Unaweza Kuhubiri Isivyo Rasmi!
1. (a) Inamaanisha nini kuhubiri isivyo rasmi? (b) Ni wangapi katika mkutano huu ambao walihubiriwa isivyo rasmi kwa mara ya kwanza?
1 Ni watu wangapi katika kutaniko lenu waliojifunza kweli kwa mara ya kwanza kupitia mahubiri yasiyo rasmi? Huenda ukashangaa kujua ni wangapi. Kuhubiri isivyo rasmi hutia ndani kuwaeleza habari njema watu tunaokutana nao katika shughuli zetu za kila siku, kama vile tunaposafiri, tunapowatembelea watu wa ukoo au majirani, tunaponunua vitu, tunapokuwa shuleni, kazini, na mahali penginepo. Katika kikundi kimoja cha Mashahidi 200 waliobatizwa, asilimia 40 kati yao walihubiriwa isivyo rasmi kwa mara ya kwanza! Kwa hiyo, njia hiyo ya kuhubiri ina matokeo sana.
2. Ni mifano gani ya mahubiri yasiyo rasmi inayopatikana katika Biblia?
2 Waeneza-injili katika karne ya kwanza walihubiri isivyo rasmi mara kwa mara. Kwa mfano, Yesu alipokuwa akisafiri kupitia Samaria, alimhubiria mwanamke fulani aliyekuwa akiteka maji katika chemchemi ya Yakobo. (Yoh. 4:6-26) Filipo alianza mazungumzo na ofisa Mwethiopia aliyekuwa akisoma kitabu cha Isaya kwa maneno haya: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” (Mdo. 8:26-38) Paulo alipokuwa ametupwa gerezani huko Filipi, alimhubiria mlinzi wa jela. (Mdo. 16:23-34) Baadaye, Paulo alipokuwa chini ya kifungo cha nyumbani ‘alikuwa akiwakaribisha kwa fadhili wale wote walioingia ndani kwake, akiwahubiria ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo.’ (Mdo. 28:30, 31) Wewe pia unaweza kuhubiri isivyo rasmi hata kama wewe ni mwenye haya. Jinsi gani?
3. Ni nini kinachoweza kutusaidia ikiwa sisi ni wenye haya?
3 Jinsi ya Kuanza: Wengi wetu huona ikiwa vigumu kuanzisha mazungumzo na watu tusiowajua. Hata huenda ikawa vigumu kuwahubiria watu tunaowajua. Hata hivyo, tutachochewa kuwahubiria ikiwa tutatafakari wema wa Yehova, hazina za kiroho ambazo amewapa watumishi wake, na hali mbaya ambazo watu wanakabiliana nazo katika ulimwengu. (Yona 4:11; Zab. 40:5; Mt. 13:52) Zaidi ya hayo, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie ‘kujipa ujasiri.’ (1 The. 2:2) Mwanafunzi mmoja wa Shule ya Gileadi alisema: “Nimetambua kwamba sala inasaidia wakati ambapo ni vigumu kwangu kuzungumza na watu.” Ikiwa unasita kusema, toa sala fupi ya kimyakimya.—Neh. 2:4.
4. Tunaweza kujitahidi kufanya nini mwanzoni, na kwa nini?
4 Tunapohubiri isivyo rasmi, hatuhitaji kuanza mazungumzo kwa njia rasmi au kwa kusoma andiko kama tunavyofanya tunapohubiri nyakati nyingine. Linaweza kuwa jambo bora kujitahidi kuanzisha mazungumzo bila kuhisi kwamba ni lazima tuhubiri moja kwa moja. Wahubiri wengi wanasema kwamba kwa kufanya hivyo wanapata ujasiri wa kuwaambia watu kuhusu habari njema hatimaye. Ikiwa mtu hataki mazungumzo, hakuna haja ya kumlazimisha azungumze nawe. Malizia mazungumzo kwa upole na uendelee na shughuli zako.
5. Ni nini ambacho humsaidia dada mmoja mwenye haya kuhubiri isivyo rasmi?
5 Dada mmoja mwenye haya huanza kwa kumtazama mtu na kutabasamu anapokuwa akinunua vitu sokoni. Mtu huyo anapotabasamu pia, dada huyo husema maneno machache. Ikiwa mtu huyo anaitikia vema, dada huyo hupata ujasiri wa kuendeleza mazungumzo. Dada huyo husikiliza kwa makini na kujaribu kujua ni ujumbe gani unaomfaa mtu huyo. Kwa kufanya hivyo, amewapa watu vichapo vingi na hata ameanzisha funzo la Biblia.
6. Tunaweza kuanzishaje mazungumzo yasiyo rasmi?
6 Kuanzisha Mazungumzo: Tunaweza kufanya nini ili kuanzisha mazungumzo? Yesu alipozungumza na mwanamke fulani katika kisima, alianza kwa kumwomba maji tu. (Yoh. 4:7) Kwa hiyo, tunaweza kuanzisha mazungumzo kwa salamu za kirafiki au kuuliza swali. Mnapoongea, unaweza kupata nafasi ya kutoa wazo la Kimaandiko na labda upande mbegu ya kweli. (Mhu. 11:6) Wengi wamefanikiwa kwa kusema maneno yenye kuamsha fikira ambayo huwafanya wengine watake kupata habari zaidi. Kwa mfano, unaposubiri kumwona daktari, unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema, “Nitafurahi sana wakati ambapo sitakuwa mgonjwa tena.”
7. Kuwa watambuzi kunaweza kutusaidiaje kuhubiri isivyo rasmi?
7 Kuwa watambuzi kutatusaidia pia kuanzisha mazungumzo. Tunapomwona mzazi aliye na watoto wenye tabia nzuri, tunaweza kumpongeza na kumwuliza, “Ni nini ambacho kimekusaidia kufanikiwa kuwa mzazi mzuri?” Dada mmoja husikiliza mambo ambayo wafanyakazi wenzake huzungumzia na kisha kutayarisha ujumbe wake kulingana na mambo yanayowapendeza. Alipojua kwamba mwanamke fulani kazini alikuwa akipanga harusi, alimpa nakala ya gazeti la Amkeni! iliyohusu jinsi ya kupanga harusi. Jambo hilo liliongoza kwa mazungumzo zaidi ya Biblia.
8. Tunaweza kutumiaje vitabu vyetu kuanzisha mazungumzo?
8 Njia nyingine ya kuanzisha mazungumzo ni kwa kusoma vitabu vyetu tunapokuwa mahali ambapo wengine wanaweza kutuona. Ndugu mmoja hufungua makala inayovutia katika gazeti la Mnara wa Mlinzi au Amkeni! na kuanza kusoma. Anapotambua kwamba mtu aliye karibu anatazama gazeti hilo, yeye huuliza swali au kutoa maelezo mafupi kuhusu makala anayosoma. Mara nyingi hilo humwezesha kuanzisha mazungumzo na kutoa ushahidi. Kuacha kimojawapo ya vitabu vyetu mahali ambapo watu wanaweza kukiona, kunaweza kuwachochea wafanyakazi au wanafunzi wenzetu kuuliza maswali kukihusu.
9, 10. (a) Tunaweza kutumiaje nafasi zinazojitokeza ili kuhubiri isivyo rasmi? (b) Je, umefanikiwa kufanya hivyo?
9 Kutumia Nafasi Zinazojitokeza: Kwa kuwa kazi ya kuhubiri inahitaji kufanywa kwa uharaka sana, tunapaswa kuwa na mipango mizuri kuhusiana na mahubiri yasiyo rasmi. Tunapaswa kutumia nafasi zinazojitokeza katika shughuli zetu za kila siku ili kuhubiri. Fikiria kimbele kuhusu watu ambao huenda utakutana nao, na ufikirie jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo ya kirafiki. Beba Biblia yako na vitabu vinavyotegemea Biblia ambavyo unaweza kuwatolea watu ambao watapendezwa.—1 Pet. 3:15.
10 Kwa kufikiria kimbele, wahubiri wengi wametafuta njia za kutumia nafasi zinazojitokeza za kuhubiri isivyo rasmi. Dada fulani anayeishi katika jengo lenye ulinzi mkali hutumia eneo la burudani la jengo hilo, kupanga vipande vya michezo-fumbo ambavyo hutokeza picha za mandhari maridadi. Watu wanaposimama na kuongea naye kuhusu mandhari hizo nzuri, yeye hutumia nafasi hiyo kuanzisha mazungumzo na kuwaambia juu ya ahadi ya Biblia ya “mbingu mpya na dunia mpya.” (Ufu. 21:1-4) Je, unaweza kufikiria njia nyingine za kutumia nafasi zinazojitokeza ili kuhubiri isivyo rasmi?
11. Tunaweza kuwafuatiaje watu wanaopendezwa tunapowahubiria isivyo rasmi?
11 Kufuatia Wanaopendezwa: Ukipata mtu anayependezwa, fanya mipango ili ufuatie upendezi. Ikifaa, unaweza kumwambia: “Nimefurahi sana kuzungumza nawe. Ninaweza kukupata namna gani ili tuzungumze tena?” Wahubiri wengine huwapa watu anwani zao na namba zao za simu na kusema: “Nimefurahia sana mazungumzo yetu. Ikiwa ungependa kujua zaidi kuhusu mambo ambayo tumezungumzia, unaweza kunipata kupitia anwani hizi.” Ikiwa huwezi kumfuatia mtu huyo, jaza fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43) bila kukawia na umpe mwandishi wa kutaniko lenu.
12. (a) Kwa nini tuweke rekodi ya muda tunaotumia kuhubiri isivyo rasmi? (b) Kuhubiri isivyo rasmi kumekuwa na matokeo gani? (Ona sanduku “Kuhubiri Isivyo Rasmi Kuna Matokeo!”)
12 Tunapaswa kuripoti muda tunaotumia kuhubiri isivyo rasmi. Hivyo, hakikisha umeweka rekodi ya muda huo hata kama ni dakika chache tu. Fikiria hili: Ikiwa kila mhubiri angehubiri isivyo rasmi kwa dakika tano kila siku, hiyo ni jumla ya saa milioni 17 kila mwezi!
13. Ni nini kinachopaswa kutusukuma kuhubiri isivyo rasmi?
13 Tuna sababu nzuri sana za kuhubiri isivyo rasmi, yaani, upendo kwa Mungu na kwa jirani. (Mt. 22:37-39) Mioyo iliyojaa uthamini wa sifa za Yehova na makusudi yake hutusukuma tuseme juu ya “utukufu wa fahari ya ufalme wake.” (Zab. 145:7, 10-12) Hangaiko la moyoni kwa jirani zetu hutusukuma tutumie kila nafasi inayojitokeza kuhubiri habari njema wakati ukiwa ungalipo. (Rom. 10:13, 14) Kwa kujitayarisha kimbele, sote tunaweza kuhubiri isivyo rasmi na kupata shangwe ya kumjulisha ukweli mtu aliye na moyo mnyoofu.
[Blabu katika ukurasa wa 4]
Unaweza kuwa na matokeo ukijitahidi kukutana tu na watu na kuanzisha mazungumzo
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Kwa kujitayarisha vizuri, wahubiri wengi wametafuta njia za kutumia nafasi zinazojitokeza za kuhubiri isivyo rasmi
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Madokezo ya Kuanzisha Mazungumzo
◼ Mwombe Yehova akusaidie ili uanzishe mazungumzo
◼ Tafuta watu wanaoonekana kuwa wenye urafiki na wasio na haraka
◼ Watazame, utabasamu, na useme maneno machache ya mambo ambayo mnaweza kukubaliana
◼ Wasikilize vizuri wanapoongea
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Kuhubiri Isivyo Rasmi Kuna Matokeo!
• Ndugu mmoja aliwahubiria watu waliokuwa karibu naye alipokuwa katika gereji moja akisubiri gari lake lirekebishwe. Pia aliwapa mialiko kwenye hotuba ya watu wote katika kusanyiko la wilaya. Katika kusanyiko la mwaka uliofuata, ndugu huyo alisalimiwa na ndugu ambaye hakumfahamu. Alikuwa mmoja wa watu ambao alikuwa amewapa mwaliko katika gereji mwaka uliotangulia! Mtu huyo alienda kusikiliza hotuba hiyo ya watu wote na akaomba funzo la Biblia. Yeye na mke wake walikuwa tayari wamebatizwa.
• Dada mmoja ambaye alijifunza ukweli kupitia mahubiri yasiyo rasmi, huchukulia watu anaokutana nao kupitia watoto wake kama eneo lake la kibinafsi. Watu hao wanatia ndani majirani na wazazi anaokutana nao shuleni na katika mikutano ya wazazi. Anapojitambulisha, yeye husema kwa maneno machache ya kutoka moyoni kwamba Biblia imemsaidia sana katika kuwalea watoto na kisha anabadili mazungumzo na kuelekeza fikira juu ya jambo lingine. Lakini kwa kuwa ameshataja kuhusu Biblia, yeye huona ikiwa rahisi kuirejelea baadaye katika mazungumzo. Kwa kutumia mbinu hiyo, amewasaidia watu 12 kufikia ubatizo.
• Dada mmoja alipotembelewa na mwanamume mwuza bima, alitumia fursa hiyo kuhubiri isivyo rasmi. Alimwuliza mwanamume huyo kama angependa kuhakikishiwa afya njema, furaha, na uzima wa milele. Alisema ndiyo na kumwuliza dada huyo ni mpango gani wa bima alikuwa akizungumzia. Dada huyo alimwonyesha ahadi za Biblia na akampa kimojawapo ya vitabu vyetu ambacho alisoma kwa jioni moja tu. Mipango ilifanywa ili mwanamume huyo ajifunze Biblia. Akaanza kuhudhuria mikutano na baadaye akabatizwa.
• Dada mwingine alianza mazungumzo na mwanamke fulani aliyeketi kando yake ndani ya ndege walimokuwa wakisafiria na akaweza kutoa ushahidi. Safari yao ilipofika kikomo, dada huyo alimpa mwanamke huyo anwani yake na namba za simu na kumtia moyo awaombe Mashahidi wa Yehova watakapomtembelea wajifunze naye Biblia. Siku iliyofuata, Mashahidi wawili walibisha mlango wa mwanamke huyo. Mwanamke huyo alianza kujifunza Biblia, akafanya maendeleo kwa haraka na akabatizwa. Muda si muda, alikuwa anaongoza mafunzo matatu ya Biblia.
• Ndugu mmoja kipofu mwenye umri wa miaka 100 anayeishi katika nyumba ya kuwatunza wazee husema hivi mara nyingi, “Tunahitaji Ufalme.” Maneno hayo yamewafanya wauguzi na wazee wengine wanaoishi huko wamwulize maswali na hivyo ndugu huyo anapata nafasi ya kuwaeleza mambo kuhusu Ufalme. Mwanamke mmoja anayefanya kazi huko alimwuliza ndugu huyo mambo ambayo atafanya katika Paradiso. Ndugu huyo alijibu, “Nitapata kuona na kutembea tena na hivyo nitakiteketeza kwa moto kiti changu cha magurudumu.” Kwa kuwa ndugu huyo ni kipofu, yeye humwomba mwanamke huyo amsomee magazeti. Wakati binti ya ndugu huyo alipomtembelea, mwanamke huyo alimwomba binti huyo magazeti hayo akayasome nyumbani. Muuguzi mmoja alimwambia binti huyo, “Sasa, sote katika makao yetu tunakazia sana maneno: ‘Tunahitaji Ufalme.’”
• Dada fulani alikuwa akiwahudumia wateja kwenye mkahawa mmoja alipowasikia wanaume kadhaa waliokuwa wameketi humo wakizungumzia mambo ya siasa. Mwanamume mmoja akasema kwamba serikali haiwezi kusuluhisha matatizo yetu. Dada huyo akajiambia moyoni, ‘Hii ni nafasi nzuri.’ Alitoa sala fupi na akawaendea wanaume hao. Baada ya kujitambulisha, aliwaambia kuhusu serikali ambayo itasuluhisha matatizo yote ya wanadamu, yaani, Ufalme wa Mungu. Kisha akawatolea broshua aliyokuwa nayo. Muda si muda, meneja wa mkahawa huo akatokea. Dada huyo alidhani kwamba meneja angemwambia aondoke. Kinyume na hilo, meneja huyo alimwambia kuwa alikuwa akimsikiliza na yeye pia angependa broshua. Mfanyakazi mwenzake ambaye pia alikuwa akimsikiliza alimjia huku akitiririkwa na machozi. Mfanyakazi huyo alikuwa akijifunza Biblia awali na sasa alitaka kuanza kujifunza tena.