Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 9/1 kur. 400-406
  • Rehema ya Mungu Yaonyeshwa Wakati wa Har–Magedoni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Rehema ya Mungu Yaonyeshwa Wakati wa Har–Magedoni
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MFANO MDOGO WA REHEMA YA KIMUNGU WAKATI WA HAR-MAGEDONI
  • WALE AMBAO “SI WATU WANGU”
  • TUMAINI LA KUPATA REHEMA YA KIMUNGU KWA WATU MMOJA MMOJA
  • ULINGANIFU WA UNABII
  • Rehema ya Mungu Kwa Wanadamu Katika Karne Yetu ya Ishirini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Unabii wa Hosea Hutusaidia Kutembea Pamoja na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Kitabu Cha Biblia Namba 28—Hosea
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Hosea
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 9/1 kur. 400-406

Rehema ya Mungu Yaonyeshwa Wakati wa Har–​Magedoni

1, 2. (a) Yehova aliweka mfano wa ndoa yake mwenyewe katika ndoa ya nani? (b) Israeli waligeukaje kuwa wazinzi siku za Mfalme Yeroboamu wa Kwanza?

NDOA kati ya wanaume na wanawake zimepatwa na magumu wakati wa utawala wa dhambi na uovu duniani. Ndivyo ilivyokuwa kwa ndoa ya Mungu na taifa la kale la Israeli.

2 Mungu alionyesha mfano wa ndoa yake mwenyewe katika ndoa ya nabii wake Hosea. Hosea alikuwa amekwisha oa Gomeri binti Diblaimu kwa agizo la Mungu. Ndoa hiyo ilifananisha ndoa ya Yehova na Israeli wa kale kupitia kwa agano la Torati ya Musa lililofanywa katika Mlima Sinai mwaka wa 1513 K.W.K. Baada ya Mfalme Sulemani, mwana wa Daudi kufa mwaka wa 997 K.W.K., taifa la Israeli lililokuwa limeolewa zamani liligawanyika sehemu mbili. Kabila la Yuda na Benyamini yalibaki chini ya ufalme wa Yuda, makabila mengine kumi yakawa chini ya ufalme wa Israeli. Mfalme wa kwanza wa makabila kumi hayo alikuwa Yeroboamu mwana wa Nebati wa kabila la Efraimu. Ufalme wa Israeli ulivunja mapatano yake ya ndoa na Yehova ukiwa chini ya Yeroboamu wa Kwanza huyo; ulikataa ibada Yake iliyokuwako Yerusalemu ukaanza ibada yake wenyewe ya sanamu, ya ndama wawili wa dhahabu, mmoja akiwa Dani na mwingine Betheli. Hivyo, ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulipata kuwa mzinzi, kama Gomeri mke wa nabii Hosea.

3. Yehova aliagiza mtoto wa pili wa Gomeri aitwe nani na kwa sababu gani?

3 Gomeri alipomzalia Hosea mwana halali aitwaye Yezreeli, ndoa ya Hosea iliendeleaje ikifananisha ndoa ya Yehova na taifa la Israeli la makabila kumi na mawili? Hosea aendelea kuisimulia habari hiyo, akisema hivi: “Akachukua mimba tena, akazaa mtoto mwanamke. [Yehova] akamwambia [Hosea], Mwite jina lake Lo-ruhama; kwa maana sitairehemu nyumba ya Israeli tena, [kwa maana nitawapeleka mbali hakika]. Lakini nitairehemu nyumba ya Yuda; nitawaokoa kwa [Yehova], Mungu wao; wala sitawaokoa [Wayahudi] kwa upinde, wala kwa upanga, wala kwa silaha, wala kwa farasi, wala kwa wapanda farasi.”​—Hos. 1:6, 7.

4. Baba ya binti Gomeri alikuwa nani, nalo jina lake lilielekezwa kwa nani kwa unabii?

4 Katika habari iliyo juu, Hosea hasemi kwamba Gomeri alimzalia “yeye” binti. Kwa hiyo kwa kawaida inafahamika kwamba mtoto mwanamke huyu aliyeitwa Loruhama alikuwa ‘mtoto wa uasherati.’ (Hos. 1:2) Tendo la uzinzi huo wa Gomeri mke wa Hosea lililingana na uhusiano wa ndoa kati ya Yehova Mungu na taifa la Israeli. Kwa habari ya Hosea, jambo la muhimu ni maana ya jina alilopewa binti Gomeri​—na sababu ya Yehova kumwambia Hosea amwite jina hilo la kuchukiza, la kuogofya. Jina la binti Lo-ruhama lamaanisha kwa halisi “Mwanamke Asiyehurumiwa.” Yehova alitumia jina hilo kwa unabii juu ya taifa la Israeli la makabila kumi lenye kufanya uzinzi, lenye makao ya kifalme katika mji wa Yezreeli. Kwa sababu gani?

5. Kulikuwa na matokeo gani Yehova alipokosa kuonyesha rehema juu ya ufalme wa Israeli wa makabila kumi, nayo Jumuiya ya Wakristo itapatwaje na jambo kama hilo?

5 Jumuiya ya Wakristo yapaswa kusikiliza Yehova anapotoa sababu katika karne yetu ya 20, kwa sababu jina Lo-ruhama latumika sasa. Sababu anayotoa Yeye yaihusu Jumuiya ya Wakristo leo: “Kwa maana sitairehemu nyumba ya Israeli tena.” (Hos. 1:6) Sasa Jumuiya ya Wakristo ndiyo isiyoonyeshwa rehema. Kama ufalme wa Israeli wa makabila kumi, jumuiya hiyo inafanya uzinzi wa kiroho juu ya Yehova Mungu, ambaye inajidai kuwa katika uhusiano wa ndoa naye kupitia kwa “agano jipya” lililopatanishwa na Yesu Kristo mwaka wa 33 W.K. (Yer. 31:31-34; Luka 22:19, 20; Ebr. 8:6-12) Kulitokea nini kwa sababu tangu siku za Hosea Yehova hakuwa na rehema tena kwa ufalme wa Israeli wa makabila kumi? Ufalme huo wenye kufanya uzinzi wa kiroho uliharibiwa baada ya muda unaopungua karne moja, yaani, mwaka wa 740 K.W.K. Vivyo hivyo, Jumuiya ya Wakristo itaangamizwa wakati wa “dhiki kubwa” inayokuja itakayofikia upeo wake wakati wa Har–​Magedoni, kwa sababu Yehova hana rehema tena kwa jumuiya hiyo ya kisasa iliyo kama Israeli ya kale.​—Mt. 24:21, 22.

6. Kulingana na Hosea 1:7, Yehova aliondoa rehema yake juu ya Israeli wote wakati wa uharibifu wa ufalme wa makabila kumi?

6 Wakati Yehova alipokuwa akiufutilia mbali ufalme wa Israeli wa makabila kumi, je! hakuwa na huruma hata kidogo? Alikosa kabisa kuonyesha rehema juu ya makabila yote ya taifa ambalo hapo kwanza lilikuwa limeingia katika uhusiano wa ndoa naye kupitia kwa agano la Torati lililofanywa katika Mlima Sinai? Yehova mwenyewe ajibu maulizo hayo, akisema: “Lakini nitairehemu nyumba ya Yuda; nitawaokoa kwa [Yehova], Mungu wao; wala sitawaokoa kwa upinde, wala kwa upanga, wala kwa silaha, wala kwa farasi, wala kwa wapanda farasi.”​—Hos. 1:7.

7, 8. (a) Ni kwa sababu gani Yehova alikuwa na rehema juu ya nyumba ya Yuda? (b) Kwa sababu ya mamlaka kuu ya ulimwengu ya wakati huo, ingempasa Yehova afanye nini ndiyo aokoe Yuda bila kutumia vifaa vya vita?

7 Itafaa tuangalie sababu ya kusadikisha iliyomfanya Yehova achague kuonyesha rehema kwa ufalme wa Yuda wa makabila mawili, pamoja na mji wake mkuu Yerusalemu. Katika Hosea 11:12 Yehova aeleza wazi sababu yake ya kuonyesha rehema, anaposema hivi: “Efraimu amenizinga kwa maneno ya uongo, na nyumba ya Israeli [iliyowakilishwa na kabila lililo kuu, Efraimu] kwa udanganyifu; na Yuda hata sasa [“anazunguka akitembea na,” NW] aliye Mtakatifu, naye ni mwaminifu.”a Nyumba ya Yuda bado ‘ilizunguka ikitembea’ na Yehova kama Aliye Mtakatifu Zaidi, Mungu wake. Kwa hiyo, kwa ajili ya jina lake, Yehova alilazimika kuiokoa nyumba ya Yuda. Ndiyo sababu alisema hivi: “Nitawaokoa kwa [Yehova], Mungu wao.”

8 Yehova alikusudia kuiokoa nyumba ya Yuda wakati ule ule alipoupeleka mbali na kuukomesha ufalme wa makabila kumi, yaani, “ufalme wa nyumba ya Israeli.” Ili afanye hivyo, ilimpasa Yehova apambane na Milki ya Ashuru. Ashuru ilikuwa ndiyo mamlaka kuu ya ulimwengu ya siku hizo, kwa kuimarisha sana mambo yake ya kijeshi. Chini ya hali hizo, ilimpasa Yehova afanye jambo lisilo la kawaida ndiyo aiokoe nyumba ya Yuda bila ya kutumia upinde, upanga, vita, farasi wavuta magari wala wapanda farasi.

MFANO MDOGO WA REHEMA YA KIMUNGU WAKATI WA HAR-MAGEDONI

9. Baada ya uharibifu wa Samaria, Yehova alipata tatizo gani kwa habari ya Yerusalemu?

9 Mwaka wa 740 K.W.K. Yehova alitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kama “shoka” lake kuikata “nyumba ya Israeli” yenye kufanya uzinzi na kuabudu sanamu. Makao yake ya kifalme katika Yezreeli yalinyang’anywa yakawa matupu, mji wake mkuu Samaria ukapinduliwa, Waisraeli wenye kuokoka wakapelekwa uhamishoni katika mikoa ya mbali ya Ashuru. (Isa. 10:15) Hilo lilitisha Yerusalemu, ambako Mfalme Hezekia wa jamaa ya kifalme ya Daudi alitawala ufalme wa Yuda wa makabila mawili. Miaka minane baadaye majeshi ya Ashuru yaliishambulia nchi ya Yuda yakaanza kupunguza miji yake. Mfalme mshambuliaji wa Ashuru, Senakeribu, alikuwa na pinde nyingi, panga nyingi, vifaa vya vita, farasi wavuta magari na wapanda farasi. Ni kwa njia gani, sasa, Yehova angeonyesha rehema juu ya nyumba ya Yuda? Hali ikawa ya kumtatiza sana Yehova.

10, 11. Sasa Yehova alilokoaje nyumba ya Yuda apate kutukuza jina lake mwenyewe?

10 Alipokuwa akiuzingira mji wa Libna, Senakeribu alimpelekea Mfalme Hezekia wa Yerusalemu neno mkataa, akiwa karibu maili 20 (kilomita 32) kutoka huko. Yehova alichukizwa akamwongoza nabii wake Isaya kutoa ujumbe wa kukaidi wajumbe Waashuru waliokuwa mbele ya kuta za Yerusalemu waurudishe kwa Senakeribu mwenye makufuru. Mfalme huyo alipopokea ujumbe huo wenye kumwonya, Yehova aliokoa Yuda apate kutukuza jina lake mwenyewe.

11 “Ikawa usiku uo huo,” twaambiwa na maandishi katika 2 Wafalme 19:35-37, “malaika wa [Yehova] alitoka, akakiingia kituo cha Waashuru, akawapiga watu mia na themanini na tano elfu. Na watu walipoondoka asubuhi na mapema, kumbe! hao walikuwa maiti wote pia. Basi Senakeribu mfalme wa Ashuru akaondoka, akaenda zake, akarudi akakaa Ninawi. Ikawa, alipokuwa akiabudu nyumbani mwa Nisroki, mungu wake, Adrameleki na Shareza [“wanawe,” NW] wakampiga kwa upanga; wakaikimbilia nchi ya Ararati. Na Esar-hadoni mwanawe akatawala mahali pake.”

12. Wonyesho huo wa rehema ya Yehova juu ya nyumba ya Yuda ulikuwa mfano mdogo wa nini?

12 Je! huo haukuwa wonyesho mkubwa wa rehema ya Yehova juu ya ufalme wa Yuda uliokuwa ukiendelea kuwa mwaminifu wakati huo kwa uhusiano wa kiroho wa ndoa pamoja Naye? Linalotufariji sisi leo ni kwamba, huo ulikuwa mfano mdogo wa rehema ambayo Yehova ataonyesha wakati wa vita inayokuja katika Har–​Magedoni. (Ufu. 16:14, 16) Mungu hataonyesha rehema hata kidogo kwa majeshi yenye kumpinga duniani yatakayokuwa chini ya Shetani Ibilisi yakishambulia mashahidi waaminifu wa Yehova wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika inayoitwa Har–​Magedoni.b Yehova ataokoa mashahidi wake waaminifu duniani bila kutumia pinde, panga, vita, farasi wala wapanda farasi wala vifaa vinginevyo vya kijeshi.

13. Wakati huo jina Lo-ruhama litahusu nani, na kwa hiyo ni nani watakaookoka Mungu atakapoonyesha ghadhabu juu ya “vyombo vya ghadhabu”?

13 Huo utakuwa wakati wa kuonyesha ghadhabu ya kimungu juu ya “vyombo vya ghadhabu” na wa kuonyesha rehema ya kimungu juu ya mabaki waliotiwa mafuta waliofananishwa na “nyumba ya Yuda,” ambao ni warithi pamoja na Kristo. (Rom. 9:22) Wao watakuwa wakishikamana na agano jipya, agano ambalo kwalo Yehova ameoa Israeli wa kiroho. Jina Lo-ruhama (Asieyehurumiwa) haliwahusu mabaki kama linavyohusu Jumuiya ya Wakristo sasa, kwa maana wao ni Waisraeli waaminifu wa kiroho. (Gal. 6:16; Yak. 1:1; Ufu. 7:4-8) Mabaki ya kiroho wataokolewa na Yehova “Mungu wao!” Wataokoka!

14, 15. (a) Ilitukiaje kati ya Yehonadabu mwana wa Rekabu na Mfalme Yehu? (b) Wazao wa Yehonadabu waliokoka mabaya gani ya taifa, na Warekabu hao walifananisha nani leo?

14 Zamani za kale, wakati Mfalme Senakeribu alipoutisha Yerusalemu, si “nyumba ya Yuda” peke yake iliyoonyeshwa rehema na Yehova. Watu wasio Wayahudi wenye kujulikana kama Warekabu walionyeshwa pia. Walikuwa wazao wa Yehonadabu mwana wa Rekabu Mkeni. Wakati Mfalme Yehu wa Israeli alipokuwa akipanda gari kuelekea Samaria akaharibu ibada ya Baali huko kwa agizo la Yehova, alimkaribisha Yehonadabu waende pamoja akamwambia: “Fuatana nami, ukaone wivu wangu kwa [Yehova].” (2 Fal. 10:15-27) Yehonadabu alifanya hivyo.

15 Wakati wa kuanguka kwa Samaria mwaka wa 740 K.W.K. wazao wa Yehonadabu Mrekabu waliokoka. Waliokoka pia Senakeribu alipoishambulia nchi ya Yuda mwaka wa 732 K.W.K. Baadaye Warekabu walishirikiana na ufalme wa Yuda siku za Yeremia nabii. Hizo zilikuwa siku za mwisho za Yerusalemu kabla mji huo haujaharibiwa na Wababeli mwaka wa 607 K.W.K. Kwa sababu Warekabu walikuwa waaminifu, Yehova aliahidi kuwaokoa wakati wa uharibifu wa Yerusalemu. (Yer. 35:1-19) Watu hao walioonyeshwa rehema na Yehova walifananisha nani? Walifananisha “mkutano mkubwa” wa waabudu wa Yehova wanaoshirikiana na mabaki waliotiwa mafuta leo. Hawa pia wataokoka “dhiki kubwa” inayokuja, wakiwa na tumaini la kukaa katika dunia ya paradiso.​—Ufu. 7:9-17.

WALE AMBAO “SI WATU WANGU”

16. (a) Kukataliwa kwa Jumuiya ya Wakristo isiwe sehemu ya watu wa Yehova kutamaanisha nini kwayo? (b) Mwana wa pili wa mke wa Hosea aliitwa nani, na kwa sababu gani?

16 Sasa, kabla ya kutokea “dhiki kubwa” karibuni, huu ndio wakati wetu wa kujifaidi na rehema ya Yehova. Na tusisahau jambo hili kamwe: Jumuiya ya Wakristo haitaonyeshwa rehema hata kidogo wakati wa dhiki inayokuja. Kwa hiyo, yatupasa tujitenge nayo. Wakati huo jumuiya hiyo itaonyeshwa wazi kabisa kwamba si sehemu ya watu wa Yehova. Itaharibiwa! Huyo ndiye Lo-ruhama (Asiyehurumiwa) wa leo. (Hos. 1:6) Kukataliwa kwake kabisa kulitangulia kuonyeshwa katika mambo zaidi yaliyotukia katika ndoa ya nabii Hosea. Akimtaja mkewe Gomeri asema hivi: “Basi, akiisha kumwachisha Lo-ruhama, akachukua mimba, akazaa mtoto I mwanamume. [Yehova] akasema, Mwite jina lake Lo-ami; kwa maana ninyi si watu wangu, wala mimi sitakuwa Mungu wenu.” (Hos. 1:8, 9) Sura ya kwanza ya kitabu cha unabii cha Hosea yamalizika kwa maneno hayo katika tafsiri za Biblia za Kiyahudi na katika chapa za Septuagint Version ya Kigiriki ya Hosea.

17. Kwa sababu gani Lo-ami ni jina lililomfaa mwana wa pili wa Gomeri, na kwa hiyo Yehova aliuambia nini ufalme wa Israeli wa makabila kumi?

17 Mwana wa pili wa mke wa Hosea Gomeri anafahamika pia kwamba hakuzaliwa na Hosea, bali alikuwa mtoto wa uzinzi wa Gomeri. Hosea hasemi kwamba Gomeri alimzalia yeye mwana huyo wa pili. Kwa hiyo Yehova alikuwa na sababu nzuri ya kuagiza kivulana aitwe Lo-ami, kwa maana jina hilo lamaanisha “Si Watu Wangu.” Lilikuwa na maana ya unabii. Alipokuwa akieleza sababu ya kumpa kivulana jina hilo la kuogofya, Yehova aliiambia hivi “nyumba ya Israeli” ya makabila kumi: “Kwa maana ninyi si watu wangu, wala mimi sitakuwa Mungu wenu.” Kwa kusema hayo Yehova alijitangaza kutokuwa tena Mume wa Kimbinguni wa “nyumba ya Israeli” yenye kuvunja agano.

18. Ni wakati gani na kwa njia gani Yehova alijulisha kwamba ufalme wa Israeli wa makabila kumi haukuwa watu wake?

18 Yehova aliacha ikajulikana wazi kwamba yeye hakuwa tena Mungu wala Mume wa kiroho wa “nyumba ya Israeli” yenye kuasi imani. Yehova alifanya hivyo alipoacha mji mkuu wa Israeli Samaria utekwe na Waashuru mwaka wa 740 K.W.K. Hivyo hiyo “nyumba ya Israeli” haikuwa tena watu Wake; ilikuwa Lo-ami, au, “Si Watu Wangu,” kama alivyosema. Kama mke aliyetalikiwa, watu hao walipelekwa uhamishoni Ashuru. Hiyo “nyumba ya Israeli” yenye kufanya uzinzi ilidharau nafasi iliyopewa katika agano la Torati la Musa ya kuwa “ufalme wa makuhani” kwa Yehova.​—Kut. 19:5, 6.

19. Yesu Kristo atajulisha Jumuiya ya Wakristo kwamba haishiriki kutimiza kusudi la agano Jipya wakati maneno gani yake yatakapotimia?

19 “Agano jipya” la Yehova lililopatanishwa na Yesu Kristo Musa Mkuu, lina kusudi kama hilo. Kusudi hilo halitatimizwa katika Jumuiya ya Wakristo ya kisasa, iliyo kama Israeli ya kale. Jumuiya hiyo imejaribu kutawala duniani katika taratibu iliyopo ya mambo kwa kutumikia kama mke wa kidini wa watawala wa kisiasa wa ulimwengu huu. Yesu Kristo ataijulisha jumuiya hiyo kwamba si yenye urithi pamoja naye katika ufalme wa kimbinguni, wakati maneno yake yatakapotimia: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.”​—Mt. 7:21-23.

TUMAINI LA KUPATA REHEMA YA KIMUNGU KWA WATU MMOJA MMOJA

20, 21. (a) Ni wakati gani watu mmoja mmoja wa “nyumba ya Israeli” iliyohamishwa waliporuhusiwa kujifaidi na rehema ya Yehova, na kwa njia gani? (b) Yehova alitaja jambo hilo kwa kusemaje katika Hosea 1:10, 11?

20 Ufalme wa Israeli wa makabila kumi, uliokuwa mfano wa Jumuiya ya Wakristo, haukuanzwa tena katika nchi waliyopewa na Mungu katika Mashariki ya Kati. Hata hivyo, washiriki mmoja mmoja wa hiyo “nyumba ya Israeli” iliyokataliwa waliruhusiwa kujifaidi na rehema ya Yehova na kumrudia wawe sehemu ya watu wake wanaokubaliwa. Wangekuwa na pendeleo hilo wakati mamlaka iliyofuata Ashuru, Mamlaka ya Ulimwengu ya Babeli, ingepinduliwa. Ndipo Koreshi Mshindi angefungua waabudu waliohamishwa wa Mungu wa Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Akitaja jambo hilo, Yehova aliendelea kusema hivi kupitia kwa nabii wake Hosea:

21 “Tena itakuwa ya kwamba hesabu ya wana wa Israeli itafanana na mchanga wa bahari, usioweza kupimwa wala kuhesabiwa; tena itakuwa, badala ya kuambiwa, Ninyi si watu wangu, wataambiwa, Ninyi ndio wana wa Mungu aliye hai. Na wana wa Yuda na wana wa Israeli watakusanyika pamoja, nao watajiwekea kichwa kimoja, nao watakwea watoke katika nchi hii; kwa maana siku ya Yezreeli [Mungu Atapanda] itakuwa kuu sana.”​—Hos. 1:10, 11.

22. Unabii huo ulitimizwa kwa halisi wakati gani, nayo “siku ya Yezreeli” ilipataje kuwa “kuu sana” kwao?

22 Utimizo halisi wa unabii huo wenye rehema ulitukia mwaka wa 537 K.W.K., wakati mwenye kushinda Babeli, Koreshi Mwajemi, alipoacha mabaki yenye uaminifu ya “wana wa Yuda na wana wa Israeli” waondoke Babeli, nchi ya uhamisho. Walitoka kwa umoja wakajenge upya hekalu la Yehova Yerusalemu, wakiwa chini ya maagizo ya Koreshi mtumishi wa Yehova. (2 Nya. 36:20-23; Ezra 1:1-11) Wakati huo mabaki wangeweza kuongezeka sana tena katika nchi yao, wakiwa kama chembe za mchanga wa pwani zisizopimwa, zisizohesabiwa. Kwa njia hiyo ‘siku ya Yezreeli ingekuwa kuu sana.’ Hapa jina Yezreeli, linalomaanisha “Mungu Atapanda,” litatimizwa kwa njia ya kufaa. Mungu hupanda wana wa watu wake waliorudishwa kama mbegu, akiwazidisha.

23. (a) Taifa la Israeli liliacha kuwa watu wa Yehova baada ya Yeye kukataa nani, na kwa kuchukua hatua gani? (b) Yehova alionyesha rehema juu ya nani wa taifa hilo alilolikataa, na kwa njia gani?

23 Kwa hiyo, Yehova asingewaita tena Lo-ami, au, “Si Watu Wangu.” Kwa njia halisi wangeitwa “wana wa Mungu aliye hai.” Katika Warumi 9:25, 26 na 1 Petro 2:9, 10 mitume Paulo na Petro waliandika wakitaja Wakristo wale waliofananishwa na wana hao. Wana wa asili wa Israeli walipomkataa Yesu kama Masihi mwaka wa 33 W.K., walikoma kuwa watu wa Yehova. Yeye alifuta agano la Torati ambalo kwalo alikuwa amelioa taifa la Israeli la makabila kumi na mawili siku za Musa. Lakini kwa rehema alikubali mabaki wenye imani wa taifa la Israeli wa asili akawaingiza katika agano jipya lililopatanishwa na Mwanawe, Yesu Masihi. Kwa njia hiyo alianza taifa jipya, Israeli wa kiroho.​—Gal. 6:16; Yak. 1:1; Rum. 2:28, 29; Ufu. 7:4-8.

24. Ni kwa sababu gani na wakati gani Yehova aligeukia wale wasiokuwa kamwe watu wake, naye aliwafanyaje watu wake?

24 Linalosikitisha ni kwamba, Waisraeli wengi wa asili hawakuwa Wakristo wenye kutimiza hesabu ya “uzao wa Ibrahimu” ambao katika huo mataifa yote ya kidunia yatabarikiwa. Kwa hiyo Yehova aligeukia wale wasiopata kamwe kuwa watu Wake, watu ambao “Si Watu Wangu,” Lo-ami. Alifungulia waaminifu wasio Waisraeli njia mwaka wa 36 W.K., wawe sehemu ya Israeli wa kiroho katika agano jipya. Walifanywa sehemu ya “uzao wa Ibrahimu.” ambao ungekuwa kama mchanga ulioko pwani.​—Gal. 3:8-29; Mwa. 22:18.

25. (a) Ni nani “kichwa kimoja” ambaye mabaki ya Israeli wa kiroho ‘waliokusanywa namoja’ ‘wangejiwekea,’ na ni ukombozi gani ungetokea? (b) Ni nani wanaotazamia kuokoka vita katika Har–​Magedoni pamoja na mabaki hao?

25 “Kichwa kimoja” ambacho Waisraeli wa kiroho ‘waliokusanywa pamoja’ ‘wangejiwekea’ ni Yesu Kristo, Mfalme anayetawala sasa. Mabaki wenye kutubu walikombolewa kutoka mamlaka ya Babeli Mkuu mwaka wa 1919 W.K., baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, kupitia kwake huyo aliye Koreshi Mkuu. Mabaki hao walitumiwa kurudisha duniani ibada safi ya Yehova. Yehova amewafanya Waisraeli hao wa kiroho waliokombolewa “wana wa Mungu aliye hai.” Kulingana na rehema yake wanatazamia kuokolewa katika “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” inayokaribia katika Har–​Magedoni, naam, waendelee kuishi na kuiona Taratibu Mpya yake ikianza. “Mkutano mkubwa” wa waabudu wenzao wanatazamia pia kupokea rehema ya Mungu na kuokoka pamoja na mabaki, kama Warekabu wa kale.

26, 27. (a) Lazima wale wanaoitumainia rehema ya Mungu sasa watambue Jumuiya ya Wakristo ikoje kiroho, na kwa sababu gani hawataki kuwa “watoto” wake? (b) Yehova anawaagiza wawaambie nini wale walio vyombo vya rehema yake?

26 Je! sisi leo twaitumainia rehema ya Yehova? Ikiwa ndivyo, lazima tutambue kwamba Jumuiya ya Wakristo ni mwasherati-mke wa kiroho. Kwa kujichafua na dini ya Kibabeli, imejifanya sehemu ya Babeli Mkuu. Itaharibiwa pamoja na milki hiyo ya ulimwengu ya dini ya uongo katika “dhiki kubwa” inayokuja. Hatutaki kuwa ‘watoto wa uasherati’ wake. Sisi kama vyombo vya rehema ya Yehova twataka kutenda kama Yeye anavyotuagiza sasa:

27 “Waambieni ndugu zenu wanaume, [Watu wangu]; na ndugu zenu wanawake Ruhama [neno la Kiebrania linalomaanisha mwanamke aliyeonyeshwa rehema]. Msihini mama yenu, msihini; kwa maana yeye si mke wangu, wala mimi si mume wake; na ayawekee mbali mambo ya uasherati wake yasiwe mbele ya uso wake, na mambo ya uzinzi wake yasiwe kati ya maziwa yake; nisije nikamvua nguo zake akawa uchi, nikamweka katika hali aliyokuwa nayo siku ya kuzaliwa kwake, na kumfanya kama jangwa, na kumweka kama nchi kame, na kumfisha kwa kiu; naam, sitawaonea rehema watoto wake; kwa maana ni watoto wa uzinzi. Maana mama yao amezini; yeye aliyewachukua mimba ametenda mambo ya aibu; maana alisema, Nitafuatana na wapenzi wangu, wanipao chakula changu na maji yangu, sufu yangu na kitani yangu, mafuta yangu na vileo vyangu.”​—Hos. 2:1-5.

28. Tutakuwa watii kwa kuunga Yehova mkono katika kesi gani mbele ya ulimwengu wote, na kwa hiyo tutakubali hatua gani atakayochukua katika “dhiki kubwa”?

28 Kwa kutii, basi, acheni tumwunge mkono Yehova Mume wa Kimbinguni anapoendesha kesi yake juu ya Jumuiya ya Wakristo, inayojidai kwa unafiki kuwa katika uhusiano wa agano pamoja naye ikiwa mke wake. Acheni tuonyeshe mbele za Mahakma Iliyo Kuu Zaidi ya ulimwengu wote kwamba jumuiya ‘hiyo ina hatia ya uasherati wa kiroho, uzinzi, kwa kujifanya rafiki ya ulimwengu. (Yak. 4:4) Imefuata walimwengu wenye vyeo vikubwa, walio mashuhuri na matajiri, wapate kutosheleza tamaa zake za kichoyo za kutaka vitu vya kimwili. Ijapokuwa imeonywa kwa upole na Mungu imekuwa shupavu ikakataa kutoa uasherati wake mbele ya uso wake na uzinzi wake kati ya maziwa (matiti) yake. Watoto wake wa kidini, washiriki wake wa makanisa, ni ‘wana wa uasherati’ wa kiroho. Sisi tutakubaliana na Yehova kwa moyo atakapoagiza jumuiya hiyo iharibiwe katika “dhiki kubwa.”

29. Imetupasa tuwe na uhusiano wa kijamaa na nani, nasi twaweza kutumainia kuonyeshwa rehema zaidi ya Yehova wakati wa vita gani inayokuja?

29 Acheni tujione kuwa ndugu za wale tunaotambua kulingana na Maandiko kuwa ni watu wa Yehova, ambao yeye awasema kuwa “watu wangu!” Acheni tujione kuwa na uhusiano wa kijamaa, kama unaokuwa kati ya dada na dada, pamoja na tengenezo jaminifu la kweli lililosafishwa ambalo Yehova ameonyesha rehema katika huu “wakati wa mwisho” wa historia ya ulimwengu huu kabla ya “dhiki kubwa” inayokaribia sana. (Mt. 24:21, 22; Ufu. 7:14) Acheni tulitambue tengenezo hilo kuwa ndiye Ruhama wa kisasa na kuliambia, “Ewe mwanamke uliyeonyeshwa rehema!” (Hos. 2:1, NW) Tukifanya hivyo kwa unyofu tunaweza kutumainia kuonyeshwa rehema zaidi na Yehova, atakapoionyesha kwa watu wake wanaostahili wakati wa “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” mahali panapoitwa kwa Kiebrania Har–​Magedoni.​—Ufu. 16:14, 16. (Itaendelezwa)

​—Kutoka The Watchtower, March 1, 1976.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama pia An American Translation; Leeser; English Revised Version; Revised Standard Version.

b Tazama makala “Kukombolewa Kunakokuja na Shoka Lenye Kupinga Dini,” katika toleo la Julai 15, 1976 la Mnara wa Mlinzi.

[Chati katika ukurasa wa 404]

ULINGANIFU WA UNABII

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Ndoa ya Hosea na Gomeri

Ndoa ya Yehova na Israeli 1513 K.W.K.

Ndoa ya Yehova na Israeli wa kiroho 33 K.W.K.

‘Uasherati’

Kugeukia ibada ya miungu ya uongo kwa ufasadi

Kuwa rafiki ya ulimwengu chini ya mungu wake, Shetani

Yezreeli (Mungu Atapanda)

Yehova kutawanya, aharibu ufalme wa Israeli wa makabila kumi mwaka wa 740 K.W.K.

Jumuiya ya Wakristo, haitaonyeshwa tena rehema na Mungu bali itaharibiwa

Lo-ruhama (Asiyehurumiwa)

Ufalme wa Israeli wa makabila kumi usioaminika, wakataliwa na Yehova

Jumuiya ya wakristo, haitaonyeshwa tena rehema na Mungu bali itaharibiwa

Nyumba ya Yuda yaokolewa

Yerusalemu, mji mkuu wa ufalme wa makabila mawili waokolewa na Yehova wasishambuliwe na adui Waashuru (Warekabu waliachiliwa pia)

Mabaki ya Israeli wa kiroho wakombolewa na Yehova katika Har–​Magedoni (“mkutano mkubwa” wataachiliwa pia)

Lo-ami (Si Watu Wangu)

Ufalme wa Israeli wa makabila kumi wenye kuvunja agano

Jumuiya ya Wakristo, haina uaminifu kwa Mfanya “agano jipya”

Zamani “si watu wangu,” lakini sasa ni “wana wa Mungu aliye hai”

Waisraeli warudishwa kutoka uhamishoni babeli 537 K.W.K.

Waamini wa Mataifa yasiyo ya Kiyahudi wawa sehemu ya Israeli wa kiroho, kuanzia 36 W.K; Waisraeli wa kiroho warudishwa 1919 W.K.

“Kichwa kimoja”

Mfalme Koreshi

Yesu Kristo

“Siku ya Yezreeli itakuwa kuu sana”

Mungu azidisha Waisraeli waliorudishwa

Tangu 1919 W.K. Yehova amepanda watu wake waliorudishwa, akawazidisha

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki