Mwalimu Aliyekuwa Tofauti
NI VIGUMU kuangalia nyuma katika kipindi fulani cha wakati wa historia na kufahamu “roho” yake, yaani, maono ya ndani na nia za watu walioishi wakati huo. Kutusaidia tufahamu namna Yesu alivyokuwa tofauti na waalimu wa siku zake, tunaweza kuangalia maoni ya marabi. Wengi wao walikuwa na maoni ya juu sana juu ya Israeli, wakifundisha kwamba ‘Israeli lilikuwa katika mawazo ya Mungu kabla ya kuumbwa kwa ulimwengu wote.’ Vilevile walikazia sana uhitaji wa kuwa na maarifa ya desturi na walijisifia sana kuwa wazao wa Ibrahimu. Mwanachuo wa Biblia Edersheim anasema hivi: “Machukio makubwa, pamoja na kudharau njia zote za Mataifa, mawazo na mashirika; ibada ya kushika sana Torati; kujitakia haki, na kujivunia ukoo, na zaidi kujivunia maarifa” yote hayo yaliwafanya “wampinge kabisa aliyedai kuwa Masihi, aliyekuwa tofauti kabisa nao na mawazo yao.”
Hii inatusaidia kujua namna hata wale wasiokuwa na elimu wangeweza kuona tofauti iliyokuwako kati ya mafundisho ya Yesu na yale ya marabi. Kama asemavyo Mathayo: “Makutano walishangaa mno kwa mafundisho yake [Yesu]; kwa maana alikuwa akiwafundisha . . . si kama waandishi wao.”—Mat. 7:28, 29.