Sura ya 1
Kwa Nini Yehova Awe Na Mashahidi?
MASHAHIDI WA YEHOVA wajulikana ulimwenguni pote kwa kuendelea kuongea na watu kila mahali juu ya Yehova Mungu na Ufalme wake. Pia wana sifa ya kuwa jamii ya watu washikamanao na imani zao zijapokuwa namna zote za upinzani, hata kifo.
“Wateswa wakuu wa mnyanyaso wa kidini katika Marekani katika karne ya ishirini walikuwa Mashahidi wa Yehova,” chasema kitabu The Court and the Constitution, kilichotungwa na Archibald Cox (1987). “Mashahidi wa Yehova . . . wamesumbuliwa na kunyanyaswa na serikali ulimwenguni pote,” asema Tony Hodges. “Katika Ujerumani ya Nazi walisakwa na kupelekwa ndani ya kambi za mateso. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Sosaiti [ya Watch Tower] ilipigwa marufuku katika Australia na Kanada. . . . Sasa [katika miaka ya 1970] Mashahidi wa Yehova wanahangaishwa Afrika.”—Jehovah’s Witnesses in Africa, Chapa ya 1985.
Ni nini sababu ya mnyanyaso huo? Ni nini shabaha ya kuhubiri huko? Je, kweli Mashahidi wa Yehova wamepewa utume na Mungu? Kwa nini Yehova hata awe na mashahidi—tena mashahidi wa kibinadamu wasio wakamilifu? Majibu yahusiana na masuala fulani yanayojadiliwa katika kesi ya mahakama ya ulimwengu wote mzima—hiyo ikiwa ndiyo kesi ya maana zaidi iliyopata kujadiliwa. Ni lazima tuchunguze masuala hayo ili kuelewa kwa nini Yehova ana mashahidi na kwa nini mashahidi hao wako tayari kuvumilia hata upinzani ulio mkali zaidi.
Enzi Kuu ya Yehova Yakaidiwa
Masuala muhimu haya yahusu uhalali wa enzi kuu, au utawala mkuu zaidi, wa Yehova Mungu. Yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima kwa sababu ya hali yake ya kuwa Muumba, Uungu wake, na Uweza-Yote wake. (Mwa. 17:1; Kut. 6:3; Ufu. 4:11) Hivyo ana haki ya kuwa na mamlaka juu ya kila kitu mbinguni na duniani. (1 Nya. 29:12) Lakini sikuzote yeye husimamia enzi kuu yake kwa upendo. (Linganisha Yeremia 9:24.) Basi, yeye huomba apewe nini kama shukrani kutoka kwa viumbe vyake vyenye akili? Kwamba wampende na kuithamini enzi kuu yake. (Zab. 84:10) Hata hivyo, maelfu ya miaka iliyopita shtaka lilivurumishwa dhidi ya enzi kuu halali ya Yehova. Jinsi gani? Na nani? Mwanzo, kitabu cha kwanza cha Biblia, chaangazia jambo hilo.
Charipoti kwamba Mungu aliumba wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, na akawapa makao mazuri ya kibustani. Yeye pia aliwapa amri hii: ‘Matunda ya kila mti wa bustani mwaweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya msile, kwa maana siku mtakapokula matunda ya mti huo mtakufa hakika.’ (Mwa. 2:16, 17) “Mti wa ujuzi wa mema na mabaya” ulikuwa nini, na kula baadhi ya matunda yake kungemaanisha nini?
Ulikuwa mti halisi, lakini Mungu aliutumia kwa kusudi la ufananisho. Kwa sababu aliuita “mti wa ujuzi wa mema na mabaya” na kwa sababu aliamuru kwamba wanadamu wawili wa kwanza wasile baadhi ya matunda, kwa kufaa mti huo ulifananisha haki ya Mungu kuamulia wanadamu yaliyo “mema” (yenye kumpendeza Mungu) na yaliyo “mabaya” (yasiyompendeza Mungu). Hivyo kuwapo kwa mti huo kulitahini staha ya mwanadamu kuelekea enzi kuu ya Mungu. Kwa kuhuzunisha, wanadamu wawili wa kwanza hawakumtii Mungu, wakala baadhi ya tunda lililokatazwa. Walishindwa mtihani huo ulio rahisi lakini wenye maana sana wa utii na uthamini.—Mwa. 3:1-6.
Kitendo hicho chenye kuonekana kana kwamba ni kidogo kilikuwa uasi dhidi ya enzi kuu ya Yehova. Jinsi gani hivyo? Kuelewa jinsi ambavyo sisi wanadamu tumefanyizwa ni ufunguo wa kuelewa umaana wa jambo ambalo Adamu na Hawa walitenda. Yehova alipoumba wanadamu wa kwanza wawili, aliwapa zawadi nzuri ajabu—hiari. Akikamilisha zawadi hiyo, Yehova aliwapa uwezo wa akili uliotia ndani nguvu ya ufahamu, ya kufikiri, na ya kuamua. (Ebr. 5:14) Hawakuwa kama maroboti (mashine-watu) wasiofikiri; wala hawakuwa kama wanyama, ambao hutenda sanasana kwa silika. Ingawa hivyo, uhuru wao ulikuwa wa kadiri, ukitegemea sheria za Mungu. (Linganisha Yeremia 10:23, 24.) Adamu na Hawa walichagua kula baadhi ya tunda lililokatazwa. Hivyo walitumia vibaya uhuru wao. Ni nini kilichowaongoza kwenye mwendo huo?
Biblia yaeleza kwamba kiumbe-roho wa Mungu alikuwa amechukua mwendo wa kimakusudi wenye upinzani na ukinzani kwa Mungu. Huyu, ambaye baadaye akaja kujulikana kuwa Shetani, alisema kupitia nyoka katika Edeni na kumwongoza Hawa, na kupitia Hawa, Adamu, waache kujitiisha chini ya enzi kuu ya Mungu. (Ufu. 12:9) Kwa kula matunda ya mti huo, Adamu na Hawa waliweka uamuzi wao juu ya ule wa Mungu, wakionyesha kwamba walitaka kujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya.—Mwa. 3:22.
Hivyo suala lililotokezwa lilikuwa, Je, Yehova ana haki ya kutawala wanadamu, na je, anatumia enzi kuu yake kwa masilahi bora zaidi za raia zake? Suala hilo lilidokezwa waziwazi na maneno haya ya Nyoka kwa Hawa: “Ati! hivi ndivyo alivyosema Mungu, Msile matunda ya miti yote ya bustani?” Dokezo lilikuwa kwamba Mungu alikuwa akinyima kimakosa mwanamke huyo na mumeye kitu fulani chema.—Mwa. 3:1.
Uasi katika Edeni ulitokeza suala jingine: Je, wanadamu wanaweza kuwa waaminifu kwa Mungu wakitahiniwa? Suala hilo lenye kuhusiana lilieleweshwa karne 24 baadaye kuhusiana na Ayubu mwaminifu. Shetani, aliyetoa ‘sauti’ akimfanya nyoka aonekane kusema, alimshtaki Yehova waziwazi, akisema: “Je, huyo Ayubu yuamcha BWANA [“Yehova,” NW] bure?” Shetani alidai hivi: “Wewe hukumzingira kwa ukigo pande zote, pamoja na nyumba yake, na vitu vyote alivyo navyo? kazi za mikono yake umezibarikia, nayo mali yake imeongezeka katika nchi.” Hivyo Shetani alidokeza kwamba unyoofu wa Ayubu ulisukumwa na tamaa za kibinafsi. Alishtaki zaidi hivi: “Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” Kwa kuwa, kama vile Yehova alivyokuwa ameona, ‘hapakuwa na mmoja kama Ayubu duniani,’ kwa kweli Shetani alikuwa akidai kwamba angeweza kumwondoa kutoka Kwake mtumishi yeyote wa Mungu. (Ayu. 1:8-11; 2:4) Hivyo watumishi wote wa Mungu walishtakiwa kwa njia isiyo ya moja kwa moja kuhusu uaminifu-maadili na uaminifu-mshikamanifu wao kwa enzi kuu Yake.
Yakiisha kutokezwa, ilikuwa lazima masuala hayo yajibiwe. Kupita kwa wakati—kama miaka 6,000 sasa—na kushindwa vibaya sana kwa serikali za kibinadamu kwaonyesha wazi kwamba wanadamu wanahitaji enzi kuu ya Mungu. Lakini je, wao wanaitaka? Je, kuna wanadamu ambao watadhihirisha utambuzi wa kutoka moyoni kwa enzi kuu adilifu ya Yehova? Ndiyo! Yehova ana mashahidi wake! Lakini kabla hatujafikiria ushuhuda wao, acheni kwanza tuchunguze yahusikayo katika kuwa shahidi.
Linalomaanishwa na Kuwa Shahidi
Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “shahidi” huandaa ufahamu wa ndani juu ya maana ya kuwa shahidi kwa ajili ya Yehova. Katika Maandiko ya Kiebrania, nomino iliyofasiriwa “shahidi” (‘edh) imetolewa katika kitenzi (‘udh) kinachomaanisha “rudia” au “rudia kusema, fanya tena.” Kuhusu nomino (‘edh), Theological Wordbook of the Old Testament chasema hivi: “Shahidi ni yeye, ambaye kwa kukariri, huthibitisha ushuhuda wake kwa mkazo. Neno hilo [‘edh] ni neno ambalo hutumika kwa ukawaida katika lugha ya mahakama.” A Comprehensive Etymological Dictionary of the Hebrew Language for Readers of English huongezea hivi: “Maana ya awali [ya kitenzi ‘udh] yaweza [labda] kuwa ilikuwa ‘yeye alisema kwa kurudiarudia na kwa nguvu.’”
Katika Maandiko ya Kikristo, maneno ya Kigiriki yaliyofasiriwa “shahidi” (marʹtys) na “kutoa ushahidi” (mar·ty·reʹo) yalikuwa pia na wazo la kisheria, ingawa baada ya muda yalipata maana pana zaidi. Kulingana na Theological Dictionary of the New Testament, “wazo la shahidi [latumiwa] katika maana ya ushahidi wa mambo ya hakika yawezayo kuhakikishwa na pia katika ile ya ushahidi kwa mambo ya kweli, m.y., kujulisha na kukiri masadikisho.” Hivyo shahidi husimulia mambo hakika kutokana na ujuzi wa moja kwa moja wa kibinafsi au hupiga mbiu ya maoni au mambo ya kweli ambayo anasadiki.a
Mwendo wa uaminifu wa Wakristo wa karne ya kwanza ulisogeza mbele hatua moja zaidi maana ya neno “shahidi.” Wengi wa Wakristo hao wa mapema walitoa ushahidi chini ya mnyanyaso na kwa kukabili kifo. (Mdo. 22:20; Ufu. 2:13) Tokeo ni kwamba, kufikia kama karne ya pili W.K., neno la Kigiriki kwa shahidi (marʹtys, ambalo kutokana nalo pia limetolewa neno “martyr”) lilipata maana iliyotumika kwa watu walio tayari “kuthibitisha uzito wa ushahidi au ukiri wao kwa kifo.” Hawakuitwa mashahidi kwa sababu walikufa; walikufa kwa sababu walikuwa mashahidi waaminifu-washikamanifu.
Basi, ni nani waliokuwa mashahidi wa mapema wa Yehova? Ni nani waliokuwa tayari kupiga mbiu “kwa kurudiarudia na kwa nguvu”—kwa maneno na kwa jinsi walivyoishi—kwamba Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu aliye halali, astahiliye? Ni nani waliokuwa tayari kudumisha uaminifu-maadili kwa Mungu, hata kifo?
Mashahidi wa Yehova wa Ramaniema
Mtume Paulo asema hivi: “Kwa sababu tuna wingu [Kigiriki, neʹphos, kuonyesha tungamo la wingu] kubwa hivyo la mashahidi likituzingira.” (Ebr. 12:1, NW) Hilo ‘tungamo la wingu’ la mashahidi lilianza kufanyika upesi baada ya uasi dhidi ya enzi kuu ya Mungu katika Edeni.
Kwenye Waebrania 11:4 (NW), Paulo atambulisha Abeli kuwa shahidi wa kwanza wa Yehova, akisema: “Kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu, Mungu akitoa ushahidi kwa habari ya zawadi zake; na kupitia hiyo yeye, ijapokuwa alikufa, bado asema.” Abeli alitumikaje kuwa shahidi kwa ajili ya Yehova? Jibu lahusu sababu iliyofanya dhabihu ya Abeli iwe ya “thamani kubwa zaidi” ya ile ya Kaini.
Kwa maneno rahisi, Abeli alitoa toleo lifaalo kwa kusudi lifaalo na kulitegemeza kwa kazi zifaazo. Zawadi yake aliyoitoa ilikuwa dhabihu ya damu ikiwakilisha uhai wa wazaliwa wa kwanza wa kundi la wanyama wake—hali Kaini alitoa mazao yasiyo na uhai. (Mwa. 4:3, 4) Dhabihu ya Kaini ilikosa kichocheo cha imani iliyofanya toleo la Abeli likubalike. Kaini alipaswa kurekebisha ibada yake. Badala yake, yeye alidhihirisha mwelekeo wake mbaya wa moyo kwa kukataa shauri na onyo la Mungu na kwa kumwua kimakusudi Abeli mwaminifu.—Mwa. 4:6-8; 1 Yoh. 3:11, 12.
Abeli alionyesha imani ambayo wazazi wake waliikosa. Kwa mwendo wake wa uaminifu, yeye alijulisha usadiki wake kwamba enzi kuu ya Yehova ni adilifu na yenye kustahili. Muda wa ile karne moja hivi aliyoishi, Abeli alionyesha kwamba binadamu aweza kuwa mwaminifu kwa Mungu kufikia kuthibitisha ushuhuda wake kwa kifo. Na damu ya Abeli yaendelea ‘kunena,’ kwa maana rekodi yenye kupuliziwa ya ufia-imani wake ilihifadhiwa katika Biblia kwa ajili ya vizazi vya wakati ujao!
Karibu karne tano baada ya kifo cha Abeli, Henoko alianza ‘kwenda pamoja na Mungu,’ akifuatia mwendo wenye kupatana na viwango vya Yehova vya mema na mabaya. (Mwa. 5:24) Kufikia hapo, kukataliwa kwa enzi kuu ya Mungu kulikuwa kumeongoza kwenye ongezeko kubwa la mazoea ya kutomhofu Mungu miongoni mwa wanadamu. Henoko alisadiki kwamba Mwenye Enzi Aliye Mkuu Zaidi angechukua hatua dhidi ya watu wasiomhofu Mungu, na roho ya Mungu ilimsukuma kupiga mbiu ya kuharibiwa kwao kwa wakati ujao. (Yuda 14, 15) Henoko aliendelea kuwa shahidi mwaminifu hadi kifo, kwa maana Yehova ‘alimhamisha,’ yaelekea akimwepusha na kifo cha jeuri mikononi mwa adui zake. (Ebr. 11:5, NW) Hivyo jina la Henoko lingeweza kuongezwa kwenye orodha iliyokuwa ikikua ya lile ‘wingu kubwa la mashahidi’ wa nyakati za kabla ya Ukristo.
Roho ya kutomhofu Mungu iliendelea kuenea katika mambo ya kibinadamu. Wakati wa maisha ya Nuhu, aliyezaliwa kama miaka 70 baada ya kifo cha Henoko, wana wa kimalaika wa Mungu walikuja duniani, kwa wazi wakivaa umbo la kibinadamu, na kukaa unyumba na wanawake wenye kuvutia. Wazao waliowazaa waliitwa Wanefili; walikuwa majitu miongoni mwa wanadamu. (Mwa. 6:1-4) Ni nini lilikuwa tokeo la muungano huo usio wa asili wa viumbe-roho pamoja na wanadamu na la jamii ya mchanganyiko iliyozaliwa? Maandishi yaliyopuliziwa hujibu hivi: “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote. Mungu akaiona dunia, na tazama, imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani.” (Mwa. 6:5, 12) Lo, ni sikitiko kama nini kwamba dunia, mahali pa kuweka miguu pa Mungu, ‘ilijaa jeuri.’—Mwa. 6:13; Isa. 66:1.
Tofauti na hivyo, “Nuhu alikuwa mtu wa haki [“mwadilifu,” NW],” ambaye alithibitika kuwa “mkamilifu katika vizazi vyake.” (Mwa. 6:9) Alionyesha unyenyekeo wake kwa enzi kuu ya Mungu kwa kufanya ‘sawasawa na vile Mungu alivyoamuru.’ (Mwa. 6:22) Akitenda kwa imani, ‘alijenga safina kwa ajili ya kuokoa watu wa nyumbani mwake.’ (Ebr. 11:7, NW) Lakini Nuhu alikuwa ni zaidi ya mjenzi tu; akiwa “mhubiri [au kijumbe] wa uadilifu,” alionya juu ya uharibifu uliokuwa unakuja. (2 Pet. 2:5, NW) Hata hivyo, ijapokuwa Nuhu alitoa ushahidi kijasiri, kizazi hicho kiovu ‘hakikujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote.’—Mt. 24:37-39, NW.
Kufuatia siku za Nuhu, Yehova alikuwa na mashahidi miongoni mwa wazee wa ukoo wa baada ya Furiko. Abrahamu, Isaka, Yakobo, na Yusufu hutajwa kuwa sehemu ya mapema ya lile wingu la mashahidi wa kabla ya Ukristo. (Ebr. 11:8-22; 12:1) Walionyesha kuwa waliunga mkono enzi kuu ya Yehova, wakifanya hivyo kwa kuendeleza uaminifu-maadili. (Mwa. 18:18, 19) Hivyo walichangia kutakaswa kwa jina la Yehova. Kuliko kutafuta usalama katika ufalme fulani wa kidunia, ‘walitangaza hadharani kwamba wao walikuwa watu wasiojulikana na wakaaji wa muda katika nchi,’ kwa imani ‘wakingojea jiji lililo na misingi halisi, ambalo mjenzi na mfanyi wa jiji hilo ni Mungu.’ (Ebr. 11:10, 13, NW) Walimkubali Yehova kuwa Mtawala wao, wakitia nanga ya tumaini lao katika Ufalme wa kimbingu ulioahidiwa kuwa wonyesho wa uhalali wa enzi kuu yake.
Katika karne ya 16 K.W.K., wazao wa Abrahamu walikuwa watumwa wenye kuhitaji kukombolewa kutoka utumwa wa Kimisri. Hapo ndipo Musa na Haruni ndugu yake walipokuja kuwa wahusika wakuu katika ‘pigano la miungu.’ Walitokea mbele ya Farao na kujulisha neno mkataa la Yehova: “Wape watu wangu ruhusa waende.” Lakini Farao mwenye kiburi akafanya moyo wake mgumu; hakutaka kupoteza taifa kubwa la wafanyakazi watumwa. “BWANA [“Yehova,” NW] ni nani,” yeye akajibu, “hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao? Mimi simjui BWANA [“Yehova,” NW], wala sitawapa Israeli ruhusa waende zao.” (Kut. 5:1, 2) Kwa itikio hilo lenye madharau, Farao, ambaye yeye mwenyewe aliaminiwa kuwa mungu aliye hai, alikataa kutambua Uungu wa Yehova.
Suala la uungu likiwa limetokezwa, sasa Yehova akachukua hatua na kuthibitisha kwamba yeye ndiye Mungu wa kweli. Farao, kupitia makuhani wake wenye kufanya mizungu ya kiuchawi, aliitisha nguvu za muungano wa miungu ya Misri kukaidi nguvu za Yehova. Lakini Yehova alipeleka mapigo kumi, kila moja likitangazwa na Musa na Haruni, kuonyesha mamlaka yake juu ya nguvu-asili za dunia na viumbe na pia ukuu wake upitao wote juu ya miungu ya Misri. (Kut. 9:13-16; 12:12) Kufuatia pigo la kumi, Yehova alitoa Israeli kutoka Misri kwa “mkono wenye uwezo.”—Kut. 13:9.
Musa, ‘mpole sana zaidi ya wanadamu wote,’ alihitaji ushujaa mwingi na imani ili kwenda kumwona Farao, si mara moja, bali mara nyingi. (Hes. 12:3) Hata hivyo, Musa hakupunguza kamwe uzito wa ujumbe ambao Yehova alimwamuru amtolee Farao. Hata tisho la kifo halingeweza kunyamazisha ushuhuda wake! (Kut. 10:28, 29; Ebr. 11:27) Musa alikuwa shahidi katika ile maana halisi ya neno hilo; alishuhudia “kwa kurudiarudia na kwa nguvu” Uungu wa Yehova.
Kufuatia ukombozi huo kutoka Misri katika 1513 K.W.K., Musa aliandika kitabu cha Mwanzo. Hivyo enzi mpya ikaanza—enzi ya kuandika Biblia. Kwa kuwa yaonekana Musa ndiye aliyeandika kitabu cha Ayubu, alikuwa na ufahamu fulani juu ya suala kati ya Mungu na Shetani. Lakini kadiri kuandikwa Biblia kulivyoendelea, masuala yanayohusu enzi kuu ya Mungu na uaminifu-maadili wa binadamu yangeandikwa wazi katika maandishi; hivyo wahusika wote wangepata ujuzi kamili juu ya masuala makubwa yaliyohusika. Wakati huohuo, katika 1513 K.W.K., Yehova aliweka msingi wa kutokeza taifa la mashahidi.
Taifa la Mashahidi
Katika mwezi wa tatu baada ya kuondoka Misri, Yehova aliwaleta Waisraeli katika uhusiano wa pekee wa agano pamoja naye, akiwafanya “mali [yake] ya pekee.” (Kut. 19:5, 6, NW) Kupitia Musa, sasa yeye alishughulika nao wakiwa taifa, akiwapa serikali ya kitheokrasi yenye msingi juu ya agano la Sheria likiwa katiba yao ya kitaifa. (Isa. 33:22) Walikuwa watu wa Yehova waliochaguliwa, waliopangwa kitengenezo kumwakilisha akiwa Bwana Mwenye Enzi Kuu wao.
Hata hivyo, katika karne zilizofuata, taifa hilo halikukiri sikuzote enzi kuu ya Yehova. Baada ya kukaa katika Bara Lililoahidiwa, nyakati fulani Israeli waliacha ibada ya kweli na kuabudu miungu ya roho waovu ya mataifa. Kwa sababu ya wao kushindwa kumtii akiwa Mwenye Enzi Kuu aliye na haki, Yehova aliwaruhusu watekwe nyara, na hivyo ikaonekana kwamba miungu ya mataifa ilikuwa na nguvu kuliko Yehova. (Isa. 42:18-25) Lakini katika karne ya nane K.W.K., Yehova aliikabili waziwazi miungu ya mataifa ili aondoe kabisa wazo baya hilo na kujibu kabisa lile swali, Ni nani aliye Mungu wa kweli?
Kupitia nabii Isaya, Yehova alitokeza kabiliano hili: “Ni nani miongoni mwao [miungu ya mataifa] awezaye kuhubiri neno hili [kutoa unabii kwa usahihi], na kutuonyesha mambo ya zamani [yaani, kutoa mambo kimbele]? na walete mashahidi wao [ikiwa wao ni miungu], wapate kuhesabiwa kuwa na haki; au na [waache watu wa mataifa] wasikie, wakaseme, Ni kweli”! (Isa. 43:9) Ndiyo, acheni miungu ya mataifa itokeze mashahidi ambao wangeweza kushuhudia unabii wa miungu yao kwamba, “Ni kweli”! Lakini hakuna hata mmoja wa miungu hao ambaye angeweza kutokeza mashahidi wa kweli kutetea uungu wayo!
Yehova alijulisha Israeli daraka lao katika kujibu kabisa lile swali, Ni nani aliye Mungu wa kweli? Alisema: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . mtumishi niliyemchagua; mpate kujua, na kuniamini, na kufahamu ya kuwa mimi ndiye; kabla yangu hakuumbwa Mungu awaye yote, wala baada yangu mimi hatakuwapo mwingine. Mimi, naam, mimi, ni BWANA [“Yehova,” NW], zaidi yangu mimi hapana mwokozi. Nimetangaza habari, nimeokoa, nimeonyesha, na hapakuwa mungu wa kigeni kati yenu; kwa sababu hiyo nyinyi ni mashahidi wangu, . . . nami ni Mungu.”—Isa. 43:10-12.
Hivyo, Israeli, watu wa Yehova, walijumuika kuwa taifa la mashahidi. Wangeweza kuthibitisha kwa mkazo enzi kuu ya Yehova iliyo haki yake, anayoistahili. Kwa msingi wa maono yao ya wakati uliopita, wangeweza kupiga mbiu kwa usadikisho kwamba Yehova ndiye Mkombozi Mkuu wa watu wake na ndiye Mungu wa unabii wa kweli.
Kutoa Ushahidi Kuhusu Mesiya
Ujapokuwa ule ushuhuda mwingi wa “wingu kubwa” hilo la mashahidi wa kabla ya Ukristo, upande wa Mungu wa masuala hayo haukujibiwa kabisa. Kwa nini sivyo? Kwa sababu katika wakati uliowekwa na Mungu, baada ya mambo kudhihirishwa waziwazi kwamba wanadamu wanahitaji utawala wa Yehova na kwamba hawawezi kujitawala peke yao kwa mafanikio, ni lazima Yehova atekeleze hukumu juu ya wote wanaokataa kuheshimu mamlaka yake halali. Isitoshe, masuala yaliyotokezwa yafika mbali zaidi ya mambo ya kibinadamu. Kwa kuwa malaika mmoja alikuwa ameasi katika Edeni, swali la uaminifu-maadili kwa enzi kuu ya Mungu lilifika juu kwenye viumbe wa kimbingu wa Mungu na kuwahusisha. Hivyo, Yehova alikusudia mwana-roho fulani aje duniani, ambako Shetani angekuwa na fursa yote ya kumtahini. Mwana huyo wa roho angepewa fursa ya kujibu, kwa njia kamilifu, lile swali, Je, mtu yeyote atakuwa mwaminifu kwa Mungu chini ya jaribu lolote ambalo huenda likaletwa dhidi yake? Baada ya yeye kuthibitisha uaminifu-mshikamanifu wake, mwana huyo wa Mungu angepewa uwezo akiwa mtetezi mkuu wa Yehova, ambaye angeharibu waovu na kutimiza kabisa kusudi la awali la Mungu kuhusu dunia.
Lakini huyo angetambuliwaje? Katika Edeni, Yehova alikuwa ameahidi kutokea kwa “mbegu” ambaye angemchubua kichwani yule Mpinzani aliye kama nyoka na kutetea enzi kuu ya Mungu. (Mwa. 3:15, NW) Kupitia manabii wa Kiebrania, Yehova aliandaa kirefu maelezo juu ya “mbegu” huyo wa Kimesiya—hali za malezi yake na utendaji mbalimbali, hata wakati ambao angetokea.—Mwa. 12:1-3; 22:15-18; 49:10; 2 Sam. 7:12-16; Isa. 7:14; Dan. 9:24-27; Mika 5:2.
Kufikia katikati ya karne ya tano K.W.K., Maandiko ya Kiebrania yalipokamilishwa, unabii mbalimbali ulikuwa umekwisha kuandikwa, ukingoja kuwasili kwa Mesiya ili autimize. Ushuhuda wa shahidi huyo—kwa kweli, shahidi mkuu zaidi wa Mungu—utafikiriwa katika sura inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa kielelezo, Wakristo fulani wa karne ya kwanza wangeweza kutoa ushahidi juu ya mambo hakika ya kihistoria juu ya Yesu—juu ya maisha, kifo, na ufufuo wake—kwa kutumia ujuzi wao wenyewe. (Mdo. 1:21, 22; 10:40, 41) Hata hivyo, watu ambao baadaye walikuwa na imani katika Yesu wangeweza kutoa ushahidi kwa kupigia wengine mbiu ya umaana wa uhai, kifo, na ufufuo wake.—Mdo. 22:15.
[Blabu katika ukurasa wa 11]
Wanadamu waweza kuchagua kunufaishwa na enzi kuu ya Yehova. Lakini kwanza ni lazima wasikie habari zayo
[Blabu katika ukurasa wa 13]
Abeli ndiye aliyekuwa shahidi wa kwanza wa Yehova
[Blabu katika ukurasa wa 14]
Henoko alitoa ushahidi juu ya hukumu ya Mungu dhidi ya wasiomhofu Mungu
[Blabu katika ukurasa wa 17]
Yehova alijulisha taifa zima daraka lalo likiwa mashahidi wake
[Blabu katika ukurasa wa 18]
“Ninyi ni mashahidi wangu, . . . nami ni Mungu”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Matukio katika Edeni yalitokeza masuala muhimu: Je, enzi kuu ya Yehova ni adilifu? Je, viumbe wake watakuwa waaminifu kwake?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nuhu alikuwa mhubiri wa uadilifu kabla Mungu hajaharibu ulimwengu kwa njia ya gharika
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Musa na Haruni walimtolea Farao ushuhuda kwa bidii juu ya Uungu wa Yehova