Apokalipsi—Je, Tuiogope Au Tuitumainie?
“Leo, Apokalipsi imekuwa jambo halisi liwezalo kutukia wala si tukio tu linaloelezwa katika Biblia.”—Javier Pérez de Cuéllar, aliyekuwa katibu-mkuu wa Umoja wa Mataifa.
JINSI mtu huyo mashuhuri ulimwenguni alivyotumia neno “apokalipsi” inaonyesha namna watu wengi wanavyolielewa na kuliona likitumiwa katika sinema na vichwa vya vitabu, makala za magazeti, na ripoti za magazeti. Neno hilo lafanya mtu afikirie msiba wa ulimwenguni pote. Lakini kwa kweli neno “apokalipsi” lamaanisha nini? Na jambo muhimu hata zaidi, kitabu cha Biblia kinachoitwa Apokalipsi au Ufunuo kina ujumbe gani?
Neno “apokalipsi” latokana na usemi wa Kigiriki unaomaanisha “kufunua,” au “kugubua.” Ni jambo gani lililogubuliwa, au kufunuliwa, katika Ufunuo wa Biblia? Je, ni ujumbe maalumu wa uangamizo, yaani dalili ya uharibifu ambao hauna waokokaji? Mwanahistoria Jean Delumeau wa Taasisi ya Ufaransa alitangaza hivi alipoombwa maoni yake juu ya Apokalipsi: “Hicho ni kitabu cha faraja na tumaini. Watu wametilia chumvi yaliyomo katika kitabu hicho kwa kuzingatia sehemu zake zinazozungumzia maangamizo.”
Kanisa la Mapema na Apokalipsi
“Wakristo” wa mapema waliionaje Apokalipsi na tumaini ambalo inataja la Utawala wa Miaka Elfu (Milenia) wa Kristo juu ya dunia? Mwanahistoria uyo huyo alisema: “Naona kwamba Wakristo wa karne chache za kwanza sanasana walikubali fundisho la milenia. . . . Miongoni mwa Wakristo wa karne za mapema walioamini Milenia hasa ni Papias, askofu wa Hierapolis katika Asia Ndogo, . . . Mtakatifu Justin, aliyezaliwa Palestina, na aliyeuawa kwa sababu ya imani yake kule Roma mwaka wa 165 hivi, Mtakatifu Irenæus, askofu wa Lyons, aliyekufa mwaka wa 202, Tertullian, aliyekufa mwaka wa 222, na . . . yule mwandishi mkuu Lactantius.”
Kuhusu Papias, ambaye inasemekana aliuawa huko Pergamum kwa sababu ya imani yake mwaka wa 161 au 165 W.K., kichapo The Catholic Encyclopedia chasema: “Inaonekana Askofu Papias wa Hierapolis, mfuasi wa Mtakatifu Yohana, alitetea fundisho la milenia. Alidai kwamba alifundishwa na watu walioishi wakati wa Mitume, na Irenæus asimulia kwamba ‘Wazee’ wengine, ambao walikuwa wamemwona mwanafunzi Yohana na kumsikiliza, walijifunza kutokana naye kwamba milenia ni sehemu ya fundisho la Bwana. Kulingana na Eusebius . . . Papias alisisitiza katika kitabu chake kwamba ufufuo wa wafu ungefuatwa na miaka elfu moja ya ufalme wa kidunia wa Kristo ulio halisi na mtukufu.”
Jambo hilo latufahamisha nini kuhusu matokeo ya kitabu cha Apokalipsi, au Ufunuo, kwa waamini wa awali? Je, kilitokeza woga au tumaini? Kwa kupendeza, wanahistoria huwaita Wakristo wa kale chiliasts, neno linalotokana na maneno ya Kigiriki khiʹli·a eʹte (miaka elfu). Ndiyo, wengi wao walijulikana kuwa waamini wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, ambao ungefanya dunia kuwa paradiso. Mahali pekee katika Biblia ambapo tumaini la milenia limetajwa hususa ni katika Apokalipsi, au Ufunuo. (20:1-7) Basi, badala ya kuwaogopesha waamini, Apokalipsi iliwapa tumaini zuri ajabu. Katika kitabu chake The Early Church and the World, Cecil Cadoux, profesa wa historia ya kanisa katika Oxford, aandika: “Japo hatimaye maoni ya miaka elfu yalikataliwa, hayo yaliaminiwa sana na Kanisa kwa muda mrefu, yakifundishwa na baadhi ya waandishi wenye kuheshimika zaidi.”
Sababu Iliyofanya Tumaini la Apokalipsi Likataliwe
Kwa kuwa ni wazi kulingana na historia kwamba Wakristo wengi wa mapema walitumainia Utawala wa Milenia wa Kristo juu ya dunia paradiso, sasa ilikuwaje kwamba hayo “maoni juu ya ile miaka elfu” ‘yalikataliwa hatimaye’? Kulizuka uchambuzi wenye msingi mzuri kwa sababu, kama asemavyo msomi Robert Mounce, “kwa kusikitisha, wengi walioamini miaka elfu walikuwa na maoni yenye kupita kiasi na wakawa wanaona kwamba ile miaka elfu ingekuwa na aina mbalimbali za vitu vya kimwili na anasa tele.” Lakini maoni hayo yenye kupita kiasi yangalirekebishwa bila kukataa tumaini la kweli la Milenia.
Mbinu zilizotumiwa na wapinzani wa fundisho la milenia zilikuwa zenye kushangaza sana. Kamusi Dictionnaire de Théologie Catholique yasema juu ya mfuasi wa kanisa Mroma Caius (aliyeishi mwishoni mwa karne ya pili, na mwanzoni mwa karne ya tatu) kwamba “ili kushinda fundisho la milenia, alikataa katakata kwamba Apokalipsi [Ufunuo] na Gospeli ya Mtakatifu Yohana ni vya kweli.” Hiyo Dictionnaire yaendelea kusema kwamba Dionysius, askofu wa karne ya tatu wa Aleksandria, aliandika hoja zinazopinga fundisho la milenia akisema kwamba “ili kuzuia wale walioshikilia maoni hayo wasitegemeze imani yao kwenye Apokalipsi ya Mtakatifu Yohana, yeye alikana mara moja ukweli wa kitabu hicho.” Upinzani mkali kama huo dhidi ya tumaini la baraka za milenia duniani waonyesha uvutano wenye hila uliokuwa ukiendelea miongoni mwa wanatheolojia wa wakati huo.
Profesa Norman Cohn aliandika hivi katika kitabu chake The Pursuit of the Millennium: “Katika karne ya tatu kulikuwa na jaribio la kwanza la kuharibu fundisho la milenia, wakati ambapo Origen, ambaye huenda ndiye alikuwa mashuhuri zaidi kati ya wanatheolojia wa Kanisa la kale, alipoanza kusema kwamba Ufalme haungetawala kihalisi bali ungekuwa katika nafsi za waamini tu.” Akitegemea falsafa za Kigiriki badala ya Biblia, Origen alichafua tumaini zuri ajabu la baraka za kidunia chini ya utawala wa Ufalme wa Kimesiya na kulifanya liwe “kitu [fulani] . . . katika nafsi za waamini.” Mwandishi Mkatoliki Léon Gry aliandika: “Uvutano mkubwa wa falsafa ya Kigiriki . . . uliharibu hatua kwa hatua maoni ya utawala wa miaka elfu.”
“Kanisa Limepoteza Ujumbe Wake wa Tumaini”
Augustine ndiye Mkuu wa Kanisa ambaye bila shaka alichangia zaidi kuchanganya falsafa za Kigiriki na Ukristo ambao kufikia wakati wake ulikuwa umepotoka kabisa. Ingawa hapo awali alikuwa mtetezi mkuu wa fundisho la milenia, hatimaye alikataa jambo lolote lile lililohusiana na Utawala wa wakati ujao wa Milenia wa Kristo juu ya dunia. Akasema kwamba Ufunuo sura ya 20 imeandikwa kwa mafumbo.
Kichapo The Catholic Encyclopedia chasema: “Hatimaye Augustine alishikilia maoni ya kwamba hakutakuwa na milenia. . . . Yeye atuambia kwamba ufufuo wa kwanza, ambao unatajwa katika sura hii warejezea kuzaliwa upya kwa njia ya kiroho wakati wa ubatizo; ile sabato ya miaka elfu inayofuata historia ya miaka elfu sita, ndiyo uhai wote wa milele.” Kichapo The New Encyclopædia Britannica chasema: “Maoni ya Augustine ya kwamba ile milenia si halisi yakawa fundisho rasmi la kanisa . . . Warekebishaji Waprotestanti ambao ni wafuasi wa mapokeo ya Kilutheri, Calvin, na Anglikana . . . waliendelea kushikilia sana maoni ya Augustine.” Basi, wafuasi wa makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wakawa hawana tumaini la milenia.
Isitoshe, kulingana na mwanatheolojia Mswisi Frédéric de Rougemont, “kwa kukana kabisa imani yake ya awali katika utawala wa miaka elfu, [Augustine] alisababisha madhara makubwa sana katika Kanisa. Akiwa na mamlaka nyingi sana, aliidhinisha kosa ambalo lilifanya [Kanisa] likose tumaini lake la kidunia.” Mwanatheolojia Mjerumani Adolf Harnack alikubali kwamba kukana imani katika Milenia kuliwanyima watu wa kawaida “dini wanayoielewa,” wakibadili “dini na matumaini yao ya zamani” kwa “dini ambayo hawaielewi.” Makanisa matupu katika nchi nyingi yanathibitisha wazi kwamba watu wanahitaji imani na tumaini ambazo wanaweza kuelewa.
Katika kitabu chake Highlights of the Book of Revelation, msomi wa Biblia George Beasley-Murray aliandika: “Kwa sababu ya uvutano mkubwa sana wa Augustine na pia kukubaliwa kwa fundisho la milenia katika madhehebu fulani, Wakatoliki na Waprotestanti wameungana kulikataa fundisho hilo. Wanapoulizwa wana tumaini gani tofauti kwa mwanadamu katika ulimwengu huu, jibu rasmi linakuwa: Hakuna tumaini lolote. Ulimwengu utaharibiwa Kristo ajapo na mahali pake patachukuliwa na mbingu na helo za milele ambamo historia itasahauliwa. . . . Kanisa limepoteza ujumbe wake wa tumaini.”
Tumaini Zuri Ajabu la Apokalipsi Lingali Lipo!
Mashahidi wa Yehova husadiki kwamba ahadi nzuri ajabu zinazohusu Milenia zitatimizwa. Alipohojiwa kwenye programu ya televisheni ya Ufaransa juu ya habari isemayo “Mwaka wa 2000: Woga wa Apokalipsi,” mwanahistoria Mfaransa Jean Delumeau alisema hivi: “Mashahidi wa Yehova wanafuata kabisa fundisho la milenia, kwa sababu wao husema kwamba karibuni . . . tutaingia katika kipindi cha miaka 1,000 chenye furaha japo kupitia magumu.”
Hilo ndilo jambo ambalo mtume Yohana aliona na kufafanua katika kitabu chake Apokalipsi, au Ufunuo. Aliandika: “Nikaona mbingu mpya na dunia mpya . . . Ndipo nikasikia sauti kubwa kutoka katika kiti cha ufalme ikisema: ‘Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa vikundi vya watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.’”—Ufunuo 21:1, 3, 4.
Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi ya ulimwenguni pote ya kufundisha watu Biblia ili kuwawezesha watu wengi iwezekanavyo wawe na tumaini hilo. Watafurahi kukusaidia ujifunze mengi zaidi kulihusu.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Papias alidai kwamba alipokea fundisho la Milenia moja kwa moja kutoka kwa watu walioishi wakati wa mitume
[Picha katika ukurasa wa 7]
Tertullian aliamini Utawala wa Milenia wa Kristo
[Hisani]
© Cliché Bibliothèque Nationale de France, Paris
[Picha katika ukurasa wa 7]
“Kwa kukana kabisa imani yake ya awali katika utawala wa miaka elfu, [Augustine] alisababisha madhara makubwa sana katika Kanisa”
[Picha katika ukurasa wa 8]
Dunia paradiso iliyoahidiwa katika Apokalipsi ni jambo la kutumainiwa kabisa