Rehema ya Mungu Kwa Wanadamu Katika Karne Yetu ya Ishirini
“Ni kama vile alivyosema katika Hosea, Nitawaita watu wangu wale wasiokuwa watu wangu, na mpenzi wangu yeye asiyekuwa mpenzi wangu. Tena itakuwa mahali pale walipoambiwa, Ninyi si watu wangu, hapo wataitwa wana wa Mungu aliye hai.”—Rum. 9:25, 26.
1. Wake wanaweza kufurahia rehema gani wanayoonyeshwa na waume zao?
SOTE tunafurahi kwamba wakati wa kuzaliwa kwetu wazazi wetu waliturehemu tulipokuwa hatujiwezi. Wake huwa wenye furaha wakati waume zao wanapowarehemu kwa sababu ya udhaifu wa kike, kuchafuka kwa moyo na fikira zao za kudhania mambo yasivyo. Wake hao wanaweza kufahamu kwamba ombi la kuonyesha rehema lililotolewa karne kumi na tisa zilizopita linafaa hata leo: “Ninyi waume, kaeni na wake zenu kwa akili; na kumpa mke heshima, kama chombo kisicho na nguvu; na kama warithi pamoja wa neema ya uzima.”—1 Pet. 3:7.
2. Kwa sababu gani wengine hawafurahii rehema ya Mungu leo, wakidhani wana rehema zaidi kuliko yeye?
2 Wako watu wengine wanaojaribu kutumia katika maisha zao maneno yaliyotolewa katika Mahubiri juu ya Mlima yanayojulikana sana: “Heri wenye rehema; maana hao watapata rehema.” (Mt. 5:7) Wao ni wenye furaha kwa sababu wanamwiga Muumba wa wanadamu kwa kuonyesha rehema kwa taifa letu potovu. Wengine wenye kuongezeka wanatia shaka kama rehema ni mojawapo ya sifa za Muumba. Wanalalamika wakisema: “Ikiwa kuna Mungu, sababu gani anauruhusu uovu wote huu na kuacha nyakati kama hizi zenye magumu ziweko duniani? Ikiwa yeye ni mwenye nguvu zote, kwa sababu gani haonyeshi rehema na kuzikomesha zote atuache tufurahie maisha?” Walalamikaji hao wanajiacha waamini kisio lenye kushtusha la kwamba, “Mungu amekufa!” Yaani, “amekufa” katika maana ya kwamba haonyeshi rehema kwa wanadamu. Huenda wakakata shauri kwamba wao wenyewe hurehemu zaidi watu wengine kuliko Mungu huyo ‘aliyekufa.’ Hawaoni ushuhuda wo wote wa rehema ya Mungu katika karne yetu ya 20.
3. Ni kwa njia gani Mungu amekuwa na kusudi lenye rehema kwetu kwa kuvumilia uovu mpaka sasa?
3 Walakini, je! tumepata kusimama tufikiri kama kuruhusu kwa Mungu uovu na maisha magumu hivyo kuna sababu yenye rehema? Kama Mungu asingaliuvumilia uovu, asingalionyesha rehema kwa utaratibu. Je! uovu haukukaa duniani hapa kwa maelfu ya miaka kabla sisi hatujazaliwa? Ndiyo! Kwa hiyo, kama Mungu Mwenye Nguvu Zote angaliukomesha uovu huo kabla hatujazaliwa, tungalikuwa hai leo?
4. Tutashukuru wanadamu gani wanane kwa uhai tulio nao leo, na kwa sababu gani?
4 Tunapochunguza maandishi ya kweli ya historia tunaona kwamba Muumba wa mbingu na dunia alikomesha jeuri na uovu uliokuwapo ulimwenguni pote zaidi ya karne 40 zilizopita, mwaka wa 2370 K.W.K. Alileta gharika ya dunia yote na ni wanadamu wanane tu waliookoka wakiwa katika safina kubwa sana isiyopenywa na maji. Makumi ya maelfu ya jamaa zisizoingia katika safina aliyojenga Nuhu pamoja na wana wake watatu zilikatiliwa mbali na msiba huo mkubwa wa ulimwengu. Nuhu, Shemu, Hamu na Yafethi pamoja na wake zao waaminifu ndio imetupasa tushukuru kwa sababu tu hai leo katika karne hii ya 20.—Mwa. 6:1 mpaka 9:19.
5, 6. (a) Sasa ni ulizo gani linalotokea juu ya muda wa rehema ya Mungu? (b) Paulo atupa maoni gani yaliyosawazika katika Warumi 9:21-26?
5 Basi, twaweza kuuona uhai wetu leo kama ushuhuda wa rehema ya Mungu, sivyo? Naam, tunaonyeshwa “rehema” ijapokuwa jeuri ipo na uasi unaongezeka katika karne yetu ya 20. Lakini sasa ulizo kubwa ni hili: Ni kwa muda gani Mungu ataendelea kuvumilia uovu duniani pote kwa ajili ya wenye kutumia kwa faida saburi na rehema yake? Si kwa muda mrefu sana, kulingana na vionyesho vyote vya Biblia. Kwa hiyo, tusilalamike juu ya kuruhusiwa kwa uovu duniani na Mungu. Bali, na tutumie kwa faida rehema ya kimungu. Tukifanya hivyo, Mungu hatakomesha uhai wetu karibuni atakapoukomesha uovu wote uliomo kati ya wanadamu. Kwa rehema atatuingiza katika taratibu mpya yenye haki na amani hapa duniani. Kwa hiyo, na tuwe na maoni yaliyosawazika kama aliyokuwa nayo mtume Mkristo Paulo, alipoandika hivi:
6 “Au mfinyanzi je! hana amri juu ya udongo, kwa fungu moja la udongo kuumba chombo kimoja kiwe cha heshima, na kimoja kiwe hakina heshima? Ni nini basi, ikiwa Mungu kwa kutaka kuonyesha ghadhabu yake, na kuudhihirisha uweza wake, kwa uvumilivu mwingi, alichukuliana na vile vyombo vya ghadhabu vilivyofanywa tayari kwa uharibifu; tena, ili audhihirishe wingi wa utukufu wake katika vile vyombo vya rehema, alivyovitengeneza tangu zamani vipate utukufu; ndio sisi aliotuita, si watu wa Wayahudi tu, ila na watu wa Mataifa [yasiyo ya Kiyahudi] pia? Ni kama vile alivyosema katika Hosea, Nitawaita watu wangu wale wasiokuwa watu wangu, na mpenzi wangu yeye asiyekuwa mpenzi wangu. Tena itakuwa mahali pale walipoambiwa, Ninyi si watu wangu, hapo wataitwa wana wa Mungu aliye hai.”—Rum. 9:21-26; angalia pia 1 Petro 2:9, 10.
TATIZO LA NDOA YA MUNGU MWENYEWE
7. Hosea alikuwa nani, naye Paulo alitaja maneno yake kutoka tafsiri gani?
7 Hosea huyo alikuwa nani, ambaye mtume Paulo alitaja maneno yake? Alikuwa nabii wakati wa karne za tisa na nane kabla ya Wakati wetu wa Kawaida. Mtume Paulo alitaja maneno yake kutokana na tafsiri za Hosea 1:10 na 2:23 katika Septuagint Version ya Kigiriki. Humo twasoma hivi: “Lakini itakuwa kwamba katika mahali ambamo waliambiwa, Ninyi si watu Wangu, wataitwa watoto wa Mungu Aliye Hai.” “Nami nitampanda mwanamke huyo kwa ajili Yangu mwenyewe katika nchi hiyo na kumpenda mwanamke huyo asiyependwa; nao wasiokuwa watu Wangu nitawaambia, Ninyi m watu Wangu: nao watasema, Wewe Bwana ndiwe Mungu wangu.”—The Septuagint Bible iliyotafsiriwa na Charles Thomson.
8. Kulingana na maneno aliyosema kupitia kwa Hosea, Yehova alimaanisha tatizo la namna gani lilikuwa kati yake na yule asiye mpenzi?
8 Yehova Mungu ndiye anayesema hivyo kwa kumtumia nabii Mwebrania Hosea kama mnenaji Wake. Aliposema, ‘Nitampenda mwanamke huyo asiyependwa,’ au, ‘Nitamwita mpenzi wangu yeye asiyekuwa mpenzi wangu,’ Yehova alimaanisha kwamba kulikuwa kumekuwa na tatizo kati yake na mwanamke asiyekuwa mpenzi wake kwa muda fulani. Kulingana na vile Yehova anavyolisema jambo hilo, lilikuwa tatizo la ndoa kati yake na mwanamke huyo. Anamfananisha mwanamke huyo na mke wa mwanadamu.
9. Ni nani yule ambaye Yehova asema amemwoa?
9 Ni nani ambaye Yehova asema amemwoa? Si mwanamke halisi. Kulingana na maneno ya Yehova mwenyewe, yeye anaonyesha mwanamke huyo ni taifa, taifa la Israeli lililotokana na wazee wa ukoo Ibrahimu, Isaka na Yakobo. Kwa hiyo huyo ni mke aliye taifa, mke aliye tengenezo. Yehova alikuwa amelioa tengenezo la makabila kumi na mawili ya Israeli. Taifa la makabila kumi na mawili ya Israeli lilikuwa limeolewa na Mungu wake, Yehova, kama mke mwenye kununuliwa wa Mashariki ya Kati.
10. Ni wakati gani, wapi na namna gani ndoa hii ya mfano ilifanywa?
10 Ndoa hiyo ilifanywa wakati gani? Huo ulikuwa mwaka wa 1513 K.W.K., baada ya Yehova kuyanunua makabila kumi na mawili ya Israeli. Kwa njia gani? Kwa kuwakomboa utumwani katika nchi ya Misri. Wakati huo, Yehova aliwaleta kwenye Mlima Sinai katika Mkono wa nchi wa Uarabu, wakiongozwa na nabii mwenye kuonekana kwa macho, Musa. Yehova alimtumia Musa kama mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu kuanzisha kifungo cha umoja huko kati yake mwenyewe na Waisraeli aliokomboa. Alipendekeza wafanye agano pamoja naye. Agano hilo lingetegemea orodha ya sheria ambayo taifa la Israeli lingekubali kutii, kama vile siku hizo mwanamke alivyokuwa mtii kwa sheria ya mumewe. (Rum. 7:2) Akiwa juu ya Mlima Sinai Yehova aliwaambia Waisraeli hivi: “Sasa basi ikiwa mtaitii sauti yangu kweli kweli, na kulishika agano langu, hapo ndipo mtakapokuwa tunu kwangu kuliko makabila yote ya watu; maana dunia yote pia ni mali yangu, nanyi mtakuwa kwangu ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kut. 19:1-6) Baada ya kupashwa sawasawa habari zilizohusika, Waisraeli waliingia katika agano hilo kwa hiari.
11. Ni kwa njia gani taifa la Israeli lilipaswa kuendelea kufungwa pamoja na Yehova katika ndoa hiyo?
11 Kwa njia hiyo, huko katika jangwa la Sinai, ndoa ilifanywa Yehova akiwa ndiye Mume wa Kimbinguni na taifa la Israeli likiwa mke-tengenezo wake wa kidunia. Uhusiano huo mtakatifu ulianzishwa kwa kumwaga damu ya dhabihu za wanyama. Sehemu ya damu hiyo ilinyunyizwa juu ya kitabu cha sheria ya Mungu na sehemu nyingine juu ya Waisraeli. (Kut. 24:1-8; Ebr. 9:19, 20) Tangu wakati huo, kadiri agano la Torati lilivyoendelea kutumika, Waisraeli walipaswa kuwa waaminifu na wanyofu kwa Yehova Mungu wao, kama vile mwanamke anavyopaswa kuwa mwaminifu na mnyofu kwa mume wake. Kulingana na Amri Kumi, walipaswa kumwabudu Yehova kama Mungu wao bila kutumia sanamu zo zote. (Kut. 20:1-6) Walipaswa kujichukua kama “tunu” yake, kama mali isiyo ya mtu mwingine ye yote. Walipaswa kuendelea kuwa taifa takatifu kwa Yehova, lililo kando na mataifa ya kilimwengu. Kwa kufuata mwendo huo wangefanya kifungo cha ndoa kiwe imara, kisichochafuliwa.—Yer. 2:2, 3; 31:31, 32.
12. Kwa sababu gani ni jambo la maana tufikirie ndoa ya kale iliyokuwa kati ya Yehova na taifa la Israeli na kitu cha kisasa kinacholingana na taifa hilo?
12 Leo ndoa za kisheria zinavunjika sana, ingawa ni za watu wawili, mwanamume na mwanamke. Kwa hiyo, je! ndoa kati ya Yehova na taifa zima la mamilioni ya watu ingeendeleaje? Yatupasa tupendezwe na habari hiyo leo, kwa maana lililoipata ndoa hiyo ya kale lilifananisha jambo litakalopata ndoa ya namna hiyo baadaye. Lililoipata ndoa ya Yehova na Israeli lilihusu taifa moja tu. Lakini litakaloipata ndoa yake ya baadaye litahusu ulimwengu mzima wa kidini, naam, litaihusu jamaa nzima ya kibinadamu. Hiyo yamaanisha kwamba sisi leo tunahusika. Kwa hiyo, huenda sote tukapatwa na mabaya wakati ujao ulio karibu. Ndiyo sababu ni jambo la maana kwetu kuifikiria ndoa hiyo ya kale kati ya Yehova na Israeli na ndoa ya kisasa iliyo kama hiyo ya zamani.
HOSEA ATUMIWA KUFANANISHA MAMBO
13. Kwa sababu gani ufalme wa Israeli ulihamishwa kutoka jamaa ya Sauli ukapelekwa kwa jamaa ya Daudi, nao ukoo wa kifalme wa Daudi ungekoma nani akitokea?
13 Baada ya karne kadha taifa la Israeli halikuridhika kuwa na Yehova tu kama Mume wa Kimbinguni na Mfalme wao asiyeonekana. Kwa hiyo, mwaka wa 1117 K.W.K. yeye alitoa ruhusa Sauli wa kabila la Benyamini atiwe mafuta awe mfalme wao wa kwanza wa kibinadamu, kulingana na ombi lao. Sauli akawa asiyeaminika kwa Yehova. Kwa hiyo jamaa yake haikuruhusiwa iendelee kutawala Israeli yote. Yehova aliuhamisha ufalme akampa Daudi mwana wa Yese wa kabila la Yuda, Mwaka wa 1077 K.W.K. Daudi alianza kutawala. Mwaka wa 1070 K.W.K. aliufanya Yerusalemu mji mkuu juu ya makabila kumi na mawili yote ya Israeli. Kwa kuwa Daudi aliendelea kuwa mwaminifu kwa ibada inayofaa, Yehova alifanya agano zito naye la kuendeleza ufalme wa milele katika jamaa yake. Kwa hiyo ukoo wa kifalme wa Daudi ungemtokeza Masihi, atakayekuwa mfalme wa milele.—Matendo 13:20-24; 2 Sam. 7:1-17.
14, 15. (a) Ni kwa sababu gani na wakati gani ufalme wa ukoo wa Mfalme Daudi kupitia kwa Sulemani ulipunguzwa? (b) Ni kwa njia gani ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulifanya uzinzi, nao ulijishikamanisha na mungu gani?
14 Mrithi wa kwanza wa Daudi, Mfalme Sulemani, alipata kuwa mpumbavu mwishowe kwa kuiacha ibada safi ya Yehova Mungu. Aliadhibiwa na Mungu, ufalme wa warithi wake ukapunguzwa ukawa wa makabila mawili, Yuda na Benyamini, baada ya mwana wa Mfalme Sulemani Rehoboamu kukalia kiti cha enzi. Ndipo makabila kumi yalipojitenga yakaanza ufalme wa kujitegemea, Yeroboamu mwana wa Nebati akiwa ndiye mfalme. Mfalme huyo mwasi alianzisha ibada tofauti na ibada ya Yehova iliyokuwa katika hekalu la Sulemani Yerusalemu. Aliugeuza ufalme wa Israeli wa makabila kumi uabudu ndama wawili wa dhahabu, mmoja akiwa Betheli na yule mwingine Dani. Siku za Omri, mfalme wa saba wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi, mji wa Samaria ulijengwa ukawa mji mkuu wa taifa hilo.
15 Katika Samaria mwana wa Mfalme Omri Ahabu alianzisha ibada ya mungu wa Sidoni Baali akamjengea Baali hekalu huko. (1 Fal. 16:23-33) Kwa kufuata mwendo huo wa kutoaminika ufalme wa makabila kumi ulimwacha Mume wa Kimbinguni wa Israeli wote ukajishikamanisha kwa ufisadi na mungu wa uongo Baali awe mume wa taifa.—Hos. 9:10.
16. Wafalme wa ufalme wa Yuda kufika kwa Hezekia walijiongozaje kwa mambo ya dini?
16 Namna gani wafalme wa ufalme wa makabila mawili wa Yuda? Wao walisita-sita kuamua kati ya kufuata ibada safi ya Yehova na kushikamana na miungu ya uongo. Mfalme Ahazi, mfalme wa kumi na mbili anapohesabiwa kuanzia Daudi, aligeukia ibada ya uongo. Hata aliifunga milango ya hekalu la Yehova Yerusalemu. Lakini mwanawe, Mfalme Hezekia, alifungua tena milango ya hekalu akarudishia ufalme wa Yuda ibada safi. Hosea aliwafaidi sana kwa kuendelea kutoa unabii mpaka utawala wa Mfalme Hezekia. Nabii huyo aliishi wakati kulipokuwa na mambo yale yale aliyokuwa akisema.
JE! NI MGAWO WA KUCHUKIZA WA UTUMISHI?
17, 18. Hosea alipewa mgawo wa namna gani na kwa sababu gani sisi tunajua mambo anayotueleza ya mgawo huo si uongo?
17 Sisi tungeonaje tukitimiza umri wa kuoa kisha baba zetu wanaotupangia ndoa watuagize tuoe mwanamke ambaye tumeambiwa atakosa kuwa mwaminifu, atakuwa mzinzi na mwishowe atuache awe mpenzi wa mtu mwingine? Twaweza kuchukia hilo, sivyo? Lakini Hosea alipatwa na jambo kama hilo. Si jambo la kuwazia, si uongo, si hadithi!
18 Hosea, ambaye ni mtu aliyeishi kweli, anatueleza mambo ya hakika katika kitabu cha unabii chenye jina lake. Anahakikishwa kuwa msema kweli kwa sababu ametajwa mara zisizopungua saba katika maandiko ya baadaye yaliyoongozwa na Mungu, kutoka Mathayo mpaka Ufunuo.a Anatajwa hata na Mwanzishi wa Ukristo mwenyewe. Kwa hiyo, Hosea anapotueleza habari za mgawo wake wa utumishi akiwa nabii wa Yehova, tuna sababu kamili ya kuamini anatuambia kweli tupu, badala ya kutusimulia hadithi ya kutunga afurahishe wasomaji wa vitabu vya mambo ya umalaya. Vilevile, maana ya unabii ya mwendo wa Hosea inakuwa kweli sana kwa sababu inapatana na mambo yaliyopata taifa lililopo hata sasa.
19. Hosea asema kazi yake ya unabii ilikuwa wakati wa tawala za wafalme gani wa Yuda na wa Israeli?
19 Anapotaja kipindi hasa alichoishi katika historia iliyoandikwa ya makabila kumi na mawili ya Israeli, Hosea aanza kueleza habari zake kwa kusema: “Hili ndilo neno la [Yehova] lililomjia Hosea, mwana wa Beeri, siku za Uzia, na Yothamu, na Ahazi, na Hezekia, wafalme wa Yuda; na siku za Yeroboamu, mwana wa Yoashi, mfalme wa Israeli.” (Hos. 1:1) Uzia, Yothamu, Ahazi na Hezekia walikuwa wazao wa Mfalme Daudi nao waliutawala ufalme wa Yuda wa makabila mawili wakiwa Yerusalemu. Uzia alianza kutawala mwaka wa 829 K.W.K. naye Hezekia aliacha kutawala mwaka wa 716 K.W.K. Kwa hiyo tawala za wafalme hao zilikuwa za miaka 113 zikiunganishwa pamoja. Kwa upande mwingine, Yeroboamu mwana wa Yoashi ndiye aliyekuwa wa pili kuwa na jina hilo na hivyo alikuwa Yeroboamu wa Pili, akiwa katika ukoo wa wafalme walioutawala ufalme wa Israeli wa makabila kumi.
20. Yeroboamu wa Pili alikuwa mjukuu wa nani, naye Hosea alianza kazi yake ya unabii wakati gani wa utawala wa mfalme huyo?
20 Babu mkubwa wa Yeroboamu huyo alikuwa Mfalme Yehu mwana wa Nimshi. Yehu aliharibu ibada ya Baali katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Aliagiza Malkia Yezebeli atupwe nje dirishani akafe, kwa maana alikuwa ameendeleza ibada ya Baali katika Israeli kwa njia mbaya sana. Baadaye Yeroboamu wa Pili akawa mfalme wakati Mfalme Amazia alipokuwa akitawala Yuda. Yeroboamu aliendelea kutawala hata Mfalme Uzia, mrithi wa Amazia, akamkuta akitawala. Kwa hiyo, wakati Yeroboamu alipokuwa akitawala Mfalme Uzia akiendelea bado na utawala wake, au baada ya mwaka wa 829 K.W.K., ndipo Yehova Mungu alipomwagiza Hosea aanze kazi yake ya unabii.
21. Yehova alimwagiza Hosea atwae mke wa namna gani, na kwa sababu gani?
21 Je! twaweza kuwaza vile Hosea alivyoona baada ya tukio analofuata kusimulia? “Hapo kwanza [Yehova] aliponena kwa kinywa cha Hosea, [Yehova] alimwambia Hosea, Enenda ukatwae mke wa uzinzi, na watoto wa uzinzi; kwa maana nchi hii inafanya uzinzi mwingi, kwa kumwacha [Yehova].”—Hos. 1:2.
22. Ni kwa njia gani mwanamke ambaye Hosea angetwaa alikuwa “mke wa uzinzi,” nao watoto wake wangekuwaje “watoto wa uzinzi,” na kwa sababu gani?
22 Je! tumeshtuka kwa sababu Hosea aliagizwa aanze kazi yake ya unabii kwa kupewa amri hiyo? Yehova hakuwa akimwamuru Hosea aoe mwanamke aliyekuwa malaya tayari. Mwanamke ambaye Hosea aliagizwa amtwae kama mke hakuitwa ‘mwanamke (au, mke) anayefanya uasherati,’ bali Yehova alimwita “mke wa uzinzi [kwa halisi, wa uasherati].” Tena, kwa kuwa mwanamke huyo angetumiwa kama mfano wa “mke” wa Yehova wa kidunia, asingemfananisha vizuri akiwa mwanamke mtembezi au malaya hapo mwanzoni. Yehova alioa “bikira,” mwanamke safi, ili amzalie watoto halali wa kiroho. Kwa hiyo usemi “watoto wa uzinzi [“watoto wa uasherati,” NW]” ni unabii wa namna ya “watoto” ambao Yeye angezaliwa kiroho, namna ya “watoto” ambao wangekuwa baadaye. Kwa sababu gani iwe hivyo? “Kwa maana,” asema Yehova, “nchi hii inafanya uzinzi [“uasherati,” NW] mwingi, kwa kumwacha [Yehova].” “Nchi” iliyomaanishwa hapa ilikuwa ya ufalme wa Israeli wa makabila kumi.
23. Hosea alitwaa nani akawa mke wake, naye alimzalia nini?
23 Ingawa wakati huo Hosea alikuwa na matumaini mabaya juu ya ndoa yake, aliitii amri ya kimungu. Alianza kazi yake akiwa nabii wa Yehova. “Basi akaenda akamwoa Gomeri, binti Diblaimu; naye akachukua mimba, akamzalia mtoto mwanamume.”—Hos. 1:3.
24. Yehova alisema kivulana aitwe nani, na kwa sababu gani?
24 Mwana huyo alikuwa mwana halali wa Hosea, wala hakuwa ‘mwana wa uzinzi’ aliyepaswa kulelewa na Hosea. Siku ya nane baada ya kuzaliwa mwana huyo, wakati ambao angetahiriwa, Hosea angempa jina gani? Jina la kivulana huyo lingekuwa na maana ya unabii; hivyo Yehova aliyekuwa akisimamia mfano huo wa unabii ndiye aliyemtafutia Hosea jina la mtoto. Jina hilo lingeonyesha mojawapo la makusudi ya Yehova. “[Yehova] akamwambia, Mwite jina lake Yezreeli; kwa maana bado kitambo kidogo, nitaipatiliza nyumba ya Yehu damu ya Yezreeli, na kuukomesha ufalme wa nyumba ya Israeli. Tena itakuwa siku ile, nitauvunja upinde wa Israeli katika bonde la Yezreeli.”—Hos. 1:4, 5.
25. (a) Hivyo mabaya yalitabiriwa kupata nyumba gani ya kifalme na taifa gani? (b) Ni kwa njia gani taifa la Israeli halikupaswa kufanya uzinzi wa kiroho Juu ya Yehova?
25 Hivyo mabaya yalitabiriwa kuipata nasaba ya kifalme ya Mfalme Yehu na ufalme mzima wa Israeli wa makabila kumi baada ya kizazi chake cha nne. Taifa hilo la kwanza la Israeli lilikuwa limeolewa kiroho na Yehova Mungu katika jangwa la Sinai huko nyuma mwaka wa 1513 K.W.K. Huo ndio wakati agano la Torati ya Musa lilipoanzishwa kati ya Israeli na Yehova. Kulingana na mapatano ya ndoa, taifa la Israeli la makabila kumi na mawili lilipaswa kuwa jaminifu na nyofu kwa Yehova kwa kumwabudu Yeye peke yake kama Mungu wao. Israeli hawakupaswa kuwa na hatia ya uzinzi kwa kumwacha yeye waabudu miungu ya uongo.
26. Mke wa Hosea alifananisha nani?
26 Ndoa ya Yehova na Israeli ilifananishwa na ndoa ya Hosea na Gomeri, ambaye jina lake lamaanisha “Kumalizika.” Kwa kufaa basi, Gomeri alifananisha taifa la Israeli; lakini siku za Hosea Israeli walifananishwa na sehemu ile yake ambayo ilipata kuwa ufalme wa Israeli wa makabila kumi tu. Baadaye, zaidi ya miaka 150 ya kutawala kwa ufalme huo, mambo katika “nchi” yalikuwa kama Yehova alivyosema: “Nchi hii inafanya uzinzi mwingi, kwa kumwacha [Yehova].”
27. Ingawa Israeli walikuwa na mwanzo safi, hali ya taifa ikawaje, kulingana na Hosea 10:1, 2?
27 Ingawa Israeli walikuwa wamekuwa na mwanzo safi wakiongozwa na nabii Musa, hali ya taifa hilo ilikuwa kama Yehova alivyomwongoza nabii wake kusema, katika Hosea 10:1, 2, NW: “Israeli ni mzabibu wenye kuharibika.b Anaendelea kujizalia matunda. [Israeli alikuwa mzabibu ovyo, naye alizaa sana. (Tafsiri ya Moffatt) ] Kwa kadiri ya wingi wa matunda yake amezidisha madhabahu zake. Kwa kadiri ya wema wa nchi yake, walisimamisha nguzo nzuri [mawe matakatifu (Moffatt)]. Moyo wao umekuwa mnafiki; sasa wataonekana wenye hatia.”
MAANA YA UNABII YA JINA “YEZREELI”
28. Jina Yezreeli lina maana gani, na kwa sababu gani lilimfaa mwana wa Hosea, kulingana na maana yake ya unabii?
28 Kwa sababu ya hatua ambayo Yehova alikusudia kuchukua juu ya Israeli mzinzi wa kiroho, Yehova alimwagiza Hosea amwite mwana wake wa kwanza, aliyezaliwa na Gomeri, Yezreeli. Jina hilo lilifaa sana. Katika lugha yake Hosea, Kiebrania, lilikuwa na maana ya “Mungu Atapanda [Mbegu].” Naam, ‘kupanda,’ lakini si kwa njia yenye mafaa. ‘Kupanda’ hapa kuna maana ya ‘kutawanya, kutapanya,’ kwa maana mtu apapopanda mbegu huitawanya. Hatua ya Yehova ya kutawanya “nyumba ya Yehu” ya kifalme ingekuwa na maana ya kuivunja, kuiharibu. Hatua kama hiyo juu ya ufalme wa Israeli wa makabila kumi ingemaanisha kuiharibu, kuivunja-vunja.—Linganisha Luka 22:31.
29. Mfalme Yehu alifanya nini juu ya ibada ya Baali, lakini alifanya nini juu ya ibada ya ndama, akavunja amri gani?
29 Makao ya kifalme ya Mfalme Ahabu wa Israeli yalikuwa mji wa Yezreeli, ingawa mji wake mkuu ulikuwa Samaria. Nasaba ya baadaye ya Mfalme Yehu ilikuwa na makao yake ya kifalme katika Yezreeli pia. Yehu alikuwa ameng’oa kwa nguvu ibada ya Baali katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi, kwa kutii agizo la Yehova Mungu. Hata hivyo, yeye aliendeleza ibada ya ndama wawili wa dhahabu bila kujali ibada ya Yehova Yerusalemu. Kwa kuendeleza ibada hiyo ya sanamu za kuchongwa nyumba ya Yehu ilivunja Amri Kumi. Walivunja pia amri ya kutoua.—Kut. 20:2-6, 13.
30. Yehova aliipatilizaje nyumba ya Yehu damu waliyomwaga Yezreeli?
30 Hivyo matendo ya umwagaji wa damu yalianza kutendwa na nasaba yenye kuabudu ndama ya Mfalme Yehu, nayo makao yao ya kifalme yalikuwa Yezreeli. Mpaji wa Amri Kumi asingeweza kuachilia matendo hayo. Kwa hiyo alisema hivi: “Nitaipatiliza nyumba ya Yehu damu ya Yezreeli.” (Hos. 1:4) Kulingana kabisa na maneno hayo, nasaba ya Mfalme Yehu iliyotawala Israeli ilikomeshwa kwa jeuri baada ya Zekaria, mwana wa Yeroboamu wa Pili, kutawala miezi sita tu. Aliuawa.—2 Fal. 15:8-12.
31. Utawala wa kifalme wa nyumba ya Israeli ulikomeshwaje, nao ulikuwaje kama “bonde la Yezreeli”?
31 Hivyo nasaba ya kifalme ya Mfalme Yehu iliyotawala Israeli ilikoma mwaka 791 K.W.K. Lakini ufalme wa Israeli wa makabila kumi uliendelea kuwako miaka 51 zaidi, mpaka mwaka wa 740 K.W.K. Ndipo Yehova ‘alipoukomesha ufalme wa nyumba ya Israeli.’ (Hos. 1:4) Alitumia Mamlaka ya Ulimwengu ya Ashuru kuuvunja “upinde [wa pigano] wa Israeli katika bonde la Yezreeli.” Taifa hilo lenye kuasi imani lilishushwa mji wao mkuu wa Samaria ulipopinduliwa. Uwezo wa taifa ulitawanywa waokokaji Waisraeli walipohamishwa wakapelekwa mikoa ya mbali ya Milki ya Ashuru, wakiwa wametawanywa kama mbegu. Mambo hayo mabaya sana yaliyowapata yalilingana na maana ya mfano ya maneno “bonde la Yezreeli [Mungu Atapanda Mbegu].” Hiyo haikuwa sawa na wakati mkombozi wa Israeli, Mwamuzi Gideoni, alipotawanya Wamidiani watekaji akiwa na mashujaa wateule 300 tu, karibu na Megido, karibu na “bonde la Yezreeli.” (Amu. 6:33, 34) Lakini mwaka wa 740 K.W.K., ufalme wa Israeli wa makabila kumi ‘ulikoma,’ ukatoweka usiwe na mkombozi wala uwezo wa kupigana uendelee kuwako.
32. Kwa sababu gani imetupasa tujaribu kufahamu katika karne yetu ya 20 maana ya mambo ambayo tumeona?
32 Je! tunafahamu maana ya jambo hilo kwetu leo? Yatupasa kufahamu, kwa maana katika karne yetu ya 20, linatimizwa katika kitu cha kisasa kilicho sawa na Israeli wenye uzinzi wa kiroho, wasioaminika. Kitu hicho ni Jumuiya ya Wakristo, yenye karibu washiriki wa kanisa mamilioni milioni moja (bilioni) duniani pote. Kwa kuwa Jumuiya ya Wakristo inakaribiwa na mabaya, twaweza kuuliza, Iko wapi, basi, rehema ya Yehova Mungu? Tukiendelea kuchunguza mambo ambayo Yehova alimtendea nabii wake Hosea tutafahamu wazi jambo hilo.
[Maelezo ya Chini]
a Angalia Mathayo 2:15; 9:13; 12:7; Luka 21:22; 23:30; Ufunuo 3:17; 6:8, 16, na kuzilinganisha na Hosea 11:1; 6:6; 9:7; 10:8; 12:8; 13:14.
b Tazama kitabu cha maneno au kamusi inayoitwa “Lexicon In Veteris Testimenti Libros,” iliyoandikwa na Koehler na Baumgartner, ukurasa 144, safu ya 2, mistari 9, 10.
[Chati katika ukurasa wa 397]
WAFALME WA YUDA NA WA ISRAELI WAKATI WA MAISHA YA HOSEA
(Yaonyesha Miaka ya Kutawazwa)
Wafalme wa Yuda K.W.K. Wafalme wa Israeli
kama 843 Yeroboamu ya Pili
Uzia (Azaria) 829
kama 792 Zekaria
791 Shalumu
kama 790 Menahemu
780 Pekahia
778 Peka
Yothamu 777
Ahazi kama 761
kama 748 Hoshea
Hezekia kama 745