Kwa Nini Watu Huogopa Apokalipsi?
“KWA miaka mingi, Wakristo washupavu wamekuwa wakitoa unabii kwamba karibuni jamii nzima itaporomoka kwa njia [fulani],” asema Damian Thompson, mwandikaji wa mambo ya dini, katika gazeti la Time. “Sasa, [Wakristo] hao wanashangaa kwamba mambo hayo yanachukuliwa kwa uzito, na isitoshe yanaenezwa na watu walewale ambao walikuwa wakiwadhihaki: watayarishi wa programu za kompyuta, wakuu wa biashara na wanasiasa.” Anasisitiza kwamba ule woga wa kwamba kompyuta zote ulimwenguni hazitaweza kufanya kazi mwaka wa 2000 “umefanya watu ambao hawafuatii kamwe mambo ya kidini waamini milenia” na wanaogopa kuzuka kwa misiba kama vile “hofu za umma, serikali kushindwa kufanya kazi, fujo zinazotokana na uhaba wa chakula, na ndege kugonga majengo marefu.”
Kwa kuongezea mahangaiko hayo yanayopata watu wengi kuna utendaji wenye kusumbua wa dini kadhaa ndogo-ndogo, ambazo huitwa dini za “kutabiri uharibifu.” Mnamo Januari 1999, katika makala yenye kichwa “Jerusalem na Ving’ora vya Apokalipsi,” gazeti la Ufaransa Le Figaro, lilisema: “Vikosi vya usalama vya [Israeli] vinakadiria kwamba ‘waamini wa milenia’ zaidi ya mia moja watakuwa wakingojea kule kuja kwake au apokalipsi kwenye Mlima wa Mizeituni au karibu na mlima huo.”
Kitabu cha 1998 Britannica Book of the Year kina ripoti ya pekee juu ya “Madhehebu Zinazotabiri Uharibifu.” Kinataja baadhi ya madhehebu za kujiua, kama vile Heaven’s Gate, People’s Temple, na Order of the Solar Temple, na Aum Shinrikyo (Kweli Kuu), ambayo ilipanga mashambulizi hatari ya gesi yenye sumu katika gari-moshi la chini ya ardhi jijini Tokyo mwaka wa 1995, na kuua watu 12 na kuwajeruhi maelfu wengine. Akijumlisha ripoti hiyo, Martin E. Marty, profesa wa dini kwenye Chuo Kikuu cha Chicago, aliandika: “Inasisimua kufungua kalenda kwenye mwaka wa 2000—na yaelekea kutachochea unabii na harakati chungu nzima. Huenda harakati nyingine zitakuwa hatari. Ni lazima tukabili wakati huo tukiwa thabiti.”
Historia ya Kuogopa Apokalipsi
Apokalipsi, au Ufunuo, ni jina la kitabu cha mwisho katika Biblia, kilichoandikwa mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. Kwa sababu ya unabii wa kitabu hicho na lugha yake yenye mifano mingi, kivumishi “-a apokalipsi” kilianza kutumiwa kurejezea fasihi iliyoanza kuandikwa muda mrefu kabla ya kitabu cha Ufunuo. Mfano wa kihekaya wa fasihi hii warudi nyuma hadi wakati wa Uajemi ya kale na hata kupita wakati huo. Kwa hiyo, kitabu The Jewish Encyclopedia chataja “uvutano wa wazi wa Babiloni katika hekaya nyingi zilizoingizwa katika fasihi hii [ya apokalipsi ya Kiyahudi].”
Fasihi ya apokalipsi ya Kiyahudi ilienea sana tangu mwanzo wa karne ya pili K.W.K. hadi mwisho wa karne ya pili W.K. Akieleza sababu za kuwapo kwa maandishi haya, msomi mmoja wa Biblia aliandika: “Wayahudi waligawanya wakati wote katika mihula miwili. Kulikuwa na muhula huu wa sasa, ambao ni mbaya kabisa . . . Basi Wayahudi walingojea mwisho halisi wa mambo. Kuna muhula ambao ungekuja na ambao ungekuwa mzuri kabisa, ule muhula bora wa Mungu, wenye amani, ufanisi na uadilifu . . . Basi muhula huu wetu ungekuwaje ule muhula ambao ungekuja? Wayahudi waliamini kwamba wanadamu hawangeweza kuleta mabadiliko hayo, kwa hiyo, walitazamia Mungu aingilie mambo hayo. . . . Siku ya kuja kwa Mungu iliitwa Siku ya Bwana nayo ingekuwa wakati mbaya sana wenye kutisha na wenye uharibifu na wenye hukumu ambao ungekuwa dalili ya muhula mpya. Fasihi yote ya apokalipsi inazungumzia matukio haya.”
Je, Kweli Inafaa Kuogopa Apokalipsi?
Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chataja “vita ya siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote,” au Har–Magedoni, na katika vita hiyo waovu wataharibiwa, kisha kufuatwa na kipindi cha miaka elfu (ambayo nyakati nyingine huitwa Milenia) ambapo Shetani atafungwa ndani ya abiso na Kristo atahukumu wanadamu. (Ufunuo 16:14, 16; 20:1-4) Katika Enzi za Kati, wengine waliuelewa unabii huo vibaya kwa sababu “Mtakatifu” Augustine wa Katoliki (354-430 W.K.) alisema kwamba Milenia ilianza wakati Kristo alipozaliwa na ingefuatwa na Hukumu ya Mwisho. Yaonekana kwamba Augustine hakufikiria sana wakati uliohusika, lakini mwaka wa 1000 ulipokaribia, watu wakaanza kuwa na wasiwasi. Wanahistoria hawakubaliani juu ya jinsi ambavyo woga wa apokalipsi ulivyoenea katika enzi hizo za kati. Hata uwe ulienea kwa kadiri gani, kwa hakika watu hawakupaswa kuwa na woga.
Leo vilevile, kuna watu wa kidini na wale wasio wa kidini wanaoogopa kwamba kutakuwa na apokalipsi yenye kutisha sana mwaka wa 2000 au wa 2001. Lakini kweli tunapaswa kuogopa? Na je, ujumbe ulio katika kitabu cha Ufunuo, au Apokalipsi, unapasa kuogopewa au, badala yake, ujumbe huo unapasa kutumainiwa? Endelea kusoma tafadhali.
[Picha katika ukurasa wa 4]
Watu wa Enzi za Kati hawakupaswa kuogopa Apokalipsi
[Hisani]
© Cliché Bibliothèque Nationale de France, Paris
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Maya/Sipa Press