“Wahudumu Wa Mungu Wetu” Na Wasaidizi Wao Leo
1. Utumishi wa watu wote ulio mkubwa zaidi unaofanyiwa wanadamu leo ni gani, na wale wanaoufanya wanaitwaje katika unabii?
KAZI YA MUNGU ya kutengeneza upya katika njia ya kiroho ndiyo utumishi mkubwa zaidi unaofanyiwa wanadamu wote leo. Wale anaotumia kama watumishi wake kwa wote si wanasiasa, bali ni wale wanaoitwa kwa unabii “wahudumu wa Mungu wetu.” (Isa. 61:6) Kiongozi wao ndiye Mtumishi wa Wote aliye mkubwa zaidi wa Yehova Mungu. Yeye alikuwa Yesu Kristo, ambaye, katika siku zake karne 19 zilizopita, alifanya kazi kubwa sana ya kuwatengeneza upya wanadamu maskini.
2. Ni kwa sababu gani Yesu na mitume hawakufanya kazi ya kutengeneza upya mazingira na nchi ya Palestina?
2 Huko nyuma huduma ya watu wote ya Yesu Kristo na mitume wake haikuyatengeneza upya mazingira ya nchi ya Palestina ambayo katika hiyo walihubiri bahari njema za ufalme wa Mungu. Ungekuwa ubatili kufanyia kazi jambo kama hilo, kwa sababu mtiwa mafuta Yesu aliwafundisha mitume wake kwamba “siku ya kisasi upande wa Yehova” ilikuwa inakuja juu ya Wayahudi, nayo ilikuja katika miaka ya 70-73 W.K. kupitia kwa majeshi ya Warumi, yaliyoiacha nchi ya Uyahudi katika hali ya ukiwa. Ngome ya Masada iliyokuwa pwani ya Bahari ya Chumvi ndiyo iliyokuwa ngome ya mwisho ya Wayahudi kuanguka mikononi mwa Warumi. Lakini namna gani juu ya kazi ya kutengeneza upya iliyoanzishwa na Yesu na kuendelezwa na mitume wake? Ilizidi kuendelea wakati huo wote wa magumu hata na baada ya hapo, mpaka ule “ukengeufu,” au uasi uliotabiriwa ulipoanza, baada ya mitume kufa.—2 The. 2:3.
3. Kulingana na Isaya 61:1-4, ni nani walio “miti mikubwa ya haki” ya mfano, na inawapasa wafanye kazi gani?
3 Katika unabii wa Isaya 61, kazi ya kutengeneza upya katika njia ya kiroho ililinganishwa na kutengeneza upya nchi iliyoachwa ukiwa kwa muda mrefu pamoja na miji yake iliyoharibiwa. Kwa hiyo, baada ya kueleza namna Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu angepata “uzuri” kwa kutokeza “miti mikubwa ya haki” katika paradiso ya kiroho, unabii wa Isaya unaendelea kusema hivi: “Nao watajenga mahali pa kale palipoharibiwa, watapainua mahali palipokuwa ukiwa zamani, watatengeneza miji iliyoharibiwa, mahali palipoachwa kizazi baada ya kizazi.” (Isa. 61:4) Wajenzi wanaosemwa habari zao hapa ni wale wanaotajwa katika mistari mitatu iliyotangulia wanaopokea faraja na kupewa uhuru wa kidini na kurudishwa katika kibali na “nia njema” ya Yehova. Ndio wanaopewa kazi ya kutengeneza upya.
4. Je! Yesu alitumia utimizo wa unabii wa Isaya 61:4 katika mkoa wa Uyahudi baada ya utumwa wa Babeli, nao utimizo wa unabii huo unaendelea kwa muda gani?
4 Mkoa wa Uyahudi na Yerusalemu ambao katika huo Yesu Kristo na mitume wake walifanya kazi nyingi sana ya kuhubiri ufalme wa Mungu, ulikuwa umekwisha tengenezwa upya kwa muda mrefu na mabaki Wayahudi waaminifu baada ya kufunguliwa kwao kutoka utumwa wa Babeli na kurudi katika nchi yao katika mwaka 537 K.W.K. Lakini je! Yesu aliyetiwa mafuta alitumia unabii huo wa Isaya 61:4 juu ya hayo yaliyokuwa yametimizwa wakati uliyopita katika nchi halisi ya Uyahudi? Hapana! Alipotumia maneno ya mstari wa kwanza na wa pili katika Isaya 61, katika sinagogi la Nazareti, alionyesha kwamba kutimizwa kwa sura hiyo kungeanzia naye, katika siku zake. Alionyesha kwamba utimizo wake ulikuwa na maana ya kiroho wala haukuhusu hali ya asili, ya halisi na mazingira ya watu. Kwa hiyo, kutimizwa kwa unabii huo kunaendelea mpaka karne hii ya 20, katika siku zetu.
5. Ni kwa sababu gani kulikuwa na uhitaji wa kazi ya kutengeneza upya kiroho kwa habari ya watu wa Yehova baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, nayo ilianza wakati gani?
5 Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ya 1914-1918 ilileta matokeo yenye kuharibu sana mabaki waliotiwa mafuta wa watumishi wa Yehova walio wakf na kubatizwa. Tengenezo lao la kidunia lililemazwa katika njia nyingi. Wakati vita hiyo ya kwanza yenye kuenea pote ilipokwisha, hesabu fulani ya Wakristo watiwa mafuta waliokuwa wakiongoza katika utumishi na ibada ya Yehova Mungu walijikuta bado wamo katika kifungo cha muda mrefu gerezani. Walakini katika mwaka 1919 walifunguliwa, si kutoka kifungo halisi tu, bali, la maana zaidi, kutoka katika Babeli Mkuu (kutia na Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani). Kazi ya kutengeneza upya ya namna ya kiroho ilianzishwa pasipo kupoteza wakati.
6. Kusanyiko la Cedar Point la 1919 lilijulisha ulimwengu uhakika gani, naye Yehova alisimamisha kitu gani kwa ajili ya mabaki ya watiwa mafuta wake?
6 Katika mwaka wa 1919 kusanyika la kwanza la International Bible Students Association katika Cedar Point, Ohio, U.S.A. lilikuwa la maana sana. Liliujulisha ulimwengu kwamba mabaki ya Wakristo wa kweli waliotiwa mafuta kwa roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu walikuwa hai tena, kana kwamba wametoka kwa wafu. Walikuwa wamerudishwa kwenye kibali yake na walikuwa wakitenda kazi tena waziwazi katika ‘kuhubiri habari njema hizi za Ufalme kuwa ushuhuda kwa mataifa yote’ kama ilivyotabiriwa katika Mathayo 24:14. Matokeo ya jitihada hizi za kupainia katika kazi ya kutengeneza upya katika njia ya kiroho zaonekana ulimwenguni pote hata mpaka wakati huu. Yehova Mungu amesimamisha paradiso ya kiroho kwa ajili ya mabaki yake waliotiwa mafuta kwa roho yake, kwa sifa yake.
NI NANI ANAYEWAWEKA “WAHUDUMU WA MUNGU WETU”?
7. Kulingana na Isaya 61:5-7, kazi hii ya kutengeneza upya ya mabaki ya watiwa mafuta ingevuta fikira za watu kadiri gani?
7 Ajabu kama inavyoweza kusikika, kazi ya mabaki ya watiwa mafuta wa Yehova ya kutengeneza upya katika njia ya kiroho ingevuta fikira za watu wa mataifa yote. Unabii wa Isaya ulitabiri jambo hili. Baada ya kumaliza kufikiria Isaya 61:4, tunaendelea kusoma hivi: “Na wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu. Bali ninyi mtaitwa makuhani wa [Yehova]; watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu; mtakula utajiri wa mataifa, na kujisifia utukufu [utajiri] wao. Badala ya aibu yenu mtapata maradufu, na badala ya fedheha wataifurahia sehemu yao [fungu lao]; basi katika nchi yao watamiliki maradufu; furaha yao itakuwa ya milele.”—Isa. 61:5-7.
8. Ni wakati gani na kwa njia gani mambo mabaya yaliyotabiriwa yalipokuja, na yalichochewa na nani?
8 Na tusikose kuangalia hili: Wale ambao kwao unabii huu wenye kutia moyo unatimizwa ni lazima kwanza wapatwe na aibu na fedheha, na wanyimwe “sehemu” yao na “fungu” lao. Wakati wa Vita ya Kwanza ya Ulimwengu mambo kama hayo yasiyopendeza na yasiyostahiliwa yaliwapata mabaki ya watiwa mafuta wa Yehova, hata kutoka kwa Jumuiya ya Wakristo wenye kutaka sana vita. Ndiyo, hata mpaka siku zetu hizi viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wanaendelea kuleta aibu na fedheha juu ya mabaki ya watiwa mafuta ya Waisraeli wa kiroho.
9. Ni wapi ambapo wakiwa humo mabaki ya watiwa mafuta hawatapatwa na aibu, fedheha au kukosa chakula cha kiroho, nao waliingia humo namna gani?
9 Walakini, hao Waisraeli wa kiroho sasa hawamo katika nchi ya Babeli Mkuu, wakiwa watumwa wa kidini na kufungwa gerezani humo. Katika masika ya mwaka wa 1919, wakati viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo hawakuwa tena na mataifa wenye kupenda vita ambao wangeweza kuwatumia kama watesi, Yehova aliwaweka huru mabaki wake waaminifu waliotiwa mafuta. Aliwarudisha katika kile ambacho unabii wa Isaya unaita “nchi yao.” Katika nchi hiyo yao waliyopewa na Mungu ndimo hawangepatwa tena na aibu, fedheha au kukosa chakula cha kiroho. Ingekuwa paradiso ya kiroho, ambamo wangepata “maradufu.”
10. Kwa habari ya namna mabaki ya watiwa mafuta wanavyoitwa na wapinzani wa kidini na wanavyoitwa na Yehova, ni jambo gani la maana kwa mabaki?
10 Bila shaka, viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo iliyoasi imani pamoja na wapenzi wake walimwengu bado wana njia zao za kuwaita mabaki waliorudishwa wakiwa tengenezo la kidini lililopo. Lakini unabii wa Isaya ulisema mabaki ya watiwa mafuta waliorudishwa wangeitwaje? Isaya 61:6 linaelekezwa kwa mabaki waliorudishwa likisema: “Bali ninyi mtaitwa makuhani wa [Yehova]; watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu; mtakula utajiri wa mataifa.” Vile Yehova anavyowaita mabaki wake watiwa mafuta ndilo jambo la maana kwao, wala si vile wapinzani wa kidini wanavyowaita.
11. Katika Israeli wa kale, ni nani waliotiwa ndani ya ukuhani, lakini unabii wa Isaya 61:6 unaohusu makuhani unaelekezwa kwa akina nani?
11 Unabii wa Isaya 61:6 haungetimizwa hata kidogo katika taifa la nabii Isaya na Yesu Kristo. Kwa sababu gani? Kwa sababu ni washiriki wanaume waliostahili wa jamaa ya Haruni, ndugu ya Musa peke yao, waliotiwa mafuta kuwa makuhani. Wengine wa kabila la Lawi walitumikia kama wasaidizi wa makuhani wa Kiharuni katika hekalu. Yale makabila mengine 12 ya Israeli walileta sadaka na matoleo yao kwa makuhani wa Kiharuni na pia walisaidiwa na Walawi waliofanya kazi katika hekalu. Je! hayo makabila 12 waliona kwamba walikuwa wamebaguliwa kwa sababu walikatazwa wasitumikie katika ukuhani au katika utumishi wa Kilawi. Hapana! Waliwatii wale waliokuwa wamewekwa na Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu. Kwa hiyo, chini ya torati ya Musa, Israeli halingekuwa taifa la makuhani hata kidogo, taifa ambalo washiriki wake wote walikuwa makuhani. Walakini, kwa habari ya wanafunzi waliotiwa mafuta wa Kristo, taifa lote la Kikristo la Israeli ambalo wao ndio washiriki wake linaambiwa hivi: “Ninyi mtaitwa makuhani wa [Yehova].”
12. Ni wangapi walio makuhani, katika Israeli wa kiroho, naye Kuhani Mkuu ni nani?
12 Washiriki wote wa Israeli hawa wa kiroho ni “makuhani” waliowekwa na Yehova. Yesu Kristo Painia (Mtangulizi) wao ndiye Kuhani Mkuu wa Yehova, ambaye chini yake taifa hili la “makuhani” latumikia Mungu.
13. Mitume Petro na Yohana walithibitishaje kwamba mpango huu wa Yehova uliwahusu wanafunzi watiwa mafuta wa Kuhani Mkuu Yesu Kristo?
13 Nabii Isaya aliongozwa na Mungu atabiri uhakika huu. Baadaye, mitume wa Yesu Kristo walioongozwa na Mungu walihakikisha kwamba mpango huu wa Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu ulitumika kwa wanafunzi watiwa mafuta wa Kuhani Mkuu wa kimbinguni Yesu Kristo. Kwa wanafunzi hao, mtume Petro anaandika hivi: “Ninyi nanyi, kama mawe yaliyo hai, mmejengwa mwe nyumba ya [kiroho], ukuhani mtakatifu, mtoe dhabihu za roho, zinazokubaliwa na Mungu, kwa njia ya Yesu Kristo. Bali nyinyi ni mzao mteule, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa milki ya Mungu, mpate kuzitangaza fadhili zake yeye aliyewaita mtoke gizani mkaingie katika nuru yake ya ajabu.” (1 Pet. 2:5, 9) Kuongezea hayo, mtume Yohana aliwaandikia wale waliopendwa na Yesu Kristo hivi: “Yeye atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme, na makuhani kwa Mungu, naye ni Baba yake; utukufu na ukuu una Yeye hata milele na Milele.”—Ufu. 1:5, 6.
14. Uhakika huu ulirudiwaje katika Ufunuo 5:9, 10?
14 Zaidi ya hayo Yohana anaandika juu ya heshima aliyopewa Mwana-Kondoo wa Mungu, Yesu Kristo mbinguni, ambayo inahusu ukuhani, katika maneno haya: “Ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa, ukawafanya makuhani kwa Mungu wetu.”—Ufu. 5:9, 10.
15. Chapa ya 1977 ya Encyclopedia Americana inasema nini kuhusu “Ukuhani wa waamini wote” kama ulivyofundishwa na Waprotestanti?
15 Katika Enzi za mwanzo-mwanzo za Waprotestanti walitumia maneno hayo kwa makundi yao ya kidini. Katika ukurasa 681 wa Kitabu cha 22 chenye kuonyesha haki ya uchapaji cha The Encyclopedia Americana cha 1977, chini ya kichwa kidogo “Ukuhani wa Waamini Wote,” chasema hivi:
“Fundisho kubwa la kidini la [Waprotestanti] lilikuwa ukuhani wa waamini wote. Wakiamini kwamba wokovu unapatikana bure kwa neema ya Mungu, inayokubaliwa kwa imani, [Waprotestanti] walitoa sababu kwamba hakukuwa na uhitaji wa viongozi wa kidini wenye kulipwa mishahara wa kupatanisha kupitia kwa mahubiri na sakramenti [ushirika]. Kila mwamini anaweza kutenda kama kuhani, akihubiri habari njema za wokovu, na mwenye kusikiliza anaweza kuitikia kwa imani. Zaidi ya hayo, kwa kuwa matendo mema ni kutumikia jirani, kila kazi inayoifaidi jamii inaonwa kuwa kazi ya Kikristo. Kile kinachojulikana kama ‘Kazi zenye matendo mema za Waprotestanti’ kilitokana na kuona kazi za kila siku kama jambo kubwa ambalo katika hilo twaweza kumtumikia Mungu.”
16. Katika kitabu chake alichowaandikia “Waungwana Wakristo wa Taifa la Kijeremani,” Martin Luther alisema nini kuhusu ukuhani wa ulimwenguni pote?
16 Katika Kitabu cha 17 chenye kuonyesha haki ya uchapaji cha The Encyclopedia Americana cha 1927, 1929, katika sehemu ya juu ya ukurasa wa 753, chini ya “Luther,” tunasoma hivi:
“Sasa [Martin] Luther aliandika vitabu viwili vinavyojulikana sana akieleza maoni yake: ‘To the Christian Nobility of the German Nation,’ na ‘Babylonian Captivity.’ Katika kile cha kwanza anatangaza ukuhani wa ulimwengu wote na kukataa ukuhani wo wote unaowekwa kwa kipekee. Pia anapinga haki ya Papa ya kufasiri Biblia, ambayo anatangaza kwamba ni ya watu wote.”
Kwa mfano, Martin Luther aliandika hivi katika kitabu chake ‘to the Nobility’: “Sisi sote tuliwekwa wakf kuwa makuhani [mapadre] wakati wa ubatizo wetu. . . . Kwamba Papa au askofu anatia mtu mafuta, kumtia taji, kumwekelea mikono, kumweka wakf, na kumvalisha mavazi tofauti na ya watu wa kawaida kunaweza kumfanya mnafiki au mjinga, walakini hakutamfanya Mkristo au mtu wa kiroho hata kidogo.”
17. Ni kwa sababu gani wakristo wa karne ya kwanza hawakujiita kwa jina la cheo la kuhani, namna gani Yesu Kristo mwenyewe alipokuwa hapa duniani?
17 Kama vile Wakristo wa nyakati za mitume, washiriki wa mabaki ya watiwa mafuta leo hawajichukulii wenyewe jina la cheo la kuhani. Kwa sababu gani wafanye hivyo? Je! wao wote si washiriki wa ukuhani ule mmoja wa kiroho na kwa hiyo hawapaswi kutofautishwa mmoja na mwenzake? Ndiyo! ukuhani mkuu wa Yesu Kristo ndilo jambo kubwa ambalo Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyoongozwa na Mungu yanaelekeza kwalo likiwa ndilo la kufikiriwa na mabaki ya wale waliotiwa mafuta kwa roho. (Ebr. 3:1-6) Hata Yesu Kristo mwenyewe, alipokuwa hapa duniani, hakujiita kuhani, hata ingawa wakati huo alikuwa akitumikia kama yeye aliyefananishwa na kuhani mkuu wa kwanza, Haruni ndugu ya Musa.
18. (a) Je! wanadamu wanawaweka makuhani, kama wanavyowaweka wazee, waangalizi na watumishi wa huduma? (b) Mabaki ya watiwa mafuta wamo katika mahali gani leo, katika hekalu la kiroho la Yehova nao wanafanya nini humo?
18 Ni kweli kwamba mitume kama vile Paulo na Barnaba waliweka wanaume waliostahili wawe wazee au waangalizi na watumishi wa huduma katika makundi ya Kikristo, walakini wao hawakuweka “makuhani” hata kidogo. (Matendo 14:23; Flp. 1:1) Yehova Ndiye anayeweka makuhani wake kupitia kwa Yesu Kristo. Hata ingawa hawajichukulii majina hayo ya vyeo, mabaki ya watiwa mafuta wa leo wamo katika kile kilichofananishwa na “ua wa makuhani” katika hekalu katika Yerusalemu. Katika ua huo wa mfano katika hekalu la kiroho la Yehova, wanamtolea “dhabihu za roho” kupitia kwa Yesu Kristo, Kuhani Mkuu.—1 Pet. 2:5.
19. (a) Washiriki wa Israeli wa kiroho wanasemekana kuwa nini pia katika Isaya 61:6? (b) Je! neno la Kiebrania lililotumiwa hapo linamaanisha zaidi ya kutumikia tu kama “mtumishi”?
19 Sasa tukirudi katika Isaya 61:6, tunaona kwamba andiko hili pia linawaambia washiriki wa Israeli wa kiroho hivi: “Watu watawaiteni wahudumu wa Mungu wetu.” Hapa katika maandishi ya Kiebrania neno linalotafsiriwa “wahudumu” ni m’sharethʹ (katika wingi), wala si obed, linalomaanisha “mtumishi,” kama ilivyo katika Isaya 65:13. Neno la Kiebrania m’sharethʹ pamoja na namna nyingine za sharath’ neno la kiarifa yanatumiwa mara nyingine kuhusiana na makuhani wa Israeli. Yoeli 2:17 linatumia usemi “makuhani, wahudumu wa [Yehova].” (Kut. 28:35, 43) Katika tafsiri ya kwanza ya Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya kigeni wafasiri waliokuwa wakisema Kigiriki walikubali tofauti iliyo kati ya maneno haya mawili ya, Kiebrania obed na m’sharethʹ, kwa hiyo katika kutafsiri kwao Isaya 61:6 katika tafsiri ya Kigiriki ya Septuagint Version wao walitumia neno la Kigiriki leitourgosʹ kwa neno m’sharethʹ.
20. (a) Maana ya msingi ya neno la Kigiriki leitourgos’ ni gani? (b) Kwa sababu gani limetumiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuhusu viumbe vya kibinadamu na kuhusu viumbe vya kimbinguni?
20 Kwa msingi, neno hilo linamaanisha, “anayefanyia watu wote kazi,” yaani, mkuu anayetumikia watu wote au mhudumu, kama vile hakimu. (Rum. 13:6) Linaweza kutumiwa kwa mtu anayetumikia katika cheo kitakatifu, kama wakati mtume Paulo anapojisema mwenyewe kama “mtutumishi kwa Kristo Yesu kwa watu wote kwa mataifa, nikifanya kazi takatifu ya habari njema za Mungu.” (Rum 15:16, NW) Yesu Kristo, kama Kuhani Mkuu wa Mungu, anaitwa “mhudumu wa patakatifu, na wa ile hema ya kweli.” (Ebr. 8:1, 2) Kwa habari ya mtu anayejulikana sana na watu wote kama vile Amnoni mwana wa Mfalme Daudi, mtu aliyemtumikia angeonwa kuwa mtumishi kwa watu wote. (2 Sam. 13:18) Malaika wa mbinguni wanaonwa kuwa watumishi kwa watu wote, kwa kuwa mtume Paulo anapotumia maneno kutoka Zaburi 104:4, anasema hivi: “Na kwa habari za malaika asema, Afanyaye malaika zake kuwa pepo, na watumishi [“kwa watu wote,” NW] wake kuwa miali ya moto.” (Ebr. 1:7) Pia, katika Waebrania 1:14, NW, Paulo anawataja malaika “wote [kuwa] roho kwa ajili ya utumishi kwa watu wote.”
21. Katika Zaburi 103, NW, majeshi ya kimbinguni ya Mungu yameitwaje?
21 Zaburi 103:21, NW, linaelekezwa kwa “majeshi” ya Yehova ya kimbinguni, na hapo wanaitwa “wahudumu wake.” Mambo yote yanapoangaliwa, neno hili “wahudumu” kama linavyoonekana katika Isaya 61:6 linamaanisha zaidi ya kuwa tu mtumishi au kutoa utumishi mtakatifu.
22. (a) Yesu Kristo alimtolea Mungu utumishi wa watu wote ulio mkuu zaidi kuliko ule uliotolewa na nani? (b) Katika Wafilipi 2:17, NW, Paulo aliutaja utendaji wa Kikristo kuwa nini?
22 Waebrania 10:11, NW, linasema kuhusu kila kuhani wa Israeli wa kale kama akisimama kila siku “na kutoa utumishi wa watu wote na kutoa dhabihu zile zile mara nyingi.” (Tazama pia Luka 1:23, NW) Kuhusu Mwana wa Mungu, ambaye ni mkuu kuliko malaika, Waebrania 8:6, NW linasema: “Sasa Yesu amepokea utumishi wa watu wote ulio bora zaidi, hivi kwamba pia kulingana na hayo yeye ni mpatanishi wa agano lililo bora zaidi.” Katika kundi la Antiokia, Shamu, manabii Wakristo fulani pamoja na waalimu, kutia na Paulo na Barnaba, walisemekana kuwa “wakihudumia Yehova hadharani.” (Matendo 13:1, 2, NW) Paulo, ambaye ndiye aliyeanzisha kundi la Filipi, Makedonia, anasema juu ya huduma yao ya kipekee hivi: “Mimi namwagwa kama toleo la kinywaji juu ya dhabihu na utumishi wa watu wote ambao katika huo imani imewaongoza.” (Flp. 2:17, NW) Kwa hiyo Wakristo hao wote waliotiwa mafuta walitenda kama watumishi wa Mungu kwa watu wote.—Isa. 61:6.
23. Toleo la Juni 1882 la Watch Tower lilivutaje fikira kwenye utumishi wa watu wote uliofanywa na washiriki wa mwili wa kiroho wa Kristo?
23 Vivyo hivyo leo, mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta wanamtolea Mungu “utumishi kwa watu wote” wakiwa jamii ya “mtumwa mwaminifu mwenye akili.” (Mt. 24:45-47) Kuwako kwa jamii kama hiyo ya watumishi wa Mungu kwa watu wote kulionyeshwa mapema katika toleo la kila mwezi la Juni 1882, ukurasa wa 7, fungu la 5, la Zion’s Watch Tower, chini ya kichwa cha habari “Waalimu Wanadamu ni wa Lazima.” Humo wachapaji walisema hivi:“. . . Na tunapoamini kwamba kila mshiriki wa mwili wa Kristo aliye wakf ni MHUDUMU katika maana fulani, na wote ‘wametiwa mafuta wahubiri habari njema,’ hata hivyo, kuna washiriki mbalimbali waliopewa kazi za namna mbalimbali, kama vile kulivyo na viungo na kazi mbalimbali katika mwili wa kibinadamu, ambao kulingana na Maandiko umetumiwa ufananishe mwili wa Kristo—Kanisa.” Kwa hiyo mabaki wote wa mwili wa kiroho wa Kristo waliotiwa mafuta kwa kufaa wanaonwa na kusemwa kuwa “wahudumu wa Mungu wetu.”—Isa. 61:6.
WAMEJULIKANA KATIKA MATAIFA YOTE
24, 25. “Wahudumu wa Mungu wetu” wanaweza kuibiwaje na kutendwa isivyo haki, lakini ni nani anayeahidi kusahihisha mambo wakati unaofaa ufikapo?
24 “Wahudumu wa Mungu wetu” wanapaswa kutimiza madaraka yao na kujiongoza wenyewe katika njia inayoheshimu msimamo wao mbele za Mungu. Kwa kawaida huenda watu wakawafahamu vibaya na huenda wakawaona kama wadhalimu na kuwaona na makosa. Huenda wakanyimwa sifa njema wanayostahili pamoja na kufikiriwa wanakostahili. (2 Kor. 6:8-10) Walakini Hakimu Mkuu Kuliko Wote ahukumuye wote atanyosha mambo wakati hali itakapolingana na kusudi lake kufanya hivyo. Yeye anataka haki ya hukumu. Katika Isaya 61:8, 9 anawaambia wale wanaotendwa vibaya hivi:
25 “Maana mimi, [Yehova], naipenda hukumu ya haki, nauchukia wivi na uovu; nami nitawalipa malipo katika kweli, nitaagana nao agano la milele. Na kizazi chao kitajulikana katika mataifa, na uzao wao katika kabila za watu, wote wawaonao watakiri ya kuwa wao ni kizazi kilichobarikiwa na [Yehova].”
26. Mabaki ya Israeli wa kiroho yalikuja kujulikanaje kati ya mataifa na jamaa, nao walikuja kujuaje “kizazi kilichobarikiwa na [Yehova]”?
26 Ili ‘wajulikane’ mabaki ya Waisraeli wa kiroho waliotiwa mafuta walipaswa kutoka kati ya mataifa na jamaa. Wakati wa vita ya Kwanza ya Ulimwengu, ndiyo, hata na wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu pia, ‘waliibiwa’ na mataifa yote. Kwa sababu ya kushtakiwa uongo na adui zao wa kidini pamoja na wasaidizi wao, waliteswa sana. Walinyimwa “malipo” ambayo walistahili kweli kweli kwa sababu ya jitihada zao na utendaji wao katika utumishi wa Yehova kwa watu wote. Walakini, kwa kuwafanya mashahidi wake na wahubiri wa habari njema za Ufalme, Yehova alionyesha wale aliowakubali. (Mt. 24:14; Isa. 43:10, 12) Aliwatia nguvu kwa roho yake takatifu watolee ulimwengu wote ushuhuda. Katika njia hiyo mataifa na jamaa walikuja kujua “kizazi kilichobarikiwa na [Yehova].”—Isa. 61:9.
27. Ni akina nani kati ya mataifa waliokubali msimamo wa mabaki nao walitaka kuishi na akina nani, wapi, wakimtumikia Mungu?
27 Jamaa na mataifa hawakuwakubali mabaki waliotiwa mafuta wa Yehova. Walakini watu mmoja mmoja walifanya hivyo. Wapendao haki ya hukumu, haki na kweli walijitokeza. Sana sana kuanzia na masika ya mwaka 1935 wao waliendelea kujiunga pamoja na mabaki waliotiwa mafuta kwa sababu walikuwa “wahudumu wa Mungu wetu.” Tangu wakati huo, hawa ambao si Waisraeli wa kiroho, “kizazi kilichobarikiwa na [Yehova],” wamekuwa “mkutano mkubwa.” Katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova lililofanywa mwaka wa 1935 huko Washington, D.C., ilijulishwa kwamba “mkutano” huu usio na hesabu wa wale wasiokuwa Waisraeli wa kiroho walilingana na mfano wa kinabii wa Ufunuo 7:9-17. Kwa sababu wao si Waisraeli wa kiroho, wao ni “wageni” na “watu wa kabila nyingine” kwa mabaki waliotiwa mafuta. (Isa. 61:5) Waliona kwamba hao mabaki walikuwa wakiishi katika paradiso ya kiroho, inayoonyeshwa na “miti mikubwa ya haki” wakiwa na makundi mfano wa miji. Wao pia walitaka kuwa katika paradiso hiyo ya kiroho, wamtumikie Mungu humo.—Tazama You May Survive Armageddon into God’s New World, kur. 296-299, mafu. 14-16; uku. 368, Na. 30.
28. Mabaki wa watiwa mafuta wanaona wakitimiziwa maneno ya Isaya 61:5 katika mwenendo gani wa “mkutano mkubwa”?
28 Wakiangalia kabisa mambo yote yanayohusika katika uamuzi na mwendo waliokuwa wakichukua, waliliacha tengenezo la ulimwengu lililochafuliwa na linaloharibika. Wakajiunga na tengenezo la Yehova lionekanalo. Bila shaka hawangeweza kumtumikia wakiwa kama Waisraeli wa kiroho, walakini walitamani kweli kweli kuwasaidia mabaki waliotiwa mafuta katika kutangaza habari njema za ufalme wa Yehova kupitia kwa Kristo. Kwa hiyo walibatizwa wakawa wafuasi walio wakf wa Yesu Kristo. Wakaanza kutumikia pamoja na Waisraeli wa kiroho. Kwa sababu hiyo, kwa furaha mabaki waliotiwa mafuta wanaona maneno ya Isaya 61:5 yakitimizwa kwao: “Na wageni watasimama na kulisha makundi yenu, na watu wa kabila nyingine watakuwa wakulima wenu, na watunzaji wa mizabibu yenu.”
29. Kwa unyenyekevu wa akili, “mkutano mkubwa” wanafurahi kufanya nini kwa ajili ya “wahudumu wa Mungu wetu,” kukiwa na matokeo gani?
29 Kwa unyenyekevu “mkutano mkubwa” wanaona kwamba ni heshima na pendeleo kubwa kutumikia katika paradiso ya kiroho pamoja na wale wanaoitwa na Isaya 61:6 “makuhani wa [Yehova]” na “wahudumu wa Mungu wetu.” Wao wanajua kwamba hawa Wakristo wa kiroho wanaoitwa hivyo na Yehova Mungu lazima waangalie zaidi mambo ya kiroho katika hekalu lake la kiroho. Kwa hiyo wanafurahi kuwasaidia na kushirikiana na mabaki waliotiwa mafuta ili wao waangalie zaidi mambo ya kiroho yaliyo ya maana zaidi. Haya yote yanasaidia katika kuifanya paradiso ya kiroho kuwa nzuri na kuifanya itoe matunda zaidi kwa utukufu wa Mungu.
30. Isaya 61:5 linaonyesha “wageni” na “watu wa kabila nyingine” wakitoa utumishi gani, lakini Ufunuo 7:14, 15, linautajaje utumishi wao?
30 Hivyo, “wageni” na “watu wa kabila nyingine” wa mfano wa leo wanawasaidia mabaki ili waweze kutimiza wajibu walio nao kwa kutiwa mafuta kwa roho ya Yehova. Katika Isaya 61:5 kazi ya wasaidizi hao inaonyeshwa kuwa kulisha kondoo, kulima, na kutunza mizabibu. Walakini katika njozi ya Ufunuo ya wageni kutoka katika mataifa yote, kabila, jamaa na lugha, habari inayowahusu inasema hivi: “Nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo. Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake.”—Ufu. 7:14, 15.
31. Bila kujali ulimwengu unavyowaona, wale wa “mkutano mkubwa” wanaonwaje na Mungu aketiye katika kile kiti cha enzi?
31 Hivyo wale wa “mkutano mkubwa” wanaonyeshwa wakifanya utumishi mtakatifu kwa Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote anayeketi katika kiti chake cha enzi. Bila kujali namna ulimwengu unavyowaona, wao ni watumishi Wake.
32. Isaya 61:5, 6 litatimizwaje kwa halisi zaidi kwa habari ya mabaki na “mkutano mkubwa” wakati wa ile miaka elfu?
32 “Mkutano mkubwa” huo wa “wageni” na watu wa kabila nyingine “dhiki kubwa” inayokuja. Lo! namna Isaya 61:5 inavyoeleza kwa uzuri kazi watakayoifanya baadaye, wakati wa utawala wa miaka elfu wa Kristo! Wakati huo “makuhani wa [Yehova]” ambao ndio “wahudumu wa Mungu wetu” watatukuzwa pamoja na Kuhani Mkuu Yesu Kristo mbinguni. Wakiwa huko watatumikia wanadamu hata zaidi katika utumishi wao wa kikuhani. (Ufu. 20:6) Lakini “mkutano mkubwa” wataachwa hapa katika dunia iliyosafishwa ambayo itageuzwa yote iwe paradiso halisi. Hivyo, basi, ni nani watakaokuwa mapainia katika kutengeneza upya na kupamba mahali pa kidunia pa kuweka miguu ya Mungu? Basi, watakuwa ni “mkutano mkubwa” wa waokokaji wa dhiki ambao wameendelea kukaa katika paradiso ya kiroho pamoja na mabaki waliotiwa mafuta.
33. “Mkutano mkubwa” utatoshelezaje mahitaji na tamaa ya chakula wakati huo, na ni nani watakaowekea mfano katika utumishi na ibada ya Yehova?
33 Je! kutakuwa na mavazi ya kutengenezwa wakati huo? Manyoya kutoka kwa kondoo watakaolishwa na “mkutano mkubwa” yatakuwa mengi kiasi cha kutosha kutimiza kusudi hilo. Je! mkate pamoja na mazao mengine ya shambani yatahitajiwa? “Wakulima” watatosheleza mahitaji hayo. Watunzaji wa mizabibu watatoa divai iliyo nzuri sana ya kuufurahisha moyo wa mwanadamu. Maendeleo ambayo “mkutano mkubwa” utakuwa umefanya katika kurudisha paradiso duniani yatapendeza macho ya wale watakaofufuliwa kutoka katika wafu na yataonyesha uangalizi uliotangulia kufanyiwa hawa wote waliokombolewa na Kuhani Mkuu. Ijapokuwa hayo yote, “mkutano mkubwa” hawataacha kumtolea Yehova Mungu utumishi mtakatifu kwa ukawaida kupitia kwa Yesu Kristo katika nyua za kidunia za hekalu la kiroho la Mungu. Wataongoza katika jambo hili na kutoa mfano mzuri kwa wale wote watakaofufuliwa kutoka kwa wafu.—Luka 23:43.
[Picha katika ukurasa wa 18]
“Wahudumu wa Mungu wetu” wa kisasa wanafanya kazi ya kutengeneza upya kiroho iliyotabiriwa na nabii Isaya naye Yesu akaianza. Roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu imewatia nguvu watangaze habari njema za Ufalme kwa wapole katika dunia yote.