Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 12/15 kur. 7-11
  • Uzuri wa Enzi Kuu ya Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uzuri wa Enzi Kuu ya Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIFA KUU ZA ENZI KUU YA YEHOVA
  • “HABARI NJEMA” ZINAZOKAMATANA NA ENZI KUU YA MUNGU
  • SABABU GANI UITII ENZI KUU YA MUNGU
  • KUTUMIKIA INAVYOFAA CHINI YA ENZI KUU YA MUNGU
  • ENZI KUU YA YEHOVA INAONGEZA FURAHA NA SIFA
  • Unga Mkono Enzi Kuu ya Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • Serikali Moja Ile ya Ulimwengu Mmoja Chini ya Enzi Kuu ya Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Enzi Kuu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Enzi Kuu ya Yehova na Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 12/15 kur. 7-11

Uzuri wa Enzi Kuu ya Yehova

“Neno moja nimelitaka kwa [Yehova], nalo ndilo nitakalolitafuta, nikae nyumbani mwa [Yehova], siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa [Yehova]. Na kutafakari hekaluni mwake.”​—Zab. 27:4.

1. Ni jambo gani linalokuja katika akili wakati maneno “Enzi Kuu” yanapotajwa?

MANENO “enzi kuu” yana maana gani kwako? Bila shaka yanakufanya ufikiri juu ya ukuu, sana sana ukuu wa mtawala​—⁠mamlaka ya serikali. Utawala unaweza kuwa mkali, ukitoa hukumu kulingana na sheria pasipo kuonyesha rehema; au unaweza kutumia upendeleo kwa wengine na kuwaonea wengine. Ni utawala mchache sana wa kibinadamu unaotenda kwa kuongozwa na upendo wa kweli kwa raia zake.

2. Yehova ni mwenye enzi kuu kwa sababu ya haki gani?

2 Biblia inasema kwa habari ya Mungu kwamba yeye ni “Mwenye Enzi Kuu” na “Bwana Mwenye Enzi Kuu.” (Matendo 4:24, Rotherham; Revised Standard Version; The New English Bible; New World Translation) Ni haki gani inayomfanya awe mwenye enzi kuu? Ufunuo 4:11 linajibu hivi: “Umestahili wewe [Yehova], . . . na Mungu wetu, kuupokea utukufu na heshima na uweza; kwa kuwa wewe ndiwe uliyeviumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako, navyo vikaumbwa.”

3. Mfalme Daudi aliielezaje enzi kuu ya Yehova?

3 Yehova anatumia enzi kuu ya namna gani? Je! iko tofauti na namna nyingine za utawala? Mfalme Daudi, aliyetawala juu ya ufalme wa kale wa Israeli chini ya enzi kuu ya Yehova, alisema hivi: “Ee [Yehova], ukuu ni wako, na uweza, na utukufu, na kushinda, na enzi; maana vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani ni vyako; ufalme ni wako, Ee [Yehova], nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote.”​—1 Nya. 29:11.

SIFA KUU ZA ENZI KUU YA YEHOVA

4. Zaburi 89:14 na Kutoka 34:6, 7 yanatupaje mfano wa enzi kuu ya Yehova?

4 Kwa hiyo, enzi kuu ya Yehova ina uzuri, wema na heshima. Mwandikaji wa zaburi anaandika hivi: “Haki na hukumu ndio msingi wa kiti chako [cha enzi], fadhili na kweli zahudhuria mbele ya uso wako.” (Zab. 89:14) Musa alipoomba auone utukufu wa Mungu, aliambiwa kwamba hawezi kuuona uso wa Mungu, kwa kuwa hakuna awezaye kumwona Mungu akaishi. (Kut. 33:18, 20) Hata hivyo, Mungu alishuka katika wingu katika Mlima Sinai na kutangaza kwa Musa: “[Yehova], [Yehova], Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha tatu na cha nne.”​—Kut. 34:6, 7.

5. (a) Ni sifa gani zake mwenyewe ambazo Yehova alimjulisha Musa kwa mara ya kwanza katika Mlima Sinai? (b) Ijapokuwa Yehova ni mwenye rehema, ni kwa sababu gani mtu anayefanya makosa anaadhibiwa, naye Yehova anaonaje juu ya kutoa adhabu?

5 Angalia kwamba mambo ya kwanza ambayo Yehova alimjulisha Musa yalikuwa rehema, fadhili, kutokuwa na wepesi wa hasira, fadhili za upendo, kweli na kusamehe. Katika mahali pengine anasema hivi: “Mimi ni [Yehova], nitendaye wema, na hukumu, na haki, katika nchi; maana mimi napendezwa na mambo hayo.” (Yer. 9:24) Walakini, mtu ye yote anapomkosea Mungu, hawezi kuepuka kupatwa na matokeo ya mfululizo wa mambo ambayo yeye mwenyewe ameanzisha. Kwa mfano, mtu anayezini, wale walio karibu naye wanapatwa na matokeo ya kitendo chake. Jamaa yake yote inapatwa na matokeo hayo. Na wale wanaomwacha Mungu au wanaokataa enzi yake kuu wataadhibiwa. Wakati watu waasi walipoanza kujenga mnara wa Babeli, Mungu alizuia mpango wao kwa kuvuruga lugha yao. Ndipo walipotawanyika katika nchi yote na kuongoza wazao wao waliokuja kuwa waabudu wa sanamu na wazoevu wa mambo mabaya sana. (Mwa. 11:1-9) Walakini, Mungu hafurahii kuwaadhibu au kutaabika kwa wale wanaofanya makosa. Yeye anasema hivi: “Mimi sikufurahii kufa kwake afaye, . . . basi ghairini, mkaishi.”​—Eze. 18:32.

6. Kwa hiyo, basi, nyingine za sifa zenye kutokeza za enzi kuu ya Yehova ni sifa gani, nayo inalinganaje na utawala wa kibinadamu?

6 Ni wazi kutokana na Maandiko hayo yanayotajwa kwamba kati ya sifa zilizo kuu za enzi kuu ya Mungu ni fadhili za upendo, rehema, haki na kutopendelea anapotoa hukumu. Kwa hiyo, tunapoangalia enzi kuu ya Mungu, inatupasa tuione katika njia iliyo tofauti na utawala wa kibinadamu. Je! isingekuwa vizuri pia ikiwa ungeweza kuona upendo ulio safi na rehema kwa wote zikitoka katika makao makuu ya serikali unayoishi chini yake?

“HABARI NJEMA” ZINAZOKAMATANA NA ENZI KUU YA MUNGU

7. “Habari njema” ina uhusiano (ukamanatano) gani wa moja kwa moja na enzi kuu ya Mungu, na kwa hiyo, kutangaza “habari njema” kunaendeleza nini?

7 Habari njema za Ufalme zina ukamatano wa moja kwa moja na enzi kuu ya Mungu. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo katika Rumi hivi: “Mungu na ashukuriwe, kwa maana mlikuwa watumwa wa dhambi, lakini mliitii kwa mioyo yenu ile namna ya elimu ambayo mliwekwa chini yake.” Wale wanaosikia kwa moyo mzuri na kutii hawaambiwi hapa kwamba “habari njema” ‘iliwekwa chini yao, bali kwamba wao ‘waliwekwa chini ya namna hiyo ya elimu,’ injili hiyo au habari njema za Ufalme. Sasa wao ni raia wenye nia na wanaounga mkono enzi kuu ya Mungu. Wao nao wanapotangaza “habari njema,” wanaozipokea wanawekwa chini ya namna hiyo ya elimu. Hii inaongeza nini duniani? Haki, fadhili za upendo na rehema. Kwa kuwa, mahali pa uchafu na uasi wao wa sheria waliokuwa nao hapo zamani, wao ‘sasa wanatoa viungo vya miili yao vitumiwe na haki.’​—Rum. 6:17-19.

SABABU GANI UITII ENZI KUU YA MUNGU

8. Sababu ya kutii enzi kuu ya Mungu ni nini?

8 Sababu ya kutii enzi kuu ya Mungu ni nini? Ni kumpenda Mungu kwa sababu ya sifa zake, na vilevile kupenda yaliyo mema na yenye kufaa kuumba kote. Mtu anayefahamu yanayomaanishwa na enzi kuu ya Yehova anaipendelea kuliko enzi nyingine zote. Kwa kweli, wale wanaounga mkono utawala wa Mungu wanapendelea kuwa nao kuliko kujitegemea kabisa, ikiwa ingaliwezekana. Kwa sababu gani? Kwa sababu wanajua kwamba watakuwa na furaha zaidi chini ya enzi kuu ya Mungu kuliko wanavyoweza kuwa ikiwa wangeweza kufanya lo lote watakalo. Wao wanajua kwamba hekima, upendo, maarifa na uweza wa Mungu ni mkubwa sana kuliko wao, hauwezi kulinganishwa. Wanadamu hawawezi kuendeleza maisha yao milele, wala hawawezi kuleta amani, haki na haki ya hukumu duniani pote. “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu,” akasema Yeremia, mwunga-mkono mwaminifu wa enzi kuu ya Yehova.​—Yer. 10:23.

9. Yehova anawasihije wale wasioikubali enzi yake kuu?

9 Maoni ya Yehova kuelekea wale wasiokubali enzi kuu yake ni yenye fadhili kuu. Nabii wake alisema hivi: “Mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie [Yehova], naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa. Maana mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu; asema [Yehova]. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”​—⁠Isa. 55:7-9.

KUTUMIKIA INAVYOFAA CHINI YA ENZI KUU YA MUNGU

10. Takwa la maana sana ili kutumikia kwa kufaa chini ya enzi kuu ya Mungu ni takwa gani?

10 Kutumikia inavyofaa kwa ajili ya enzi kuu ya Mungu, au chini yake mtu anapaswa amjue Yehova Mungu na Mwanawe Yesu Kristo, Mfalme wa ufalme wa Mungu. “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Kumjua Mungu ni kuwa na uhusiano (urafiki) wa karibu pamoja naye, kuwa msiri wake na wa Mwanawe, aliyesema hivi: “Hakuna amjuaye Mwana, ila Baba; wala hakuna amjuaye Baba, ila Mwana, na ye yote ambaye Mwana apenda kumfunulia.” (Mt. 11:27) Amjuaye Mungu anajua sifa zake za ajabu, na kwa msaada wa roho ya Mungu anasaidiwa asitawishe sifa hizo, hivi kwamba anakaribia zaidi na zaidi katika kuuonyesha mfano wa Mungu. (2 Kor. 3:18) Ikiwa mtu hasitawishi matunda ya roho hiyo, yeye hajamjua Mungu. Kwa mfano, mtume Yohana anasema hivi: “Yeye asiyependa, hakumjua Mungu, kwa maana Mungu ni upendo.”​—1 Yohana 4:8.

11. Mtu anayekubali enzi kuu ya Mungu anatendaje? Toa mifano?

11 Mtu anayekubali enzi kuu ya Mungu anatendaje? Sifa zake kuu zitakuwa upendo, rehema, fadhili na kuwafanyia wanadamu wenzake mema. Ikiwa yeye ni mzee katika kundi fulani au ikiwa anaangalia kazi yo yote ya ndugu zake Wakristo, au ya wengine, yeye hatakuwa akitoa amri au kutaka mengi mno. Mtume Paulo ambaye alikuwa na mamlaka zaidi kutoka kwa Mungu kuliko mwanamume mwingine ye yote aliyeko duniani leo, aliliambia kundi katika Rumi: “Ndugu zangu, nawasihi, kwa huruma zake Mungu.” (Rum. 12:1) Alipokuwa Rumi, Paulo alimpata mtu jina lake Onesimo, aliyeziamini “habari njema.” Alipofumbua (alipofahamu) kwamba Onesimo alikuwa mtumwa aliyekuwa ametoroka kutoka kwa bwana yake Filemoni, Mkristo aliyekuwa katika mji wa Kolosai katika Asia Ndogo, Paulo alimshauri Onesimo amrudie bwana yake. Kisha akamwandikia Filemoni, akimsihi amsamehe Onesimo, amkubali sasa kama ndugu. Ebu angalia Paulo alivyosihi kwa fadhili: “Nijapokuwa nina ujasiri katika Kristo kukuagiza likupasalo; lakini, kwa ajili ya upendo nakusihi.” “Kwa kuwa nakuamini kutii kwako ndiyo maana nimekuandikia, nikijua ya kuwa utafanya zaidi ya hayo nisemayo.”​—Filemoni 8, 9, 21.

12. (a) Ni kwa sababu gani tumaini alilolionyesha Paulo katika Filemoni ni maoni yanayofaa wanayopaswa kuwa nayo waangalizi? (b) Kristo alionyeshaje kwamba aliwatumaini Paulo na Timotheo?

12 Bila shaka Filemoni hangejisikia kwamba angekuwa akitenda kwa kushurutishwa, kwa hiyo angefurahia kutii. Angekuwa tayari kabisa kutii kusihi kwa Paulo, vilevile angekuwa na wajibu wa kufanya hivyo zaidi, kwa sababu Paulo alimtumaini sana. Vivyo hivyo, mzee au mwangalizi awatiaye wengine moyo na kutumaini ndugu wanapopewa kazi atapata matokeo zaidi kuliko mwangalizi aamuruye, au anayejiona kwamba hakuna mtu awezaye kufanya kazi fulani vizuri kama anavyoweza kuifanya yeye mwenyewe. Kumtumaini ndugu kunamsaidia atumie akili zake pamoja na jitihada. Mwangalizi kama huyo anawakilisha enzi kuu ya Mungu katika njia inayofaa naye anafuata mfano wa Kristo. Kristo alimtendea hivyo Paulo. Kwa kuthamini Paulo alisema hivi: “Namshukuru Kristo Yesu Bwana wetu, aliyenitia nguvu kwa sababu aliniona mwaminifu, akaniweka katika utumishi wake.” (1 Tim. 1:12) Naye Paulo alionyesha kwamba Mungu, Kristo na yeye mwenyewe waliutumaini uaminifu wa Timotheo pamoja na uwezo wake wa kutimiza utumishi aliogawiwa, alipoandika hivi: “Ee Timotheo, ilinde hiyo amana.”​—1 Tim. 6:20.

13, 14. (a) Mkristo atawakilishaje enzi kuu ya Mungu kwa kufaa anapojifunza na wenye kupendezwa? (b) Ni wajibu gani wa maana sana wa waangalizi unaoonyeshwa na maneno ya mtume Paulo kwa Timotheo na kwa wazee wa mji wa Efeso?

13 Mkristo mwema atawakilisha enzi kuu ya Mungu inavyofaa anapojifunza na wengine, kwa kujitahidi awafundishe watu hawa yote awezayo, kama alivyoagiza Yesu: “Mkafanye wanafunzi . . . kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20, NW) Ikiwa yeye ni mwangalizi, yeye hataonea wivu maarifa yake au aogope kwamba huenda mtu mwingine akamshinda kwa kujua mambo mengi zaidi au kwa kusitawisha uwezo mwingi zaidi. Mtume alimwagiza Timotheo hivi: “Mambo yale uliyoyasikia kwangu mbele ya mashahidi wengi, hayo uwakabidhi watu waaminifu watakaofaa kuwafundisha na wengine.”​—2 Tim. 2:2.

14 Mwangalizi anapaswa kuwafundisha wale walio karibu naye yote anayoyajua ili waweze kufanya kazi hiyo. Si kwamba tu anawasaidia kwa kufanya hivyo, bali vilevile anawawezesha kutimiza mambo ikiwa yeye hayupo. Kwa njia hiyo mwangalizi huyo anaonyesha kwamba anahangaikia kweli kweli hali njema na maendeleo ya kundi, wala hajifikirii mwenyewe tu. Kwa maana, ingekuwaje ikiwa angekuwa mgonjwa, au afe, au ahamie mahali pengine? Paulo aliwaambia waangalizi katika Efeso hivi: “Sikujiepusha katika kuwatangazia neno lo lote liwezalo kuwafaa, bali naliwafundisha waziwazi, na nyumba kwa nyumba.” Alikutana na wanaume hawa alipokuwa akitoa ushuhuda waziwazi. Yeye hakuwafundisha tu mpaka kubatizwa. Mahali pake, ‘aliwashuhudia’ kabisa mpaka wakapata ufahamu kamili wa kusudi la Mungu, enzi yake kuu kupitia kwa Kristo pamoja na uhusiano wao nayo. Vilevile aliwaambia hivi: “Sikujiepusha na kuwahubiri habari ya kusudi lote la Mungu.”​—Matendo 20:20, 21, 27.

ENZI KUU YA YEHOVA INAONGEZA FURAHA NA SIFA

15. Ni hali gani inayopaswa kuwapo katika mahali ambapo enzi kuu ya Mungu inakubaliwa?

15 Ikiwa kila Mkristo atakumbuka sifa bora za enzi kuu ya Mungu, ataongeza furaha. Kwa habari ya Yehova, imesemwa hivi: “Heshima na [ukuu] ziko mbele zake; nguvu na furaha zipo mahali pake.” (1 Nya. 16:27) Pasipo furaha, ambalo ni tunda la roho ya Mungu, kuvunjika moyo, ubaridi, hata machafuko yanakuwapo. Mtume aliwauliza Wakristo Wagalatia ambao walikuwa wamekuwa dhaifu kiroho, “Basi wapi furaha yenu [mliyokuwa nayo mlipoziamini habari njema kwa mara ya kwanza]?” (Gal. 4:15, ZSB) Hali ya furaha ndiyo hali inayositawishwa na enzi kuu ya Mungu kati ya wale wote wanaompenda Mungu na wanaomtumikia kwa moyo wote. Mtunga zaburi aliimba hivi: “Heri watu wale waijuao sauti ya shangwe, Ee [Yehova], huenenda katika nuru ya uso wako. Kwa jina lako hufurahi mchana kutwa, na kwa haki yako hutukuzwa. Maana fahari ya nguvu zao ni Wewe, na kwa radhi yako pembe yetu itatukuka.”​—Zab. 89:15-17.

16. Enzi kuu ya Yehova itailetea nini dunia?

16 Kuanzia mbingu zenye nyota, ambazo “zauhubiri utukufu wa Mungu,” mpaka dunia yenyewe, ni wazi kwamba uumbaji wa Mungu ni mkuu na wenye fahari. (Zab. 19:1) Kuna amani, utaratibu na uzuri katika fahari ya jua, mwezi na nyota, nayo dunia pamoja na viumbe vyenye uhai juu yake, ina uzuri usioweza kulinganika, isipokuwa mahali ambapo mwanadamu ameharibu. Ebu wazia namna dunia itakavyokuwa mahali pazuri wakati wanadamu watakapoletwa katika umoja na enzi kuu ya Mungu! Si uzuri tu wa vitu vyenye mwili katika mbingu na duniani, bali sana sana sifa zilizo za maana sana na za ajabu sana za Aliye Juu Zaidi, wakati ambapo ‘kumjua Yehova kutakapojaa duniani kama maji yanavyoifunika bahari,’ bila shaka kutawafanya wote watakaokuwa wakiishi wakati huo waimbe juu ya uzuri wa enzi kuu ya Mungu.​—Isa. 11:9; Zab. 150.

17. “Habari njema” inapaswa ituongozeje leo?

17 Vilevile, tuutazamiapo wakati huo wa furaha sana, na tujitoe sana kwa furaha sasa, wakati wa siku hizi zinazomalizika za hii “taratibu mbovu ya mambo,” tuwajulishe wote watakaosikiliza “habari njema tukufu za Mungu wa furaha.” Kwa kuwa Yehova peke yake ndiye anayepaswa kusifiwa kwa kuwa ndiye “Bwana Mwenye Enzi Kuu, . . . Yeye aliyeziumba mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.”​—Matendo 4:24, NW; Gal. 1:4, NW; 1 Tim. 1:11, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki