Kumkaribia Mungu Kulinisaidia Niwezane na Hali
SIKUPENDEZWA na dini. Mashirika yote ya dini yalionekana kuwa na unafiki kwangu. Sikudhani ilinufaisha watu, isipokuwa kuwafanya wasiwavumilie wengine. Hiyo ilikuwa miaka ya 1960. Rais wa U.S. alikuwa ameuawa, na maelfu walikuwa wakifa katika vita iliyokuwa Vietnam. Ulimwengu ulijaa machafuko. Maisha yangu mwenyewe yalikuwa yakiharibika. Kungewezaje kuwa na Mungu aliyenijali mimi au ainabinadamu?
Nilikuwa mwenye miaka 27, nimeolewa na mwenye watoto wawili wadogo, na nilikuwa nikifanya kazi ya wakati wote katika hospitali ya wenye akili punguani wakati jirani mmoja alipoanza kunieleza kuhusu Biblia. Kwa kushangaza, nilijipata nikisikiliza. Alizungumza juu ya zile alizoita siku za mwisho. Alionekana kuwa tofauti, na nilitaka majibu. Aliniachia kitabu kiitwacho Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Nilikisoma kwa usiku mmoja, nikachunguza maandiko yote, na nikajipata nikijiuliza, ‘Kwa kweli je! nimeipata kweli?’
Ikiwa nilikuwa nimeipata, ilitokeza tatizo. Nilizaliwa katika familia ya Kiyahudi, nilikuwa na mume Myahudi na watoto wawili wadogo, na watu wa ukoo wa Kiyahudi. Nilijua wangelikasirika ikiwa ningekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Sikutaka kuumiza familia yangu bila sababu; nilitaka nihakikishe. Nilianza kusoma fasihi ya Biblia kwa bidii. Kwa muda wa juma moja nikasadiki kwamba hiyo ilikuwa ile kweli. Niliwajibika kujifunza kweli. Kwa hiyo nilianza kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Katika muda wa majuma kadha nilikuwa nikimhubiri kila mtu. Nilichachawa kujua kwamba jina la Mungu ni Yehova, kwamba alinijali mimi na ainabinadamu yote, na kwamba uhai wa milele kwenye dunia paradiso uliwezekana. Nilibatizwa mnamo Juni 12, 1970.
Kama nilivyokuwa nimedhania, familia yangu pamoja na watu wa familia ya karibu walikasirika sana, na wengine walinikataa. Mume wangu alijifunza kwa kukatiza-katiza kwa miaka mingi lakini hakuwa mwamini kamwe. Hata hivyo, watoto wangu walikuja kuwa Mashahidi wa Yehova. Kuanzia mwanzoni, nilitaka niwe mhudumu wa wakati wote, nikihubiri habari njema za Ufalme wa Mungu mlango kwa mlango. Lakini nilikuwa na familia inayokua na mume asiyeamini. Hata ingawa nilifanya kazi ya wakati wote, tulifukuzwa kutoka nyumba mbili, na mara kadha tulikosa mahali pa kwenda. Maisha yalikuwa magumu sana.
Wakati mmoja nyumba yetu ilikuwa itwaliwe kwa kukosa kulipa. Tulipaswa tutoke kwa nyumba hiyo kufikia saa sita Jumapili hiyo, na hatukuwa na mahali pa kwenda. Nilifanya yote niliyoweza, na hatimaye Jumamosi asubuhi, siku kabla, niliamua kwamba ningeenda kufanya vile Yesu alisema kwenye Mathayo 6:33—kutafuta kwanza Ufalme na kumngojea Yehova aandae vitu nilivyohitaji. Nilienda kwenye huduma ya hadharani. Ninakumbuka nikilia kwa sababu ya mkazo ambao hali hiyo ilikuwa imetokeza, lakini katika muda wa dakika tano, nilihisi vizuri zaidi. Wakati wote nimepata kwamba kuhubiri kuna matokeo mazuri sana kwangu; kunanisaidia nisahau matatizo yangu, na roho ya Yehova huniweka nikiwa mwenye furaha na mwenye matokeo na kuyapa uhai wangu maana. Kwa vyovyote, niliporudi nyumbani siku hiyo, bado hatukuwa na mahali pa kwenda, lakini nilihisi vizuri zaidi.
Jioni hiyo tulipata simu kutoka kwa shirika la maliasili ambalo lilikuwa likishughulikia mahitaji yetu. Ilikuwa saa 5:30 usiku, na wakala wa maliasili alihangaishwa sana kwamba hatukuwa na mahali pa kwenda hivi kwamba alipata mahali ambapo tungeishi kwa muda hadi nyumba ambayo tulipaswa kupata iwe tayari. Kwa hiyo Mashahidi wenzi walituhamisha kwenye nyumba hiyo Jumapili. Tuliishi humo, nguo zetu zikiwa zingali kwenye masanduku, kwa majuma matatu na hatimaye tukahamia kwenye nyumba yetu ilipokuwa tayari. Haikuwa rahisi, lakini Yehova alituandalia mahitaji yetu. Hayo yaliniimarisha sana na kujenga imani yangu. Ilikuwa tu kama vile Mfalme Daudi alivyosema kwenye Zaburi 37:25: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”
Kulikuwa na matatizo katika kusimamia pesa za familia. Nyakati nyingine ningechukua usimamizi wa pesa na kunyorosha kila kitu. Nilijaribu kwa kila njia kuhifadhi ndoa wakati wa miaka hiyo, sanasana kwa ajili ya kumpenda Yehova na maoni yake kuhusu mpango wa ndoa, na kwa ndani nilitumaini kwamba mume wangu angebadilika na kukubali kweli.
Nilisali nyakati zote kuhusu kufanya upainia wa kawaida, na nikajiandikisha kuwa painia msaidizi kwa kila fursa.a Nilijua kwamba kuhubiri kulikuwa njia bora na ya maana zaidi ambayo ningeweza kutumia maisha yangu. Nilimpenda Yehova na nilitaka nimtumikie kwa nafsi yote. Pia nilipenda watu na nilitaka kuwasaidia. Nilikuja kuthamini kutokana na maisha yangu mwenyewe yaliyo magumu jinsi kanuni za Biblia zinavyonufaisha na kujua kwamba watu walihitaji tumaini ambalo Ufalme uliandaa. Lakini nilihofu kwamba familia yangu haingepata riziki ikiwa ningeacha kufanya kazi. Ni kama hatukuwa tukipata riziki.
Nilipiga Mayowe, Mnajisi Akatoroka
Kisha jambo fulani likatukia maishani mwangu lililonipa imani kwamba Yehova wakati wote angeniandalia na kunitunza. Mtu fulani alivunja nyumba yangu na kujaribu kuninajisi. Alinishambulia nikiwa nimelala, na nilipoamka, alitisha kuniua ikiwa ningepiga yowe au kusonga. Ingawa niliogofywa, Yehova alinisaidia nitulie na kuwa na akili ya kusali na kufikiria ni hatua ipi ingelikuwa bora zaidi ya kuchukua. Nilijua yale iliyosema Biblia kuhusu kupiga mayowe, lakini pia nilihisi kwamba angeniua ikiwa ningepiga mayowe, na kisha watoto wangu wangeamka, na angewaua. Niliona jina langu limetokea kati ya matangazo ya waliokufa na kusali kwamba Yehova alinde watoto wangu ikiwa ningekufa. Ijapokuwa hivyo, nilifanya yale ambayo Biblia ilionyesha—nilipiga mayowe. (Kumbukumbu la Torati 22:26, 27) Mnajisi akatoroka. Niliamini kwelikweli kwamba ningekufa usiku huo. Nilimkaribia Yehova hata zaidi.
Niliacha kazi yangu na nikaanza kutumika nikiwa painia wa kawaida katika 1975. Nilipainia kwa miaka sita, na mume wangu alilipa gharama za kuishi. Kwa kusikitisha, nilipatwa na kisukari nikiwa na umri mchanga na wakati mmoja nilikuwa mgonjwa sana. Ili niiweze hali niliendelea kumtegemea Yehova hata zaidi. Kujapokuwa hali zangu, hiyo ilikuwa miaka ya kufurahisha na yenye matokeo zaidi niliyopata kuwa nayo kufikia wakati huo. Yehova alinibariki kwa wanafunzi wengi wa Biblia waliofanya maendeleo kufikia ubatizo. Wengine waliendelea wakawa mapainia wao wenyewe.
Kisha, katika 1980, maisha yetu yakavunjika. Tulikosana na mume wangu. Watoto wangu walitamaushwa sana, kwa hiyo kwa ajili yao nilijaribu kuokoa ile ndoa, lakini mume wangu hakuitikia jitihada zangu. Kufikia hapo, nilijua kwamba wakati ulifika wa kupata talaka ya Kimaandiko. Watoto wangu waliathirika vibaya sana kwa kuondoka kwake.
Nilikuwa nikijaribu sana kuendelea na upainia wakati huo na niliweza kuendelea kwa karibu mwaka mmoja. Hata hivyo, binti yangu alianza kuasi dhidi ya kila kitu, kutia mimi na kweli, baada ya kushindwa kuwezana na hali hiyo. Niliacha kupainia wakati huo kwa sababu ya mwenendo wake. Hilo lilinivunja moyo sana; utegemeo wangu ulikwisha. Nilihisi mpweke sana, kama kwamba kila kitu isipokuwa Yehova, kilikuwa kimetokomea mbali.
Ni karibu wakati huu kwamba Yehova aliandaa ndugu wawili wapenzi walionisaidia zaidi ya vile wanavyoweza kujua. Mmoja alikuwa mwangalizi wa mzunguko, na mwingine mzee katika kundi jingine aliyejua hali zetu, kwa kuwa alikuwa amejifunza na mume wangu. Sijui ninaweza kumshukuru Yehova kivipi kwa zawadi hizo za wanaume. Wakati wote wao watakuwa watu wa karibu sana kwangu.
Si muda mrefu baada ya hapo, kwamba binti yangu aliolewa nje ya kweli, akiwa mchanga mno. Hilo lilikuwa pigo kwa familia na likatutamausha sana. Halafu kidogo mwanangu akaacha kweli. Nilisali kwa Yehova daima asaidie familia yangu iendelee katika kweli. Wao walikuwa na thamani kubwa kwangu, na jambo pekee nililotaka sana kwao ni kubaki na Yehova. Hiyo ilikuwa imekuwa sala yangu ya daima wakati wa maisha yangu katika kweli. Wakati huo ulikuwa mbaya zaidi kwangu kuliko miaka yote 20 ya ndoa—na hiyo ilikuwa mibaya. Hata hivyo, nilijua kwamba kwa njia fulani Yehova angetusaidia tuvumilie, na hata iweje, ningefanya mapenzi yake.
Ninakumbuka tukio moja vizuri. Nilikuwa bado nikipainia, na hatukuwa na pesa lakini tulihitaji karibu dola 70 ili kufikia mwisho wa juma na kuwa na pesa za usafiri kwa kazi ya juma ambalo lingefuata. Nilikuwa nimefanya kazi siku mbili nikiwa mfanyakazi wa muda. Mara nyingi, nililazimika kungoja karibu juma moja ili kupata pesa nilizochuma—karibu dola 40. Sikuwa na pesa za chakula, wala za usafiri. Usiku uliofuata nilikuwa na funzo la Biblia na mwanamke ambaye alinisaidia kwa nauli ya usafiri wa gari ya moshi la chini ya ardhi.
Asubuhi iliyofuata ilikuwa Ijumaa. Nilienda kuchukua barua, na kulikuwa barua mbili. Moja ilikuwa hundi niliyotazamia juma ambalo lingefuata. Ilifika jijini na kurudi katika siku zinazopungua tatu. Nilishangaa. Bado nilihitaji dola 29 au 30 ili niiweze hali. Katika barua ya pili mlikuwa na hundi ya dola 29, zile tu nilizohitaji. Jambo linalostaajabisha kikweli kuhusu hayo ni kwamba katika Februari wa mwaka huo, serikali ilikuwa imenipatia zawadi ya pesa kwa ajili ya mafuta ya kupasha joto nyumba yangu. Sasa kulikuwa Agosti, na serikali ikaamua kwamba iliniwia dola 29—katika Agosti, kwa ajili ya kupasha joto? Kwa nini wangefikiri wananiwia chochote, na isitoshe, eti mafuta katika Agosti? Hilo liliniimarisha imani kama nini!
Vitu vya Kimwili Si Ndiyo Suluhisho
Nilianza kufanya kazi wakati wote na kujifunza kuendesha kompyuta katika kazi nilizofanya. Miaka ambayo sikufanya upainia ilikuwa migumu sana. Hata ingawa nilikuwa na kazi nzuri na nikawa na pesa na vitu vya kimwili, sikuwa na furaha. Watoto wangu walijitegemea na walikuwa wakipata matatizo makubwa sana. Binti yangu alikuwa anarudi katika kweli lakini bado alikuwa na matatizo. Mwanangu alikuwa akipata matatizo pia. Baada ya kipindi cha wakati, nilihisi kwamba nilikuwa nikipoteza uhusiano ule wa karibu sana na Yehova ambao nilithamini sana. Nilihisi kwamba nilikuwa nikielea mbali kutoka kwa Yehova, hata ingawa hakuna mtu mwingine angeweza kuona hivyo. Nilihudhuria mikutano yote, nikajifunza, nikaenda kwenye utumishi, lakini haikutosha. Nilijaribu kushirikiana zaidi na marafiki, lakini hilo vilevile halikusaidia.
Nikaanza kujihurumia. Nilianza kutafuta mawazo yangu ya ndani na kujifikiria. Je! sikustahili kupata mambo zaidi? Bila shaka, fikira za aina hiyo ndizo alizotaka Shetani. Kwa mara ya kwanza, nikaanza kuhisi nikivutiwa na wafanyakazi wenzi. Nikafikiri, ‘Si kitu, nitawahubiri.’ Na nilifanya hivyo. Lakini kwa ndani nilihisi kwamba moyo wangu ulikuwa unaanza kupuuza mambo ambayo haungepaswa kuyapuuza. Hayakuwa matatizo kutoka nje. Tatizo lilikuwa mimi. Singeweza kuitoroka dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia. Nilisali kwa Yehova.
Nilikuwa nikifanya kazi wakati wote. Nilihitaji kuacha ufanisi wa mali nilizokuwa nimekusanya. Nilikuwa nikisafiri kwenda na kurudi kwa saa tatu kila siku kutoka Kisiwa Long hadi Wall Street. Wakati mwingi sana! Pia, kushughulika na watu wengi wa ulimwengu kwenye magari-moshi hakukusaidia. Nilianza kuzungumza na wazee na kwenda kwenye makusanyiko miisho-juma ili niweze kukazia mambo ya maana. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu, sikulazimika kuhangaikia vitu vya kimwili, kwa hiyo mbona sasa nilitaka kung’ang’ana tena? Baada ya mwaka mmoja wa sala, huku nikifikiria kwa uangalifu ikiwa nilipaswa nichukue hatua, niliichukua.
Nilihamia eneo la Brooklyn Heights. Nilikuwa nimezuru kundi huko na nilijua kwamba hali ya kiroho humo ndiyo tu niliyohitaji. Mashahidi wengi waaminifu, wakitumikia wakati wote kwa miaka mingi sana—nilihisi nimestarehe. Katika muda wa miezi sita nilikuwa tayari kuacha kazi-maisha yangu na kupainia. Nilianza kazi isiyo ya wakati wote, na katika 1984, niliwekwa tena kuwa painia wa kawaida.
Kwa muda wa miaka, Yehova ameniandalia baraka nzuri ajabu, kutia na masomo mengi sana ya thamani. Nimejaribu kuendelea kuwa mwenye tumaini na kupata somo kutoka kwa kila jaribu. Si jambo la aibu kuwa na matatizo; dhambi ni kukosa kutumia kanuni za Biblia ili kuyatatua. Hapa katika Brooklyn, sina matatizo yaleyale niliyokuwa nayo katika miaka yangu ya mapema katika kweli. Pesa si tatizo tena. Mume asiyeamini si tatizo tena. Moyo wangu umerekebishwa. Nimebarikiwa kuwa na watoto wengi wa kiroho.
Lakini wakati wote kuna matatizo na magumu mapya. Katika 1987 mwanangu Marc, alipatwa na mkazo wa akili na akaugua mshuko mbaya wa moyo, lakini Yehova ametusaidia tuvumilie hayo. Sasa Marc anafikilia na anafanya vizuri sana kundini. Binti yangu, Andrea, alirudi kwenye kweli na akabatizwa na analea watoto wake katika kweli. Kwa kuwa tunakaribia kwa kasi dhiki iliyo kuu, ninatazamia matatizo yaendelee na labda yawe makubwa hata zaidi, lakini sikuzote Yehova atatusaidia tuvumilie vizuizi vyotevyote au magumu yoyote ambayo yaweza kuja.
Kwelikweli, Yehova amenisaidia kuwa na maisha yenye furaha na mazao mengi. Ninatazamia kutumia muda uliobaki nikiendelea kuwa karibu naye na kufanya mapenzi yake.—Kama ilivyosimuliwa na Marlene Pavlow.
[Maelezo ya Chini]
a “Kupainia” ni usemi unaotumiwa kumaanisha utendaji wa kuhubiri wakati wote.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Marlene Pavlow, mhubiri wa wakati wote wa habari njema za Ufalme