Mileani (Miaka Elfu)—Ni Nini?
Imeonwaje? Je! twaweza kuitazamia katika wakati ujao?
“Wakati ambao tamaa za mwanadamu za amani, uhuru kutokana na uovu, na utawala wa haki juu ya dunia vitatimizwa hatimaye kupitia kwa uwezo wa Mungu.”
HIVYO ndivyo kitabu Encyclopaedia Britannica kinavyoeleza fundisho la Biblia la “kipindi cha miaka 1,000, kinachojulikana kama mileani.”
Je! hukubali kwamba tungependa masimulizi hayo yawe jambo halisi? Bila shaka tungependa kufurahia ‘amani, uhuru kutokana na uovu na haki juu ya dunia.’ Walakini je! taraja hilo ni sehemu ya kusadiki kwako juu ya mileani?
Kwa watu wengi sivyo, kwa kuwa wanafahamu machache sana au hawafahamu hata jambo moja juu ya mileani. Ndivyo ilivyo kwa mamilioni ambao wamehudhuria makanisa, kwa sababu dini nyingi hazitaji jambo hili sana. Ni kama jambo ambalo Mungu alitia ndani ya Biblia lakini lisilokuwa la kuvutia au lenye maana tena.
Hata hivyo, kama tulivyoona, Neno la Mungu hushikamanisha mileani na masimulizi juu yake akiondoa huzuni, machozi na kifo. Kwa hiyo tuna sababu nzuri kutaka kufahamu yale anayosema na kumaanisha Yehova Mungu kwa habari ya mileani. Wakati wetu ujao na ule jamaa yetu waweza kuhusika sana.
Unaweza kufungua Biblia yako katika Ufunuo sura ya 20 ili upate mengi ya yale ambayo Biblia inasema juu ya utawala wa Kristo wa miaka elfu. Mtume Yohana anashiriki nasi aliyopendelewa kuona.
Kwa hiyo, kulingana na Biblia, mileani ni kipindi kile ambacho Shetani hatakuwa huru kudanganya wanadamu, wafu watafufuliwa na kuhukumiwa, na jamii ya wanadamu itatawalwa kwa haki na Yesu Kristo na warithi-washirika wake.
Huenda ukashangaa kwa kufaa, hata hivyo, sababu gani ni mambo machache sana yanayosemwa juu ya hili katika makanisa au katika mambo ya kidini. Ukweli ni kwamba ikiwa ungeuliza, utapata kwamba dini nyingine hushikilia kwamba mileani si kipindi halisi cha miaka 1,000 wakati ambapo Kristo atatawala. Fundisho jingine la kawaida ni kwamba mileani ni mfano tu wa utawala wa Kristo ulioanza karibu miaka 2,000 iliyopita na ingali inaendelea. Wewe utaamini nini? Twaweza kusaidiwa sana kufahamu jambo hili la maana kwa kuyafikiria yale ambayo mtume Yohana na mitume wenzake waliamini na vilevile yaliyotokea baada ya mitume wa waaminifu wa Yesu kufa kufikia mwisho wa kame ya kwanza.
KWELI ZA UFALME ZAPOTOSHWA
Wakati sisi leo tunaposoma Biblia, ni rahisi kuthamini kwamba ufalme wa kimbinguni wa Mungu ulikuwa mojawapo la mambo makuu ambayo Yesu alifundisha wanafunzi wake. Kwa kweli, alianza kwa ujumbe huu: “Tubuni; kwa maana ufalme wa mbinguni umekaribia.” (Mt. 4:17; Yohana 18:36) Yeye aliwaambia mitume wake kwamba angepaswa kufa walakini angefufuliwa na kwamba angewatayarishia mahali mbinguni. (Mt. 16:21; Luka 22:28-30; Yohana 14:2, 3) Hapo kwanza, mitume hao hawakufahamu alivyosema, kwa kuwa walidhani kwamba Ufalme huo ungesimamishwa duniani. (Yohana 20:9; Matendo 1:6, 7) Walakini baada ya kupokea roho takatifu, walitambua kwamba Ufalme huo ungekuwa mbinguni. Hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa maana sisi, wenyeji wetu uko mbinguni.” Ili kupata uzima wa kimbinguni, ingewapasa kufa na kufufuliwa kama viumbe vya kiroho, kwa kuwa “nyama na damu haziwezi kuurithi ufalme wa Mungu.”—Flp. 3:20; 1 Kor. 15:50.
Walakini, kweli hizi za Kibiblia zilizo wazi zilifunikwa baada ya mitume wa Yesu kufa. Jambo hilo lilitokeaje? Paulo alisema hivi: “Baada ya kuondoka kwangu . . . watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:29, 30) Ndiyo, wakati wa karne ya kwanza mitume walitoa uvutano wenye kuzuia ambao ulisaidia kuweka fundisho la Kikristo likiwa safi. Walakini baada ya hao wote kufa ukengeufu uliingia. (2 The. 2:3-8; 1 Tim. 4:1-4) Jambo hilo lilikuwa na uvutano fulani juu ya yaliyofundishwa juu ya mileani. Sisi hatumo gizani juu ya hili, kwa kuwa maandishi yaliyopo ya karne ya pili na ya tatu yanatusaidia kufahamu yaliyotokea.
MAONI YA MADHEHEBU (KIDINI) JUU YA MILEANI
Katika karne iliyofuata kifo cha mtume Yohana, maoni yalitokea kwamba wakati wa mileani Kristo angetawala duniani, pengine kutoka Yerusalemu uliojengwa upya. Mwana-historia J. Mosheim anadokeza kwamba wazo hili yawezekana lilitokana na kuunganishwa kwa tumaini la Kikristo la “ufalme wa Mwokozi wetu wa mbinguni” na tumaini la Kiyahudi lililokuwako la “ufalme wa kidunia wa Masihi.” Madhehebu ya Wamontano (wafuasi wa Montano) ilijitokeza katika Asia Ndogo, ikifundisha kwamba Yesu angetawala huko kutoka Frigia. Wao, na wengine, walifundisha kwamba mambo mengi mazuri ajabu yengetukia wakati wa kutawala kwa Kristo na warithi-washirika duniani wakati wa mileani. Kwa mfano, iliaminiwa kwamba watawala hao wangefurahia anasa za mwili za namna zote, kutia ndani zile zilizo kati ya watu wa kiume na wa kike. Na wao wangekuwa na miili ya nyama ‘iliyo bora zaidi ya yetu na yenye kufanana na ya mbinguni.’ Maoni hayo yasiyosawazika yakaja kuonwa kuwa mfano wa wale wenye kuiamini mileani. Kama matokeo, ‘fundisho lote la mileani likapoteza sifa yalo,’ anaripoti Dakt. A. Neander.
Maoni ya pili yalitokea ambayo yaliongeza mvurugo. Kulingana nayo, “miaka elfu” ilikuwa ya mfano tu. Inawezekana kuwa mwalimu mwenye uvutano zaidi katika jambo hili alikuwa mwanafunzi wa dini wa Kikatoliki Agostino. Kitabu Encyclopaedia Britannica kinatuambia hivi:
‘Baada ya kuongolewa kwake kwenye Ukristo, Agostino, aliyekuwa mponda maisha hapo kwanza, kwa kushindilia alipendelea namna ya maisha ya kujinyima ulimwengu na kujinyima raha kupita kiasi. Kwa kweli, hali yake yakutopendezwa tena na mambo ya ulimwengu yenye thamani ilikuwa kamili kuliko ile ya wamileani, kwa kuwa alikataa matazamio yo yote ya ulimwengu uliofanywa upya na kusafishwa ambao waamini wangetazamia kufurahia na kuyaona kuwa anasa za mwili.
Kitabu New Catholic Encyclopedia kinaripoti kwamba Agostino ‘aliendeleza wazo la kwamba kwa kweli mileani ilikuwa imeanza tangu kuzaliwa kwa Kristo.’ Uhakika wa kwamba huenda usiwe umesikia mengi juu ya mileani yaelekea unahusiana na jambo hili, kwa kuwa Kanisa la Katoliki sasa hushikilia kwamba “utawala wa miaka 1,000 wa Yesu [ni] mfano wa muda wote wa maisha ya Kanisa . . . Kufungwa minyororo kwa Shetani wakati wa kipindi iki hiki kwaonyesha kwamba uvutano wa Shetani umepunguzwa sana.”
Maoni haya ya madhehebu yenye kupingana yamepunguza kupendezwa katika mileani. Walakini kwa kuwa wakati wetu ujao unahusika, ebu na tuchunguze maoni haya mawili juu ya mileani na kuamua yale tunayopaswa kuamini juu ya msingi wa Neno la Mungu Biblia.
WAPI NA WAKATI GANI?
Makanisa mengi hufundisha kwamba Kristo atarudi katika mwili, hata kama vile katika karne ya pili wazo lilitokea kwamba Yesu na wafalme-makuhani wake washirika wangetawala katika mwili duniani wakati wa mileani. Walakini, Yesu mwenyewe alisema hivi: “Bado kitambo kidogo na ulimwengu haunioni tena; bali ninyi [wale aliokuwa akienda kutayarishia mahali mbinguni mtaniona]. Na kwa sababu mimi ni hai, ninyi nanyi mtakuwa hai.” (Yohana 14:2, 3, 18, 19) Hivyo, Yesu alionyesha kwamba yeye angetawala mbinguni. Je! twapaswa kufahamu hivyo tusomapo Ufunuo sura ya 20? Ndiyo, kwa kuwa Biblia haijipingi.
Kikitoa sababu za kupinga fundisho la utawala wa mileani katika mwili duniani, kitabu cha Hastings’ Encyclopoedia of Religion and Ethics kinaeleza hivi:
“Katika masimulizi haya [Ufunuo 20] sehemu mpya ni utawala wa miaka 1,000 wa wafia imani pamoja na Kristo, . . . Utawala huu hausemekani kuwa ukiwa duniani, wala ufufuo wa kwanza hausemekani kuwa wa kimwili . .. Iwapo wafia imani wanaorudishwa kwenye uzima ndio watakatifu wanaokaa katika Yerusalemu ambao wanashambuliwa na Gogu wa Magogu, ni jambo la kushangaza kwamba Kristo (ambaye wanatawala pamoja naye) hawashambulii adui hao. Uharibifu wao unatoka mbinguni.”—Kit. cha Tano, uku. 387.
Jambo hilo linapatana na yale ambayo tumekwisha kuona tayari katika Biblia juu ya Yesu na warithi washirika wake wakitawala katika ufalme wa kimbinguni, ama sivyo? Biblia haisemi kwamba hao “wenye kuushiriki mwito wa mbinguni” wakati wo wote, hata kwa miaka l,000, watapata miili ya kibinadamu. (Ebr. 3:1) Mahali pake, inaonyesha wazi kwamba Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho ‘watafufuliwa mwili wa roho,’ kama vile Yesu Kristo, ili wapate kuingia mbinguni kwenyewe.—1 Kor. 15:42-49; Ebr. 9:24
Kwa kuwa wale wanaourithi Ufalme huo wanaenda mbinguni, mawazo yote ya madhehebu juu ya Yesu na “watakatifu” wakitawala katika mwili kutoka Yerusalemu au Frigia wa kidunia na kujiingiza katika anasa za mwili hayana msingi.
Maoni hayo yanaonekana yakipotoa mafundisho mawili ambayo yanatolewa na Biblia: (1) Ufalme huo ni serikali ya kimbinguni ambayo washiriki wake Yesu, mitume na wengine wenye kufufuliwa kwenda mbinguni katika “ufufuo wa kwanza.” (Ufu. 20:6) (2) Chini ya serikali hiyo ya kimbinguni dunia, ikiwa imeondolewa waovu, itarudishwa kwenye hali zenye amani za paradiso ifurahiwe na watumishi wa Mungu wa kibinadamu.—Luka 23:43, NW; Ufu. 19:11–20:3; 22:1, 2, 17.
Unaweza kuona kwamba la pili la matukio hayo lingali halijatokea. Jambo hilo laonyesha kwamba mileani ingali ni ya wakati ujao, ama sivyo?
Kama tulivyoonyesha, wengine husema kwamba mileani si kipindi halisi cha miaka 1,000, ila ni kipindi kirefu, kisichojulikana ambacho pengine kilianza karne nyingi zilizopita. Je! jambo hilo laweza kuwa sahihi? Ni kweli kwamba hesabu fulani au vipindi vya wakati katika kitabu cha Ufunuo ni vya mfano, kwa kuwa ujumbe wa kitabu hicho ulitolewa katika ‘ishara’ nyingi. (Ufu. 1:1, 4; 2:10) Walakini, je! kunayo sababu kuamini kwamba hiyo “miaka elfu” si ya mfano?
Katika Ufunuo sura ya saba mtume huyo anatofautisha kati ya hesabu iliyowekwa ya wale wanaotawala na Kristo (144,000) na hesabu kubwa zaidi isiyo na hesabu inayookoka “dhiki kubwa.” Yohana anatofautishaje? Anakitaja kikundi hicho cha pili kama “mkutano mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu.” (Ufu. 7:4, 9) Baadaye, anaitaja ile hesabu iliyo kamili, “wale mia na arobaini na nne elfu.” (Ufu. 14:3) Vivyo hivyo, katika Ufunuo 20:8, Yohana anasema kwamba hesabu kubwa isiyo na kipimo ya watu wanaoasi mwishoni mwa mileani ni “kama mchanga wa bahari.” Wala mtume Yohana, katika Ufunuo sura ya 20, hatumii “maelfu” kwa wingi, ambayo nyakati nyingine inatumiwa mahali kwingineko kuonyesha hesabu kubwa na pengine isiyo na kipimo. (Ufu. 5:11; Dan. 7:10; 1 Sam. 18:7; Zab. 68:17; 119:72) Kwa hiyo inaonekana hakuna sababu nzuri kukata shauri kwamba usemi “miaka elfu” wa sura ya 20 unamaanisha kipindi kirefu walakini kisicho na mwisho. Mahali pake, Yohana anatumia Usemi huo katika njia inayoonyesha kipindi cha urefu uliowekwa—“hiyo miaka elfu.”—Ufu. 20:6.
Ingawa hivyo, je! twaweza kuwa na hakika juu ya urefu wa kipindi hicho kilichowekwa? Akiwa na maoni kuwa Ufunuo ulikuwa ukishughulika na Wayahudi karibu na mwisho wa karne ya kwanza, J. J. Wettstein alidai kwamba mileani ilikuwa miaka 50 tangu kifo cha Mfalme Domitian (96 W.K.) mpaka vita ya Kiyahudi wakati wa utawala wa Hadrian. Wazo jingine lilikuwa kwamba siku moja ilisimamia mwaka. Kulingana na maoni haya, kukiwa na siku 360 katika mwaka, mileani ingekuwa na urefu wa miaka 360,000 (360 x 1,000). Kwa habari ya mafasiri hayo, Mwalimu wa chuo kikuu A. T. Robertson aliandika hivi: “Namna zote za mawazo zinatolewa, bila ya yo yote kuweza kumtosheleza mtu.”
Njia iliyo moja kwa moja ni kuyakubali maneno ya Yohana kuwa vile yalivyo hasa—miaka 1,000. Wengi wameona katika hili utawala unaofaa wa Yesu Kristo, ambaye Biblia humwita “Bwana wa sabato.” (Mt. 12:8) Itakuwa kama siku ya mapumziko ya sabato baada ya miaka 6,000 ambayo katika hiyo kutokamilika kwa kibinadamu kumetawala tamasha ya kidunia.—2 Pet. 3:8.
Yohana mwenyewe anaonyesha kwamba mileani inafuata vita ya Kristo yenye ushindi juu ya adui zake zote za kidunia. (Ufu. 19:11-21) Kwa kuwa jambo hilo halijatokea bado, twaweza kuwa na hakika kwamba mileani bado ni ya wakati ujao. Kutimizwa kwa unabii wa Biblia katika wakati wetu kunatoa ushuhuda kwamba karibuni Kristo atafanya vita na kuharibu adui za Mungu za kidunia, kama vile inavyosimuliwa na maneno ya unabii wa Yesu mwenyewe.—Mt. 24:3-22.
Ushuhuda wote wa Kibiblia na wa kihistoria unaoonyesha kwamba sisi twaishi katika siku za mwisho wa taratibu hii mbovu ya mambo watupa msingi imara wa kutazamia mileani ya amani ianze katika wakati ujao ulio karibu.—2 Tim. 3:1-5.