ENZI KUU
Cheo cha juu zaidi katika mamlaka au utawala; mamlaka au uongozi wa bwana, mfalme, maliki, au mkuu mwingine; mamlaka ambayo, hatimaye huamua serikali inayotawala nchi.
Neno ʼAdho·naiʹ linapatikana mara nyingi katika Maandiko ya Kiebrania, na maneno ʼAdho·naiʹ Yehwihʹ yanapatikana mara 285. ʼAdho·naiʹ ni wingi wa neno ʼa·dhohnʹ, linalomaanisha “bwana au mkuu.” Neno hilo kwa wingi ʼadho·nimʹ linaweza kutumiwa kuwarejelea watu wengi, kama “mabwana,” au “wakuu.” Lakini neno ʼAdho·naiʹ bila kiambishi tamati hutumiwa sikuzote katika Maandiko kumrejelea Mungu, na kwa wingi linatumiwa kuonyesha utukufu au ukuu. Mara nyingi watafsiri hulitafsiri kuwa “Bwana.” Neno hilo linapotumiwa pamoja na neno Mungu (ʼAdho·naiʹ Yehwihʹ), kwa mfano, katika Zaburi 73:28, hutafsiriwa kuwa “Bwana MUNGU” (AT, KJ, RS); “Bwana Mungu” (Dy [72:28]); “Bwana, Mkuu wangu” (Kx [72:28]); “Bwana Yehova” (Yg); “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova” (NWT). Katika Zaburi 47:9; 138:5; 150:2, tafsiri ya Moffatt inatumia neno “enzi kuu,” lakini hairejelei neno ʼAdho·naiʹ.
Neno la Kigiriki de·spoʹtes linamaanisha yule ambaye ana mamlaka kuu zaidi, au anayemiliki kila kitu na mwenye nguvu zisizo na mipaka. (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words, 1981, Buku la 3, uku. 18, 46) Linatafsiriwa “bwana,” “mkuu,” “mmiliki,” na linapotumiwa moja kwa moja kumhusu Mungu linatafsiriwa “Bwana” (KJ, Yg, na nyingine), “Mtawala wa vitu vyote” (Kx), “Bwana Mwenye Enzi Kuu” (NW), katika Luka 2:29, Matendo 4:24, na Ufunuo 6:10. Katika andiko hilo la mwisho, Knox, The New English Bible, Moffatt, na Revised Standard Version zinalitafsiri kuwa “Bwana Mwenye Enzi Kuu”; tafsiri ya Young na Kingdom Interlinear zinatumia neno “mkuu.”
Kwa hiyo, ingawa katika Kiebrania na Kigiriki hakuna maneno tofauti yanayofafanua neno “enzi kuu,” maana ya neno hilo inapatikana katika maneno ʼAdho·naiʹ na de·spoʹtes yanapotumiwa katika Maandiko kumrejelea Yehova Mungu, ili kuonyesha ukuu wa utawala wake.
Enzi Kuu ya Yehova. Yehova Mungu ndiye Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote (“mwenye enzi kuu ya dunia,” Zb 47:9, Mo) kwa sababu yeye ni Muumba, ni Mungu, na kwa sababu ya ukuu wake akiwa Mweza-Yote. (Zb 17:1; Kut 6:3; Ufu 16:14) Yeye ndiye Mmiliki wa kila kitu na Chanzo cha mamlaka yote na nguvu, Mtawala Mkuu zaidi katika serikali. (Zb 24:1; Isa 40:21-23; Ufu 4:11; 11:15) Mtunga-zaburi aliimba hivi kumhusu: “Yehova amekiimarisha kabisa kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake unatawala kila kitu.” (Zb 103:19; 145:13) Wanafunzi wa Yesu walisali hivi kwa Mungu: ‘Bwana Mwenye Enzi Kuu, wewe Ndiye uliyeumba mbingu na dunia.’ (Mdo 4:24, NW; Mo) Katika taifa la Israeli, Mungu mwenyewe alitimiza majukumu yote matatu ya serikali, yaani, alihukumu, alitunga sheria, na kutawala. Nabii Isaya alisema hivi: “Yehova ni Mwamuzi wetu, Yehova ni Mpaji-sheria wetu, Yehova ni Mfalme wetu; yeye Ndiye atakayetuokoa.” (Isa 33:22) Katika Kumbukumbu la Torati 10:17, Musa anamfafanua Mungu kwa njia ya pekee kuwa Mwenye Enzi Kuu.
Yehova ana haki na mamlaka ya kuwakabidhi wengine majukumu kwa sababu yeye ni mwenye enzi kuu. Daudi aliwekwa kuwa mfalme wa Israeli, na Maandiko yanazungumzia ‘ufalme wa Daudi’ kana kwamba ulikuwa ufalme wake. Lakini Daudi alikiri kwamba Yehova ndiye Mtawala Mwenye Enzi Kuu zaidi aliposema: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na fahari na utukufu, kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova, Wewe Ndiye unayejikweza mwenyewe ukiwa mkuu juu ya vyote.”—1Nya 29:11.
Watawala wa Dunia. Watawala wa mataifa yaliyo duniani wana mamlaka ya kadiri kwa sababu Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova amewaruhusu kuwa nayo. Andiko la Ufunuo 13:1, 2 linaonyesha kwamba serikali za kisiasa hazipewi mamlaka na Mungu, yaani, serikali hizo hazitawali kwa sababu zimepata mamlaka na nguvu kutoka kwa Mungu. Linasema kwamba yule Joka, Shetani Ibilisi, ndiye anayempa yule mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba na pembe kumi “nguvu zake na kile kiti chake cha ufalme na mamlaka kubwa.”—Ufu 12:9; ona WANYAMA WA MWITUNI, WA MFANO.
Kwa hiyo, ingawa Mungu ameruhusu tawala mbalimbali za wanadamu zije na kwenda, mfalme mmoja mkuu, alichochewa kusema hivi baada ya kujionea mwenyewe enzi kuu ya Yehova: “Utawala wake ni utawala wa milele na ufalme wake ni wa kizazi baada ya kizazi. Wakaaji wote wa dunia wanaonwa kuwa si kitu, naye hufanya kulingana na mapenzi yake mwenyewe miongoni mwa jeshi la mbinguni na wakaaji wa dunia. Na hakuna yeyote anayeweza kumzuia au kumuuliza, ‘Umefanya nini?’”—Da 4:34, 35.
Kwa hiyo, kwa muda wote ambao Mungu ataruhusu serikali za wanadamu zitawale, Wakristo watatii agizo hili la mtume Paulo: “Kila mtu na ajitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kupitia Mungu; mamlaka zilizopo zimewekwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.” Kisha mtume huyo anasema kwamba serikali hizo zinapochukua hatua ya kumwadhibu yule anayefanya mabaya, ‘mamlaka hiyo kubwa’ au mtawala (hata ingawa si mwabudu mwaminifu wa Mungu) anatenda kwa njia isiyo ya moja kwa moja akiwa mhudumu wa Mungu katika cheo hicho, akionyesha ghadhabu dhidi ya yule anayefanya mabaya.—Ro 13:1-6.
Kuhusu mamlaka hizo ‘kusimamishwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri,’ Maandiko yanaonyesha kwamba hilo halimaanishi kuwa Mungu ndiye aliyeanzisha serikali hizo au anaziunga mkono. Badala yake, anaziongoza kutimiza kusudi lake zuri, linalopatana na mapenzi yake kuhusiana na watumishi wake duniani. Musa alisema: “Aliye Juu Zaidi alipoyapa mataifa urithi wao, alipowatenganisha wana wa Adamu, aliweka mpaka wa mataifa kulingana na idadi ya wana wa Israeli.”—Kum 32:8.
Mwana wa Mungu Akiwa Mfalme. Baada ya mfalme wa mwisho aliyeketi kwenye “kiti cha ufalme cha Yehova” huko Yerusalemu kuondolewa (1Nya 29:23), nabii Danieli alipewa maono yaliyoonyesha jinsi ambavyo Mwana wa Mungu angewekwa rasmi baadaye kuwa Mfalme. Cheo cha Yehova akiwa Mzee wa Siku kinaonekana wazi anapompa Mwanawe utawala. Simulizi hilo linasema: “Nikaendelea kuangalia katika maono ya usiku, na tazama! mtu fulani kama mwana wa binadamu alikuwa akija na mawingu ya mbinguni; naye akaja mbele za Mzee wa Siku, nao wakamleta karibu Naye. Naye akapewa utawala, heshima, na ufalme, ili watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wamtumikie. Utawala wake ni utawala wa milele ambao hautapitilia mbali, na ufalme wake hautaangamizwa.” (Da 7:13, 14) Tukilinganisha andiko hili na andiko la Mathayo 26:63, 64, hatuna shaka kwamba “Mwana wa binadamu” anayetajwa katika maono ya Danieli ni Yesu Kristo. Anakuja mbele za Yehova na kupewa utawala.—Linganisha Zb 2:8, 9; Mt 28:18.
Enzi Kuu ya Yehova Yapingwa. Mfuatano wa matukio katika Biblia unaonyesha kwamba uovu umekuwepo karibu miaka yote ambayo mwanadamu ameishi duniani. Wanadamu wote wamekuwa wakifa, na dhambi na uasi dhidi ya Mungu umeongezeka. (Ro 5:12, 15, 16) Kwa kuwa Biblia inataja kwamba Mungu alimuumba mwanadamu akiwa mkamilifu, maswali yafuatayo yamezuka: Dhambi, kutokamilika, na uovu ulianzaje? Na kwa nini Mungu Mweza-Yote ameacha mambo hayo yaendelee kwa karne nyingi? Tutapata majibu ya maswali hayo tukichunguza jinsi enzi kuu ya Mungu ilivyopingwa kisha suala muhimu sana linalowahusu wanadamu likatokea.
Matakwa ya Mungu kwa wanaomtumikia. Kwa karne nyingi, Yehova Mungu amethibitisha kwa maneno na matendo yake kwamba yeye ni Mungu wa upendo mshikamanifu, Mungu anayetekeleza haki na hukumu kamilifu, na anayewaonyesha rehema wale wanaotaka kumtumikia. (Kut 34:6, 7; Zb 89:14; ona REHEMA; UADILIFU.) Hata anawatendea kwa fadhili watu wasio na shukrani na waovu. (Mt 5:45; Lu 6:35; Ro 5:8) Anafurahia kudhihirisha enzi yake kuu kwa upendo.—Yer 9:24.
Kwa hiyo, watu anaotaka waishi katika ulimwengu wake ni wale wanaomtumikia kwa sababu wanampenda na kwa sababu ya sifa zake nzuri. Lazima wampende Mungu kwanza kisha jirani yao. (Mt 22:37-39) Lazima wapende enzi kuu ya Yehova; lazima waitamani na kuipenda kuliko utawala mwingine wowote. (Zb 84:10) Lazima wawe watu ambao hata ikiwa wangeweza kujitegemea wenyewe, wangechagua enzi yake kuu kwa sababu wanajua kwamba yeye ni mtawala mwenye hekima zaidi, mwadilifu zaidi, na mtawala bora kuliko mwingine yeyote. (Isa 55:8-11; Yer 10:23; Ro 7:18) Watu hao hawamtumikii Mungu kwa sababu wanamwogopa tu akiwa mweza-yote wala kwa sababu ya ubinafsi bali kwa sababu wanapenda uadilifu wake, haki yake, na hekima yake na kwa sababu wana ujuzi kuhusu ukuu wa Yehova na upendo wake mshikamanifu. (Zb 97:10; 119:104, 128, 163) Wanakubaliana na mtume Paulo aliyesema: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika! Kwa maana ‘ni nani ameijua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake?’ Au, ‘Ni nani amempa yeye kwanza, hivi kwamba iwe lazima arudishiwe?’ Kwa sababu vitu vyote vimetoka kwake, kupitia yeye na kwa ajili yake. Kwake yeye na kuwe na utukufu milele. Amina.”—Ro 11:33-36.
Watu hao wanamjua Mungu, na kumjua kikweli kunamaanisha kumpenda na kushikamana na enzi yake kuu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kila mtu anayekaa katika muungano na yeye hana mazoea ya kufanya dhambi; mtu yeyote aliye na mazoea ya kufanya dhambi hajamwona wala kumjua.” Na pia, “Yeyote ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.” (1Yo 3:6; 4:8) Yesu alimjua Baba yake vizuri kuliko mtu mwingine yeyote. Alisema hivi: “Baba yangu amenikabidhi vitu vyote, na hakuna mtu anayemjua Mwana kikamili isipokuwa Baba; wala hakuna anayemjua Baba kikamili isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.”—Mt 11:27.
Kukosa kukuza upendo na uthamini. Kwa hiyo, enzi kuu ya Yehova ilipingwa na Shetani ambaye, ingawa alifurahia manufaa ya kuwa chini ya enzi kuu ya Mungu, hakuthamini wala kuongeza ujuzi wake kumhusu Mungu na hivyo hakumpenda zaidi. Alikuwa kiumbe wa roho wa Mungu, yaani, malaika. Wanadamu wa kwanza Adamu na Hawa walipoumbwa, kiumbe huyo alipata nafasi ya kushambulia enzi kuu ya Mungu. Kwanza, alijaribu kumpotosha Hawa, kisha akampotosha Adamu ili wasijitiishe chini ya enzi kuu ya Mungu (mbinu iliyofanikiwa). Alitaka kuanzisha utawala wake unaompinga Mungu.
Ni wazi kwamba Hawa, ambaye alijaribiwa kwanza, hakuwa amemthamini Muumba, yaani, Mungu wake, na pia hakuwa ametumia fursa aliyokuwa nayo ya kumjua. Aliisikiliza sauti ya yule malaika mwasi aliyezungumza kupitia kiumbe duni, nyoka. Biblia haisemi kwamba Hawa alishangaa alipomsikia nyoka akizungumza. Inasema kwamba nyoka alikuwa “mwenye kujihadhari kuliko wanyama wote wa mwituni walioumbwa na Yehova Mungu.” (Mwa 3:1) Haisemi ikiwa nyoka alikula matunda yaliyokatazwa ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” kisha akaonekana amepata hekima ya kuweza kuzungumza. Malaika huyo mwasi, alipomtumia nyoka kuzungumza na Hawa, alimpa nafasi ya kujitegemea (kama Hawa alivyodhani), yaani, ‘kuwa kama Mungu, akijua mema na mabaya,’ naye alifaulu kumsadikisha kwamba hangekufa.—Mwa 2:17; 3:4, 5; 2Ko 11:3.
Alipokabili uasi katika nyumba yake, Adamu ambaye pia hakumthamini wala kumpenda Muumba na Mwandalizi wake, hakuwa mshikamanifu kwa Mungu wake alipojaribiwa, basi akakubali kushawishiwa na Hawa. Adamu alipoteza imani katika Mungu na uwezo wa Mungu wa kumwandalia mtumishi wake mshikamanifu vitu vyote vizuri. (Linganisha na jambo ambalo Yehova alimwambia Daudi baada ya kufanya dhambi na Bath-sheba, katika 2Sa 12:7-9.) Jibu la Adamu alipoulizwa kuhusu kosa lake linaonyesha kwamba alimkasirikia Yehova: “Mwanamke uliyenipa nikae naye, alinipa tunda kutoka katika mti huo, basi nikala.” (Mwa 3:12) Hakuamini uwongo wa Nyoka kwamba hangekufa, kama Hawa alivyoamini, lakini wote wawili, Adamu na Hawa, waliazimia kujitegemea na kumwasi Mungu kimakusudi.—1Ti 2:14.
Adamu hangesema, “Mungu ananijaribu.” Badala yake, kanuni hii ilitumika: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, baada ya kufanywa, huleta kifo.” (Yak 1:13-15) Kwa hiyo, waasi hao watatu, yaani, yule malaika, Hawa, na Adamu—walitumia uhuru wa kuchagua ambao Mungu aliwapa kutenda dhambi kimakusudi na kupoteza hali yao ya kutokuwa na dhambi.—Ona UKAMILIFU; DHAMBI, I.
Suala lililozuka. Ni nini kilichopingwa? Upinzani huo wa malaika ambaye baadaye aliitwa Shetani Ibilisi, ulioungwa mkono na Adamu alipoasi, ulisababisha nani avunjiwe heshima na kupata suto? Je, alipinga ukweli kuhusu ukuu wa Yehova, uwepo wa enzi yake kuu? Je, enzi kuu ya Mungu ilikuwa hatarini? La, kwa sababu Yehova ndiye mwenye mamlaka kuu zaidi na nguvu zote, na hakuna yeyote mbinguni au duniani anayeweza kumnyang’anya. (Ro 9:19) Kwa hiyo, ni wazi kwamba suala lilihusu haki, kustahili, na uadilifu wa enzi kuu ya Mungu, yaani, ikiwa alitawala kwa njia inayofaa, kwa uadilifu, na kwa faida ya raia wake au la. Swali ambalo Hawa aliulizwa linaonyesha jambo hilo: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Yule Nyoka alidokeza kwamba jambo hilo si la kuaminika—kwamba Mungu aliwazuia isivyofaa, aliwanyima kitu fulani ambacho wanadamu hao wawili walikuwa na haki ya kuwa nacho.—Mwa 3:1.
“Mti wa ujuzi wa mema na mabaya” ulikuwa nini?
Adamu na Hawa waliasi kwa kula tunda la “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Muumba, akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, alikuwa na haki kamili ya kuweka sheria kuhusiana na mti huo, kwa sababu Adamu, ambaye alikuwa kiumbe, si mwenye enzi kuu, alikuwa na mipaka, naye alipaswa kutambua ukweli huo. Ili kuwe na amani na upatano ulimwenguni, viumbe wote wenye akili walipaswa kutambua na kuunga mkono enzi kuu ya Muumba. Adamu angeonyesha anatambua hilo kwa kuepuka kula tunda la mti huo. Kwa sababu angekuwa baba ya wote ambao wangeijaza dunia, alipaswa kutii na kuwa mshikamanifu, hata katika jambo dogo sana. Kanuni hii ilitumika: “Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo si mwaminifu katika lililo kubwa pia.” (Lu 16:10) Adamu alikuwa na uwezo wa kutii kikamili. Ni wazi kwamba tunda lenyewe halikuwa baya kiasili. (Jambo walilokatazwa halikuwa uhusiano wa kingono, kwa sababu Mungu alikuwa amewaamuru ‘waijaze dunia.’ [Mwa 1:28] Biblia inasema kwamba lilikuwa tunda la mti halisi.) Maelezo ya chini ya Mwanzo 2:17 katika The Jerusalem Bible (1966) yanafafanua vizuri kilichowakilishwa na mti huo:
“Ni Mungu pekee aliye na pendeleo la kuwa na ujuzi huo na ingekuwa dhambi kwa mwanadamu kuupata, 3:5, 22. Basi, haumaanishi kujua kila jambo, kwa sababu mwanadamu mwenye dhambi hana uwezo huo; wala si uwezo wa kutofautisha mema na mabaya, kwa sababu tayari mwanadamu asiye na dhambi alikuwa nao na Mungu hangemnyima kiumbe mwenye akili uwezo huo. Ni mamlaka ya kujiamulia mema na maovu na kutenda kwa njia inayofaa, haki ya kuwa huru kabisa kimaadili, kudai kuwa na uhuru kamili wa kimaadili unaomfanya mwanadamu akatae kutambua kwamba yeye ni kiumbe. Dhambi ya kwanza ilikuwa shambulizi dhidi ya enzi kuu ya Mungu, dhambi ya kiburi.”
Shetani adai watumishi wa Mungu wana ubinafsi. Maneno ambayo Shetani alimwambia Mungu kuhusu mtumishi wake mwaminifu Ayubu yanafunua zaidi suala hilo. Shetani alisema: “Je, Ayubu anamwogopa Mungu bure? Je, wewe hukuweka ukuta wa ulinzi kumzunguka yeye na nyumba yake na kila kitu alicho nacho? Umeibariki kazi ya mikono yake, na mifugo yake imeenea nchini. Lakini, ili mambo yabadilike, nyoosha mkono wako na upige kila kitu alicho nacho, na kwa hakika atakutukana mbele za uso wako mwenyewe.” Kisha akasema: “Ngozi kwa ngozi. Mtu atatoa kila kitu alicho nacho ili aokoe uhai wake.” (Ayu 1:9-11; 2:4) Shetani alidai kwamba Ayubu hakumpenda Mungu kutoka moyoni, kwamba alimtumikia Mungu na kumtii kwa sababu tu za kibinafsi, ili kupata faida. Kwa hiyo Shetani alimchongea Mungu kuhusu enzi yake kuu na watumishi wa Mungu kuhusu utimilifu wao kwa enzi hiyo kuu. Kwa maneno mengine, alidai hakuna mwanadamu yeyote duniani anayeweza kuendelea kuwa mtimilifu kwa enzi kuu ya Yehova ikiwa yeye, Shetani, ataruhusiwa kumjaribu.
Yehova aliruhusu masuala hayo mawili yajibiwe kwa pamoja. Hata hivyo, hakutilia shaka uadilifu wa enzi yake kuu. Hakuhitaji kuthibitishiwa jambo lolote. Upendo wake kwa viumbe wake wenye akili ulimchochea kuruhusu muda upite ili kusuluhisha jambo hilo. Aliruhusu wanadamu wajaribiwe na Shetani, mbele ya viumbe wote ulimwenguni. Naye akawapa viumbe wake pendeleo la kuthibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo, na hivyo Jina la Mungu pamoja na la watumishi wake kuondolewa lawama. Kwa sababu ya mtazamo wa Shetani wa ubinafsi, ‘aliachwa katika hali ya akili isiyokubalika.’ Kwa kweli alijipinga mwenyewe alipozungumza na Hawa. (Ro 1:28) Kwa maana alidai kwamba Mungu hakutawala kwa njia ya haki na uadilifu, na wakati uleule, inaonekana alitarajia kutendewa haki na Mungu: Inaonekana alifikiri Mungu angehisi kwamba anapaswa kumruhusu aendelee kuishi ikiwa angethibitisha dai lake kwamba viumbe wa Mungu si waaminifu.
Uhitaji muhimu wa kusuluhisha suala hilo. Uhusiano kati ya viumbe wote walio hai na Enzi kuu ya Mungu ulitegemea kabisa kusuluhishwa kwa suala hilo. Kwa sababu baada ya kusuluhishwa, suala hilo halingerudiwa kamwe. Inaonekana kwamba Yehova alitaka sana viumbe wote wajue na kuelewa kikamili mambo yote yaliyohusika katika suala hilo. Hatua ambayo Mungu alichukua inaonyesha kwamba habadiliki, inatetea zaidi utawala wake, na kufanya enzi yake kuu itamanike hata zaidi na kuimarika kabisa katika akili za wote wanaoichagua.—Linganisha Mal 3:6.
Suala linalohusu uadilifu. Basi suala hilo halihusu ni nani aliye na nguvu na uwezo; linahusu hasa uadilifu. Hata hivyo, kwa sababu Mungu haonekani na kwa sababu Shetani amejitahidi sana kupofusha akili za watu, nyakati nyingine hata watu wametilia shaka nguvu za Yehova na kuwapo kwake. (1Yo 5:19; Ufu 12:9) Wanadamu wameelewa kimakosa sababu inayomfanya Mungu awe na subira na fadhili na hivyo wamezidi kuasi. (Mhu 8:11; 2Pe 3:9) Kwa hiyo, ili mtu amtumikie Mungu kwa utimilifu ni lazima awe na imani na apate mateso. (Ebr 11:6, 35-38) Hata hivyo, Yehova anakusudia watu wote wajue jina lake na enzi yake kuu. Alimwambia hivi Farao kule Misri: “Nimekuacha uendelee kuishi kwa sababu hii hasa: ili nikuonyeshe nguvu zangu na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.” (Kut 9:16) Vivyo hivyo, Mungu ameruhusu wakati upite ili ulimwengu huu na mungu wake, Shetani Ibilisi, waendelee kuwapo na uovu wao uzidi, na ameweka wakati wa kuwaangamiza. (2Ko 4:4; 2Pe 3:7) Mtunga-zaburi alitoa sala hii ya kinabii: “Na watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zb 83:18) Yehova mwenyewe ameapa hivi: “Kila goti litapigwa mbele zangu, kila ulimi utaapa kuwa mshikamanifu na useme, ‘Kwa hakika katika Yehova kuna uadilifu wa kweli na nguvu.’”—Isa 45:23, 24.
Suala hilo lilihusisha nani? Ni nani waliohusika? Kwa kuwa mwanadamu alishawishiwa kufanya dhambi, na malaika pia alifanya dhambi, suala hilo lilihusisha viumbe wa mbinguni wa Mungu, hata Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, aliye na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova Mungu. Mwana huyo ambaye sikuzote alifanya mambo yanayompendeza Baba yake, alitamani sana kutetea enzi kuu ya Yehova. (Yoh 8:29; Ebr 1:9) Mungu alimchagua atimize mgawo huo, akamtuma duniani, ili azaliwe akiwa mtoto wa kiume kupitia bikira Maria. (Lu 1:35) Alikuwa mkamilifu, naye alidumisha ukamilifu huo na kubaki bila lawama maisha yake yote, hata kufikia kifo cha aibu. (Ebr 7:26) Kabla ya kifo chake alisema hivi: “Sasa ulimwengu huu unahukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” Pia alisema: “Mtawala wa ulimwengu anakuja, naye hana uwezo juu yangu.” (Yoh 12:31; 14:30) Shetani hakuwa na uwezo wa kuvunja utimilifu wa Kristo, naye alihukumiwa kwamba ameshindwa, tayari kutupwa nje. Yesu ‘aliushinda ulimwengu.’—Yoh 16:33.
Yesu Kristo, Mteteaji wa uadilifu wa enzi kuu ya Yehova. Kwa hiyo, Yesu Kristo alithibitisha kikamili kabisa kwamba Ibilisi ni mwongo, akajibu kikamili swali hili: Je, kuna mwanadamu anayeweza kubaki mwaminifu kwa Mungu akikabili kishawishi au jaribu la aina yoyote? Hivyo, Yesu aliwekwa rasmi na Mungu Mwenye Enzi Kuu kuwa Mtimizaji wa makusudi Yake, yule ambaye angetumiwa kuondoa uovu katika ulimwengu wote, na pia kumwondoa Ibilisi. Atatumia mamlaka hiyo, na ‘kila goti litapigwa na kila ulimi utakiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.’—Flp 2:5-11; Ebr 2:14; 1Yo 3:8.
Katika mamlaka ambayo Mwana amepewa, anatawala katika jina la Baba yake, ‘akiangamiza’ serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote ambazo zinapinga enzi kuu ya Yehova. Mtume Paulo anafunua kwamba baadaye Yesu Kristo anaonyesha heshima kubwa sana kwa enzi kuu ya Yehova, kwa kuwa “vitu vyote vitakapotiishwa kwake, ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yule aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”—1Ko 15:24-28.
Kitabu cha Ufunuo kinaonyesha kwamba baada ya Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo kufikia mwisho, akiwa ametiisha kila mamlaka inayojaribu kupinga enzi kuu ya Yehova, Ibilisi atafunguliwa kwa muda mfupi. Atajaribu kufufua suala hilo, lakini hatapewa muda mrefu kwa sababu tayari suala litakuwa limetatuliwa. Shetani na wafuasi wake wataangamizwa kabisa.—Ufu 20:7-10.
Wengine wanaounga mkono upande wa Yehova. Ingawa uaminifu wa Kristo uliunga mkono kikamili upande wa Mungu, wengine pia wamepewa fursa ya kufanya hivyo. (Met 27:11) Mtume Paulo anataja matokeo ya maisha ya Kristo ya utimilifu, na ya kifo chake cha kidhabihu: “Kupitia tendo moja la kutetewa matokeo kwa watu wa namna zote ni wao kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Ro 5:18) Kristo amewekwa kuwa Kichwa cha “mwili,” yaani, kutaniko (Kol 1:18), ambalo washiriki wake wanashiriki katika kifo chake cha utimilifu, naye anafurahi kushirikiana pamoja nao wakiwa warithi pamoja naye, wafalme wenzi katika utawala wake wa Ufalme. (Lu 22:28-30; Ro 6:3-5, 8:17; Ufu 20:4, 6) Ingawa wanaume waaminifu wa zamani hawakuwa wakamilifu, walidumisha utimilifu wakitazamia mpango huo wa Mungu. (Ebr 11:13-16) Na wengine wengi ambao hatimaye wanapiga magoti kwa heshima wanafanya hivyo pia wakitambua kutoka moyoni enzi kuu ya Mungu ya uadilifu, inayofaa. Kama mtunga-zaburi alivyoimba kinabii: “Kila kitu kinachopumua—na kimsifu Yah. Msifuni Yah!”—Zb 150:6.