Sura ya Sita
Suala Ambalo Lazima Sote Tukabili
1, 2. (a) Shetani alizusha suala gani katika Edeni? (b) Mambo aliyosema yalidokezaje suala hilo?
UNAHUSIKA katika suala muhimu sana ambalo limewahi kuwakabili wanadamu. Tumaini lako la kuishi milele linategemea msimamo wako kuhusiana na suala hilo. Suala hilo lilizuka uasi ulipotokea katika Edeni. Wakati huo, Shetani alimwuliza Hawa hivi: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” Naye akajibu kwamba Mungu alisema hivi kuhusu matunda ya mti mmoja: “Msiyale . . . msije mkafa.” Halafu Shetani akasema kuwa Yehova ni mwongo, na kwamba uhai wa Hawa na wa Adamu hautegemei kumtii Mungu. Shetani alidai kwamba Mungu anawanyima viumbe wake kitu fulani kizuri—uwezo wa kujiwekea kanuni zao wenyewe maishani. Shetani alidai hivi: “Mungu anajua ya kwamba siku mtakayokula matunda ya mti huo, mtafumbuliwa macho, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.”—Mwanzo 3:1-5.
2 Shetani alikuwa akidokeza kwamba wanadamu watafanikiwa wakijiamulia mambo yao wenyewe badala ya kutii sheria za Mungu. Kwa hiyo alipinga njia ya Mungu ya kutawala. Dai hilo lilizusha suala muhimu sana la enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote, yaani, haki yake ya kutawala. Basi swali ambalo liliulizwa ni hili: Ni utawala gani unaowafaa wanadamu zaidi, utawala wa Yehova au utawala usiomtegemea Yehova? Yehova angeweza kuwaangamiza Adamu na Hawa mara moja, lakini hatua hiyo haingesuluhisha ifaavyo suala hilo. Kwa kuruhusu jamii ya binadamu isitawi kwa muda mrefu, Mungu angeonyesha matokeo mabaya ya kumkataa yeye na sheria zake.
3. Shetani alizusha suala gani la pili?
3 Shetani aliendelea kuishambulia haki ya Yehova ya kutawala baada ya mambo yaliyotukia Edeni. Alitilia shaka uaminifu wa watumishi wa Yehova. Hili likawa suala la pili ambalo linahusiana na lile la kwanza. Alitilia shaka uaminifu wa wazao wa Adamu na Hawa na malaika wote wa Mungu, hata uaminifu wa Mwana mpendwa na mzaliwa wa kwanza wa Yehova. Kwa mfano, katika siku za Ayubu (Yobu), Shetani alidai kwamba watu humtumikia Yehova kwa sababu ya ubinafsi wala si kwa sababu wanampenda au wanapenda utawala wake. Alibisha kwamba wakipatwa na magumu, wote watashindwa na tamaa za ubinafsi.—Ayubu 2:1-6; Ufunuo 12:10.
Historia Imethibitisha Nini?
4, 5. Historia imethibitisha nini kuhusu mwanadamu kuelekeza hatua zake mwenyewe?
4 Jambo muhimu katika suala la haki ya Mungu ya kutawala ni hili: Mungu hakuwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kujitawala kwa mafanikio. Ili wafaidike, aliwaumba ili wategemee sheria zake adilifu. Nabii Yeremia alikiri hivi: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu. Ee BWANA, unirudi.” (Yeremia 10:23, 24) Kwa hiyo Neno la Mungu linasihi hivi: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe.” (Mithali 3:5) Mungu alitunga sheria za asili ili ziwaongoze wanadamu waendelee kuwa hai na vilevile alitunga sheria za maadili ambazo ikiwa wanadamu wangezitii, wangekuwa na umoja.
5 Bila shaka, Mungu alijua kwamba wanadamu hawawezi kamwe kufanikiwa bila utawala wake. Wanadamu wamejaribu kujitawala bila mafanikio kwa kuanzisha mifumo mbalimbali ya kisiasa, ya kiuchumi, na ya kidini. Tofauti hizo zimesababisha ugomvi ambao umetokeza jeuri, vita, na kifo. ‘Mtu mmoja amekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9, Chapa ya 1989) Mambo yamekuwa hivyo katika historia yote ya wanadamu. Kama Neno la Mungu lilivyotabiri, waovu na walaghai wameendelea “kutoka ubaya hadi ubaya zaidi.” (2 Timotheo 3:13) Ingawa wanadamu walifanya maendeleo makubwa sana kisayansi na kiviwanda katika karne ya 20, karne hiyo ndiyo iliyokuwa na misiba mibaya sana katika historia yote. Maneno ya Yeremia 10:23 yamethibitishwa kabisa, kwamba wanadamu hawakuumbwa wajielekeze wenyewe.
6. Mungu atakomeshaje utawala wa wanadamu hivi karibuni?
6 Matokeo yenye kuhuzunisha na ya kudumu ya kumkataa Mungu yamethibitisha pasipo shaka yoyote kwamba utawala wa wanadamu hauwezi kufanikiwa. Utawala wa Mungu ndio tu unaoweza kuleta furaha, umoja, afya, na uhai. Na Neno la Mungu linaonyesha kwamba Yehova hataendelea kuwaruhusu wanadamu wajitawale. (Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5) Hivi karibuni, ataingilia mambo ya wanadamu na kuitawala dunia. Unabii wa Biblia unasema: “Katika siku za wafalme hao [serikali za wanadamu zilizopo] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [mbinguni] ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake [wanadamu hawataitawala tena dunia]; bali utavunja falme hizi [zilizopo sasa] zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Kuokoka na Kuingia Katika Ulimwengu Mpya wa Mungu
7. Ni nani watakaookoka, utawala wa Mungu utakapokomesha utawala wa wanadamu?
7 Ni nani watakaookoka utawala wa Mungu utakapokomesha utawala wa wanadamu? Biblia inajibu: “Wanyofu [wale wanaotetea haki ya Mungu ya kutawala] watakaa katika nchi, na wakamilifu watadumu ndani yake. Bali waovu [wale ambao hawatetei haki ya Mungu ya kutawala] watatengwa na nchi.” (Mithali 2:21, 22) Mtunga-zaburi alisema hivi pia: “Bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo . . . Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:10, 29.
8. Mungu atateteaje kikamili haki yake ya kutawala?
8 Baada ya mfumo wa Shetani kuharibiwa, Mungu ataleta ulimwengu wake mpya, ambao utakomesha kabisa jeuri, vita, umaskini, mateso, magonjwa, na kifo ambacho kimewakabili wanadamu kwa miaka mingi. Biblia inaeleza vizuri sana baraka ambazo wanadamu watiifu watapata: “Naye [Mungu] atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Mungu atatumia serikali yake ya Ufalme wa mbinguni inayoongozwa na Kristo, kutetea (kuthibitisha) kabisa haki yake ya kuwa Mwenye Enzi Kuu, yaani, kuwa Mtawala wetu.—Waroma 16:20; 2 Petro 3:10-13; Ufunuo 20:1-6.
Msimamo wa Watu Wengine Kuhusiana na Lile Suala
9. (a) Wale ambao wamedumisha uaminifu kwa Yehova wamelionaje neno lake? (b) Noa alithibitishaje uaminifu wake, na mfano wake unatufunza nini?
9 Miaka nenda miaka rudi, kumekuwa na wanaume na wanawake wenye imani ambao wamedumisha uaminifu wao kwa Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu. Walijua kwamba uhai wao unategemea kumsikiliza na kumtii. Mfano mmoja ni Noa. Mungu alimwambia hivi Noa: “Mwisho wa kila mwenye mwili umekuja mbele zangu . . . Ujifanyie safina.” Noa alifuata mwongozo wa Yehova. Watu wengine walioishi wakati huo walipuuza onyo wakaendelea na maisha yao bila kujali jambo ambalo lingetukia. Lakini Noa alijenga safina kubwa sana, akawahubiria wengine kwa bidii kuhusu njia za Yehova za uadilifu. Biblia yaendelea kusema hivi: “Ndivyo alivyofanya Nuhu [“Noa,” NW], sawasawa na vyote alivyomwamuru Mungu, hivyo ndivyo alivyofanya.”—Mwanzo 6:13-22; Waebrania 11:7; 2 Petro 2:5.
10. (a) Abrahamu na Sara waliungaje mkono haki ya Yehova ya kutawala? (b) Tunajifunza nini kutokana na mifano ya Abrahamu na Sara?
10 Abrahamu na Sara waliweka mfano mzuri walipounga mkono haki ya Yehova ya kutawala, walifanya yote aliyowaamuru. Waliishi katika jiji lenye ufanisi la Uru wa Wakaldayo. Lakini Yehova alipomwambia Abrahamu ahamie nchi nyingine ya kigeni ambayo hakuifahamu, Abrahamu ‘alienda kama BWANA alivyomwamuru.’ Inaelekea Sara aliishi raha mustarehe—akiwa na makao, rafiki na jamaa zake. Lakini alimtii Yehova na mumewe akaenda nchi ya Kanaani, ingawa hakujua maisha yangekuwaje huko.—Mwanzo 11:31–12:4; Matendo 7:2-4.
11. (a) Musa aliunga mkono haki ya Yehova ya kutawala ajapokabili hali zipi? (b) Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Musa?
11 Musa pia aliunga mkono haki ya Yehova ya kutawala. Naye alifanya hivyo licha ya magumu ya kukutana ana kwa ana na Farao wa Misri. Si kwamba Musa alijiamini mno. Alitilia shaka uwezo wake wa kusema vizuri. Lakini alimtii Yehova. Kwa msaada wa Yehova na wa Haruni, nduguye, Musa alimpelekea Farao mwenye shingo ngumu ujumbe wa Yehova tena na tena. Hata baadhi ya wana wa Israeli walimlaumu Musa vikali. Lakini kwa uaminifu Musa alifanya yote ambayo Yehova alimwamuru, na alitumiwa kuwakomboa Waisraeli kutoka Misri.—Kutoka 7:6; 12:50, 51; Waebrania 11:24-27.
12. (a) Ni mfano gani unaoonyesha kwamba kuwa waaminifu kwa Yehova si kutii tu yale ambayo Mungu ameandika? (b) Kufahamu uaminifu wa aina hiyo kutatusaidiaje kufuata andiko la 1 Yohana 2:15?
12 Wale waliokuwa waaminifu kwa Yehova hawakufikiri kwamba walipaswa kutii tu mambo ambayo aliandika. Mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi Yosefu afanye uzinzi naye, hakukuwa na amri iliyoandikwa na Mungu ambayo ilikataza uzinzi. Hata hivyo, Yosefu alijua mpango wa ndoa ulioanzishwa na Yehova katika Edeni. Alijua kwamba kufanya ngono na mke wa mtu mwingine hakumpendezi Mungu. Yosefu hakutaka kujaribu kujua Mungu angemruhusu kuwaiga Wamisri kwa kadiri gani. Alifuata njia za Yehova kwa kutafakari jinsi ambavyo Mungu amekuwa akishughulika na wanadamu kisha akadhamiria kutii yale aliyotambua kuwa mapenzi ya Mungu.—Mwanzo 39:7-12; Zaburi 77:11, 12.
13. Ibilisi alithibitishwaje kuwa mwongo katika kisa cha (a) Ayubu? (b) wale Waebrania watatu?
13 Wale wanaomjua Yehova vyema hawamwachi hata wakijaribiwa vikali sana. Shetani alidai kwamba Ayubu, ambaye Yehova alimsifu sana, angemwacha Mungu endapo angepoteza mali zake zote au ikiwa afya yake ingezorota. Lakini Ayubu alithibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo, hata ingawa hakujua kisababishi cha matatizo yaliyompata. (Ayubu 2:9, 10) Miaka mingi baadaye, Shetani alijaribu kuthibitisha madai yake kwa kumfanya mfalme wa Babiloni mwenye hasira awatishe vijana watatu Waebrania kwamba angewatupa katika tanuru ya moto kama hawangeinama na kuabudu sanamu ambayo alikuwa ameisimamisha. Walipolazimishwa kuchagua kati ya kuitii amri ya mfalme au sheria ya Yehova iliyokataza ibada ya sanamu, walisema kwa uthabiti kwamba wanamtumikia Yehova na kwamba yeye ndiye Mtawala wao Mkuu. Uaminifu kwa Mungu ulikuwa muhimu sana kwao kuliko uhai wao!—Danieli 3:14-18.
14. Tunawezaje kuthibitisha kwamba sisi ni waaminifu kabisa kwa Yehova tujapokuwa tu wanadamu wasiokamilika?
14 Je, mifano hiyo inatufundisha kwamba ni lazima mtu awe mkamilifu ili awe mwaminifu kwa Yehova au kwamba mtu anayekosea hafai kabisa? La hasha! Biblia inatuambia kwamba Musa alikosea nyakati nyingine. Ingawa Yehova hakufurahia jambo hilo, yeye hakumkataa Musa. Mitume wa Yesu Kristo walikuwa pia na udhaifu mbalimbali. Yehova anafurahi akiona kwamba hatupuuzi mapenzi yake kimakusudi kwa njia yoyote ile licha ya kwamba tumerithi hali ya kutokamilika. Tukitumbukia katika dhambi kwa sababu ya udhaifu, ni muhimu tutubu kutoka moyoni na kuacha kabisa mwenendo huo. Tukifanya hivyo tunathibitisha kwamba tunapenda kwelikweli mambo ambayo Yehova anasema ni mema na kuchukia yale anayosema ni mabaya. Tunaweza kuwa na uhusiano mzuri na Mungu tukidhihirisha imani katika dhabihu ya Yesu inayofunika dhambi.—Amosi 5:15; Matendo 3:19; Waebrania 9:14.
15. (a) Kati ya wanadamu wote, ni nani aliyedumisha uaminifu mkamilifu kwa Mungu, na hilo lilithibitisha nini? (b) Twajifunza nini kutokana na mwenendo wa Yesu?
15 Lakini, je, wanadamu hawawezi kutii utawala wa Yehova kikamilifu? Jibu la swali hilo lilikuwa “siri takatifu” kwa miaka ipatayo 4,000. (1 Timotheo 3:16) Adamu ajapokuwa mkamilifu, hakujitoa kwa Mungu kikamilifu. Basi ni nani angeweza kufanya hivyo? Bila shaka wazao wake wote hawangeweza kufanya hivyo kwa sababu walikuwa wenye dhambi. Yesu Kristo ndiye mwanadamu pekee aliyefanya hivyo. (Waebrania 4:15) Mwenendo wa Yesu ulionyesha kwamba Adamu, ambaye aliishi katika mazingira mazuri zaidi, angeweza kudumisha uaminifu mkamilifu kama angetaka. Uumbaji wa Mungu haukuwa na kasoro. Kwa hiyo, tunajitahidi kumwiga Yesu Kristo ambaye alijitoa kabisa kwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, Yehova, na akatii sheria zake.—Kumbukumbu la Torati 32:4, 5.
Tuko Upande Upi?
16. Kwa nini tunapaswa kuwa macho daima kuhusiana na msimamo wetu kuhusu suala la haki ya Yehova ya kutawala?
16 Kila mmoja wetu leo anakabili suala la haki ya kuutawala ulimwengu. Tukisema waziwazi kwamba tuko upande wa Yehova, tunakuwa shabaha ya Shetani. Anatuletea mkazo kwa kila njia, naye ataendelea kufanya hivyo hadi mwisho wa mfumo huu mwovu wa mambo. Ni lazima tuwe macho daima. (1 Petro 5:8) Mwenendo wetu unaonyesha tunaunga mkono upande gani wa lile suala muhimu la haki ya Yehova ya kutawala na suala la uaminifu wetu kwa Mungu tunapokabili majaribu. Hatupaswi kamwe kuuona mwenendo usiofaa kuwa sawa tu eti kwa sababu umeenea ulimwenguni. Ni lazima tujitahidi kufuata kanuni za Yehova za uadilifu katika kila jambo maishani mwetu ili tudumishe uaminifu wetu.
17. Kwa nini tunapaswa kuepuka uwongo na wizi?
17 Kwa mfano, hatupaswi kumwiga Shetani, ambaye ni “baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Ni lazima tuseme kweli kila wakati. Mara nyingi vijana wa ulimwengu huu wa Shetani huwadanganya wazazi wao. Lakini vijana Wakristo hawafanyi hivyo, na hivyo wanathibitisha kwamba madai ya Shetani eti watu wa Mungu wataacha kuwa waaminifu kwake wakijaribiwa ni ya uwongo. (Ayubu 1:9-11; Mithali 6:16-19) Kisha kuna shughuli za kibiashara ambazo zinaweza kuonyesha iwapo mtu anamfuata “baba ya uwongo” badala ya Mungu wa kweli. Hatushiriki kamwe katika shughuli kama hizo. (Mika 6:11, 12) Wizi haukubaliwi kamwe, hata ikiwa mtu ana uhitaji au ikiwa yule anayeibiwa ni tajiri. (Mithali 6:30, 31; 1 Petro 4:15) Sheria za Mungu zinapinga wizi hata ikiwa ni zoea la kawaida mahali tunakoishi au hata ikiwa kile kilichoibiwa si kitu kikubwa.—Luka 16:10; Waroma 12:2; Waefeso 4:28.
18. (a) Ni jaribu gani litakalowapata wanadamu wote mwishoni mwa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja? (b) Tunapaswa kujizoeza kufanya nini sasa?
18 Wakati wa Utawala wa Kristo wa Miaka Elfu Moja, Shetani na mashetani wake watatiwa katika abiso wasiweze kuwajaribu wanadamu. Kitakuwa kitulizo kilichoje! Lakini watafunguliwa kwa muda mfupi baada ya hiyo miaka elfu moja. Shetani na wafuasi wake watawashambulia wanadamu wakamilifu ambao wanadumisha uaminifu wao kwa Mungu. (Ufunuo 20:7-10) Ikiwa tutakuwa na fursa ya pekee ya kuwa hai wakati huo, tutaunga mkono upande gani wa lile suala la yule aliye na haki ya kutawala ulimwengu? Kwa kuwa wanadamu wote watakuwa wakamilifu, uasi wowote utakuwa wa kimakusudi na mtu atakayeasi ataangamizwa milele. Ni muhimu kuzoea sasa kutii maagizo yote ya Yehova, iwe ni kupitia Neno lake au tengenezo lake! Tunapofanya hivyo tunaonyesha kwamba tumejitoa kabisa kwake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu.
Mazungumzo ya Kurudia
• Ni lazima sote tukabili suala gani muhimu? Tulihusikaje?
• Wanaume na wanawake wa nyakati za kale walidumishaje uaminifu wa pekee kwa Yehova?
• Kwa nini ni muhimu kumheshimu Yehova kila siku kwa mwenendo wetu?