Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w76 9/15 kur. 418-424
  • Uaminifu kwa Agano la Ndoa Wamfanya Mungu Aonyeshe Rehema

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uaminifu kwa Agano la Ndoa Wamfanya Mungu Aonyeshe Rehema
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ADHABU ZA UZINZI WA KIROHO
  • Kupatanishwa kwa Rehema ya Mungu Kabla ya Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Rehema ya Mungu Yaonyeshwa Wakati wa Har–Magedoni
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Unabii wa Hosea Hutusaidia Kutembea Pamoja na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Rehema ya Mungu Kwa Wanadamu Katika Karne Yetu ya Ishirini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
w76 9/15 kur. 418-424

Uaminifu kwa Agano la Ndoa Wamfanya Mungu Aonyeshe Rehema

“Nami nitakuposa uwe wangu kwa milele; naam, nitakuposa kwa haki, na kwa hukumu, na kwa ufadhili [upendo mwaminifu] na kwa rehema. Nami nitakuposa kwa uaminifu; nawe utamjua [Yehova].”​—⁠Hos. 2:19, 20.

1. Katika karne yetu ya 20, ni maulizo gani yanayotokea juu ya hatua anayoweza kuchukua mume kuelekea mke mwenye hatia ya matendo ya uzinzi?

MKE asiye mwaminifu, mwenye hatia ya matendo ya uzinzi, hapaswi kutazamia kuonyeshwa rehema na mume wake wa kisheria. Hana sababu imara ya kujiona salama kwa kutegemea wapenzi wake wa nje ya ndoa wamruzuku nyakati zote. Baada ya kutosheleza nyege zao naye kwa muda mrefu, hata wapenzi wake wanaweza kuchoshwa na mwanamke huyo malaya wakatafute mwili mwingine. Ikitukia hivyo, yeye atakwenda wapi? Uaminifu kwa mapatano yake ya ndoa wapaswa kumrudisha kwa mumewe wa kisheria. Lakini je! yeye ataonyesha rehema na kumkubali tena mke wake mzinzi? Ni mara ngapi inapokuwa hivyo katika ulimwengu huu usio na rehema, katika karne yetu ya 20?

2. Ni mawazo na matendo ya nani yaliyo makuu kuliko yetu sisi wanadamu, na kwa hiyo Yeye alifanyia watu Wake wa agano nini mwaka wa 537 K.W.K.?

2 Hata hivyo, yuko mtu anayeambia wanadamu hivi: “Mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu . . . Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” Ni nani huyo mwenye mawazo na matendo bora hivyo? Ni Yeye aliye juu yetu sisi wanadamu kama mbingu zilivyo juu. Huyo, mwenye kusema maneno yaliyotangulia, ajisema kuwa Yehova, naye afanya hivyo kupitia kwa nabii wake wa kale Isaya mwana wa Amozi. (Isa. 55:8, 9; 1:1) Yehova aliyasema maneno hayo alipokuwa akitabiri kurudishwa kwa watu wake wa agano waliokuwa wamehamishwa akionyesha wangetoka nchi ya kipagani ya Babeli warudie nchi yao waliyopewa na Mungu katika Mashariki ya Kati. Tofauti na vile wanadamu wote walivyowaza, Mungu huyo mwenye rehema aliwarudisha watu hao mwaka wa 537 K.W.K.

3. Watu hao walirudishwa ili kutatua tatizo gani, nao Mlima Sinai katika Uarabu ulihusikaje katika habari hii?

3 Watu hao wahamishwa walirudishwa kwenye nchi yao ya mbali iliyokuwa imekuwa ukiwa miaka 70 ili kutatua tatizo la ndoa ambalo Yehova alikuwa nalo. Karibu miaka elfu kabla ya hapo yeye alikuwa amewaposa watu hao wahamishwa, taifa la kale la Israeli. Walioana katika ujirani wa Mlima Sinai katika pembe ya chini ya magharibi ya Mkono wa Nchi wa Uarabu. Aliyewaoza alikuwa nabii Musa, aliyetenda kama mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu. Mungu alitangaza orodha ya sheria za msingi za kuongozea uhusiano wa ndoa, yaani, Amri Kumi, na ya kwanza yasema hivi: “Mimi ni [Yehova], Mungu wako, niliyekutoa katika nchi ya Misri, katika nyumba ya utumwa. Usiwe na miungu mingine ila mimi.”​—⁠Kut. 20:1-3.

4. Makabila kumi na mawili hayo ya Israeli yaliyokombolewa yalikuwa mali ya nani hasa, nao walichagua kuingia katika uhusiano gani, na kwa njia gani?

4 Kwa kukomboa makabila kumi na mawili ya Israeli kutoka uonezi na uzuizi katika Misri ya kale, Yehova alimnunua au alimkomboa “mke” huyo, yaani, taifa. (Isa. 63:7-9) Kwa haki lilikuwa mali yake. Kwa hiyo yeye, akiwa ndiye Mwenyeji-Mume, alichagua kuingiza taifa hilo lililo kama mke katika mapatano ya ndoa na yeye mwenyewe. Mapatano hayo mazito yalikuwa na msingi wa orodha ya sheria za Mungu nayo yanatajwa kwa ujumla kama agano la Torati ya Musa. Ili kupata baraka na usalama kwa sababu ya kuwa na Mungu kama Mwenyeji wa Kimbinguni wao, Waisraeli waliingia katika uhusiano wa ndoa. Waliahidi kuwa waaminifu kwa mapatano yao ya ndoa, agano la Torati ya Musa. Wakawa watu wa pekee wa agano la Mungu duniani. Kwa hiyo Yehova akasema: “Nalikuwa mume kwao.”​—⁠Yer. 31:31, 32.

5. Likiwa katika ulimwengu wenye ufisadi, taifa la Israeli liliona ni vigumu kufanya nini, naye Gomeri mke wa Hosea alitumiwa kufananisha nani?

5 Likiwa katikati ya ulimwengu wenye ufisadi uliojishikamanisha na Baali na miungu mingine mingi ya uongo, taifa la Israeli liliona ni vigumu sana kufuata agano lake la ndoa, mapatano yake na Yehova akiwa Mungu na Mwenyeji-Mume. Kwa hiyo kwa ujumla taifa hilo lilifanya uzinzi wa kiroho juu ya Yehova. (Yak. 4:4) Mwaka wa 997 K.W.K. ulitokea mgawanyiko katika ufalme wa Israeli wa makabila kumi na mawili. Uzinzi wa sehemu inayoitwa ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulifananishwa na mke wa nabii Hosea, aitwaye Gomeri.

6, 7. (a) Yehova alipataje kuwa na kesi juu ya ufalme wa Israeli wa makabila kumi? (b) Huo ufalme wa Israeli ulimfuata nani kwa mbio usifaulu, nao ulipaswa kurudia nani?

6 Gomeri akawa “mke wa uasherati.” Akawa na “watoto wa uasherati.” (Hos. 1:1-3, NW) Hiyo ilifananisha vile ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulivyoingia katika mapatano ya kisiasa na mataifa yenye kuabudu sanamu. Taifa la Israeli lililokuwa kama mke lilianza kutegemea mataifa hayo ya kipagani badala ya kumtegemea Mwenyeji-Mume wao, Yehova. Lilianza kuabudu miungu ya mataifa hayo likavunja waziwazi agano lake la ndoa na Mkombozi wake na Mwenyeji-Mume, Yehova. Kwa sababu hiyo Yeye alikuwa na kesi na ufalme wa Israeli huo wenye kufanya uzinzi wa kiroho. Kulingana na masharti ya agano la ndoa, yeye alikuwa na haki ya kisheria na wajibu wa kuchukua hatua juu ya Israeli wenye kuasi imani. Mwishowe alifanya hivyo. Aliliambia taifa hilo hivi:

7 “Basi kwa ajili ya hayo, angalia, nitaiziba njia yako kwa miiba, nami nitafanya kitalu juu yake, asipate kuyaona mapito yake. Naye atawafuatia wapenzi wake, lakini hatawapata; atawatafuta, lakini hatawaona; ndipo atakaposema, Nitakwenda nikamrudie mume wangu wa kwanza; kwa maana hali yangu ya zamani ilikuwa njema kuliko hali yangu ya sasa. Maana hakujua ya kuwa mimi ndiye aliyempa ngano, na divai, na mafuta, na kumwongezea fedha na dhahabu, walivyovitumia kwa ajili ya Baali [au, walivyovifanya vikawa sanamu ya Baali].”​—⁠Hos. 2:6-8.

8. Hivyo, Yehova alikusudia kutia nani adabu, lakini bila kubadili uamuzi gani wake?

8 Kulingana na maneno hayo, Yehova alikusudia kutia adabu watu wa ufalme wa Israeli wa makabila kumi. Si kwamba hiyo ingeokoa ufalme wa taifa hilo, kwa maana Yehova asingebadili maneno aliyokuwa amesema mapema katika unabii wa Hosea: ‘Nitaukomesha ufalme wa nyumba ya Israeli. Tena itakuwa siku ile, nitauvunja upinde wa Israeli katika bonde la Yezreeli.’​—⁠Hos. 1:4, 5.

9. (a) Ni nani angeweza kufaidika na adhabu iliyotolewa kwa ufalme wa Israeli? (b) Agano la ndoa kati ya Israeli na Yehova lilikwisha kulipotukia nini?

9 Bado, kulikuwa na Waisraeli mmoja mmoja ambao wangeweza kufaidika kutokana na adhabu iliyotolewa kwa taifa lenye kuasi imani. Kwa mfano, fikiria wale Waisraeli elfu saba wasiompigia Baali magoti. (1 Fal. 19:18; Rum. 11:1-5) Tusisahau uhakika huu: Wakati Yehova alipokomesha ufalme wa Israeli akaacha Waisraeli wenye kuokoka wahamishwe kupelekwa Ashuru mwaka wa 740 K.W.K., hakufuta agano la ndoa na taifa zima la Israeli. Wakati Yehova alipoacha Yerusalemu uharibiwe mwaka wa 607 K.W.K. na Wayahudi wenye kuokoka wakahamishwa kupelekwa Babeli, yeye hakutangua agano la Torati ya Musa ambalo kwalo taifa la Israeli la makabila kumi na mawili lilikuwa limeingia katika uhusiano wa ndoa naye kama Mume wa Kimbinguni. Uhusiano wa ndoa ya kisheria kati ya Yehova na Israeli wote haukufutwa mpaka viongozi wa Kiyahudi walipomwua Yesu Kristo mwaka wa 33 W.K.​—⁠Kol. 2:14.

10. “Wapenzi” wa ufalme wa Israeli walishindwaje kumsaidia, lakini ni nani angeweza kufaidika kutokana na adhabu ya Yehova?

10 Ingawa ufalme wa Israeli wa makabila kumi ulitafuta msaada wa mataifa ya kilimwengu yaliyokuwa yamekuwa wapenzi wake wenye nyege, wakati wa Yehova wa kufanya hesabu na Israeli ulilifikilia taifa bila rehema. Lisingeweza kusaidiwa na ye yote wa “wapenzi” wake ambao lilitafuta kwa bidii. Lilizuiwa lisipate msaada wa kulifaa, kama kwamba kwa kichaka chenye miiba. Waliokuwa wapenzi wake hawakuweza kuwapa Israeli msaada, ingawa walitaka kufanya hivyo. Baada ya miaka mitatu ya kuzingirwa na Waashuru, mji mkuu wa Israeli Samaria ulianguka mwaka wa 740 K.W.K. Waisraeli wenye kuokoka walihamishwa wakapelekwa nchi ya wenye kuwateka. Ufalme huo wa Israeli wa makabila kumi haukurudishwa tena katika nchi waliyopewa na Mungu. Basi, ni nani angeweza kufaidika kutokana na adhabu ya Yehova? Ni watu mmoja mmoja tu kati ya wahamishwa waliokuwa Ashuru. Wangefikiria mambo. Wangekumbuka vile mambo yalivyokuwa mazuri wakati babu zao walipomtumikia Yehova kama Mume wa Kimbinguni na Mungu wao. Baada ya kutambua sasa hali bora ya mambo, wangeacha ibada ya Baali na kutafuta uhusiano mpya wa agano na Yehova.

11, 12. Ni wakati gani Waisraeli wahamishwa katika Ashuru waliporudia ibada ya Yehova Yerusalemu, na hilo lilitokeaje?

11 Ni wakati gani Waisraeli wahamishwa waliokuwa Ashuru walipopewa nafasi ya kurudia ibada ya Yehova kwa umoja katika mahali alipopaweka yeye? Ilikuwa kwanza katika mwaka wa 537 K.W.K., wakiwa chini ya mamlaka mpya ya ulimwengu. Kwa njia gani? Karibu na mwaka wa 632 K.W.K., mji mkuu wa Ashuru Ninawi uliangushwa na Wababeli, nayo Mamlaka ya Ulimwengu ya Babeli ikawa ndiyo kubwa zaidi ya zote. Kwa hiyo mikoa ya Ashuru ikawa mikoa ya Milki ya Babeli pamoja na Waisraeli wahamishwa. Karibu miaka 25 baadaye Yehova alifikiliza hukumu yake kwa kuadhibu ufalme wa Yuda uliokuwa umekwisha asi wakati huo. Hivyo, mwaka wa 607 K.W.K., aliacha Yerusalemu na hekalu lake la ibada Iiharibiwe. Maelfu ya Wayahudi wenye kuokoka walihamishwa wakapelekwa Babeli, wakaungane na wahamishwa Waisraeli katika mikoa iliyokuwa ya Ashuru.

12 Katika mwaka wa 70 baadaye, Yehova aliona kwamba tengenezo lake potovu duniani lilikuwa limeadhibiwa kutosha. Kwa rehema Yehova alikuwa amemwinua Koreshi Mwajemi aliyetabiriwa apindue Babeli mwaka wa 539 K.W.K. Muda mfupi baada ya hapo, mwaka wa 537 K.W.K., Yehova alimwongoza Koreshi Mkuu atangaze kufunguliwa kwa Waisraeli wenye kutubu warudie nchi yao waliyoipenda.

13. Kwa sababu gani, kulingana na Kumbukumbu la Torati 24:1-4, hiyo ilikuwa rehema ya pekee aliyoonyesha Mungu kwa watu wake wa agano walio kama mke?

13 Je! hilo halikuwa tendo la pekee la rehema kwa upande wa Mume wa Kimbinguni kuelekea watu wake wa agano, makabila kumi na mawili ya Israeli? Ndiyo; kwa maana kulingana na agano la Torati ya Musa jambo hilo halikupaswa kutazamiwa. Katika Torati, twasoma hivi: “Mtu akiisha kutwaa mke kwa kumwoa, asipopata kibali machoni mwake, kwa kuwa ameona neno ovu kwake, na amwandikie hati ya kumwacha, akamtilie mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake. Naye akiisha kuondoka katika nyumba yake, ana ruhusa kwenda akawa mke wa mtu mwingine. Na huyo mumewe wa sasa akimchukia, na kumwandikia hati ya kumwacha, na kumpa mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake; au akifa yeye mumewe wa sasa, aliyemtwaa kuwa mkewe; yule wa kwanza aliyemwacha asimtwae kuwa mkewe tena, akiisha kutiwa unajisi; kwa kuwa haya ni machukizo mbele za [Yehova]; kwa hiyo usiitie dhambini nchi, akupayo [Yehova], Mungu wako, iwe urithi.”​—⁠Kum. 24:1-4.

14. Katika Yeremia 3:1, Yehova alisemaje kwamba alikuwa na sababu za kutaliki Israeli milele?

14 Katika siku za nabii Yeremia, Yehova alitia mkazo juu ya sheria hiyo kwa Wayahudi wenye kuvunja agano katika ufalme wa Yuda. Akikazia uhakika wa kwamba alikuwa na sababu za kutaliki Israeli milele, Yehova alimwongoza Yeremia kusema: “Watu husema, Mtu akimwacha mkewe, naye akienda zake, akawa mke wa mtu mwingine, je! mtu huyo atamrudia tena? je! nchi hiyo [ya Yuda] haitatiwa unajisi? Lakini wewe umefanya mambo ya ukahaba na wapenzi wengi; nawe, je! utanirudia mimi? asema [Yehova].”​—⁠Yer. 3:1.

15. Ni wakati gani na namna gani uhusiano wa ndoa ulivunjika, na Wayahudi mmoja mmoja walionyeshwaje rehema na Yehova?

15 Kwa sababu ya jambo hilo, rehema ya Yehova ipitayo mambo yote ndiyo iliyoruhusu agano lake la ndoa na Israeli liendelee kuwapo kwa karne nyingi baada ya Yerusalemu kuharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Lakini hatua ya mwisho ilifika mwaka wa 33 W.K., wakati taifa lilipomkataa Masihi Yesu likamfanya auawe nje ya kuta za Yerusalemu. Ndipo taifa lilipotalikiwa litoke katika uhusiano wa ndoa na Yehova Mungu. Je! historia ya Kiyahudi tangu wakati huo inahakikisha hivyo? Ndiyo. Hata hivyo, kwa rehema Yehova aliruhusu Wayahudi mmoja mmoja waliomwamini Masihi Yesu wafanye upya uhusiano wao naye katika agano jipya, agano lililopatanishwa na Masihi Yesu.

16. Kwa sababu gani mabaki ya Waisraeli wa kiroho wataokoka wasiharibiwe pamoja na Jumuiya ya Wakristo, na ni nani wengine watakaojifaidi na rehema ya Yehova?

16 Leo Jumuiya ya Wakristo inajidai kuwa katika agano hilo jipya. Lakini, ingawa inadai hivyo, ingawa mwaka 1975 ulikuwa Mwaka Mtakatifu wa Kanisa Katoliki la Rumi, ingawa watu wengine zaidi wameanza kupendezwa tena na dini, Jumuiya ya Wakristo imehukumiwa maangamizi wakati wa “dhiki kubwa” inayokaribia sana kuupata ulimwengu huu usiomcha Mungu. Hata hivyo, Yehova ameita mabaki yenye kutubu ya Waisraeli wa kiroho watoke katika Jumuiya ya Wakristo iliyo ya Kibabeli, kwa sababu ya rehema yake yenye upendo. Kwa njia hiyo wataepuka kuharibiwa pamoja na jumuiya hiyo. (Ufu. 18:4) Lakini si mabaki tu ya Waisraeli wa kiroho yametoka humo. “Mkutano mkubwa” wa watu wengine wenye mfano wa kondoo umejifaidi na rehema ya Yehova iliyopanuliwa tangu mwaka wa 1935 W.K. Wametoka katika sehemu zote za Babeli Mkuu wakajiunga na mabaki kumtolea Yehova ibada ya pekee.​—⁠Ufu. 7:9-17; Yohana 10:16.

ADHABU ZA UZINZI WA KIROHO

17, 18. (a) Kwa sababu gani Jumuiya ya Wakristo ina lazima ya kupatwa na laana za Mungu? (b) Akionya hivyo, Yehova alisema nini katika Hosea 2:9-13?

17 Lazima matengenezo ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo yapate adhabu za kufanya umalaya kwa kuwa rafiki za wanasiasa na wanajeshi, kwa sababu yanajidai kuwa katika uhusiano wa agano na Mungu wa Biblia. Na wakumbuke kwamba Israeli ya kale ilipaswa kupatwa na laana za Mungu zikiwa adhabu za kuvunja agano la Torati ya Musa lililofanywa kati yake na Yehova akiwa Mume wa Kimbinguni wa tengenezo lake lililo kama mke. Yehova aliendelea kumwambia Hosea, akimwonya hivi:

18 “Basi kwa ajili ya hayo, nitaitwaa tena ngano yangu kwa wakati wake, na divai yangu kwa wakati wake, nami nitamnyang’anya sufu yangu na kitani yangu, vya kumfunika uchi wake. Na sasa nitafunua aibu yake mbele ya macho ya wapenzi wake, wala hapana mtu atakayemwokoa katika mkono wangu. Tena nitaikomesha furaha yake yote, na sikukuu zake, na siku zake za mwandamo wa mwezi, na sabato zake, na makusanyiko yake yote yaliyoamriwa. Nami nitaiharibu mizabibu yake na mitini yake, ambayo alisema, Hii ndiyo ujira wangu niliopewa na wapenzi wangu; nami nitaifanya kuwa msitu, na wanyama wa mashamba wataila. Nami nitamwadhibu kwa sababu ya siku za Mabaali, aliowafukizia uvumba; hapo alipojipamba kwa pete masikioni mwake, na kwa vito vyake vya thamani, na kufuatana na wapenzi wake, na kunisahau mimi, asema [Yehova].”​—⁠Hos. 2:9-13.

19. Kulingana na agano la Torati, Yehova alipaswa kufanya nini juu ya taifa lenye uzinzi?

19 Na tuangalie kwamba Israeli walimsahau Yehova. Taifa hilo lilistahili kutendewaje kwa sababu hiyo? Kulingana na maonyo yake ya wazi katika agano lake la ndoa na Israeli, yeye alipaswa kuwanyima baraka zake za vitu vya kimwili kwa sababu ya kumtendea ukafiri kama Mume wa Kimbinguni. Hakupaswa kuruzuku mzinzi, yaani, taifa lililovunja agano lake likaanza kuabudu sanamu za Baali na kuzini na wapenzi wa kilimwengu. Yehova angeweza kwa haki kufunua wazi kutotegemeka na upotovu wa adili wa taifa, hata rafiki zake wa kilimwengu waligeukie kwa dharau.

20. Yehova angelifanyaje taifa lenye uzinzi liwe kama maiti, na ni kwa njia gani hakuna mtu angeweza kulinyakua katika mkono wa Yehova wa hukumu

20 Yehova angelifanya taifa hilo liwe kama msitu usiolinda mtu ye yote na wanyama-mwitu. Taifa lisingeweza kudai kutoadhibiwa kwa sababu tu lilikuwa limetokana na wazee wa ukoo, Ibrahimu, Isaka, Yakobo (Israeli) na wakuu wa makabila kumi na mawili waliokuwa wana wa Yakobo. Uhusiano wa kimwili na wanaume hao hautafaa cho chote wala hautanyakua taifa mkononi mwa Yehova atakapofikiliza hukumu kali.

21. Ujapokuwa ukoo wa Israeli, wao hawakufaa kushiriki kutimiza agano gani la mapema la Yehova?

21 Hiyo haikumaanisha kwamba Yehova hakukumbuka wala kushikamana na agano alilokuwa amefanya na rafiki yake Ibrahimu huko nyuma mwaka wa 1913 K.W.K. Yehova alijiapia mwenyewe juu ya agano hilo naye hatalivunja kamwe, lakini Israeli wenye kufanya uzinzi hawakustahili kushiriki kutimiza agano hilo ingawa walikuwa wazao wa asili wa Ibrahimu. Yehova alimwambia babu yao Ibrahimu hivi: “Uwe baraka; nami nitawabariki wakubarikio, naye akulaaniye nitamlaani; na katika wewe jamaa zote za dunia watabarikiwa.” (Mwa. 12:2, 3) “Katika kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia.’’!​—⁠Mwa. 22:17, 18.

22. Ijapokuwa Yehova aliacha falme za Israeli na Yuda zipinduliwe, kwa sababu gani alihifadhi uzao wa Ibrahimu, Naye alifanya nini kwa mabaki ya uzao huo?

22 Aliye mkuu wa uzao wa Ibrahimu, yaani, Masihi, hakuwa amekuja wakati Samaria ulipoharibiwa mwaka wa 740 K.W.K. wala wakati Yerusalemu ulipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Hata hivyo Mzao wa Kimasihi wa Ibrahimu alipaswa kupitia katika ukoo wake wa asili. Ni kweli, Yehova aliacha adui waupindue ufalme wa Israeli na ufalme wa Yuda, lakini bado ulipaswa kuhifadhi uzao wa asili wa Ibrahimu. Kwa sababu gani? Kwa sababu Masihi wa kubarikia mataifa yote ya dunia alipaswa apitie katika ukoo huo. (Mt. 1:1-3; Gal. 3:8-29) Kwa kusudi hilo Yehova alihifadhi kwa rehema mabaki ya Waisraeli wenye kutubu wakati wa miaka 70 ya uhamisho iliyofuata kupinduliwa kwa ufalme wa Yuda huko Yerusalemu. Yeye alishikamana kwa uaminifu na agano lake la ndoa pamoja na mabaki waaminifu. Halafu alimtokeza yeye aliyefananisha Masihi, yaani, Koreshi mwenye kushinda Babeli. Kwa kumtumia mkombozi huyo Yehova alirudisha mabaki ya uzao wa Ibrahimu kwenye nchi ya Yuda.

23. Atabiri kupatanishwa kwake mwenyewe na watu wake wa agano walio kama mke, Yehova alisema nini katika Hosea 2:14-16?

23 Kwa hiyo, ili atabiri kupatanishwa Kwake tena pamoja na watu wake wa agano walio kama mke, Yehova alimwongoza nabii Hosea kuendelea kusema hivi: “Kwa hiyo angalia, mimi nitamshawishi, na kumleta nyikani, na kusema naye maneno ya kumtuliza moyo. Nami nitampa mashamba yake ya mizabibu toka huko, na bonde la Akori kuwa mlango wa tumaini; naye ataniitikia huko, kama siku zile za ujana wake, na kama siku ile alipopanda kutoka nchi ya Misri. Tena siku hiyo itakuwa, asema [Yehova], utaniita Ishi [neno la Kiebrania linalomaanisha mume Wangu], wala hutaniita tena Baali [mwenyeji Wangu].” (Hos. 2:14-16) Au, kulingana na mstari wa kumi na sita katika tafsiri ya Leeser: “Na itatukia siku hiyo, asema Bwana, kwamba wewe utaniita mimi Ishi [mume wangu], nawe hutaniita mimi tena Ba’ali [bwana wangu].”​—⁠Hos. 2:18; Leeser; Rotherham.

24.Yehova alisemaje na tengenezo lake lililo kama mke “nyikani,” na kulipa tengenezo mashamba ya mizabibu kulimaanisha nini?

24 Wakati Waisraeli walipokuwa wahamishwa katika nchi ya Babeli, walikuwa kama kwamba wamo “nyikani.” Huko Yehova ‘alishawishi’ mabaki yenye kutubu kwa rehema ‘akasema maneno ya kuwatuliza moyo.’ Alifanya hivyo kwa kuwaadhibu kwa upendo kupitia kwa manabii Ezekieli na Danieli. Yehova alikuwa ameahidi kulipa tengenezo lake lililoadhibiwa na lililo kama mke “mashamba yake ya mizabibu toka huko.” Hiyo ilimaanisha angelitoa “nyikani” mwa Babeli, na kulirudisha kwenye nchi ya Yuda na Yerusalemu iliyokuwa imekaa ukiwa muda mrefu.

25. Ilikuwa na maana gani kwa tengenezo lililo kama mke kupewa na Yehova “bonde la Akori kuwa mlango wa tumaini”?

25 Wakati Yehova alipotaja “bonde la Akori,” aliwakumbusha jambo hili: Baada ya Waisraeli kushambulia na kuharibu Yeriko mji wa Wakanaani, Akani mwenye pupa alipigwa kwa mawe akafa, pamoja na jamaa yake, kwa sababu alivunja amri ya Yehova. Kwa njia hiyo Akani aliletea Israeli matatizo alipokosa kutii, akateka nyara kwa sababu ya choyo. Kwa kufaa bonde ambalo Akani alipigwa kwa mawe akafa liliitwa “Bonde la Akori,” nalo jina Akori lamaanisha “Fadhaa.” (Yos. 7:10-26) Kwa hiyo ahadi ya Yehova kulipa tengenezo lake lililo kama mke “bonde la Akori kuwa mlango wa tumaini” ilimaanisha tengenezo lingerudishwa katika nchi ya kwao kulikokuwa na bonde hilo.

26. Tengenezo lililo kama mke lilimwitikiaje Yehova “nyikani,” Naye alihakikishaje kwamba uhusiano wa ndoa ungefanywa upya?

26 Namna gani sasa juu ya mabaki wenye kutubu wa tengenezo la Yehova lililo kama mke? Je! ‘waliitikia’ alipowashawishi na kuwaambia maneno ya ‘kuwatuliza moyo’? Historia ya Biblia yajibu, Ndiyo! Huko nyuma wakati taifa la Israeli lilipokuwa katika siku za “ujana” wake, lilikuwa ‘limeitikia’ kwa moyo. Lilikubali ukaribishaji wa Yehova liwe tengenezo lake lililo kama mke kwa kuingia katika agano la Torati ya Musa pamoja Naye. Vivyo hivyo, mabaki wenye kutubu katika Babeli ya kale waliitikia wakitaka kufanya upya vifungo vya ndoa kati ya Israeli na Mume wake wa Kimbinguni, Yehova. Ili kuhakikisha uhusiano huo wa ndoa ungefanywa upya, Yehova alimtumia Masihi wa mfano, Koreshi Mkuu, akarudisha mabaki yenye uaminifu ya Waisraeli kwenye nchi ya Yuda na Yerusalemu.

27. Sasa mabaki walifanya nini juu ya ibada ya Baali, nalo tengenezo lililo kama mke lilionyesha nini kwa kumwita Yehova “Mume wangu”?

27 Watu wa Yehova wa agano waliorudishwa hawakufuata tena ibada ya Baali wala namna nyingine za ibada ya sanamu. Mabaki waliokubaliwa tena walirudisha ibada ya Mume wa Kimbinguni wa Israeli kwa juhudi, yeye akiwa Mungu wao katika nchi aliyokuwa amewapa. Walishukuru sana kama babu zao walipokombolewa mikononi mwa Misri na majeshi yake. Mume wa Kimbinguni wa Israeli alielekea kuwa karibu zaidi nao, akiwapenda sana sana. Kwa hiari tengenezo hilo lililo kama mke lilimwita Yehova kwa mapenzi. Kwa hiyo, kwa njia ya kiroho lilimwita, “Mume wangu,” badala ya “Mwenyeji wangu.” Hali kutaka tena kuwa mali yake tu, kama kwamba ni mali ya mnyapara. Lilitaka kujiona kuwa msaidizi wake, kama vile mwanamke wa kwanza Hawa alivyokusudiwa awe kwa mumewe, Adamu. (Mwa 2:19-24) Hilo lilikuwa jambo la kupendeza namna gani!

28. Ni nini leo kilicho kizuri kama wonyesho huo wa kale wa rehema ya kimungu?

28 Ulinganifu wa kisasa wa jambo hilo katika karne yetu ya 20 unapendeza pia. Hata leo matokeo mazuri sana yanasababishwa na rehema ya Yehova inayoongozwa na uaminifu wake kwa agano lake la ndoa ya kiroho. Wenye furaha ni wale wanaoonyeshwa rehema naye sasa!

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki