Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w81 9/15 kur. 10-16
  • Wakristo na Tumaini la Mileani

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakristo na Tumaini la Mileani
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WAKRISTO WA KWANZA WALIITWA “WAMILEANI”
  • BADO WALIKUWA NA TUMAINI LA PARADISO JUU YA DUNIA
  • KRISTO HAKUBATILISHA TUMAINI LA MILEANI
  • TUMAINI LA MILEANI LAFUNULIWA KABISA
  • “SIRI TAKATIFU” YAELEZWA
  • TUMAINI JIPYA LENYE KULETA MABADILIKO MAKUBWA
  • MWITO WA KIMBINGUNI KWA HESABU NDOGO YA “WALIOCHAGULIWA”
  • Lile Tumaini la Miliani Lashinda
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
  • Kujipanga Kitengenezo Sasa kwa Ajili ya Miaka Elfu Itakayokuja
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kushangilia Katika Tumaini Letu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Apokalipsi—Je, Tuiogope Au Tuitumainie?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1981
w81 9/15 kur. 10-16

Wakristo na Tumaini la Mileani

“Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”​—Mt. 6:9, 10.

1. (a) Jumuiya ya Wakristo inasema namna gani juu ya tumaini la mileani? (b) Kwa sababu gani Mashahidi wa Yehova hawasumbuliwi na jambo hilo?

KWA Wakatoliki wa Kanisa Roma, na kwa kweli, dini nyingi zilizoimarishwa sana za Waprotestanti, haziwatajii kamwe wanakanisa juu ya tumaini la mileani (miaka elfu). Wanasema kwa dharau juu ya tumaini hilo kuwa “umileani” (kufuata miaka 1,000), na juu ya wale wanaoifuata kuwa “wamileani.” Walakini Mashahidi wa Yehova hawaonei haya sadikisho hilo, maana mambo ya hakika ya kihistoria yasiyokanushika yanaonyesha kwamba tumaini la mileani lilifuatwa na Wakristo wa kwanza.

WAKRISTO WA KWANZA WALIITWA “WAMILEANI”

2. Vitabu encyclopedia viwili vinasema nini juu ya kuamini mileani kati ya Wakristo wa kwanza?

2 Kikitaja Wakristo wanaoamini utawala wa miaka 1,000 wa Kristo, kitabu Encyclopedia Americana kinasema hivi: “Wale walio na maoni hayo ni wamileani au wafuasi wa miaka elfu moja, nayo imani yao ni ufuataji wa miaka elfu moja (Kigiriki: chilioi, 1,000). Inakubaliwa kote kote kwamba maoni hayo, angaa yalikuwa yameenea sana katika kanisa la kale, kama hayakuwa kila mahali.” Kitabu cha Kifaransa Encyclopcedia Universalis kinatuambia hivi: “Katika Jumuiya ya Wakristo ya [nchi za] Magharibi umileani ulikuwa na sehemu kubwa sana katika Ukristo-Uyahudi wakati wa karne tatu za kwanza. . . . Umileani ulikuwa umeimarishwa sana wakati wa karne za kwanza za Ukristo.”

3, 4. (a) Kuna mambo gani yenye kuonyesha kwamba haikuwa lazima Wakristo waungojee Ufunuo kabla ya kuwa na matumaini ya mileani? (b) Huenda wengine wakadai nini juu ya tumaini la mileani?

3 Kuna ushuhuda kwamba matumaini yanayohusiana na miaka 1,000 ya utawala wa Kristo, Wakristo walikuwa nayo hata kabla ya Yohana kupokea Ufunuo mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. Kwa kusoma maandishi ya manabii Wayahudi, walikuwa wamepata habari za kimbele za tumaini zuri sana la mileani lililotolewa na Kristo katika Ufunuo, sura za 20 na 21. Kwa kupendeza, kitabu Encyclopcedia Britannica (chapa ya 1966) kinathibitisha jambo hilo, kinaposema hivi: “Kati ya Wakristo wa kwanza wazo la mileani . . . lilitokana hasa na matazamio ya Kiyahudi juu ya yaliyoandikwa yatawapata wanadamu na ulimwengu mwishowe.” Juu ya jambo ilo hilo kitabu New Encyclopcedia Britannica (1977) cha vitabu 30 kinasema hivi: “Katika Kitabu cha Ufunuo kuchanganywa kwa Ukristo na matazamio ya Kiyahudi ya kuharibiwa kwa uovu na wema kushinda mwishowe kulikamilishwa. . . . Wakati wa mamia chache ya miaka ya kwanza ya historia ya Ukristo [33-133 W.K.], namna hiyo ya umileani, au ya miaka elfu, kwa kawaida ilifunzwa na kukubaliwa ndani ya kanisa.”​—Maneno yaliyolazwa ni yetu.

4 Huenda wengine wakajibu hivi: ‘Pengine, walakini tumaini la mileani la Wakristo hao wa kwanza halikuhusu dunia. Lilikuwa tumaini la kimbinguni.’ Hata hivyo, mambo ya hakika ya kihistoria yanaonyesha nini, nayo Biblia pia? Ebu tuone.

BADO WALIKUWA NA TUMAINI LA PARADISO JUU YA DUNIA

5, 6. Kulingana na waandikaji mbalimbali, Wakristo wa Karne ya kwanza walishikilia maoni gani?

5 Kuna ushuhuda mwingi kwamba Wakristo wa kwanza hawakuwaza kamwe kwamba unabii na ahadi zote katika Maandiko ya Kiebrania juu ya kurudishwa kwa paradiso juu ya dunia zilikuwa zimefutiliwa mbali na kuja kwa Masihi au Kristo. Kitabu Dictionnaire de Theologie Catholique kinakubali hivi: “Vyanzo vya kuamini mileani vinatangulia wakati wa kipindi cha Ukristo. Imani hiyo juu ya utawala wa kidunia wa Masihi ulianza katika matumaini ya Israeli.”

6 Katika kitabu A History of Christianity, mwanahistoria Kenneth Scott Latourette anasema hivi juu ya Wakristo wa kwanza waliokuwa na tumaini la kurudi kwa pili kwa Kristo: “Wengi walikuwa na maoni kwamba kabla ya mwisho kabisa wa mambo na kutimizwa kabisa kwa kusudi la Mungu katika utimizo mkamilifu wa mapenzi Yake, tumaini ambalo lilikuwa jambo la kawaida kwa Wakristo wote, Kristo angerudi, asimamishe ufalme wake duniani na kutawala kwa miaka elfu. . . . Wazo juu ya kizazi au vizazi vya miaka elfu moja kwa urefu halikuwa la Wakristo tu, bali pia lilikuwa kati ya wenye kufuata dini ya Kiyahudi.”

7. Ni nini linaloonyesha kwamba Wakristo wa kwanza hawakushindwa kutofautisha kati ya paradiso na mbingu?

7 Hivyo, kuna ushuhuda mwingi kwamba Wakristo wa kwanza walikuwa “wamileani” (waliamini juu ya miaka elfu moja), maana jina hilo lilitumiwa kwa wale waliokuwa na tumaini la utawala wa miaka 1,000 wa Kristo Masihi. Yesu alikuwa ameonyesha kwamba atatawala akiwa mbinguni, walakini hakubatilisha tumaini la Kimasihi la hapo mbele la Wayahudi, kurudishwa kwa paradiso juu ya dunia wakati wa mileani hiyo. Kwa kupendeza, kitabu cha Kikatoliki Supplement au Dictionnaire de la Bible kinakubali kwamba “katika maandishi ya Kiyahudi, kama vile katika vitabu vya kwanza vya Kikristo, neno Paradiso mara nyingi halimaanishi mbingu.”​—Maneno yaliyolazwa ni yetu.

KRISTO HAKUBATILISHA TUMAINI LA MILEANI

8. (a) Kuja kwa Yesu kulikuwa uhakikisho thabiti wa jambo gani? (b) Maandiko yanaonyeshaje kwamba paradiso itarudishwa duniani?

8 Katika Mahubiri yake ya Mlimani yajulikanayo sana, Yesu alisema hivi: “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza.” (Mt. 5:17) Au, kama vile Biblia Today’s English Version inavyotafsiri sentensi hiyo ya mwisho: “Sikuja kuwafutilia mbali, bali kufanya mafundisho yao yatimie.” Kwa kuwa Yesu alikuja kutimiza mafundisho ya manabii, kuja kwake kulikuwa uhakikisho kwamba unabii wao kuhusu kurudishwa kwa paradiso duniani ungetimizwa. Hapa pana unabii mchache kati ya huo: Zaburi 37:11, 29; 72:1-8, 16-19; 115:16; Isaya 9:6, 7; 11:1-10; 45:18; Danieli 2:34, 35, 44, 45; 7:13, 14.

9. Sala ya Kielelezo inahusianishaje Ufalme na tumaini la mileani?

9 Vilevile katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alionyesha wazi kabisa kwamba dunia itakuwa na sehemu ya kutimiza katika utimizo wa mapenzi au kusudi la kimungu. Alifunza wafuasi wake waombe hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mt. 6:9, 10) Alihusianisha kutimizwa kwa mapenzi ya Mungu juu ya dunia na kuja kwa ufalme wa Mungu, ambao ni ufalme wa Kimasihi. Hivyo, Sala ya Bwana, ambayo imerudiwa mara mamilioni na Wakatoliki na Waprotestanti wakati wa karne zote, kwa kweli, kati ya mambo mengineyo, ni sala ya kuomba ahadi za Kimasihi zinazohusiana na tumaini la mileani zitimizwe.

TUMAINI LA MILEANI LAFUNULIWA KABISA

10. (a) Ni wakati gani na jinsi gani Yesu alifunua wazi kabisa tumaini la mileani? (b) Yeye alitoa maelezo gani yenye kuchangamsha moyo?

10 Miaka 25 baada ya kuharibiwa kwa Yerusalemu na Waroma katika mwaka 70 W.K. (jambo ambalo lilikomesha matumaini ya Kiyahudi ya kukombolewa kwa taifa lao na Masihi wa kisiasa) Yesu Masihi wa kweli, alifunua kabisa tumaini la kweli la mileani. Katika maandishi yake ya Ufunuo ambayo alipokea kutoka kwa Mungu kupitia kwa Yesu Kristo mtume Yohana aliandika hivi:

“Kisha nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake. Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani akamfunga miaka elfu. . . .

“Kisha nikaona viti vya enzi, wakaketi juu yake, nao wakapewa [uwezo wa, NW] hukumu. . . . Heri, na mtakatifu, ni yeye aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hao mauti ya pili haina nguvu; bali watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, nao watatawala pamoja naye hiyo miaka elfu.

“Kisha nikaona mbingu mpya na nchi mpya; . . . Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao . . . Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”​—Ufu. 20:1-6; 21:1-4.

“SIRI TAKATIFU” YAELEZWA

11. Tumaini la mileani lililofunuliwa na Yesu lililinganaje na tumaini la asili la Kimasihi la Wayahudi?

11 Je! huwezi kuona ufanani kati ya maelezo haya ya utawala wa mileani wa Kristo na tumaini la asili la Kimasihi la Wayahudi, “tumaini la wakati ujao mzuri ajabu wa Kimasihi . . . kizazi chenye ufanisi mwingi wa raha nyingi ya kiparadiso . . . ulimwengu wa amani kamili na upatano kati ya viumbe vyote . . . ‘mbingu mpya na dunia mpya,’ “tukirudia kutaja maneno ya kitabu The Jewish Encyclopedia?

12, 13. Ni nini linaloonyesha kwamba wanafunzi wa Yesu walikuwa wangali wakitazamia utawala wa kidunia wa Masihi?

12 Walakini, haiwezi kukanwa kwamba kulikuwa na habari za maana juu ya ufalme wa Kimasihi ambazo Wayahudi hawakuzifahamu na kwamba hata wale mitume 12 na wanafunzi wengine wa kwanza wa Kristo walitatizwa kuzielewa. Muda mfupi baada ya kutoa Mahubiri ya Mlimani yake, alimofundisha wanafunzi wake wasali ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yatukie duniani, kama katika mbingu, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Kwenu ninyi ile siri takatifu ya ufalme wa Mungu imepewa, lakini kwa wale walio nje mambo yote yanatukia katika mifano.”​—Marko 4:11, NW.

13 Yesu aliwafundisha wanafunzi wake mambo mengi juu ya ufalme wa Kimasihi wakati wa huduma yake yote ya kidunia. Kwa kweli, hata baada ya kifo chake na mpaka wakati alipopaa kwenda kwa Baba yake wa kimbinguni aliendelea kuwaambia “mambo yaliyouhusu ufalme wa Mungu.” Hata hivyo, ulizo lao la mwisho kabisa kumwuliza yeye lilikuwa: “Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?”, kwa njia hiyo wakionyesha wazi kwamba wangali walimtazamia Masihi aurudishe ufalme wa kimwili wa Israeli. (Matendo 1:3, 6) Walikuwa na maoni yenye kufaa kwa kufikiri kwamba ufalme wa Kimasihi ulihusu utawala, serikali, lakini walikosea walipowaza kwamba Masihi angetawala duniani na kwamba serikali yake ingekuwa ya Wayahudi peke yao.

14. (a) Ni nini lililowezesha wanafunzi wa Kristo wajitenge na tumaini lao lenye makosa? (b) Ni sehemu gani za maana za ile “siri takatifu” ambazo Wakristo wa kwanza walipata kuzielewa polepole?

14 Ni baada tu ya kumiminwa kwa roho takatifu kwenye Pentekoste wanafunzi wa Kristo walipojitenga na wazo la ufalme wa Kimasihi wenye utukuzo wa taifa na kuelewa sehemu mpya na za maana za “ile siri takatifu ya ufalme wa Mungu.” Upande mmoja wa “siri takatifu” hiyo ulikuwa kwamba Masihi angekuwa mfalme wa kimbinguni na kwamba serikali yake ingekuwa katika mbingu. (Yohana 18:36; Matendo 2:32-36; 1 Tim. 3:16) Pande nyingine za “siri takatifu” hiyo—kweli zilizokuwa mpya na kuleta mabadiliko makubwa kwenye akili za Wayahudi waaminifu zilizofinyangwa na Maandiko wala si na filosofia ya Kigiriki—zilikuwa kwamba hesabu ndogo ya wanadamu ingechaguliwa wawe “watakatifu” watakaokuwa wenzi wenye kushirikiana na Masihi katika ufalme wake, kwamba wangetawala pamoja naye katika mbingu, na kwamba hawangechaguliwa kati ya Wayahudi peke yao bali kati ya Mataifa au watu wasio Wayahudi pia.​—Dan. 7:13, 14, 27; Luka 12:32; 22:28-30; Yohana 14:1-3; Efe. 3:3-6; Kol. 1:26, 27.

TUMAINI JIPYA LENYE KULETA MABADILIKO MAKUBWA

15. Kwa sababu gani wazo lenyewe la kwenda mbinguni lilileta mabadiliko makubwa sana kwa mabaki waaminifu wa Kiyahudi?

15 Hayo yote yalikuwa jambo jipya kabisa. Tumaini la asili la Kimasihi la Wayahudi lilikuwa tumaini la kidunia, na ni baada tu ya kuchochewa na mapokeo ya uongo ya kidini na filosofia ya uongo kwamba wengine wao walipata kuamini kuna nafsi isiyokufa, baada ya muda mwingi sana kupita katika historia yao. Mabaki waaminifu wa Kiyahudi walioshikamana na Maandiko ya Kiebrania yaliyoongozwa na Mungu na kumkubali Yesu kuwa ndiye Masihi wa kweli hawakuamini kamwe kwamba watu wanazaliwa wakiwa wamerithi hali ya kutokuweza kufa. Kwa hiyo wazo la Masihi fulani mwenye kutawala dunia akiwa mbinguni na la wao wenyewe kuwa watawala wenzake katika mbingu lilikuwa jambo lenye kuwaletea mabadiliko makubwa sana.

16. Petro aliandika nini juu ya hili tumaini jipya lenye kuleta mabadiliko makubwa?

16 Katika barua aliyoandikia Wakristo wa kwanza waliokuwa wameupokea mwito huo huo wa pekee wakawe makuhani na wafalme pamoja na Masihi wa kimbinguni, mtume Petro aliandika hivi: “Awe mbarikiwa Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa sababu kulingana na rehema yake kuu alitupa sisi uzaliwa mpya kwenye tumaini lililo hai kupita kwa ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenye urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa kando katika mbingu kwa ajili yenu ninyi . . . Lakini ninyi ni ‘mbari iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme.’ 1 Pet. 1:3, 4; 2:9, NW.

17. Paulo alionyeshaje kwamba ule mwito kwenye uzima katika mbingu ulikuwa jambo jipya?

17 Mtume Paulo pia aliandika habari za mwito huo wa pekee kwenye maisha ya kimbinguni, akisema: “Yeye alituokoa sisi na kutuita sisi kwa mwito mtakatifu . . . sasa umefanywa uonekane kwa uwazi kupita kwa udhihirisho wa Mwokozi wetu, Kristo Yesu, ambaye amefuta kifo lakini akaweka nuru juu ya uzima na kutokuharibika.” (2 Tim. 1:9, 10, NW) Kama uzima katika mbingu ndio uliokuwa umekuwa tumaini la mabaki waaminifu kati ya Wayahudi, kwa sababu gani ilimlazimu Kristo ‘aweke nuru’ (afahamishe) juu ya huo “mwito mtakatifu” kwenye kutokuharibika? Hapana, ni wazi kwamba mwito huo kwenye uzima wa kimbinguni ulikuwa jambo jipya kabisa kwa Wakristo hawa wa kwanza waliochaguliwa kati ya Wayahudi na Mataifa.

MWITO WA KIMBINGUNI KWA HESABU NDOGO YA “WALIOCHAGULIWA”

18, 19. Eleza jinsi barua ya pili ya Paulo kwa Timotheo na barua ya kwanza ya Petro zinavyoonyesha kwamba si wote wale wanaotumainia kuishi milele watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo katika mbingu. (Ufu. 5:9, 10)

18 Lakini je! wale wote wanaomkubali Kristo na kutumaini kuishi milele wanaupokea huu “mwito mtakatifu” kwenye uzima usioharibika katika mbingu? Akionyesha kwamba mwito huu wa pekee umekusudiwa kwa hesabu ndogo ya ‘wateule’ (Union Version) au “waliochaguliwa,” Paulo anaongeza hivi: “Kwa sababu hiyo mimi ninaendelea kuyavumilia mambo yote kwa ajili ya waliochaguliwa, ili wao pia waweze kuupata wokovu ulio katika umoja pamoja na Kristo Yesu pamoja na utukufu wa milele. Wenye uaminifu ni ule usemi: Kwa uhakika ikiwa sisi tulikufa pamoja, sisi tutaishi pamoja pia; ikiwa sisi tutaendelea kuvumilia, sisi tutatawala pamoja tukiwa wafalme pia.”​—2 Tim. 2:10-12, NW.

19 Ikiwa wote wanaookolewa wanaitwa kwenye “utukufu wa milele” ili ‘watawale pamoja kama wafalme’ na Kristo Yesu, watatawala nani? Na ikiwa wote watakuwa “ukuhani wa kifalme,” ni kwa ajili ya nani watatenda kama makuhani wa kifalme?

20. Barua za Paulo kwa Wagalatia na Warumi zinaonyeshaje kwamba hesabu ya Waisraeli wa kiroho ni ndogo?

20 Fikiria yafuatayo: Katika barua yake kwa Wagalatia, Paulo anasema kwamba Wakristo waliochaguliwa kati ya Wayahudi na watu wasio Wayahudi na ‘kubatizwa ndani ya Kristo’ “ni uzao wa Ibrahimu kweli kweli, warithi kwa habari ya ahadi,” naye anawaita “yule Israeli wa Mungu.” (Gal. 3:26-29; 6:16, NW) Na katika barua yake kwa Warumi, mtume uyo huyo anasema juu ya ile “siri takatifu” ya watu wasio Wayahudi kuitwa na Mungu kwa sababu ya “ukosefu wa imani” wa Wayahudi wengi, kisha anaongeza kwamba—na kifungu hiki cha maneno ni cha maana sana—“mpaka hesabu iliyojaa [“hesabu kamili,” TEV] ya watu wa mataifa iwe imeingia.” Anaeleza kwamba “katika njia hii,” yaani, kwa njia ya Mataifa kuitwa waijaze hesabu iliyotakiwa, “Israeli yote itaokolewa.” Kwa wazi hiyo inamaanisha Israeli wa kiroho, wale “waliochaguliwa” kati ya Wayahudi na watu wasio Wayahudi ambao ni “‘Israeli’ kweli kweli” au “Israeli kikweli.”​—Rum. 11:7, 17-26, NW; 9:6 (The New English Bible); 2:28, 29, NW.

21. (a) Kuna Waisraeli wa kiroho wangapi? (b) Ni andiko gani linalohakikisha kwamba hawachaguliwi kati ya malaika?

21 Kwa kuwa watu wasio Wayahudi wangeupokea huu “mwito mtakatifu” mpaka tu wakati ambao “hesabu iliyojaa” ingefikiwa ya wale wenye kufanyiza “yule Israeli wa Mungu,” ni jambo la wazi kwamba hesabu ya hao Waisraeli wa kiroho ni ndogo. Basi, ni hesabu gani? Fungua Ufunuo 7:1-8. Hapo kikomo kilicho wazi kimewekwa juu ya hesabu ya Wakristo ‘waliotiwa muhuri’ wawe sehemu ya Israeli wa kiroho. Kwamba hesabu hiyo ndogo haikuchaguliwa kati ya malaika inahakikishwa na Ufunuo 14:1-4 (NW), ambapo hesabu iyo hiyo inasemwa kuwa “wamenunuliwa kutoka kwenye dunia,” “wamenunuliwa kutoka kati ya wanadamu kama matunda ya kwanza kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo.”

22. Kwa wale 144,000, tumaini lao lenye msingi wa Biblia ni la aina gani?

22 Kwa hao 144,000 waliozaliwa kwa roho, tumaini lao lenye msingi wa Biblia ni tumaini la kimbinguni. Watakapokwisha kushiriki katika “ule ufufuo wa kwanza,” “watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja naye kwa ile miaka elfu.” —Ufu. 20:6, NW.

23. Ni maulizo gani yanayotokezwa na maneno “matunda ya kwanza” na “wafalme”?

23 Lakini ikiwa hawa “waliochaguliwa” ni “matunda ya kwanza,” ni jambo la wazi kwamba matunda mengine yatafuata, Na ikiwa ‘watatawala kama wafalme,’ ni nani watakaokuwa raia zao na tumaini la hao ni nini? Tutaona tunapoendelea na uchunguzi huu.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Papias wa Hierapoli, Irenaeus wa Lyons na Justin wa Rumi—“watakatifu” wa karne ya pili na “Mababa” wenye kutambuliwa na Kanisa Katoliki—wote waliikubali mileani. —The Catholic Encyclopedia.

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Katika kupigana kwao na tumaini la mileani, mpresbiteri wa Kirumi Kayo na “Mtakatifu” Dionisio walijishusha kwa kuukataa unyofu wa Ufunuo, aliopewa mtume Yohana. —Dictionnaire de Theologie Catholique.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Wakati wa Mileani, Yesu atatawala akiwa mbinguni juu ya dunia itakayokuwa imerudishwa kuwa paradiso.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki