Sababu Ya Kufurahi Na Kumshangilia Mungu
1. Ni kwa sababu gani mabaki ya Waisraeli wa kiroho wanajawa na furaha leo katika utimizo wa Isaya 61:10?
KUNA furaha kubwa sana isiyoweza kuneneka kwa mmoja kuwekwa huru kutokana na utumwa na kufungwa gerezani katika Babeli Mkuu, ile milki ya ulimwengu ya dini ya uongo. Kuna sababu ya kufurahia kurudishwa katika kibali na nia njema ya Mungu wa dini ya kweli. Mabaki ya Waisraeli ya kiroho waliotiwa mafuta wanapofikiria leo namna walivyokombolea na kurudishwa Naye, wanajawa na furaha. Nabii Isaya aliyeongozwa na Mungu anatia maneno vinywani mwao anaposema: “Nitafurahi sana katika [Yehova], nafsi yangu itashangilia katika Mungu wangu; maana amenivika mavazi ya wokovu, amenifunika vazi la haki, kama bwana arusi ajipambavyo kwa kilemba cha maua, na kama bibi arusi ajipambavyo kwa vyombo vya dhahabu.”—Isa. 61:10.
2. Je! mabaki ya watiwa mafuta bado wanavalia “mavazi ya wokovu,” na ni kwa sababu gani hawatafukuzwa watoke katika paradiso ya kiroho?
2 Kuanzia na mwaka wa baada ya vita wa 1919 na kuendelea Yehova amefanyia mabaki ya Waisraeli wa kiroho “wokovu” kwa kuwaweka huru kutoka kwa Babeli Mkuu na hawara zake. Ijapokuwa mateso yote ya kidini walioyapata tangu wakati huo, mabaki ya watiwa mafuta bado ‘wamevikwa mavazi ya wokovu.’ Mabaki wameazimia kuendelea kuvaa mavazi haya yanayowatambulisha (yanayowafanya wajulikane) mpaka Babeli Mkuu na hawara zake wazinzi waangamizwe katika “dhiki kuu” inayokuja. Kwa kufanya hivyo hawatafukuzwa na kuhamishwa hata kidogo watoke katika paradiso ya kiroho ambayo katika hiyo Yehova amewaleta tangu 1919.
3. Ni kwa sababu gani kulikuwa na uhitaji wa mabaki ya watiwa mafuta wavikwe “vazi la haki”?
3 “Vazi la haki” ni kitu ambacho kimeongezwa katika “mavazi ya wokovu” ambayo Yehova amewavika mabaki wake waliorudishwa (katika kibali). Mabaki wa Waisraeli wa kiroho walionekana kuwa wasio haki katika njia ya kidini, machoni pa ulimwengu, sana sana kwa sababu ya kushtakiwa uongo na viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo. Waliitwa makafiri, manabii wa uongo, Makristo wa uongo, wadanganyi, na watoto wa Ibilisi. Kufanywa shabaha ya mateso ya ulimwenguni pote kulionekana kukihakikisha ukweli wa mashtaka hayo, sana sana katika Jumuiya ya Wakristo. Walakini Yehova aliwaonaje?
4. Yehova alionyeshaje kwamba yeye aliwaona mabaki hawa waliotubu, na kumtafuta Mungu kuwa wenye haki, akiwashuhudia kuwa na haki?
4 Hakimu mkuu anayewahukumu wote hakuwahukumu vibaya na kuwavika mavazi ya wafungwa wa gereza, na kuwafukuzia mbali wasiwemo ndani ya tengenezo lake. Kwa sababu ya kumtafuta na kutafuta Neno lake, yeye aliwapokea tena mabaki wake waliotubu na kuwarudisha katika kibali yake. Yeye aliwapa pendeleo tukufu sana la kuwa mashahidi wake, mabalozi wake, wahubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu” kwa ajili ya kutolea mataifa yote ushuhuda kabla ya taratibu hii mbovu ya mambo kwisha. Yeye alifanya waitwe kwa jina lake, Yehova. (Mt. 24:14, NW; Isa. 43:10) Kisha akawatumia sana walijulishe jina lake na makusudi yake katika pembe nne za dunia. Hii imehakikisha kwamba mabaki ni wenye haki!
5. Kwa hiyo, kwa usemi wa mfano, mabaki hao walipataje kugeuza mavazi yao, wakiwa na furaha kama inayokuwa wakati gani?
5 Hii imewafanya mabaki washuhudiwe haki, wakatangazwa kuwa haki mbele ya ulimwengu wote. Kwa njia ya mfano, hii imekuwa kuwavika “vazi la haki.” Katika njia hii walipata kugeuza mavazi yao, wakatoa yale yenye uchafu na kuvaa yale yenye mapambo. (Isa. 52:1, 2) Furaha yao kwa sababu hii ilichapwa mapema katika makala (tungo) kuu yenye kurasa sita katika toleo la Februari 1, 1925, la Watch Tower iliyokuwa na kichwa “Vazi la Haki,” iliyokuwa juu ya msingi wa andiko la Isaya 61:10. Furaha yao imekuwa kama ya bwana arusi na bibi arusi wake katika siku ya arusi yao!
6. Furaha hii ya mabaki walioshuhudiwa haki imekuwa ya kuendelea kadiri gani, na ni akina nani ambao wamefurahi pamoja nao, kwa wonyesho wa nini?
6 Basi, kwa habari ya kufurahi, yale yaliyotabiriwa na Isaya yametimia: “Furaha yao itakuwa ya milele.” (Isa. 61:7) Leo, miaka 43 tangu 1935 W.K., mabaki waliookolewa na kushuhudiwa haki, wameendelea kufurahi sana, walakini, zaidi ya hayo, “mkutano mkubwa” wa wasaidizi wao wamejiunga katika furaha hiyo. Wakichukua maoni ya Biblia, wamekuja kuwaona mabaki ya watiwa mafuta kuwa “makuhani wa [Yehova]” na “wahudumu wa Mungu wetu.” Wamefahamu kwamba mabaki haya ya watiwa mafuta wamevikwa “mavazi ya wokovu” na kufunikwa kwa “vazi la haki.” Wanaonyesha furaha yao wenyewe kwa kumtumikia Yehova Mungu pamoja na mabaki haya waliokubaliwa wa makuhani na watumishi kwa watu wote. Ijapokuwa hawa “mkutano mkubwa” wanaitwa “wageni” na “watu wa kabila nyingine” nao wanafananishwa na wachungaji, wakulima na watunzaji wa mizabibu, usaidizi pamoja na msaada ambao wametoa kwa mabaki ya watiwa mafuta ni mkubwa sana. Paradiso ya kiroho imefaidika kwa kuwamo kwao.—Mt. 25:31-46.
7. Ni kwa sababu gani mwujiza huu wote wa karne hii ya 20 ulipaswa uje, kama vile majira ya masika yanavyokuja kwa ukawaida katika nchi ya Palestina?
7 Mwujiza huu wa karne hii ya 20 ulipaswa utokee katika kutimiza unabii wa Biblia, kama vile ilivyo hakika kwamba lazima majira ya masika ije kwa ukawaida katika nchi ya Palestina. Unabii wa Isaya 61:11 haungekosa kutimia hata kidogo: “Maana kama nchi itoavyo machipuko yake, na kama bustani ioteshavyo vitu vilivyopandwa ndani yake; ndivyo [Yehova] Mungu atakavyootesha haki na sifa mbele ya mataifa yote.”
8. Ni kwa sababu gani Yehova hangeacha mambo bila kusahihishwa, naye amewalipa watumishi wake “malipo” yao kadiri gani?
8 Lo! namna Yehova ametenda kulingana na neno lake! Yeye hangeacha mambo bila kusahihishwa. Yeye ndiye Mungu “[apendaye] hukumu ya haki, [auchukia] wivi na uovu.” (Isa. 61:8) Katika wakati wa malipo alipaswa awalipe watumishi wake wenye kufanya kazi kwa bidii “malipo katika kweli.” Yeye alifanya “agano jipya” lililoahidiwa watumishi wake watiwa mafuta, nao “mkutano mkubwa” wamefaidika pia kutokana nalo. (Yer. 31:31-34) Amekwisha shuhudia mashahidi wake Wakristo kuwa watumishi wake waliokubaliwa na hata atawashuhudia tena “mbele ya mataifa yote.” Hii itafanya haki yake mwenyewe itokee ionekane na ulimwengu wote. Pia itamletea sifa ya milele kutoka vinywani mwa wapendao haki, kweli na ibada safi.
9. Tunapaswa kujitambulisha sikuzote kwa mavazi gani?
9 Basi, tupilieni mbali “roho ya kushuka moyo”! Sikuzote na tujitambulishe kwa “vazi la sifa” na kumshangilia Yehova Mungu kupitia kwa Kuhani wake Mkuu mtiwa mafuta Yesu Kristo.—Isa. 61:1-3.