Habari za Ufalme Na. 36
Milenia Mpya—Unaweza Kutarajia Nini Wakati Ujao?
MIlenia Mpya—Je, Ni Mwanzo wa Enzi Mpya?
KARNE ya 20 ilikwisha Desemba 31, 1999, saa sita usiku.a Karne hiyo ilijaa misukosuko mingi. Ingawa pia katika karne hiyo kulitokea tekinolojia nyingi mpya, maendeleo makubwa ya matibabu, maendeleo makubwa ya mawasiliano, na uchumi uliositawi haraka ulimwenguni kote. Basi wengi wameipokea milenia mpya kuwa ishara ya matumaini na mabadiliko. Je, labda vita, umaskini, uchafuzi wa mazingira, na ugonjwa zitakoma katika kipindi hiki?
Wengi hutumaini hivyo. Lakini je, kweli milenia mpya yaweza kuleta mabadiliko yatakayokupa faida—mabadiliko yatakayofanya maisha kuwa salama kwako na kwa familia yako? Hebu chunguza namna mbalimbali za matatizo machache tu kati ya matatizo mengi yanayotukabili.
Uchafuzi
Nchi zilizoendelea kiviwanda “zinasababisha kuharibika kwa mazingira na uchafuzi uliosambaa sana na kuharibika kwa mfumo wa kutegemeza viumbe katika mazingira yake ulimwenguni kote.” Hali za sasa zikiendelea, “mazingira ya asili yatazidi kuharibika.”—“Global Environment Outlook—2000,” Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa.
Ugonjwa
“Kufikia mwaka wa 2020, yatarajiwa kuwa magonjwa yasiyoambukizwa yatasababisha vifo saba kati ya vifo kumi vya watu katika nchi zinazoendelea, ikilinganishwa na vifo vinavyopungua vitano leo.”—“The Global Burden of Disease,” Harvard University Press, 1996.
Wataalamu fulani husema kwamba “kufikia mwaka wa 2010, watu milioni 66 watakuwa wamekufa katika nchi 23 ambako kuna mlipuko mbaya sana wa [UKIMWI].”—“Kupambana na UKIMWI: Ushuhuda Kutoka Katika Nchi Zinazoendelea,” ripoti ya Jumuiya ya Ulaya na Benki ya Dunia.
Umaskini
“Karibu watu bilioni 1.3 huishi kwa kutumia pesa zinazopungua dola moja kila siku, na karibu bilioni moja hawapati chakula cha kutosha.”—“Human Development Report 1999,” Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa.
Vita
“Huenda jeuri ndani ya [nchi mbalimbali] ikafikia viwango vikubwa zaidi. Jeuri hiyo, ambayo huletwa na [tofauti] za kikabila na kidini . . . itakuwa ndiyo msingi wa . . . mapigano mengi zaidi katika miaka ishirini na mitano ijayo . . . , nayo itaua mamia ya maelfu ya watu kila mwaka.”—“New World Coming: American Security in the 21st Century,” Tume ya Marekani ya Usalama wa Kitaifa/Karne ya 21.
Basi, furaha na misisimko kutokana na milenia mpya huficha uhakika wa kwamba sasa kuna uwezekano mkubwa zaidi wa uchafuzi, ugonjwa, umaskini, na vita kuliko wakati mwingine wowote. Kinachosababisha matatizo hayo ni pupa, kutoaminiana, na ubinafsi—tabia ambazo utafiti wa kisayansi, tekinolojia, au siasa peke yake haziwezi kuondoa.
Milenia Itakayowaletea Wanadamu Baraka
MWANDIKAJI mmoja wa kale alisema hivi: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Mwanadamu hana uwezo na haki ya kuitawala dunia. Muumba wetu, Yehova Mungu, ndiye pekee aliye na haki na ujuzi wa kuyatatua matatizo ya wanadamu.—Waroma 11:33-36; Ufunuo 4:11.
Lakini hayo yatakuwa lini? Jinsi gani? Kuna uthibitisho mwingi sana unaoonyesha kwamba tunakaribia kikomo cha “siku za mwisho.” Tafadhali fungua Biblia yako, na usome 2 Timotheo 3:1-5. Maandiko hayo huelezea waziwazi tabia ambazo watu wangekuwa nazo katika “nyakati [hizi] za hatari.” Pia Mathayo 24:3-14 na Luka 21:10, 11 huelezea “siku za mwisho.” Sura hizo zakazia mambo yanayoonekana ambayo yametendeka tangu mwaka wa 1914, kama vile vita vya ulimwenguni kote, magonjwa, na upungufu mwingi wa chakula.
“Siku za mwisho” zitakoma karibuni. Andiko la Danieli 2:44 lasema: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, . . . bali utavunja falme hizi [za duniani] zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Basi ilitabiriwa kwamba Mungu angeusimamisha Ufalme, au serikali, ya kuitawala dunia. Andiko la Ufunuo 20:4 lasema kuwa serikali hiyo itatawala kwa kipindi cha miaka elfu—milenia! Hebu ona baadhi tu ya njia ambazo hali za maisha zitakuwa bora kwa wanadamu wote wakati wa Milenia hiyo yenye utukufu:
Uchumi. “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.”—Isaya 65:21, 22.
Afya. “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.” “Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”— Isaya 33:24; 35:5, 6.
Mazingira. Mungu ‘atawaleta kwenye uangamizi wale wanaoiangamiza dunia.’—Ufunuo 11:18.
Mahusiano ya Wanadamu. “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA.”—Isaya 11:9.
Mamilioni ya watu wanaamini ahadi hizo za Biblia, nao wamepata maoni mazuri yenye kutarajia mema wakati ujao. Kwa hiyo, wako katika hali bora ya kukabiliana na mibano na matatizo maishani. Biblia yawezaje kuwa kiongozi maishani mwako?
Ujuzi Unaoongoza Kwenye Uhai!
LO, HUENDA sayansi na tekinolojia zikavutia nyakati fulani! Ijapokuwa hivyo, ujuzi wa mwanadamu haujafanya maisha yawe salama na yenye furaha kwa watu walio wengi. Ujuzi pekee uwezao kutimiza hayo umeelezwa katika Biblia kwenye Yohana 17:3, linalosema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’
Ujuzi huo umo katika Biblia. Ingawa wengi wana maoni mbalimbali kuhusu kitabu hiki kitakatifu, ni wachache tu ambao wamewahi kukichunguza wenyewe. Namna gani wewe? Hapana shaka kwamba kuisoma Biblia hutaka jitihada kiasi fulani. Lakini kuna faida. Biblia ndicho kitabu pekee ambacho ‘kimepuliziwa na Mungu na ni chenye manufaa kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.’—2 Timotheo 3:16.
Basi waweza kuanzaje kuifahamu Biblia? Mbona usiwaruhusu Mashahidi wa Yehova wakusaidie? Wao huwafundisha mamilioni ya watu nyumbani kwao, bila malipo. Nao hutumia vichapo vinavyotegemea Biblia, kama vile broshua iitwayo Mungu Anataka Tufanye Nini? ili wakusaidie kujifunza. Ina majibu mafupi kwa maswali mengi ambayo huenda ukawa nayo kuhusu Biblia, kama vile: Mungu ni nani? Ni nini kusudi la Mungu kwa dunia? Ufalme wa Mungu ni nini? Biblia yaweza kuboreshaje maisha ya familia yako?
Iwapo ungependa mmoja wa Mashahidi wa Yehova akutembelee kwako, tafadhali jaza hati iliyo hapa chini. Watafurahi kukupa habari zaidi kuhusu Utawala mtukufu wa Milenia wa Ufalme wa Mungu!
□ Naomba broshua iitwayo Mungu Anataka Tufanye Nini? Onyesha lugha unayotaka
□ Tafadhali wasilianeni nami kuhusu funzo la Biblia nyumbani bila malipo
[Maelezo ya Chini]
a Hapa twarejezea maoni ya watu wengi katika nchi za Magharibi kuhusu milenia mpya. Kihalisi, milenia hii mpya itaanza Januari 1, 2001.