Kujipanga Kitengenezo Sasa kwa Ajili ya Miaka Elfu Itakayokuja
“Watatawala wakiwa wafalme pamoja na yeye kwa miaka elfu.”—UFUNUO 20:6.
1. Hali ya mambo hapa duniani itakuwaje zaidi ya miaka elfu tokea sasa?
ETI! Je! tunamaanisha kwamba zaidi ya miaka elfu tokea sasa, aina ya binadamu watakuwa wangali hapa hapa duniani? Ndilo tunalomaanisha hasa! Isitoshe, aina yote ya binadamu watakuwa wakamilifu katika mwili, moyo, na akili—kama walivyokuwa mwanamume na mwanamke wa kwanza mwanzoni mwa kuwapo kwao wakiwa binadamu katika tufe hili. Ndiyo, miaka elfu tokea sasa, wanadamu watakuwa katika mfano na sura ya Mungu aliye Mponyi wao. (Mwanzo 1:2-30) Watakuwa wakishangilia maisha kikamili katika “shamba la Edeni,” paradiso ya raha, katika dunia iliyosafishwa ambayo haitakuwa imerundamana wanadamu wenye kuikaa. (Mwanzo 2:15) Yote haya yatakuwa kwa utimizo wa kusudi la awali la Muumba kuelekea dunia na wale ambao wangekaa juu yayo. Tendo hilo lenye kupendeza litamtetea kuwa mwaminifu kwa ahadi yake ya upendo ya kubariki aina ya binadamu ijapokuwa upinzani wote.
2. Watu wa karne 19 hivi zilizopita walipata maono gani kuhusu jinsi aina ya binadamu waliokamilika watakavyokuwa?
2 Tendo hilo lililobarikiwa litakamilisha Utawala wa Miaka Elfu ya Mungu kupitia Mwana wake aliyetukuzwa, aliyetumia miaka 33 1/2 duniani akiwa mwanadamu mkamilifu zaidi ya karne 19 zilizopita. Kwa habari ya sura aliyokuwa nayo wakati huo, tunasoma hivi: “Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.” (Yohana 1:14) Kwa kuona jinsi Yesu alivyokuwa, watu wa Israeli wakati huo walijua jinsi kiumbe mkamilifu wa kibinadamu alivyo. (Luka 3:23, 38) Ndiyo, karne 19 zilizopita watu fulani waliona jinsi aina ya kibinadamu iliyokamilika itakavyokuwa katika Paradiso ya kidunia inayokuja.
3, 4. (a) Utawala wa Yehova kupitia Yesu Kristo na wale 144,000 utakuwa wa urefu gani hasa? (b) Ni usemi gani unaotumiwa kwa kipindi hicho cha wakati, na hilo lilionyeshwaje katika vichwa vya vichapo fulani vya Mnara wa Mlinzi?
3 Urefu wa utawala wa Ufalme wa Yehova kupitia Yesu Kristo na wanafunzi wake 144,000 waliotukuzwa ulitabiriwa kuwa ungekuwa wa miaka elfu moja. Kuhusu Utawala huo wa Miaka Elfu, mtume Yohana mzee alisema hivi: “Na mimi niliona viti vya ufalme, na kulikuwa wale walioketi juu yavyo, na nguvu na kuhukumu zilipewa kwao. Ndiyo, mimi niliona nafsi za wale waliouawa kwa shoka kwa ajili ya ushahidi waliotoa kwa Yesu na kwa ajili ya kusema juu ya Mungu, na wale ambao hawakuwa wameabudu wala hayawani-mwitu wala mfano wake na ambao hawakuwa wamepokea alama juu ya kipaji cha uso wao na juu ya mkono wao. Na wao wakaja kwenye uhai na wakatawala wakiwa wafalme pamoja na Kristo kwa miaka elfu moja. (Mabaki ya wafu hayakuja kwenye uhai mpaka miaka elfu ilipokuwa imekwisha.) Huu ndio ufufuo wa kwanza. Mwenye furaha na mtakatifu ni yeyote aliye na sehemu katika ufufuo wa kwanza; juu ya hawa kifo cha pili hakina mamlaka. Lakini wao watakuwa makuhani wa Mungu na wa Kristo, na watatawala wakiwa wafalme pamoja na yeye kwa miaka elfu.”—Ufunuo 20:4-6. NW.
4 Kwa kuwa miaka elfu ni mileani, kipindi hicho kinaitwa Utawala wa Kristo wa Mileani. Wale wanaokubali na kufundisha fundisho hili la Biblia wakati fulani huitwa wamileani au wakiliasti, kulingana na neno la Kigiriki kwa “elfu.” Jambo la kupendeza ni kwamba, mabuku ya Studies in the Scriptures (ambayo yalitangazwa kwa chapa wakati mmoja na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti) hapo awali yaliitwa Millennial Dawn. Na kitabu cha nyimbo ambacho kilitumiwa wakati mmoja na Wanafunzi wa Kimataifa wa Biblia kilikuwa na kichwa Hymns of the Millenial Dawn.
5. Hali ya Shetani na roho wake waovu itakuwa nini wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo?
5 Ule usemi “miaka elfu moja” kwenye Ufunuo 20:4, NW si wa mfano bali unarejezea miaka elfu moja ya kalenda-jua. Wakati wa Mileani hiyo, Shetani Ibilisi na makundi yake ya roho waovu watakuwa katika abiso, kwa kuwa kabla tu ya kueleza juu ya Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, mtume Yohana alisema: “Na mimi nikaona malaika mmoja akija chini kutoka katika mbingu mwenye ufunguo wa abiso na mnyororo mkubwa katika mkono wake. Na yeye akakamata drakoni, nyoka wa awali kabisa, ambaye ndiye Ibilisi na Shetani, na akamboba yeye kwa miaka elfu moja. Na yeye alimvurumisha ndani ya abiso na akaifunga na akatia muhuri juu yake, ili asipate kuongoza vibaya mataifa tena mpaka miaka elfu ilipokuwa imekwisha. Baada ya vitu hivi ni lazima yeye aachwe legelege kwa kitambo kidogo.” —Ufunuo 20:1-3, NW.
6. (a) Ni tarehe gani ambayo baadhi ya Wakatoliki Waroma wametoa kuwa mwisho wa Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo? (b) Kama madai ya Wakatoliki yangekuwa ya kweli, tayari wakati kidogo huo wa kufunguliwa kwa Shetani kutoka lile shimo lisilo na mwisho umekuwa wa urefu gani?
6 Baadhi ya Wakatoliki Waroma wamedai kwamba Utawala wa Miaka Elfu wa Yesu Kristo ulimalizika katika 1799 wakati majeshi Wafaransa walipoteka Roma na wakamwondosha papa asiwe mtawala wao, hivi kwamba akasafirishwa kwenda Ufaransa akiwa mfungwa, ambako alifia. Makasisi Wakatoliki wamesema kwamba ndipo Shetani na roho waovu wake walipofunguliwa kutoka “lile shimo lisilo na mwisho,” au “abiso,” ili kufanya upya kazi yao ya udanganyifu kwa “wakati kidogo.” (Ufunuo 20:1-3, Douay Version ya Katoliki) Ikiwa hiyo ingekuwa kweli, ingemaanisha kwamba tayari “wakati kidogo” huo umeendelea kwa miaka 190, mwisho wao ukiwa hauonekani.
7. Biblia inaonyesha nini kuhusu wakati na hali ya Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo?
7 Hata hivyo, kulingana na Maandiko, Utawala wa kweli wa Mileani wa Yesu Kristo ungali mbele. Utimizo wa kisasa wa unabii wa Biblia unaonyesha umekaribia sana. Wakati wa Mileani ya kweli, Shetani na roho waovu wake watawekwa katika abiso kihalisi, na Yesu Kristo na warithi washiriki wake 144,000 watatawala juu ya aina yote ya wanadamu bila kuzuiwa na tengenezo la Ibilisi. Baraka ya milele ya aina yote ya wanadamu waliokombolewa, kwa kutimiza agano la Yehova pamoja na “rafiki” yake Abrahamu, itaanza na “umati mkubwa,” utakaookoka “dhiki” isiyo na ulinganisho ambayo mfumo huu mbovu unamalizika kwayo. Itaenea kwa mabilioni ya wanadamu wafu watakaokombolewa kwa “damu ya Mwana-Kondoo,” Yesu Kristo. (Yakobo 2:21-23; Ufunuo 7:1-17; Mwanzo 12:3; 22:15-18; Mathayo 24:21, 22, NW) Kwa kusudi hili, hawa watafufuliwa kutoka usingizi wao wa kifo katika makaburi ya ukumbusho ili wapate uhai duniani.—Yohana 5:28, 29.
Tengenezo la Kikristo
8. Kitabu The New Creation kilieleza juu ya tengenezo gani, lakini hakikutangulia kuona kazi gani ya kitengenezo?
8 Katika utimizo wa kusudi la kimungu, tengenezo jipya limetangulia mibaraka hiyo kwa karne nyingi. Kuhusu tengenezo hilo, tunasoma hivi: “Mtu akiwa ndani ya [katika umoja na, NW] Kristo amekuwa kiumbe kipya.” “Kutahiriwa si kitu, wala kutokutahiriwa, bali kiumbe kipya [uumbaji mpya, NW].” (2 Wakorintho 5:17; Wagalatia 6:15) Kule nyuma katika 1904, kitabu The New Creation kilielekeza fikira kwenye hili tengenezo jipya lililoanza kuwapo katika karne ya kwanza W.K. (Studies in the Scriptures, Mfululizo wa 6, Somo 5, lenye kichwa “Tengenezo la Uumbaji Mpya”) Kwa sababu ya maono yacho kuhusu kile ambacho mwisho wa Nyakati za Mataifa katika 1914 ungemaanisha, kitabu hicho hakikutangulia kuona kazi ya ajabu ya kitengenezo ambayo ilitazamiwa itendeke baada ya matokeo yenye kulemaza ya vita ya ulimwengu ya kwanza ya historia ya binadamu.—Luka 21:24, KJ.
9. Mabaki wa uumbaji mpya waliiamkia pindi ipi?
9 Ilistaajabisha sana wakati mabaki ya uumbaji mpya walipohifadhiwa mpaka mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza katika 1918 na kuendelezwa hai katika mnofu mpaka wakaingia mwaka wa 1919 baada ya vita. Lakini hali za mileani zilikuwa hazijaanza. Kwa uwazi, basi, kulikuwa na kazi nyingi zaidi ya kufanywa na mabaki wa uumbaji mpya kabla ya kutimiliza tumaini lao la kimbingu la kushiriki pamoja na Yesu kristo katika kazi ya mileani. Basi, uhitaji mkubwa ulikuwa kuwarudisha na kuwapanga upya mabaki. Kwa hiyo, wao waliiamkia pindi hiyo kwa imani isiyovunjwa-vunjwa na kwa hamu nyingi ya kazi iliyoko mbele.
10. Ni maswali gani yaliyotokea kuhusiana na mamilioni waliotazamiwa kuokoka na kuingia katika mfumo mpya wa mambo?
10 Kuokoka duniani kwa aina ya binadamu fulani kupita msiba mkuu wa mwisho wa mfumo huu mbovu na kuingia katika Utawala wa Mileani wa Yesu Kristo kulitazamiwa na mabaki wapakwa-mafuta. Hasa ilikuwa hivyo baada ya hotuba ya watu wote “Huenda Mamilioni Wanaoishi Sasa Wasife Kamwe” iliyotolewa katika Los Angeles, Kalifornia, katika mwaka wa vita wa 1918. Je! mamilioni haya ya waokokaji wa Har–Magedoni wakati ujao wangejipanga kitengenezo? (Ufunuo 16:14-16) Kabla ya kuingizwa katika Mileani ili wawe sehemu ya “dunia mpya,” je! wangejitia katika kazi ya kuhubiri Ufalme pamoja na mabaki? (2 Petro 3:13) Maswali haya yangejibiwa na matukio ya baada ya vita.
11. (a) Ni jambo gani ambalo lingepasa kufanywa na kondoo wengine ambao walitazamiwa kuwa kundi moja na mabaki? (b) Kwa nini kuwa na matumaini tofauti hakukuwa sababu ya kuwa na mgawanyo kati ya mabaki na kondoo wengine?
11 Maneno yanayofuata ya Mchungaji Mwema, Yesu Kristo, yalionekana wazi kwa wakati wake: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) Ikiwa mabaki wapakwa-mafuta walihitaji kujipanga kitengenezo kwa ajili ya kazi ya baada ya vita tangu 1919, na ikiwa baadaye kondoo wengine wangekuwa kundi moja pamoja na mabaki walio katika zizi hili, ingekuwaje halafu? Basi, hao kondoo wengine wangehitaji kujipanga kitengenezo pia pamoja na mabaki wale! Uhakika wa kwamba kondoo wengine walikuwa na tumaini tofauti—lile la uhai katika paradiso ya kidunia yenye raha—haikuwa sababu ya kuwa na mgawanyo kati yao na mabaki. Wote walikuwa wanafuata yule Mchungaji mmoja, na hakungekuwa na mtengano kati ya vikundi hivyo viwili mpaka kutukuzwa kwa mabaki wapakwa-mafuta katika Ufalme.
12. (a) Ni nini kilicho cha maana zaidi kuliko wokovu wa aina ya kibinadamu? (b) Ni lini na jinsi gani kuutangaza Ufalme kukawa kwenye umaana wa kwanza?
12 Wokovu wa wanadamu kutoka dhambi na kifo, mwisho wa utawala wa ulimwengu wa Shetani, na kurudishwa kwa aina ya binadamu tiifu kwenye Paradiso iliyosimamishwa upya duniani pote ni sehemu zenye kutokeza za kusudi la upendo la Yehova. Hata hivyo, kuna jambo lenye umaana mkubwa sana kwa ulimwengu wote mzima. Hilo ni nini? Ni kutetewa kwa enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ya Yehova Mungu pamoja na kutakaswa kwa jina lake takatifu. Kufaa kwa wakati wa kutangaza Ufalme wa Yehova kupitia Mfalme anayetawala, Yesu Kristo, kulikaziwa katika 1922 kwenye mkusanyiko wa pili wa Wanafunzi wa Biblia wa Kimataifa katika Cedar Point, Ohio. Kwa kuwa Nyakati za Mataifa zilikuwa zimekwisha katika 1914, ulikuwa wakati unaofaa wa kutekeleza maneno ya kiunabii ya Yesu: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakuja.” (Mathayo 24:14, NW) Ufalme ambao ungetetea enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ya Yehova na kutakasa jina lake takatifu ulikuwa umesimamishwa mbinguni katika 1914, na Yesu Kristo alikuwa akitawala katikati ya adui zake. Hizi zilikuwa habari njema za ajabu ambazo zingehubiriwa kwa njia zote zinazopatikana kwa kumtangaza Mfalme na Ufalme wake!
13. Kwa ajili ya kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme, Mungu aliandaa nini, na kwa nini?
13 Yehova ni mtengeneza mambo kwa kiwango cha ulimwengu wote mzima, kwa kuwa yeye ndiye Aliye Juu Zaidi, Aliye Mkuu Zaidi. Sasa yeye alihakikisha kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme wake katika mataifa yote ipangwe kitengenezo kabisa hapa duniani kabla mwisho haujaja. Basi, washiriki wanaobaki wa wapakwa-mafuta waliundwa kuwa tengenezo la kimataifa ili watimize penzi lake. Lazima hawa wapige mbiu katika ulimwengu kwamba kwa sababu ya Shetani kupinga enzi kuu ya ulimwengu wote mzima ya Yehova, uhakika na uhaki wa enzi kuu hiyo lazima utetewe, uthibitishwe kuwa haki, kwa wakati wote.
Kujipanga Kitengenezo Kabla ya Mileani
14. (a) Kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, ni tengenezo jipi lililokuja kuwa sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova la ulimwengu wote mzima? (b) Daudi alithibitikaje kuwa mtengeneza mambo mwenye kutokeza?
14 Kwa karne 15 kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, Yehova Mungu alikuwa na tengenezo lionekanalo duniani. Yeye alitumia mnabii Musa akiwa mpatanishi Wake katika kupanga taifa la Israeli kitengenezo baada ya kukombolewa kutoka Misri, milki ya ulimwengu ya kwanza katika historia ya Biblia. Chini ya Sheria aliyopewa Musa, Israeli ikawa sehemu ionekanayo ya tengenezo la ulimwengu mzima la Yehova. Mtengeneza mambo mwenye kutokeza miongoni mwa watu hawa wachaguliwa wa Mungu alikuwa mfalme-mchungaji Daudi, ambaye tunasoma hivi kwa habari yake: “Daudi akawapanga kitengenezo [wale Walawi waliotumikia katika patakatifu pa Yehova] katika migawanyo, baada ya Gershoni, Kohathi, na Merari, wana wa Lawi.” “Yeye aliwapanga kitengenezo [makuhani] kwa kupiga kura miongoni mwao, kwa kuwa kulikuwako maofisa watakatifu na maofisa wa Mungu katika nasaba ya Eliezari na katika ile ya Ithamari.” — 1 Nyakati 23:3, 6; 24:1, 5, The New English Bible.
15. (a) Waisraeli waliondoka Misri kwa njia gani? (b) Ni nani pia waliochagua kuondoka Misri, na je! walibaki na Waisraeli?
15 Mamia ya miaka kabla ya wakati wa Daudi, Waisraeli walipoondoka Misri, hawakutimka mbio kwa kusongamana ovyo ovyo bali waliondoka katika njia yenye utaratibu. Hili lilionyesha kazi nzuri ya kupanga mambo kitengenezo upande wa mpatanishi wao, Musa. Umati mkubwa wa wasio Waisraeli uliondoka pamoja nao, ukichagua kuwa sehemu ya watu wa Mungu mwenye kufanya miujiza, Yehova, aliyekuwa mwenye nguvu kuliko miungu yote ya Misri. Ijapokuwa magumu mengi, wakati fulani baadaye hili “kundi kubwa la watu waliochangamana” wenye nia njema kuelekea watu wachaguliwa wa Yehova lilikuwa lingali pamoja nao katika jangwa lenye kuogofya la Sinai. (Kutoka 12:37-51; Hesabu 11:4) Pamoja na Waisraeli, kwa wazi umati huo wa watu waliochangamana uliingia Bara Lililoahidiwa chini ya uongozi wa mwandamizi wa Musa, Yoshua, kwa maana Mungu alikuwa ameagiza rasmi uandalizi huo ufanywe huko kwa hao wakaaji wageni.
16. (a) Kundi la watu waliochangamana lilitangulia kufananisha nani? (b) Ni lazima hao wafanye nini ili waokoke mwisho wa mfumo huu wa mambo?
16 Kundi hilo la watu waliochangamana kutoka Misri ya Farao lilitangulia kufananisha mkutano mkubwa wa karne ya ishirini. Wao si Waisraeli wa kiroho lakini ni kondoo wengine wa Mchungaji Mwema, Yesu Kristo. Wao wanatazamia ukombozi kamili kutoka Misri ya mfano, mfumo wa mambo wa ulimwengu ambamo Farao Mkubwa Zaidi, Shetani Ibilisi, ni Mungu wao. (Yohana 10:16; 2 Wakorintho 4:4; Ufunuo 7:9) Lakini ni lazima wafanye nini ili waokoke uharibifu mkali sana wa ulimwengu wa kale wa Shetani na kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa chini ya Yoshua Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo? (2 Petro 3:13) Lazima waende kwa usambamba na mipango ya kitengenezo ya kiini hasa cha tengenezo lionekanalo la Yehova, mabaki wapakwa mafuta.
17. Katika ulimwengu huu usiopangwa kitengenezo, wale wa umati mkubwa wanatendaje, nao wanatazama mbele kwenye nini?
17 Hasa tangu katikati ya mwongo wa nne wa karne ya 20 umati mkubwa wa kondoo wengine umeingizwa ndani ya kundi moja lililopangwa kitengenezo chini ya Mchungaji aliyetukuzwa, Mfalme anayetawala, Yesu Kristo. Katika ulimwengu unaoendelea kuvurugika zaidi na zaidi ijapokuwa kuwapo kwa tengenezo la Umoja wa Mataifa, wale wa umati mkubwa wanaunga mkono mabaki wapakwa-mafuta kwa moyo wote na hivyo wanatoa ushuhuda wa uwezo wenye kuunganisha wa roho takatifu ya Yehova. Kwa kupiga moyo konde, wanaendelea kuwa wamepangwa kitengenezo pamoja na mabaki huku wakitazama mbele kwenye utumishi wa pekee duniani wakati wa Utawala wa Yesu Kristo wa Miaka Elfu.
Mawazo Yako Ni Nini?
◻ Maandiko yanaonyesha nini kuhusu wakati na hali ya Utawala wa Yesu Kristo wa Mileani?
◻ Ni nini la maana kuliko wokovu wa aina ya kibinadamu?
◻ Kabla ya Wakati wa Kawaida wetu, ni tengenezo jipi lililokuja kuwa sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova la ulimwengu wote mzima?
◻ Wale waliotangulia kufananisha kundi la watu waliochangamana wataokokaje waingie katika Utawala wa Miaka Elfu?