“Roho ya Uhai Itokayo kwa Mungu Ikawaingia”
(Funzo la Kitabu)
1. Kulingana na maneno ya Yesu katika Mathayo 28:18-20, ni utendaji gani wa pekee wa roho takatifu utakoma hivi karibuni?
UTENDAJI wa pekee wa roho takatifu ya Mungu umekuwa ukiendelea sasa kwa karne 19 nao utakoma hivi karibuni. Ukomapo, ndipo itakapokoma kazi ya kufanya wanafunzi wa Yesu, Masihi. Mwana wa Mungu aliyefufuliwa alitaja jambo hili, wakati alipowaambia mitume wake hivi alipokuwa juu ya mlima mmoja katika jimbo la Kirumi la Galilaya: “Mamlaka yote imepewa kwangu mimi mbinguni na duniani. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja na ninyi siku zote mpaka mwisho wa taratibu ya mambo.”—Mt. 28:18-20, NW.
2. Licha ya Yesu Kristo aliyetukuzwa, ni kitu gani kingine ambacho kingekuwa pamoja na wanafunzi wake mpaka “mwisho wa taratibu ya mambo”?
2 Mitume hao walikuwa wamefahamiana vyema sana na hiyo roho takatifu ambayo katika jina lake waliamriwa wakabatize wote wanaokuwa wanafunzi wa Kristo kutoka katika mataifa yote. Katika muda wa miaka walioshirikiana karibu karibu na Bwana wao Yesu, waliuona utendaji wake wenye nguvu kupitia kwake katika kuhubiri Ufalme, kufundisha na kufanya miujiza. (Matendo 10:38) Usiku wa Sikukuu ya Kupitwa ya mwisho kuwa pamoja nao Nisani 14, 33 W.K., aliwaambia hivi ili kuwafariji: ‘Nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiyo roho ya kweli; ambayo ulimwengu hauwezi kuipokea.’ (Yohana 14:16, 17) Kwa hiyo, si kwamba tu Yesu Kristo aliyefufuliwa na kutukuzwa angekuwa pamoja na wanafunzi wake mpaka “mwisho wa taratibu ya mambo,” bali pia msaidizi wao mtendaji, hiyo roho takatifu, ingekuwa pamoja nao mpaka wakati huo, kwa kuwa ingekuwa pamoja nao “milele.”
3, 4. (a) Sababu gani ulizo linaulizwa kama Yesu Kristo amekuwa pamoja na Jumuiya ya Wakristo siku zote mpaka sasa? (b) Yesu alisema ni jambo gani lingeonyesha kama roho takatifu ilikuwa pamoja na mtu anayedai kuwa Mkristo?
3 Hilo latupendeza sisi leo! Tupo hapa katika kipindi hicho kinachoitwa “mwisho wa taratibu ya mambo.” (Mt. 24:3, NW) Tangu Vita ya Kwanza ya Ulimwengu katika mwaka 1914 matukio katika ulimwengu na kati ya wanafunzi wa Kristo yanatimiza aliyotabiri Yesu katika unabii wake kama vile ulivyoandikwa katika Mathayo 24:3 mpaka 25:46. (Vilevile Marko 13:3-37; Luka 21:7-36) Yesu Kristo, akitumia “mamlaka yote” mbinguni na duniani, amekuwa pamoja na wanafunzi wake “siku zote” mpaka sasa. “Msaidizi” aliyeahidiwa, ile roho takatifu, imekuwa pamoja nao vilevile. Walakini siku hizi wengi wanadai kuwa wanafunzi wa Kristo au Wakristo. Kulingana na tarakimu za karibuni zinazopatikana, Jumuiya ya Wakristo ina wanakanisa zaidi ya 900,000,000. Hivyo, basi, tutazamie ushuhuda wa kwamba Yesu Kristo amekuwa pamoja na Jumuiya ya Wakristo? Je! roho takatifu imekuwa ikitenda juu yake?
4 Basi, kwa habari hii, ulizo hilo litajibiwa kulingana tu na idadi ya wale wanaodai kuwa Wakristo? Hapana, kwa kuwa Yesu alisema kwamba jambo la kuamulia ni matendo ya kimungu:
“Mtawatambua kwa matunda yao. . . . Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni. Ndiposa kwa matunda yao mtawatambua.
“Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.”—Mt. 7:16-21.
5. Je! leo Jumuiya ya Wakristo ina wingi wa “tunda la roho” au wa “matendo ya mwili”?
5 Tangu wakati Jumuiya ya Wakristo ilipoanzishwa katika kame ya nne W.K. na Mtawala Mrumi, Konstantino Mkuu mpagani asiyebatizwa bado, tunda lake halijapata kuwa zuri. Baada ya kupewa nafasi kwa karne 16 isitawishe “tunda la roho,” tengenezo lake la kidini halina wingi wa “upendo, furaha, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujiweza.” Badala yake, “matendo ya mwili” huitambulisha Jumuiya ya Wakristo.—Gal. 5:19-23, NW.
6, 7. Ni katika njia gani Jumuiya ya Wakristo inafanana na kundi katika Laodikia, na je! imetubu na kuchukua shauri ya Yesu kwa kundi hilo?
6 Jumuiya ya Wakristo inayosemekana kuwa na washiriki wengi wa kanisa, inafanana leo na ‘kundi lililokuwako Laodikia.’ Katika Ufu. 3:14-18, Yesu Kristo aliyetukuzwa aliambia hivi kundi hilo:
“Nayajua matendo yako, yakuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto. Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu. Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi. Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri; na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane; na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona.”
7 Je! Jumuiya ya Wakristo imetubu na kuchukua shauri hilo la Kristo? Kushiriki kwake katika vita viwili vya ulimwengu, mateso yake juu ya vikundi vilivyo vidogo vya kidini, ufuatiaji wake wa mambo ya kimwili, adili zake zilizopotoka, kujitia kwake katika siasa ili kuiongoza na kuiendeleza taratibu ya mambo ya kale iliyopo, haya yote na mambo mengine mengi hujibu Hapana!
8. Kwa sababu gani, ni kama kwamba Yesu aliyetukuzwa ana wajibu wa kuitapika Jumuiya ya Wakristo kutoka kinywani mwake asiitumie katika kazi leo?
8 Katika wakati huu wa “mwisho wa taratibu ya mambo,” Yesu Kristo hakupata kuwa na mwendo mwingine wa kuchukua ila ‘kuitapika’ kutoka kinywani mwake. Kwa habari ya kiroho, yeye si mwenye baridi yenye kuburudisha wala mwenye moto wenye kusisimua kwake. Yeye hawezi kummeza ili amfaidi. Ni mwenye “uvuguvugu” kwa kudai kuwa Mkristo huku akijifanya rafiki na chombo cha kutumiwa na ulimwengu huu. Mfalme anayetawala Yesu Kristo hawezi kuvumilia hayo. Yeye anamwona kuwa adui ya Mungu Baba yake. (Yak. 4:4) Yeye hana ushirika wo wote na adui za Baba yake. Yeye hayumo ndani ya paradiso ya kiroho pamoja naye. Kwa hiyo hawezi kumtumia katika ile kazi aliyotabiri ifanywe na wanafunzi wake wa kweli katika wakati huu.—Mt. 24:14.
9. Kwa sababu ya kuendesha utendaji wake katika jina la dini, Jumuiya ya Wakristo ilichukiwa na mataifa yote, au yenyewe ilielekeza chuki ya namna hiyo kwa akina nani?
9 Jumuiya ya Wakristo imefanya matendo yake na kuendesha utendaji wake katika jina la dini. Je! utendaji huu umeifanya ‘ichukiwe na mataifa yote kwa ajili ya jina langu [mimi Kristo]’? (Mt. 24:9) Kinyume chake, imeongoza katika kuwachukia wengine. Nani hao? Historia ya kisasa inaonyesha wao ni akina nani. Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu kulikuwako kikundi cha mataifa yote cha wanafunzi wa Biblia waliokuwa wakionyesha kutoka katika Maandiko yaliyoongozwa kwa roho kwamba “majira ya Mataifa” yalikoma katika mwaka ambao katika huo Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilitokea—1914. (Luka 21:24) Kwa hiyo mataifa yote, wale wanaodai kuwa Wakristo pamoja na wale wasiodai hivyo, wangeangamizwa kwa sababu ya kuupinga ufalme wa Yesu Kristo uliosimamishwa, Mfalme ambaye sasa atawala mbinguni akiwa katika mkono wa kuume wa Mungu. Wale wote ambao wangetamani kuokoka wasiharibiwe pamoja na Jumuiya ya Wakristo walihitaji kutoka katika Ukristo wa jina tu, watoke katika makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Mafundisho kama hayo ya ujasiri ya hawa wanafunzi wa Biblia wenye kuongozwa na dhamiri yaliwafanya wachukiwe ulimwenguni pote.
10. Wakati wa vita ya Kwanza ya Ulimwengu, Jumuiya ya Wakristo ilikusudia kuangamiza kikundi gani kidogo cha kidini, na kwa kutumia njia gani?
10 Washiriki wa kikundi hiki kidogo cha kidini chenye kuchukiwa walikuwa Wakristo waliojulikana kama Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote. Katika kujifunza kwao Biblia na katika kazi yao ya kutangaza walitumia vitabu na magazeti ya Watch Tower Bible and Tract Society, ambayo makao yake makuu yako Brooklyn, New York. Jumuiya ya Wakristo ilielekeza mateso yake kwa hawa wanafunzi wa Biblia wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Ilikusudia kuwaangamiza. Viongozi wake wa kidini waliwashtakia uongo wakatumia sehemu za kisiasa na za mahakma za ulimwengu huu ziwachukulie hatua za kuwazuia.
11. Ni sababu gani Watch Tower Bible and Tract Society ilihusika?
11 Yakafuata marufuku juu ya vitabu na magazeti ya Sosaiti. Katika nchi mbalimbali kazi ya wanafunzi wa Biblia ilikatazwa. Katika sehemu nyingine wananchi watukuzaji wa taifa walichochewa watokeze ghasia juu ya kikundi hiki kidogo chenye amani kilichosingiziwa. Katika masika ya mwaka 1918 wanaume wenye kujulikana walioshirikiana na makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn walipelekwa kifungoni kwa mashtaka ya uongo!
12. Ufunuo 11:7-12 unaonyeshaje kama Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imeua kabisa kazi ya kutoa ushuhuda?
12 Kwa kuwa sasa msimamizi pamoja na mwandishi-mweka hazina wa Sosaiti pamoja na wengine sita wa wafanya kazi wenzao wenye kujulikana walikuwa wakizuiliwa gerezani kana kwamba walikuwa wahalifu, Jumuiya ya Wakristo ilijisikia kwamba ilikuwa imeua tengenezo la mashahidi waaminifu wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo. Lakini je! walikuwa wamepata pigo la mauti? Kwa kitambo tu miili ya mashahidi hawa wa Ufalme ilionekana kana kwamba ilikuwa imekufa kabisa. Walakini je! utendaji wao ulikuwa umekomeshwa kabisa. Lugha ya mfano ya Ufunuo 11:7-12 inajibu hivi:
“Hata watakapomaliza ushuhuda wao, yule mnyama atokaye kuzimu atafanya vita nao, naye atawashinda na kuwaua. Na mizoga yao itakuwa katika njia ya mji ule mkuu, uitwao kwa jinsi ya [ki]roho Sodoma, na Misri, tena ni hapo Bwana wao aliposulibuwa. Na watu wa hao jamaa na kabila na lugha na taifa waitazama mizoga yao siku tatu u nusu, wala hawaiachi mizoga yao kuwekwa kaburini. Nao wakaao juu ya nchi wafurahi juu yao na kushangilia. Nao watapelekeana zawadi wao kwa wao, kwa kuwa manabii hao wawili waliwatesa wao wakaao juu ya nchi.
Na baada ya siku hizo tatu u nusu, roho ya uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao; na hofu kuu ikawaangukia watu waliotazama. Wakasikia sauti kuu kutoka mbinguni ikiwaambia, Pandeni hata huku. Wakapanda mbinguni katika wingu, adui zao wakiwatazama.”
13. Kwa maoni ya Jumuiya ya Wakristo, tengenezo la kutoa ushuhuda lilikuwa na wakati ujao wa namna gani, walakini ni nguvu gani ambayo haikuifikiria?
13 Kwa wakati mfupi, kama vile siku tatu u nusu, tengenezo la hawa watangazaji wa unabii wa Biblia tena walio mashahidi wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa walipatwa na aibu mbele ya watu wote. Watu waliokuwa wameteswa na kweli za Biblia zilizohubiriwa walifurahia kuzuiliwa kwa hawa mashahidi wa Ufalme. Kwa maoni ya Jumuiya ya Wakristo, tengenezo la mashahidi hawa lilikuwa ‘limekufa.’ Walakini je! roho ya Mungu ilikuwa imeuawa? Haikujionyesha kuwa imekufa wakati mwili wa Yesu Kristo aliyetundikwa mtini ulipokuwa ukilala kaburini kwa sehemu ya siku tatu. Kwa hiyo, karne 19 baadaye, haikujionyesha kuwa ‘imekufa’ baada ya tengenezo la mashahidi wa Ufalme lilipokuwa linalala hali limekufa kwa “hizo siku tatu u nusu,” kwa usemi wa kulinganisha.
14. Ili Mathayo 24:14 lipate kutimizwa, ni jambo gani lililohitajika, nalo ni jambo gani lililotukia katika masika ya mwaka 1919?
14 Sasa wakati ulikuwa umeendelea na kuingia katika mwaka wa tano wa “mwisho wa taratibu ya mambo.” Utabiri wa Yesu, katika Mathayo 24:14, NW, ulikuwa bado utatimizwa: “Na habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; ndipo ule mwisho utakapokuja.” Jumuiya ya Wakristo, ikiwa na madoa ya damu ya vita ya ulimwengu, haikuelekea au haikuwa safi vya kutosha kutimiza unabii huo. Hivyo, basi, kulikuwako jambo gani la kufanya? Roho ya Mungu Mwenye Nguvu Zote ilihitaji ianze kutenda. Nayo ilifanya hivyo, si kwa ajili ya Jumuiya ya Wakristo yenye hatia ya damu, bali kwa ajili ya mashahidi wa Ufalme walioonekana kana kwamba ‘wamekufa.’ Kulingana na ukweli wa mfano wa Ufunuo 11:11, “roho ya uhai itokayo kwa Mungu ikawaingia, wakasimama juu ya miguu yao.” Masika ya mwaka 1919 uliofuata baada ya vita ndio uliokuwa wakati wao wa kutiwa nguvu.
15. Ni akina nani walioanza kufanya kazi walipofunguliwa, nalo andiko la Mathayo 24:14 lilipataje kuangaliwa upya?
15 Jambo la kushangaza ni kwamba, karibu na mwisho wa Machi wa 1919, wajumbe wa Sosaiti pamoja na wafungwa wenzao walifunguliwa kwa dhamana wakaanza kufanya kazi. Unabii wa Yesu katika Mathayo 24:14 ulipata kufikiriwa upya. Maelezo yenye kushangaza juu yake yalitolewa katika toleo la Julai 1, 1920 la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza), kur. 199, 200. Yalionyesha waziwazi kwamba kuhubiri ulimwenguni pote kulikotabiriwa hakukuwa kuhubiriwa kwa ufalme unaokuja kulikofanywa karne 19 zilizopita za “Wakati wa Injili.” Kulikuwa kuhubiriwa kwa ufalme uliokwisha simamishwa. Hivyo, kuhubiri huko kulikuwa kazi ya kutangaza iliyokuwa ifanywe kuanzia mwaka 1914 W.K. na kuendelea.
16. Ufunuo huo ulikuwa na matokeo gani juu ya mashahidi hao, nao mwaka wa 1919 ulifikia upeo wake kwa tukio gani?
16 Ufunuo huu kupitia kwa ‘roho ya kweli’ ulitia nguvu mpya katika kazi ya kuhubiri Ufalme ya mashahidi hao. Na kama upeo mzuri sana wa mwaka 1919, mwaka waliotiwa nguvu mpya, kusanyiko la watu wote la kwanza baada ya vita la mashahidi hao wa Ufalme lilifanywa huko Cedar Point, Ohio, U.S.A. Maelfu kutoka United States na Canada walihudhuria. Msimamizi wa Sosaiti, ambaye alikuwa sasa ameondolewa mashtaka ya uongo ya wakati wa vita, alitangaza kazi mpya ya Ufalme iliyokuwa mbele. Alihutubia wasikilizaji wapatao 7,000.
17. Adui hao walikuwa na sababu gani ya kuogopa kwa kuinuliwa kwa mashahidi hao kutoka kwa hali iliyokuwa kama kifo?
17 Kwa sababu ya kuhuishwa kwenye kushangaza kwa hawa mashahidi wa ufalme wa Mungu uliosimamishwa, hofu kuu iliwaangukia adui za Ufalme, sana sana Jumuiya ya Wakristo. Ikiwa adui hao walikuwa na sababu ya kuwaogopa wakati huo, ijapokuwa mashahidi wa Ufalme walikuwa baki dogo tu, walikuwa na sababu kubwa zaidi ya kuogopa baadaye. Mashahidi hao wangepata kujulikana sana ulimwenguni pote kuliko vile wanafunzi wa Kristo walivyopata kujulikana katika wakati mwingine wo wote uliotangulia. Waliitwa ili wapate kujilikana sana hivyo kana kwamba kwa sauti kuu kutoka mbinguni, ikiwaambia: “Pandeni hata huku.”
18. Katika mwaka 1922 mashahidi hao walionyeshaje kwamba wao hawakusita kuingia kwenye kazi ambayo ingewafanya wajulikane ulimwenguni pote?
18 Wao hawakusita, wakakataa kuingia kwenye kazi ya kuutangaza Ufalme ambayo ingewainua juu sana wapate kujulikana na watu wote. Wakichochewa na roho ya Mungu yenye kutia nguvu, waliingia kwenye kazi hiyo pasipo woga. Shauku iliongezeka wakati wa kusanyiko la pili la watu wote lililofanywa huko Cedar Point, Ohio, U.S.A., katika mwaka 1922, wakati msimamizi wa Sosaiti alipofikia upeo wa hotuba yake ya utangulizi na kutoa mwito, “Mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake”! Maelfu ya wahudhuriaji walitoa mshindo kwa kushangilia katika kuitikia mwito huu wenye nguvu wa kuhubiri Ufalme mpaka mwisho!
WAKATI UFAAO WA KUSHUHUDIA UFALME ULIMWENGUNI POTE
19. Sababu gani ilifaa kwamba Yohana atoe habari iliyoko katika Ufunuo 11:15-18 baada tu ya kutoa habari kuhusu kuhuishwa kwa mashahidi hao?
19 “Roho ya uhai itokayo kwa Mungu” ilikuwa imewaingia katika mwaka 1919 W.K. mashahidi hao waliozuiliwa kwa kusudi hilo la kuhubiri Ufalme ulimwenguni pote. Kwa hiyo, kwa kufaa sana, mara tu baada ya mtume Yohana kutoa habari juu ya mashahidi hao wawili waliotukuzwa yeye anatoa habari hii inayofuata:
“Malaika wa saba akapiga baragumu, pakawa na sauti kuu katika mbingu, zikisema, Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki milele na milele.
Na wale wazee ishirini na wanne waketio mbele za Mungu katika viti vya enzi vyao wakaanguka kifulifuli, wakamsujudia Mungu wakisema, Tunakushukuru wewe, [Yehova] Mungu Mwenyezi, uliyeko na uliyekuwako, kwa sababu umeutwaa uwezo wako ulio mkuu,’ na kumiliki. Na mataifa walikasirika, hasira yako nayo ikaja, na wakati ukaja wa kuhukumiwa waliokufa, na wa kuwapa thawabu yao watumwa wako manabii na watakatifu, na hao walichao jina lako, wadogo kwa wakubwa, na wa kuwaharibu hao waiharibuo nchi.”—Ufu. 11:15 :18.
20. (a) Tangazo lililofanywa kwa sauti kuu lilikuwa habari kwa mbingu peke yake? (b) Kwa sababu ya utabiri wa Yesu, kulikuwa sasa na uhitaji wa nani?
20 Tangazo hilo lililofanywa kwa sauti kuu, “Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo wake, naye atamiliki milele na milele,” linastahili kurudiwa hapa duniani na mashahidi watiwa mafuta wa Yehova. Alichukuwa ufalme wake juu ya dunia mwishoni mwa Nyakati za Mataifa katika mwaka 1914. Hizi hazikuwa habari kwa mbingu peke yake. Zilihusu ulimwengu wa wanadamu. Walihitaji kuzisikia. Wangezisikiaje pasipo wahubiri, watangazaji? Yesu alitabiri kwamba zingehubiriwa ulimwenguni pote kabla ya mwisho wa taratibu hii ya mambo kufika. Mabaki ya wanafunzi wake watiwa mafuta ndio waliopewa mgawo wa kuanza kuhubiri huko kuanzia na wakati wa kuhuishwa kwao katika mwaka 1919 na kuendelea.—Mt. 24:14; Marko 13:10; Rum. 10:14, 15; angalia Isaya 32:15.
21. Sababu gani mabaki ya wanafunzi watiwa mafuta wa Kristo hawajitangulizi kwa kuhubiri Ufalme, kama vile inavyoweza kudai Jumuiya ya Wakristo, na ni sababu gani Zekaria 4:6 lazima litimizwe juu yao?
21 Mabaki ya wanafunzi watiwa mafuta wa Yesu Kristo ndio waliopewa mgawo na kutumwa wakafanye kazi hiyo ya kuhubiri. (Isa. 61:1-3) Ikiwa Jumuiya ya Wakristo inawashtaki kwamba wanajitanguliza kwa kufanya kazi hii ya kuhubiri Ufalme, basi sababu gani Jumuiya ya Wakristo yenyewe haifanyi kazi hii ya kuhubiri? Walakini haifanyi hivyo. Inashiriki katika siasa za ulimwengu huu na kubariki tengenezo la Umoja wa Mataifa lisilo la Kikristo. Kwa kuwa mabaki ni wachache sana wakilinganishwa na mamia ya mamilioni ya wanakanisa wa Jumuiya ya Wakristo, lazima andiko, la Zekaria 4:6, NW, kama alivyosema Yehova litimizwe juu ya mabaki ya watiwa mafuta: “Si kwa nguvu ya jeshi, wala kwa uwezo, bali kwa roho yangu.”
22. Tukiamua kulingana na kazi ya kuhubiri Ufalme inayofanywa, Yoeli 2:28, 29 limetimizwa juu ya nani?
22 Roho takatifu, ambayo Yehova alitabiri kwamba angeimimina katika siku za mwisho, haijaacha kutenda, kwa kuwa mabaki wangali wakibatiza wanafunzi wa Kristo kwa jina la roho hiyo. (Mt. 28:19, 20; Yoeli 2:28, 29; Matendo 2:14-21) Kusudi lililojulishwa lililomfanya Mungu amimine roho yake juu ya kila namna ya mwili lilikuwa kwamba wenye kuipokea wangetabiri. Mambo ya hakika yanathibitisha kwamba mabaki ya wanafunzi watiwa mafuta wa Kristo wamekuwa wakifanya kazi hiyo ya kutabiri katika mataifa yote kwa ushuhuda kuhusiana na ufalme wa Mungu. Basi, ni jambo linalopatana na akili kwamba, lazima wawe ndio waliomiminiwa roho hiyo ya Mungu. Roho hiyo ndiyo inayotegemeza kazi yao ya kuhubiri ulimwenguni pote. Sababu gani tubishanie hilo?
23. Wakati wa miaka 12 iliyofuata ya kutabiri huko, ushuhuda ulitolewa juu ya nani, na ni kwa sababu gani hilo lilihitajika?
23 Baada ya miaka 12 ya kazi hiyo ya kutabiri juu ya ufalme wa Mungu, mabaki ya watiwa mafuta walikuwa wamepata kumfahamu vizuri zaidi Yehova Mungu, Chanzo cha kimbinguni cha roho hiyo iliyomiminwa. Walikuwa wamezidisha kazi ya kumshuhudia na kila mahali walikuwa wametangaza kuwa jina lake ndilo Jina lililo kuu zaidi kuliko yote katika kuumba kote. Walikuwa wamejitoa kweli kweli wawe mashahidi Wake na kujihakikisha kuwa wao ndio waliokuwa “watu . . . kwa ajili ya jina lake.” (Isa. 43:10-12; Matendo 15:14) Na tusishushe umuhimu na kufaa kwa wakati wa kazi hii ya kumshuhudia Yehova pamoja na Masihi wake Yesu. Kupatana na unabii wa Yoeli 2:28-32 ilikuwa itangulie “siku ya [Yehova] iliyo kuu na itishayo.” Isipokuwa watu wawe wamepashwa habari, wasingeweza kumwitia mtu anayefaa kwa ajili ya wokovu wakati wa “siku” hiyo. Yoeli 2:32 linatupasha habari kwamba “mtu awaye yote atakayeliitia jina la [Yehova] ataponywa.” Ilikuwa lazima ushuhuda juu ya Yehova utolewe!
24. Katika mwaka 1931 mabaki hao watiwa mafuta walichukua jina gani jipya, na ni kwa sababu gani hili halikuwa tendo la vivi hivi tu?
24 Kwa hiyo halikuwa jambo lisilokusudiwa kwamba Jumapili, Julai 26, 1931, katika kusanyiko la mataifa yote la International Biblie Students Association huko Columbus, Ohio, U.S.A., wakusanyikaji elfu nyingi walikubali kwa moyo wote azimio la kwamba waitwe kwa jina lenye maana na la Kimaandiko. Jina walilochukua wakusanyikaji hao kwa kukubali Azimio hilo lilikuwa “Mashahidi wa Yehova.” Baada ya tendo lililochukuliwa katika kusanyiko hilo la mataifa yote huko Columbus, makundi ya International Bible Students Association kuuzunguka ulimwengu walikubali azimio kama hilo. Hivyo walijitangaza kuwa Mashahidi wa Yehova. Hili halikuwa tendo la vivi hivi tu kwa upande wa mabaki ya watiwa mafuta wa Waisraeli wa kiroho. Kwa kutimiza madaraka yanayowekwa juu yao na jina hilo, wameishi kulingana na hili jina lao jipya.
25. Mashahidi wa Ufalme waliotiwa nguvu upya walikwezwaje kwenye cheo chenye kutokeza sana kuhusiana na jina hilo la kimungu, na kwa kukubali wajibu wa Isaya 43:10-12?
25 Kwa hakika, “roho ya uhai itokayo kwa Mungu” ilikuwa imewaingia mabaki ya watiwa mafuta naye alikuwa amewaita wapate cheo chenye kutokeza mbele ya adui zao wote. Pasipo kuwaogopa adui hao, walikuwa wamekubali mwaliko wa Mungu, “Pandeni hata huku.” (Ufu. 11:11, 12) Wao hawakuona aibu ya kulichukua jina la kimungu, jina lililo takatifu zaidi. Kuhubiri na kutabiri kwao nyumba kwa nyumba na mji kwa mji kumelitukuza jina hilo kuuzunguka ulimwengu wote. Hatimaye kulikuwako na wateteaji wa kisasa wa jina lililo kuu zaidi katika ulimwengu wote! Ni jambo linalosikitisha kusema kwamba, taifa la kale la Israeli wa asili lilishindwa kuwa vile unabii wa Isaya 43:10-12 ulivyokuwa umesema, kwanza, kwao: “Ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], na mtumishi [wangu] niliyemchagua; . . . na hapakuwa mungu wa kigeni kati yenu; kwa sababu hiyo ninyi ni mashahidi wangu, asema [Yehova], nami ni Mungu.” Kwa hiyo mabaki ya kisasa ya Waisraeli wa kiroho wakubali kwa furaha wajibu wa kuwa Mashahidi wa Yehova.
26. Mabaki waliotiwa nguvu upya hawataki kurudia hali gani kama ilivyoonyeshwa na kundi katika Sardi, Asia Ndogo?
26 Kwa kuwa sasa mabaki ya Waisraeli wa kiroho wametiwa nguvu mpya kwa “roho ya uhai itokayo kwa Mungu,” wao hawataki kurudia hali kama ile iliyoonyeshwa na kundi lililokuwako Sardi wa kale, huko Asia Ndogo.—Ufu. 3:1-3.
27. Mabaki ya watiwa mafuta ya Waisraeli wa kiroho wanayatii maneno ya Yesu katika Ufunuo 2:5 ili wajilinde wasipoteze pendeleo gani?
27 Katika ulimwengu huu uliotiwa giza kidini mabaki ya watiwa mafuta ya Waisraeli wa kiroho wanataka kung’aa kama mianga, wakitoa nuru katika jina la Mungu na katika makusudi yake ya kuokoa wanadamu. Wao wanajilinda wasipoteze pendeleo la kuwa, wote pamoja, kinara cha taa cha kiroho. Wanayatii maneno ya Yesu Kristo aliyetukuzwa aliyoliambia kundi katika Efeso wa kale:
“Ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako, nami nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.”—Ufu. 2:5.
—Kutoka Holy Spirit—The Force Behind the Coming New Order, Sura ya 8.