Roho Yamtegemeza Mfalme wa Nasaba ya Daudi
1, 2. (a) Ni nani aliyekuwa chanzo cha asili cha Daudi na cha nasaba yake ya wafalme wenye kutawala juu ya Israeli? (b) Chanzo hicho cha asili kilipataje kuwa shina la mti na mizizi yake, nacho chanzo hicho cha asili kilifikia mzao aliyekusudiwa katika nani?
BAADAYE katika njozi ile aliyompa Yohana, Bwana-arusi wa kimbinguni Yesu Kristo alisema hivi: “Mimi ndimi niliye Shina na Mzao wa Daudi; ile nyota yenye kung’aa ya asubuhi.” (Ufu. 22:16) Yese wa Bethlehemu ndiye aliyekuwa baba ya Daudi naye alikuwa wa kabila la Yuda. Kwa hiyo Yesu alikuwa mzao wa Yese kupitia kwa Daudi. Vilevile, Yese ndiye aliyekuwa chanzo cha asili cha Mfalme Daudi pamoja na nasaba ya wafalme wa Daudi juu ya Israeli.
2 Ufalme wa Daudi ulikuwa kama mti wenye shina na mizizi katika Yese. Katika mwaka 607 K.W.K., Yerusalemu ulipoharibiwa na mfalme wake kupelekwa Babeli, ufalme huo ulio kama mti ulipata kukatwa. Ufalme wa nyumba ya Daudi haukurudishwa tena katika Yerusalemu. Kile kilichobaki kilikuwa kama kisiki cha mti pamoja na mizizi yake. Hiki kilifananisha Yese baba ya Daudi. Yese aliacha kuwa na mzao wake akitenda kama mfalme mwenye kutawala juu ya Israeli. Walakini bado kulikuwako nguvu ya uhai katika kisiki na mizizi hiyo ya mti, kwa kuwa nasaba ya wazao wa Yese kupitia kwa Mfalme Daudi ilikuwa bado ikiendelea. Ilifikia mshiriki wake aliyekusudiwa katika Masihi Yesu.
3. (a) Yesu Kristo alitiaje nguvu mpya ufalme ambao chanzo chake kilikuwa Yese? (b) Ufalme huo ulipewa mamlaka wakati gani, nayo ni nguvu gani inayompa nguvu Mfalme aliye mzao wa Yese kupitia kwa Daudi?
3 Kwa kuzaliwa kupitia kwa bikira Mariamu Myahudi katika Bethlehemu, Yesu akawa kama “tawi” kutoka kwa shina la Yese na kama “chipukizi” kutoka katika mizizi ya Yese. Akiwa hivyo angeweza kutia nguvu mpya ufalme uliokuwa na msingi wake katika Yese, baba ya wafalme wenye kutawala juu ya Israeli. Yehova Mungu alipomtia mafuta Yesu kwa roho takatifu, “tawi” au “chipukizi” hili la mfano likawa Mfalme-Mwekwa wa ufalme wa nyumba ya Daudi. Mwishoni mwa Majira ya Mataifa katika mwaka 1914, Mungu alimkalisha katika kiti cha enzi mbinguni akiwa Mfalme. Kwa habari ya utendaji wake Isaya 11:1-5 asema hivi:
“Basi litatoka chipukizi katika shina la Yese, na tawi litakalotoka katika mizizi yake litazaa matunda. Na roho ya [Yehova] itakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha [Yehova]; na furaha yake itakuwa katika kumcha [Yehova]; wala hatahukumu kwa kuyafuata ayaonayo kwa macho yake, wala hataonyo kwa kuyafuata ayasikiayo kwa masikio yake; bali kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili; naye ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake, na kwa pumzi ya midomo yake atawaua wabaya. Na haki itakuwa mshipi wa viuno vyake, na uaminifu mshipi wa kujifungia.”
4. (a) Lile “tawi” la mfano linapigaje dunia kwa fimbo ya kinywa chake? (b) Yeye atawauaje wabaya kwa pumzi ya midomo yake?
4 Wakati wa “dhiki ile iliyo kuu” inayokuja lile ‘chipukizi litokalo katika shina la Yese la mfano, kweli kweli “ataipiga dunia kwa fimbo ya kinywa chake.” Amri za kifalme zikitoka katika kinywa chake zitakuwa kama fimbo yenye kuvunja vipande vipande mipango ya kijamii ya wanadamu duniani, ile taratibu ya kale ya mambo. Amri zake ni zenye nguvu, zenye uharaka, zikitokeza tendo, nazo zatoka kinywani mwake zikiwa na matokeo yenye kuleta kifo juu ya adui zake wa kidunia wenye shingo ngumu.
5. Mfalme anawakomboaje milele wanyenyekevu wapole kutokana na waonezi waovu, akisaidiwa na roho ya Mungu? .
5 Huku kusema kwa mamlaka ya mwuaji wa adui wabaya kunalingana na “upanga mkali unaofananishwa ukitoka katika kinywa cha Mfalme “ili awapige mataifa kwa huo. Naye atawachunga [hao mataifa] kwa fimbo ya chuma.” (Ufu. 19:11-15) Kwa kufanya hivyo, mfalme wa Kimasihi anayetegemezwa na roho ya Yehova, anawakomboa wanyenyekevu wapole wa dunia. Atawalapo akiwa pamoja na wafalme wenzake 144,000, yeye hatawaruhusu waonezi wabaya wapate kuwa na mamlaka tena juu ya dunia.
6. Ni kukusanywa tena kwa akina nani ambako kumetabiriwa katika Isaya 11:10-12, nao wanakusanywa na kuingizwa wapi na kukiwa na hali gani?
6 Tangu kukalishwa kwake katika kiti cha enzi mbinguni mwishoni mwa Majira ya taifa katika mwaka 1914, lile “chipukizi” la mfano kutoka katika mizizi ya Yese limetumikia katika kutimiza sehemu nyingine zaidi ya unabii wa Isaya, sura ya saba. Yeye ameongoza kazi ya kukusanywa tena kwa mabaki ya warithi wa shirika wake walio watiwa mafuta kutoka kafika sehemu zote za dunia ambako walikuwa wametawanywa wakati na baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu. Amewaingiza katika paradiso ya kiroho ambamo wanafurahia amani na umoja pamoja na Mungu na kuzaa “tunda la roho” kwa wingi sana. (Gal. 5:22, 23) Hali ya kinyama ya ulimwengu hairuhusiwi humo! (Isa. 11:6-9) Isaya aliangalia mbele kwenye wakati wa kukusanywa na kurudisha kwa Israeli wa kiroho, akasema hivi:
“Na itakuwa katika siku hiyo, shina la Yese lisimamalo kuwa ishara kwa kabila za watu, yeye ndiye ambaye mataifa watamtafuta; na mahali pake pa kupumzikia patakuwa na utukufu.
“Na itakuwa katika siku hiyo, [Yehova] atapeleka mkono wake mara ya pili, ili ajipatie watu wake watakaosalia, kutoka Ashuru, na kutoka Misri, na kutoka Pathrosi, na kutoka Kushi, na kutoka Elamu, na kutoka Shinari, na kutoka Hamathi, na kutoka visiwa vya bahari. Naye atawatwekea mataifa bendera, atawakutanisha watu wa Israeli waliotupwa, atawakusanya watu wa Yuda waliotawanyika, kutoka ncha nne za dunia.”—Isa. 11:10-12.
7. Lile “chipukizi la mfano litokalo katika mizizi ya Yese linasemekana hapa kuwa nini, naye amefanywaje atumikie kama “ishara” kwa mataifa?
7 Hapa “chipukizi” la mfano litokalo katika mizizi ya Yese lasemekana lenyewe kuwa “shina” la Yese. Mwishoni mwa majira ya mataifa katika mwaka 1914 mfalme huyu wa Kimasihi aliinuliwa katika mamlaka ya kifalme. Akitangazwa ulimwenguni pote, ametumika kama “ishara” ambayo kwayo mabaki yote ya Waisraeli wa kiroho waliotawanyika lazima wakusanyike, kwa kuwa yeye ndiye Mfalme anayetawala. Tangu hapo, hawa waliokusanywa na kurudishwa tena wametimiza kusudi la kutiwa mafuta kwao la kuweka mbele wanadamu wote mfalme wa Kimasihi na ufalme wake.
8. Watu mmoja mmoja wa mataifa wamegeuka na kumtafuta nani sasa, nao ni akina nani ambao wamejibu maulizo yao, kukawa na matokeo gani?
8 Watu mamia ya maelfu kutoka katika mataifa yote wamegeuka sasa na kumtafuta mfalme wa Kimasihi aliye kama ishara. Wao wameridhika kwamba Yesu Kristo aliyetukuzwa kweli kweli ndiye Masihi wa Yehova aliyeahidiwa. Mabaki ya watiwa mafuta, wakiwa na majibu ya maulizo yao wamewasaidia wafanye hivyo. Kwa furaha wamejikusanya katika upande wa ufalme wa Yehova wa Kimasihi, wakiushangilia kuwa tumaini peke yake kwa wanadamu wote. Tayari wamekuwa “mkutano mkubwa,” ambao hesabu ya mwisho katika wakati wa “ile dhiki iliyo kuu” hatujui.—Ufu. 7:9-17.
“DUNIA MPYA”
9. Yehova ataziimarisha zile mbingu mpya na dunia mpya kadiri gani, nalo ni tendo la namna gani ambalo huenda likahitajiwa ili kuwaingiza watu wake katika hiyo Taratibu Mpya?
9 Taratibu mbovu ya kale, ambayo imejiimarisha sana katika dunia lazima iondoke—na kuingia katika uharibifu! Sasa Yehova anatayarisha mambo yote kwa ajili ya taratibu mpya yenye utukufu! Yeye ‘amepanda’ “mbingu” mpya za kiserikali, akaziimarisha sana katika tengenezo lake la ulimwengu wote hivi kwamba haziwezi kung’olewa na wanadamu wala mashetani. “Dunia mpya” ambayo atasimamisha ataiweka juu ya msingi imara hivi kwamba hakuna cho chote kitakachoweza kuifanya itikisike ipate kuharibika. Katika hii taratibu mpya yeye atawaleta mabaki ya Israeli wa kiroho pamoja na “mkutano mkubwa” hata kama itakuwa lazima afanye kama vile alivyofanya katika Bahari ya Shamu huko nyuma katika siku za Musa, akiyachafua maji na kuyafanya mawimbi yake yavume ili kwamba afanyize njia kusudi watu wake waliokombolewa wapate kupita. Hivi ndivyo asemavyo katika Isaya 51:15, 16:
“Mimi ni [Yehova], Mungu wako, niichafuaye bahari, mawimbi yake yakavuma. [Yehova] wa majeshi ndilo jina lake. Nami nimetia maneno yangu kinywani mwako, nami nimekusitiri katika kivuli cha mkono wangu, ili nizipande mbingu, na kuiweka misingi ya dunia, na kuuambia Sayuni, Ninyi ni watu wangu.”
10. Yehova ameweka maneno yake katika kinywa cha nani, na ni kwa sababu gani yeye amewalinda hawa kwa kivuli cha mkono wake?
10 Hakuna kizuizi cho chote ambacho adui wanaweka mbele ya Yehova kitakuwa kisichoshindika kwake. Kama vile katika Mlima Sinai Yehova alivyoweka maneno yake vinywani mwa watu wake wateule kupitia kwa mpatanishi Musa, na baada ya hapo akawaongoza chini ya kivuli chenye ulinzi cha mkono wake na kuwaingiza katika Nchi ya Ahadi, ndivyo amefanya kwa ajili ya mabaki ya Israeli wa kiroho. Yeye ameweka neno lake, ujumbe wa wakati huu, vinywani mwa mabaki ya kiroho ili wapate kukiri mbele ya ulimwengu wote, kwa ajili ya wokovu wao wenyewe na wa wale watakaosikia na kuitikia. “Mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine” wametenda ifaavyo juu ya yale ambayo wamesikia nao wametia maneno ya Mungu vinywani mwao. Kwa sababu hawa wote wamekuwa mashahidi wake Wakristo, Yehova huwalinda chini ya kivuli cha mkono wake katika ulimwengu huu.
11. (a) Yehova atawafanya hawa mabaki waliolindwa kuwa sehemu ya nini, naye atakiri nini juu yao? (b) Mungu atafanya “mkutano mkubwa” uliolindwa kuwa nini, nao watasemekana kuwa watu wa nani?
11 Yehova ana kusudi fulani katika tendo hili lake. Kusudi lake ni kwamba mwishowe awafanye hawa mabaki waaminifu sehemu ya “mbingu” mpya za kiserikali kama warithi wa shirika pamoja na Mfalme Yesu Kristo. Na kwa habari za “mkutano mkubwa” wa “kondoo wengine,” Yehova atawafanya kuwa sehemu ya kwanza ya ile “dunia mpya,” ile jamii mpya ya kidunia katika Taratibu Mpya. Kwa kuhifadhi hai mabaki waaminifu wa Israeli wa kiroho waipite “ile dhiki iliyo kuu” inayokuja, yeye atakuwa akiwaambia hawa Israeli wa kiroho ambao ‘wanakaribia Mlima Sayuni wa kimbinguni,’ “Ninyi ni watu wangu.” (Ebr. 12:22; Isa. 51:16) Vilevile, “maskani ya Mungu” yenye ulinzi itaanza kuwa pamoja na “mkutano mkubwa” uliookoka, na, kama vile Ufunuo 21:3 unavyosema, “watakuwa watu wake.”
12. Ni roho gani ambayo haitakuwapo katika hiyo Taratibu Mpya, nao wale wanaotazamia kuiingia wanajazwa kwa kitu gani sasa?
12 Roho takatifu itatenda na kuenea katika hiyo taratibu mpya yenye kuizunguka dunia. Yehova atakuwa amekwisha kuiondoa ile “roho” yenye kuchafua ‘itendayo kazi sasa katika wana wa kuasi.’ Hao “wana wa kuasi” watakuwa wamekwisha haribiwa katika “ile dhiki iliyo kuu” naye Shetani Ibilisi na mashetani zake watakuwa wamekwisha kufungiwa shimoni. (Efe. 2:2; Ufu. 201-3) Wanapojitayarisha kwa ajili ya hiyo Taratibu Mpya, wale wanaotazamia kuiokoka hiyo “dhiki iliyo kuu” wanaendelea ‘kujazwa kwa roho’ kutoka kwa Mungu.—Efe. 5:18.
13. Katika hiyo Taratibu Mpya ni jambo gani litakalotokea ambalo hata sayansi ya utabibu ya kisasa haiwezi kutokeza jambo la kulingana nalo?
13 Twaweza kujaribu tu kuwazia namna itakavyokuwa hapa duniani baada ya “vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi” katika Har–Magedoni na baada ya Shetani na mashetani zake kufungiwa katika “shimo.” Ndipo roho takatifu itakapotenda kwa uhuru duniani pote. Tunakumbushwa jinsi roho takatifu ilivyotenda kiajabu katika siku za Yesu Kristo na mitume wake walipokuwa duniani karne 19 zilizopita. Miujiza yenye kustaajibisha ilifanyika, kwa furaha isiyoneneka ya watu waliofaidika kutokana nayo. Sayansi ya utabibu ya kisasa iliyoendelea sana haina jambo linaloweza kulingana na maponyo na mapozo ya mara moja yaliyofanyika kupitia kwa roho takatifu. Hata watu walifufuliwa kutoka kwa wafu! Na hata jambo lililo bora zaidi ya hayo, vilevile kulikuwako maponyo ya kiroho, kwa njia ya kutangaza na kufundisha juu ya ufalme Mungu wa Kimasihi. Kulikuwako kuwekwa huru kwa wale waliokuwa wamefungwa katika utumwa wa dini ya kimapokeo, ya uongo na yenye kuleta kifo.—Kutoka Holy Spirit—The Force Behind the Coming New Order, Sura ya 9.