Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g95 6/22 kur. 22-25
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
  • Amkeni!—1995
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tumaini kwa Wakati Ujao
  • Kushinda Vizuizi
  • Kuingia na Kutoka Kwenye Makao ya Utunzaji
  • Mpokeaji wa Utunzaji Wenye Upendo
  • Kukabiliana na Hali Yenye Kuzidi Kuwa Mbaya
  • Kutokubali Kushindwa
  • Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Nashukuru kwa Ajili ya Utegemezo wa Yehova Usioshindwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Familia Iliyonipenda Kikweli
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1995
g95 6/22 kur. 22-25

Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu

KWENYE asubuhi ya Mei 18, 1963, niliamka nikiwa na furaha kuliko kawaida. Ilikuwa mwanzo wa siku yenye jua, ujoto na yenye kuvutia. Lakini kabla ya kueleza kwa nini siku hiyo ilikuwa ya pekee kwangu, acheni niwaeleze mambo machache kunihusu.

Nilizaliwa katika Philadelphia, Pennsylvania, Marekani, Mei 20, 1932, msichana mchanga zaidi katika familia ya mabinti wanne. Mama yangu alikufa nilipokuwa na miaka miwili, na baba akaoa tena nilipokuwa na miaka mitano. Baada ya kipindi fulani cha wakati, tulipata ndugu na dada sita wachanga katika familia yetu. Tulikuwa Wabaptisti, na wakati mmoja hata nilifikiri kuhusu kuwa mwalimu wa kufundisha watoto elimu ya kidini siku ya Jumapili.

Nilizaliwa nikiwa na baridi yabisi, ambayo ilichangia wakati mgumu sana wa utotoni. Nilipokuwa na miaka tisa, daktari fulani aliniambia hali yangu ingezidi kuwa mbaya zaidi kadiri miaka ilivyozidi kupita. Kwa kusikitisha, utabiri wake ulithibitika kuwa kweli. Kufikia wakati nilipokuwa na miaka 14, sikuweza kutembea tena. Hatimaye mikono yangu, nyayo, na miguu ikalemaa kabisa, na msogeo wa viungo vya nyonga zangu ukakazana na kuwa wenye maumivu. Vidole vyangu vilihabirika umbo sana hivi kwamba nilikuwa na wakati mgumu kuandika au kunyanyua tu vitu. Kwa sababu ya hali yangu, sikuweza kurudi kwenye shule ya umma.

Nilipolazwa hospitalini nikiwa na miaka 14, nilikuwa na furaha kwa sababu wauguzi waliniruhusu nifanye mambo madogo ili kuwasaidia. Nilifurahia kazi hii mno. Baadaye nilifikia hatua ya kutoweza kuketi bila kusaidiwa. Madaktari waliwaambia wazazi wangu kwamba hakukuwa na lolote ambalo wangeweza kufanya ili kunisaidia, kwa hiyo baada ya kukaa hospitalini kwa miezi mitatu, nilipelekwa nyumbani.

Kwa miaka miwili iliyofuata, hadi nilipokuwa na miaka 16, sikufanya mengi isipokuwa kujilaza kitandani. Masomo ya nyumbani yaliandaliwa, lakini hali yangu ikazidi kuzorota. Nilipata kidonda kwenye kifundo cha mguu wa kulia, na vilevile homa ya baridi yabisi ambayo ilihitaji nirudi hospitalini. Nilifikisha umri wa miaka 17 nikiwa huko. Kwa mara nyingine tena nilibaki hospitalini kwa miezi mitatu. Niliporudi nyumbani, sikustahili tena kuwa na masomo ya nyumbani.

Nilipokaribia miaka 20, nilikuwa mwenye huzuni sana na nilitumia wakati wangu mwingi nikilia. Nilijua kuna Mungu, na mara nyingi nilisali anisaidie.

Tumaini kwa Wakati Ujao

Nikiwa ningali katika Hospitali Kuu ya Philadelphia nikipokea tiba zaidi kwa kifundo changu cha mguu, nilikaa katika chumba kimoja na msichana fulani mchanga aitwaye Miriam Kellum. Tukawa marafiki. Dada ya Miriam, Catherine Miles alipozuru, Catherine angeshiriki nami habari kutoka kwenye Biblia. Baada ya kutoka hospitalini, niliweza kwa njia fulani kuwasiliana sikuzote na Catherine, ambaye alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Kwa kusikitisha, mama yangu wa kambo hakunipenda sana. Nilipokuwa na miaka 25, nilihamia kwa mmoja wa dada zangu wakubwa, na ilitukia kwamba Catherine alikuwa amehamia nyumba fulani iliyokuwa karibu. Nilimpigia simu, na akaanza kujifunza Biblia pamoja nami kwa kutumia kitabu Let God Be True kikiwa msaada wa kujifunzia. Ilikuwa furaha iliyoje kujifunza kwamba sitakuwa mlemavu sikuzote na kwamba siku moja uovu wote utamalizwa! (Mithali 2:21, 22; Isaya 35:5, 6) Kweli hizi zilinipendeza, pamoja na tumaini la ufufuo na taraja la kuona mama yangu tena.—Matendo 24:15.

Nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova mara hiyo. Mume wa Catherine alikuwa akinibeba hadi kwenye gari lao na kunipeleka kwenye Jumba la Ufalme. Nilipokwenda mikutanoni, nilihisi kutiwa moyo na upendo nilioonyeshwa.

Kushinda Vizuizi

Kwa kuhuzunisha, dada yangu na mume wake walitengana, jambo lililohitaji niishi kwa mara nyingine tena na baba yangu na mama wa kambo. Kwa kuwa mama yangu wa kambo alichukia sana Mashahidi wa Yehova, ilinilazimu kujifunza Biblia kwa siri kuanzia 1958 hadi 1963. Hangeruhusu yeyote wa Mashahidi wa Yehova kuja ndani ya nyumba. Ningejifunza na Mashahidi tofauti kwenye simu au nilipokuwa hospitalini.

Kizuizi kingine kilikuwa kwamba nyakati fulani mama yangu wa kambo alikuwa akikataa kunilisha na kuniosha. Wakati mmoja hakuosha nywele zangu kwa miezi minane. Pia hakuniruhusu kusoma barua zozote ambazo hakuwa ameziidhinisha kwanza. Hata hivyo, utunzaji wa Yehova ulikuwa dhahiri, kwa kuwa ndugu yangu aliruhusu barua zangu zipelekwe nyumbani kwake. Mpango huu ulimwezesha Pat Smith, dada Mkristo ambaye nilikuwa nikiwasiliana naye kwa njia ya barua, kuweza kuwasiliana nami na kuandaa kitia-moyo cha Kimaandiko. Ndugu yangu alikuwa akinipitishia kisiri barua za Pat; nilikuwa nikizijibu, na ndugu yangu alikuwa akizipeleka kisiri.

Katika 1963, ilinilazimu kurudi hospitali, na Pat Smith aliendelea kujifunza nami huko. Siku moja aliniuliza hivi: “Je, ungependa kubatizwa kwenye kusanyiko letu la mzunguko?”

“Ndiyo!” nikajibu.

Nilikuwa katika wadi ya kuelimisha walemavu jinsi ya kuishi na mapungukio ya kutojiweza kimwili na ningeweza kupata ruhusa ya siku moja. Katika siku ya kusanyiko la mzunguko, Pat, pamoja na Mashahidi wengine, walikuja kunichukua. Akina ndugu walihitaji kuninyanyua kuvuka kigawaji na kuniteremsha ndani ya maji ili nibatizwe. Sasa nilikuwa mmoja wa watumishi wa Yehova! Hiyo ilikuwa Mei 18, 1963, siku ambayo sitasahau kamwe.

Kuingia na Kutoka Kwenye Makao ya Utunzaji

Katika Novemba, ilikuwa nitoke hospitalini. Sikutaka kurudi nyumbani kwa sababu nilijua utumishi wangu kwa Yehova ungepungua sana huko. Kwa hiyo nilifanya mipango kuingia katika makao ya utunzaji. Huko nilianza kushiriki katika huduma kwa kuandika barua kwa watu ambao ilikuwa vigumu kwa Mashahidi kuwapata katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Nilisoma pia safu za matangazo ya vifo katika magazeti ya habari na kuandikia watu wa ukoo wa wale waliokufa majuzi, nikitia ndani maandiko yenye kufariji kutoka kwenye Biblia.

Halafu, katika Mei 1964, nilihamia New York City kuishi na dada yangu mkubwa zaidi pamoja na mumeye. Mumeye alininunulia kiti-magurudumu changu cha kwanza, nikaanza kuhudhuria mikutano. Ilikuwa shangwe iliyoje kutoa hotuba yangu ya kwanza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi nikiwa katika New York City!

Mapema katika 1965, baadhi ya marafiki kutoka Philadelphia waliniomba nikae nao kwa majuma mawili. Nilipokuwa ningali Philadelphia, dada yangu aliniandikia na kuniambia kwamba hakunitaka tena na kwamba nilipaswa kukaa mahali nilipokuwa. Nilipanga kuingia tena katika makao ya utunzaji. Nilipokuwa nikiishi huko, niliendelea kuhudhuria mikutano na kutolea watu ushahidi kwa kuandika barua. Ilikuwa wakati huu kwamba niliweza kupanua huduma yangu kwa kushiriki katika kazi inayoitwa upainia-msaidizi.

Mpokeaji wa Utunzaji Wenye Upendo

Wonyesho zaidi wa utunzaji wa Yehova ulikuwa msaada niliopewa na Kutaniko la West la Mashahidi wa Yehova katika Philadelphia. Zaidi ya kunipeleka kwenye mikutano ya Kikristo, waliniandalia vitabu na ugavi mwingine niliohitaji kwa ajili ya huduma yangu.

Katika 1970 uthibitisho zaidi wa utunzaji wa Yehova ulitukia wakati ambapo mipango ilifanywa ili nihamie kwa Maude Washington, dada Mkristo na muuguzi aliyestaafu. Ingawa alikuwa akikaribia miaka 70 wakati huo, yeye alinitunza kwa hiari kwa miaka miwili iliyofuata hadi aliposhindwa kuendelea kufanya hivyo zaidi.

Nilipokuwa ningali na Maude, akina ndugu wa Kutaniko la Ridge katika Philadelphia walifanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha kwamba niliweza kuhudhuria mikutano yote. Hii ilihitaji wanibebe kupanda na kushuka ngazi tatu za madaraja ya orofa mara tatu kwa juma. Ninawashukuru kama nini wale waliofanya kazi kwa uaminifu kunisaidia kufika mikutanoni!

Katika 1972, wakati ambapo Dada Washington hangeweza kunitunza tena, niliamua kupata chumba changu mwenyewe. Rekebisho hili halingewezekana bila msaada wenye kujidhabihu na upendo wa dada Wakristo katika Kutaniko la Ridge. Walifanya mipango ya kunilisha, kuniosha, na kushughulikia mahitaji yangu ya kibinafsi. Wengine walisaidia kwa kufanya ununuzi na kwa kushughulikia shughuli nyinginezo muhimu.

Kila asubuhi hao akina dada walifika ili kunilisha na kunivisha kwa ajili ya hiyo siku. Baada ya kunisaidia kuketi kwenye kiti-magurudumu changu, wangenipeleka hadi kwenye dawati langu katika pembe ndogo ya chumba, karibu na dirisha. Hapo ningeketi, nikijihusisha katika huduma kwa kutumia simu na kwa kuandika barua. Nililiita eneo hili la chumba changu pembe ya paradiso, kwa kuwa niliipamba kwa picha nyingi za kitheokrasi. Ningetumia siku yote katika huduma yangu hadi mtu mwingine alipokuja usiku ili kunipeleka kitandani.

Katika 1974 afya yangu ilihitaji niingie hospitalini. Nilipokuwa huko, madaktari walijaribu kunisonga nitiwe damu. Juma moja hivi baadaye, baada ya hali yangu kuboreka, wawili wa hao madaktari walikuja kunitembelea. “Ah, nawakumbuka ninyi wawili,” nikawaambia. “Mlijaribu kunisadikisha nitiwe damu.”

“Ndiyo,” wao wakajibu, “lakini tulijua hatungefaulu.” Nilikuwa na fursa ya kuwatolea hao madaktari ushahidi kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo na kuhusu dunia iliyo Paradiso.—Zaburi 37:29; Yohana 5:28, 29.

Wakati wa miaka kumi ya kwanza niliyoishi peke yangu, niliweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Sikuikosa isipokuwa nilipokuwa mgonjwa. Ikiwa halihewa ilikuwa mbaya, akina ndugu na dada walikuwa wakifunga miguu yangu kwa blanketi na kuifunika ili kuiweka ikiwa mikavu. Mara kwa mara mwangalizi asafiriye angekuja kuniona. Wakati wa ziara zake, yeye “alikuwa akiandamana” nami kwa funzo la Biblia nililoongoza kwa kutumia simu. Hizi zilikuwa nyakati za shangwe kuu kwangu.

Kukabiliana na Hali Yenye Kuzidi Kuwa Mbaya

Katika 1982, nilifikia hatua ambapo sikuweza tena kutoka kitandani. Sikuweza kuhudhuria mikutano, wala kupainia, jambo ambalo nilikuwa nimefanya kwa miaka 17 mfululizo. Hali hizi zilinihuzunisha sana, na mara nyingi nilikuwa nikilia. Hata hivyo, utunzaji wa Yehova ulikuwa dhahiri—wazee Wakristo walipanga kuwe na Funzo la Kitabu la Kutaniko katika chumba changu kidogo. Jinsi ninavyoshukuru bado kwa uandalizi huu!

Kwa kuwa nilikuwa siwezi kutoka kitandani siku nzima na sikuweza kufika kwenye dawati langu, nilianza kujizoeza kuandika kwenye kikaratasi ambacho nilikuwa nikiwekelea juu ya kifua changu. Mwanzoni, mwandiko wangu haukuweza kusomeka, lakini kwa mazoezi mengi, ulikuja kuwa wenye kusomeka. Kwa kipindi cha wakati niliweza tena kutoa ushahidi kwa kuandika barua, na hili liliniletea kiasi fulani cha shangwe. Kwa kusikitisha, hali yangu imezorota zaidi, na siwezi tena kushiriki katika sehemu hii ya huduma.

Ingawa sijaweza kuhudhuria kimwili mkusanyiko wa wilaya tangu 1982, najaribu kuwa katika hali ya pindi ya wakati wa mkusanyiko. Dada mmoja Mkristo huniletea beji na kuibana kwenye gauni yangu ya kulala. Pia, mimi huifungulia televisheni kwenye mchezo wa besiboli kwenye Stediamu ya Veteran katika Philadelphia na kufikiri kuhusu mahali nilipokuwa nikikaa wakati wa mikusanyiko huko. Kwa kawaida, mtu mwingine hurekodi programu ya mkusanyiko ili niweze kuisikiliza yote.

Kutokubali Kushindwa

Ingawa siwezi kufanya mengi kama nilivyokuwa nikifanya zamani katika huduma, bado mimi hutaka kuongea na watu kuhusu kweli za Biblia. Kuweza kupainia na kusaidia idadi kadhaa ya wenye kupendezwa kujifunza Biblia kumekuwa chanzo cha shangwe. Ingawa haijawa rahisi kuishi peke yangu kwa miaka 22 iliyopita, nimefurahia uhuru wa kumtumikia Yehova bila kizuizi, jambo ambalo singeweza kufanya ikiwa ningebaki nyumbani.

Nimeona pia uhitaji wa kufanya kazi kwa bidii ili kurekebisha utu wangu mwenyewe. Nyakati fulani matamko yangu hayajatolewa sikuzote kwa shukrani ninapotoa mwongozo kwa wale ambao wamejitolea kunisaidia. (Wakolosai 4:6) Naendelea kusali kwa Yehova anisaidie kuboresha sehemu hii. Ninashukuru kwelikweli roho ya subira na ya kusamehe inayoonyeshwa na wale ambao wamenivumilia katika upendo kwa hiyo miaka yote. Msaada wao wenye upendo ni baraka ambayo kwa ajili yayo nawashukuru wao na Yehova.

Ingawa kimwili nimekuwa siwezi kuhudhuria mikutano kwa miaka mingi—sijatoka nje ya chumba changu kwa wakati huo wote isipokuwa mara moja kwenda hospitali—bado nina shangwe na furaha. Ni kweli, nyakati nyingine mimi hushuka moyo, lakini Yehova hunisaidia kutoka katika hali hiyo. Sasa nafurahia kusikiliza mikutano kupitia njia ya simu kutoka Jumba la Ufalme. Kwa kumtegemea Yehova kupitia sala na kutumaini katika yeye, sijajihisi kamwe nikiwa peke yangu. Ndiyo, naweza kwelikweli kusema kwamba nimenufaika kutokana na utunzaji wa Yehova.—Kama ilivyosimuliwa na Celeste Jones.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Nililiita eneo hili ambapo nilishiriki katika huduma pembe ya paradiso

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki