Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w91 7/15 kur. 27-30
  • Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Unyenyekevu Ni Nini?
  • Lazima Uwe Halisi
  • Maoni ya Yehova
  • Unaonyeshwa na Mungu na Kristo
  • Manufaa za Unyenyekevu
  • Unyenyekevu na Tengenezo la Mungu
  • Unyenyekevu na Nidhamu
  • Baki Ukiwa Umejivika Unyenyekevu
  • Unyenyekevu
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • Sitawisha Unyenyekevu wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Yehova Anawathamini Watumishi Wake Wanyenyekevu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • Yesu Aliweka Kielelezo Cha Unyenyekevu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
w91 7/15 kur. 27-30

Kwa Nini Kujivika Unyenyekevu?

MWANDISHI Mwamerika Edgar Allan Poe alikuwa tu amemaliza kuwasomea marafiki wake hadithi yake mpya. Walisema kwa ucheshi kwamba alikuwa ametumia jina la shujaa fulani mara nyingi mno. Poe aliitikiaje? Rafiki mmoja alikumbuka hivi: “Roho yake yenye kiburi haikuweza kuvumilia karipio hilo la wazi, kwa hiyo kwa hasira ya ghafula, kabla marafiki wake hawajaweza kumzuia, alikuwa ametupa kila ukurasa katika moto uliokuwa ukiwaka.” Hadithi “yenye kuchekesha sana, iliyokuwa huru kabisa na . . . huzuni yake ya kawaida,” ikawa imepotea. Labda unyenyekevu ungaliiokoa.

Ingawa kiburi kinasukuma watu wafanye mambo yasiyo ya hekima, kimeenea ulimwenguni. Lakini watumishi wa Yehova wanapaswa kuwa tofauti. Ni lazima wavae vazi lililobuniwa vizuri la unyenyekevu.

Unyenyekevu Ni Nini?

Mtume Paulo alirejezea kwenye vazi la Kikristo lenye urembo la unyenyekevu alipowaandikia waamini wenzake katika jiji la kale la Kolosai. Aliwahimiza hivi: “Kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu [udhalili wa akili, NW], upole, uvumilivu.”—Wakolosai 3:12.

Naam, unyenyekevu ni “udhalili wa akili.” Ni “unyenyekevu wa akili; kutokuwa na kiburi; upole.” Mtu mnyenyekevu ni “mwenye kiasi katika roho; si mwenye kiburi.” Yeye ni “mwenye heshima kwa kina kirefu au kwa adabu.” (The World Book Dictionary, Buku 1, ukurasa 1030) Unyenyekevu si woga au udhaifu. Kwa kweli, kiburi huonyesha udhaifu, huku kuonyesha unyenyekevu mara nyingi huhitaji moyo mkuu na nguvu.

Katika Maandiko neno la Kiebrania linalofasiriwa “jinyenyekeze” kwa uhalisi humaanisha “jikanyage chini kwa miguu.” Hivyo, mwandishi wa Mithali mwenye hekima alishauri hivi: “Mwanangu, kama . . . umekamatwa kwa maneno ya kinywa chako, . . . fanya hivi ukajiokoe, kwa kuwa umejitia mkononi mwa jirani yako; nenda ukanyenyekee [ukajikanyage chini kwa miguu], na kumsihi jirani yako.” (Mithali 6:1-3) Yaani, ondolea mbali kiburi, kiri kosa lako, nyosha mambo.

Lazima Uwe Halisi

Si watu wote waonekanao kuwa wanyenyekevu walio na unyenyekevu halisi. Watu fulani mmoja mmoja waonekanao kuwa wanyenyekevu huenda kwa kweli wakawa wenye kiburi na watafanya vyovyote wawezavyo ili kupata wanachotaka. Halafu kuna wale wanaotumia vazi la unyenyekevu wa uwongo ili kuwavutia wengine. Kwa mfano, mtume Paulo alikabili wengine walioonyesha “unyenyekevu wa uwongo,” naye alionyesha kwamba yeyote aliyefanya hivyo kwa kweli alikuwa “amepumbazika kwa fikira danganyifu za kidunia.” Mtu kama huyo alikuwa akidhania kwa kukosea kwamba kuwa na pendeleo la Mungu kulitegemea juu ya kama alikula, alikunywa, au aligusa vitu fulani au aliadhimisha siku za kidini au sivyo. Ni kweli, huenda ikawa alionekana kuwa mwenye kumcha Mungu na mnyenyekevu, lakini unyenyekevu wake wa uwongo haukuwa na thamani yoyote. (Wakolosai 2:18, 23, HNWW) Kwa hakika, ulimwongoza kufikiri kwamba zawadi ya uhai ilipewa kwa wale waliokataa vitu vya kimwili. Ulitoa pia namna ya kijanja ya upendo wa vitu vya kimwili kwa sababu makatazo ya mwenye kujinyima vitu vya kimwili yalikazia fikira vitu vya kimwili ambavyo alidai kuchukia.

Kwa upande mwingine, unyenyekevu wa kweli unamzuia mtu asijifikiri yu bora katika mavazi, mapambo, na mtindo-maisha. (1 Yohana 2:15-17) Mtu aliyejivika vazi la unyenyekevu havuti fikira kwa kadiri isiyofaa kwake mwenyewe au kwa uwezo wake mbalimbali. Badala ya hivyo, unyenyekevu unamsaidia awatendee wengine katika njia ya ufikirio na kujiona mwenyewe jinsi Mungu amwonavyo. Jinsi gani hivyo?

Maoni ya Yehova

Nabii Samweli alipokuwa karibu kumpaka mafuta mfalme mpya kwa ajili ya taifa la Israeli, alifikiria kwamba Eliabu mwana wa Yese ndiye aliyekuwa chaguo la Yehova. Lakini Mungu alimwambia Samweli hivi: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA [Yehova, NW] huutazama moyo.” Wana wa Yese saba walikataliwa. Daudi ndiye aliyekuwa chaguo la Mungu, aliyethibitika kuwa mtu mwenye imani na mwenye unyenyekevu.—1 Samweli 13:14; 16:4-13.

Vazi la unyenyekevu linatulinda tusiwe wenye kiburi, wenye kujitanguliza kwa kiburi—na kutokubaliwa na Mungu. Yeye “huwapinga wajikuzao, bali huwapa neema wanyenyekevu.” (Yakobo 4:6) Maoni yake yanaonekana katika maneno ya mtunga zaburi: “Ingawa BWANA [Yehova, NW] yuko juu, amwona mnyenyekevu, naye amjua mwenye kujivuna tokea mbali.” (Zaburi 138:6; 1 Petro 5:5, 6) Yale ambayo Mungu hutazamia kwa watumishi wake ni wazi kutoka kwa swali hili, lililozushwa kwenye Mika 6:8, ZSB: “BWANA [Yehova, NW] anataka nini kwako ila kutenda haki, na kupenda rehema [fadhili, NW] na kutembea kwa unyenyekevu [kiasi, NW] na Mungu wako?”

Unaonyeshwa na Mungu na Kristo

Si ajabu kwamba Yehova hututazamia kuonyesha unyenyekevu! Ni mojawapo ya sifa zake mwenyewe. Mungu alipomkomboa kutokana na adui zake Daudi aliimba hivi: “Nawe [Yehova] umenipa ngao ya wokovu wako, . . . na unyenyekevu wako umenikuza.” (Zaburi 18:35; 2 Samweli 22:1, 36) Ingawa Yehova yumo katika mbingu zilizo juu zaidi, yeye “hutazama chini kabisa, naam, huzitazama mbingu na nchi. Humwinua fukara kutoka mavumbini; humnyanyua maskini kutoka unyonge wake, na kumweka pamoja na wakuu.” (Zaburi 113:5-8, HNWW) Mungu huonyesha unyenyekevu kwa kuzoea rehema kuelekea ainabinadamu yenye dhambi. Kushughulika kwake pamoja na watenda dhambi na kutoa kwake Mwanae kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi ni wonyesho wa unyenyekevu, upendo, na sifa zake nyinginezo.—Warumi 5:8; 8:20, 21.

Yesu Kristo, aliyekuwa “mpole na mnyenyekevu wa moyo,” aliweka mfano mkuu zaidi wa unyenyekevu wa kibinadamu. (Mathayo 11:29) Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ye yote atakayejikweza, atadhiliwa; na ye yote atakayejidhili, atakwezwa.” (Mathayo 23:12) Huo haukuwa usemaji tu. Jioni kabla ya yeye kufa, Yesu aliosha miguu ya mitume wake, akifanya utumishi uliotolewa na watumwa kidesturi. (Yohana 13:2-5, 12-17) Yesu alitumikia Mungu kwa unyenyekevu kabla ya kuja duniani na amekuwa akionyesha unyenyekevu tangu ufufuo wake kwenye cheo kitukufu mbinguni. Kwa hiyo Paulo aliwaonya kwa upole waamini wenzake ‘wahesabu wenzio kuwa bora kuliko nafsi zao’ na wawe na mwelekeo wa Yesu Kristo wenye unyenyekevu.—Wafilipi 2:3, 5-11.

Kwa kuwa Mungu na Kristo huonyesha unyenyekevu, ni lazima wale watakao kibali cha kimungu waonyeshe sifa hiyo. Ikiwa tumekuwa wenye kiburi nyakati fulani, ingekuwa hekima kujinyenyekeza na kumwomba Mungu msamaha. (Linganisha 2 Nyakati 32:24-26.) Na badala ya kuwa na mawazo matukufu juu yetu wenyewe, tunahitaji kutumia shauri la Paulo: “Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge.” (Warumi 12:16) Lakini, unyenyekevu waweza kunufaishaje sisi na wengineo?

Manufaa za Unyenyekevu

Faida moja ya unyenyekevu ni kwamba inatuzuia tusijigambe juu ya sisi wenyewe. Hivyo hatuwaudhi wengine na tunaepuka aibu ya kibinafsi kama hawapati mshangao kwa ajili ya vitendo vyetu. Twapaswa kujigamba juu ya Yehova, si juu ya sisi wenyewe.—1 Wakorintho 1:31.

Unyenyekevu unatusaidia kupata mwelekezo wa kimungu. Yehova alituma malaika kwa Danieli akiwa na njozi kwa sababu nabii huyo alikuwa amejinyenyekeza mbele ya Mungu alipokuwa akitafuta-tafuta mwelekezo na ufahamu. (Danieli 10:12) Ezra alipokuwa karibu kuongoza watu wa Yehova nje ya Babuloni wakiwa na dhahabu na fedha nyingi ya kurembesha hekalu katika Yerusalemu, alitangaza kufunga ili waweze kujinyenyekeza mbele za Mungu. Tokeo likawa nini? Yehova aliwalinda juu ya shambulio la kiadui pindi ya ile safari ya hatari. (Ezra 8:1-14, 21-32) Kama Danieli na Ezra, na tuonyeshe unyenyekevu na kutafuta mwelekezo wa Yehova badala ya kujaribu kutimiza majukumu yenye kutolewa na Mungu katika hekima na uwezo wetu wenyewe.

Kama tumejivika vazi la unyenyekevu, tutawastahi (tutawaheshimu) wengine. Kwa mfano, watoto walio na unyenyekevu huwastahi na kuwatii wazazi wao. Wakristo wanyenyekevu huwastahi waamini wenzao wa mataifa, rangi, na malezi mengineyo, kwa kuwa unyenyekevu unatufanya tusipendelee.—Matendo 10:34, 35; 17:26.

Unyenyekevu unaendeleza upendo na amani. Mtu mnyenyekevu hapigani na waamini wenzake kwa juhudi ya kuimarisha haki zake zenye kudhaniwa. Paulo alifanya tu mambo yaliyokuwa yenye kujenga na hangesumbua dhamiri ya ndugu. (Warumi 14:19-21; 1 Wakorintho 8:9-13; 10:23-33) Unyenyekevu unatusaidia pia kuendeleza upendo na amani kwa kuwasamehe wengine kwa ajili ya dhambi zao dhidi yetu. (Mathayo 6:12-15; 18:21, 22) Unatusukuma kumwendea mtu aliyeudhiwa, kukiri kosa letu, kumwomba msamaha wake, na kufanya tuwezavyo ili kusahihisha kosa lolote ambalo huenda ikawa tumelifanya. (Mathayo 5:23, 24; Luka 19:8) Ikiwa mtu aliyeudhiwa anatukaribia, unyenyekevu unatuchochea kusuluhisha mambo kwa amani katika roho ya upendo.—Mathayo 18:15; Luka 17:3.

Ukombozi unategemea kuonyesha unyenyekevu. Kwa mfano, kuhusu Mungu, inasemwa hivi: “Watu wanaoonewa [wanyenyekevu, NW] wewe utawaokoa; ila macho yako ni juu ya wenye kiburi, uwadhili.” (2 Samweli 22:28) Mfalme Yesu Kristo ‘apandaye katika kusudi la ukweli na unyenyekevu na uadilifu,’ atawaokoa wale wanaojinyenyekeza mbele yake na mbele ya Baba yake. (Zaburi 45:4, NW) Wale waonyeshao unyenyekevu waweza kupata faraja katika maneno haya: “Mtafuteni BWANA [Yehova, NW], enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia, ninyi mliozitenda hukumu zake; itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA [Yehova, NW].”—Sefania 2:3.

Unyenyekevu na Tengenezo la Mungu

Unyenyekevu unaongoza watu wa Mungu kuthamini tengenezo lake na kukaa pamoja nalo wakiwa washika uaminifu wa maadili. (Linganisha Yohana 6:66-69.) Ikiwa hatupewi pendeleo la utumishi tulilokuwa tukitazamia kupokea, unyenyekevu utatusaidia tushirikiane pamoja na wale wenye daraka ndani ya kundi. Na ushirikiano wetu wenye unyenyekevu unaweka mfano mzuri.

Kwa upande mwingine, unyenyekevu unatuzuia kutokana na kuonyesha majivuno kuhusu mapendeleo yetu ya utumishi miongoni mwa watu wa Yehova. Unatuzuia kutokana na kutafuta sifa kwa kazi ambayo tumependelewa kufanya katika tengenezo la Mungu. Tena, ikiwa tunatumikia tukiwa wazee, unyenyekevu unatusaidia kutendea kundi la Mungu kwa wororo.—Matendo 20:28, 29; 1 Petro 3:8.

Unyenyekevu na Nidhamu

Vazi la unyenyekevu linatusaidia kupokea nidhamu. Watu wanyenyekevu hawako kama Mfalme Uzia wa Yuda, ambaye moyo wake ulikuja kuwa wenye kujigamba sana hivi kwamba alijitwalia bila haki majukumu ya kikuhani. Yeye ‘alimwasi Yehova, Mungu wake; kwani aliingia hekaluni mwa Yehova, ili afukize uvumba juu ya madhabahu ya kufukizia.’ Uzia alipowaghadhibikia makuhani kwa kumsahihisha, alipatwa na ukoma. Lo! ni bei iliyoje kulipa kwa ajili ya kukosa unyenyekevu! (2 Nyakati 26:16-21; Mithali 16:18) Usiwe kamwe kama Uzia na kuacha kiburi kikuzuie kukubali nidhamu kutoka kwa Mungu kupitia Neno na tengenezo Lake.

Kuhusu hilo Paulo aliwaambia Wakristo Waebrania waliopakwa mafuta: “Mmeyasahau yale maonyo, yasemayo nanyi kama kusema na wana, Mwanangu, usiyadharau marudia ya Bwana [nidhamu kutoka kwa Yehova, NW], wala usizimie moyo ukikemewa naye; maana yeye ambaye Bwana [Yehova, NW] ampenda, humrudi, naye humpiga kila mwana amkubaliye. . . . Kila adhabu wakati wake haionekani kuwa kitu cha furaha, bali cha huzuni; lakini baadaye huwaletea wao waliozoezwa nayo matunda ya haki yenye amani.” (Waebrania 12:5-11) Pia, kumbuka kwamba “maonyo ya kumwadilisha mtu ni njia ya uzima.”—Mithali 6:23.

Baki Ukiwa Umejivika Unyenyekevu

Ni muhimu kama nini Wakristo wajivike vazi la unyenyekevu sikuzote! Linatusukuma kuvumilia tukiwa wahubiri wa Ufalme, tukitoa ushahidi kwa unyenyekevu kutoka nyumba kwa nyumba katika kutafuta-tafuta wale walio na “mwelekeo wenye kufaa kwa ajili ya uhai wa milele.” (Matendo 13:48, NW; 20:20) Kwa kweli, unyenyekevu unatusaidia kuendelea kumtii Mungu katika mambo yote, ingawa wapinzani wenye kiburi huchukia mwendo wetu wenye uadilifu.—Zaburi 34:21.

Kwa sababu unyenyekevu unatusukuma ‘kumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote,’ anafanya mapito yetu yanyoke. (Mithali 3:5, 6) Kwa hakika, tunaweza kutembea pamoja na Mungu na kuonea shangwe upendeleo na baraka yake ikiwa tumejivika tu sifa hiyo nzuri. Kama vile mwanafunzi Yakobo alivyoandika: “Nyenyekeeni mbele ya Bwana [Yehova, NW], naye atawainueni.” (Yakobo 4:10, HNWW) Acheni basi tujivike unyenyekevu, lile vazi lenye urembo lililobuniwa na Yehova Mungu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki