Nashukuru kwa Ajili ya Utegemezo wa Yehova Usioshindwa
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA SHARON GASKINS
DUNIA paradiso! Nilijiona mwenyewe nikiruka huku na huku kondeni, nikikimbiza vipepeo, nikicheza na vitoto vya simba. Lilisikika kuwa jambo zuri sana! Lakini kulikuwako shaka. Tumaini langu lilikuwa limeishia katika hali ya kukata tamaa mara nyingi kama nini!
Kwa muda mrefu kadiri niwezavyo kukumbuka, kiti chenye magurudumu kimekuwa mwandamani wangu wa daima. Tangu nizaliwe na kuendelea, ugonjwa wa kupooza kwa ubongo ulininyang’anya shangwe za utoto. Watoto wengine walifurahia kucheza na viatu vyenye magurudumu na kuendesha baiskeli, lakini mimi niliketi nikiwa peke yangu, nisiweze hata kutembea. Kwa hiyo Mama aliponipeleka kwa mponyaji wa imani mmoja baada ya mwingine, tulikuwa tukitumaini kwa bidii kuona muujiza. Lakini, tena na tena, tungeondoka bila kuponywa. Hilo lilinikatisha tamaa, lakini lilimvunja moyo mama kama nini!
Akitamani tumaini la kweli, mama yangu alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova mapema katika 1964. Wakati huo nilikuwa karibu umri wa miaka sita na nusu.
Lilikuwa jambo zuri ajabu kujifunza kwamba wakati mmoja kulikuwako paradiso yenye kupendeza kwenye dunia hii. Kwa kuhuzunisha, mwanamume wa kwanza, Adamu, alikuwa ameipoteza, lakini nilitamani ukaribu wa Mungu ambao Adamu alikuwa amefurahia wakati mmoja. Ingalikuwa namna gani kufurahia uhusiano na Mungu? Au kuishi wakati Mwana wake mwenyewe alipokuwa duniani? Ndoto zangu za mchana zilinipeleka pia hadi Paradiso ya wakati ujao. Hata katika umri huo wa uchanga, ilikuwa wazi kwangu kwamba tulikuwa tumeipata kweli.
Mama alianza kupeleka familia kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Mikutano yao ilikuwa tofauti sana na ile tuliyokuwa tumeona katika makanisa! Watu na mazingira yalisisimua sana hisiamoyo zangu.
Mwanzoni, lilikuwa jambo gumu kwa mama yangu kutupeleka kwenye Jumba la Ufalme. Zaidi ya mimi, kulikuwako watoto wengine wachanga watatu, na hatukuwa na gari. Tulienda kwa teksi wakati ambapo angeweza kuilipia. Ningali nakumbuka jinsi alivyong’ang’ana Jumapili moja. Hakukuwa na teksi karibu. Kisha, kwa ghafula, mtu alitokea akatupeleka katika lori lake. Tulichelewa kufika kwenye mkutano, lakini tulifika. Tulimshukuru Yehova kama nini!
Upesi akina ndugu na dada wetu wapendwa wa kiroho waliokuwa na magari walifanya kwa upendo zamu za kutusafirisha. Kitia-moyo cha mama cha kutokosa mikutano kamwe isipokuwa kama tulikuwa wagonjwa kwelikweli kulikaza juu ya akili yangu changa umaana wa ‘kukusanyika pamoja.’ (Waebrania 10:24, 25) Akisukumwa na yale aliyokuwa amejifunza, mama yangu alijiweka wakfu kwa Yehova akabatizwa katika 1965.
Kufikia wakati huo nilikuwa na umri mkubwa wa kutosha kuthamini mikutano kikamili zaidi. Katika Kundi la Cypress Hills katika Brooklyn, New York, kulikuwako watu wa Ulaya, weusi, Wahispania, na wengine wakiabudu pamoja. Ilionekana kuwa jambo lifaalo sana kwa watu wenye kumhofu Mungu kuishi katika udugu huo wa kweli.—Zaburi 133:1.
Mama yangu alinifundisha namna ya kujitayarisha kwa ajili ya mikutano. Hilo halikuwa tatizo kiakili, lakini lilikuwa tatizo kimwili. Kupooza kwa ubongo hugeuza kazi sahili kuwa kazi kubwa. Ilikuwa vigumu, na ingali vigumu, kuchora mstari ulionyooka ili kutia alama majibu katika fasihi yetu ya Biblia. Hata hivyo, kwa kujizoeza, nilifanya maendeleo katika kuchora mistari.
Akili yangu ilikuwa imejaa mambo ya kusema. Lakini yalipokuwa yakitoka kinywani mwangu, maneno hayo yalikuwa yanavurugika. Kujistarehesha kulikuwa muhimu ili misuli yangu isivutane. Nilihitaji pia kukaza fikira juu ya kutamka kila neno kwa wazi iwezekanavyo. Ningefadhaika ikiwa elezo lisingetoka jinsi lilivyopasa au nilipojua kwamba watu hawakuelewa maneno yangu. Lakini mara walipopata kunijua, akina ndugu na dada kundini waliweza kuelewa vema zaidi usemi wangu. Hata hivyo, bado nina siku njema na siku zenye matatizo kwa habari hiyo.
Miezi Sita ya Kuudhisha
Nikiwa na miaka minane, nilikuwa na ono la miezi sita ambalo limeniathiri hadi leo. Ujapokuwa utaratibu wote wa kitiba wa kimwili, kikazi, na kiusemi nilioupata tayari, madaktari walinipeleka kwenye hospitali ya kuwatibu walemavu katika West Haverstraw, New York. Mama yangu na mimi tulivunjika moyo. Miaka kadhaa mapema zaidi, wakati madaktari waliponichungua kimakosa kuwa punguani, aliwaambia kwamba asingenipeleka kamwe kukaa katika hospitali ya wenye kurukwa akili. Kwa hiyo hata mtengano wa muda ulikuwa vigumu kwake. Hata hivyo, aliona kwamba ili niweze kuishi maisha yenye matokeo bila kumtegemea yeye na baba yangu ilimaanisha niweze kujitegemea kimwili kadiri iwezekanavyo.
Makao hayo yalikuwa mazuri, lakini nilihisi nimeachwa. Kulia-lia machozi na mifoko yangu ya hasira ilionyesha hisia zangu juu ya mahali hapo. Wazazi wangu hawakuweza kusafiri mara nyingi ule mwendo wa muda wa saa tatu ili kunitembelea, hasa kwa kuwa Mama alikuwa na mimba ya mtoto wake wa tano. Walipolazimika kuondoka, niliudhika sana hivi kwamba daktari alisema ni lazima wanitembelee mara chache zaidi. Niliruhusiwa kwenda nyumbani mara mbili tu.
Matabibu walinifundisha namna ya kutembea kwa msaada wa kanda na mikongojo myepesi. Ilionekana kana kwamba ni mizito mno. Hata hivyo, uzito huo ulinisaidia nidumishe usawaziko wangu na kunizuia nisianguke chini. Hiyo ilikuwa hatua ya kwanza ya kutembea peke yangu bila kanda.
Kukata-kata chakula, kufunga vifungo—kazi yoyote iliyohitaji nitumie vidole vyangu—ilikuwa imekuwa ngumu sana kwangu au haikuwezekana. Lakini kwa kadiri fulani nilijifunza namna ya kujilisha na kujivisha nguo. Hilo baadaye lilisaidia katika utumishi wangu kwa Mungu.
Mazoezi yangu yalipokwisha, nilirudi nyumbani tena. Mama alinipa kazi mara hiyo ili niweze kutumia stadi zangu mpya. Kufanya hivyo lilikuwa pigano la kihisiamoyo, kwani ingawa nilitaka kujifanyia mambo mwenyewe, kuyatimiza kulifadhaisha, kulitumia wakati mwingi, na kulichosha. Kwani, kujivisha kwa ajili ya mkutano kulikuwa kazi ya muda wa saa mbili!
Tulipohamia mwendo wa kuvuka barabara tu kutoka kwa Jumba la Ufalme, kwa kweli nilikuwa nikitembea peke yangu hadi huko. Huo ulikuwa ushindi mkubwa sana!
Siku Yenye Furaha Zaidi Maishani Mwangu
Mama yangu alihakikisha kwamba familia ilikuwa na chakula cha kiroho chenye usawaziko. Alijifunza na mimi akanitazamia nisome kila toleo la magazeti yetu, Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kulikuwako mikutano ya kutayarisha na ya kuhudhuria. Ingawa akili na moyo wangu ulitwaa ndani kwa bidii ujuzi huo, mawazo mazito juu ya kuweka wakfu maisha yangu kwa Yehova na kuufananisha kwa ubatizo wa maji yalikuwapo pia. Mama alinisaidia nione kwamba ujapokuwa ulemavu wangu, Mungu aliniona nikiwa na daraka langu mwenyewe la kiroho. Nisingetazamia kuingia ulimwengu mpya kwa ajili ya ustahili wa mama yangu, kuokoka kwa kumtegemea yeye.
Nilimpenda Mungu, lakini nilijishuku mwenyewe. Je! ningeweza kufurahia afya kamilifu wakati wowote? Miaka yangu ya ubalehe ilikuwa yenye msukosuko. Hali hiyo ilinifanya kuwa tofauti na wengine—utambuzi wenye kumwumiza tineja. Ilikuwa vigumu kwangu kukubali mipaka yangu. Mara nyingi ningeshindwa na hasira, na hiyo ilihitaji kudhibitiwa kabla ya ubatizo. (Wagalatia 5:19, 20) Na namna gani ikiwa nisingeweza kutimiza wakfu wangu kwa Yehova?
Kwa ombi la mama yangu, mzee wa kundi alisema na mimi. Alitaja lile swali la nabii Eliya kwa Waisraeli: “Mtasita-sita katikati ya mawazo mawili hata lini?” (1 Wafalme 18:21) Kwa wazi, Yehova hakupendezwa na kusita-sita kwangu kufanya uamuzi.
Niliamka kiroho na kuomba kwa bidii msaada wa Yehova na kuomba kuwa na azimio la kuweka wakfu maisha yangu kwake. Dada mmoja kundini alijifunza na mimi. Alikuwa mchanga zaidi ya mimi na alikuwa amepoteza mama yake akiwa mchanga. Hata hivyo, alikuwa amejiweka wakfu kwa Mungu akiwa angali mchanga sana.
Nikiwa na miaka 17, nilikuwa nimeamua kabisa. Nilitaka kumtumikia Yehova vizuri kadiri niwezavyo. Agosti 9, 1974—nilipobatizwa—ilikuwa siku yenye furaha zaidi maishani mwangu.
Shangwe Katika Huduma
Kushiriki katika huduma kulitokeza vizuizi vilivyo kama mlima. Ugumu mkubwa zaidi ulikuwa kufanya nieleweke. Nilikuwa nikisema kwa wazi iwezekanavyo. Kisha, ilipohitajiwa, mshiriki wangu katika huduma ya shambani alikuwa akirudia maelezo yangu kwa mwenye nyumba. Wengine hawakuitikia ifaavyo, wakiniona kuwa mwenye kutumiwa vibaya na Mashahidi. Lakini kuhubiri ni haki yangu na tamaa yangu ya kuhisiwa moyoni.
Kutembea nyumba kwa nyumba hata kwenye barabara moja kwaweza kunichosha kabisa. Nyumba nyingi katika eneo letu la kutolea ushahidi zina ngazi, hivyo siwezi kuzifikia. Katika majira ya kipupwe, barabara zenye barafu hufanya kazi ya nyumba kwa nyumba isiwezekane kwangu. (Matendo 20:20) Hata hivyo, ndugu wa kiroho wamesaidia sana, na Yehova amenibariki sasa na kiti cha magurudumu chenye mota, kinachofanya huduma iwe rahisi zaidi.
Baada ya muda fulani nilianza kutoa ushahidi kwa barua. Kuandika barua kwa mkono kusingefaa kwa sababu maandishi yangu hayasomeki na watu wengi. Kwa hiyo taipureta ya stima ikawa mwandishi wangu. Kuchapa kwangu kwa taipureta kulikuwa polepole sana kwa sababu ya kutoweza kudhibiti mkono wangu vizuri. Karibu nusu ya wakati, ninalenga herufi moja kwenye taipureta na kugonga herufi nyingine. Yaweza kuchukua muda wa saa moja au zaidi kuchapa ukurasa mmoja tu.
Ujapokuwa ukosefu wa nguvu, mara kwa mara mimi hutumikia nikiwa painia msaidizi, nikitumia muda wa saa 60 au zaidi katika huduma kila mwezi. Hilo huhitaji ratiba nzuri, bidii zaidi, na utegemezo wa waamini wenzangu. Roho yao ya upainia hunitia moyo. Mama pia ameniwekea kielelezo kizuri kwa kutumikia akiwa painia wa kawaida au painia msaidizi huku akikabili magumu, afya mbaya, na ugumu wa kuwalea watoto saba katika nyumba iliyogawanyika kidini.
Kuishi Peke Yangu
Nikiwa na miaka 24, niliamua kuondoka na kuishi peke yangu. Kuhamia kwangu sehemu ya Bensonhurst ya Brooklyn kulithibitika kuwa baraka. Kundi la Marlboro lilikuwa kama familia yenye ukaribu. Kuwa pamoja nao kuliimarisha imani kama nini! Hata kukiwa na magari mawili au matatu tu kundini, ndugu wa kiroho walinipeleka kwa mikutano yote. Hata hivyo sikukaa huko kwa muda mrefu.
Nikihisi kutofaulu hata kidogo, nilirudi kwa familia yangu nikatumbukia katika kipindi cha kushuka moyo sana cha miaka mitatu. Mifoko ya hasira ikarudia tena. Kisha kukaja mawazo ya kujiua na majaribio mengi ya kufanya hivyo. Kifo kilikuwa taraja la daima na lenye kuhofisha. Lakini nilianza kumtegemea Mungu nikaahidi kuonyesha uthamini kwa ajili ya zawadi yake ya uhai. Faraja na shauri lilitoka kwa wazee. Hilo, pamoja na sala, funzo la binafsi, saburi kwa upande wa familia yangu, na msaada wa kitiba, ulisahihisha fikira zangu.
Kupitia Mnara wa Mlinzi, Yehova aliandaa kwa wororo mwono-ndani katika mshuko wa moyo mbaya sana. Naam, yeye kwa kweli hujali watu wake na kuelewa hisia zetu. (1 Petro 5:6, 7) Hatimaye mshuko huo wa moyo wenye kina ulipungua. Miaka kumi baadaye, Yehova bado hunisaidia nishughulikie hali ya kufadhaika na mshuko wa moyo. Nyakati nyingine hisia za kutofaa kitu karibu hunilemea. Hata hivyo, sala, funzo la Biblia, na familia yangu ya kiroho ni misaada mizuri ajabu ya kuokoka hali hii.
Baada ya kutafuta-tafuta nyumba nyingine bila kufanikiwa, nilikuwa nimeazimia kwa moyo usiotaka kuishi na familia yangu kwa maisha yangu yote. Kisha Yehova akajibu sala zangu. Mahali palipatikana katika sehemu ya Bedford-Stuyvesant ya Brooklyn. Kufikia mwisho wa kiangazi cha 1984, nilihama, nami nimekuwa huko tangu wakati huo.
Washiriki wa Kundi la Lafayette lenye upendo walinisafirisha kwenye mikutano kwa fadhili. Ningali nakumbuka vema Funzo la Kitabu la Kundi la kwanza nililohudhuria. Lilifanywa kwenye orofa ya nne—na hakukuwa na lifti! Ni kwa msaada wa Yehova tu kwamba niliweza kupanda na kushuka ngazi hizo. Baadaye mahali paliandaliwa ambapo ningeweza kufikia kwa urahisi. Na sasa Yehova amenibariki na pendeleo la kuwa na Funzo la Kitabu la Kundi ndani ya nyumba yangu.
Roho nzuri ajabu ya painia huenea kundi hili. Nilipokuja, kulikuwa na mapainia karibu 30, na baadhi yao walinipa uangalifu wa pekee. Mazingira hayo ya kuonyesha bidii yalinisukuma kuwa painia msaidizi mara nyingi zaidi.
Katika Aprili 1989 Makundi ya Lafayette na Pratt yalijenga Jumba la Ufalme jipya kwenye barabara ileile ya nyumba yangu. Hilo lilitukia wakati ufaao kabisa, kwani kwa sababu ya kudhoofika zaidi kimwili, kutembea kulikuwa tatizo tena. Hata hivyo, kwa skuta yangu yenye mota na kwa utegemezo na msaada wa ndugu na dada wa kiroho, safari za kwenda na kurudi kutoka kwa mikutano ni zenye kupendeza. Ninathamini sana kama nini msaada huo wenye upendo!
Nashukuru kwa Ajili ya Utegemezo wa Mungu
Ingawa miguu yangu si thabiti, moyo wangu ni imara. Elimu nzuri ilifanya maisha yawe rahisi zaidi, na Mungu amenitegemeza. Nyakati nyingine sikujua chakula changu kingetoka wapi, lakini Yehova amenitegemeza na amekuwa Mwandalizi mwaminifu. Kwa kweli ninayapenda sana maneno haya ya Daudi: “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, lakini sijamwona mwenye haki ameachwa, wala mzao wake akiomba chakula.”—Zaburi 37:23-25.
Mara kadha Yehova ameniwezesha nidumishe msimamo wa Kimaandiko kwa kunisaidia kukataa kukubali damu wakati wa upasuaji. (Matendo 15:28, 29) Hivi karibuni, baba yangu alikufa. Kumpoteza mtu wa karibu namna hiyo kulinisononesha sana. Ni nguvu kutoka kwa Yehova tu ambayo imenisaidia kuvumilia hilo na majaribu mengine.
Afya yangu huenda ikazidi kudhoofika, lakini kumtumainia kwangu Mungu na uhusiano wangu na yeye ndiyo hunitegemeza. Nashukuru kama nini kuwa miongoni mwa watu wa Yehova na kuwa na utegemezo wake usioshindwa!