Ufunuo—Wakati Gani?
NI KAMA kusoma gazeti la karibuni zaidi—vita, matetemeko ya ardhi, magonjwa ya kipuku, maradhi mengineyo, njaa kubwa, uhalifu, na woga! Matukio hayo na mengine zaidi yametabiriwa katika Biblia. Yanaonyesha waziwazi kuwa nyakati ambamo sote tunaishi ndizo “siku za mwisho.” Hiyo inaamaanisha kipindi kinachoongoza kwenye ufunuo unaokaribia sana ambao uliahidiwa. Unaweza kuwaje na uhakika juu ya jambo hilo?
Wewe unashuhudia kutimizwa kwa unabii mbalimbali wa Biblia leo. “Ni lazima uukubali uhakika uliopo,” inasema Biblia, “kizazi cha mwisho cha ulimwengu huu kitakuwa wakati wa taabu-taabu. Watu hawatapenda kingine ila pesa na nafsi zao wenyewe; watakuwa wenye kichwa kikubwa, wenye majisifu, na wenye kutukana; wasio na heshima kwa wazazi, wasio na shukrani, wasio na kicho kwa Mungu, wasio na shauku ya upendo wa asili; watakuwa . . . watu wasiojulia wema wote,.. . wenye kuvimba kwa kujiona kuwa ndio wa maana. Watakuwa watu wanaoweka anasa katika mahali pa Mungu, watu wanaohifadhi namna ya nje-nje ya dini, lakini daima wakitenda kinyume chake.” (2 Timotheo 3:1-5, The New English Bible) Je, wewe huzioni hali hizo hizo kila upande?
Watu wengi walio hai leo, labda hata wewe, wanakumbuka nyakati ambazo hali hazikuwa mbaya kama zilivyo sasa. Watu walikuwa wakifikiriana zaidi. Watoto walikuwa wakiheshimu zaidi wazazi wao na watu wenye umri mkubwa. Wanaume, wanawake, na watoto hawakuogopa kutembea barabarani, hata usiku. Lakini nyakati zinabadilika kwa haraka sana. Hata kama baadhi ya hali hizo hazionekani kuwa zimeenea sana katika eneo lenu, hakika uwezekano wa vita ya nyukilia kutokea—kwa sababu ya mwanadamu mwenye kichwa kikubwa kung’ang’ania sana kuwa na mamlaka nyingi kuliko wengine, unatuhusu sisi sote.
Ndiyo, sawa na ambavyo Mungu kupitia Neno lake, Biblia, ametabiri waziwazi sana “kizazi cha mwisho cha ulimwengu huu,” ndivyo, pia, ametuandalia habari zinazohusu wakati wa ufunuo, wa Yesu kuja kufikiliza hukumu.
Ni Karibu Kuliko Vile Wengi Wanavyofikiri
“Sasa mimi natabiri mambo mapya,” Mungu anasema. “Kabla hayajatokea mimi nawaambia juu yayo.” (Isaya 42:9, The Jerusalem Bible) Ndiyo, yeye ametupangia katika Biblia matukio yale makubwa-makubwa yatakayotukia kabla tu ya ufunuo wenyewe.
Kwa mfano, Yesu alisema juu ya ujumbe utakaotangazwa ulimwenguni pote kisha akaukamatanisha na ufunuo. Alisema: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14, NW) “Mwisho” huo ni kutia ndani ufunuo. Leo, Mashahidi wa Yehova wanatumia mamia ya mamilioni ya saa kila mwaka wakitangaza kwa bidii ujumbe huo wa Ufalme mlango kwa mlango na kwa njia nyingine yo yote inayowezekana, katika nchi zaidi ya 200 duniani t pote!
Akitoa ulinganisho wa kuvuta fikira kwa faida ya wafuasi wake, Yesu alilinganisha wakati unaoelekeza kwenye ufunuo na wakati ulioitangulia Gharika ya siku za Noa. Wakati wa Noa watu walikuwa wakijishughulisha sana na kula na kunywa na kujifurahisha sana hata ‘wasiutambue’ ujumbe wa Noa kuhusu uharibifu uliokuwa karibu sana. Hawakujali maonyo yake.—Mathayo 24:37-39.
Siku zetu zinalingana sana na hali zilizokuwako kabla ya Gharika! Watu wanajishughulisha sana na kawaida zao za kila siku hivi kwamba wanakuwa hawatii maonyo na ushuhuda wa kwamba ufunuo unakaribia.
Hata hivyo, ufunuo uko karibu kuliko vile wengi wanavyofikiri. Kwa habari ya ishara ya siku za mwisho, Yesu alitangaza kwamba “kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” (Mathayo 24:34) Yesu alikuwa akisema juu ya kizazi kipi?
Kizazi cha 1914
Akimaanisha “kile kizazi cha utawala wa Viktoria chenye amani na ufanisi wa kadiri katika Uingereza,” aliyekuwa Waziri Mkuu Harold Macmillan alisema kwamba alifikiria ‘ulimwengu alimozaliwa’ kuwa “ungekuwa mzuri zaidi na zaidi.” Lakini “kwa ghafula, bila kutazamiwa, asubuhi moja mwaka 1914 mambo yote yakafikia kikomo.” Akiuita mwisho wa “miaka 100 ya amani na maendeleo,” Macmillan alikumbuka jinsi Vita ya ya Kwanza ilivyokuwa alama ya “mwisho wa kipindi” na “mwanzo wa mvurugo ambao bado unatukia.” Wengine wengi, hasa wale walioishi kupita mwaka 1914 walio hai bado, wanajua hiyo ni kweli.
Ndiyo, kama vile gazeti hili limevuta kwenye fikira za wasomaji walo muda wa miaka yote, ushuhuda unaonyesha kwamba kizazi cha 1914 ndicho kizazi kilichotajwa na Yesu.a Hivyo, “kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote [kutia na ufunuo] yatakapotimia.”
Ingawa miaka zaidi ya 70 imepita tangu 1914, kungali kuna watu mmoja mmoja walioishi wakakipita kipindi hicho. Kulingana na The American Legion Magazine la Desemba 1984, katika United States karibu watu 272,000 waliokuwako wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza wangali hai. Ni hali moja katika nchi nyinginezo. Hata hivyo, hesabu yao inapungua haraka sana. Kwa hiyo ni muda gani zaidi utakaoendelea kupita kabla mtu wa mwisho aliyekuwapo wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hajatokomea?
Ingawa huenda takwimu hiyo ikavuta fikira zetu kwenye saa za mwisho-mwisho za kizazi cha 1914, ni kwa kadiri gani tunaweza kutaja waziwazi wakati barabara wa kutokea kwa ufunuo?
“Mwivi Ajavyo Usiku”
Biblia inatangulia kuonya hivi: “Kwa habari ya nyakati na majira,. . . ninyi wenyewe mnajua yakini ya kuwa siku ya [Yehova] yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.” (1 Wathesalonike 5:1, 2) Je, ungekuwa na sababu ya kutazamia mwivi akupelekee telegramu kukutangazia wakati anapopanga kuvunja nyumba yako?
Basi kwa kufaa, Yesu anatushauri hivi kwa habari ya saa barabara: “Angalieni, kesheni, kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo.” (Marko 13:32-37) Hata hivyo, tumeona kwamba Yesu alieleza matukio mbalimbali yanayoelekeza waziwazi kwenye kizazi cha 1914. Na Biblia inaeleza matukio ya wakati ujao yatakayokuwa ishara ya ufunuo unaokaribia sana. Tunaweza kutazamia sana?
Badiliko la Matukio
Mtume Paulo alisema: “Wakati wo wote wanaposema: ‘Amani na usalama!’ ndipo uharibifu wa ghafula utakapokuwa juu yao papo kwa hapo sawasawa na utungu juu ya mwanamke mwenye mimba; nao hawataokoka kwa vyo vyote.” (1 Wathesalonike 5:3, NW) Kwa hiyo, tunaposonga mbele kuelekea kwenye mwisho kamili wa hizi “siku za mwisho,” tunaweza kutazamia fikira za pekee sana zielekezwe kwenye “Amani na usalama!” kwa utimizo wa maneno ya Paulo. Halafu iweje?
Unabii mbalimbali wa Biblia unaonyesha kwamba dini ya ulimwengu, inayoelezwa kuwa ‘Babeli Mkuu,’ itashambuliwa kwa ghafula na serikali za kisiasa za kidunia na kufikia mwisho wa ghafula sana! (Ufunuo 17:5, 16; 18:10, 17) Huo utakuwa ndio mwanzo wa “dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa.” (Mathayo 24:21) Lakini jambo hilo litakuwa na matokeo gani juu ya wale ambao ‘wamekesha’ na kulinda wauone ufunuo?
Wakristo wa kweli wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atawakomboa. (2 Petro 2:9) Ndiyo, maadamu wao wanajua Yehova Mungu na kumtumikia bila choyo, hawatakuwa na cha kuwaogopesha wakati Mungu na Kristo watakapojitokeza kupigana vita ya Har–Magedoni.—Ufunuo 11:17, 18; 16:14, 16.
Halafu, ufunuo utaongoza kwenye hatua ya kuwatenga wawe mbali na wanadamu Shetani Ibilisi na majeshi yake yasiyoonekana. (Ufunuo 20:2, 3) Ndiyo, ghadhabu inayokuja itachukua hatua inayozidi kuondolea dunia watu wasiotaka kutumikia Mungu. Hata roho waovu wanaoleta leo mavutano yao juu ya ulimwengu unaotuzunguka wataondolewa. (2 Wathesalonike 1:6-9) Hiyo itamaanisha baraka ya milele kwa waokokaji wa ufunuo.
Ufunuo—Utangulizi wa Paradiso
Kwa habari ya wakaaji wa dunia, kitabu cha Ufunuo kinatuambia kwamba Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao. Hakutakuwa tena na kifo wala maombolezo wala kilio wala maumivu, kwa maana utaratibu wa zamani wa mambo [utakuwa] umepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4, New International Version) Badala ya matokeo yenye kuleta majonzi baada ya ufunuo, Biblia inafunua kwamba mwanadamu atakuwa na uwezo wa kuishi milele katika paradiso duniani.—Zaburi 37:9-11, 29.
Ati paradiso? Ati uzima wa milele duniani? Ebu wazia, watu wa mataifa yote wenye afya na furaha kwa ukamili, wakifurahia maisha yaliyo ya kweli kweli! ‘Jambo hilo lingeweza kuwaje matokeo ya ufunuo?’ huenda ukauliza. Mungu ametoa ahadi yake. Itakuwa kama wakati aliposhughulika na Israeli, kwamba “halikuanguka neno lo lote katika jambo lo lote lililokuwa ni jema ambalo [Yehova] alikuwa amelinena . . . ; yalitimia mambo yote.”—Yoshua 21:45.
Kwa hiyo, kwa habari ya siku na saa barabara ya ufunuo hakuna mtu anayejua, lakini ushuhuda unaonyesha kwamba tunaishi katika kipindi cha ufunuo. Wakati utakapotokea kwa ghafula, na tupatikane tukiwa macho na ‘tukiwa tunalinda.’ Kwa maana “ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—Marko 13:33, 37; 1 Yohana 2:17; Mathayo 24:36, NW.
[Maelezo ya Chini]
a Ili kupata maelezo zaidi juu ya 1914, ona kitabu “Ufalme Wako Uje,” kilichochapishwa na Sosaiti yetu, sura ya 14.