Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa
—United States of America
WANAFUNZI wa Biblia walikuwa na maafisi ya makao katika Allegheny, Pennsylvania. Walakini, karibu na mwaka wa 1890, kazi ya kuhubiri habari njema na kukusanya wenye mfano wa kondoo iliyokuwa ikienda mbio mbio ilifanya iwe lazima mpanuko uweko. Kwa hiyo, watu wa Yehova wakajenga jengo lao wenyewe. Lilimalizwa mwaka wa 1889 likjulikana kama “Bible House.” Hapo kwanza lilikuwa haki ya Tower Publishing Company kwa sheria, nalo shirika hili la kibinafsi lilisimamiwa na C. T. Russell likachapia Watch Tower Society vitabu kwa miaka kadha. Katika Aprili 1898, kiwanda na mali hiyo vilitolewa kama msaada kwa Watch Tower Society.
“Bible House” ikawa makao makuu ya Sosaiti kwa karibu miaka 20.
“Mambo yalikuwaje katika Bible House mwaka wa 1907?” auliza Ora Sullivan Wakefield. Akijibu ulizo lake mwenyewe, asema hivi kwa ufupi: “Katika ‘jamaa’ yetu tulikuwa 30 tu na kwa kuwa tulikuwa wachache hiyo ilikuwa jamaa kweli kweli. . . . Sote tulikula, tukalala, tukafanya kazi na kuabudu katika jengo ilo hilo moja. Kanisa dogo pia lilikuwa na mahali pa ubatizo chini ya jukwaa.”
Ebu wazia hilo! Huko nyuma mwaka wa 1890 waliwako karibu washirika 400 tu wenye kutenda wa Watch Tower Society. Lakini roho takatifu ya Yehova ilikuwa ikifanya kazi nayo ilikuwa ikitokeza matokeo mazuri. (Zek. 4:6, 10) Kwa hiyo, miaka iliyofuata wa 1890 ilikuwa na maongezeko. Kwa kweli, mamia ya watu walikusanyika Machi 26, 1899, kukumbuka kifo cha Yesu Kristo, nayo ripoti isiyokamilika ilionyesha vikundi 339 vilikusanyika vikiwa na washiriki 2,501. Kweli, watu wenye mfano wa kondoo walikuwa wakimiminika ‘kuingia zizini.’—Mik. 2:12, NW.
Ukuzi wa kazi ya kuhubiri ulikuwa umechochewa na safari ya C. T. Russell ya kwenda ng’ambo mwaka wa 1891. Katika safari hiyo ya maili 17,000 alikwenda pamoja na kikundi chake Ulaya, Asia na Afrika. Baada ya hapo kukawa na bohari la kuwekea vitabu London. Pia, mipango ilifanywa kuchapa vitabu vya Sosaiti katika Kijeremani, Kifaransa, Kisweden, Kidano-Norwegia, Kipoland, Kigiriki na baadaye, Kiitaliano.
‘NA TWENDE NYUMBANI KWA YEHOVA’
Daudi alifurahi iliposemwa hivi: “Na twende nyumbani kwa [Yehova].” (Zab. 122:1) Kulingana na hilo, Wanafunzi wa Biblia wa kwanza walifurahi kuwa na mikutano na makusanyiko. (Ebr. 10:23-25)
Mikutano hiyo ya zamani ilikuwaje? Mmojawapo ulikuwa juu ya kitabu Tabernacle Shadows of the Better Sacrifices, kilichochapwa kwanza na Sosaiti mwaka wa 1881. Kilizungumza maana ya unabii ya hema (tabernacle) ya Israeli na dhabihu zilizotolewa humo. Hata watoto walifaidika sana kutokana na masomo hayo. Sara C. Kaelin anayekumbuka kwamba mikutano hiyo ilifanywa katika nyumba moja anaeleza hivi: “Kikundi kilikuwa kimeongezeka na nyakati nyingine iliwapasa watoto wakalie ngazi za kwenda orofani, lakini wote walipaswa wajifunze maulizo na kuyajibu. Fahali alifananisha nini? Ua ulifananisha nini? Patakatifu palifananisha nini? Patakatifu Sana palifananisha nini? Siku ya Upatanisho ilifananisha nini? Kuhani Mkuu alifananisha nani? Kuhani mdogo alifananisha nani? Hayo yalikazwa kikiki katika akili zetu hata tungeweza kuona kwa akili zetu Kuhani Mkuu akifanya kazi zake na tulijua yaliyomaanishwa.”
“Wenye Kujitolea watakiwa!”—hicho ndicho kilichokuwa kichwa cha kuvutia cha makala iliyokuwa katika Zion’s Watch Tower la Aprili 15, 1899. Ilipendekeza njia mpya ya kueneza sana kweli za Biblia—njia ambayo bila shaka ingewazukia viongozi wa dini za Jumuiya ya Wakristo (Kristendomu) bila kutazamia. Ili mtu ashiriki katika kazi hii, ilikuwa lazima awe shujaa na mwenye moyo mkavu. (Zab. 31:24) Watu wa Yehova wakati huo walipewa nafasi ya kushiriki katika ugawaji mkubwa sana wa makala 300,000 za kijitabu kipya kilichoitwa “Mpambano Baina ya Biblia na Mageuzi.” Kilipaswa kipewe kwa watu walipokuwa wakitoka makanisani Jumapili. Maelfu ya Wakristo wenye kujitolea yaliitikia kwa moyo wote, kazi kubwa ikafanywa United States, Canada na Ulaya.
KUTUMIA MAGAZETI YA KILIMWENGU
“Sehemu nyingine [ya kazi] isiyoweza kusahauliwa vivi hivi tu,” asema George E. Hannan, “ni kuchapisha kwa Pastor Russell mahubiri katika magazeti ya kilimwengu.” The Watch Tower la Desemba 1, 1916 lilisema, “Zaidi ya magazeti ya kilimwengu 2,000 yalichapwa hotuba zake wakati mmoja, zikasomwa na jumla ya wasomaji milioni kumi na tano. Mwishowe, zaidi ya magazeti 4,000 ya kilimwengu yalichapwa mahubiri hayo.” Basi, hiyo ilikuwa njia nyingine ya kuenezea kweli za Biblia.
“KAZI YA MPANUKO YA DARASANI”
Utendaji wa ushujaa wa watumishi wa Yehova uliongezeka sehemu nyingine ya kazi yao ilipotokea mwaka wa 1911. Shughuli hiyo ya kutoa hotuba za watu wote mahali pengi ilijulikana kama “kazi ya mpanuko ya darasani.” Wahudumu 48 wenye kusafiri walianza kazi hii mpya kwa kugawiwa sehemu za kwenda kutolea hotuba za watu wote. Lakini si hilo tu lililohusika katika “kazi ya mpanuko darasani.” Majina na nyumba za wenye kupendezwa waliohudhuria hotuba hizo yaliandikwa, nao watu hao walitembelewa nyumbani kwao na Wanafunzi wa Biblia, kujaribu kuwakusanya pamoja wawe makundi mapya.
KUSAFIRI PAMOJA NA WAHAJI
Mwaka wa 1894, wajumbe 21 wenye kusafiri wa Watch Tower Society walitumwa wakafanye mikutano ya watu wote na kujenga makundi ya Wanafunzi wa Biblia kiroho. Walisafiri kwa njia ile ile moja, na makundi yalipoongezeka watu wahaji wengine, kama walivyoitwa wakati huo, walitumwa. Wahaji walitumikia faida za watu wa Mungu kutoka miaka ya 1890 kufikia mwishoni mwishoni mwa miaka ya 1920. Nia yao ilikuwa kama ya Paulo, aliyewaambia Wakristo Warumi hivi: “Ninatamani sana kuwaona, nipate kuwapa karama ya rohoni, ili mfanywe imara; yaani, tufarijiane mimi na ninyi, kila mtu kwa imani ya mwenzake, yenu na yangu.”—Rum. 1:11, 12.
MPANUKO MAJIRA YA MATAIFA YAKARIBIAPO KUKOMA
Miaka kumi ya kwanza ya karne ya 20 ilipokwisha, Wanafunzi wa Biblia walijua kwamba mataifa yalikuwa yanaishiwa na wakati. Kwa Muda mrefu watu wa Mungu walikuwa wametazamia mwaka wa 1914 kama mwisho wa Majira ya Mataifa yenye urefu wa miaka 2,520. (Luka 21:24) Sasa ni miaka michache sana iliyokuwa imebaki yakome, naye C. T. Russell alijitayarisha kuwa na shughuli ya ulimwenguni pote ya kutoa ushuhuda kwa mataifa. Lakini “Bible House” katika Allegheny ilikuwa ndogo sana kwa kazi hiyo kubwa ya mataifa yote.
Kwa hiyo, mwaka wa 1908 wajumbe kadha wa Watch Tower Society, kutia na J. F. Rutherford (ambaye wakati huo alikuwa ndiye wakili wake), walitumwa mji wa New York, Sababu gani? Wakanunue makao yenye kufaa zaidi ambayo Russell mwenyewe alikuwa ameyaona akiwa safarini mapema. Wakaenda, wakainunua “Plymouth Bethel” ya zamani ikiwa katika Hicks Street, Brooklyn, New York. Lilikuwa jengo la kanisa lililomalizwa mwaka wa 1868 liwe la Plymouth Congregational Church lililokuwa karibu, ambako wakati mmoja Henry Ward Beecher ndiye aliyekuwa pasta. Wajumbe hao wa Sosaiti wakanunua nyumba ya Beecher pia yenye orofa nne katika 124 Columbia Heights, iliyokuwa karibu tu.
Yaliyokuwa makao ya zamani ya Beecher sasa yakawa ndiyo makao mapya makuu ya wafanya kazi wa Sosaiti waliokuwa zaidi ya 30, nayo yaliitwa “Betheli,” maana yake “Nyumba ya Mungu.” Jengo la Hicks Street lililojengwa tena kwa mtindo mpya likajulikana kama “The Brooklyn Tabernacle.” Lilikuwa na afisi za Sosaiti na jumba kubwa sana la kukusanyikia. Januari 31, 1909, watu 350 walihudhuria mzinduo (kuwekwa wakf) wa makao mapya makuu ya Sosaiti.
Chumba cha C. T. Russell cha kujifunzia kilikuwa katika Betheli. Chumba cha kulia kilikuwa katika orofa ya chini, kikiwa na meza ndefu iliyokuwa na nafasi ya watu 44. Jamaa ilikuwa ikikusanyika huko kuimba wimbo, kusoma “Vow” (“Nadhiri”) na kusali pamoja kabla ya kiamsha-kinywa. Mwanzoni mwa chakula andiko la Biblia lilisomwa kutoka Daily Heavenly Manna for the Household of Faith, nalo lilizungumzwa wakati wa kiamsha-kinywa.
Kutoka Betheli ulikuwa ukipita karibu majumba matatu ndiyo ufike “Brooklyn Tabernacle,” ambalo lilikuwa jengo la kupendeza la zamani lenye matofali mekundu likiwa na orofa mbili pamoja na nyingine ya chini. Lilikuwa na afisi kuu za Sosaiti, chumba cha kutungia mambo ambamo ndimo chapa za kuchapia The Watch Tower zilimopangiwa, chumba cha kuwekea vifaa na chumba cha vitabu vya kusafirishwa pia. Orofa ya pili ilikuwa na jumba kubwa la kukusanyikia lenye nafasi ya kukaa ya watu 800. Ndugu Russell alihutubu humo kwa kawaida.
Kwa muda fulani wafanya kazi wa Sosaiti wa makao makuu walikuwa na nafasi kubwa ya kukaa katika 124 Columbia Heights. Baadaye, jengo lililokuwa karibu na lao katika 122 Columbia Heights likanunuliwa, makao ya Betheli yakapanuliwa. Mwaka wa 1911 mjengo zaidi wenye kupanua orofa tisa upande wa nyuma katika mtelemko kufika Furman Street ulikwisha. Ulikuwa na nafasi kubwa zaidi ya kukaa na ya vifaa vingine, kutia na chumba kipya cha kulia. 111 kuwa na uenyeji wa kisheria wa mali hizo, mwaka wa 1909 watumishi wa Yehova waliunda shirika People’s Pulpit Association, ambalo sasa linajulikana kama Watchtower Bible and Tract Society of New York, Incorporated. Shirika hilo pamoja na mashirika mengine yaliyoundwa na watu wa Mungu katika nchi mbalimbali yanashirikiana yote pamoja na pamoja na baraza inayoongoza ya mashahidi wa Yehova.