Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
Imesimuliwa na Harry S. Yoshikawa
JIRANI zetu katika mtaa mdogo nilikokulia katika Hawaii, karibu miaka 50 iliyopita, walikuwa wacheza kamari, wapiganaji na wevi. Baba alikuwa mvuvi ovyo tu mwenye kuvaa matambara, naye alikuwa hodari wa vita.
Baba alifundisha ndugu yangu nami jinsi ya kujikinga tufanyiwapo matata, tulipokuwa wadogo. Tuliingia mashindano ya kupigana, tukawa tukishinda au tukachukua nafasi ya. pili. Nilipotimu miaka kumi na mitatu tulikwenda Japan muda wa miezi sita, tukazidi kuzoezwa jinsi ya kupigana. Mtu mmoja aliyekuwa bingwa wa ubondia Hawaii katika uzani wa katikati alinizoeza kutupa ngumi pia.
Kazi yangu kila juma ikawa kuchapa watu. Nikabandikwa jina nikaitwa Kadogo Mponda-watu, ingawa sikuwa kadogo. Rafiki zangu wakawa wakinichukua usiku wa manane, ati kwa kusudi la kuchapana na watu tu katika Honolulu au Waikiki.
Mwaka 1944 niliingia jeshini nikapelekwa Ulaya. Vita ya ulimwengu ya pili ilikuwa ikiendelea, nayo, iliogofya. Ilipokwisha, nilianza jamii ya kupiga muziki iliyoitwa “Wachanua Pwani,” vilevile nikaanza kikoa (timu) cha kupigana ngumi katika Hawaii. Tulisafiri Ulaya yote tukifurahisha wanajeshi na raia pia. Tulitia nyimbo zetu katika santuri, vilevile tukafanya matangazo radioni.
VIJANA WAWILI NITAKAOKUMBUKA DAIMA
Wakati wa vita katika Ubelgiji, mapema mwaka 1945, ndipo niliposikia mara ya kwanza jambo ambalo sikulithamini sana. Nilikuwa sajini (askari) wa daraja la kwanza, na kila juma kijana mmoja wa miaka karibu kumi na minane alikuwa akija afisini mwangu. Akawa akinieleza jinsi Mungu atakavyosimamisha serikali itakayoleta amani duniani. Nilipomwuliza sababu hakuandikwa jeshini, alisema alikuwa amekwisha ingia jeshini—jeshi la Kristo. Nilishangaa.
Baada ya kutoka vitani Ulaya mwaka 1946, kijana mwingine alinieleza habari za Biblia. Kwanza nilidhani alinieleza kwa sababu nilikuwa nikipiga watu, nikilewa na kufanya mambo mengine ya utukutu. Niliyakumbuka maneno ya kijana yule mwingine Mbelgiji, nikashangaa kuona kwamba yalipatana na ya huyu.
Kijana huyu alikuwa akigawia watu magazeti katika barabara moja iliyokuwa karibu na jumba la sinema. Nilimsikitikia nilipodhani anataabika, nikajitolea kumnunulia magazeti yote aliyokuwa nayo, ili aende zake nyumbani au twende pamoja sinemani. Sikuzote alikataa. Nilishangaa sana, maana vijana wa umri wake hawawi hivyo.
NDOA HAIKUNIBADILI
Mara kwa mara niliacha kupiga watu ili kuchumbia wasichana, na mwishowe nikaoa. Lakini ndoa haikunizuia nisipigane na watu kila juma.
Nyakati nyingine niliporudi nyumbani kulikuwa na vita tofauti. Mke wangu alinikasirikia kwa sababu nilimwacha pamoja na watoto. Siku moja nilirudi nyumbani saa 12 jioni nikijigamba kwa sababu ya kushinda pigano la barabarani, nikamkuta mke wangu ananingoja katika orofa ya juu. Nilijaribu kutembea pole-po-o-ole katika orofa ya chini, nikijifanya nimelewa, lakini hakudanganyika. Alikuwa akiningoja mie, akanitandika kwa geta, yaani kiatu cha mbao.
JINSI NILIVYOANZA KUBADILIKA
Mwaka 1954 nilianza kubadili maisha yangu. Mfanya kazi mwenzangu katika shirika la bas alinipa vijitabu viwili, Basis for Belief in a New World na After Armageddon—God’s New World. Nilivichukua nikakesha nikivisoma na kuvirudia. Niliona kwamba dini hii ilikuwa tofauti na dini nilizojua.
Nilielezwa kwamba jamaa moja yenye kufuata dini hiyo iliishi katika jumba moja nasi. Basi nikaenda nyumba kwa nyumba nikiwatafuta. Ilikuwa jioni ya Jumanne, nami nilipofika, funzo la Biblia lilikuwa likiendelea katika nyumba hiyo. Niliwauliza kama ni Mashahidi wa Yehova, lakini hawakunijibu, labda kwa sababu niliongea kwa sauti mbaya ya kukosa adabu, tena mavazi ya kazi niliyovaa yalikuwa makuu-kuu. Labda walidhani nilikuwa nikitafuta matata.
Hata hivyo, walinikaribisha wakanionyesha upole mwingi sana, nami nikastarehe. Basi, tabia zangu mbaya zilianza kwisha. Niliona aibu kwa sababu ya mwenendo na usemi wangu. Watu hao walinieleza mengi katika Biblia, wakanitia moyo nijifunze Biblia ninapokuwa peke yangu na kuhudhuria mikutano yao yote ya kujifunza Biblia. Niliondoka hapo nikijua kwamba watu hao ndio wanaoifuata kweli.
Walipendekeza nijifunze na mfanya kazi mwenzangu katika shirika la bas; alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Acha nikuambie—huyo ni mtu niliyetaka kuchapa siku moja, ati kwa sababu sikupenda sura yake! Lakini nilitaka kujifunza, kwa hiyo nikanyenyekea nikamwomba anifunze Biblia.
Nilipokaribia nyumba yake, aliniona. Akadhani nimekuja na matata. Mkewe alinisalimu, akanionyesha fadhili nyingi sana za Kikristo. Woga ulimtoka mumewe, nikaanza kufunzwa Biblia. Baada ya miezi miwili nikaanza kutumia busara nyingi kueleza rafiki zangu na watu wa ukoo wangu mambo niliyokuwa nikijifunza.
Nilimwambia mke wangu waziwazi kwamba tumeacha kuwa wafuasi wa Buddha, na kwamba hatutasherehekea tena Krismasi wala sikukuu nyingine za kipagani. Nikamwambia lazima akubali uamuzi huo ama sivyo akione. Alidhani nimekuwa mwenda-wazimu, akawaomba wazazi wangu wamsaidie, maana ‘mwana wao’ alikuwa akitenda mambo ya kiajabu. Mama alimfariji sana akamwambia: “Usiwe na wasiwasi, mwanangu hapendezwi na jambo muda mrefu. Wewe mpe miezi mitatu, nawe utaona akiisahau kabisa dini hiyo ya kipumbavu na Yehova.”
KUTOA USHUHUDA HADHARANI
Lakini wakati huu mama alikosea. Baada ya muda mfupi nilijiunga na wenzangu kutoa ushuhuda hadharani. Naikumbuka sana mara ya kwanza nilipokaribia kuleta msiba. Mwangalizi-msimamizi alikwenda nami kugawia watu magazeti ya Biblia barabarani.
Nilipaza sauti nikiambia wapitaji, “Someni Amkeni!” Mtu mmoja alinijibu vibaya akasema: “Mimi nimeamka sana wala siitaki takataka hiyo.” Ndipo utu wangu wa zamani uliponirudia ghafula.
“Kumbe! Wasema umeamka sana, eh?! Haya, nitakuonyesha. Utalala sasa hivi.” Niligeuka nikamkimbiza majumba mawili. Mwangalizi aliogopa sana akanifuata na kunifikia, akasema amefurahi sana kwa sababu sikumpata jamaa huyo. Akanieleza kwamba kama ningalimchapa ningaliletea jina la Mungu lawama. Nikamwambia kama mapolisi wangalinikamata, ningaliwaambia mimi ni Mpentekoste, si mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
Mwangalizi alitumia subira akanisahihisha, akaniambia huo ungalikuwa uongo. Baada ya hapo hakutaka kuwa mbali, bali alikaa pale pale kando yangu. Niliaibika weee, tena nilipokwenda nyumbani nikamwomba Yehova anisamehe, maana kusudi langu halikuwa kuletea jina lake lawama.
Kisa kingine kilitokea nilipotembelea watu nyumbani kwao mara ya kwanza. Mlango wa kwanza nilikuta mwanamke mzuri. Alinisikiliza nilipomhubiri, akaniuliza-uliza maulizo yasiyohusu Biblia. Aliniuliza, “Wewe umeoa? Wewe una watoto wangapi? Wewe unapikiwa na nani?”
Mume wake alitaka kujua anaongea na nani, basi akaja. Akaniambia kwamba napoteza wakati wangu, kwa maana akili ya mkewe si nzuri. Lakini mkewe aliendelea kuniuliza maulizo, nami nikamtolea mahubiri yangu yote ya Biblia. Jambo hilo lilinipa nguvu za kwenda nyumba iliyofuata. Lo! mwenye nyumba hiyo alipendezwa akachukua vitabu vitatu vya kujifunza Biblia! Mwishoni mwa siku nikawa nimeangusha vitabu saba zaidi.
NIKAFANYA MABADILIKO MAKUBWA
Tumbako ilikuwa imeniingia sana hivi kwamba, nilipoishiwa na sigareti wakati mmoja, nilimwamsha mke wangu nikamwagiza aende kwa jirani akaombe sigareti kadha. Lakini nilipojifunza Neno la Mungu nilijua kwamba kuvuta tumbako hakuruhusiwi katika maisha ya Mkristo. Kwa hiyo baada ya kujifunza miezi mitatu niliacha kuvuta sigareti.
Niliamua kuonyesha nimejiweka wakf kwa Yehova kwa kubatizwa majini, Julai 17, 1954. Sasa nilitaka sana jamaa yangu ijiunge nami katika ibada ya kweli.
Desturi ya nchi za Mashariki ni kwamba mke ndiye anayepaswa kufanya kazi zote za nyumbani, bila ya kusaidiwa na mumewe. Mimi nilikuwa nimeunga sana mkono desturi hiyo. Lakini kwa kuwa nilizidi kutaka mke wangu ajifunze Biblia, baada ya muda mfupi nilijikuta nikisafisha vyombo, nikisuza nguo chafu za kushikia watoto, nikisaidia kupika na kutunza watoto.
Wakati mmoja tulikuwa na mandari (picnic) na rafiki zetu katika ufuo wa bahari, lakini mimi nikaanza kuwasomea Biblia badala ya kujifurahisha nikiendesha ubao katika mawimbi ya bahari. Wao hawakutaka niwahubiri nyakati zote, kwa hiyo wakaanza kwenda zao. Walivunjika moyo waliponiona bado nikiwafuata na huku nimeishika Biblia. Mwishowe, mke wangu, rafiki yetu na mkewe walikubali kujifunza Biblia kwa ukawaida.
Mama aliweza kuona kwamba sikuacha kumtumikia Yehova, kama alivyodhani ningefanya. Alifahamu kwamba utu mpya niliositawisha haukuwa wa muda tu. Basi, yeye pia alikubali kujifunza Biblia ajue ni jambo gani lililonibadili.
Juni 25, 1955, ilikuwa mojawapo siku zenye furaha zaidi maishani mwangu. Ilikuwa siku ya ubatizo katika kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Unadhani ni watu gani waliokuwa wameketi mbele wakitaka kubatizwa? Ni mke wangu, mama, rafiki yetu na mkewe—wote wanne wakiwa tayari kuonyesha kwamba walijiweka wakf kwa Yehova.
Tangu wakati huo nimefurahi kuona madereva kadha wenzangu, katika shirika la bas, wakizikubali kweli za Biblia na kuwa Mashahidi wa Yehova. Mmoja wao ni dereva niliyefinya ukutani wakati mmoja nikitaka kumchapa. Sasa yeye ni mwangalizi wa kusafiri.
NAFASI ZA KUTUMIKIA
Mwaka uliofuata kubatizwa kwangu, nilianza kutumiwa katika vyeo mbalimbali kundini. Halafu mwaka 1958 nikawekwa niwe mwangalizi-msimamizi, vilevile niwe mwangalizi wa mji wa Honolulu.
Ilionekana kwamba nisingeweza kutumikia wakati wote kama “painia,” kwa sababu ya madaraka ya jamaa. Watoto wangu wanne walikuwa bado wakienda shuleni. Lakini jamaa nzima tulishiriki katika upainia wa muda wakati wo wote tulipoweza. Halafu mwaka 1963 mke wangu akawa painia wa kawaida.
Kundi letu lilikuwa na watu wanaopenda upainia. Miezi mingine, zaidi ya nusu ya washiriki wa kundi walipainia kwa muda; na wakati mmoja tulifanya hivyo tukiwa 72. Kwa sababu wengi hivyo walipainia katika kundi moja, mipango mizuri sana ilitakiwa, vilevile hali ya kusaidiana. Tulipanga kwa uangalifu mipango ya kukaa na watoto, kusafiri na kufanya kazi eneoni. Sote tulifurahi sana mwezi huo.
Mwaka 1967 nilikaribishwa nishiriki katika kazi ya mzunguko, kutembelea makundi kadha katika visiwa vya Hawaii na kuyatia moyo. Nilipendezwa sana na jambo hilo, lakini nisingeweza kulikubali kabla ya kuzungumza na jamaa yangu, kwa maana watatu kati ya watoto wetu walikuwa bado wakienda shuleni.
Watoto wangu wema walikubali kufanya kazi ya kibarua na kunisaidia vyo vyote walivyoweza, ili niweze kuanza mgawo mpya huo. Binti mmoja alisema: “Baba, sikuzote wewe unatutia moyo tupainie, na wewe je? Hii ndiyo nafasi yako ya kumtumikia Yehova wakati wote.”
Tulipokuwa katika kazi ya mzunguko tuliona hali nyingi tofauti, na nyakati nyingine zilitufurahisha. Sijaisahau mojawapo. Jirani wawili walikuwa wamegombana kikweli, kwa maana mmoja alikata mwembe wa mwenzake uliokuwa umening’inia upande wa ua wake. Walitupiana maneno makali na kutishana. Nilipofika mlangoni kwa mwanamume aliyekata mti, huo, alidhani mimi ni mpelelezi anayechunguza kisa hicho, kwa hiyo akanikaribisha.
Nilipoanza kusema mtu huyo aliwaza, ‘Mpelelezi huyu anatumia njia ya ajabu, anajaribu kunifundisha adabu kwa kutumia Biblia!’ Lakini, baada ya muda mfupi alijua mimi ni Shahidi, akanieleza kwamba kabla ya hapo hakuwaruhusu Mashahidi wa Yehova waingie nyumbani mwake. Alikisha jamaa nzima ikajiunga naye kujifunza Biblia nyumbani mwake, nza na kufanya maendeleo makubwa. Baadaye, watu kumi wa ukoo wake na rafiki zake wakawa Mashahidi.
Sasa watoto wetu ni watu wazima. Mwana mmoja alitumikia Betheli ya Brooklyn miaka minne, yaani katika makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova. Sasa anatumikia na mkewe akiwa mwangalizi wa wilaya na wa mzunguko katika American Samoa. Binti wawili ni mapainia wa pekee, naye mwana wetu yule mwingine ni mwenye bidii pia akizihubiri habari njema na mkewe, tena wana kitoto kisichana. Mke wangu nami tungali katika kazi ya mzunguko.
Watu wengi leo hawakumbuki kwamba nilikuwa na sifa mbaya ya kupiga watu barabarani. Wengine wanashangaa sana kuona nilivyobadilika. Hiyo ni kwa sababu ninajulikana mahali pengi visiwani kama mhudumu Mkristo mwenye amani, na lo! ni furaha namna gani kumwakilisha hivyo Mungu wetu Mkuu, Yehova!
[Picha katika ukurasa wa 438]
Nilianza kumsaidia mke wangu na kazi za nyumbani, ingawa hiyo si desturi katika nchi za Mashariki