Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 9/22 kur. 19-23
  • Pigano Langu Gumu na Lililo Refu la Kutafuta Dini ya Kweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Pigano Langu Gumu na Lililo Refu la Kutafuta Dini ya Kweli
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Utafutaji Waanza
  • Mnyanyaso wa Familia Waanza
  • Upinzani wa Familia Yangu Washindwa
  • Baba Yangu Akosa Kutimiza Ahadi Yake, na Apotoa Andiko
  • Magumu Mengi, Baraka Nyingi
  • Napata Familia Mpya Yenye Upendo
  • Je! Ilifaa Nijitahidi Kushinda Watu Wote?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
    Amkeni!—1993
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 9/22 kur. 19-23

Pigano Langu Gumu na Lililo Refu la Kutafuta Dini ya Kweli

Sikuzote nilihofu kwamba ningeenda helo, nilijua kwamba sikuwa mwema kiasi cha kwenda mbinguni. Nilihisi mambo yangeenda vizuri kwangu kwenda purgatori, kwa hiyo nilisali kwa bidii na kuwasha mishumaa ili kuepuka kuishia helo.

MAGURUDUMU ya gari langu yalipokuwa yakiteleza kwenye barabara zenye barafu za njia za milimani katika Oregon, Marekani, nilijiuliza ni taabu gani nilikuwa nimejiingiza. Hii ilikuwa mara yangu ya kwanza kuendesha gari katika barafu, na sasa nilikuwa katikati ya upepo wa theluji kwenye barabara nisizozifahamu, kukiwa na mabonde yakining’inia pande zote mbili, nikiwa siwezi kabisa kuona umbali zaidi ya gari langu. Nilifikiri kwamba tungekufa, kwa hiyo nilisali kwa Mungu ahifadhi abiria wangu pamoja nami na kwamba ningemlipa kwa kurudi kanisani.

Hata hivyo, tulifaulu, na nikatimiza nadhiri yangu ya kurudi kanisani. Nilipata kanisa la mahali hapo katika Seattle kwa kutazama orodha ya majina na simu na nikaenda Jumapili iliyofuata. Nilipata hisi ileile ya utupu niliyokuwa nayo mbeleni. Hilo kanisa lilikazia kitu kilekile kama kanisa langu la mapema, pesa. Kikapu cha michango kilipitishwa mara tatu! Naweza kukumbuka nikimwambia Mungu kwamba nilihitaji kutafuta njia nyingine ya kumwabudu.

Nikiwa mtoto, nililelewa nikiwa Mkatoliki kamili katika nyumba ya kijeshi. Nilihudhuria shule ya Kikatoliki. Nakumbuka nikiwa katika darasa la katekizimu na kumwuliza mtawa wa kike: “Kwa nini hatutumii Biblia?” Niliambiwa kwamba nilikuwa mnyonge katika imani, na wazazi wangu walijulishwa juu ya tatizo langu zaidi ya mara moja.

Nililelewa nikiwa na hofu yenye kuendelea ya Mungu. Nilikuwa na dhana isiyo wazi kumhusu. Alikuwa Mungu aliyestahili kuabudiwa lakini aliyekutesa usipomwabudu ifaavyo. Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka 17, niliwaeleza wazazi wangu kuwa singeenda kanisani tena. Nilihisi nikiwa karibu zaidi na Mungu mahali penginepo licha ya kanisani. Nilikuwa nikitembea ufuoni, na ikiwa jambo fulani lilinisumbua, ningezungumza na Mungu kulihusu. Nilimwomba radhi kwa kuzungumza naye bila kupitia kasisi, nikimjulisha kwamba nilihitaji tu kumjulisha kilichokuwa akilini mwangu. Nilivunjika moyo pia kwa sababu ya kila kitu nilichoona kikitendeka ulimwenguni. Ilikuwa enzi ya mahipi, na rafiki zangu walijiingiza katika ile dhana ya kuwa kila kitu chakubalika, ngono na dawa za kulevya. Niliona matokeo yenye huzuni ya mimba zisizotakwa, utoaji-mimba, kutumia dawa kupita kiasi—sikutaka kushiriki kabisa!

Utafutaji Waanza

Becky, rafiki wa karibu, nami tuliamua kuacha koleji na kutafuta kitu kilicho bora zaidi. Lazima kulikuwa na kitu kilicho bora zaidi! Tuliamua kumtembelea mama yake katika Jimbo la Washington. Niliwaeleza wazazi wangu kwamba nilihitaji kwenda mbali, kujaribu kusahau matatizo yaliyokuwa yakinisumbua. Huo ndio wakati tuliingia katika dhoruba ya theluji huko Oregon. Baada ya kutoka kanisani kwa kuudhika Jumapili hiyo katika Seattle, nilienda nyumbani na kuongea na mama ya Becky, Edna, kuhusu hisia zangu. Aliniambia kwamba alijua mtu fulani ambaye angeweza kujibu maswali yangu. Yeye alipigia simu Mashahidi wa Yehova kwenye Jumba la Ufalme.

Nakumbuka nikiwangoja waje. Ilichukua siku tatu. Lakini walipokuja, nilifikiri walikuwa watu walioonekana kuwa Wakristo kuliko wote ambao nimepata kuona maishani mwangu. Walikuwa Clarence na Edith Meunier. Clarence alikuwa mhitimu wa Watchtower Bible School of Gilead na kwa wazi aliyajua Maandiko vizuri. Nilivutiwa mara moja walipoeleza kwamba Mungu alikuwa na jina—Yehova. Nilihisi kama kwamba taa ilikuwa imewaka kichwani mwangu. Funzo la kwanza liliendelea kwa muda wa saa tatu, wakaja siku mbili baadaye kwa funzo lingine.

Nilifurahi sana. Muda mfupi baadaye nilipigia wazazi wangu simu na kuwaeleza kuwa nilikuwa nimepata kweli. Niliwaambia kwamba Mungu ana jina, Yehova, na kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakifundisha kweli ya Biblia. Nilijua kwamba walikuwa hawajapata kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova na kwamba wangefurahi tu kama mimi kujifunza nilichokuwa nimejifunza. Hata hivyo, walikuwa wamesikia juu ya Mashahidi wa Yehova na walikasirika sana. Walikuja kunichukua turudi California.

Nilipofika nyumbani, nilijua kwamba nilihitaji kuwasiliana na kutaniko mara hiyo. Nilipata Jumba la Ufalme na kwenda kwenye mkutano uliofuata na kuketi. Dada mmoja alinitazama na kutabasamu, kwa hiyo nikamwuliza ikiwa angejifunza nami. Alishangaa sana akakubali kwa haraka. Nilifurahi sana kuwa pamoja na kutaniko tena kwa sababu nilikuwa nimeanza kujihisi nikiwa mbali na wengine. Nilihitaji ushirika.—Waebrania 10:24, 25.

Mnyanyaso wa Familia Waanza

Wazazi wangu bado walikuwa wakipinga sana dini yangu mpya wakanipeleka kwa daktari wa akili. Wazazi wangu walipoombwa ripoti, yeye aliwaambia kwamba nilikuwa nikiasi. Niliwaambia kwamba sikuwa nikiasi. Ilikuwa mara yangu ya kwanza maishani kupata kitu kilichonipa majibu kwa maswali yangu, na kilichonipa sababu ya kuishi.

Baada ya hili, nilipoenda kwenye Jumba la Ufalme, wazazi wangu walighadhibika mno. Waliniambia kwamba ningeenda chuo chochote kile nilichotaka, kufuatia masomo yoyote niliyotaka, na wangelipia, lakini lazima niache kabisa kushughulika na Mashahidi wa Yehova. Kilichofanya hili hasa liwe gumu kuvumilia kilikuwa upendo niliokuwa nao kwa familia yangu. Siku moja hasa isiyofurahisha, mama yangu aliniambia ilikuwa afadhali anione nikiwa kahaba kuliko kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ningeweza kuwa chochote isipokuwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wazazi wangu waliniambia lazima niondoke nyumbani. Zaburi 27:10 ilikuja akilini: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” Dada mmoja kutanikoni alikuwa na nyumba iliyokuwa tupu, na akaniruhusu kuitumia.

Nilikutana na dada kwenye Jumba la Ufalme ambaye, kama mimi, alikuwa mpya. Aliitwa Chris Kemp, tukawa marafiki wazuri sana na kuanza kuishi pamoja. Tulibatizwa Julai 18, 1969, katika Dodger Stadium katika Los Angeles.

Kwenye mikutano ya kutaniko, tulikuwa tukimtazama dada painia wa wakati wote, Dana Wolff. Alikuwa wa kiroho sana. Tuligundua kwamba alihitaji mahali pa kuishi, kwa hiyo tukapata mwenzi wa chumba mzuri sana.

Nakumbuka sehemu yangu ya kwanza mikutanoni. Nilikuwa na wonyesho, na nilijizoeza kwa kurudia-rudia. Ulikuwa wonyesho wa kutoa kitabu, na niliukariri. Hata hivyo, dakika ya mwisho, niliuandika na kuuweka mfukoni mwangu. Nilipanda jukwaani na sikukumbuka chochote. Nilisema: “Halo . . . Halo . . . Halo.” Nilisema halo karibu mara tano. Sikuweza kukumbuka chochote. Kisha nikaangalia wasikilizaji na kusema: “Kwa kawaida sifanyi hivi kwa wenye-nyumba.” Kisha nikatoa karatasi yangu iliyokunjamana na kusoma kile nilichopaswa kusema neno baada ya neno. Nilipomaliza, nilienda kwenye kiti changu na kulia.

Ndugu aliyeniomba nitoe hiyo sehemu aliuliza wasikilizaji: “Tulijifunza nini kutokana na utoaji huo?” Jumba lote lilikuwa kimya. Kisha nikasimama, na nikitazama wasikilizaji nikasema: “Wangewezaje kujifunza chochote? Nilifanya vibaya mno! Bila shaka hawakujifunza chochote!” nikaketi tena na kuendelea kulia. Najua sehemu zangu mikutanoni afadhali kidogo sasa—hazingekuwa mbaya zaidi ya ile.

Si muda mrefu baada ya hilo, Dana alianza kuzungumza kuhusu kutaka kutafuta mtu ambaye angehamia naye sehemu iliyokuwa na uhitaji mkubwa zaidi wa mapainia. Usiku huo Chris nami tulienda katika chumba chetu na kuzungumzia jambo hilo. Tulirudi siku iliyofuata na kumwuliza Dana: “Namna gani sisi?” Dana alishangaa sana. Tulikuwa wapya; tulibatizwa majuzi mno kuweza kuwa mapainia! Hatukuwa hata kidogo kile alichofikiria kuwa wenzi. Lakini kwa vyovyote, aliandikia Watchtower Society, tukapewa mgawo sote watatu kwenda Middlesborough, Kentucky.

Upinzani wa Familia Yangu Washindwa

Tulikuwa tukipanga vitu vyetu ili kuondoka wakati ambapo wazazi wangu walipiga simu kuniambia kwamba singeweza kutoka na gari langu nje ya jimbo la California. Wao walikuwa waaminishaji wa gari langu na waliniambia kwamba wangeita polisi ikiwa ningejaribu kwenda nalo nje ya hilo jimbo. Kisha tuliamua kwenda kwa basi. Katika sherehe ya kuagwa, ndugu mmoja ambaye nilikuwa nimekutana naye wakati mmoja alisema hivi: “Nimesikia kwamba unawiwa dola 3,000 kwa gari lako.” Nikasema ndiyo. Akasema alitaka kulipa. Nikasema kwamba singeweza kumruhusu kufanya hilo. Yeye akafanya mipango nikutane na akina ndugu katika kutaniko letu. Wao wakasema: “Ikiwa yeye anataka, mwache afanye hivyo. Usipinge roho ya Yehova.” Kwa hiyo gari lililipiwa. Wazazi wangu walikasirika lakini wakashangaa kwamba mtu fulani angefanya hivyo. Tukaelekea Kentucky siku iliyofuata.

Tulipofika Middlesborough, tulipewa nyumba ya kuishi iliyokuwa nyuma ya Jumba la Ufalme zee. Hakukuwa na kizuia baridi. Ilikuwa baridi sana wakati wa kipupwe. Kulikuwa na baridi hata wakati wa kiangazi, lakini tulifurahia kuwa nayo kwa kuwa hatungeweza kulipa kodi. Tulikuwa na kipasha-joto kimoja kidogo tu. Wakati wa kipupwe tulivaa tabaka kadhaa za nguo, hata wakati wa kwenda kulala. Nyakati fulani asubuhi kungekuwa na utando wa barafu sakafuni pote, na soksi zetu zingekwama sakafuni. Sikuzote tulikuwa na nyundo chooni ili kuvunja barafu iliyotanda kwenye maji ya choo kwa sababu yalikuwa yakiganda usiku.

Chris nami tulikuwa tumekuwa wahudumu wa wakati wote kwa miezi mitano tu, lakini tulikuwa tayari tunaongoza mafunzo mengi ya Biblia yaliyokuwa mazuri, na ilifurahisha kuwa huko. Tulifurahi sana kwamba sote tulikuwa na wastani wa zaidi ya saa 150 kwa mwezi katika miezi michache ya kwanza ya kupainia. Dana alitaka kuwa painia wa pekee wa muda kwa wakati wa kiangazi kwa hiyo akaamua kwenda makao makuu ya Mashahidi katika New York. Hatukuwa tumepata kwenda huko, kwa hiyo tuliamua kwenda pamoja naye. Tulipokuwa huko, Dana alienda kwenye Idara ya Utumishi, nasi tulienda naye. Tulishangaa sana kupewa mgawo wa kuwa mapainia wa pekee wa wakati wote sote watatu.

Baba Yangu Akosa Kutimiza Ahadi Yake, na Apotoa Andiko

Mwezi ule nilioanza upainia wa pekee, Shetani aliongeza jitihada zake za kunidhoofisha. Nilipata bili kutoka banki ikitaarifu kwamba ilinilazimu nianze kulipa dola 32.80 kwa mwezi kwa ajili ya elimu yangu ya chuo. Hili lilikuja bila kutazamiwa, kwa kuwa sikuzote wazazi wangu walikuwa wameniambia kwamba wangelipia elimu yangu ya chuo ikiwa ningedumisha wastani wa A, jambo ambalo nilikuwa nimefanya. Nilimwandikia baba yangu na kumwomba asinione kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika jambo hili bali anione nikiwa binti yake. Nilimkumbusha kwa njia ya upendo makubaliano tuliyokuwa tumefanya kuhusu elimu yangu, kwamba ikiwa ningedumisha hizo gredi alizotaka, angelipia elimu yangu. Nilimwomba asiniwekee mzigo huu kwa sababu ingekuwa vigumu sana kwangu kudumisha malipo haya, kwa kuwa nilikuwa nikipata dola 50 tu kwa mwezi ambazo ndizo nilizoishi kwazo. Kulipa dola 32.80 kwa mwezi kungeniacha na dola 17.20 tu kuishi kwazo.

Baba yangu alijibu barua ikiwa na andiko ndani. Yeye aliandika hivi: “Kwa kuwa sikuzote wewe hutumia Biblia, vipi andiko hili: ‘Ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, na asile chakula.’ Hutumii elimu yako kwa chochote chenye manufaa, kwa hiyo utatoa malipo hayo kwenye banki.”—2 Wathesalonike 3:10.

Nilipopata huo ujumbe mfupi, wenye kuchoma, niliumia sana. Niliingia garini mwangu, nikaenda mahali fulani peke yangu, na kulia kwa sababu sikujua la kufanya. Kisha nikaacha kulia na nikaghadhibika. Nilifahamu kwamba haikuwa wazazi wangu waliokuwa dhidi yangu bali Shetani. Nilimpazia sauti Shetani aniondokee, kwamba hangeshinda, na kwamba hangefaulu kunifanya niache upainia.

Magumu Mengi, Baraka Nyingi

Nilipata kazi ya nusu wakati nikifanya saa 20 kwa juma—saa 11 kwa siku moja na saa 9 siku iliyofuata—nikaendelea na upainia wa pekee. Nilijifunza haraka jinsi ya kutumia kwa faida maduka yauzayo vitu vilivyotumiwa. Kabati yangu ya nguo za wakati wa kipupwe ilikuwa na skati nne zilizonunuliwa kwa dola moja. Koti langu la kipupwe lilikuwa dola 1.50. Nilifanya kazi ya kusugua sakafu ili niweze kununua jozi ya viatu ya dola 20. Sote tulihitaji kujikakamua. Ili kujaribu kuweka pesa akiba, nilifungua akaunti ya akiba. Nyakati fulani ningeweka senti 25 na kisha kuzitoa ili kununua petroli. Nafikiri wenye kushughulikia pesa bankini walichukia kuniona nikiingia banki. Hatimaye walifunga akaunti yangu—sikuzote ilikuwa na pesa kiasi kidogo mno. Ningeenda katika kituo cha petroli na kuweka petroli ya senti 25. Baada ya muda nafikiri watumishi wa kituo hicho walikuwa wakitweta wakati wowote nilipokuwa nikiingia. Kulikuwa na nyakati ambapo hatukuwa na pesa za petroli. Nyakati nyingi tungeingia garini tukijua kwamba ni petroli kiasi kidogo iliyobaki na pia kwamba tulikuwa na funzo la Biblia. Nyakati fulani tungeenda posta, tungepata dola moja katika barua yetu kutoka kwa mtu fulani—ikitosha tu kutusaidia kuendelea na maisha. Katikati ya taabu zote hizo, tungeweza kuona mkono wa Yehova katika maisha yetu. Iligusa moyo sana.

Nakumbuka nikikusanya chupa zilizotupwa na kuziuza ili kununua stampu tu. Niliweka pesa kwa miezi mitatu ili kununua viatu vya dola 8. Kisha jambo la kibinafsi kuliko yote likanipata. Kihalisi nilikuwa na chupi mbili tu. Nilisali kwa Yehova na kumwambia kwamba nilihisi hili halikuwa jambo lifaalo kuomba, lakini kwamba sikujua nilikuwa nifanye nini. Majuma mawili baadaye, nilipata kifurushi kilichokuwa na chupi 17, kamisi, blausi, na vitu vingine! Vyote kutoka kwa mtu fulani ambaye sikuwa nimesikia kutoka kwake kwa mwaka mmoja.

Moja ya matatizo makuu katika hilo eneo lilikuwa kuuzwa alkoholi isivyo halali. Kwa sababu ya mazoea yao yasiyo halali, watu katika maeneo fulani walikuwa wenye ubaguzi sana na wenye kushuku wageni. Hata hivyo, nilikuwa na mafunzo mengi, na hatimaye nilikuwa nikifanya kazi katika utumishi wa shambani saa 25 hivi kwa juma nikiwa peke yangu. Sikupata kuhisi nikiwa karibu zaidi na Yehova kuliko wakati huo kwa sababu ilinilazimu kumtegemea yeye kikamili. Unajifunza kwamba jambo la maana si vitu ulivyo navyo bali uhusiano wako pamoja na Yehova. Unajifunza kwamba vitu vya kimwili havikufanyi uwe na furaha; ni Yehova anayekufanya uwe na furaha.—Luka 12:15.

Napata Familia Mpya Yenye Upendo

Mwezi ule niliomaliza kulipa bili yangu ya elimu yangu ya koleji ndio uliokuwa mwezi ambao nilikutana na yule ambaye angekuwa mume wangu na rafiki bora zaidi, Jeff Malone. Yeye alikuwa Betheli, na mwaka mmoja baadaye tulioana. Nilipoolewa na Jeff, sikuolewa naye tu bali pia nilimpata mama yake, dada yake, na mjombake, ambao nawapenda sana. Upendo wetu sote kwa Yehova unatuunganisha zaidi ya kifungo chochote kile. Jeff nami tulipewa mgawo katika Union City, Tennessee, tukiwa mapainia wa pekee. Tulikuwa pale kwa miezi minne tu wakati tulipopeleka ombi la utumishi wa Betheli na kukubaliwa.

Tuliondoka Betheli katika 1980, na binti yetu, Megan, alizaliwa baadaye mwaka huo. Mwana wetu, J. T., alizaliwa katika 1983. Wakati huu Jeff nami tunatumikia tukiwa mapainia wa kawaida katika Kutaniko la Forest Hill katika Fort Worth, Texas.

Tuliamua kwamba tungefanya chochote tuwezacho ili kulea watoto wetu wampende Yehova. Ingawa Jeff anatumika akiwa mzee, yeye sikuzote ameweka faida za kiroho za familia kwanza. Tumefuata madokezo ya Sosaiti kuhusu kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, kuwasomea watoto vichapo, kushiriki katika utumishi wa shambani, kuzungumzia andiko la siku na kwenda kwenye miradi ya ujenzi wa Jumba la Ufalme. Sote mara nyingi hutumia zaidi ya saa nzima kulaza watoto—tukiwaimbia nyimbo, kuwasomea hadithi za Biblia, kutoa sala na kila mmoja wao kandokando. Mradi wetu wa kifamilia ni kwamba sote tuwe katika utumishi wa wakati wote. Kuna jambo moja ambalo sikuzote tumehisi kuwa la maana sana kwa miaka yote hiyo—kubaki pamoja tukiwa familia, kufanya mambo tukiwa familia, kote katika kazi na mchezo.

Nikitazama nyuma, naweza kuhakikisha kwamba Daudi alieleza kwa usahihi aliposema hivi: “Nimrudishie BWANA nini, kwa ukarimu wake wote alionitendea?” (Zaburi 116:12) Hakuna kitu ambacho Shetani ameweza kufanya ambacho Yehova hajaweza kukitangua. Nina familia ya karibu, yenye upendo nikiwa na Jeff na Megan na J. T., sote tukiunganishwa katika kumtumikia Yehova; na kwa kuongezea hilo, nimepata familia nzuri mno ya ulimwenguni pote kwa sababu ya kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova. Ni jambo ambalo kwalo nitakuwa mwenye shukrani milele.—Kama ilivyosimuliwa na Karen Malone.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Karen pamoja na mume na watoto wake wawili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki