Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 9/15 kur. 16-21
  • Lile Tumaini la Miliani Lashinda

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Lile Tumaini la Miliani Lashinda
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UZIMA WA WAKATI UJAO KWA UFUFUO
  • TUMAINI LA KIMBINGUNI NA LA KIDUNIA
  • TUMAINI LA MILEANI KWA VIKUNDI VIWILI
  • TUMAINI LA MILEANI LINGALI HAI!
  • SI “NDOTO YA KUTAKA VITU VYA KIMWILI”
  • PARADISO—YA KIROHO NA YA KIMWILI
  • TUMAINI LINALOWEZA KUWA LAKO
  • Wakristo na Tumaini la Mileani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Mileani (Miaka Elfu)—Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kumfurahia “Mungu wa Tumaini”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Ufufuo wa Uzima na Mwingine wa Hukumu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1979
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 9/15 kur. 16-21

Lile Tumaini la Miliani Lashinda

1. Ni maulizo gani yaliyotokezwa na kuja kwa Masihi?

WAKATI Masihi aliyengojwa kwa muda mrefu alipowajia Wayahudi, je! yeye aliithibitisha imani yao ya asili juu ya uzima wa wakati ujao kwa ufufuo, au alilipendelea wazo lao la kipagani walilokuwa wameanza karibuni la kwamba watu wanazaliwa wakiwa wamerithi nafsi isiyoweza kufa? Alipotokeza wazi tumaini la kimbinguni, je! Yesu Kristo alimaanisha kwamba wote wale wanaookolewa wangekwenda mbinguni? Au Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki ya Kikristo pia yanatolea mamilioni ya watu tumaini la uzima wa milele juu ya dunia?

UZIMA WA WAKATI UJAO KWA UFUFUO

2. Yesu alifundisha nini juu ya tumaini la uzima wa wakati ujao?

2 Tofauti sana na kufundisha wazo la kipagani la kwamba watu wanazaliwa wakiwa wamerithi nafsi ya kibinadamu isiyoweza kufa, Yesu alionyesha kwamba tumaini lo lote la uzima wa wakati ujao linategemea ufufuo. Alisema: “Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake. Naye akampa amri ya kufanya hukumu kwa sababu ni Mwana wa Adamu. Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka; wale waliofanya mema kwa ufufuo wa uzima, na wale waliotenda mabaya kwa ufufuo wa hukumu.”​—Yohana 5:26-29.

3. Wengine wa wanachuo wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo sasa wanakubali nini juu ya nafsi?

3 Jambo la kupendeza ni kwamba wanachuo wengine wa kidini wa kisasa wa Jumuiya ya Wakristo wameanza kufuata wazo la kwamba wala Maandiko ya Kiebrania wala ya Kigiriki ya Kikristo hayaungi mkono kwamba watu wanazaliwa wakiwa wamerithi hali ya kutokuweza kufa. Kwa mfano, kamusi The New International Dictionary of New Testament Theology (Vol. 3, 1978) inatilia mkazo “jinsi lile AK [Agano la Kale] lisivyozoeana na wazo la nafsi yenye kuwa mbali na mwili, au nafsi ambayo inakuwa mbali na mwili wakati wa kufa.” Tena: “Mt. 10:28 inafundisha si uwezekano wa kutokufa kwa nafsi bali kutokuweza kubadilishwa kwa hukumu ya kimungu ya wasiotubu. . . . Lile AJ [Agano Jipya] linamchukua mwanadamu kabisa kama kitu kimoja kilichoungana na kuahidi kugeuzwa kwa mtu mzima, wala si kuokoka kwa sehemu moja tu. . . . hakuwezi kuwako hali ya kutokuweza kufa bila ya mtu kufufuliwa kwanza.”

TUMAINI LA KIMBINGUNI NA LA KIDUNIA

4. Mashahidi wa Yehova wanakubali nini, lakini wanakataa nini, na kwa sababu gani?

4 Mashahidi wa Yehova hawakatai kwamba Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanafundisha kwamba Wakristo wengine wanaupokea “mwito wa mbinguni.” (Ebr. 3:1) Wanalokataa ni kwamba huo “mwito wa mbinguni” unaondolea mbali kusudi la asili la Mungu kuifanya dunia ilimwe iwe paradiso na kujazwa na mbari yenye haki ya wanaume na wanawake. Hawawezi kulikubali wazo la kwamba unabii wote ulio katika Maandiko ya Kiebrania wenye kutabiri kurudishwa kwa paradiso duniani umekuwa maandishi yaliyokufa. Wao wanazidi kusadikishwa juu ya jambo hilo kwa sababu ahadi ya “dunia mpya” ambamo “haki itakaa” inathibitishwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.​—2 Pet. 3:13, NW; Ufu. 21:1-4.

5, 6. Biblia inaelezaje wazi tumaini lenye msingi wa Maandiko lenye sehemu mbili: (a) la kimbinguni? (b) la kidunia?

5 Kujifunza Biblia kwa uzito kumeongoza Mashahidi wa Yehova waamini kwamba tumaini la Kikristo lenye msingi wa Maandiko lina sehemu mbili: Zawadi ya kutokuweza kufa mbinguni kwa watu wachache wenye kikomo, na uzima wa milele duniani kwa walio wengi zaidi. Tumaini la kimbinguni la ‘kutawala kama wafalme’ pamoja na Kristo linatolewa kama “neema” ya pekee isiyo ya kawaida (UV) au “fadhili zisizostahilika” kwa wale 144,000 “wateule” (UV) au “waliochaguliwa,” kuanza na mitume na wanafunzi wa kwanza wa Kristo. (Luka 12:32; Rum. 5:17, NW; 8:33; Ufu. 5:9, 10; 7:1-4; 14:1-4) Kati ya hawa, kwa sasa walio hai duniani ni ‘waliobaki’ wachache tu wa wale ambao ‘wameendelea kuwa hai mpaka kuwapo kwa Bwana.’​—1 The. 4:14-17, NW; Ufu. 12:17.

6 Tumaini la kidunia ndilo tumaini la asili ambalo Adamu na Hawa wangaliweza kulifikia, kama wangalibaki chini ya enzi kuu ya Yehova Mungu wasijitafutie uhuru wa kujiamulia mema na mabaya. (Angalia sura tatu za kwanza za Mwanzo.) Mwanadamu “ni wa kidunia kwa maumbile.” (1 Kor. 15:47, The Jerusalem Bible) Hamu zake na kwiu zake za asili ni za kidunia. “Mbingu ni mbingu za [Yehova], bali nchi amewapa wanadamu.” (Zab. 115:16) Nayo Biblia inasema waziwazi kwamba Yehova ‘hakuiumba dunia bure, bali aliifanya ikaliwe na watu.’ (Isa. 45:18) Kwa hiyo tumaini la uzima wa milele katika hali za kiparadiso ni jambo la asili na la ki-Maandiko pia. Si jambo la kuaibikia.

TUMAINI LA MILEANI KWA VIKUNDI VIWILI

7. Ahadi ya ki-Abrahamu na unabii wa Danieli zinatolea makundi ya watu duniani tumaini gani?

7 Kwa kuwa wale Waisraeli wa kiroho 144,000 ndio “uzao” au “wazao wa kweli wa Abrahamu” na “warithi wa kweli wa ahadi yake ‘ (Gal. 3:26-29, tafsiri ya Phillips), ni vizuri kukumbuka kwamba ahadi aliyopewa Abrahamu ilisema hivi pia: “Kwa njia ya uzao wako mataifa yote ya dunia kwa uhakika yatajibarikia yenyewe.” (Mwanzo 22:16-18, NW) Nabii Danieli alitaja pia “watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote” ambao “mwana wa Adamu,” Yesu Kristo, atatumia “ufalme, na mamlaka” juu yao akiwa katika “mbingu.” Anafanya jambo hilo akiwa pamoja na wale “wateule,” wanaoitwa ‘watu watakatifu wake Aliye juu.” —Dan. 7:13, 14, 27; 2 Tim. 2:10.

8. Ni nini linaloonyesha kwamba Paulo na Yohana walijua kwamba wokovu si wa “waliochaguliwa” peke yao?

8 Wakristo wa kwanza walifahamiana na unabii huo unaozungumza juu ya vikundi hivyo viwili: “uzao” na “mataifa,” “watakatifu” na ‘watu wa taifa zote.’ Akithibitisha jambo hilo, baada ya kuzungumza juu ya wale watakaokuwa ‘warithi pamoja na Kristo’ na ambao ‘watatukuzwa pamoja naye’ mbinguni, mtume Paulo anazungumza juu ya “viumbe” wa kibinadamu ambao ‘tazamio lao la shauku nyingi’ ni ‘kuwekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu,’ au dhambi, na kuwa na “uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu.” (Rum. 8:15-21) Akiandikia Wakristo ambao, kama yeye, walishiriki tumaini la kimbinguni, mtume Yohana alisema juu ya Kristo kuwa “kipatanisho kwa dhambi zetu [zile za “wateule”]; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.”​—1 Yohana 2:2; 3:1-3.

9. (a) Labda Yohana alikuwa ameona njozi gani mbali-mbali alipoiandika barua yake ya kwanza? (b) Njozi hizo zinathibitishaje kuwako kwa vikundi viwili vya wenye kuokolewa?

9 Yohana alipoandika maneno hayo, inaelekea sana alikuwa amekwisha pata Ufunuo ambao, baada ya kuona Waisraeli wa kiroho 144,000 waliotiwa “muhuri,” aliona “mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” Hao wanaiokoka ile “dhiki kubwa” nao wanaongozwa na “Mwana-Kondoo,” Kristo Yesu, “kwenye chemchemi za maji yenye uhai.” (Ufu. 7:4-17) Na, bila shaka, ni katika Ufunuo uo huo Yohana aliona pia njozi ya utawala wa mileani wa Kristo, ambao kwa mara nyingine unataja vikundi viwili: ‘walio na sehemu katika ufufuo wa kwanza,’ ambao “watatawala [wakiwa wafalme, NW],” na “watu,” watakaobarikiwa na Mungu na ambao “watakuwa watu wake.”​—Ufu. 20:1–21:8.

10. Leo, ni vikundi gani viwili vinavyolishiriki tumaini la mileani, nazo hesabu za vikundi hivyo zinatofautianaje?

10 Leo, tumaini la mileani linashinda katika mioyo ya wale walio wa “kundi dogo” walioitwa ‘waketi kwenye viti vya enzi’ pamoja na Kristo mbinguni ili watawale kwa mileani moja (miaka elfu moja). (Luka 12:32; 22:28-30) Tumaini hilo la mileani linashirikiwa pia na wale wa “mkutano mkubwa” ambao wamejiunga na mabaki Wakristo waliotiwa mafuta kutangaza “habari njema hizi za ufalme . . . kwa ushuhuda kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Vikundi hivyo viwili viliwakilishwa kwenye sherehe ya Chakula cha Bwana cha Jioni iliyofanywa Machi 31, 1980. Wale wenye kushiriki mifano ya mkate na divai walikuwa 9,564 tu ulimwenguni pote, na kweli hao ni wachache tu “waliobaki” wa wale 144,000 watakaotawala pamoja na Yesu katika ufalme wake wa mileani. Lakini pamoja na hao, wengine 5,717,092 walihudhuria kama watazamaji, kwa njia hiyo wakionyesha kuthamini mpango mzuri sana wa Yehova uliowezeshwa kupitia dhabihu ya Mwanawe. Hawa wanalifurahia taraja la uzima wa milele juu ya dunia ya paradiso.

TUMAINI LA MILEANI LINGALI HAI!

11. Ni wakati gani na jinsi gani tumaini la mileani litatimizwa?

11 Naam, tumaini la mileani lingali hai sana leo. Litatimia baada ya “dhiki kubwa,” wakati Kristo na wale 144,000 “waliochaguliwa” waanzapo utawala wao katika mbingu kwa miaka 1,000, na “mkutano mkubwa” wa watu wenye mfano wa kondoo, pamoja na mabilioni ya watakaofufuliwa duniani, waingiapo ndani ya baraka kubwa za ajabu katika makao ya kidunia ya ufalme huo wa Kimasihi.​—Mt. 25:34; Ufu. 20:12, 13.

12. Mileani imeelezwa kuwa nini katika encyclopedia moja?

12 Leo wanadamu wanahitaji sana sana tumaini kama hilo. Watu wenye hekima ya kilimwengu hawalifahamu sana tumaini hilo. Hivyo, “Macropaedia” iitwayo Britannica (kitabu kikubwa chenye maarifa ya namna nyingi) ya mwaka wa 1977, inaieleza mileani kama ifuatavyo: “Kipindi hiki. cha miaka 1,000, kinachojulikana kama mileani, kinaonwa kuwa wakati ambao kwiu za mwanadamu kwa amani, uhuru wa kutokuwa na uovu, na utawala wa haki juu ya dunia zitatimizwa mwishowe kupitia uwezo wa Mungu. . . . umileani unahusiana na mataraja ya kidunia ya jamii ya kibinadamu. . . . umileani unajaribu kutumia mifano ya waziwazi kujibu maulizo kama: Ni nini utakaokuwa mwisho kamili wa ulimwengu huu? Je! wakati wo wote wanadamu wataitimiza ile ndoto ya vizazi vingi ya kukaa katika paradiso ya kidunia au wanadamu wote wataharibiwa katika maangamizi ya ghafula ya moto utakaotokezwa na upumbavu wao wenyewe au na hukumu ya Mungu?”​—Sisi ndio tumelaza maneno.

13. (a) Je! wewe unaamini dunia itaharibiwa katika maangamizi ya ghafula ya moto”? Sababu ya jibu lako ni nini? (b) Kusudi la asili la Mungu kwa dunia ulikuwa nini?

13 Kwa waandikaji fulani wa encyclopedia na viongozi wa kidini wasio na imani, huenda maulizo hayo yakawapendeza kwa ajili ya kuyatumia katika masomo yao. Lakini kwa watu wengi wenye mioyo minyofu katika nchi zote hayo ni matatizo ya kisasa yanayowasumbua sana hata watake sana kujua majibu. Mashahidi wa Yehova wamepata jibu la maulizo haya katika Biblia. Kwao, tumaini la kuishi milele “katika paradiso ya kidunia” si “ndoto ya vizazi vingi.” Tumaini hilo lina misingi imara, kwa kuwa linategemea uanachuo timamu wa Biblia. Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki pia yanaonyesha kwamba Mungu hataruhusu waovu waiharibu dunia “katika maangamizi ya ghafula ya moto.” (Ufu. 11:18; Isa. 45:18) Wala yeye mwenyewe hataiharibu dunia. (Zab. 104:5) Baada ya kuumba mwanadamu na kumweka katika paradiso ya mahali pamoja, Mungu alimfunulia kusudi Lake, yaani, mwanadamu ‘aitiishe’ dunia kwa kupanua hali za paradiso ulimwenguni pote, na ‘kuijaza dunia [si kuijaza kupita kiasi]’ na mbari ya wanaume na wanawake ‘waliofanywa kwa sura ya Mungu.’​—Mwa. 1:26-28; 2:15.

14. Tumaini la mileani linaingiaje vizuri katika “kusudi milele” la Mungu?

14 Hayo bado ndiyo “mapenzi” ya Mungu ambayo yatafanywa “duniani kama huko mbinguni,” kupitia ufalme wake wa Kimasihi. (Mt. 6:10) Kawaida yote ya Biblia inaonyesha bila shaka lo lote kwamba Mungu hajaliacha kusudi hili la asili. (Isa. 46:9, 10) Mileani, au utawala wa Kristo wa miaka 1,000, inaingia vizuri katika “kusudi la milele” la Mungu, ambalo sehemu yake moja ni “kukusanya vitu vyote pamoja tena katika yule Kristo, vitu vilivyo katika mbingu na vitu vilivyo juu ya dunia.” (Efe. 3:11; 1:8-10) Ndiyo kusema, mileani yenyewe haitakuwa ndiyo mwisho; hiyo ni njia ya kufikia lengo fulani, kutimizwa kwa kusudi la asili la Mungu kwa dunia.

SI “NDOTO YA KUTAKA VITU VYA KIMWILI”

15, 16. Padre mmoja Mkatoliki amelieleza tumaini la mileani kwa njia gani, lakini inaonekana amesahau nini?

15 Wapinzani wa kidini wanawadhihaki Mashahidi wa Yehova kwa kulihubiri tumaini la mileani. Na hata hivyo wadhihaki hao wanafurahia kabisa kusema watu wote wazuri watakwenda mbinguni na waovu wote kwenye mateso ya milele katika moto, na kwa njia hiyo kuiacha dunia kabisa isiwe na “kusudi la milele” la Mungu. Kwa mfano, padre Mfaransa wa Dominica, H. C. Chery, ambaye amekuwa na mazoea ya kulaumu-laumu Mashahidi wa Yehova, analiita tumaini la paradiso itakayorudishwa duniani “ndoto ya kutaka vitu vya kimwili.”

16 Kwanza, anapaswa huyu padre Mkatoliki akumbushwe kwamba hata siku moja tumaini la mileani halijalaumiwa kwa njia rasmi na Kanisa Katoliki wala kusemwa kuwa la kupinga imani. Hilo halishangazi, kwa maana msingi wake ni Biblia na lilionwa kuwa “moja la mafundisho yanayohitajiwa sana ya imani ya Kikristo” na wengi wa “Mababa wa Kanisa” wa zamani zaidi na wenye kusifiwa zaidi. Je! Polycarp, Papias, Irenaeus, Justin Martyr na Tertullian walikuwa pia ‘waotaji wa ndoto ya kutaka vitu vya kimwili’?

17. Kwa sababu gani hakuna mtu anayeweza kuwalaumu Mashahidi wa Yehova kwa haki juu ya kuwa ‘waotaji wa ndoto ya kutaka vitu vya kimwili’?

17 Ni kweli kwamba wengine wao, na wengine katika nyakati za baadaye, walitoa sifa isiyofaa juu ya tumaini la mileani, kwa kutoa matumizi ya kimwili juu ya baraka za mileani zilizotabiriwa au hata kutumia habari hizo kwa uhusiano wa jamii ya watu na kwa njia ya kisiasa. Lakini hakuna mtu mwenye unyofu anayeweza kuwalaumu Mashahidi wa Yehova kwamba wanafanya hivyo leo. Hata sasa, katika ulimwengu wenye kuzoea anasa, Wakristo hawa wanapigana sana na utafutaji wa vitu vya kimwili na wa anasa katika maisha zao wenyewe na ndani ya makundi yao. Wao wanakazia mambo ya maana ya kiroho. Wanajua kabisa kwamba wo wote kati yao wakinaswa na utafutaji wa vitu vya kimwili katika huu “wakati wa mwisho,” huenda wasiione mileani kamwe. (Luka 21:34-36; Dan. 12:4) Tena, wao hawana matumaini ya kuileta mileani kupitia mipango ya kibinadamu ya kutengeneza hali ya watu ya kijamii. Wao wanategemea kabisa hatua ya Mungu ya kukatiza mambo kupitia mfalme wake wa Kimasihi. Akiwa ndiye kiongozi wa majeshi ya kimbinguni yenye kupiga vita, huyu ‘Mfalme wa Wafalme’ atapiga vita aukomeshe uovu wote duniani.​—Ufu. 19:11—20:3.

PARADISO—YA KIROHO NA YA KIMWILI

18. Tunaweza kuitazamia paradiso ya kiroho isitawi zaidi namna gani wakati wa mileani?

18 Tayari Mashahidi wa Yehova wanaishi katika paradiso ya kiroho. Zaidi ya hilo, wao wanatazamia kwa uhakika kuwa watu wa kiroho zaidi wakati wote wa utawala wa Kristo wa miaka 1,000, wakati ambao “vitabu vya kukunjwa” vya mfano, vyenye kufunua matakwa ya Mungu, ‘vitafunguliwa.’​—Ufu. 20:12, NW.

19. Kwa sababu gani mileani itahitaji kujinyima kwingi na kufanya kazi ngumu?

19 Kwa kusoma kwa uangalifu maandiko yanayosema juu ya utawala wa Kristo wa mileani (kwa mfano, Ufunuo 20:11–21:8), Mashahidi wa Yehova wanajua pia kwamba mileani ni wakati utakaohitaji kujinyima kwingi sana upande wa wale wanaoshiriki tumaini la kidunia. Kutakuwako kazi nyingi za kufanya katika kuilima dunia na kuirembesha, lakini hawatatumia uchoyo wasitawishe hali za paradiso kwa ajili yao wenyewe tu na jamaa zao. Kwa kweli utawala wa miaka 1,000 wa Kristo ni “siku” moja ya hukumua kwa wale watakaoiokoka “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokaribia mbiombio (Matendo 17:30, 31; Ufu. 16:14, 16); vilevile ndiyo siku ya hukumu kwa mamilioni ya wafu watakaofufuliwa na kuhukumiwa kulingana na kazi watakazozoea katika paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29; Luka 23:42, 43) Wafufuliwa hao wasiohesabika watahitaji kufundishwa bila uchoyo njia za haki na wale watakaokuwa tayari wanaishi chini ya utawala wa Masihi wa mileani. (Linganisha Isaya 11:1-9.) Hata! hiyo si “ndoto ya kutaka vitu vya kimwili”! Vilevile kazi nyingi ngumu zitahitaji kufanywa kwa njia ya kiroho pia.

20. Ni jambo gani litakalotukia ile miaka 1,000 imalizikapo, na kutakuwa na taraja gani kwa walio waaminifu?

20 Isitoshe, mileani itakuwa mwanzo tu. Baada ya jaribu fulani la mwisho, wakati ile miaka 1,000 itakapokuwa imekwisha, wanaume na wanawake watakaobaki waaminifu kwa enzi kuu ya Mungu ya ulimwengu wote wataingizwa upesi ndani ya umilele wa uzima juu ya dunia ya paradiso.b—1 Kor. 15:24-28; Ufu. 20:7-10.

TUMAINI LINALOWEZA KUWA LAKO

21, 22. (a) Nyakati zote Mashahidi wa Yehova wanafurahi kufanya nini? (b) Tumaini lao ni nini kwa wakati ujao ulio karibu?

21 Hilo ndilo tumaini linalofurahiwa sana sasa na mashahidi wa Kikristo wa Yehova zaidi ya 2,000,000 katika nchi zaidi ya 200. Tumaini hilo li hai sana katika akili na mioyo yao, hai sana kiasi cha kwamba nyakati zote wanakuwa wenye furaha kuwapa wengine ‘sababu ya lile tumaini lililo ndani yao.’​—1 Pet. 3:15, NW.

22 Tangu mwaka wa 1914, matukio ya ulimwengu yenye kutimiza unabii wa Biblia yanaonyesha kwamba sasa tunaishi katika “wakati wa mwisho,” na kwamba “wakati wa taabu” usiopata kuwa na kifani u karibu. (Dan. 12:1-4; Mt. 24:3-21) Mabaki ya “waliochaguliwa” na “mkutano mkubwa” wa wenzao wameahidiwa kuokoka waipite hiyo “dhiki kubwa.” (Mt. 24:22; Ufu. 7:9, 10, 14) Baada ya hapo, matumaini yao mbalimbali ya mileani yatatimizwa. Je! wewe unaamini hilo? ‘Mungu apaye tumaini na akujaze wewe na furaha yote na amani kwa kuamini kwako, ili upate kujawa sana katika tumaini.’​—Rum. 15:13, NW. —Kutoka The Watchtower, April 15, 1981.

[Maelezo ya Chini]

a Angalia sura ya 7, “Mambo ya Kutazamiwa kwa Waamuzi kwa Miaka Elfu,” katika kitabu God’s Kingdom of a Thousand Years Has Approached, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society.

b Kwa maelezo zaidi, tafadhali usome sura 12 mpaka 16 za kitabu Life Does Have a Purpose, kilichochapishwa na Watch Tower Bible and Tract Society.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Chini ya utawala wa Masihi wa mileani, watakaofufuliwa watafunzwa njia za haki

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki