Miaka 6,000 ya Kutimizwa kwa Ajabu kwa Kusudi la Yehova juu ya Wanadamu
WAKATI Adamu alipokataa waziwazi enzi kuu ya Yehova yenye kustahili, Yehova alitendea wanadamu kwa njia yenye rehema na upendo. Hakumwua Adamu papo hapo na kuanza kuumba tena mtu mwingine akae hapa duniani badala yake. Bali, Mungu alichagua kumruhusu Adamu aendelee kuishi na kuanza kuzaa jamaa ya kibinadamu. Jamaa hiyo iliyotokana na Adamu ‘ilitiishwa chini ya ubatili’ na Mungu kwa sababu ilipata laana ya mauti kwa kuirithi kwa Adamu. Wanadamu wenyewe wasingeweza kupata njia yo yote ya kujikomboa na hali hiyo yenye huzuni. Lakini, walitiishwa chini ya ubatili “katika tumaini,” kwa sababu Mungu alikusudia kuwe na njia ya kutokea kwa waaminifu kati ya wazao wa Adamu, kwa sababu ya fadhili zake zisizostahilika na zisizo na kifani. Kwa njia hiyo wangeweza “kutolewa katika utumwa wa uharibifu” na kuingizwa katika “uhuru wa utukufu” wakiwa watoto wa Mungu waliorudishwa. Tumaini hilo la ajabu lilitajwa katika unabii ambao Yehova mwenyewe alitoa huko nyuma katika Edeni. Sasa chunguza maandishi, mileani baada ya mileani, uone kama Mungu amekuwa mkawivu katika kutimiza kusudi lake akomboe wanadamu.—Rum. 8:20, 21; Mwa. 3:15; 2 Pet. 3:9.
KUTOKA 4026 MPAKA 3026 K.W.K.
Wakati wa mileani zilizotangulia kuumbwa kwa mwanadamu, Mungu alikuwa ameonyesha upendo mwingi sana na fikira kwa kutayarisha makao ya paradiso kwa ajili ya jamaa ya kibinadamu. Lakini mwanadamu alipoasi katika Edeni, Yehova, akiwa ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu, alifanya kesi, akahukumu Adamu na Hawa kufa, akawafukuza watoke katika bustani ya furaha. Yehova alichukua hatua kulingana na sifa yake ya haki ya hukumu. Lakini hukumu yake haikuwa ya kufutilia mbali taifa la kibinadamu. Aliruhusu wenzi wawili wa kwanza wazae watoto, wajapokuwa wenye dhambi sasa. Yehova alitangaza pia kwamba angetokeza “uzao” uponde Shetani na wafuasi wake, alipokuwa akiwahukumu Adamu na Hawa. Hiyo ilionyesha kwamba angetendea wazao wa Adamu kwa rehema, hata wangeweza kuwa na tumaini la kupona na kupata uzima kupitia kwa “uzao” huo ulioahidiwa.—Mwa. 3:8-24.
Kaini alipomwua ndugu yake Habili, Yehova alionyesha wazi kwamba wanadamu wangepasishwa kutoa hesabu ya hatia ya damu. Mungu huyu mwenye haki alimwongoza Henoko mwaminifu kutoa unabii wa kwamba Yehova angekuja “na watakatifu wake, maelfu maelfu, ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu.” Kwa hiyo Yehova alionyesha wazi kwamba sikuzote angetenda kwa haki juu ya waovu, lakini akatoa tumaini tukufu kwa rehema yake kwa ajili ya wale ambao wangetaka kumheshimu.—Mwa. 4:9-11; Yuda 14, 15; Kut. 34:6, 7.
KUTOKA 3026 MPAKA 2026 K.W.K.
Mwanzoni mwa mileani hii Nuhu alizaliwa. Yehova alimtumia Nuhu kutoa mfano wa unabii wa ukombozi ambao mwishowe Yeye angewaletea wanadamu. Kwa njia gani? Yehova alitokeza badiliko kubwa la ghafula kwa kuleta Gharika kufikiliza hukumu yake juu ya wasiomcha Yeye. Ni Nuhu na jamaa yake peke yao waliookoka, pamoja na namna namna za aina zote za wanyama wakiwa katika safina, wakatokea halafu katika dunia iliyosafishwa. Zaidi ya mileani mbili baadaye, Masihi, Yesu, alieleza maana ya unabii ya Gharika. Alisema hivi: “Kwa maana kama zilivyokuwa siku za Noa, ndivyo kutakavyokuwa kuya kwa Mwana wa watu. Kwa kuwa kama kwa siku zile mbele ya garika walivyokuwa wakikula na kunywa, wakioa na kuolewa, mupaka siku Noa alipoingia safina, nao hawakuyua hata garika ilipokuya na kuwaondosha wote; ndivyo kutakavyokuwa kuya kwa Mwana wa watu.” Kwa njia hiyo “Mwana wa watu,” Yesu mwenyewe, alielekeza kwenye “siku ile na saa ile” ambapo Yehova Mungu angeleta dhiki kubwa juu ya dunia, aiondolee watu wasiomcha Yeye.—Mwa. 6:13-22; Mt. 24:36-39, Swahili Congo Bible.
Baada ya Gharika, Yehova aliutangaza uhai kuwa mtakatifu akakataza ulaji wa damu yo yote, alipokuwa akimpa mwanadamu ruhusa ya kula nyama ya wanyama. Lakini hata Nuhu alipokuwa hai bado, jamii ya kibinadamu iliyosafishwa ikawa potovu na kudharau sheria ya Mungu, huku Nimrodi aliyekuwa mwindaji mtukutu akijiinua awe mfalme wa kwanza wa dunia. Yehova alikuwa amekusudia jamii ya kibinadamu ienee ng’ambo katika dunia yote. Nimrodi alipopinga kusudi hilo kwa kiburi kwa kujaribu kutawala ulimwengu wa wanadamu akitumia utawala wa mji mmoja naye akiwa mtumia nguvu na “mungu,” Yehova alichukua hatua! Kwa kuvuruga lugha ya wanadamu, Yehova alitawanya wanadamu “usoni pa nchi yote.” Hivyo alionyesha hakuna anayejaribu kuchezacheza na kusudi lake alilolitaja atakayefaulu.—Mwa. 9:1-7; 10:9,10; 11:1-9; Isa. 55:11.
KUTOKA 2026 MPAKA 1026 K.W.K.
Yehova alikuwa amejulisha kwamba “uzao” ulioahidiwa na Mkombozi wa wanadamu angekuja kupitia kwa ukoo wa mwana wa Nuhu Shemu. Ibrahimu alitokea katika ukoo huo, akiwa mwanamume aliyehesabiwa haki kwa sababu ya imani yake yenye nguvu. Mungu alifanya agano na Ibrahimu, akasema kwamba kupitia kwa uzao wa Ibrahimu, mataifa yote ya dunia “watajibarikia.” Kwa kuacha Ibrahimu afikie hatua ya kutaka kumtoa Mwanawe Isaka kama dhabihu, Mungu alionyesha mfano wa dhabihu ya wakati ujao ya Mwana wake mwenyewe akiwa ukombozi wa wanadamu na pia alionyesha mfano wa tumaini tukufu la ufufuo. Mungu alitumia pia kilembwe cha Ibrahimu Yusufu katika Misri awe mfano wa vile Masihi angetokezwa kama mwokozi wa wanadamu. Katika nchi ya karibu ya Usi, ‘kushikamana na utimilifu’ kwa Ayubu kumhakikisha Shetani kuwa mwongo kulikuwa mfano wa vile Masihi, na vilevile watumishi wengine waaminifu wa Mungu, wangevumilia mateso mengi kushuhudia makusudi ya Yehova.—Mwa. 22:3-18; Ebr. 11:17-19; Mwa. 47:21-27; Ayubu 2:3.
Nusu ya mileani hii ilipokwisha, Yehova aliondoa Israeli Misri wakiwa chini ya Musa, akawaambia hivi: “Mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” Mungu alimpa Musa torati yenye maelezo mengi, pamoja na maagizo ya hema, utumishi wa hema hiyo na ukuhani. Hayo yote yalikuwa mifano midogo ya usimamizi wa Yehova wa wakati ujao wa kuunganishia vitu vyote chini ya Masihi. Mileani hii ilipokuwa ikikaribia kwisha, Mungu alifanya agano na Mfalme Daudi mwaminifu, ambalo lilitoa ahadi ya kuketi kwa Masihi juu ya kiti cha enzi cha ufalme wa Mungu milele, akiwa ‘mzao wa Daudi.’ Mileani hii ilipokuwa ikiisha, mwana wa Daudi Sulemani alimaliza kujenga hekalu kuu la Yehova katika Yerusalemu. Kweli, kusudi la Mungu lilikuwa likisonga mbele likatimizwe!—Kut. 19:5, 6; Efe. 1:9, 10; 1 Nya. 17:11-14; 2 Nya. 5:1.
KUTOKA 1026 MPAKA 26 K.W.K.
Hekalu tukufu la Yehova lililojengwa na Sulemani liliwekwa wakf mwaka wa kwanza wa mileani ya nne. Hii ilikuwa katikati ya kuumbwa kwa Adamu na siku zetu za leo. Kwa kufaa, Sulemani alisali hekalu katika Yerusalemu lipate kuwa nyumba ya sala ya mataifa yote. Lakini Yehova alikuwa amechagua Israeli kwa njia ya pekee wawe chombo ambacho kwacho Yeye angefunua kusudi Lake la kimungu kwa kuponya wanadamu, na kupitia kwao aliendelea kutoa mifano ya unabii ya matukio ya wakati ujao.—1 Fal. 8:1-66; Marko 11:17.
Walakini, Israeli waliasi imani. Mwaka wa 740 K.W.K., Yehova alitumia Ashuru kama ‘fimbo ya hasira yake’ kwa kuadhibu na kupeleka ufalme wa kaskazini wa Israeli uhamishoni. Mwaka wa 607 K.W.K., vilevile alitumia Babeli kuharibu Yuda na Yerusalemu. Baada ya miaka 70 mabaki waaminifu wa Wayahudi walirudi kutoka uhamishoni Babeli walijenge hekalu upya na kurudisha ibada ya kweli katika Yerusalemu.—Isa. 10:5-11; Yer. 25:8-14.
Mungu alimtumia nabii Danieli aseme kwa unabii kwamba “masihi aliye mkuu” angetokea juma 69 za miaka baada ya kutolewa amri ya kuujenga Yerusalemu wenyewe upya, nayo amri hiyo ilitolewa mwaka wa 455 K.W.K. Kwa hiyo Masihi, Mtiwa Mafuta wa Mungu, angetokea mwaka wa 29 W.K. Mungu alionyesha vilevile kwamba utawala wa Mataifa wa dunia ulioruhusiwa Naye kuanzia mwaka wa 607 K.W.K., ungekuwa wa miaka 2,520, hivyo umalizike mwaka wa 1914 W.K.—Dan. 9:24-27; 4:16, 23, 25, 32.
Maandishi ya kweli ya Maandiko ya Kiebrania yalimalizwa katika mileani hii, mwishoni mwa karne ya tano K.W.K. Lakini vizuizi vya lugha havikupaswa vizuie kuenea kwa habari za maana zilizokuwamo katika vitabu hivyo vitakatifu vya kukunja. Katika karne ya tatu K.W.K., tafsiri ya Greek Septuagint ya Maandiko ya Kiebrania ilianza kufanywa Misri; ilitayarishwa kufaidi Wayahudi wenye kusema Kigiriki waliokuwa wametawanyika katika nchi nyingine.—Rum. 3:1, 2; 15:4.
KUTOKA 26 K.W.K. MPAKA 975 W.K.
Matukio ya karne ya kwanza W.K. ni ya maana sana sana kwa wanadamu. Kuanzia masika ya mwaka wa 29 W.K. Yohana Mbatizaji alikuwa ‘akimtengenezea njia’ Masihi. Katika vuli ya mwaka huo, Yohana alimbatiza Yesu, na wakati huo Yehova akamtia Yesu mafuta ‘kwa roho takatifu na nguvu.’ Hivyo Yesu akawa Masihi, Mfalme Aliyekusudiwa na Kuhani Mkuu wa Yehova, wa kuletea wanadamu wokovu wa milele. Kwa kuhubiri na kufanya miujiza wakati wa huduma ya pekee ya miaka mitatu na nusu, Yesu alionyesha vile angetimiza kusudi la Yehova akipata kuwa mtawala wa Ufalme. Hiyo ingetia na kufufua wafu, na kuponya na kurudisha wanadamu kwenye ukamilifu katika paradiso ya kidunia. Yesu alitundikwa katika mti wa mateso, akiwa amelaaniwa na makuhani wa Kiyahudi na wakuu wa Kirumi. Baada ya kufa na kuzikwa kwake, Yehova alimtangaza kuwa mwenye haki kabisa kwa kumfufua kwa wafu na kumpeleka kwenye uzima wa kimbinguni. Ndipo Yesu kama Kuhani Mkuu alipompa Mungu mbinguni thamani ya dhabihu hiyo kamilifu ya kibinadamu, ili faida zake zipate kutumiwa kwa ajili ya wanadamu.—Mt. 3:3, 13-17; Matendo 10:37-43; 1 Tim. 3:16; Ebr. 9:24-28.
Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., Yehova alimimina roho yake juu ya wanafunzi wa Yesu waliokuwa wamekusanyika, akawaingiza katika agano jipya wakiwa Israeli wa kiroho, agano lililopatanishwa na Kristo. Kuanzia na kuongolewa kwa Kornelio na nyumba yake mwaka wa 36 W.K., Mataifa waliofanywa Wakristo waliingizwa vilevile katika huyu “Israeli wa Mungu.” “Kundi dogo” hili la Wakristo waliotiwa mafuta lilikuwa na tumaini la ajabu la kushiriki pamoja na Kristo katika ufalme wake wa kimbinguni!—Matendo 2:1-4; 10:24, 44-48; Ebr. 9:15; Gal. 6:15, 16.
Wakati wa karne ya kwanza W.K., kundi la Kikristo likawa thabiti. Mitume kadha na wanafunzi wengine wa Yesu waliandika Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki. Mwishoni mwa karne hiyo maandishi ya kweli ya Biblia yalikamilika. Sasa kusudi lote la ajabu la Yehova Mungu lilikuwa limeandikwa. Maandiko yaliyoongozwa na Mungu yalionyesha hesabu ya unabii mbalimbali wa Mungu uliokuwa umetimizwa au uliokuwa unaendelea kutimizwa. Yalitoa tumaini hakika la kutimizwa kwa ahadi zote za Yehova kupitia kwa ufalme wa Mwana wake.—Matendo 9:31; 2 Tim. 3:16 17; 2 Pet. 1:19-21.
Habari njema zilihubiriwa na Wakristo waliotiwa mafuta “katika viumbe vyote vilivyo chini ya mbingu” zikiwa safi kabisa. Lakini baada ya kufa kwa mitume uasi mkuu wa imani uliokuwa umetajwa kwa unabii uliingia, nalo kundi la Kikristo likachafuliwa “mbwa-mwitu” walipojipenyeza ndani, “makafiri,” ambao walizidharau fadhili za Mungu zisizostahilika. Mwaka wa 325 W.K. waasi-imani walianza Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) ya unafiki ikisimamiwa na Rumi ya upagani, nalo jambo hilo likaleta giza tititi la kiroho. Mileani ya tano ilikaribia mwisho wake makusudi ya Ufalme mtukufu wa Yehova yakiwa hayafahamiki wala kuthaminiwa sana. Lakini ahadi za Mungu zilizidi kuwa hakika! Yeye hasemi uongo.—Kol. 1:13, 23; Matendo 20:29, 30; Yuda 4; Tito 1:2.
KUTOKA 975 MPAKA 1975 W.K.
Wakati wa mileani ya sita Yehova aliendelea kujaribu watiwa mafuta wake wa kweli walipokuwa wakivumilia mateso. Mwishowe, giza lilianza kutoweka kidogo kidogo Biblia ilipokuwa ikitafsiriwa katika lugha za kawaida za watu kisha ikaanza kuenezwa katika Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) yote, hasa kuanzia karne ya kumi na sita. Miaka ya 1870 ufahamu wa kweli za msingi za Biblia ulianza kurudi kwa njia ya kusisimua. Yehova alianza kukusanya watiwa mafuta wake. Wakiwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” wakawa mashuhuri tena kwa kuendesha mpango mkubwa wa kulisha. Wakristo watawa walianza kutazamia sana mwaka wa 1914 W.K., kwa maana ungekuwa ndio mwisho wa Majira ya Mataifa. Kweli, mwaka wa 1914 ndipo Yehova alipomtawaza Kristo Yesu katika ufalme wa kimbinguni, juu ya Mlima Sayuni wa kimbinguni, akiwa amemiliki “ufalme wa ulimwengu.” Sehemu zote za “ishara” aliyotaja Yesu kwa unabii yenye kuonyesha kuwapo kwake katika utukufu wa kimbinguni na “mwisho wa taratibu ya mambo” zilionekana waziwazi zikitimizwa, nazo zinaendelea kutimizwa. Hiyo imewapa Wakristo wa kweli sababu kubwa ya kufurahi na kuwafanya wautangaze ufalme wa Mungu uliosimamishwa kwa bidii.—Ufu. 20:4; Mt. 24:3-14, 32-34, 45-47; 25:31-33, NW.
Kutoka mwaka wa 1919 na kuendelea, paradiso ya kiroho ilirudishwa kwa mabaki ya Mungu yaliyotiwa mafuta duniani. Na kuanzia na mwaka wa 1935 “mkutano mkubwa” wa waabudu wengine wanyenyekevu ulitokea, ukajiunga na mabaki yaliyotiwa mafuta ya jamii ya Ufalme wa Yehova kuimba sifa za Yehova duniani mwote. Kukusanywa kwa “mkutano mkubwa” huo kumeendelea miaka 40. Sasa zaidi ya watumishi hawa wa Mungu milioni mbili wanatazamia kupita katika “dhiki kubwa” inayokaribia kasi kasi waingie katika dunia iliyosafishwa, ambamo paradiso halisi itarudishwa pote pote, na kwa umilele wote! Katika karibu makundi ya Kikristo 35,000, katika nchi 207 za dunia, watu wa Mungu wenye bidii wanatayarishwa kuokoka, wakiwa tayari pia kwa kazi ya umoja iliyo mbele yao inayohusiana na paradiso halisi duniani.—Yohana 10:16; Ufu. 7:9, 10, 14, 15; linganisha Isaya 35:1-10; 65:17-23.
YEHOVA ANATENDA HATUA KWA HATUA KWA AJILI YA WANADAMU
Kweli, Yehova ni Mungu mwenye maendeleo. Yeye hakawii kutimiza sehemu zote za kusudi lake lenye fahari ili kubariki na kufaidi viumbe vyake. Huenda watu wasiomcha Mungu wakazidhihaki habari njema zinazoonyesha kwamba Masihi amekwisha “kuwapo” siku zetu akiwa anatawala kama Mfalme kama ilivyoahidiwa. Lakini dhihaka zao zitawarudia wao katika “siku ile na saa ile” ambayo Yehova amechagua kumfunua “Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake.” Kwa sababu hiyo wale wasiomjua Mungu na wasiozitii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu watapatwa na uharibifu wa moto na kisasi. Twaweza kuwa na hakika juu ya jambo hili—Yehova “hakawii kuitimiza ahadi yake.” Tunapoingojea ‘siku ya Yehova’ ya kuchukua hatua kwa saburi, tunaweza kuwa na furaha kwamba “mkutano mkubwa” utakaoiokoka “dhiki kubwa” unaendelea kuongezeka haraka haraka. Kwa hakika tunaweza kujitahidi sana kuwasaidia.—2 The. 1:7-10; 2 Pet. 3:3, 4, 9; 1 Tim. 4:10.
Mfululizo wa matendo ya kimungu ambao umesimuliwa sasa hivi, unaoongoza kwenye kuponywa kwa mwanadamu, unasisimua mioyo yetu. Tukiwa na hakika kabisa kwamba makusudi yote ya ajabu yatatimizwa juu ya wampendao, tutafuata maongozi yake na yale ya Mfalme wake, Yesu Kristo, moja kwa moja kupita “dhiki kubwa” na kuingia katika utawala wa Ufalme wa mileani ambao bado unakuja. Naam, Yehova Mungu ametenda na anaendelea kutenda “makuu” kwa ajili ya wanadamu.—Isa. 12:2-5.