Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 12/15 kur. 3-5
  • Unyenyekevu—Sifa Inayotamanika Sana

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Unyenyekevu—Sifa Inayotamanika Sana
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUSITAWISHA UNYENYEKEVU
  • UNYENYEKEVU UNALETA AMANI
  • KUTUMIKIA KWA UNYENYEKEVU
  • Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Unyenyekevu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Yehova Anawathamini Watumishi Wake Wanyenyekevu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 12/15 kur. 3-5

Unyenyekevu​—Sifa Inayotamanika Sana

MARA nyingi sana kiburi​—mahali pa unyenyekevu na upole​—ndiyo sifa yenye kutokeza sana inayoonyeshwa na wanadamu wenye makosa. Walakini, Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote Aliye Mkuu Zaidi ni mnyenyekevu. Hii inaonyeshwa na nia ya Yehova Mungu ya kuwatendea kwa huruma wenye dhambi wanyonge wanaotafuta kibali na baraka yake kwa bidii.

Unyenyekevu wa Yehova unaonyeshwa vizuri sana katika sura ya tatu katika kitabu cha Maombolezo. Humo nabii Yeremia anaeleza maoni yake ya ndani kuhusu taabu nyingi sana iliyowapata Waisraeli mikononi mwa Wababeli. Kama taifa, Waisraeli walishindwa kabisa, wakaangamizwa. Walakini, baadaye, Yehova Mungu angewakumbuka watu wenye kutubu wa taifa hilo. Tumaini hili linaonyeshwa na maneno ya sala ya Yeremia katika Maombolezo 3:19, 20: “Kumbuka mateso yangu, na msiba wangu, pakanga na nyongo [“mmea wenye sumu. Bila shaka nafsi yako itakumbuka iiname juu yangu,” NW]. Nafsi yangu ikali ikiyakumbuka hayo, nayo inainama ndani yangu.” Ndiyo, katika kuuonyesha unyenyekevu wake usio na kifani, Mungu Mwenye Nguvu Zote ‘angeinama’ chini au ajishushe ili awaangalie kwa kibali wale waliotubu na kuwainua watoke katika hali yao iliyoshushwa.

Kwa hiyo, Yehova Mungu, ijapokuwa yeye ni mkuu kuliko wote naye hana daraka kwa ye yote, anajinyenyekeza na kuwapa kibali hata wale walio katika hali ya chini sana. Hivyo basi, ni jambo linalofaa kwamba yeye anawataka watumishi wake wawe wanyenyekevu. Ni wale tu walio wanyenyekevu anaoangalia kwa kibali, akiwafanya vyombo vya kufikiriwa naye kipekee. Neno lake linatuambia hivi: “Ingawa [Yehova] yuko juu, amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” (Zab. 138:6; Yak. 4:6) Umbali mkubwa unawatenganisha wenye kiburi na Yehova Mungu ambaye hukaa katika mbingu zilizo juu zaidi. Hata hivyo, yeye anaona makusudi yao na kwa hiyo, anawakataa wasiwe watumishi wake. Yeye hawajui hata kidogo.

KUSITAWISHA UNYENYEKEVU

Walakini, ikiwa tunatamani kukubaliwa na Yehova, tutafanya vizuri tukifikiria mfano wa watumishi wake wanyenyekevu wa kale. Mmoja wao alikuwa Daudi. Ijapokuwa alikuwa ametiwa mafuta awe mfalme, yeye hakujaribu kujitwalia cheo hicho kwa kutumia nguvu, bali alikuwa na nia ya kuvumilia kutendewa kwa aibu na kuteswa na Mfalme Sauli. Daudi hakujivuna moyoni mwake. Yeye hakuwaonea kijicho wale waliokuwa na vyeo vya juu wala hakuwadharau wale waliokuwa na hali ya chini na waliokuwa na taabu. Yeye alijua kwamba uwezo wake ni wa kiasi tu naye hakujaribu kufanya mambo asiyoyaweza. Ndiyo sababu angeweza kusema hivi: “[Ee Yehova], moyo wangu hauna kiburi, wala macho yangu hayainuki. Wala sijishughulishi na mambo makuu, wala na mambo yashindayo nguvu zangu.”​—Zab. 131:1.

Daudi alihitajiwa ajitahidi ili asitawishe unyenyekevu huu, kwa kuwa alikubali hivi kwa uongozi wa Mungu: “Hakika nimeituliza nafsi yangu, na kuinyamazisha. Kama mtoto aliyeachishwa kifuani mwa mama yake; Ndivyo [nafsi] yangu ilivyo kwangu.” (Zab. 131:2) Kwa wazi basi, katika wakati mmoja nafsi ya Daudi, yaani, tamaa iliyojaa nafsini mwake, ilihitaji kutulizwa ili aweze kuuonyesha unyenyekevu wa kweli. Tamaa zake na hamu yake kubwa ilitokeza ndani yake fujo kama ile ya mtoto anayetaka sana kunyonya matiti ya mama yake. Walakini, mtoto akiisha achishwa, haichukui mtoto muda mrefu kabla ya kuzoea chakula cha namna nyingine naye hutosheka na kushikwa tu na mama yake. Vivyo hivyo, Daudi alifaulu kuituliza tamaa yake. Akijua kwamba utukuzo unatoka kwa Yehova, yeye alimngojea kwa subira na kwa hiyo yeye angeweza kuwatia moyo Waisraeli wenzake wafanye vivyo hivyo: “Ee Israeli, umtarajie [Yehova], tangu leo na hata milele.”​—Zab. 131:3.

Vivyo hivyo leo unyenyekevu utamfanya mwanamume asubiri kwa habari ya kutumiwa kama mtumishi wa huduma au kama mzee katika kundi la watu wa Mungu. Yeye hatajaribu kujitokeza mbele ili apate kujulikana bali atajitahidi katika kufanya ‘mema kwa wote, sana sana kwa wale wa jamaa ya waaminio.’ (Gal. 6:10) Ijapokuwa huenda sifa zake njema zikakosa kuonekana kwa muda, anaweza kuwa na hakika kwamba hazitaendelea kutoonekana. Kama lisemavyo 1 Timotheo 5:25: “Matendo mema ni dhahiri, au hata ikiwa sivyo, hayawezi kufunikwa milele.”​—New English Bible.

UNYENYEKEVU UNALETA AMANI

Kwa kuendeleza roho ya unyenyekevu pasipo kutokeza matata kwa sababu ya kutotumiwa katika cheo fulani, mwanamume kama huyo anasaidia kuendeleza amani kati ya ndugu zake Wakristo. Hata kama uamuzi wenye makosa uliokuhusu ulitolewa, sikuzote haliwi jambo la hekima kujaribu kulifunua wazi ili uonyeshe kwamba huna makosa. Ijapokuwa huenda mtu akaweza kuonyesha kwamba hana makosa, huenda akaumiza wengine kwa kufanya hivyo. Kwa kweli, huenda akaharibu heshima ya kundi kwa wazee wao waliowekwa. Bila shaka hii inaweza kufanya iwe vigumu sana kwake kufanya kazi pamoja na wazee ambao alivunjia heshima mbele ya wengine.

Ikiwa ndugu anaona kwamba kosa lilifanywa katika kufanya uamuzi, anaweza kujiuliza maulizo haya: Je! kosa hilo lilikuwa zito sana hivi kwamba linapaswa kufunuliwa ijapokuwa huenda kukawa na matokeo mabaya? Au, je! haliwezi kungojea, likasahihishwa baadaye? Je! kutokeza matata isivyofaa kwa sababu yake hakutaleta taabu ambayo huenda ikaharibu amani ya kundi?

Mtu mnyenyekevu anajua kwamba, hata yeye, anafanya makosa pia, na kwa hiyo anakuwa na nia ya kukubali mashauri ya Maandiko na kuyatumia. Ikiwa uamuzi wenye makosa ulifanywa juu yake, anaweza kujitahidi afaidike na jambo hilo, asifanye makosa kama hayo yeye mwenyewe anaposhughulika (watendea) na wengine.

KUTUMIKIA KWA UNYENYEKEVU

Kwa habari ya wazee na watumishi wa huduma waliowekwa, watafanya vema wakiiga mfano wa mtume Paulo katika kutumikia wengine kwa unyenyekevu. Yeye aliandika hivi kwa habari yake mwenyewe na ya wafanya kazi wenzake: “Hatukutafuta utukufu kwa wanadamu, wala kwenu, wala kwa wengine tulipokuwa tukiweza kuwalemea kama mitume wa Kristo; bali tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile [mama] mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na [nafsi] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (1 The. 2:6-8) Unyenyekevu wa namna hiyo wa kuwa na nia ya kutumikia pasipo kuwa na tamaa ya kupata “utukufu” pamoja na kutoa kama huko kwa wakati na nguvu za mtu, katika kuonyesha upendo wa kujitolea, unavutia mioyo ya wengine na kumfanya mtu kuwa chombo kizuri cha kutumiwa na Yehova, kwa baraka ya wanadamu wenzake.

Zaidi ya kutusaidia tuonyeshe roho ya mtu anayetumikia wengine, unyenyekevu pia unaongeza kuwathamini waamini wenzetu. Paulo aliwashauri Wafilipi ‘wasitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu akimhesabu mwenzake kuwa bora kuliko nafsi yake.’(Flp. 2:3) Mtu anayefuata shauri hili anaona sifa njema za wengine, sifa ambazo katika njia fulani zaweza kuwa bora kuliko zake mwenyewe. Kujiona kwa unyenyekevu namna hiyo kunamzuia asiwe na haraka au kusisitiza njia zake mwenyewe au kujaribu kutojali mapendekezo ya wengine. Yeye anajua kwamba kunaweza kuwa na njia fulani za kufanya jambo fulani na ya kwamba huenda uamuzi wake usiwe bora zaidi. Kwa hiyo yeye anakuwa na nia ya kufikiria maono ya ndani pamoja na maoni ya wengine. Yeye anakuwa mwangalifu asijitwalie sifa yote kwa kutimiza jambo ambalo wengine walishiriki. Unyenyekevu wake unawafanya wengine watamani kushirikiana naye.

Bila shaka unyenyekevu ni wa maana sana katika kuhifadhi uhusiano mwema na Mungu pamoja na wanadamu wenzetu. Kwa hiyo ni sifa ambayo sisi sote kama watumishi waliojitoa kwa Yehova tutataka kusitawisha zaidi na zaidi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki