Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 7/22 kur. 21-24
  • Familia Iliyonipenda Kikweli

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Familia Iliyonipenda Kikweli
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Familia Yangu Yanikataa
  • Kutupwa Nje Mara ya Pili
  • Toleo Lenye Kushawishi
  • Kupata Familia Nyingine
  • Kusaidia Familia Iliyonikataa
  • Nilikuwa Mwana Mpotevu
    Amkeni!—2006
  • Yehova ni Ngome Yangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Uchaguzi Wangu Kati ya Baba Wawili
    Amkeni!—1998
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 7/22 kur. 21-24

Familia Iliyonipenda Kikweli

KWA mtoto, mtoto yeyote, familia ni ya maana sana. Familia changamfu na yenye upendo husaidia kuandaa mahitaji ya mtoto ya kimwili na ya kihisia-moyo. Hiyo huwa na fungu muhimu sana katika mazoezi, elimu, na ukuzi. Humfanya mtoto ahisi akiwa salama. Ni tukio la kuhuzunisha kama nini kukataliwa na familia yako, kama nilivyofanywa!

Nilizaliwa katika familia kubwa katika mashariki mwa Nigeria. Baba yangu alikuwa chifu mwenye wake saba. Alikuwa na watoto 30, nami nilikuwa wa 29.

Siku moja katika 1965, nilipokuwa na umri wa miaka kumi, nilikuja nyumbani kutoka shuleni nikamkuta baba yangu ameketi varandani. Wanaume wawili waliingia katika uga wa makao yetu wakiwa wamebeba mikoba, na baada ya salamu changamfu, walijitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Baba yangu aliwasikiliza kwa makini. Walipomtolea magazeti mawili, baba yangu alinitazama na kuuliza ikiwa niliyataka. Niliitikia kwa kukubali, kwa hiyo akanichukulia magazeti hayo.

Hao Mashahidi waliahidi kurudi tena, nao walifanya hivyo. Kwa miaka miwili iliyofuata, wao walikuja kuzungumza juu ya Biblia pamoja nami. Hata hivyo, ziara zao hazikuwa za kawaida, kwa kuwa ulikuwa mwendo wa kilometa kumi kutoka kijiji changu hadi mahali walipoishi.

Familia Yangu Yanikataa

Nilikuwa na umri wa miaka 12 wakati baba yangu alipougua na kufa. Siku nane baada ya mazishi, ndugu yangu mkubwa zaidi aliita familia kwa ajili ya mkutano. Watu 20 hivi walikuwako. Sote tulifikiri alikuwa azungumze kuhusu gharama za mazishi. Hata hivyo, kwa mshangao wangu, yeye alisema kwamba aliita mkutano ili kuzungumza kuhusu ndugu yake mdogo—mimi! Yeye aliwaeleza kwamba nilipendezwa na kuzunguka “nikiomba” pensi nne kama kwamba familia haikuwa na fedha za kunilisha. Yeye aliongeza kwamba kuzunguka nikichuuza magazeti kwa pensi nne kulikuwa kupaka matope jina la familia. Alisema kwamba lazima nichague nilitaka kuwa wa nani—wa Mashahidi au wa familia yangu.

Mama yangu alikuwa amekufa, lakini mmoja wa mama zangu wa kambo alilia na kunitetea. Yeye aliomba kwamba wasitumie jambo hili kuwa udhuru wa kuninyima sehemu yangu katika urithi. Lakini kwao maoni ya mwanamke hayakuwa na maana. Familia iliunga mkono ndugu yangu na kudai uamuzi kutoka kwangu.

Niliomba wakati wa kulifikiria jambo hilo. Walikubali kunipa hadi jioni iliyofuata. Nikiwa peke yangu katika chumba changu, nilianza kulia. Nilijihisi nikiwa mnyonge, aliyekataliwa, na mwoga. Nilijiuliza kile ambacho kingenipata.

Hadi wakati huo, sikuwa nimehudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme kamwe na sikuwa nimeshiriki katika kuhubiri na Mashahidi. Nilikuwa tu na ujuzi wa kijuu-juu wa mafundisho ya Biblia, na hakukuwa na Mashahidi katika kijiji changu wa kuongea nao.

Nilisali kwa Yehova, nikimwitia kwa jina kwa mara ya kwanza katika maisha yangu. Nilimwambia kwamba nilikuwa nikijifunza kwamba yeye alikuwa ndiye Mungu wa kweli. Nilimwomba anitegemeze na kunisaidia kufanya uamuzi ufaao, uamuzi ambao haungemchukiza.

Jioni iliyofuata familia ilikutana tena na kudai uamuzi wangu. Nilieleza kwamba baba yangu, aliyenipa uhai, ndiye aliyeanzisha funzo langu na hao Mashahidi. Yeye alilipia magazeti yangu na Biblia. Kwa kuwa hakuchukizwa kwamba nilikuwa nikijifunza Biblia pamoja na hao Mashahidi, sikuelewa kwa nini ndugu yangu mkubwa zaidi alipaswa kutumia hili dhidi yangu. Halafu nikasema kwamba sikujali walichonifanyia, ilikuwa ni lazima nimtumikie Yehova.

Hawakufurahishwa na maneno haya. Mmoja wao alisema: “Panya huyu mdogo ni nani hata atuzungumzie namna hii?” Mara hiyo hiyo ndugu yangu alitembea kwa hatua za kishindo kuingia ndani ya chumba changu, akashika nguo zangu, vitabu vyangu, na kisanduku changu cha kadibodi na kuvitupa ardhini nje.

Nilipata makao kwa mwanashule mwenzangu aliyeishi kijijini, na nilikaa na familia yake kwa miezi mitano hivi. Wakati huohuo, nilimwandikia mjomba wangu katika Lagos, ambaye alinialika kuja kuishi naye.

Kwa miezi kadhaa nilihifadhi fedha kwa kukusanya na kuuza kokwa za mchikichi. Mama yangu wa kambo ambaye alinitetea alinipa fedha kadhaa pia. Nilipokuwa na za kutosha, niliondoka kwenda Lagos. Sehemu moja ya mwendo, nilipanda nyuma ya lori la kubeba mchanga.

Kutupwa Nje Mara ya Pili

Nilipofika Lagos, nilifurahia kujua kwamba mjomba wangu alikuwa akijifunza pamoja na Mashahidi. Mara moja nikaanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwenye Jumba la Ufalme. Hata hivyo, upendezi wa mjomba wangu katika kumtumikia Yehova ulitoweka haraka ndugu yangu mkubwa alipokuja kuzuru. Yeye alimwambia mjomba wangu kwamba ulikuwa uamuzi wa familia kwamba sipaswi wala kutegemezwa wala kuruhusiwa kwenda shuleni, kwa kuwa niliendelea kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Yeye alimtisha mjomba wangu halafu akarudi nyumbani.

Juma moja baada ya kuondoka kwa ndugu yangu, mjomba wangu aliniamsha usiku-kati na kunirushia karatasi fulani iliyokuwa na maandishi. Akaweka kalamu mkononi mwangu na kudai kwamba nitie sahihi ya jina langu. Nilipotazama uso wake uliokunjamana, nilijua kwamba hili lilikuwa jambo zito. Nikasema: “Mjomba, kwa nini usiniruhusu niitie sahihi asubuhi?”

Yeye alisema kwamba nisimwite mjomba bali nitie sahihi karatasi saa hiyo. Nilijibu kwamba hata muuaji wa kimakusudi ana haki ya kujua mashtaka dhidi yake. Kwa kweli nilikuwa na haki ya kusoma hiyo karatasi kabla ya kuitia sahihi.

Hatimaye kwa hasira, alikubali niisome. Ilianza na kitu kama hiki: “Mimi U. U. Udoh, nimeapa kutokuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nimekubali kuchoma mikoba yangu ya vitabu na vitabu na kuahidi kutoshughulika na Mashahidi wa Yehova kamwe . . . .” Baada ya kusoma mistari michache ya kwanza, nilianza kucheka. Nilieleza mara moja kwamba sikumaanisha kumdharau bali kwamba lilikuwa jambo lisilowezekana kutia sahihi hati kama hiyo.

Mjomba wangu alikasirika mno na kuniamrisha niondoke nyumbani mwake. Nilipakia nguo zangu na vitabu katika mkoba wangu kimya-kimya, nikaenda varandani nje ya nyumba yake, na kulala chini sakafuni. Mjomba wangu aliponiona pale, alisema kwamba kwa kuwa kodi aliyolipa ilitia ndani varanda pia, ilinipasa kuondoka kwenye hilo jengo.

Toleo Lenye Kushawishi

Nilikuwa nimekaa Lagos kwa majuma mawili tu na sikujua pa kwenda. Sikujua mahali alipoishi ndugu aliyekuwa akija kunipeleka kwenye Jumba la Ufalme. Kwa hiyo, kulipopambazuka, nilianza kutembea na kuzurura, nikimwomba Yehova anisaidie.

Kufikia mwisho wa siku, nilijikuta kwenye kituo cha petroli. Nilimfikia mwenye kituo hicho na kumwomba ikiwa angeweza kufungia mkoba wangu ofisini usiku kucha ili kwamba wevi wasiuibe kutoka kwangu. Ombi hili lilimfanya atake kujua zaidi na kuniuliza kwa nini sikwenda nyumbani. Nilimweleza habari yangu.

Huyo mwanamume alikuwa mwenye huruma na alijitolea kuniajiri kuwa mvulana wa kufanya kazi nyumbani mwake. Hata alisema angenipeleka shuleni ikiwa ningemsaidia nyumbani mwake. Lilikuwa toleo lenye kushawishi, lakini nilijua kwamba kuwa mvulana wa kufanya kazi nyumbani kulihusisha kufanya kazi kila siku tangu mapema asubuhi hadi kuchelewa mno usiku. Pia, wavulana wafanyao kazi nyumbani walikatazwa kushirikiana na watu wa nje ya nyumba, kwa hofu ya kwamba huenda wakapanga njama na wevi kuja kupora nyumba. Hata chini ya hali bora kabisa, yaelekea ningekuwa na Jumapili moja tu kwa mwezi ambayo singekuwa kazini. Kwa hiyo nilimshukuru kwa unyofu kwa upendezi wake lakini nikakataa toleo lake. Nilisema kwamba ikiwa nilimfanyia kazi, ingekuwa vigumu kwangu kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme.

Huyo mwanamume alisema hivi: “Waweza kuzungumziaje mikutano hali hauna hata mahali pa kukaa?” Nilijibu kwamba ikiwa nilinuia kutohudhuria mikutano, ningeishi katika nyumba ya baba yangu. Ilikuwa kwa sababu ya dini yangu kwamba nilifukuzwa nyumbani. Chote nilichohitaji kutoka kwake kilikuwa mahali pa kuweka mkoba wangu. Kwa kusikia hayo, yeye alikubali kuniwekea mkoba salama.

Kupata Familia Nyingine

Nililala nje ya hicho kituo cha petroli kwa siku tatu. Sikuwa na fedha za kununua chakula, kwa hiyo nilikuwa bila chochote kabisa cha kula katika kipindi hicho. Siku ya nne, nilipokuwa nikizurura, nilimwona mwanamume fulani kijana akitoa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa watu barabarani. Nilimkimbilia kwa shangwe na kumuuliza ikiwa alimjua Ndugu Godwin Ideh. Alitaka kujua kwa nini niliuliza, kwa hiyo nilimwelezea yote yaliyonipata.

Nilipomaliza, mara moja aliweka magazeti yake mkobani mwake na kuuliza: “Kwa nini uteseke hivyo hali kuna maelfu ya Mashahidi wa Yehova hapa katika Lagos?” Alipungia mkono teksi na kunipeleka kwenye kile kituo cha petroli ili nichukue mkoba wangu. Halafu akanipeleka kwenye nyumba yake na kunipikia chakula. Kisha akatumana Ndugu Ideh, aliyeishi karibu aje.

Ndugu Ideh alipokuja, walibishana juu ya ni nani kati yao nilipaswa kuishi naye. Wote walinitaka! Hatimaye walikubali kunigawa—nusu ya wakati ningekaa na mmoja na nusu nyingine na yule mwingine.

Muda mfupi baada ya hapo nilipata kazi ya kuwa tarishi. Nilipopata mshahara wangu wa kwanza, nilizungumza na ndugu hao wawili na kuwauliza walitaka nichangie kiwango gani kwa ajili ya chakula na kodi ya nyumba. Wao walicheka na kusema kwamba sikuhitaji kulipa chochote.

Muda mfupi baadaye nilijisajilisha kwa ajili ya shule ya jioni na vilevile masomo ya kibinafsi, na hatimaye nikamaliza elimu yangu ya msingi. Mambo yaliendelea kuwa bora kwangu kifedha. Nilipata kazi bora zaidi, kama karani, na kwa wakati nikapata mahali pangu mwenyewe pa kuishi.

Nilibatizwa Aprili 1972. Nilikuwa na umri wa miaka 17. Nilitaka kuingia katika utumishi wa painia ili kuonyesha uthamini wangu kwa Yehova kwa yote aliyokuwa amenifanyia, hasa wakati wa kipindi hicho kigumu. Nilijiandikisha kuwa painia wa muda nilipoweza, lakini ilichukua miaka mingi kuja kuwa wa kudumu. Mwishowe, katika mwaka wa 1983, nilijiandikisha kuwa painia wa kawaida.

Kufikia wakati huo nilithamini kwa ukamili familia yangu ya kiroho. Maneno haya ya Yesu kwa hakika yalithibitika kuwa kweli kwangu: “Hakika nawaambia, hakuna mtu aliyeacha nyumba, au mke, au ndugu, au wazazi, au wana, kwa ajili ya ufalme wa Mungu, asiyepokea zaidi mara nyingi katika zamani hizi, na katika ulimwengu ujao uzima wa milele.”—Luka 18:29, 30.

Hao Mashahidi walikuwa wamenionyesha kwelikweli upendo na walinitunza. Walikuwa wamenipa makao nilipokuwa sina fedha. Kupitia msaada wao na msaada wa Baba yangu wa kimbingu, nilikuwa mwenye ufanisi kiroho. Sikuwa nimepokea elimu ya kilimwengu tu bali pia nilikuwa nimejifunza njia za Yehova.

Hawa ndio watu ambao familia yangu ya asili ilikuwa imenisonga kuwakataa. Nilipokataa kufanya hilo, familia yangu ilinikataa. Je, ndugu na dada zangu wa kiroho walinitia moyo kukataa familia yangu ya asili? Sivyo hata kidogo. Biblia hufundisha hivi: “Kama mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”—Luka 6:31.

Kusaidia Familia Iliyonikataa

Mara tu baada ya kutoka nyumbani, vita ya Nigeria ya wenyewe kwa wenyewe ililipuka. Kijiji changu kiliharibiwa. Wengi wa rafiki zangu na watu wa ukoo walipoteza maisha zao, kutia ndani mama yangu wa kambo ambaye alikuwa amenitetea. Uchumi ulikuwa umeharibika.

Vita ilipokwisha, nilisafiri hadi nyumbani na kutembelea mmoja wa ndugu zangu ambaye alikuwa ameshiriki katika kunifukuza nilipokuwa mvulana. Mkeye na binti zake wawili walikuwa wagonjwa na walikuwa wamelazwa hospitalini. Kwa hiyo nilimwonea huruma na kumuuliza ningeweza kufanya nini ili kusaidia.

Labda kwa sababu ya dhamiri yenye hatia, yeye aliniambia kwamba hakuhitaji chochote. Nilieleza kwamba hakupaswa kufikiri kwamba ningetafuta kulipiza kisasi kwa kile familia ilinifanyia. Nilimwambia kwamba nilijua walitenda hivyo kwa kutojua na kwamba nilitaka kabisa kumsaidia.

Kisha akaanza kulia na kuungama kwamba hakuwa na fedha na kwamba watoto wake walikuwa wakiteseka. Nilimpa fedha zilinganazo na dola 300 (za Marekani) na kumuuliza ikiwa angetaka kufanya kazi katika Lagos. Niliporudi Lagos, nilimtafutia kazi na kumwalika kuja kuishi pamoja nami. Alikaa nami kwa miaka miwili, akichuma fedha ili kuwapelekea mke na watoto wake. Katika wakati huo nililipia kwa furaha malazi na chakula chake.

Yeye alisema kwamba alijua Mashahidi wa Yehova walikuwa dini ya kweli. Alisema pia kwamba ikiwa hakuwa amekuwa mlimwengu sana, yeye pia angekuwa Shahidi. Lakini aliahidi kupangia mkeye na watoto wake funzo la Biblia.

Katika mwaka wa 1987, nilialikwa kuchukua kazi ya mzunguko. Katika Aprili 1991, nilimwoa Sarah Ukpong. Katika 1993, tulialikwa kuacha kazi ya mzunguko na kutumikia kwenye tawi la Nigeria. Tulikubali mwaliko huo na tulitumikia kwa furaha huko hadi mke wangu alipokuwa mja-mzito.

Ingawa familia yangu ilinitupa nje, nilikumbatiwa na familia ya kiroho—wazazi, ndugu, dada, na watoto. Ni shangwe iliyoje kuwa mshiriki wa familia hii ya kipekee ya tufeni pote, moja ambayo naipenda kikweli na inayonipenda kikweli!—Kama ilivyosimuliwa na Udom Udoh.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Udom na Sarah Udoh

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki