Kutakuwako Baraka Gani Duniani Wakati wa Ile Miaka Elfu?
Kutakuwaje wakati ‘mapenzi ya Mungu yatakapofanywa duniani’?
Je! umekwisha kuitoa sala ya kielelezo ijulikanayo sana ambayo Yesu alifundisha? Yeye alisema hivi: “Ufalme wako uje, Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mt. 6:9, 10.
INGAWA mamilioni ya watu wamerudia-rudia maneno hayo, je! unadhani kwamba wengi wamefikiria kwa uzito namna itakavyokuwa duniani wakati Mungu atakapoijibu sala hiyo kikamilifu? Je! wewe mwenyewe umekwisha kuuliza ni mambo gani ambayo wewe na jamaa yako mtaweza kufurahia iwapo mtapendelewa kuishi wakati mapenzi ya Mungu yatakapofanywa karibuni duniani kama ilivyo mbinguni?
Kitabu cha Ufunuo kinaweza kutusaidia hapa. Katika sura yacho ya 19 twasoma juu ya vita inayokuja ambayo katika hiyo Yesu Kristo ataharibu adui wote wa Mungu duniani. Sura ya 20 inatuambia kwamba kisha Ibilisi, ambaye amekuwa akitegemeza uovu, atatupwa shimoni kwa miaka 1,000 (mileani moja). Wakati wa mileani (miaka elfu moja) hiyo, Kristo atatawala kutoka mbinguni, kwa baraka ya watumishi wa kibinadamu wa Mungu, kutia ndani na wale watakaofufuliwa. Watu waovu wakiwa wamekwisha kuondolewa, kutakuwako “mbingu mpya na nchi mpya” ambazo katika hizo haki itadumu.—Ufu. 20:11; 21:1; 2 Pet. 3:13.
Je! unapendezwa na masimulizi marefu zaidi ya baraka za kidunia wakati wa mileani? Basi, Ufunuo unaendelea kutoa masimulizi juu ya namna itakavyokuwa wakati Yehova Mungu atakapogeuza fikira zake kwa jamii mpya ya kidunia ya waabudu wa kweli. Twasoma hivi:
“Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufu. 21:4.
Je! uhakika wa kwamba hakutakuwako machozi tena hauonyeshi kwamba wanadamu hawataendelea kupatwa na ukatili kama vile kutesa watoto na wake, kulala wanawake kwa nguvu, unyang’anyi, mashambulio, ujeuri na vita? Na zaidi, Mungu anatuhakikishia kwamba maumivu na kifo—ambayo wakati mwingi sasa hufuatana na maradhi na misiba—hayatakuwapo ili kuleta huzuni.
Vilevile Biblia inatupa msingi wa kutazamia baraka nyingine duniani wakati wa mileani. Kwa habari hii, hatuhitaji kuwazia au kuongeza chumvi, kama vile wengine walivyofanya katika karne za pili na tatu.
MAONI YA ZAMANI JUU YA HALI ZA KIDUNIA
Kama ambavyo toleo la Aprili 1, 1980 la gazeti hili, chini ya kichwa “Mileani—ni nini?” lilivyotaja, uasi juu ya Ukristo wa kweli ulitokea baada ya mitume kufa, na wengine wakaanza kufunza mambo yaliyopotoka. Kwa sehemu fulani, jambo hilo, lilikuwa kwa sababu waliamini kwa makosa kwamba Yesu na warithi washiriki wake wangetawala wakiwa hapa duniani. (Yohana 14:19; 2 Tim. 2:12; 1 Pet. 1:3, 4) Kwa wazi iliwazwa kwamba watawala hao wenye nguvu kupita wanadamu wangetokeza hali za kustaajabisha duniani.
Twapata mfano wa masimulizi hayo yasiyosadikika katika maandishi yaliyoandikwa ya Papias, askofu wa karne ya pili kutoka Frigia. Yeye aliwaza kwamba wakati wa mileani jambo hili lingetokea:
“Mizabibu itakuzwa, kila mmoja ukiwa na matawi elfu moja, . . . na katika kila chipukizi vichala elfu kumi, na katika kila kichala zabibu elfu kumi . . . Vivyo hivyo mbegu ya ngano itazaa masuke elfu kumi, na kila suke litakuwa na mbegu elfu kumi, na kila mbegu [itatoa] ratli kumi za unga safi mweupe.”
Bado, waandikaji wengine wa zamani walitaja masimulizi yenye kufurahisha katika Isaya, wakiamini kwamba yalikuwa yakionyesha yale ambayo utawala wa Kristo wa miaka 1,000 utafanya.
Kwa mfano, waandikaji wa karne ya pili Justin Martyr na Irenaeus walitaja unabii katika Isaya 65:17-25 na 11:6-9. Kifungu cha kwanza cha mistari hiyo chasema hivi:
“Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; maana kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu. . . . Mbwa-mwitu na mwana-kondoo watalisha pamoja, na simba atakula majani kama ng’ombe; . . . Hawatadhuru wala kuharibu katika mlima wangu mtakatifu wote, asema [Yehova].”
Vilevile Isaya sura ya 11 inazungumza juu ya wanyama wakiishi pamoja katika amani, naye simba akila nyasi kama vile ng’ombe. Na inasema kwamba kivulana atawaongoza.
Irenaeus alitambua kwamba maneno haya ni masimulizi yanayofaa ya namna kweli ya Mungu inavyoweza kufanya nyutu zibadilike katika “watu wa kinyama, wa mataifa mbalimbali na tabia tofauti tofauti, ambao wanakuja kuamini, na wakiisha kuamini, kutenda kwa kupatana na yaliyo haki.” Lakini vilevile aliwaza kwa kutoa sababu kwamba katika mileani mabadiliko haya katika wanadamu, kuwa wenye amani kuliko kuwa wakali, ni jambo la akili kwamba yangeonyeshwa na viumbe vya namna ya wanyama. Yeye aliandika hivi:
“Wakati taratibu iliyoumbwa itakapofanywa upya tena, basi wanyama watapaswa kuwa chini ya wanadamu, na kurudia chakula alichowapa Mungu hapo kwanza, matunda ya dunia, kama walivyokuwa chini ya Adamu na kumtii.”—Against Heresies 5, 33, 4.
Sisi leo tunaposoma vifungu hivyo vya maneno kutoka katika Isaya kulingana na maneno yenye kuvizunguka, twaweza kuthamini kwamba Isaya alikuwa akitabiri juu ya kurudishwa kwa watu wake kutoka utumwani Babeli katika njia ndogo au ya mfano, pili, juu ya kurudishwa kwa Waisraeli wa kiroho kutoka Babeli Mkuu katika hizi “siku za mwisho” katika maana ya mfano wa kisasa au maana kamili. Utimizo huo mdogo ulitokea yapata mwaka 537 K.W.K. Kukiwa na utawala mpya juu ya nchi hiyo, Waisraeli waliorudishwa wangeweza kujitumikisha kulima nchi yao kurudisha uwezo wake wa kuzaa, uzuri na amani. (Isa. 35:1, 2) Yehova aliwasaidia kuondoa sifa za ukali na za kinyama na kuonyesha katika maoni na njia zao amani inayofaa kati ya waabudu wa kweli.—Mik. 6:8; tazama Man’s Salvation out of World Distress at Hand! kur. 320-322, mafu. 15-19; pia “New Heavens and a New Earth,” kur. 324-333, mafu. 18-29.
Kwa kuwa amani hiyo ilisitawi kati ya Waisraeli waliorudishwa wakati huo, nayo inaonekana kati ya waabudu wa kweli leo, je! hatuwezi kuwa na uhakika wayo kwa kadiri kubwa hata zaidi wakati wa mileani? Hata hivyo, vifungu hivyo vya maneno vinatupa mengi ya kufikiria.
VIONYESHO TOKA EDENI
Katika kuonyesha mapema hali mpya ambazo Waisraeli waliorudishwa wangefurahia, Isaya alizungumza juu ya mfano wa makao ya kwanza ya mwanadamu, paradiso iliyoitwa bustani ya Edeni. Yeye aliandika hivi:
“Maana [Yehova] ameufariji Sayuni; amepafariji mahali pake palipokuwa ukiwa; amefanya jangwa lake kama bustani ya [Edeni], na nyika yake kama bustani ya [Yehova].—Isa. 51:3.
Vilevile, waandikaji wengine wa Biblia, waliitaja bustani ya Edeni kama ikifananisha hali zenye kuzaa na zenye baraka ambazo chini yake wanadamu wangetaka kuishi.—Eze. 36:35; Yoeli 2:3; Mwa. 13:10; linganisha Hosea 2:18-21.
Hivyo, katika kuzifikiria baraka za kidunia mileani, twaweza kukumbuka yale ambayo Yehova alitolea jamaa ya kibinadamu mwanzoni katika bustani ya Edeni.
Masimulizi ya Mwanzo yanatuambia kwamba Mungu aliwaweka Adamu na Hawa katika “bustani” au “paradiso.” (Mwa. 2:8, Septuagint Version) Ilikuwa zaidi sana ya bustani ya maua. Twasoma hivi: “[Yehova] Mungu akachipusha katika ardhi kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa.” Ingawa kulikuwako chakula tele chenye afya, bustani ya Edeni ilifanywa pia mahali pa kazi yenye kuthawabisha. Adamu na Hawa walipaswa kulima na kutunza bustani hiyo, jambo ambalo lingeongeza uradhi wao katika kula mazao yake mbalimbali.—Mwa. 2:9, 15, 16; linganisha Mhubiri 2:24; 5:12.
Walipokuwa wakiishi katika bustani hiyo yenye kupendeza, je! Adamu na Hawa walikuwa wanaogopa wanyama-mwitu? Je! amani yao iliharibiwa na wanyama wenye kuwindana kwa ukali? Yale ambayo Isaya aliandika katika sura za 11 na 65 yanadokeza kuwa sivyo. Vilevile tunazo habari za kweli kutoka Mwanzo:
“Mungu akasema [kwa Adamu na Hawa], Tazama nimewapa kila mche utoao mbegu, ulio juu ya uso wa nchi yote pia, na kila mti, ambao matunda yake yana mbegu; vitakuwa ndivyo chakula chenu; na chakula cha kila mnyama wa nchi, na cha kila ndege wa angani, na cha kila kitu kitambaacho juu ya nchi, chenye uhai; majani yote ya miche, ndiyo chakula chenu; ikawa hivyo.”—Mwa. 1:29, 30.
Kama ambavyo huenda ukawa unafahamu, watu wengi leo, kutia ndani wengine wa viongozi wa kidini, hawakubali yale ambayo Biblia husema juu ya bustani ya Edeni na hali zilizokuwapo hapo. Wengine hudai kwamba masimulizi juu ya Adamu na Hawa ni hadithi au fumbo tu. Kwa njia hiyo wanapingana na Yesu Kristo, kwa kuwa yeye alikubali masimulizi ya Kimaandiko kuwa ya hakika, kwa kweli hata akayataja. (Mt. 19:4, 5) Vilevile, wengi wa viongozi wa kidini hawaamini yale ambayo Neno la Mungu husema juu ya wanyama katika bustani ya Edeni. Pengine maoni yao yameongozwa na wazo la mageuzi—kwamba yale ambayo tunaona katika uhai wa wanyama sasa ni kuendelezwa kwa jambo lile ambalo limekuwa wakati wote na kwamba “kuokoka kwa vilivyo bora zaidi” wakati wote kumetawala kati ya wanyama na wanadamu.
Walakini kwa imani katika uwezo wa Mungu, na kwa nia ya kukubali yale ambayo Biblia inasema, twaweza kuamini kwamba katika Edeni wanadamu wa kwanza hawakuwa wenye dhambi, watu wenye kupigana na kwamba wanyama katika paradiso walikuwa na amani kati yao. Juu ya msingi wa yale tuliyojionea wenyewe kwa kutazama katika sehemu za kutunzia wanyama, kwenye vipindi vya televisheni vya wanyama wa porini au mashambani, je! hatuwi na hakika kwamba mwanadamu kuwa na wanyama wanaomtii na wenye amani katika paradiso kuliongeza furaha ya kuishi?—Mwa. 1:26.
KUTAZAMIA MBELE KWA UHAKIKA
Basi, twaweza kuona, kwamba Mungu alitoa msingi wa kutazamia sana baraka za kidunia: Ahadi iliyo katika Ufunuo 21:4 yamaanisha kwamba twaweza kutazamia kukoma kwa huzuni, maumivu na kifo. Na, ni jambo la akili kwamba hiyo itamaanisha mwisho wa hali za sasa zinazotokeza mambo hayo. Vilevile, tuna habari chache za bustani ya Edeni. Zinatupa sababu ya kutazamia paradiso ya kidunia iliyothawabisha, chakula chenye kushibisha na chenye afya na kwa mara nyingine tena wanadamu kutiisha tena viumbe wanyama kwa amani—Luka 23:43 ZSB; Zab. 72:16.
Hali hizi hazitakuwa katika shamba fulani mahali pamoja tu. Mahali pake, Mungu atatimiza kusudi lake la kwanza, kutiisha na kuipamba dunia yote. Makusudi yake hayashindwi kamwe.—Isa. 45:18; Mwa. 1:28; linganisha Isaya 14:24.
Baraka za kimwili si ndizo peke yake zitakazofanya utawala wa miaka elfu upendeze. Yehova anatuhakikishia juu ya mambo ambayo ni ya maana hata zaidi kwa maisha yenye kuridhisha kweli kweli—mambo ya kiroho. Kumbuka Yesu alivyomwambia mjaribu: “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.” (Mt. 4:4) Hivyo, twaweza kuwa na hakika kwamba mileani itakuwa na kula kwa wingi mambo ya kiroho yenye msingi wa Maandiko. Haki na kweli vitajaa tele, vikitokeza amani ya kudumu.—Zab. 72:1, 5-7, 17; Isa. 9:6, 7; 32:1, 16-18; linganisha Isaya 26:7-9.
IMANI SASA
Ili tufurahie baraka za mileani, au hata kuishi kufikia wakati huo, twahitaji imani. Mungu, katika hekima yake, hakutupa habari zote kabisa juu ya hali za kidunia wakati wa mileani. Yeye hajaeleza namna atakavyotimiza mambo ambayo kwa sasa huenda yakaonekana kutowezekana—kuondoa hali za ukiwa ambazo sasa zinachukua sehemu kubwa za dunia, kuondoa maradhi na hali ya kulemaa kwa miili ya kibinadamu na kuleta usawa wenye amani katika jamii ya wanyama. Hata hivyo ametia habari za kutosha katika Neno lake kuthibitisha kwamba anao uwezo unaopita wa kibinadamu kuweza kutimiza miujiza hiyo, na hata kuwafufua wafu. (Matendo 10:37, 38; Luka 7:14-16; 19:37, 38; Mwa. 7:6-16) Hata hivyo, ili mtu amtumikie Mungu imani inahitajiwa, kuamini kwamba yeye atatoa baraka za kiroho na za kimwili.—Ebr. 11:1, 6.
Wakiwa na imani hiyo Mashahidi wa Yehova wanaendesha kazi ya kuelimisha watu ya duniani pote. Wao wanasaidia watu wajifunze Biblia, wapate imani thabiti na kusitawisha uhakika wa kwamba karibuni Mungu, kupitia kwa Kristo, atachukua hatua ya mwisho ya kuondoa uovu. (Mt. 24:14, NW) Wengi wa wale ambao sasa wanaonyesha imani wataokoka na kuona mwanzo wa utawala wa Kristo wa mileani nao watafurahia baraka za kidunia tulizozizungumza. Tunakualika wewe ukubali msaada wa funzo la Biblia ambao Mashahidi wa Yehova hutoa ili kwamba wewe, pia, uweze kutazamia mbele kwa uhakika baraka wakati wa mileani.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wakati wa mileani Mungu ataondoa hali za ukiwa duniani, ataondoa maradhi na kuleta usawa wenye amani katika jamii ya wanyama