Tumaini Lenye Msingi wa Kusudi la Mungu Lenye Kufunuka
“Tumaini ambalo tunalo kama nanga ya nafsi, ni hakika na imara pia.”—Ebr. 6:19.
1. Watu fulani wa kilimwengu wameonyeshaje maoni yao juu ya tumaini?
WAGIRIKI wa kale wa kilimwengu walidharau tumaini. Walikuwa na maoni ya kwamba tumaini ni ndoto tu, kwa kuwa ajali haibadiliki. Mmoja wao hata aliita tumaini “laana ya mwanadamu.” Katika nyakati za kisasa mwandishi wa habari Mwingereza alisema, “Lililo baya zaidi kuliko uchungu wa kifo ni tumaini.” Naye mwanafilosofia wa Kijeremani Nietzache asiyeamini Mungu yuko aliandika hivi: “Tumaini ndio uovu ulio mbaya zaidi kuliko maovu yote, kwa maana linarefusha mateso ya mwanadamu.”
2. Ni jambo gani limejulikana miaka ya majuzi ya juu ya ubora wenye kuponesha wa tumaini?
2 Lakini kutoka wakati huo watu wengine wamefikia maneno mkataa yaliyo tofauti kabisa juu ya tumaini. Mchunguzi anayejulikana sana katika udaktari wa ugonjwa wa akili aliona kwamba watu waliokuwa na tumaini walikuwa na uwezo zaidi wa kuokoka hali zenye mikazo. Daktari mwingine alionyesha tumaini kuwa ndiyo njia ya pekee ya kuponya magonjwa mengi yaliyoshinda madaktari. Na mmoja wa wakuu wa Amerika wa magonjwa ya akili anatumia kurasa nyingi katika kitabu kuonyesha uwezo wenye kuponesha wa tumaini.
3. (a) Yehova amefahamuje uhitaji wetu wa tumaini? (b) Hii inaweza kuonyeshwaje kwa mfano?
3 Muumba wetu, Yehova Mungu, anajua vizuri hata zaidi uhitaji wa mwanadamu wa tumaini, zaidi kwa kuwa linahusiana na afya njema ya kiroho. (Zab. 103:14) Katika fadhili zake za upendo, amefanya mpango kuangalia uhitaji huu wa maana. Zaidi ya kutoa ahadi zenye kutia tumaini, yeye ameonyesha mara nyingi kwamba zitatimizwa. Hivyo ametoa msingi wenye kuongezeka sikuzote wa tumaini. Hii inaweza kulinganishwa na anayoweza kufanya baba kuacha watoto wake wajue anayokusudia. Pengine baba anataka kwenda katika likizo ya juma moja pamoja na jamaa nzima. Kupasha watoto habari hizo kunawapa msingi wa tumaini, taraja. Halafu, anapowaacha waone matayarisho ya safari, tumaini lao linatiwa nguvu. Mashaka ambayo yangeweza kuwako juu ya kama kweli watakwenda likizoni yanaondolewa.
4. Mungu alikuwa na kusudi gani alipoumba dunia na mwanadamu?
4 Kama vile baba angekusudia kuwa na likizo yake mwenyewe na jamaa yake hata kabla ya kuitaja kwa watoto, ndivyo Yehova Mungu alivyokuwa na kusudi kwa dunia na mwanadamu hata kabla ya kuviumba. Biblia inaonyesha kwamba Mungu ‘hakuiumba dunia ukiwa, bali aliiumba ikaliwe’ na viumbe vikamilifu vya kibinadamu, vikiishi milele katika paradiso. Alipoumba wanadamu wawili wa kwanza, alitaja kusudi lake kwao, akisema hivi: “Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale . . . kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”—Isa. 45:18; Mwa. 1:28.
5. Alitoa ahadi gani katika Edeni kuonyesha kwamba kusudi lake la mwanzo juu ya dunia na mwanadamu halikuwa limebadilika?
5 Wakati malaika fulani alipoasi akajifanya Shetani Ibilisi, nao Adamu na Hawa wakajiunga na uasi wake, je! Yehova Mungu alibadili kusudi lake juu ya dunia na mwanadamu? Hata kidogo, kwa maana wakati ule ule alitoa unabii wake wa kwanza, ambao ulielekeza mbele kwenye utimizo wa kusudi hilo. Alisema hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” Tumaini la kwamba haki ingeshinda kabisa na kusudi la Yehova juu ya dunia na wanadamu lingetimizwa lilitiwa katika ahadi hiyo (iliyoandikwa katika Mwanzo 3:15). Sehemu nyingine za Biblia zinaonyesha kwamba ahadi hii yenye kutia tumaini ilielekeza mbele kwenye Ufalme ambao ungekuwa mikononi mwa “uzao” mkuu na jamii ya washirika waaminifu.—Efe. 1:8-12; 1 Pet. 1:18-21; 2:4-9; Ufu. 5:9, 10.
NENO LA YEHOVA LIMEKUWA KWELI SIKUZOTE
6. Kwa sababu gani tunaweza kutegemea kabisa ahadi za Yehova?
6 Kwa sababu gani leo tunaweza kuwa na matumaini, kuwa na hakika kwamba Yehova Mungu ataitimiza ahadi hii? Kwa sababu, kwa upande mmoja, yeye ana uwezo na hekima kutimiza kusudi lake. Ndiyo sababu anaweza kuona “yasiyokuwako kana kwamba yamekuwako.” (Rum. 4:17) Na, kwa upande ule mwingine, sisi tunaweza kuamini kabisa unabii huo wa kwanza na ahadi ya Ufalme kwa sababu Yehova Mungu amejionyesha sikuzote kuwa mwenye kutegemeka katika kutimiza ahadi yake. (Yos. 21:45) Mungu ni mwaminifu.—1 Pet. 4:19.
7, 8. Ni mifano gani inayoweza kutolewa juu ya kutegemeka kwa neno la Yehova kutoka wakati wa Nuhu mpaka siku za Sulemani?
7 Je! maneno ya Mungu kwa Nuhu hayakutimia juu ya gharika kuu na njia ya kuiokokea waovu walipoharibiwa? (Mwa. 6:17-19; 8:15-19) Je! ahadi ya Mungu kwa Ibrahimu kwamba yeye na Sara wangepata mwana katika umri wao mzee haikutimia? (Mwa. 17:19; 21:1-3) Namna gani ahadi ya Yehova kwa Musa? Yehova aliahidi kuwakomboa Waisraeli na utumwa wa Kimisri na kuwaingiza katika nchi yenye kumiminika kwa maziwa na asali. Je! alifanya hivyo? Bila shaka alifanya hivyo, hata kama vile Yoshua anavyoshuhudia: “Nyote mnajua mioyoni mwenu, na rohoni mwenu, ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.”—Yos. 23:14.
8 Yehova aliwaahidi Waisraeli zaidi kwamba wakitii wangekuwa mali ya pekee kwake na kufurahia matokeo mazuri, amani na ufanisi. Hasa ahadi hiyo ilitimizwa chini ya utawala wa Mfalme Sulemani. Wakati wa kuwekwa wakf kwa hekalu, Sulemani angeweza kusema hivi: “Na ahimidiwe [Yehova], aliyewapa watu wake Israeli kustarehe, vile vile kama yote aliyoyaahidi. Halikukosa kupatikana neno lo lote katika ahadi yake njema, aliyoahidi kwa mkono wa Musa, mtumishi wake.”—1 Fal. 8:56; Kum. 4:3-8, 37-40.
9. Ni matukio gani ya siku za baadaye za historia ya Israeli yanayoonyesha kwamba neno la Yehova linatumainika?
9 Lakini Yehova Mungu alionya pia kwamba wakimwacha wangeadhibiwa. Kwa kweli, yeye alisema mapema kwamba wangeingia katika uhamisho wa Wababeli. Kulingana na neno lake, walipomwacha, Yehova aliwaadhibu kweli kweli. (Kum. 31:29; Isa. 39:5-7; 2 Nya. (Sik.) 36:15-21) Vivyo hivyo, kupatana na ahadi yake, alirudisha mabaki makwao. (Law. 26:41-45; Ezra 1:1-3) Mwishowe, kwa kinywa cha nabii wake mkubwa zaidi kuliko wote, Mwana wake mwenyewe, Yesu Kristo, Yehova alisema mapema juu ya uharibifu mwingine wa Yerusalemu. Huu ulitimizwa mwaka wa 70 C.E. majeshi ya Kirumi yakiwa chini ya Jemadari Tito yalipouharibu Yerusalemu na hekalu lake tukufu. (Luka 19:41-44) Hakuna shaka juu yake, Yehova amejionyesha kuwa mwaminifu na mwenye kutegemeka, mwenye kutimiza ahadi yake sikuzote. Ndiyo, ni kama vile mtume Paulo anavyotuhakikishia, “Mungu hawezi kusema uongo.”—Tito 1:2; Ebr. 6:18.
MSINGI WENYE KUZIDIZIDI WA IMANI
10. Yehova amefanya nini kutia nguvu tumaini letu?
10 Si kwamba tu tumaini letu lililo katika utimizo wa ahadi ya Yehova ya Ufalme linatiwa nguvu kwa sababu alitimiza ahadi yake nyakati nyingine nyingi, bali pia linatiwa nguvu kwa sababu tunaona kusudi lake linaelekea mbele likatimizwe kabisa. Kutoka mwanzo Yehova ametoa ushuhuda kwa watu waaminifu kupitia kwa matendo mengi yenye nguvu zisizo za kawaida kwamba unabii wake wa kwanza wa Ufalme ungetimizwa.
11, 12. Gharika na matendo ya Yehova kutoka wakati wa Ibrahimu mpaka wa Musa ilisaidiaje kutia nguvu tumaini la watumishi wake juu ya unabii wa Edeni?
11 Yenye kutegemeza unabii huo wa kwanza wa Ufalme ilikuwa gharika ya siku za Nuhu. Kwa njia gani hivyo? Basi, Gharika ilikuwa wonyesho wa kupendezwa kwa Yehova na dunia. Ilitoa ushuhuda usiokanika kwamba Mungu asingeruhusu uovu uendelee kutawala sikuzote bali angetimiza ahadi juu ya “uzao” katika wakati wake.—Mwa. 6:3.
12 Zaidi ya hayo, Yehova Mungu alifunua kwamba alikuwa anachukua hatua za kutokeza “uzao” huo na kulinda ukoo utakaomtokeza huyo. Alirudisha nguvu za uzazi za Ibrahimu na Sara, akawawezesha kupata mwana, Isaka, katika uzee wao. (Ebr. 11:11, 12) Baadaye, mjukuu wa Isaka, mwana wa Yakobo Yusufu, akawa mtumwa Misri. Yehova Mungu alitumia hali hii kuzuia jamaa kubwa ya Yakobo isitoweke katika njaa kuu ya miaka saba. (Mwa. 45:4-7) Baadaye jamaa ya Yakobo ikawa taifa katika Misri nayo ikapata kuonewa sana. Mungu alipotuma Musa akawakomboe Waisraeli na utumwa huo wenye uonezi hiyo ilikuwa hatua nyingine bado ya kutokeza “uzao.” (Kut. 3:13-17; 19:3-6) Kutoka wakati huo na kuendelea Yehova alitumia taifa zima kujulisha pande za kusudi lake juu ya “uzao.”
13. Tawala za Daudi na Sulemani zilitoa msingi gani wa tumaini?
13 Alipokuwa akishughulika na taifa la Israeli, Yehova Mungu alitoa msingi zaidi wa kuiamini ahadi yake ya kwanza ya Ufalme. Torati na ukuhani alioutoa kwa Waisraeli ilielekeza kwenye “uzao” mkuu na mambo mazuri sana ambayo yeye na makuhani-wafalme wenzake wangetimiza katika kufanya dunia hii makao mazuri, ikaliwe na taifa kamilifu la kibinadamu mpaka umilele wote. (Kol. 2:17; Ebr. 10:1; Ufu. 5:9, 10; 21:2-4) Wakati wa utawala wa Mfalme Daudi juu ya taifa zima ikawa wazi kwamba “uzao” mkuu ungepitia kwa ukoo wake wa kifalme. (2 Sam. 7:12-16) Ushindi wa Daudi na utawala mtukufu wa mwanawe Sulemani ulitoa dalili za utawala mkuu wa Ufalme wa “uzao” huo. Kama vile Daudi, yeye angepata ushindi juu ya wote wanaojiweka wampinge. (Zab. 2:1-12; 110:1, 2; Mt. 22:41-45; Matendo 4:24-30) Na, kama vile katika wakati wa Sulemani, raia zake waaminifu wangekaa katika usalama, wakifurahia matunda ya kazi zao ngumu hata washibe.—1 Fal. 4:25; Zab. 72:7, 8; Isa. 11:1-9.
14, 15. Yehova alitoa msingi gani wa tumaini kupitia kwa huduma ya Yesu ya kidunia?
14 Lo! ni ushuhuda wenye nguvu namna gani uliotokea kwamba Yehova Mungu angetimiza ahadi yake ya Kiedeni alipotuma Mwana wake mzaliwa wa pekee, Yesu Kristo, duniani! Sasa sehemu za kusudi la Yehova zikaanza kufunuka kwa upesi hata zaidi. Alipotoa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu katika dhabihu, Yesu alitoa msingi wa kisheria wa Ufalme. Kwa mwendo wake wote wa uaminifu alipotiishwa kwa mkazo mkuu na matero, alijihakikisha kustahili pia kuwa mfalme wa Ufalme. Kama vile tunavyosoma katika Biblia: “Ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata; naye alipokwisha kukamilishwa, akawa sababu ya wokovu wa milele kwa watu wote wanaomtii.” Yesu ‘aliushinda ulimwengu’ kwa sababu alikataa kuwa kama huo. Kama thawabu ya uaminifu wake imara kwa Baba yake, akawa “Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana.”—Ebr. 5:8, 9; Yohana 16:33; 1 Tim. 6:15; Ufu. 17:14.
15 Lo! Yesu alitoa mahakikisho makuu namna gani ya ushindi kamili wa haki na baraka ya milele ya wanadamu kwa miujiza mingi aliyoifanya! Hakukuwa na jambo gumu mno asiloweza kufanya. Aliponya namna zote za magonjwa na udhaifu, akalisha umati wa watu kwa mikate na samaki wachache, akatuliza upepo na bahari, akafufua wafu, hata mmoja aliyekuwa amekuwa mfu siku nne. Kwa kweli Mungu ‘alikuwa amemtia Mwanawe mafuta kwa roho takatifu na nguvu,’ kwa njia hiyo akawapa wanadamu wote msingi zaidi wa kutumainia kuja kwa Ufalme.—Matendo 10:38.
16. Yehova amekuwa akifanya nini kutoka Pentekoste ya 33 C.E. ili aendeleze kusudi lake la Ufalme?
16 Na Yehova Mungu amekuwa akifanya nini tangu ufufuo na kupaa kwa Yesu mbinguni ili afunue kusudi lake juu ya“uzao”? Amekuwa akifanya mengi, kama vile kitabu cha Matendo na mengine ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanavyoonyesha. Kuanza na Pentekoste ya mwaka wa 33 C.E., Yehova alionyesha kwa miujiza kwamba washiriki wa kundi la Kikristo watakuwa washirika na Yesu kama sehemu ya “uzao” uliokuwa umekwisha tajwa mapema kabla haujatokea katika Edeni. Kwa kweli, miaka 1,900 iliyopita Yehova Mungu amekuwa akiwachagua hawa, apate jumla ya washiriki 144,000. Kwa sasa hesabu hiyo inaelekea kuwa karibu imekamilika.—Yohana 14:1-3; Matendo 2:1-47; Ufu. 14:1, 3; 20:6.
KUSUDI LA YEHOVA LINASONGA LIKATIMIZWE SIKU ZETU
17. Kuanzia mwisho wa Majira ya Mataifa, ni ushuhuda gani umekuwa ukiongezeka kuonyesha kwamba karibuni kusudi la Mungu kwa wanadamu litatimizwa?
17 Pia katika kame hii ya 20 ushuhuda juu ya utimizo hakika wa kusudi la Mungu kwa wanadamu umeendelea kukua. Mwaka ambao vita ya ulimwengu ya kwanza ilitokea “nyakati zilizowekwa za mataifa” zilikwisha. (Luka 21:24, NW) Matukio yaliyofuata wakati huo—vita, matetemeko ya dunia, upungufu wa chakula na magonjwa ya kipuku—yanahakikisha kwamba unabii mkuu uliosemwa na Yesu (kama ulivyoandikwa na Mathayo, Marko na Luka) unaendelea kutimizwa. Pia, kama Yesu alivyokuwa amekwisha sema mapema, “habari njema ya ufalme” inahubiriwa. (Mt. 24:14; Marko 13:10) Zaidi ya watangazaji milioni mbili wenye kusema zaidi ya lugha 160 na katika zaidi ya nchi na visiwa vya bahari 200 wameshiriki. Huu wote ni ushuhuda wa kwamba Ufalme ukiwa mikononi mwa Kristo utawajilia adui zake karibuni, kwa utimizo wa ahadi ya Mungu ya Kiedeni.
18. Jina la Yehova lilijulishwaje sana, na hii imetimiza makusudi gani?
18 Biblia, zaidi kitabu cha Ezekieli, inafunua kwamba Yehova anakusudia kujulisha wanadamu wote mwishoni mwa taratibu hii ya mambo kwamba yeye peke yake, ambaye jina lake ni Yehova, ndiye Mungu mmoja wa kweli. (Zab. 83:17, 18; Ezek. 36:38; 38:23) Inafaa namna gani, basi, kwamba mwaka wa 1931 Mungu alitia wazo akilini na mioyoni mwa watu wake hapa duniani wakubali jina alilokuwa amewapa watumishi wake zamani, yaani, mashahidi wa Yehova, au, kwa ukamili zaidi, mashahidi wa Yehova wa Kikristo. (Isa. 43:10-12) Hii imekuwa baraka walau kwa njia mbili. Kwanza, imesaidia kujulisha ulimwenguni pote jina la Mungu wa kweli lisilolinganika. Na pili, imetenganisha wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo, watumishi wa kweli wa Yehova Mungu, na wengine wote wanaojidai kuwa Wakristo lakini walio hivyo kwa jina tu. Ukuu wenyewe unaopewa kwa jina hilo unasaidia kutia imani yetu nguvu kwamba wakati unakaribia kwa Yehova Mungu kujishuhudiza kwa mara ya mwisho akilini mwa viumbe vyake vyote vyenye akili, vinavyoonekana na visivyoonekana!
19. Mwangaza zaidi juu ya jamii gani ya watu umesaidia kuonyesha kwamba utimizo wa kusudi la Mungu unaelekea kwenye upeo?
19 Wenye kuendelea kutia nguvu tumaini la watumishi wa Yehova katika utimizo kamili wa kusudi lake ulikuwa mwangaza uliokuja mwaka wa 1935 kujulisha “mkutano mkubwa” unaotajwa katika Ufunuo 7:9 ni akina nani. Wakati huo ilifahamika, kwa kuchunguza Maandiko kwa uangalifu, kwamba hawa wangeokoka ‘dhiki kubwa,’ wakiwa na tumaini la kupata uzima wa milele duniani. Kutokea kwa “mkutano mkubwa” huo—hasa tangu mwaka wa 1935, na sasa katika hesabu zinazoongezeka upesi upesi—kutoka mataifa na nchi zote ni ushuhuda zaidi kwamba kusudi la Yehova linakaribia kweli kweli kutimizwa. Kwa njia gani hivyo? Kwa kuwa “mkutano mkubwa” umekwisha onekana, ‘dhiki kubwa’ watakayoiokoka bila shaka i karibu sana. Na kwa kuwa “mkutano mkubwa” ndio asili ya “nchi mpya,” kwa busara inaonekana kwamba wakati wa kuleta taratibu mpya yenye haki ya “mbingu mpya” na “nchi mpya” bila shaka u karibu sana pia.—2 Pet. 3:13.
20. Ni mwito gani unaotolewa kwa wapendao haki ambao wangali katika Babeli Mkuu, na hii inaonyesha nini juu ya wakati tunamoishi?
20 Wenye kutia nguvu pia imani na tumaini la watumishi wa Yehova umekuwa ufahamu wenye kuongezeka zaidi na zaidi kuwa ‘Babeli mkuu’ ndiyo milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Kwa uchunguzi wa uangalifu wa Maandiko Matakatifu, wamejua kwamba ‘dhiki kubwa’ itaanza na uharibifu wa dini ya uongo na wote wale walio sehemu yake. Hii imesaidia kuwaonyesha maana ya haraka kuu katika kutangaza onyo linalopatikana katika Ufunuo 18:4: “Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake.” Wale wanaokaa katika Babeli Mkuu watashiriki dhambi zake, wawe wenye hatia pamoja naye, na kwa hiyo wao pia watapata adhabu pamoja naye, wakipokea sehemu ya mapigo yake. Uhakika wenyewe wa kwamba ujumbe huu wa uharibifu unaokaribia sana wa dini yote ya uongo unatangazwa kote kote unatoa sababu zaidi kwamba ‘dhiki kubwa’ bila shaka inakuja mbio mbio.
21. Yehova ametiaje nguvu tumaini la watu wake katika nyakati za upinzani mkuu na mateso?
21 Mashahidi wa Yehova wa Kikristo kama jamii pia wametiliwa nguvu tumaini lao kwa kupata uangalizi wa Mungu wenye upendo. Kwa mfano, miaka ya kuanzia na wa 1930 upinzani mkali na mateso ulikuja katika nchi zenye kutawaliwa na serikali ya chama kimoja tu. Halafu, baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili kutokea, upinzani mwingi sana ulianza kuenea kwa karibu kila taifa duniani. Hata hivyo, mashahidi wa Kikristo wa Yehova waliona maneno ya Isaya 54:17 yenye kutoa uhakikisho kama yenye kutumika katika habari yao: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa, na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa.” Ndiyo, ujapokuwa upinzani wote na mateso kwa namna ya kifungo, kuumizwa kwa kimwili na, nyakati nyingine, kuuawa vikatili sana, watumishi wa Yehova kama jamii walitokea katika Vita ya Ulimwengu ya Pili wakiwa wenye nguvu zaidi na wengi zaidi kuliko hapo kwanza. Hata kambi za mateso za kuogofya za Nazi ya Ujeremani hazikuwa zimeharibu uamuzi wao kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Mei 3, 1945, kikundi cha Mashahidi 230 waliopona matendo ya ukatili ya kambi ya mateso walitoa maoni yao wenyewe kama ifuatavyo:
“Na ijulikane kwamba Mungu wetu mkuu, ambaye jina lake ni Yehova, ametimiza ahadi yake kwa watu wake, hasa katika eneo la Mfalme wa Kaskazini. Kipindi chenye magumu tumekipita na wale ambao wamehifadhiwa wakanyakuliwa, twaweza kusema katika tanuru ya moto, hata hawana harufu ya moto juu yao. (Tazama Danieli 3:27.) Bali, wana nguvu nyingi na uwezo kutoka kwa Yehova.”
22, 23. (a) Mwishowe washiriki wa kundi la Kikristo walijua nini juu ya kuwekwa kwa wazee na watumishi wa huduma? (b) Wazee na watumishi wa huduma wanawekwaje leo, na hii imefaidije makundi?
22 Ushuhuda wa kwamba roho ya Yehova isiyozuilika inasongeza watu wake mbele unaweza kuonekana katika yanayotokea ndani ya kundi la Kikristo. Kwa miaka mingi makundi moja moja yalitenda kwa njia za kidemokrasi, makundi ya mahali yakichagua wazee wao na mashemasi (watumishi wa huduma). (Matendo 14:23, Rotherham) Lakini mwishowe, kwa kujifunza Neno la Mungu kwa uangalifu na kusali, washiriki wa kundi la Kikristo wakapata kujua wakiongozwa na roho takatifu kwamba wenye kuwekwa wamepaswa wawekwe na wale wenye vyeo vinavyolinganika na baraza ya wazee iliyoongoza katika kundi la karne ya kwanza la Yerusalemu na wazee wengine kama vile mtume Paulo, na sawasawa na wajumbe wa Paulo, washirika wake Timotheo na Tito. (Matendo 6:2, 3; 14:23; 1 Tim. 5:22; Tito 1:5) Hii ilifanya mpango wa kundi la karne ya kwanza urudishwe polepole.
23 Hivyo, leo kuwekwa kwa wazee na watumishi wa huduma kunafanywa moja kwa moja na baraza inayoongoza ya wazee waliotiwa mafuta kwa roho ama kunafanywa nao kupitia kwa wazee wengine wenye kuwakilisha baraza hii. Wanaume wote wanaotimiza sifa za Maandiko wanawekwa ama kama watumishi wa huduma au kama wazee. Nafasi ipo kwa mwanamume ye yote ‘kufikia’ daraka la mzee kwa kujitahidi atimize sifa ambazo Biblia inaonyesha. (1 Tim. 3:1-7; Tito 1:5-9) Kwa kweli, wanaume wote wanatiwa moyo wafanye hivyo. Wale wanaoshirikiana na makundi mbalimbali duniani mwote wamepata kuthamini kwamba kuletwa kwa mpango wa kundi wenye msingi wa Biblia kumefanyika katika wakati unaofaa sana. Sasa furushi la kuangalia mahitaji ya kiroho ya makundi yenye kukua upesi upesi haliko juu ya mzee mmoja hasa au mwangalizi bali linashirikiwa na baraza. Hivyo makundi yameweza kufaidika kwa ukamili zaidi kutokana na uwezo mbalimbali wa wanaume wenye ustadi.
MPANUKO WA ULIMWENGUNI POTE
24, 25. Maongezeko makubwa sana katika hesabu za watu wa Yehova yanahakikisha nini?
24 Mambo ambayo yamekuwa yakitokea katika makundi ya watu wa Yehova miaka ya majuzi yamekuwa ya kustaajabisha. Maneno ya unabii ya Isaya 60:22 yametimizwa kwa ghafula: “Mdogo atakuwa elfu, na mnyonge atakuwa taifa hodari.” Tunapofikiria kwamba ni maelfu machache tu waliojitambua kama waabudu wa kweli wa Yehova Mungu katika siku za Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na kuwalinganisha hao na zaidi ya watangazaji wa Ufalme milioni mbili leo, lazima tukubali kwamba mdogo kweli amekuwa elfu na mnyonge taifa hodari. Kwa kweli hii inatoa uhakikisho zaidi kwamba bila shaka tunaishi katika nyakati za maana sana kwa habari ya kutimizwa kwa kusudi zuri sana la Yehova kwa wanadamu.
25 Inashangaza sana kwamba kumekuwa na ongezeko kubwa hilo wakati ambapo matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo na upagani pia yanapoteza watu wao. Taratibu kubwa za kidini zimeshindwa kushindana na mawazo ya kisiasa yenye kutaka mapinduzi na filosofia za kufuatia vitu vya kimwili na kuamini kwamba kujipatia kwa mtu faida zake mwenyewe tu ndilo jambo la maana zaidi maishani. Lakini ibada safi ya Yehova Mungu ni yenye nguvu zaidi kuliko filosofia zote, mawazo yote na dini zote za ulimwengu za taratibu hii ya kale ya mambo. Ndiyo sababu mamia ya maelfu wamekubali ibada ya kweli miaka ya majuzi nao wanafurahi kwa kuwa wamepata tumaini la kweli. Kipindi cha Septemba 1, 1973, mpaka Agosti 31, 1974, peke yake, watu 297,872 walijipatia tumaini hilo kwa kubatizwa katika maji kama wanafunzi wa Bwana Yesu Kristo.
26. Kwa sababu gani tunaweza kutazamia wakati ujao kwa matumaini?
26 Kwa kweli Yehova Mungu ametupa msingi wenye nguvu wa tumaini katika utimizo kamili wa kusudi lake kuu kwa wanadamu. Tumeona namna yeye alivyotimiza ahadi yake mara nyingi, akionyesha waziwazi kwamba hawezi kusema uongo. Tumeona pia namna Yehova Mungu amekuwa akifunulia wanadamu kusudi lake tangu alipoutoa unabii ule wa kwanza wa Ufalme katika Edeni na kufanya kazi maelfu yote ya miaka lipate kutimizwa. Yale ambayo amefanya yamesaidia kutia watumishi wake nguvu pia kwa sababu ya mambo yo yote ambayo huenda wakati ujao ukaleta. Kwa hiyo tunaweza kuutazamia wakati ujao kwa matumaini, tukiwa na hakika kwamba kusudi lake tukufu litashinda, lilete baraka ya milele ya wanadamu wenye kutii.—Luka 21:28.
[Picha katika kurasa za 348-349]
Ahadi ya Edeni
Waovu waliharibiwa siku za Nuhu
Ibrahimu apata mwana
Israeli wakombolewa na utumwa’
Mfalme Daudi kashinda adui
Utawala wenye amani wa Sulemani
Yesu aliponya wagonjwa
Kifo cha Yesu kililipia dhambi
Habari njema zahubiriwa ulimwenguni pote