Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 9/15 kur. 424-430
  • Kupatanishwa kwa Rehema ya Mungu Kabla ya Har–Magedoni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupatanishwa kwa Rehema ya Mungu Kabla ya Har–Magedoni
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UFANISI NA USALAMA WA KIROHO
  • AGANO LA MUNGU KWA HABARI YA WANYAMA
  • MAPOSO YA PILI JUU YA MSINGI WENYE KUDUMU
  • MFANO HALISI WA REHEMA YA MUNGU
  • Uaminifu kwa Agano la Ndoa Wamfanya Mungu Aonyeshe Rehema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Rehema ya Mungu Yaonyeshwa Wakati wa Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Utendaji wa Roho Iliyomwagwa Kutoka Juu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • “Roho ya Uhai Itokayo kwa Mungu Ikawaingia”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 9/15 kur. 424-430

Kupatanishwa kwa Rehema ya Mungu Kabla ya Har–​Magedoni

1. Matokeo ya kupatanishwa kwa Yehova na mabaki ya Waisraeli wa kiroho tangu mwaka wa 1919 W.K. yanaweza kufananishwaje?

WAKATI mke mpotovu aliyeachwa anapokubaliwa arudi na mumewe wa kisheria, yampasa mke awe na nia gani juu ya mumewe? Na wakati mumewe anapomwonyesha namna zote za upendo baada ya kumkubali arudi, mke amwoneje mumewe? Yampasa amheshimu sana kwa sababu ya fadhili zake zisizostahilika. Mke ana sababu ya kumkaribia mumewe zaidi kuliko hapo kwanza. Ana sababu ya kumheshimu mumewe zaidi kisha asichafue vifungo vya ndoa vilivyofanywa upya. Watu wa Yehova wa agano waliokuwa duniani kama mke walifanya vivyo hivyo kwa kupatanishwa Naye. Sasa tangu mwaka wa 1919 W.K. matokeo yamekuwa yale yale kwa habari ya mabaki yaliyopatanishwa ya Waisraeli wa kiroho.

2. Badiliko la kuita mumewe “Ishi” badala ya “Ba’ali” yangeonyesha nini kuhusu mke, na hilo likawaje kwa habari ya mabaki ya Waisraeli baada ya 537 K.W.K.?

2 Mke alipaswa kubadili nia nyakati za Biblia ndio aweze kumwita mwenzi wake wa ndoa “Mume wangu” badala ya “Mwenyeji wangu,” alipaswa kumthamini zaidi. Katika Kiebrania angemwita “Ishi” badala ya “Ba’ali.” (Hos. 2:18, Leeser) Nyakati za kale Sara alionyesha heshima kwa mzee wa ukoo Ibrahimu kwa kumwita “Bwana wangu,” au, katika Kiebrania A·do·niʹ. Alikuwa mke wake wa kisheria, naye alimheshimu Ibrahimu kama mumewe. Hakujiona kuwa mtumwa wake, mtumwa Hagari kijakazi wake Mmisri aliyenunuliwa, aliyelazimika kufukuzwa nyumbani kwa Ibrahimu. (Mwa. 18:12; 1 Pet 3:6) Kwa sababu Sara alishirikiana kwa uaminifu na mumewe mcha Mungu, Yehova alimthawabisha kwa mwujiza kwa kumpa mwanawe wa pekee akiwa na umri wa miaka 90. (Mwa. 21:1-7) Mabaki yaliyopatanishwa ya Waisraeli yalionyesha Yehova heshima kama ile aliyoonyeshwa Ibrahimu na Sara baada ya kuwakomboa Babeli mwaka wa 537 K.W.K. Mabaki yalijiona tena kuwa tengenezo halisi la Yehova lililo kama mke. Rehema yake iliongoza mabaki wakamwita Ishi, yaani, “Mume wangu.”

3, 4. (a) Tangu 1919 W.K., mabaki ya Israeli wa kiroho walithamini zaidi uhusiano gani, na ni agano gani walilokuwa wamelifahamu vibaya kwa muda mrefu? (b) The Watchtower lilichapa makala gani mwaka wa 1934?

3 Katika ulinganifu wa karne ya 20 wa jambo hilo, mabaki yenye kutubu ya Waisraeli wa kiroho walikombolewa na Babeli Mkuu mwaka wa 1919 W.K. Mpaka wakati huo, Waisraeli hao wa kiroho walikuwa wamempa Masihi Yesu na Bibi-arusi wake, kundi la Kikristo, heshima ya kupita kiasi. Lakini sasa walianza kumthamini Baba wa kimbinguni wa Masihi, Yehova Mungu. Uhusiano naye kama Mume wa Kimbinguni wa Israeli wa kiroho ulikuwa umesahauliwa, hasa tangu mwaka wa 1892 W.K. Agano jipya lake lilifahamiwa vibaya!

4 “Ni Nani Atakayemheshimu Yehova?” Hicho ndicho kilichokuwa kichwa cha makala kuu iliyochapwa katika toleo la Januari 1, 1926 la Watch Tower. Tangu wakati huo, waliendelea kupendezwa zaidi na Mungu wa Israeli wa kiroho. Mwaka wa 1934 ulifika na sehemu ya nakala za mfululizo ziitwazo “Maagano Yake” ikachapwa katika safu za The Watchtower. Wasomaji wa Watchtower walipelekewa sehemu nane za makala hiyo, tangu Aprili 1 mpaka Julai 15, 1934. Kwa kushangaza sana makala hizo zilikumbusha mabaki ya Israeli wa kiroho kwamba agano jipya la Yehova lililopatanishwa na Masihi Yesu liliwahusu wao.

5. (a) Baadaye mwaka wa 1934, ni kitabu gani kilichochapwa kikarudia habari za makala “Maagano Yake”? (b) Rehema ya Yehova iliongoza wenye kuipokea wamwite nani kuhusiana na tengenezo lake?

5 Muda mfupi baadaye, Novemba 15, 1934, kitabu kiitwacho “Jehovah” kilichapwa na Watch Tower Bible and Tract Society huko Brooklyn, New York. Sura zake kuanzia 4 mpaka 11 zilirudia makala “Maagano Yake,” iliyokuwa imechapwa mapema mwaka huo katika The Watchtower. Naam, mabaki ya Israeli wa kiroho walikuwa katika agano jipya na Yehova! Baada ya hapo uhusiano wa kiume wa Yehova na Israeli wa kiroho uliendelea kuangaliwa kidogo kidogo. Kwa kuitikia mambo yote ya rehema aliyowatendea Israeli wa kiroho waliokombolewa na kupatanishwa, tengenezo lililo kama mke lilimwita Ishi, “Mume wangu.” Tengenezo lake, si tengenezo la Shetani, ndilo lililokuwa tengenezo la pekee lenye kufaa walilopaswa kuwa mali yake. Ibada ya pekee ilikuwa ya Yehova akiwa ndiye Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote. Mabaki walitambua hivyo.

UFANISI NA USALAMA WA KIROHO

6. Kushikamana kwa mabaki na Yehova kama Mume wa Kimbinguni kulileta baraka gani, kama inavyoelezwa katika Hosea 2:17-20?

6 Ushikamano wa mabaki yaliyopatanishwa na Yehova Mume wa Kimbinguni ulileta baraka kuu. Maneno zaidi ya Yehova kupitia kwa nabii wake Hosea yalitabiri hili: “Kwa maana nitayaondoa majina ya Mabaali kinywani mwake, wala [Waisraeli waliorudishwa] hawatatajwa tena kwa majina yao. Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; nami nitavivunja upinde na upanga na silaha vitoke katika nchi, nami nitawalalisha salama salimini. Nami nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu; na kwa ufadhili, na kwa rehema. Nami nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua [Yehova].”​—⁠Hos. 2:17-20.

7. Kwa sababu gani mabaki waliorudishwa hawakutaka tena kumwita Mume wa Kimbinguni wa Israeli “Ba’ali,” nao hawakurudia kamwe ibada gani?

7 Kama mabaki yaliyorudishwa yangeendelea kumwita Yehova Ba’ali, yaani, “Mwenyeji wangu,” baada ya kurudi kutoka uhamishoni Babeli, wangeikumbuka dhambi yao wenyewe au ile ya babu zao ya kuabudu sanamu, Mabaali. Matendo ya Yehova kwa mabaki yenye kutubu yaliwafanya wachukie sana Mabaali, hivyo akaondoa majina ya Mabaali vinywani mwao. Hawakutaka tena kuwakumbuka kwa majina yao machafu. Kwa kufaa hawakutaka kumwita Mume wa Kimbinguni wa taifa la Israeli “Baali wangu,” au Ba’ali. (Hos. 2:16, New English Bible; Jerusalem; Leeser) Kwa kuendelea kumchukia Baali hivyo, hawakuabudu tena sanamu za kutengenezwa na wanadamu.

8. Mabaki Wayahudi waliomkubali Masihi walipingaje ibada ya Baali, na leo mabaki ya Israeli wa kiroho wanaepukaje kushiriki na Jumuiya ya Wakristo kumtolea Mungu hesabu?

8 Mabaki Wayahudi waliomkubali Yesu kama Masihi walipinga pia ibada ya sanamu za namna zote. Mabaki hao waliingizwa katika agano jipya lililopatanishwa na Yesu Kristo. Katika nyakati za kisasa, mabaki ya Waisraeli wa kiroho walipinga ibada ya sanamu yo yote, naye Yehova alimtumia Masihi Yesu kuwakomboa na Babeli Mkuu mwaka wa 1919 W.K. Wamejitahidi kumpa Yehova Mungu wao ibada ya pekee, hata wakafikia hatua ya kukataa kusalimu bendera ya taifa lo lote. (Kut. 20:1-6; 2 Kor. 6:15 mpaka 7:1) Hawataki kabisa kujichafua na cho chote kinachofanana na ibada ya Baali. Hawavumilii ushindani wa miungu-sanamu juu ya Yehova. Kwa njia hiyo wanaepuka kushiriki kutoa hesabu ambayo Yehova atataka Jumuiya ya Wakristo itoe. Yeye asema: “Nami nitamwadhibu kwa sababu ya siku za Mabaali, aliowafukizia uvumba; hapo alipojigamba kwa pete masikioni mwake, na kwa vito vyake vya thamani, na kufuatana na wapenzi wake, na kunisahau mimi.”​—⁠Hos. 2:13, vilevile mst. 8.

9. Mungu ataitendea Jumuiya ya Wakristo kama ufalme gani wa kale katika “dhiki kubwa,” lakini kulingana na Hosea 2:18, Yeye aahidi nini kwa mabaki wanaoharibu ibada ya Baali?

9 “Dhiki kubwa” yakaribia sana kuipata Jumuiya ya Wakristo, inayofananishwa leo na ufalme wa Israeli wa makabila kumi. (Mt. 24:21, 22) Mungu aitaka itoe hesabu naye ataitendea kama Israeli: ‘Nitaukomesha ufalme wa nyumba ya Israeli. Tena itakuwa siku ile, nitauvunja upinde wa pigano wa Israeli katika bonde la Yezreeli.’ (Hos. 1:4, 5) Haitapatanishwa kamwe na Mungu. Namna gani juu ya mabaki wenye kutubu wanaoharibu ibada ya Baali? Maneno ya Yehova katika Hosea 2:18 yawahusu: “Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; nami nitavivunja upinde na upanga na silaha vitoke katika nchi, nami nitawalalisha salama salimini.” Hiyo ni ahadi iliyoje ya usalama!

AGANO LA MUNGU KWA HABARI YA WANYAMA

10. Ni kwa njia gani Yehova ameuvunja upande wa pigano, upanga na vita vikatoka katika “nchi” ya Israeli wa kiroho tangu mwaka wa 1919 W.K., na vilevile katika karne ya kwanza?

10 Karibu karne nane zilizopita baada ya ahadi hiyo kutolewa, mabaki ya Israeli wa asili walimkubali Yesu kama Masihi. Waliiona ahadi hiyo ya kimungu ikitimizwa. Walikuwa wametolewa katika makabila kumi na mawili ya Israeli, kama vile Yuda, Benyamini, Lawi na Asheri. Hata hivyo haikutokea vita ya kikabila kati ya wanafunzi hao Waisraeli wa Yesu Kristo. Ndivyo imekuwa pia kwa mabaki ya Waisraeli wa kiroho ambao Yehova amekomboa na Babeli Mkuu tangu mwaka wa 1919 W.K. Ingawa mabaki hawa wa kisasa wametolewa kati ya watu wa mataifa yote, hakujawa kamwe na vita ya kitaifa kati yao katika ulimwengu huu upendao sana vita. (Mt. 28:19) Kwa kweli, Yehova amevunja “upinde na upanga” na vita akavitoa katika “nchi” yao au makao yao ya kiroho duniani. (Hos. 2:18) Wakiwa washiriki wa Israeli wa kiroho ambao Yehova ndiye Mume wao wa Kimbinguni, wanaendelea kuwa na amani kati yao wenyewe.​—⁠Marko 9:50.

11. Mungu amewezaje kuuvunja upinde, upanga na vita vikatoka katika makao ya kiroho duniani ya watu wa agano?

11 Hiyo imewezekanaje? Ni kwa sababu wamebadili nyutu zao zikawa kama utu wa Kiongozi wao Masihi, Mkuu wa Amani. (Isa. 9:6, 7) Kupitia kwa roho takatifu yake na Neno lake lililoandikwa, Yehova amebadili nyutu zao akaondoa maelekeo ya ukali na yenye madhara kama ya wanyama-mwitu wa dunia. (Rum. 12:1, 2) I Katika maana ya mfano Yehova ametimiza aliyosema kuhusu mabaki yake yaliyopatanishwa: “Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; . . . nami nitawalalisha salama salimini.” (Hos. 2:18) Tangu Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ya 1914-1918 W.K., ulimwengu kwa ujumla umekuwa wa kinyama zaidi na zaidi, umekuwa mbaya kuliko wanyama-mwitu. Lakini Yehova ameingiza mabaki wake waliopatanishwa katika paradiso ya kiroho yenye uhusiano wenye kukubaliwa naye. Ili mtu ye yote mwenye mashaka ajihakikishie hivyo, na afike kwenye Jumba la Ufalme la mashahidi wa Kikristo wa Yehova akaone roho ya Mungu ya amani iliyoko.

12. Makao ya kidunia ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo yatofautianaje na makao ya mabaki waliopatanishwa?

12 Makao ya kidunia ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, ambayo inajidai kuwamo katika uhusiano wa agano na Yehova Mungu, ni tofauti sana na paradiso hiyo ya ufanisi na usalama wa kiroho. Maneno yake yenye kuharibu ya Hosea 2:12 yanatimizwa juu ya jumuiya hiyo: “Nami nitaifanya kuwa msitu, na wanyama wa mashamba wataila.” Jumuiya ya Wakristo yenye uzinzi wa kiroho imekuwa kama msitu usio na usalama, usio na ulinzi wa hatari za kiroho wala wa mataifa ya kinyama yanayojidai kuwa ya Kikristo. Washiriki wake wa makanisa wanaachwa wawe mawindo ya hekima ya kilimwengu ambayo “ni ya dunia, ya tabia ya kibinadamu, na Shetani.” (Yak. 3:15) Wanaliwa kiroho. Yehova hakuipa Jumuiya ya Wakristo ahadi yo yote ya agano kuhusiana na wanyama-mwitu wala ndege. Hailalishi “salama salimini.”

MAPOSO YA PILI JUU YA MSINGI WENYE KUDUMU

13. Ni kwa habari ya sifa gani bora Yehova alisema angeposa tena tengenezo-“mke” wake?

13 Yehova, akiwa ndiye Mume wa Kimbinguni wa Israeli wa kiroho, ameonyesha rehema zisizo za kawaida kwa mabaki ya Waisraeli wa kiroho. Yeye anaendelea kuonyesha upendo thabiti na uaminifu kwa mabaki hao. Kwa roho bora hiyo, alimwambia kwa unabii tengenezo-“mke” wake anayewakilishwa na mabaki hivi: “Nami nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na kwa ufadhili [au, upendo thabiti], na kwa rehema [nyingi]. Nami nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua [Yehova].”​—⁠ Hos. 2:18, 20, na maelezo ya pembeni.

14. (a) Ni nini kinachoonyeshwa na uhakika wa kwamba Yehova asema, “Nami nitakuposa,” mara tatu? (b) Ni kwa njia gani ni rehema na haki pia, wala si kazi bure, kwa Yehova kufanya upya uhusiano wa ndoa?

14 Yehova asema mara tatu kwa mabaki wenye kutubu, “Nami nitakuposa.” Hiyo yakazia sana maneno yake. Yaonyesha upendo wake ni mwingi sana hata kumwongoza aonyeshe rehema za kimungu kwa njia ya kutokeza sana. Kufanya upya uhusiano wake wa agano la ndoa ni kwenye rehema na haki. Kwa njia gani? Ni kwa sababu afanya upya maposo juu ya msingi wa dhabihu ya upatanisho iliyotolewa na Masihi Yesu, dhabihu inayotimiza matakwa ya haki ya hukumu. (1 Yohana 1:7 mpaka 2:1) Kwa hiyo kurudishwa kwa mabaki ya Waisraeli wa kiroho katika uhusiano wenye kukubaliwa na Yehova kwahakikisha yeye ni mwaminifu na mwenye upendo thabiti. Vilevile, anapoposa mabaki kwa haki, fadhili za upendo, rehema na uaminifu, haiwi kazi bure. Wote walio thabiti wataitikia kwa uaminifu na kumtolea ibada ya pekee Mungu huyo mwenye rehema na uthabiti, mpaka wakati usiojulikana, milele! Hiyo yamaanisha wataendelea kufanya hivyo hata baada ya “dhiki kubwa” inayokuja itakayofikia upeo katika Har–​Magedoni.​—⁠Ufu. 16:14, 16.

15, 16. (a) Mabaki waliopatanishwa wanamjua Yehova kwa sababu gani? (b) Katika Hosea 2:21-23, Yehova asema nini kuonyesha Yeye ndiye Mpaji wa riziki yetu yote?

15 Yehova awaambia mabaki wenye kutubu ambao amewaposa hivi: “Nawe utamjua [Yehova].” (Hos. 2:20) Hiyo ilimaanisha wangemjua kwa sababu ya mambo aliyokusudia kufanya baada ya hapo, si kwa sababu ya kupatanishwa kwao naye kwa rehema tu. Mabaki walipofanywa wamjue kuliko wakati mwingine wo wote uliotangulia ufahamu wao juu yake uliongezeka wakamjua kuwa Chanzo cha baraka zote zinazowamiminikia nyakati zote. Kwa hiyo acheni tuone vile Yehova, akiwa ndiye Mpaji wa mahitaji yetu yote ya maisha, aongeza shairi hili la upendo na furaha:

16 “Tena itakuwa siku hiyo, mimi nitaitika, asema [Yehova], nitaziitikia mbingu, nazo zitaiitikia nchi; nayo nchi itaiitikia nafaka na divai na mafuta; nayo yataiitikia Yezreeli [maana yake, Mungu atapanda mbegu]. Nami nitapanda katika nchi kwa ajili yangu mwenyewe; nami nitamrehemu yeye asiyepewa rehema [Kiebrania: Loruhama]; nami nitawaambia wale wasiokuwa watu wangu [Kiebrania: Lo-ammi], Ninyi ndinyi watu wangu; nao watasema, Wewe ndiwe Mungu wangu.”​—⁠Hos. 2:21-23, na maelezo ya pembeni; The New English Bible; Jerusalem.

17. Mfululizo huu wa majibu au maitikio wafanyaje kazi, unaomtaja Yehova Muumba mwishowe?

17 Na tuangalie vile mfululizo huu wa majibu au maitikio unavyofanya kazi: Nyakati za kale, mabaki waliopatanishwa ambao Yehova alipanda kama mbegu katika nchi ya kwao, nchi ya Yuda, walihitaji nafaka, divai tamu na mafuta. Vitu vizuri hivi vya maisha vinatokana na nchi. Nafaka na divai tamu na mafuta viliiomba nchi iyape rutuba mashina ya nafaka na mizabibu yenye kuzaa zabibu na mizeituni yenye kutokeza mafuta, kwa ajili ya mabaki wenye shida. Nchi ilitegemea mbingu ipate mvua ili mimea yenye kukua isikauke. Kwa hiyo sasa nchi iliomba mbingu mvua ya wakati wake. Mbingu hazikukataa bali ziliitikia ombi la nchi. Lakini mbingu zina uwezo gani zikiwa peke yazo? Zinamtegemea Muumba azipe mawingu ya mvua ya kunyesha juu ya nchi. Yeye ndiye Mfanya mvua mkuu.​—⁠Yer. 10:12, 13.

18. Kwa hiyo ni jibu gani kuu linaloanza mfululizo wa matendo unaomalizika Yezreeli akipewa jibu?

18 Kwa hiyo, mwishowe, mbingu zilimwomba Yehova afanyize mawingu ya mvua na kuinyesha. Kwa ajili ya watu wake waliopatanishwa walio kama mke na waliokuwa sasa wamerudia nchi ya kwao, Yehova alizijibu mbingu. Mara moja mambo yote yalianza kutukia mfululizo kukawa na nafaka, divai tamu na mafuta kwa ajili ya watu Wake. Hivyo mazao hayo ya nchi yalimjibu Yezreeli, yaani, mabaki ambao Yehova alipanda katika nchi ya kwao.

19. Hivyo mabaki waliorudishwa walipata kumjuaje Yehova, hata wasisifu tena ibada ya Baali?

19 Kwa njia hiyo mabaki waliorudishwa wa Yehova walipata kujua kwamba kazi zote zenye faida katika mazingira yao ya asili zinawezeshwa na mpango Wake. Hazikuwezeshwa na Baali wa kuwazia wala Mabaali fulani wanaoabudiwa kila mwaka na waabudu sanamu wenye desturi za aibu na za kuchukiza sana. Kwa hiyo sasa mabaki, walioelimishwa na ujuzi sahihi, walimtolea Mungu wa kweli ibada ya pekee.

20. (a) Mabaki ya Israeli wa kiroho wanajua nani ndiye mwenye kuwapa paradiso yao ya kiroho? (b) “Mkutano mkubwa” wa wengine umeingiaje katika paradiso kiroho wakaifurahie na mabaki?

20 Namna gani sasa juu ya mabaki waliorudishwa wa Waisraeli wa kiroho leo? Wao pia wamepata kujua kwamba Mungu aliyewakomboa na Babeli Mkuu ndiye mwenye kuleta paradiso ya kiroho yenye wingi, amani na usalama ambamo amewaingiza tangu mwaka wa 1919 W.K. Mamia ya maelfu ya watu wenye kumcha Mungu wameitambua paradiso hii ya kiroho ya mabaki ya Waisraeli wa kiroho, kama vile maneno ya Ezekieli 36:35, 36 yalivyotabiri: “Nao watasema, Nchi hii, iliyokuwa ukiwa, imekuwa kama bustani ya [E]deni; . . . Ndipo mataifa, waliobaki karibu yenu pande zote, watajua ya kuwa mimi [Yehova], nimejenga mahali palipoharibika, nami nimepanda mbegu katika nchi iliyokuwa ukiwa.” Kwa hiyo “mkutano mkubwa” wa watazamaji wanyofu wameingia katika paradiso ya kiroho wafurahie wingi wake wa kiroho, amani na usalama pamoja na mabaki waliopatanishwa.

21. (a) Hivyo Yehova atangaza nani kuwa watu wake, na ni nani wanaojiunga nao kutangaza hadharani kwamba Yeye ndiye Mungu wao? (b) Yehova atimizaje maana ya jina Yezreeli hapa?

21 Katika njia hii yenye faida za kiroho Yehova aonyesha mabaki rehema waliokuwa wamenyimwa rehema yake walipokuwa wahamishwa katika Babeli Mkuu wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Kwa wale wasiokuwa watu Wake, sasa Yehova asema: “Ninyi ndinyi watu wangu.” Wakiitikia kwa moyo mabaki wanasema: “Wewe ndiwe Mungu wangu.” (Hos. 2:23) “Mkutano mkubwa” wa wenzi walio mfano wa kondoo ambao pia wanakaa sasa ndani ya paradiso ya kiroho wanajiunga na mabaki kutangaza hadharani kwamba Yehova ndiye Mungu wao. (Ufu. 7:9-17; Yohana 10:16) Wanafanya hivyo katika makao ya kidunia yaliyorudishwa ambamo Yehova amepanda mabaki ya Waisraeli wa kiroho kama mbegu, ili atimize maana ya jina Yezreeli, “Mungu atapanda mbegu.”

MFANO HALISI WA REHEMA YA MUNGU

22, 23. Kulingana na sura ya tatu ya Hosea, yeye aliagizwa afanye nini, na kwa kusudi gani?

22 Yehova afaulu kutatua tatizo la ndoa yake na watu wake wa agano kwa kuonyesha rehema akiwa na moyo mchangamfu. Ili aonyeshe hili waziwazi, Yehova alimwagiza nabii wake Hosea aonyeshe mfano halisi. Katika sura ya tatu ya unabii wake, Hosea atuambia hivi:

23 “[Yehova] akaniambia, Enenda tena, mpende mwanamke apendwaye na rafiki yake, naye ni mzinzi; kama vile [Yehova] awapendavyo wana wa Israeli, ingawa wanaigeukia miungu mingine, na kupenda mikate ya zabibu kavu [iliyohusika]. Basi nikajinunulia mwanamke huyo kwa vipande kumi na vitano vya fedha, na homeri moja ya shayiri, na nusu ya homeri ya shayiri; nami nikamwambia, Utatawa kwa ajili yangu siku nyingi; hutafanya mambo ya ukahaba, wala hutakuwa mke wa mtu awaye yote; nami nitakuwa hali iyo hiyo kwa ajili yako. Kwa maana wana wa Israeli watakaa siku nyingi bila mfalme, wala mtu mkuu, wala sadaka, wala nguzo, naivera, wala kinyago; baada ya hayo wana wa Israeli watarejea, na kumtafuta [Yehova], Mungu wao, na Daudi, mfalme wao; nao watamwendea [Yehova] na wema wake kwa kicho siku za mwisho.”​—⁠Hos. 3:1-5.

24. (a) Ndipo Hosea alipokomboa nani, kutoka kwa nani na kwa pesa ngapi? (b) Yehova alitimizaje mfano huu wa unabii mwaka wa 537 K.W.K. na mwaka wa 1919 W.K.?

24 Katika mfano wa unabii ambao Hosea aliweka kwa utii, alimfananisha Yehova. Hosea alimnunua Gomeri mkewe wa kisheria arudi kutoka kwa mwanamume asiyetajwa jina ambaye alikuwa amekuwa akiishi naye kwa uzinzi akiwa mtumwa wake. Ili amkomboe, Hosea alilipa kiasi kama shekeli 30 za fedha, ambayo ndiyo iliyokuwa bei ya mtumwa. (Kut. 21:32) Kwa kutimiza mfano huu, mwaka wa 537 K.W.K. Yehova aliwakomboa Waisraeli watumwa waliohamishwa wakapelekwa nchi ya Babeli. Alimpa mshindi wa Babeli, Koreshi Mkuu Mwajemi, bei ya ukombozi, kama inavyoonyeshwa katika Isaya 43:1-4. (Isa. 44:26 mpaka 45:4) Vivyo hivyo, mwaka wa 1919 W.K., Yehova akiwa Mume wa Kimbinguni alikomboa mabaki ya Israeli wa kiroho katika utumwa wa Babeli Mkuu na washirika wake wa siasa za kilimwengu. Kwa rehema Yehova alikomboa mabaki kwa kumtumia Koreshi Mkuu wake, yaani, Yesu Kristo, ambaye alimpa ‘mataifa kuwa urithi wake, na miisho ya dunia kuwa milki yake.’​—⁠Zab. 2:8, 9.

25. (a) Kama Ilivyofananishwa na Hosea, Yehova alitiaje adabu watu wake wa agano nyakati za kale? (b) “Daudi, mfalme wao” alitafutwaje, naye Yehova alionyesha rehema kwa watafutaji gani?

25 Baada ya Hosea kumrudisha kwa upendo mke wake Gomeri, alimtia adabu kwa kumwekea vizuizi vya kufanya ngono, na yaelekea yeye mwenyewe hakumtimizia mke huyu mambo fulani. Kwa hiyo, pia, Waisraeli wahamishwa walitiwa adabu, wasiruhusiwe kuwa na wafalme Waisraeli wala wakuu wa kifalme wala makuhani waabudu sanamu wala vitu vingine vingi vinavyohusiana na ibada ya sanamu. (Hos. 13:11) Kwa upendo, mwaka wa 537 K.W.K., Yehova aliwarudisha mabaki wake wenye kutubu na waliotiwa adabu, waliomrudia wakaacha kuasi imani ya kweli. Walianza kumtafuta na kumngojea Masihi wao atakayewakomboa na utawala wa Mataifa yasiyo ya Kiyahudi. Masihi huyo ndiye Mfalme ambaye angekuja katika ukoo wa kifalme wa Daudi. (Dan. 9:24-27) Alikuja, katika wakati wake Mungu. Mwaka wa 33 W.K. Yehova alimtukuza Masihi Yesu kama Mfalme mbinguni. Mabaki ya Waisraeli wenye kuamini walimfuata kama Mfalme wao wa Kimasihi wa mbinguni. (Kol. 1:13) Walipata rehema ya Yehova.​—⁠Rum. 9:24-26; 1 Pet. 2:9, 10.

26. Huko nyuma, ni nani akawa Lo-ruhama (Asiyehurumiwa)?

26 Taifa la Israeli lisiloamini likawa kama Lo-ruhama (Asiyehurumiwa). Yerusalemu usiotubu uliharibiwa na Warumi mwaka wa 70 W.K., na Wayahudi wenye kuokoka wakatawanywa ulimwenguni pote.​—⁠Mt. 24:15-22; Luka 21:20-24.

27. (a) Katika huu “wakati wa mwisho,” mabaki wamemjiaje Yehova wakiogopa sana, na, baada ya kumwona “Daudi, mfalme wao,” wamekuwa wakifanya nini? (b) Hiyo imefanya Yehova aonyeshe nani wengine rehema?

27 Sasa karne kumi na tisa zimepita. Tangu mwaka wa 1914 W.K. ulimwengu huu usio na rehema, kutia na Jumuiya ya Wakristo, umekuwa katika “wakati wa mwisho” wake. (Dan. 12:4) Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza mabaki wenye kutubu wa Waisraeli wa kweli wa kiroho waliokuwa ndani ya agano jipya walianza kumtafuta Yehova Mungu wao. Walimjia wakitetema, wakiogopa sana, wapate kuwa na uhusiano wa agano unaokubaliwa Naye. (Zab. 50:5) Walimwona “Daudi, mfalme wao,” yaani, Yesu Kristo ambaye sasa amekwisha tawazwa, naye atawala kama Mfalme mwenye mamlaka katika mbingu tangu mwisho wa Majira ya Mataifa mwaka wa 1914. Walianza kutimiza unabii wa wakati wake uliomo katika Mathayo 24:14 kwa shauku takatifu. Kwa hiyo, wamekuwa wakifanya nini tangu wakati huo? Hivi: Kuhubiri ‘habari njema hizi za ufalme’ duniani pote ‘kwa ushuhuda kwa mataifa yote’ kabla ya “dhiki kubwa” kutokea itakayofikia upeo wake katika Har–​Magedoni. Hii imefanya Mungu aonyeshe rehema yake kwa “mkutano mkubwa” wa watu wenye mfano wa kondoo ambao pia wanamtafuta Mungu wa kweli, Yehova, na Mfalme wake wa Kimasihi, Daudi Mkuu, hasa tangu mwaka wa 1935.

28. Rehema ya Yehova, ambayo tayari anawaonyesha mabaki na “mkutano mkubwa,” itang’aa kabisa kabisa wakati gani? Na kwa njia gani?

28 Mpaka sasa, rehema ya Yehova imekuwa nyingi na ajabu kuelekea mabaki wake waliopatanishwa pamoja na “mkutano mkubwa” wa raia za Masihi wenye mfano wa kondoo. Lakini rehema yake itang’aa kabisa kabisa wakati atakapoacha mabaki na “mkutano mkubwa” wapite hata Har–​Magedoni, ambayo ndiyo mwisho wa “dhiki kubwa” ya dunia nzima. Wakiwa vyombo vya rehema yake isiyolinganika itakayoonyeshwa mbele ya ulimwengu wote, atawaingiza katika Taratibu Mpya itakayofuata Har–​Magedoni! “Na ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba wa rehema, Mungu wa faraja yote.”​—2 Kor. 1:3.​—⁠Kutoka The Watchtower, Mar. 15, 1976.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki