Yehova ni Ngome Yangu
—kama inavyosimuliwa na Albert Olih
IJAPOKUWA usiku huo wa Novemba ulikuwa wenye joto, upepo baridi ulinistarehesha na kunituliza nikalala. Walakini niliamka ghafula nikasikia sauti yenye mkwaruzo ikiuliza, “Unafanya nini wewe hapa?” Nilikuwa nimegunduliwa na polisi aliyekuwa akifanya kazi yake usiku.
Kama ilivyo, niliogopa. Nilisimama na polepole nikamweleza namna ilivyokuwa hata nikalala chini ya mwembe karibu na uwanja wa shule hiyo. Nilipomwambia hivyo akasema: “Haya, walakini pakitokea masumbufu yo yote hapa, nitakuja kukutafuta.” Alipoondoka nililala chini tena na nikafikiria matukio yaliyonifanya niwe hapo.
MCHANGA, LAKINI MWENYE KUPENDEZWA NA DINI
Mambo yalianza katika uwanja ambao ndugu yangu alikuwa akiishi. Wakati huo ulikuwa mwaka 1946 na nilikuwa mwenye umri wa miaka 15. Nilikuwa nimetoka katika kijiji changu katika kandokando za Mto Niger nami nilikuwa nimekuja kuishi pamoja na ndugu yangu katika Lagos ili niendelee na shule. Mpangaji mwingine ambaye jina lake aliitwa Young Umoh, alivuta kupendezwa kwangu, kwa maana mara nyingi alikuwa anatembelewa na watu waliokuwa wakiitana “ndugu na dada”. Nilitaka kujua wao ni nani na nikaenda chumbani mwa Bw. Umoh ili nimwulize. Upesi nikawa nimeingia katika mazungumzo yenye kupendeza sana.
Aliposema kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova kupendezwa kwangu kuliongezeka. Mvulana mmoja mchanga pamoja na dada yake katika shule yetu walikuwa wanaitwa Mashahidi wa Yehova. Walikuwa wenye adabu nzuri sana hata mara nyingi nilitaka kujua walikuwa wanafuata dini ya namna gani. Kwa hiyo nikawa mwenye kutaka sana kusikia juu watu hao.
Bw. Umoh aliniuliza kama nilikuwa naamini Biblia nami nikamwambia kwamba siku zote nilikuwa nimefanya vema katika elimu ya dini shuleni. Nilidhani nilikuwa naijua Biblia. Hata hivyo, alipoanza kunieleza juu ya ufalme wa Mungu na baraka ambazo ungeletea wanadamu, Biblia ikawa kama kitabu kipya kwangu.
Nilisikiliza kwa makini alipokuwa akieleza jinsi utawala wa ufalme wa Mungu utakavyoibadili dunia iwe paradiso, jinsi mapenzi ya Mungu yatakavyofanywa katika paradiso hiyo, na jinsi wenye upole watakavyopokea uzima wa milele. (Mt. 6:9, 10; Luka 23:43, ZSB; Ufu. 20:5) Mambo hayo yalinifurahisha sana, nami nikaamua kumtembelea Bw. Umoh kwa mara nyingine ili nijifunze zaidi kwake.
Ni kweli kwamba hapo kwanza sikukubali kila kitu alichosema. Nilikuwa naogopa kwamba huenda akawa mmoja wa wanafunzi wa uongo tuliokuwa tumeonywa juu yao na kanisa. Hata hivyo, ingawa nilikuwa nabishana naye, nilithamini sana mambo mengi sana aliyokuwa akinifundisha katika Biblia.
Kisha siku moja akaniambia kwamba haamini Utatu wa miungu. Nilishtuka nami nikataka kuondoka chumbani mwake. Walakini yeye aliniambia, “Hujaniuliza kwa sababu gani siuamini Utatu wa miungu.” Kwa hiyo nikamwuliza, na jibu lake likaanzisha hatua zenye kuelekeza kwenye badiliko kamili la kidini maishani mwangu.
Yeye alianza kwa kuniuliza: “Je! wewe unalingana na baba yako katika kila jambo, kutia tarehe ya kuzaliwa kwako?” Kisha, akaifungua Biblia, akanionyesha mahali ambapo Yesu alisema kwamba yeye alikuwa ametumwa na Babaye na kwamba Babaye ni mkubwa zaidi yake. (Yohana 14:24, 28) Alirudi kwenye masimulizi ya ubatizo wa Yesu, akanionyesha namna ambavyo lingekuwa jambo la upumbavu kuamini kwamba Yesu alikuwa Mungu, kwa kuwa ni sauti ya Mungu kutoka mbinguni iliyomkiri Yesu kuwa mwana Wake. (Mt. 3:16, 17) Bw. Umoh pia alitaja kwamba neno “utatu” halimo ndani ya Biblia. Niliyakubali maelezo hayo kwa sababu uthibitisho huo uliotoka katika Biblia ulikuwa thabiti.
Usiku huo nilipiga magoti ili nisali walakini nikaona siwezi. Tangu utoto wangu nilikuwa nimefunzwa kuanza sala yangu kwa kusema, “Katika jina la Baba, Mwana na Roho Mtakatifu.” Walakini kwa kuwa sasa nilikuwa nimeisadikishwa kuwa hakuna Utatu wa miungu, niliona kwamba singeweza kuianza sala yangu.
Siku iliyofuata nilikosa furaha kabisa nami nikaamua kuisoma Biblia, nikaanza na kitabu cha Mathayo. Niliendelea kufanya hivyo kwa siku kadha nami nikaisoma mpaka mwisho wa Ufunuo. Kwa kadiri nilivyoisoma zaidi, ndivyo nilivyoona kwamba yale Bw. Umoh alikuwa ananifundisha yalikuwa yanapatana na Biblia. Ilikuwa ni kweli!
Nilirudi kwa rafiki yangu, nikamwambia yaliyokuwa yametokea nami nikamwuliza anifundishe kusali. Yeye alipendezwa kwamba nilikuwa nimeyasoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na akaniazima vitabu na vijitabu fulani ambavyo alisema vingenisaidia. Hakika, vitabu hivyo vingekuwa na matokeo makubwa sana juu ya maisha yangu ya kidini ya wakati ujao.
MSAADA KUTOKA KWA MISIONARI MMOJA
Mapema katika mwaka 1947 nilienda kuishi na ndugu yangu wa mzazi mmoja tofauti. Wakati huo nikiwa mwenye umri wa miaka 16 na nikiwa nimetoka tu shuleni, sikuwa na fedha za kulipa karo yangu ya shule ya masomo ya juu nami nilikuwa na matatizo ya kupata kazi.
Wakati tulipokuwa tukila jioni moja, mlango ulibishwa na, kwa mshangao wangu, mwanamume Mzungu aliingia chumbani. Halikuwa jambo la kawaida Mzungu kutembelea nyumba za Waafrika, sana-sana wale maskini. Alijijulisha mwenyewe, kwa kusema: “Mimi ni Moreton kutoka Kanada. Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nami ninawaletea habari njema za serikali itakayotawala dunia hii.”
Mshangao ulimtoka ndugu yangu, naye akasema, “Njoo ukamate.” (“Njoo ule.”) Ilimshangaza kabisa, kwa kuwa Bw. Moreton alichukua kipande cha kiazi-kikuu kutoka katika sahani, akakichovya ndani ya mchuzi mwekundu na akakila, akasema: “Hiki ni chakula kizuri sana ambacho Mungu amewapa wanadamu.” Kisha akatueleza ujumbe wake.
Ndugu yangu alinunua vitabu vitatu kutoka kwake na akanipa kile chenye kichwa “Let God Be True.” Ingawa ndugu yangu na mkewe hawakupendezwa na funzo la Biblia, mimi nilimkaribisha Bw. Moreton aje anifundishe.
Kwa kadiri wakati ulivyopita, niligundua kwamba mtu aliyekuwa akishonea jamaa yetu nguo alikuwa na kitabu icho hicho bali hakuna ye yote aliyekuwa akimsaidia kujifunza. Kwa hiyo baada ya kila funzo nililokuwa nikifanya na Bw. Moreton, nilikuwa nikienda dukani mwake na kujifunza sura iyo hiyo pamoja naye. Jambo hilo lilinisaidia nifanye maendeleo na karibuni niliweza kutumia Biblia katika kuitetea kweli.
Siku moja nilimwambia Bw. Moreton kwamba ningependa kuwa misionari kama yeye. Yeye alicheka na kusema: “Utakuwa. Walakini kuna matatizo mengi ambayo unapaswa kujitayarisha kwa ajili yayo.” Alinionyesha katika Biblia kwamba ningepaswa kukabili mateso, hata kutoka kwa watu wa ukoo wa karibu. (Mt. 10:34-38) “Hata hivyo,” yeye alisema, “Yehova hatakuacha, ukiendelea kuwa mwaminifu.” Sikujua hata kidogo kwamba karibuni ningejifunza ukweli wa hayo aliyosema.
JARIBU LA MAPEMA LA IMANI
Siku moja usiku sana katika Oktoba 1947, ndugu yangu aliniamsha nikiwa usingizini na akaweka uamuzi huu mbele yangu: ‘Acha kujifunza na Mashahidi wa Yehova urudi katika Kanisa la Anglikana, au uhame nyumba hii.’ Nilitazama kwa mshangao. Sikuwa na kazi wala sikuwa na mahali pa kwenda. Kijiji cha kwetu kilikuwa karibu maili 300 (kilometres 500) kutoka hapo. Kwa kuwa kwa wazi ndugu yangu alijua hilo, nilishangaa mahali alikotaka niende katikati ya usiku. Hata hivyo, nilifanya uamuzi wangu. Nilikataa kuacha kumtumikia Yehova.
Ndugu yangu alijawa na hasira akaanza kunipiga kwa cho chote alichoweza kupata. Mke wake alijiunga naye. Alinifukuza katika nyumba hiyo akanifuatia kwa umbali fulani. Nilikwenda kwa watu wa ukoo wengine wa karibu katika mji huo, walakini wakakataa nilale ndani usiku huo. Mtu mmoja wa ukoo alisema: “Je! wewe hukudai Yehova ni Baba yako na tengenezo lake ni mama yako? Basi, nenda kwa Yehova naye na akuchukue nyumbani mwake!”
Hapo ndipo nilipofanya azimio langu ambalo nimeliweka mpaka leo hii. Ningemtumaini Yehova awe ngome yangu na kumtumikia, hata jambo gani litokee.—Zab. 27:1, 10.
Nikiwa sina mahali pengine pa kwenda, nilikwenda kwenye uwanja mmoja karibu na shule niliyokwenda wakati mmoja na nikalala chini ya mwembe mkubwa. Hapo ndipo polisi yule alinikuta, baada ya kulala hapo mara nyingi usiku.
Wakati wa mchana nilikuwa nakwenda msituni na kukusanya kuni, ambazo niliuza ili nijinunulie chakula. Siku kadha baadaye, Bw. Moreton alinikuta. Alipoisikia hadithi yangu, alisema kwa kunitia moyo, akinikumbusha yale aliyokuwa ameniambia kuhusu matatizo iwapo nilitaka kumtumikia Yehova. Alinialika nimtembelee mahali alipokuwa akiishi.
Jambo hilo lilinifungulia njia ya kushirikiana na kikundi cha wamisionari kinachoitwa jamaa ya Betheli, na kusaidia katika kazi ya makao hayo ya misionari. Vilevile nilifurahia kula chakula pamoja na jamaa hiyo. Kwa kweli, nilijiona kuwa sehemu ya jamaa hiyo na karibuni nikaanza kuwaita “ndugu” na “dada.”
KUHUBIRI NYUMBA KWA NYUMBA
Siku moja Ndugu Moreton alinialika nikiwa sitazamii nijiunge naye katika kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa ufupi alizungumza kichwa kimoja cha Biblia katika nyumba ya kwanza na kisha akatoa kitabu cha kusaidia kujifunza Biblia.
Kisha Ndugu Moreton akanipa mfuko wake na kusema: “Unamwona jamaa yule-e-e anayesimama katika pembe ile-e-e? Nenda kamhubiri.” Moyo wangu ulikosa kudunda mara moja. Walakini nilisema sala nikiwa kimya nami nikamwendea mtu huyo, na nikiwa nakumbuka yale aliyoambiwa mtu wa kwanza kwa sababu yalikuwa yamesemwa kwa urahisi. Nilitaja andiko lile lile katika Biblia, naye akaitikia vema. Nilikuwa nimeingizwa katika kazi ya kuhubiri nami nikajua hakuna jambo lingeniachisha.
KUFIKIA KUBATIZWA NA KAZI YA UPAINIA
Nilikuwa nimejifunza kwamba, baada ya kuweka maisha yangu wakf kwa Yehova, nilipaswa kubatizwa katika maji, kama alivyobatizwa Yesu. Ubatizo wangu ulifanywa katika Desemba 1947, kwenye kusanyiko la kwanza kabisa la Mashahidi wa Yehova nililohudhuria. Sasa washiriki wote wa kikundi hiki kilichokuwa kikikua cha Mashahidi walikuwa kikweli ndugu na dada zangu wa kiroho.
Miezi michache baadaye nilijiandikisha niwe painia (mhubiri wa wakati wote). Jambo hilo lilinifungulia nafasi nyingi katika kazi ya kuhubiri na likaongeza mwendo ule niliokuwa nikipata ujuzi katika kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba.
Kati ya mazungumzo magumu kweli kweli yalikuwa yale nilipokutana na pasta (kasisi) wa dini ya Seventh-Day Adventist. Haraka-haraka akashika mazungumzo ya Sabato akinitolea hotuba, akibisha kwamba lazima Sabato iadhimishwe kila juma. Mambo yalikuwa yamenipinduka. Nikajikuta ninahubiriwa na mwenye nyumba huyo, nikiyasoma maandiko aliyoyataja na kusikiliza maelezo yake. Nikamwambia kwamba sikujua mengi juu ya Sabato lakini nikaahidi kufanya uchunguzi na kurudi baadaye.
Niliporudi, nilikuta baadhi ya washiriki wake wa kanisa wakiwa naye. Alitumaini kutumia pindi hiyo ajionyeshe kwa kundi lake. Aliponijulisha kwao, alisema hivi: “Huyu ni Shahidi wa Yehova mchanga ambaye amepotoshwa na wahubiri fulani wa uongo. Nina furaha kwamba aliyasikiliza mafundisho yangu na amekuja apewe maelezo zaidi.” Niliuliza kwamba niruhusiwe niseme kwanza. Nikaanza kwa andiko lile lile alilokuwa amelitaja katika torati ya Musa, nikataja Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na nikaeleza kwa sababu gani Wakristo hawana lazima ya kuadhimisha Sabato ya kila juma.—Rum. 10:4; Gal. 4:9-11; Kol. 2:16, 17.
Akiwa amestaajabishwa na maarifa yangu yaliyoongezeka, pasta huyo alisema: “Umeyatumia Maandiko vizuri sana. Hilo ndilo jambo washiriki wa kanisa langu wanapaswa kufanya. Wanapaswa kuweza kwenda mlango kwa mlango na kuitetea imani yao.” Jioni hiyo yeye pamoja na washiriki wake wa kanisa walikubali vitabu vya kujifunza Biblia 29.
YEHOVA NI NGOME YANGU
Ili kuangalia madaraka fulani ya kifedha, nilianza kazi na idara ya Reli ya Nigeria, nikiwa ninaishi na ndugu mwingine wa mzazi mmoja tofauti. Hapa nilikabiliwa na jaribu jingine la tegemeo langu kwa Yehova.
Nilikuwa nimekubali mgawo fulani katika programu ya kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova ambalo lingefanywa katika upande wa mashariki wa Nigeria mapema katika mwaka 1950. Hiyo ndiyo ingekuwa mara yangu ya kwanza kushiriki kwenye programu ya kusanyiko, na kwa hakika mimi sikutaka kuikosa. Kwa hiyo huko kazini mwangu nilimwandikia karani mkuu wa idara hiyo, nikiomba nipewe likizo ya siku nne bila kulipwa. Lakini akakataa. Nilikata tamaa sana hata nikashindwa kula. Kwa siku nzima sikula chakula cho chote, nikatumia wakati huo nikitoa sala kwa Yehova ili anifungulie njia.
Asubuhi iliyofuata, nilikwenda moja kwa moja kwa mnyapara wa idara yetu, ijapokuwa wafanya kazi wa cheo cha chini walikuwa wamekatazwa kufanya hivyo. Nilipomwambia kwamba mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yeye alisema: ‘‘Hilo ni jambo ambalo ningalipaswa kujua. Nimeona namna unavyofanya kazi kwa uaminifu, nawe unanikumbusha juu ya ndugu yangu katika Uingereza ambaye ndiye mshiriki pekee aliye Shahidi wa Yehova katika jamaa yetu. Sisi humwona kuwa mtu anayeshikilia mambo bila sababu kwa kuwa alikataa kujiunga na jeshi na kupigana katika vita. Lakini yeye peke yake katika jamaa ndiye tunayeweza kutumaini. Ni jambo zuri kuwa na mmoja wa Mashahidi wa Yehova akifanya kazi pamoja nasi.”
Kisha nikamweleza juu ya tamaa yangu ya kuhudhuria kusanyiko na juu ya ombi langu la likizo ya siku nne bila kulipwa. Yeye alisema: ‘‘Hakika utakwenda kwenye kusanyiko. Walakini unahitaji zaidi ya siku nne kwa sababu kusafiri kunahusika. Nitakupa juma nzima. Njoo pamoja nami.” Alinipeleka mpaka kwa karani mkuu naye akasema: ‘‘Utafurahi kujua kwamba tuna mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wao ni watu wanyofu na wenye kufanya kazi kwa bidii. Kwa hiyo mpe Bw. Olih siku saba aende kwenye kusanyiko lao, na alipwe.”
Wakati fulani baadaye mwaliko ulikuja ukinitaka nikatumikie kwenye afisi ya tawi ya Sosaiti katika Lagos. Sosaiti hiyo ni shirika lililoandikishwa linalotumikia Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, katika Aprili 1951, nikawa mshiriki wa jamaa ya Betheli ya Lagos.
Akionyesha kutokupendezwa kwake na jambo hilo, ndugu yangu alisema: “Sasa kwa kuwa umeamua kuacha kazi yako uende ukamtumikie Yehova wako, jambo lo lote likikupata wakati ujao, usinirudie, kwa sababu hakika sitakusaidia.” Nikamhakikishia kwamba nilitumaini Yehova atanitunza. Kwa hakika yeye ameendelea kufanya hivyo wakati wa miaka 30 ambayo nimekuwa nikitumikia Betheli. Hii imekuwa miaka ya furaha nyingi, yenye nafasi na mapendeleo tele.
Inatia imani kuangalia nyuma wakati wa miaka hiyo iliyopita na kuona namna Yehova amekuwa ngome yangu na namna ameendelea kunipa mahitaji yangu. Ilikuwa katika mojalapo la makusanyiko yetu katika 1953 nilipokutana na Francisca, dada mchanga Mtogo. Baada ya kuandikiana miaka mitatu tulioana. Ameendelea kutumikia pamoja nami, na, yajapokuwa matatizo ya afya amekuwa mwenye kunitia moyo sana. Utumishi wangu umefanya tusafiri mapana na marefu ya Nigeria. Nimependelewa kusema na wasikilizaji wengi katika makusanyiko yetu na kufundisha wahudumu wetu wanaosafiri (waangalizi wa mzunguko na wilaya) katika shule ambazo zimekusudiwa ziwape mazoezi.
Nakumbuka mara ya kwanza kabisa Francisca nami tuliposafiri ng’ambo. Ilikuwa twende tuhudhurie kusanyiko la mataifa yote katika London mwaka 1969. Nililiona jambo hilo kuwa ni kudhaminiwa na tengenezo la Yehova niende masomoni. Ningewezaje kusafiri London, kama tengenezo la Yehova halingenifungulia njia? Tangu wakati huo nimehudhuria makusanyiko katika nchi nyingi za Ulaya, Amerika na Afrika. Katika mwaka 1976 na 1978, ilikuwa furaha kama nini kwetu kuishi kwa muda pamoja na jamaa ya Betheli ya Brooklyn kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Sosaiti katika New York! Pamoja na washiriki wengine wa halmashauri za tawi toka ulimwenguni pote, nilikuwa nimealikwa kwa mikutano ya pekee na programu za mazoezi zilizokuwa zikifanywa chini ya uongozi wa Baraza Inayoongoza ya Mashahidi wa Yehova. Ningeomba nini zaidi, ila kwamba niweze kuendelea kuwa mwaminifu kwa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova?
Mwendo wangu wa utumishi umekuwa si rahisi sikuzote. Nimepatwa na matatizo, majaribu, magonjwa, na nimepatwa na misiba iliyoniogopesha. Imani yangu imejaribiwa. Walakini pia nimepokea utajiri wa maarifa ya Kikristo na nguvu za kiroho, pamoja na furaha zisizoelezeka katika kumtumikia Yehova na ndugu zangu.
Ahadi hii ya Yesu imetimia kwa habari yangu “Kila mtu aliyeacha nyumba au kaka au dada, au mama, au baba au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema, katika nyakati hizi, atapokea mara mia zaidi ya nyumba, ndugu, dada, mama, watoto na mashamba pamoja na mateso; na katika [mfumo wa mambo ujao] atapokea uzima wa milele. Maono yangu ya moyoni ni kama yale mtunga zaburi, ambaye alisema hivi: “Nitasema, [Yehova] ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini.”—Zab. 91:2; Marko 10:29, 30, HNWW.