juu ya suala la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima. Wale wanaopenda uadilifu wangeipata nafasi ya kuishi milele.
Wakati “Ule Mwisho” Unapokaribia
25, 26. (a) Ni mamlaka gani zaidi ambayo Kristo angepewa katika wakati unaofaa, naye angechukua hatua dhidi ya nani? (b) Hiyo ingehusuje hali duniani?
25 Kabla ya kuja kwa Mfumo Mpya huo, matukio yenye kusisimua lazima yatukie. Biblia ilitabiri mabadiliko ya maana katika mambo ya ulimwengu. Yesu Kristo angetawazwa kama mfalme wakati huo, si ili atawale juu ya wanafunzi wake tu, bali akiwa na mamlaka ya kuchukua hatua kuuelekea ulimwengu mzima. Tangazo lingefanywa mbinguni hivi: “Ufalme wa ulimwengu ukawa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atatawala akiwa mfalme milele na milele.” (Ufunuo 11:15, NW) Hatua ya kwanza ya Mfalme ingekuwa dhidi ya “mtawala wa ulimwengu” mwenyewe, Shetani Ibilisi, na mashetani wake. (Yohana 14:30, NW) Majeshi hayo maovu yangevurumishwa chini kutoka kwenye mbingu na kuzuiliwa kwenye ujirani wa dunia. Matokeo yangekuwa nini?
26 Masimulizi ya kiunabii yana maandishi ya kwamba sauti moja kutoka mbinguni ilisema: “Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Kungetukia miongoni mwa mataifa msukosuko usiopata kuwa na mfano wake, lakini ule mwisho usingekuja mara hiyo.
27. (a) Wakati “ule mwisho” ungekaribia, ni kazi gani ya kutenganisha ambayo ingetukia, na namna gani? (b) Uharibifu wa ulimwengu uliotabiriwa utakuwa mkubwa kadiri gani?
27 Huo ungekuwa wakati wa kazi kubwa ya kutenganisha. Chini ya uongozi wa Yesu Kristo aliyetawazwa, wafuasi wake waaminifu wangeisukuma kazi ya kuhubiri “habari njema hizi za ufalme” ndani ya dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya ushuhuda kwa mataifa yote. Watu kila mahali wangepewa nafasi ya kuonyesha mwelekeo wao juu ya utawala wa kimungu. (Mathayo 24:14, NW; 25:31-33) Kazi hiyo ikiisha kutimizwa, “ndipo ule mwisho utakapokuja,” kama Yesu alivyoeleza. Itakuwa “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.” (Mathayo 24:21) Wanadamu hawatauliza hivi tena, Mungu amekuwa akifanya nini? Watakaookolewa peke yao watakuwa ni wale waliojali vya kutosha wakataka kujua jambo alilokuwa akifanya na wakapatanisha maisha zao na matakwa yake kabla ya uharibifu wa ulimwengu kufika.
28. (a) Kutawazwa kwa Kristo na kutengwa kwa watu wa mataifa yote kunatukia wakati gani? (b) Kwa hiyo, ni jambo gani ambalo ni la haraka kwa wewe kama mtu mmoja kufanya?
28 Lakini mambo hayo yatatukia wakati gani? Ni wakati gani Kristo anapopewa uwezo wa kutawala akiwa Mfalme na kuanza kutenganisha watu wa mataifa yote? Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba Mungu amekuwa akifanya mambo hayo wakati wa karne hii ya 20. Kristo amekwisha kuwa katika kiti chake cha enzi cha kimbingu, na sasa kazi ya kutenganisha inakaribia ukamilisho. Wakati wa kujitambulisha mwenyewe kuwa uko upande wa Yehova wa suala la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ni mfupi sana. “Dhiki kubwa” iko karibu! Uchunguzi wa uangalifu wa unabii wa Biblia kwa msaada wa historia ya karibuni unathibitisha jambo hilo kuwa kweli. Tunakuhimiza ulifikirie kwa uangalifu.
[Picha katika ukurasa wa 62]
Kwa kuishi miongoni mwa wanadamu, mtawala mpya wa dunia akawafahamu wanadamu vizuri zaidi