Kudumisha Uaminifu wa Kimaadili wa Kikristo Katika Liberia Yenye Kukumbwa na Vita
Kama ilivyosimuliwa na mwenye kujionea mwenyewe
“NDOVU wanapopigana, nyasi zitaumia pia.” Mithali hiyo inafanya muhtasari mzuri kama nini wa lile lililotukia wakati wa vita ya hivi karibuni katika Liberia! Watu 20,000 hivi walipoteza maisha zao, na nusu ya idadi ya watu wa nchi hiyo ya milioni 2.6 walipoteza makao yao. Wengi wa wale walioumia hawakuwa askari-jeshi; walikuwa “nyasi”—wanaume, wanawake, na watoto wasioweza kudhuru wengine.
Vita ilipoanza katika Desemba 1989, Mashahidi wa Yehova karibu 2,000 katika Liberia walikuwa wakionea shangwe maongezeko ya taratibu katika idadi yao na walikuwa wakitazamia wakati ujao wakiwa na uhakika. Kwa kuhuzunisha, walikuwa sehemu ya ‘nyasi iliyoumia.’
Mweneo wa Vita
Vita ilianza kwenye mpaka wa Liberia na Côte d’Ivoire (Koti divwaa), na upesi wakimbizi wakaanza kukimbia hadi mji mkuu, Monrovia, mji ulio na wakaaji zaidi ya nusu milioni. Kutoka Machi hadi Mei ya 1990, mapigano yalipokuwa yakielekea kusini, wamishonari wa Mashahidi wa Yehova walihamishwa kwanza kutoka Ganta na kisha kutoka Gbarnga (Banga). Walikuwa miongoni mwa wakaaji wa mwisho walioiondoka miji hiyo. Vita ilifikia upeo wakati majeshi yenye silaha walipoingia Monrovia Julai 2, 1990.
Hakuna mtu yeyote aliyekuwa tayari kwa ajili ya maafa yaliyofuata. Majeshi mbalimbali matatu waliendelea kupigana barabarani wakitumia vifaru, roketi, na vyombo vya kutupilia makombora madogo, hadi mwisho wa vita. Wale ambao hawakuuawa kwa sababu ya kuwa washiriki wa kabila lililochukiwa walipatwa na uchokozi na kupekuliwapekuliwa kwa daima. Usiku mmoja wa Agosti wanaume, wanawake, na watoto zaidi ya 600 waliokuwa wamepata mahali pa salama katika Kanisa la Kilutheri la Mt. Petro waliuawa na kikosi kilichotiwa kichaa cha vita cha kuua.
Mamia walikimbia mapigano hayo wakiwa tu na nguo waliyokuwa wamevaa. Familia ziligawanyika na kwa miezi kadhaa baadaye hazikuweza kuunganika tena. Wakaaji wote wa Monrovia walionekana kana kwamba wanahama, nyumba tupu zikiwa zimekaliwa na askari-jeshi na wakimbizi waliokuwa wamekimbia kutoka sehemu nyingine za mji. Zaidi ya nusu ya idadi ya watu wa Monrovia walipoteza makao yao. Walio wengi walipoteza mali zao zote na pia angalau mtu mmoja wa ukoo katika kifo. Wengine walipoteza wengi zaidi.
Hali ilifikia upeo wa hatari hivi kwamba nchi nyingine tano za Afrika Magharibi zilituma askari-jeshi ili wajaribu kurudisha amani. Kufikia mwisho wa Oktoba 1990, sehemu kubwa ya mapigano ilikuwa imekoma. Hali ya njaa iliyofuata katika mji huo ulioteketezwa ilikuwa kama sanda. Mashirika ya kutoa msaada yaliripoti kwamba wakati mmoja karibu theluthi moja ya watoto wa Monrovia waliokuwa chini ya umri wa miaka mitano walipatwa na ugonjwa wa kukosa chakula kinachofaa na watu zaidi ya mia moja walikuwa wakifa kila siku. Watafutaji faida hawakufanya hali iwe rahisi zaidi; wengi waliiba mchele uliokusudiwa kuwa wa msaada na kisha kuuuza kwa dola 20 au zaidi kwa kila kikombe. Magonjwa yalikuwako daima, hasa kipindupindu, kwa kuwa utumishi mbalimbali wa maji, usafi, na umeme wa mji huo ulikuwa umeharibiwa kabisa.
Mashahidi wa Yehova karibu elfu moja walioishi Monrovia waliumia vibaya pia. Wengi wao walikimbia mji huo na kwenda mashambani, hali wengine waliondoka kwa meli kuelekea Ghana na Naijeria au kwa barabara kwenda Côte d’Ivoire au Sierra Leone. Kutoka Julai hadi Desemba 1990, Mashahidi zaidi ya 30 walipoteza maisha zao. Wengine waliuawa kwa bunduki, hali wengine walikufa kutokana na matokeo ya magonjwa na njaa. Alan Battey na Arthur Lawson, wamishonari Waamerika waliohitimu kutoka Shule ya Kuzoezwa ya Huduma, yaonekana walikuwa miongoni mwa wale waliouawa. Lo, jinsi tumaini la ufufuo lenye msingi wa Biblia lilivyo la faraja kwa wale kati yetu waliopoteza watu wa ukoo au rafiki katika wakati huo uliokuwa mbaya sana!—Matendo 24:15.
Udugu wa Kikristo Katika Utendaji
Vita ilipokuwa ikiendelea, Mashahidi wengi waliopoteza makao yao walikimbilia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova na nyumba ya mishonari kwenye upande ule mwingine wa mji ili wapate usalama. Wengine walitafuta himaya kwa sababu walikuwa wa kabila ambalo askari-jeshi wa eneo hilo walikuwa wakiua. Wengi wao walipewa migawo ya kazi katika ofisi ya tawi nao walisaidia sana na upishi na kusafisha, hali wengine walipewa mgawo wa kutafuta mboga zinazoweza kulika katika bwawa lililokuwa karibu wakati hali za nje ziliporuhusu.
Watu walikuwa wakilala kila mahali, katika vyumba vya wamishonari, katika ujia kati ya vyumba, katika Idara ya Usafirishaji, na katika ofisi. Tulichimba na kutunza vyoo. Wanawake walipewa migawo ya kuwa wauguzi, nao walitunza kwa mafanikio wengi waliopatwa na malaria na homa. Kuhara kulikuwa tatizo mara nyingi.
Tulipanga utaratibu wa pekee wa nyumbani, kutia na mazoezi ya jinsi ya kufanya wakati bomu linapolipuka. Hivyo, wakati majeshi yenye kupinga yalipofyatua makombora, tulizoezwa kufikia kwa haraka sehemu za tawi zenye ulinzi. Ingawa ukuta wetu wenye urefu wa meta 3 ulikuwa ulinzi wa kadiri fulani, haukuwa wa kutosha kukinza mruko wa risasi. Upesi paa yetu ilikuja kuwa na sura kama ya chombo cha kutikisia pilipili-manga kwa sababu ya mashimo yote iliyopata!
Wengi walihatarisha maisha zao ili walinde Mashahidi wenzao kutoka kwa wale waliotaka kuwaua kwa sababu walikuwa wa kabila lililochukiwa. Siku moja dada Mkristo mwenye machozi aliwasili ofisi ya tawi pamoja na watoto wake waliookoka, mmoja akiwa kitoto cha umri wa majuma mawili. Mume wake na mwana wake mtineja walikuwa tu wameuawa kwa bunduki mbele ya macho yake. Yeye na watoto wake wengine walikuwa wamefichwa kwa mafanikio na Shahidi mwingine wakati wauaji waliporudi kuwatafuta.
Familia nyingine iliwasili kwenye tawi ikiwa na mhubiri asiyebatizwa aliyekuwa amesaidia kuilinda isiuawe na watu wa kabila lake. Halafu, hali ilipobadilika na yule mhubiri asiyebatizwa alipokuwa hatarini, familia hiyo ilimwokoa kutoka kwa watu wa kabila layo.
Tena na tena, wamishonari wangesema na wanaume wenye silaha waliokuwa kwenye malango ya ofisi ya tawi ili wajaribu kuwafanya wasipekuepekue au kuteka vitu kutoka makao hayo. Wakati mmoja kikundi cha watu wenye hasira kiliingia kwa mshindo, kikituelekezea bunduki na kusisitiza kwamba tulikuwa tumewaficha watu wa kabila fulani. Walishangaa kuona jinsi Mashahidi wa mahali hapo walivyojiendesha kwa upole, wakiwa wameketi kimya na kuusikiliza mkutano wa Kikristo tuliokuwa tukifanya. Walipekuapekua nyumba lakini hawakupata lile walilokuwa wakitafuta. Tuliweza sikuzote kuhakikishia wavamizi kwamba hatukuwa tunawaficha askari-jeshi au adui yao yeyote. Tukiwa Wakristo sisi hatukuwamo.
Wakati mmoja katika pindi ya mapigano makali, kikundi cha Mashahidi waliwasili kwenye tawi wakimbeba ndugu aliyekuwa na kansa inayoua. Kwa kuhuzunisha, alikufa muda mfupi baadaye. Kaburi lilichimbwa shambani, na tulikuwa na hotuba ya maziko ya kihisiamoyo kama nini! Ndugu huyo alikuwa amekuwa mmoja wa wazee wema sana wa mahali hapo, akiwa na miaka mingi ya utumishi mwaminifu. Watu karibu na mia moja waliopoteza makao yao walikusanyika katika sebule kwa ajili ya hotuba ya ukumbusho, iliyotolewa kukiwa na sauti ya bunduki zikifyatuliwa.
Kupata Chakula na Maji
Ugavi wa chakula ulikuwa haba sana. Hata kabla ya vita kuanza, wafanya biashara walikuwa wameacha kuingiza vifaa nchini. Hivyo, chakula kidogo sana kilikuwa kimebaki mjini. Ugavi wetu wa chakula kwenye tawi ungewatosha washiriki 12 wa familia yetu kwa muda wa miezi mingi, lakini nyakati nyingine tulikuwa na watu zaidi ya 200 wakiishi nasi, kutia na jirani wasiokuwa Mashahidi waliohitaji msaada sana. Kila mtu alilazimika ale mlo mdogo mmoja kila siku; tuliweza kuendelea kuishi na posho za jinsi hiyo kwa miezi kadhaa. Kila mtu alikuwa na njaa. Watoto walikuwa wembamba sana, wakinyong’onyea mikononi mwa wazazi wao.
Upesi ugavi wetu wa chakula ulikuwa ukiisha. Tungeweza kupata wapi chakula kingine? Hakuna duka lolote lililokuwa wazi Monrovia. Kila mahali mtu alipoangalia, watu wenye njaa walikuwa wakizungukazunguka wakitafuta chakula. Watu walikula kitu chochote—kutia ndani mbwa, paka, na panya. Wamishonari wawili kutoka tawi waliamua kujaribu kwenda Kakata, mji uliokuwa na umbali wa kilometa 60 kutoka hapo, ambapo mapigano yalikuwa yameisha.
Waliweka magazeti ya Mnara wa Mlinzi na ishara katika madirisha ya gari ili kujitambulisha wenyewe kuwa Mashahidi wa Yehova. Baada ya kupita vituo mbalimbali vya uchunguzi, walisimamishwa na kuulizwa maswali na mwanamume mkubwa mwenye maungo mapana aliyekuwa na makombora madogo yakining’inia kifuani pake na bastola kwenye upande wake. Walijitambulisha wenyewe kuwa Mashahidi wa Yehova na kumwambia walitaka kwenda Kakata kupata chakula.
“Nifuateni,” akasema. “Mimi ni kamanda wa vita hapa.” Aliwapeleka kwenye makao yake makuu. Alipopata kujua kwamba walikuwa wanaweka watu waliopoteza makao yao, aliwaamuru wanaume wake wapeleke kwenye tawi letu mifuko 20 ya mchele, kila mmoja ukiwa na uzito wa kilo 45! Pia, walipewa cheti cha ruhusa kwenda Kakata, na mlinzi mwenye silaha alipewa mgawo wa kuwaongoza kwa usalama kupitia vituo vya uchunguzi vilivyobaki.
Huko Kakata walipata ndugu wetu wa Kikristo Abraham aliyekuwa na duka. Alikuwa ametuwekea akibani katoni za chakula, kutia na maziwa ya unga, sukari, mboga za mkebeni, na vifaa vingine vilivyohitajiwa. Ilipendeza kweli kweli kuona njia ambayo ndugu zetu walitunzwa kwenye safari yao. Ni lazima Yehova awe alipendezwa kwamba tulishiriki chakula chetu pamoja na rafiki na jirani zetu, kwani sasa ugavi wetu ulikuwa unajazwa tena.—Mithali 11:25.
Kwenye upande ule mwingine wa Monrovia, wamishonari katika nyumba ya mishonari walikuwa pia wakitunza wenye kupoteza makao yao, nao pia walipokea msaada kutoka kwa vyanzo visivyotazamiwa. Kwa mfano, mishonari mmoja alipata mifuko mitatu ya mchele kutoka kwa askari-jeshi mmoja aliyemkumbuka tangu wakati ambao alikuwa ametumikia katika eneo la askari-jeshi yapata miaka 16 mapema. Mishonari mwingine alipata mifuko minne ya mchele baada ya mahoji ya kibinafsi pamoja na kiongozi wa mojawapo ya mafarakano yaliyokuwa yakipigana.
Wakati mmoja ilionekana kana kwamba tungalipaswa kuacha tawi kwa sababu ya upungufu wa maji. Kwa wakati fulani kisima chetu kilikuwa chanzo cha pekee cha maji ya kunywa kwa wengi katika jumuiya. Hata hivyo, ugavi wa mafuta kwa ajili ya mtambo wa jenereta ya umeme wa bomba letu ulianza kuisha. Mwanamume mmoja aliyekuwa amepata himaya kwenye tawi katika siku za mwanzo-mwanzo wa mapigano aliposikia tatizo letu, alitupatia mafuta kwa kuthamini yale tuliyokuwa tumemfanyia, kwa hiyo ugavi wetu wa maji haukupata kuisha kamwe.
Kudumisha Nguvu ya Kiroho
Wakati sisi wamishonari wa mwisho tuliposihiwa kuondoka Liberia katika Octoba 1990, jambo kuu akilini mwetu lilikuwa, Ndugu na dada zetu watakabilianaje? Kutokana na ripoti ambazo tumepokea tangu wakati huo, ni wazi kwamba wameendelea kuwa wenye shughuli katika huduma.
Kabla ya vita hiyo wastani wa idadi ya saa kila Shahidi alitumia katika huduma ulikuwa karibu 17 kila mwezi. Hata hivyo, wakati wa vita, ujapokuwa ule uhitaji wa daima wa kutafuta chakula vichakani, Mashahidi katika makundi mengine walikuwa na wastani wa saa zaidi ya 20 kwa kila mhubiri! Isitoshe, kwa sababu ya upungufu wa magazeti ya Mnara wa Mlinzi, wengi wa dada zetu walinakili makala ya mafunzo kwa mkono ili kwamba kungekuwako nakala zaidi kuwatosha wote kwa funzo la Jumapili.
Makundi manne yaliyo karibu zaidi na Monrovia yalikuwa na Mashahidi wengi sana waliokimbia mapigano ya mjini. Rafiki hao walipoteza kila kitu walichokuwa nacho, kwa kuwa hawakuweza kurudi kwenye nyumba zao ili kuchukua kitu chochote. Kwa kweli, kwa miezi kadhaa wengi hata walikuwa kwenye pande tofauti za vita na watoto na wazazi wao wenyewe! Kwa Ukumbusho wa kifo cha Yesu Machi 30, makundi hayo manne yalikuwa na hudhurio la jumla la 1,473.
Mashahidi 300 au hivi waliobaki katika Monrovia walifanya jitihada ya pekee kufanya upainia msaidizi katika pindi ya mwezi wa Ukumbusho, hata ingawa majuma machache kabla ya hapo walikuwa wamekuwa wadhaifu sana kimwili kutokana na njaa hivi kwamba hawakuweza hata kutembea. Walijitahidi sana kuwaalika watu kwenye Ukumbusho, na 1,116 walihudhuria.
Mzee Mkristo mmoja katika Monrovia alieleza hivi: “Tuliamua kuanza kukutana katika Jumba la Ufalme letu tena kuanzia Desemba 1990. Hudhurio letu la kwanza lilikuwa 17. Baadaye liliongezeka hadi 40, na lilibaki katika idadi ya 40 na kitu, kwa muda fulani. Kisha Februari 24, hudhurio letu likaongezeka hadi 65 na juma moja baadaye hadi 85. Pia, karibu wote katika kundi waliitikia mwito wa kufanya upainia msaidizi katika Machi.”
Kutunza Wengine
“Ndugu zetu wa kanisa walikuwa wakijishughulisha sana na kuuana mmoja na mwenzake [kutoka makabila yenye kupingana] katika pindi ya vita,” akasema mtu wa ukoo wa mmoja wa Mashahidi, asiye Shahidi, “wasiwe kamwe na wakati kwa ajili ya waamini wenzao.” Lakini hali ilikuwa tofauti kama nini kwa watu wa Yehova!
Kwa mfano, mwenyekiti wa kikundi cha kutoa msaada wa ujirani, aliwaandikia ndugu waliokuwa wakilitunza tawi katika Februari 1991 hivi: “Barua hii yatumikia ikiwa ishara ya shukrani na uthamini kwenu na kwa shirika lenu kwa ajili ya mahali pa kuwekea vitu akiba ambapo mnaendelea kutupa sisi katika pindi hii ya ugawanyaji chakula kwa watu wetu. Tendo lenu la huruma laonyesha nia yenu mkiwa Sosaiti ya kuleta amani na hali njema nchini. Tafadhali endeleeni na utumishi wenu mzuri.”
Mashahidi wa Yehova katika nchi nyingine walikuwa haraka kuitikia mahitaji ya ndugu zao wa Liberia. Msaada umetolewa kutoka nchi kama vile Sierra Leone na Côte d’Ivoire katika Afrika Magharibi, Uholanzi na Italia katika Ulaya, na United States.
Msichana mmoja mdogo, ambaye mama yake aliuawa kwa sababu alikuwa wa kabila lililochukiwa, alionyesha shukrani yake kwa msaada aliopokea. Aliandika hivi: “Asanteni sana kwa vitu vyote mlivyonipelekea. Mnanifanya nihisi kana kwamba mama yangu yu karibu nami. Yeye na ndugu yangu mdogo waliuawa katika vita. Namwomba Yehova awabariki nyinyi wote. Nina umri wa miaka 11.”
Pia akishukuru kwa ajili ya msaada aliopokea, ndugu mwenye familia ya watu sita na ambaye mke wake alilazimika ajifiche kwa miezi kadhaa kwa sababu ya kabila lake aliandika hivi: “Sisi hatujaingia nyumba za watu kwa nguvu kuteka na kuuza mali yao na hata hivyo, tofauti na jirani zetu, tuna kitu cha kula kila siku kwa sababu twajua jinsi ya kutumia kwa hekima kile kidogo tulicho nacho. Hilo tumejifunza kwa Yehova.”
Yenye kuvutia sana pia ilikuwa ile roho iliyoonyeshwa na ndugu aliyekimbia hadi Côte d’Ivoire pamoja na mke na watoto wake wawili. Alikuwa ameacha nyumba yake nzuri iliyoteketezwa kabisa baadaye. Hata hivyo alisema kwamba jambo lililomwumiza zaidi lilikuwa si kupoteza nyumba yake, bali maktaba yake ya kitheokrasi!
Masomo Yenye Thamani Yaliyofunzwa
Kwa kufikiria yaliyotukia, ninathamini kwamba Yehova alitufunza sisi masomo mengi yenye thamani. Kuwajua kibinafsi wengi waliodumisha uaminifu wao wa kimaadili na kuokoka, na pia wengine waliodumisha uaminifu wao wa kimaadili na kufa, nilijifunza kuthamini umaana wa kuwa na mwelekeo wa akilini wa mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Kama tukiishi, twaishi kwa Bwana [Yehova, NW], au kama tukifa, twafa kwa Bwana [Yehova, NW]. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana [Yehova, NW].”—Warumi 14:8.
Mishonari mwingine aliyetumikia kwa muda mrefu alisema hivi: “Kupitia hayo yote, tulijifunza kwamba Yehova ni Msaidizi asiye na kifani. Kama vile Paulo alivyosema: ‘Sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti katika nafsi zetu; ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu, awafufuaye wafu.’” (2 Wakorintho 1:9; Zaburi 30:10) Aliongeza hivi: “Vita hiyo ilituelewesha wazi kwamba watu wa Yehova kwa kweli ni udugu, wenye kujivika upendo wa kujidhabihu uliokaziwa na Yesu.”—Yohana 13:35.
Barua kutoka kwa dada wa Liberia kwa wamishonari wengine wetu waliolazimika kuondoka nchini Oktoba 1990 katika pindi ya vita inaonyesha nguvu ya udugu wetu wa Kikristo. “Ni sala yangu kwamba nyinyi wote mtarudi Liberia karibuni na tuweze kuwa na kusanyiko,” yeye akaandika. “Lo! siwezi kuingojea siku hiyo. Kuifikiria tu kwanifurahisha.”
Naam, itapendeza sana kuona utaratibu wa kawaida wa utendaji wa Kikristo ukiwa umerudishwa kikamili katika Liberia. Dada yetu yu sahihi; kusanyiko la kwanza katika Monrovia baada ya kurudi kwa wamishonari na wakimbizi wengine litakuwa lenye shangwe. Hapana shaka juu ya hilo!
[Ramani katika ukurasa wa 27]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa.)
LIBERIA
Monrovia
Kakata
Gbarnga
Ganta
SIERRA LEONE
GUINEA
COTE D’IVOIRE
Bahari ya Atlantiki
[Picha katika ukurasa wa 28]
Watoto wa Mashahidi waliopoteza makao yao kwenye ofisi ya tawi katika pindi ya vita
[Picha katika ukurasa wa 31]
Wakimbizi wa Liberia wakigawanya mavazi yaliyotolewa na Mashahidi katika Côte d’Ivoire