Utendaji wa Roho Iliyomwagwa Kutoka Juu
1. Kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kwisha mwaka wa 1918, makao ya kiroho ya mabaki wa Israeli wa kiroho yalikuwa yametiwa katika hali gani?
KABLA Vita ya Ulimwengu ya Kwanza haijakwisha Novemba 11,1918, makao ya kiroho ya mabaki wenye kuteswa wa Waisraeli wa kiroho yakawa ukiwa. Kwa njia ya kiroho, yakawa kama jangwa, ambamo ‘matunda ya ufalme’ hayakuwa yakizaliwa kupitia kwa kazi ya mabaki watiwa mafuta ya kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme.” (Mt. 21:43; 24:14, NW) Mabaki ya mabalozi wa Ufalme wenye kuchukiwa na kuonewa na mataifa yote walipatwa na mashaka mioyo yao ikawa mizito.
2. Ni nini kilichoonyesha kama hali ya ukiwa ya mabaki ingeendelea kwa wakati usiojulikana, na ni nini kilicho-hitajiwa ili kuondoa hali hiyo?
2 Je! Yehova Mungu alikubali ukiwa huo uendelee milele kati ya watu wake waliokuwa wakf? Sivyo. Katika nyakati zilizotangulia Ukristo aliamuru kwamba Yerusalemu na nchi ya Yuda ikae ukiwa kwa muda mfupi, si zaidi ya miaka 70. Milki ya Babeli isingejitukuza milele juu ya mateka wake, Yerusalemu na Yuda. Vivyo hivyo, Mungu hakukusudia mateka wa Babeli Mkuu, yaani, mabaki ya Israeli wa kiroho, wakae katika hali ya ukiwa kwa wakati usiojulikana. Basi, je! ni nini kilichohitajiwa sasa kibadili hali hiyo ili kumtukuza Mungu wao, Yehova? Roho takatifu ilipaswa kufanya kazi juu yao kwa njia ya pekee!
3. Kulingana na Isaya 32:15 16, hali ya ukiwa ya watu wa Yehova ingeendelea mpaka nini kitukie?
3 Katika Isaya 32:15 Yehova alihakikishia watu wake kwamba ukiwa wao wenye kufanya waomboleze ungeendelea “hata roho itakapomwagwa juu yetu kutoka juu.” Halafu iweje? Unabii waendelea kusema, “Hata jangwa litakapokuwa shamba lizaalo sana; nalo shamba lizaalo sana litakapohesabiwa kuwa msitu. Ndipo hukumu itakaa katika jangwa, na haki itakaa katika shamba lizaalo sana.”—Isa. 32:15, 16.
4, 5. (a) Kwa hiyo, ni nini kingewapata mabaki wa Waisraeli wa kiroho? (b) Mabaki walihakikishiwaje hilo katika njozi aliyopewa Ezekieli ikionyesha bonde lililojaa mifupa mifu?
4 Kumbe basi mabaki ya Waisraeli wa kiroho walipaswa kumwagiwa roho, na kufunguliwa pia katika Babeli Mkuu. Walihakikishiwa hivyo na njozi ambayo Yehova alimpa nabii Ezekieli, wakati nabii huyo alipokuwa mhamishwa bado katika Babeli ya kale. Katika njozi aliona bonde lililokuwa limejaa mifupa iliyoachana ya Waisraeli wafu wasiohesabika.
5 Ilielekea kwamba Waisraeli wafu hao walioonekana katika njozi hawakuwa na tumaini. Vilevile Waisraeli waliokuwa hai uhamishoni katika Babeli ya kale, mamia mengi ya maili kutoka nchi yao iliyokuwa ukiwa, walielekea kutokuwa na tumaini. Hata hivyo hawakuwa bila tumaini kulingana na maoni ya Mungu Mwenye Nguvu Zote. Yeye ndiye Mungu awezaye hata kufufua wafu. Karne nyingi kabla ya hapo alitumia manabii wake Eliya na Elisha kufufua wafu kwa njia halisi, kwa roho takatifu. Kwa hiyo, katika njozi aliyompa Ezekieli, aliwaumba upya Waisraeli hao wafu akawafufua. Alipokuwa akieleza maana ya njozi hiyo, Yehova alisema hivi: “Nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi [Yehova], nitakapoyafunua makaburi yenu, na kuwatoa ninyi katika makaburi yenu katika nchi ya Babeli, enyi watu wangu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi, nami nitawawekeni katika nchi yenu, nanyi mtajua ya kuwa mimi, [Yehova], nimesema hayo, na kuyatimiza.”—Eze. 37:13, 14.
6. Ufufuo wa kiroho ulitokeaje, na mataifa walisema nini wakastaajabia waliyoona?
6 Kulingana na unabii huo, Babeli iliacha kuwa kaburi la taifa la Wayahudi. Walifufuliwa kiroho. Kama kwamba kwa mwujiza, mwaka wa 537 K.W.K. kundi la Waisraeli wahamishwa waliondoka Babeli pamoja na watumishi wao wakakaa katika nchi ya kwao. Walianza kujenga Yerusalemu upya na hekalu lake na kuifanya nchi yao iliyokuwa ukiwa muda mrefu iwe kama paradiso. Hawakuwa tena na sababu ya kujipiga-piga vifuani wakiomboleza “kwa ajili ya mashamba mazuri, kwa ajili ya mzabibu uliozaa sana,” ambayo yaliachwa yaharibike na Wababeli washindi mwaka wa 607 K.W.K. Roho takatifu ilionekana ikitenda kazi kweli kweli wakati huo! Mataifa ya upagani yalistaajabu! Zaburi 126:2 yaeleza waliyosema: “[Yehova] amewatendea mambo makuu.”
7. Maneno ya Zaburi 126:2 yalisemwa kuhusu nani katika karne yetu ya 20, na kwa sababu gani?
7 Ayo hayo yamesemwa katika karne yetu ya 20. Kuhusu nani? Si kuhusu Wayahudi wa asili waliokaa Palestina baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na baadaye wakafanya vita kwa kutumia “jeshi” ili waanzishe Jamhuri ya Israeli, mwaka wa 1948. Maneno ya unabii ya Zaburi 126:2 yalisemwa kuhusu Wanafunzi wa Biblia wenye kuchukiwa na kuteswa na mataifa yote ambao walikombolewa kutoka Babeli Mkuu mwaka uliofuata vita, 1919. Wakristo hao waliorudishwa katika hali inayofaa, waliokuwa Waisraeli wa kiroho, walimwagiwa roho kutoka juu. Hiyo iliwakumbusha Wanafunzi wa Biblia yaliyotukia siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., ingawa ‘ndimi zenye kuonekana kama za moto’ hazikuwakalia juu ya vichwa kwa mwujiza, kuwawezesha wanene lugha mbalimbali, wasizokuwa wamejifunza.—Matendo 2:1-4; Yoeli 2:28, 29; Isa. 32:15.
8. Mabaki wa Israeli wa kiroho waliokolewa wafanye kazi gani baada ya vita, na kwa sababu gani ilifaa wajipatie jina “Mashahidi wa Yehova”?
8 Kwa sababu hiyo, Wakristo hao waliotiwa nguvu kiroho wakawa wenye shauku zaidi katika utumishi wa Yehova. Sasa walijikaza kweli kweli waushuhudie Ufalme wa Mungu uliosimamishwa—ulimwenguni pote! Hilo sasa ndilo lililokuwa kusudi lao kuu maishani. Kulingana na Biblia, hiyo ndiyo sababu Mungu aliwaokoa na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na utumwa wa Babeli Mkuu. (Mt. 24:9-14) Kwa hiyo walikusanya tena wenzi wao waliotawanyika wakajitayarisha kuendesha kazi ya kuushuhudia Ufalme ulimwenguni pote, mpaka mwisho uje. Mwaka wa 1931 ulifika. Kufikia wakati huo walikuwa wameshuhudia jina la Yehova na ufalme wake wa Kimasihi duniani pote, kwa kutumia mamia ya mamilioni ya trakti za bure, makumi ya mamilioni ya vitabu vya kusaidia watu wajifunze Biblia, na kwa kutumia mamia ya vituo vya radio. Walifanya hayo yote bila “roho ya woga.” (2 Tim. 1:7) Kwa hiyo watiwa mafuta hao wenye kumtetea Yehova na ufalme wake unaosimamiwa na Kristo waliyakumbuka sana maneno ya Isaya 43:10 wakajipatia jina lenye kuungwa mkono na Biblia, “Mashahidi wa Yehova.”
9, 10. (a.) Ni nani wameshindwa kuondoa jina hilo duniani? (b) Ni nani zaidi ya mabaki wa Israeli wa kiroho wamekata shauri kwamba jina hilo litaendelea kuwako, na kwa hiyo wamefanya nini?
9 Mpaka leo hii makundi yote ya kidini ya Babeli Mkuu na wafuasi wake wa kisiasa, wa mahakmani na wa kijeshi wameshindwa kuondoa duniani jina hilo la watangazaji wa Ufalme wa Mungu. Liko tu! Wenye kulichukua wako tu!
10 “Mkutano mkubwa” wa watu wenye kumcha Mungu wamekata shauri duniani pote kwamba jina hilo litaendelea kuwako likiwa na maana, ingawa wao wenyewe si Waisraeli wa kiroho. Wameona vile Mungu aitwaye Yehova ametendea watu wachukuao jina lake, mabaki ya Israeli wa kiroho. Wameona kwamba roho ya Mungu imemwagwa juu yao. Kwa hiyo, wanaofanyiza “mkutano mkubwa” leo wamo “katika mataifa” yanayosema: “[Yehova] amewatendea mambo makuu.” (Zab. 126:2) “Mkutano mkubwa” wanataka kuabudu na kutumikia Mungu aliyeweza kufanya vile alivyofanyia mabaki wachache wa Waisraeli wa kiroho, Wamejiweka wakf kwa Mungu uyo huyo kupitia kwa Kristo, wakajipanga upande wa mabaki watiwa mafuta wa mashahidi Wakristo wa Yehova, bila kuogopa kuchukiwa na kuteswa na mataifa yote. Wao pia wamejitwalia daraka la kuwa Mashahidi Wake, bila kuona aibu.—Ufu. 7:9-17; Zek. 8:23.
KUJIKINGA NA “SEMI ZENYE KUONGOZWA NA MASHETANI”
11. Joka mnyama na nabii wa uongo wanakoroma wakisema nini, lakini mabaki na “mkutano mkubwa” wanatangazia watu nini?
11 Leo mabaki waliotiwa mafuta na “mkutano mkubwa” pia wanakabiliwa na “joka” wa kiibilisi, “mnyama” mwenye nguvu za atomiki na “nabii wa uongo” wa kisiasa. Ufunuo 12:17 waeleza wazi kwamba “joka,” Shetani Ibilisi, amekwenda akafanye vita na mabaki waliotiwa mafuta. Anafanya hivyo kwa kutumia “mnyama” wake wa kisiasa na “nabii wa uongo” aliye hapa duniani, ambaye ni Waingereza na Waamerika. Kwa hiyo semi zenye kuongozwa na mashetani zilizo kama vyura zitokazo vinywani mwao zasema watu waabudu Serikali, wafuate enzi kuu za mataifa, wafuatie mali za kimwili, na kutafuta amani na usalama wa ulimwengu kupitia kwa Umoja wa Mataifa. Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wametangaza habari njema za ufalme wa Mungu wa Kimasihi ulimwenguni pote. Ujumbe huo wa Ufalme umetangazwa katika zaidi ya nchi na visiwa vya bahari 200. Ni wazi kwamba yule joka, mnyama na nabii wa uongo wenye kukoroma kama chura wangependa kuzuia ujumbe wa Ufalme usisikike. Babeli Mkuu ya kidini, hasa Jumuiya ya Wakristo, ingependa kuuzuia, kwa maana Jumuiya hiyo inadai kwamba hakuna mwingine anayetetea Mungu, isipokuwa hiyo yenyewe.
12. Hivyo hali leo iko kama hali gani ya Mfalme Ahabu na manabii wake wa uongo na nabii wa Yehova Mikaya?
12 Hali iko kama ilivyokuwa kwa nabii wa Yehova, Mikaya, na manabii wa uongo wa Ahabu mfalme wa Israeli, karibu na mwaka wa 920 K.W.K. Manabii wa uongo hao walitabiri kwamba Mfalme Ahabu angeshinda vitani. Lakini Mikaya alitabiri kwamba angepatwa na mabaya. Alionyesha kwamba, Yehova alikuwa ameruhusu Mfalme Ahabu apumbazwe na usemi wa uongo wenye kuongozwa na roho katika vinywa vya manabii wake wa uongo ili akaangamie. Nabii wa uongo aliyeitwa Zedekia alipinga hilo. Kulingana na 1 Wafalme 22:24, alikaribia “akampiga Mikaya kofi la shavu, akasema, Roho ya [Yehova] [i]litokaje kwangu ili [i]seme na wewe?” Hata hivyo Yehova alikuwa amesema na Mikaya, kwa maana Mfalme Ahabu hakurudi akiwa hai alipokwenda vitani.—1 Fal. 22:20-38.
13. Ni kwa njia gani mabaki waliotiwa mafuta wa Israeli wa kiroho wakawa kama nabii Mikaya?
13 Kuna kisa cha kisasa kinacholingana na hicho, hasa tangu mwaka wa 1919, wakati ambao majeshi yaliyopigana katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yalipokubali kwa umoja Ushirika wa Mataifa uanzwe ili kulinda amani na usalama wa ulimwengu. Mabaki waliotiwa mafuta wa Waisraeli wa kiroho wamekuwa kama nabii Mikaya. Roho takatifu ilikuwa imekwisha mwagwa juu yao kutoka juu, wakaanza kutangaza unabii wa Biblia iliyoongozwa na Yehova, kama ilivyotabiriwa. (Yoeli 2:28, 29) Walitabiri kijasiri kulingana na unabii wa Biblia kwamba Ushirika wa Mataifa ungeshindwa. Vile-vile, walitangaza onyo kwa wafalme au watawala wa kisiasa wa Jumuiya ya Wakristo, wanaolingana na Mfalme Ahabu wa Waisraeli wenye kuasi imani.
14. Viongozi wa dini wamekataa ujumbe gani unaohusu watawala wa Jumuiya ya Wakristo, nao wametendaje kama Malkia Yezebeli?
14 Mabaki walitangaza kwamba watawala hao wenye kujidai kuwa ‘Wakristo’ watashindwa na kuharibiwa Mungu afikilizapo hukumu juu yao katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokuja katika Har–Magedoni. Itakuwa hivyo ijapokuwa viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo wamebariki serikali na majeshi ya watawala hao, kama Zedekia na kikundi chake cha manabii wa uongo. Viongozi hao wa dini wanajidai kwamba wao peke yao ndio wenye haki ya kumtetea Mungu na ndio wenye roho Yake peke yao. Kwa hiyo, wanaukataa ujumbe ambao mabaki waliotiwa mafuta wametangaza kuonyesha kwamba, watawala wa kisiasa na majeshi yao ambayo yameombewa baraka ya Mungu na viongozi hao, watapatwa na mabaya. Wamejaribu kuikomesha kazi ya kuhubiri inayofanywa na mabaki waliotiwa mafuta, kama kwamba haikuruhusiwa ifanywe na Mungu kupitia kwa roho yake. Wamefanya uchochezi mabaki waliotiwa mafuta wakateswa vikali, kama vile mke wa Ahabu, Malkia Yezebeli, alivyotesa Eliya na manabii wengine mia moja wa Yehova.—1 Fal. 18:13.
15. Viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo wataelezwa wazi wakati gani kama walikuwa na roho ya Mungu, na kwa sababu gani hawataona watawala wa Jumuiya hiyo wakipata ushindi?
15 Hivyo, viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo wamepiga mabaki waliotiwa mafuta kofi la uso wakawauliza: ‘Roho ya Yehova ilitokaje kwangu ili iseme na wewe” (1 Fal. 22:24) Karibuni viongozi wa dini wataonyeshwa wazi kama kweli wamepata kuwa na roho ya Yehova. Wao hawataona kamwe watawala wa Jumuiya ya Wakristo na majeshi yao wakishinda. Hata hawatakuwa hai wakati rafiki zao wa kisiasa na wa kijeshi watakapokuwa wakiharibiwa katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.” Kwa sababu gani? Kwa sababu, kabla vita hiyo haijaanza katika Har–Magedoni, wanasiasa hao wenye urafiki bado wanaoshirikiana sana na Umoja wa Mataifa, wataanza kuchukia viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo na wale wengine wa Babeli Mkuu nao watawaangamiza.—Ufu. 16:14, 16; 17:3-18.
16. Hata hivyo, mabaki walio kama Mikaya wataona nini?
16 Namna gani juu ya mabaki waliotiwa mafuta, ambao Yehova alimwagia roho yake kutoka juu? Wao hawakuuawa na pigo walilopigwa shavuni na viongozi wa dini wa Jumuiya ya Wakristo. Wataona ujumbe wa Biblia waliopewa na roho ya Mungu ukitimia. Naam, wataona uharibifu wa watawala wa ulimwengu wanaoelekezwa kwenye Har–Magedoni na porojo zilizo kama vyura zilizotolewa na joka, mnyama na nabii wa uongo.
“ROHO YA UTUKUFU, ROHO YA MUNGU”
17. Kwa sababu gani kushutumiwa (kulaumiwa) na kuteswa kwa mabaki na “mkutano mkubwa” katika huu “mwisho wa taratibu ya mambo” hakumaanishi kwamba hawana roho ya Mungu?
17 Mabaki waliotiwa mafuta wameteswa vikali pamoja na mashahidi wenzao “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wa Kristo walioko leo. (Yohana 10:16) Je! hiyo yamaanisha kwamba mashahidi wote hawa Wakristo wa Yehova hawana roho yake? Hapana! Kwa hakika huo ni ushuhuda unaoonyesha wanayo, kwa sababu Kristo alitabiri akasema hayo yangewapata katika “mwisho wa taratibu ya mambo.” Wanafunzi wake wa kweli wangechukiwa na mataifa yote na kuteswa kwa sababu ya kuushuhudia Ufalme wake wa Kimasihi. (Mt. 24:3, 9-14, NW) Hatupaswi kuona aibu ya kuchukiwa, kushutumiwa, na kuteswa kwa sababu ya kushikamana na jina la Kristo ambaye sasa ni Mfalme, kama kwamba tunafanya kosa.
18. Kulingana na 1 Petro 4:14, kwa sababu gani wale wanaoshutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo ni wenye furaha kweli kweli?
18 Mkristo Petro aliyefia imani karne ya kwanza aliandika hivi: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, m wenye furaha, kwa sababu roho ya utukufu, roho ya Mungu, inawakalia.” (1 Pet. 4:14, NW) Au, kama vile The New English Bible inavyosema: ‘Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, jihesabuni kuwa wenye furaha, kwa sababu wakati huo ile Roho tukufu ambayo ndiyo Roho ya Mungu inawakalia.’
19. Watu hutushutumu kwa ajili ya jina la Kristo wakiwa na kusudi gani, lakini Mungu atupa roho ya namna gani?
19 Watu wanaotushutumu kwa sababu tunatii amri ambazo Mungu ametupa kupitia kwa Kristo wanataka kutuaibisha mpaka tuache kumtumikia Mungu na kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme” kama ushuhuda ulimwenguni pote. Lakini Mungu hawapi wenye kuhubiri ufalme wake roho ya aibu wala ya kujiona kuwa wenye hatia kama kwamba wamefanya jambo baya. Roho anayowapa inatufanya tujione tumeheshimiwa, tukatukuzwa, nayo inahusiana na utukufu mwingi sana wa Mungu. Ni roho inayotuongoza “tufurahi katika dhiki pia; tukijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi; na kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini; na tumaini halitahayarishi; kwa maana pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na [roho takatifu tuliyopewa] sisi.”—Rum. 5:3-5.
20. Kupatana na Zaburi 69:9, je! tunashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo peke yake?
20 Sisi mashahidi Wakristo wa Yehova hatukupewa pendeleo la kushutumiwa kwa ajili ya “jina la Kristo” tu. Tumepewa pendeleo la kushutumiwa hasa kwa ajili ya jina la Yeye ambaye Yesu Kristo alishutumiwa kwa ajili yake. “Kristo naye hakujipendeza mwenyewe; bali kama ilivyoandikwa, Malaumu yao waliokulaumu wewe yalinipata mimi.” (Rum. 15:3) Maneno hayo yaliyotolewa katika Zaburi 69:9 yanaonyesha Yehova ndiye aliyeshutumiwa (aliyelaumiwa), naye Yesu Kristo alitia bidii nyingi sana atunze nyumba yake ya ibada.—Yohana 2:17.
21. Twaweza kusema roho inatukaliaje tunaposhutumiwa kwa ajili ya jina la Yehova?
21 Ni heshima kuu kushutumiwa kwa ajili ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. Lakini ni heshima zaidi sana kushutumiwa kwa ajili ya Yehova Mungu, Baba ya Yesu Kristo, kwa maana Baba ni mkubwa kuliko Mwana. (Yohana 14:28) Kwa kuwa “roho ya Mungu” inatukalia sisi tunaoshutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, bila shaka inatukalia hata zaidi tunaposhutumiwa kwa ajili ya jina la Baba na Mungu wake mwenyewe, Yehova. Tukiendeleza ukamilifu wetu kwa Mungu mpaka wenye kutushutumu watakapoharibiwa katika ‘dhiki kubwa’ inayokuja, “roho ya utukufu” ya Mungu haitatoka ndani yetu kamwe.—Ufu. 7:14-17; 1 Pet. 4:14.
“ROHO NA BIBI-ARUSI”
22. Kwa sababu gani porojo zilizo kama vyura zitokazo kwa “joka,” “mnyama” na “nabii wa uongo” hazituongozi pamoja na watawala wa ulimwengu, nasi tunalindwa tusiambukiwe na roho gani?
22 Twapaswa kutazamia kushutumiwa zaidi na “joka” wa kiibilisi na “mnyama” wa kisiasa na “nabii wa uongo,” ambaye ni Waingereza na Waamerika, kwa sababu hatufuatani na watawala wa kisiasa na majeshi yao kuelekea kwenye uwanja wa pigano wa Har–Magedoni. Porojo zao zilizo kama vyura na ukatili wao kwa mashahidi wa Yehova hazitatufanya kamwe tuabudu ye yote au cho chote kingine kama Mungu, wala hazitatufanya tuikane enzi kuu yake wala tuache kutafuta kwanza mambo yenye thamani nyingi ya ufalme wake wa Kimasihi. Sisi tunayo “roho ya utukufu, roho ya Mungu,” ya kuzuia ‘semi zote zenye kuongozwa’ na mashetani zinazoelekeza mataifa yote kwenye “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni. (Ufu. 16:13-16; 19:19-21) Sisi twasikiliza na kutii “semi zenye kuongozwa” zitokazo katika Neno takatifu la Mungu, Biblia. Tunapatanisha maisha zetu na semi hizo zenye kuongozwa. Kwa hiyo roho ya Yehova. ambayo iliongoza manabii waandike Biblia, ndiyo inayotenda kazi maishani mwetu. Inatulinda tusiambukiwe na “roho ya ulimwengu.”—1 Kor. 2:12, NW.
23. Sasa tunaonyesha heshima kwa kuacha sauti ya nani isikike kila mahali, nao mabaki wanaendelea kuwa mabikira safi kwa ajili ya nani?
23 Tunaonyesha heshima kwa kuacha sauti ya ‘roho na Bibi-arusi’ isikike duniani pote. Tunajua “Bibi-arusi” huyu ni nani. Yeye ndiye kundi la wanafunzi waliozaliwa kwa roho walioposwa na Bwana-arusi wa mbinguni, Yesu Kristo. Hapa duniani leo bibi-arusi huyo anawakilishwa na mabaki waliotiwa mafuta ambao karibuni wataungana na Kristo mbinguni. Kwa hiyo mabaki wa jamii ya “Bibi-arusi” hawashiriki kufanya uasherati ambao Babeli Mkuu anafanya sasa na watawala wa kisiasa wa dunia. Badala ya kujitia katika siasa na kuwa rafiki za ulimwengu, wale waliomo katika jamii ya “Bibi-arusi” wanaendelea kuwa mabikira safi kwa ajili ya Bwana-arusi wao wa mbinguni, Yesu Kristo, wanayemtangaza kila mahali kwamba atawala akiwa Mfalme katika mkono wa kuume wa Mungu mbinguni.—Ufu. 17:5, 18; 21:2-14; Yak. 4:4.
24. “Roho” inayotajwa katika Ufunuo 22:17 ni nini?
24 Ufunuo 22:17 wataja siku zetu hizi unaposema hivi: “Na [r]oho na Bibi-arusi wasema, Njoo! Naye asikiaye na aseme, Njoo! Naye mwenye kiu na aje; na yeye atakaye, na ayatwae maji ya uzima bure.” Hapa, ‘roho’ inayotajwa ni nguvu ya utendaji ya Yehova inayotoa sauti kupitia kwa semi zilizoongozwa katika unabii wa Biblia. Roho hiyo inafanya kazi ndani ya mabaki wa jamii ya “Bibi-arusi.”
25. Ni akina nani wameitikia ukaribishaji waliopewa na ‘roho na Bibi-arusi, nao wamemjia nani wapate “maji” yenye kumaliza kiu?
25 Je! kuna ye yote leo duniani anayesikiliza na kutii ukaribishaji unaotolewa na ‘roho na Bibi-arusi’? Ndiyo, hasa tangu mwaka wa 1935 W.K., wakati ambao mabaki wa jamii ya “Bibi-arusi” walijulishwa “mkutano mkubwa” wa Ufunuo 7:9-17 ni akina nani. Maelfu ya watu waliokuwa na kiu ya “maji ya uzima” yameuitikia ukaribishaji huo wa kimungu wakatoka katika Babeli Mkuu mwenye ukavu. Wameyaacha “mabirika” yaliyovunjika ya kilimwengu yasiyo na “maji” yawezayo kuendeleza uhai wa wanadamu wanaokufa. Kupitia kwa Yesu Kristo, Bwana-arusi wa mbinguni, wamemjia Yehova Mungu, aliye “chemchemi ya maji ya uzima,” “chemchemi ya uzima. “—Jer. 2:13; Zab. 36:9
26. Wale wanaokuwa washiriki wa “mkutano mkubwa” wanajiunga na mabaki wa jamii ya “Bibi-arusi” kufanya nini, na matokeo ni nini?
26 Wakati wanapoendelea kuburudishwa na “maji ya uzima.” washiriki wa “mkutano mkubwa” wanajiunga na mabaki waliotiwa mafuta wa jamii ya “Bibi-arusi” kukaribisha watu zaidi. Kwa njia hiyo “mkutano mkubwa” wa wenye kunywa maji unaongezeka. Yehova ameweka roho yake juu ya washiriki wa “mkutano mkubwa,” nao hawaoni aibu wanaposhutumiwa kwa ajili ya jina Lake na la Kristo. Hivyo habari njema zinaendelea kuhubiriwa zaidi na mabaki pamoja na “mkutano mkubwa,” kujulisha wanaume na wanawake watiifu kwamba Mungu amepanga wapate uzima katika makao ya paradiso hapa duniani chini ya ufalme wake wa Kimasihi. “Habari njema” hizo zitaendelea kuhubiriwa ulimwenguni pote mpaka mwisho utakapoijilia taratibu hii mbovu ya mambo inayoongozwa bado na “joka,” “mnyama” na “nabii wa uongo.”
27. (a) Ni nini peke yake tunachoweza kusema kimewezesha Ufalme uhubiriwe ulimwenguni pote mpaka sasa? (b) Tutapandia nini sasa tukitazamia uzima wa milele?
27 Mpaka sasa “habari njema hizi za ufalme” zimekuwa zikihubiriwa kimwujiza. Sababu imekuwa nini? Sababu ni kwamba roho takatifu imekuwa ikifanya kazi na bado yafanya kazi. Mungu ameifanyiza kazi iliyotabiriwa, yaani, kuzihubiri, habari njema za ufalme katika dunia yote ili kuyapa mataifa yote ushuhuda kabla hayajafikia mwisho wao. Wanadamu wala mashetani hawakuweza kuzuia roho Yake. Kwa sababu ya sheria yake isiyobadilika inayosema kwamba, “cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna,” na tuache kupandia mwili wetu mpotovu, tupandie roho takatifu ya Mungu. Tukiendelea kuipandia tangu sasa, katika wakati wake tutavuna kutokana na roho hiyo ya kimungu uzima wa milele katika taratibu mpya ya Mungu. (Gal. 6:7, 8) Shukrani zote na zimwendee Yehova Mungu kupitia kwa Yesu Kristo, kwa sababu katika wakati huu unaopaswa kutumiwa kwa haraka na wote wapendao haki na amani, roho Yake yafanya kazi kwa nguvu nyingi!
—Kutoka The Watchtower, Nov. 1, 1976.