Karibu Miaka 6,000 ya Kutolea Yehova Ushuhuda
UASI wa mwanamume na mwanamke katika Edeni ulitokeza ulizo kuu. Wanadamu wangechagua kumtolea Muumba wao Mungu Mwenye Enzi Kuu utumishi mtakatifu kwa sababu ya kumpenda Yeye kwa uaminifu thabiti. “Nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani,” alikuwa amejiondokea akaidanganye dunia yote inayokaliwa na watu. Kwa kupinga enzi kuu ya Yehova, alionyesha kwamba hata mwanadamu mmoja asingekuwa mwaminifu kwa Mungu. Shetani alidai kwamba asili ya mwanadamu ni choyo—kwamba mwanadamu angemtumikia Mungu kwa sababu ya vitu vya kimwili tu ambavyo angeweza kupata kwa kufanya hivyo.—Mwa. 3:1-5; Ufu. 12:9; Ayubu 1:7-12.
Yehova alikata shauri kwa hekima yake kuu ahakikishe kwa mara moja tu unyofu na haki ya enzi yake kuu. Aliona mapema kwamba wazao wengine wa Adamu wangefurahia kuunga mkono enzi Yake kuu hata Shetani akiwaletea jaribu la namna gani. Baada ya ulizo hilo kuamuliwa kabisa, enzi kuu ya Yehova ingebaki imeshuhudiwa kwa umilele wote. Hiyo ingekuwa ndiyo kanuni ya kujaribia mara moja upinzani wo wote ambao ungetokea wakati ujao na kuusukumia mbali. Lakini ingechukua karibu miaka 6,000 kuamua ulizo hilo. Na je! miaka 6,000 hiyo ya historia ya mwanadamu imeonyesha nini mpaka sasa? Je! mashahidi wa Yehova waliokuwa duniani wakati huo wameendeleza ukamilifu wao, kuhakikisha kwamba Mungu ni wa kweli na kwamba Shetani ni mwongo?—Mit. 27:11.
MILEANI YA KWANZA
Habili alikuwa ndiye shahidi wa kwanza wa Yehova kuendeleza ukamilifu wake, akaunga mkono enzi Yake kuu. (Ebr. 11:4) Kwa sababu alitoa dhabihu ya mnyama iliyokubalika kwa Yehova na ya Kaini haikukubalika, Habili aliuawa na kaka yake Kaini. ‘Msingi wa ulimwengu ulipigwa’ wakati Adamu na Hawa walipoanza kupata wana na mabinti. Habili alikuwa ndiye mwana wa pili anayetajwa. Mwanamume wa saba kutoka kwa Adamu, Henoko, ‘alitembea na Mungu’ pia akiwa shahidi mwaminifu, naye alitoa unabii juu ya hukumu ya Yehova juu ya wanadamu wasiomcha Mungu. Kwa sababu ya uaminifu wake, “Mungu alimtwaa” baada ya miaka 365 kutoka nchi ya walio hai asife kifo kama kile cha wengine.—Mwa. 4:1-15; 5:1-4, 21-24; Luka 11:49-51; Yuda 14, 15; Ebr. 11:5.
MILEANI YA PILI
Mwanzoni mwa mileani hii, mwana wa Methusela Lameki aliongozwa na Mungu atoe unabii wa kwamba mwana wake mwenyewe Nuhu angeletea wanadamu faraja. Nuhu mwenye imani nyingi, aliyezaliwa mwaka wa 1056 A.M. (anno mundi), aliishi miaka 944 kati ya umri wake wa miaka 950 katika kipindi hiki cha miaka elfu. Ingawa wana wa Mungu wa kimalaika walipata kuasi kwa kuoa duniani katika siku zake na ingawa wanadamu walielekea jeuri, Nuhu “alikwenda pamoja na Mungu” naye alikuwa “mkamilifu katika vizazi vyake.” Ili kuonyesha imani yake, kwa kuamriwa na Mungu yeye alijenga ‘safina kubwa sana, “apate kuokoa nyumba yake [ya watu saba wengine waaminifu]. Na hivyo akauhukumu makosa ulimwengu” wa wanadamu wasiomcha Mungu. Yeye alikuwa “mhubiri wa haki,” na baadaye alimtolea Mungu dhabihu za kumshukuru kwa kuwakomboa wakati wa Gharika. Kwa kutumikia wakiwa waaminifu na kumtii Yehova, Nuhu na jamaa yake walitoa uhakikisho kamili kwamba Shetani ni mwongo, wakamfisha moyo yule mwovu.—Mwa. 5:28-31; 6:9; Ebr. 11:7; 2 Pet. 2:5, Swahili Congo Bible.
MILEANI YA TATU
Nuhu aliishi miaka sita katika mileani hii. Miaka miwili baada ya kufa kwake, Ibrahimu alizaliwa. Ibrahimu alibarikiwa sana na Yehova kwa sababu alimwamini Mungu kweli kweli, akatanguliza kumtii Muumba wake kuliko starehe ya kimwili na hata akaonyesha imani ya kwamba Mungu angeweza kufufua. Akiwa ‘rafiki ya Yehova,’ Ibrahimu aliahidiwa na Mungu kwamba Masihi angepitia katika ukoo wake. Ibrahimu, mwanawe Isaka na mjukuu wake Yakobo (aliyeitwa Israeli baadaye) wote walionyesha imani nyingi, wasijishikamanishe na ufalme wo wote wa kibinadamu wakakaa hemani katika nchi ya ugenini walipokuwa wakiungojea “mji” wa mfano ambao Yehova angejenga. Wana kumi na wawili wa Yakobo wakawa wakuu wa makabila kumi na mawili ya Israeli. Kati ya wana hao, Yusufu alionyesha uaminifu mwingi kwa Mungu kwa kufuata kanuni bora za adili na kwa kuiokoa jamaa ya baba yake (ambayo ahadi iliyotolewa kwa Ibrahimu ilitegemea) wakati wa njaa kuu. Baadaye, Musa alichagua kutetea ibada ya Mungu wa kweli, akaukataa utukufu wa Misri. Kwa uthabiti alimtii Yehova kwa kuwaongoza watu wa Mungu watoke utumwani Misri wakafanywe “taifa takatifu” la mfano. Mtu wa rika lake, Ayubu, alikataa sana kuvunja ukamilifu kwa Mungu, hata alipopata hasara ya mali za kimwili na kuharibikiwa na afya yake. Yoshua, Kalebu na waamuzi wa Israeli pia walitetea sana haki. Kipindi hiki cha miaka elfu kilipokaribia kukoma, Daudi, mwana wa Yese, akawa ‘mwenye kupendeza moyo wa Mungu,’ na kwa sababu ya kushikamana kwake na Mungu kwa uaminifu Mungu akafanya naye agano la ufalme wa milele.—Mwa. 9:28, 29; 11:26; 12:1-3; Yak. 2:23; Matendo 13:22; Ebr. 11:8-32; Ayubu 1:8; 27:5.
MILEANI YA NNE
Baada ya kufa kwa mwana wa Daudi Sulemani, taifa la Israeli liligawanyika katika falme mbili. Wafalme waaminifu walikuwa wachache. Lakini, manabii wengi wa Yehova waliendeleza ukamilifu, kama vile Eliya, Isaya, Yeremia na wengine wengi. Ilisemekana wakati wa Eliya kwamba waaminifu elfu saba katika ufalme wa kaskazini wa Israeli hawakuwa ‘wamemwinamia Baali.’ Katika ufalme wa kusini, katika hekalu la Yehova Yerusalemu, maelfu ya watu, kutia na makuhani wengi wenye uaminifu thabiti, waliendelea kumwabudu Mungu wa kweli. Ufalme wa kaskazini ulipoingia uhamishoni, Wayahudi wengi wenye kumcha Mungu waliokuwa wametoka kaskazini waliendelea kuabudu Yerusalemu; na wakati Yerusalemu wenyewe ulipoachwa ukiwa, wahamishwa waaminifu katika Babeli—Ezekieli, Danieli na wengine—waliendelea kuunga mkono ibada ya kweli. Baada ya miaka 70, karibu Wayahudi 50,000 watawa na washirika wao walirudi wakajenge upya hekalu katika Yerusalemu, na kuirudisha ibada ya Yehova huko. Manabii Hagai na Zekaria waliwatia moyo kufanya hivyo. Pia, Nehemia na Wayahudi wengine waaminifu walitia bidii kufundisha watu wa Mungu Torati, hata wangeweza kufahamu kwamba “furaha ya Yehova” kweli ni “ngome.” Waandishi waaminifu pia walijitahidi kwa uangalifu kuandika kwa mkono nakala za Maandiko, nalo Neno la Mungu likaongezeka na kuenea.—1 Fal. 19:18; Neh. 8:9, 10, NW; Hag. 1:12-14; Zek. 1:1-3; Ebr. 11:32-38.
MILEANI YA TANO
Mileani hii inaanza Biblia inapotaja baraka na upendeleo wa Yehova juu ya Zekaria na mkewe Elisabeti, Yusufu na Mariamu, Simeoni, Ana na waabudu wengine wa kweli. Yohana alikuja ‘akitayarisha njia ya Yehova,’ nako kutumikia kwake bila woga kulimfanya auawe kwa ajili ya imani. Lakini yeye hakuacha yaliyo haki kwa kujitafutia usalama. Masihi aliyeahidiwa mwenyewe alitokea, aweke mfano bora wa ukamilifu. Shetani alijitahidi sana apate kosa katika uaminifu thabiti wa Yesu kwa enzi kuu ya Yehova! Lakini alishindwa kabisa kabisa. Uaminifu wa Yesu akiwa chini ya majaribu makali zaidi hata kifo chake cha kikatili, ulimnyamazisha mpinzani kabisa. Mitume na Wakristo wengine walifuata nyayo za Yesu. Lakini baada ya karne ya kwanza, jamii ya “magugu” ya Wakristo wa uongo waliopandwa na Shetani ilianza kutesa jamii ya “ngano,” Wakristo wa kweli, kama ilivyokuwa imekwisha semwa mapema kwa unabii. Karibu na karne ya nne, wengine waliolikataa fundisho la kipagani la Utatu walibandikwa jina la “Waaria.” Wengine walioendelea kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu Nisani 14 kwa uaminifu waliitwa “Wakwartodesima (au, Akina-kumi-na-nne).” Katika karne ya saba wengine walioshikamana na “Ukristo wa kweli wa mitume na Biblia” waliitwa “Wapaulo.” Lakini kubandikwa majina hivyo, pamoja na kuteswa, hakukuzuia Wakristo waaminifu waliotiwa mafuta wasiendeleze ukamilifu wao!—Luka sura 1 na 2; Mt. 13:24-30.
MILEANI YA SITA
Katikati ya utawala mkuu wa Jumuiya ya Wakristo wa uongo, Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta waliendelea kuwa wenye uaminifu thabiti kujapokuwako mateso ya ukatili mwingi na kuuawa kwa sababu ya imani na mapadre wa Kikatoliki. Kuanzia karne ya kumi na mbili ya Wakati wa Kawaida, “Wawaldensesi” katika Ufaransa walikataa mapokeo ya Kikatoliki wakapendelea kushikamana zaidi na Biblia. Wengi wa hawa waliuawa kwa sababu ya imani yao. Mmoja wao alisema hivi: ‘Msalaba haupaswi kutolewa sala bali kuchukiwa sana kama chombo alipofia Mwenye Haki.’ Kuanzia karne ya kumi na sita ya Wakati wa Kawaida, Matengenezo ya Kanisa yalifanya watu wengi na nchi nyingi zijiondoe katika mamlaka ya Kanisa Katoliki. Katika miaka ya 1870, mashahidi wa kisasa wa Kikristo wa Yehova walianza kuhubiri kwa bidii wakiwa kikundi kilichoratibishwa. Ijapokuwa kulikuwa na upinzani kutoka kwa mapadre wa Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) ‘wenye mfano wa magugu,’ jamii hiyo ya “ngano” ilitenganishwa nao, na mpaka mwaka huu wa 1976, wametoa ushuhuda katika nchi 207 kwa kuhubiri. Hasa wakati wa vita viwili vya ulimwengu, Wakristo hao waliteswa vikali. Wengi wao walikufa katika kambi za mateso za Kinazi badala ya kukana imani yao katika Yehova Mungu, na mashahidi wa Yehova wanaendelea kupatwa na majaribu katika nchi za Kikomunisti na nyinginezo. Lakini katika hayo yote wao wanaendeleza ukamilifu, wanaendelea kuzitangaza habari njema za Ufalme katika dunia yote kwa moyo wote. Kuanzia mwaka wa 1935, maelfu machache ya watiwa mafuta yameungwa na watu wengine zaidi ya milioni mbili kutolea ufalme wa Mungu ushuhuda, nao ni “mkutano mkubwa” kweli kweli unaomtegemea Yehova kama Mwenye Enzi Kuu wao wa Ulimwengu Wote na Mwanawe kama Mfalme wao wa Kimasihi!—Ufu. 2:10; 3:10; 20:4; 7:9, 10.
YEHOVA ASHUHUDIWA
Wakati mileani zilipokuwa zikipita, upande wa Yehova wa ulizo lililotokezwa Edeni umethibitishwa kabisa. Katika vizazi vyote, Yehova amekuwa na mashahidi waaminifu duniani, nao wako duniani leo wakiendelea kuongezeka kasi kasi! Baada ya mileani ya sita, wao wanamshukuru Mungu kwa ajili ya mipango yake yote ya ajabu, kutia na zawadi ya uzima wenyewe na tumaini tukufu la kupata uzima wa milele katika taratibu yake mpya. Haya yote yamewezeshwa na dhabihu ya Mwana wake mwenye kuendeleza ukamilifu, Mfalme-Masihi, Yesu Kristo. Wanaamini kwamba enzi kuu ya Yehova ndiyo enzi inayofaa. Wao wana tamaa moja ya kuzifuata njia zake za haki. Wamekata shauri kwamba Shetani hatawaondoa kamwe katika njia ya ukamilifu. Wanafurahi kushiriki kuhakikisha Shetani ni mwongo nao wanasonga mbele wakiwa na imani thabiti kujulisha “matendo makuu ya Mungu” ya kisasa. Wana furaha nyingi sana kujua kwamba Yehova yu karibu kuchukua hatua ategemeze haki na kutukuza enzi kuu yake mwenyewe kwa kumwondoa Shetani, wafuasi wake na matendo yake yote maovu katika ‘siku ya hasira ya Yehova’ inayokaribia sana!—Matendo 2:11; Sef. 2:2, 3