Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w90 12/1 kur. 26-29
  • Yehova Amenipa Nguvu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova Amenipa Nguvu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Magumu Yanaanza
  • Mwanzo wa Maisha Mapya
  • Uvumilivu Ulileta Faida
  • Mwenye Moyo Mkuu Mbele ya Wenye Mamlaka
  • Utumishi wa Pekee
  • Mgawo Mpya
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
  • ‘Nitapanda Juu Kama Vile Paa Anavyofanya’
    Amkeni!—2006
  • Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Nina nguvu ingawa mimi ni dhaifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
w90 12/1 kur. 26-29

Yehova Amenipa Nguvu

KAMA ILIVYOSIMULIWA NA EKUMBA OKOKA

MIMI nilizaliwa katika nyumba “ya Kikristo” katika nchi moja ya Afrika ya Kati, na nilikua nikiwa nampenda Mungu. Baba yangu alikuwa mhubiri mwenye bidii wa mtaani, na mara nyingi nilienda naye alipofundisha katika kanisa au katika vipindi vya sala katika makao ya faragha. Kwa kuwa ilionekana ni kama nilikuwa mvulana mchanga mwenye kujitoa, wahubiri wengine wa mtaani walinichagua nitumike kando ya padri kwenye Misa. Hata waliniambia kwamba inaelekea siku fulani ningejifunza kuwa padri mimi mwenyewe.

Hata hivyo, wakati wa usiku nilikuwa mwimbaji na mcheza dansi mashuhuri katika okestra ya mahali hapo, ile Matumba-Ngomo. Katika hali hiyo, nilijiunga na wanaume na wanawake vijana wa wilaya yetu katika aina zote za ukosefu wa adili. Lakini bado nilitazamia kuwa na mke mmoja tu na mwishowe kwenda mbinguni nikaishi pamoja na “watakatifu.” Sikuona uhitaji wa kusafisha maisha yangu kwa sababu, kulingana na fundisho la Kikatoliki, dhambi zangu zote zilisamehewa kila jioni ya Jumamosi kwenye ungamo.

Magumu Yanaanza

Katika 1969, nilipokuwa nikijifunza kwenye koleji, nilianza kuona maumivu katika maungo yangu. Sikujua yaliletwa na nini, lakini katika miezi iliyofuata, yakawa mabaya zaidi. Wazazi wangu, ingawa walikuwa Wakatoliki wenye kujulikana, waliamua kunipeleka kwa waganga tofauti wa kienyeji, waliosema kwamba mtu fulani alikuwa ameniloga, lakini asante kwa sala na dawa zao, mimi ningeponywa. Hata hivyo, nilianza kutembea kwa kuchechema, na kufikia 1970, ikawa ni kama siwezi kamwe kutembea, hata ninapoegemea mkongojo. Wakati huo, nilifikiri kwamba siku zangu za kutembea zingeisha karibuni.

Katika Februari 1972 baba yangu aliamua mwishowe kunipeleka kwenye hospitali iliyoko Wembo Nyama. Nilikuwa katika hospitali kwa muda mrefu hivi kwamba wakaanza kuniita mwenye hospitali! Watu walikuwa wakija hospitali, wanaponywa, wanaondoka, halafu muda fulani baadaye wanarudi na tatizo jingine, na bado mimi ningekuwa pale! Baba yangu alilazimika kwenda nyumbani kwa ajili ya mavuno ya mpunga, lakini kufikia sasa nilikuwa nimefunga ndoa, nikiwa na watoto wawili, na mke wangu mpenzi, ingawa alikuwa na umri wa miaka 21 tu, alinitunza na kutafuta kazi ili aweze kuangalia mahitaji yetu.

Hata hivyo, nilishuka moyo sana juu ya hali nzima. Nikiwa na umri wa miaka 24, bado hali yangu ilizidi kuwa mbaya, huku rafiki zangu wakiendelea vizuri, wengi wao sasa wakiwa na kazi zilizo thabiti. Kwangu ilionekana kwamba ingekuwa afadhali zaidi kwa kila mtu kama ningejiua. Hivyo, niligawia watoto wangu na ndugu zangu kila kitu nilichokuwa nacho, bila kuwaambia nililokuwa nikifikiria. Nilijiacha bila kitu isipokuwa shati yangu niliyoipenda sana ambayo nilitaka nizikwe nimeivaa.

Mwanzo wa Maisha Mapya

Halafu mmoja wa Mashahidi wa Yehova akagawiwa kwenye kitanda kilicho karibu na changu. Ingawa alikuwa kipofu katika jicho moja na katika hatari ya kupoteza muono wa lile jingine, alianza upesi kunitolea ushahidi kutokana na Biblia juu ya Yehova na Ufalme. Baada ya siku chache, aliondoka hospitali, lakini akaniacha mikononi mwa Mashahidi fulani waliokuwa wamemzuru. Baada ya mazungumzo zaidi, hawa pia walilazimika kuondoka, lakini mmoja wao aliendelea kujifunza nami kwa barua. Pia alinipa vichapo mbalimbali vya kujifunza Biblia, ambavyo nilisoma kwa furaha nyingi.

Kwa njia hii nilipokea chakula cha kiroho, na mshuko wangu wa moyo ukabadilika pole kwa pole kuwa furaha. Ilionekana ni kama kanisa langu lilikuwa limekuwa likinipa “asidi” ninywe, lakini sasa nilikuwa nikipokea kwa utele maji ya uhai. Nilimpa Yehova asante katika moyo wangu kwa kuniweka huru na imani zenye woga wa kishirikina, kama vile Utatu, kutokufa kwa nafsi, hofu juu ya wafu, na ibada ya mababu waliokufa.

Lakini sasa nilitaka kuondoka hospitali. Halafu nikapata habari kwamba jamaa mbili za wahudumu wa wakati wote zingegawiwa kuja Wembo Nyama, hivyo basi nikaamua kukaa mpaka kufika kwao. Lo, niliona furaha iliyoje walipokuja mwishowe wakanikuta katika kitanda changu cha hospitali! Sasa niliweza kuendelea na funzo langu la Biblia kwa kulifanya kibinafsi badala ya kupitia barua.

Baada ya siku chache, niliwauliza kama walikuwa na mikutano katika Jumba la Ufalme, kama nilivyokuwa nimesoma katika magazeti. Waliniambia kwa fadhili kwamba waliongoza mikutano yao yote katika kijumba kidogo ambamo mmoja wao aliishi. Pia walisema kwamba wangefurahi kunipeleka huko nikiwa juu ya baiskeli! Ingawa nilikuwa na maumivu makali katika uti wa mgongo wangu na katika maungo yangu yote, nilihudhuria kwa shangwe mikutano yote. Nilipotimiza sifa, hata niliweza kutoa ripoti kila mwezi nikiwa mhubiri asiyebatizwa, kuanzia Aprili 1974.

Miezi mitatu baadaye, nilifananisha wakfu wangu kwa Yehova kwa uzamisho katika maji. Niliwatolea ushahidi wafanya kazi wa tiba wa hospitali ile, kwa wagonjwa wa huko, kwa wamisionari Waprotestanti waliokuja kuzuru, na kwa washiriki wa jamaa yangu—ingawa upinzani ulioazimiwa na hawa wa mwisho. Wakati huu, nilitoa ushahidi nikiwa nimelalia kitanda changu au kuendesha kiti-magurudumu ambacho hospitali ilinitolea mpaka niweze kununua changu mwenyewe.

Uvumilivu Ulileta Faida

Ingawa jamaa yangu ilipinga, niliendelea kutembea katika njia ya Yehova nami nikabarikiwa kwa wingi. Mke wangu alichukua msimamo wake upande wa ukweli na kubatizwa katika 1975. Tuliamua kuishi katika Katako-Kombe, ambako tayari kulikuwako kundi lililokwisha kuanzishwa. Wazazi wangu walifanya wasiwasi juu yetu kwa sababu mtu fulani alikuwa amewaambia kwamba Mashahidi wote wangeuawa katika 1975. Tulipokataa kuacha ushirika wetu, waliacha kutupelekea chakula, nasi tukaingia katika shida kubwa ya kimwili. Nakumbuka kwamba katika pindi moja mwana wangu mchanga alizimia kwa njaa baada ya sisi kuwa tumeshinda siku moja na nusu bila chakula. Lakini ndipo ndugu zetu Wakristo walipotuletea samaki na unga. Baadaye, wazazi wangu walianza kutusaidia tena, lakini ndugu zetu hawakuacha kamwe kutupa msaada wa kimwili.

Katika Februari 1975 mkono wangu wa kulia ulipooza na kuanza kudhoofika. Lakini niliendeleza imani yangu na kupiga moyo konde niendelee kutumikia Yehova kwa shangwe. Nina furaha kusema kwamba baadaye mkono wangu ulipata nguvu tena, na leo bado naweza kuusogeza, jambo ambalo linaniwezesha kufungua Biblia yangu na kutumia vichapo vya Sosaiti.

Mwenye Moyo Mkuu Mbele ya Wenye Mamlaka

Katika 1977 mwongoza-tume wa mahali petu alinishtaki mbele ya tume ya jimbo, ambayo sasa tu ilikuwa imekamata painia wa pekee mmoja katika kundi la karibu. Siku moja askari alikuja kuniitia mashtaka. Nilisali pamoja na jamaa yangu, nikatia kundi moyo mkuu, halafu nikaenda naye. Asante kwa roho ya Yehova, niliweza kutoa jibu la moyo mkuu kwa mashtaka hayo, na baada ya mazungumzo ya muda mrefu pamoja na wenye mamlaka wa kiraia na wa kijeshi, niliachiliwa pamoja na yule painia wa pekee.

Miezi fulani baadaye, niliitiwa mashtaka na mwongoza-tume mwingine, na tena, kwa msaada wa Yehova, nikaweza kutetea habari njema kwa shangwe na moyo mkuu. Nilifanya mazungumzo marefu pamoja na mtu huyu, na mwishoni mwayo, akaniachilia na yeye binafsi akasukuma kiti-magurudumu changu kukileta nje ya ofisi yake. Halafu akasema kwa utulivu hivi: “Uje nyumbani kwangu jioni hii.” Baada ya ziara kadhaa, niliweza kuanza funzo la Biblia naye. Mwishowe, nilifanya mafunzo saba ya nyumbani ya Biblia pamoja na watu tofauti katika mamlaka. Walio wengi kati yao walihudhuria mikutano ya kundi iliyotengenezwa mahali pa kwao.

Utumishi wa Pekee

Nilimwomba Yehova anisaidie, ingawa ugonjwa wangu, ili nitimize nadhiri yangu kumtumikia kwa nguvu yangu yote. Bila kujiandikisha rasmi, nilijaribu kutimiza matakwa ya painia msaidizi. Yehova alinisaidia kufanikiwa, hivyo basi nikajaza ombi la utumishi huu kwa miezi ya Juni kufika Oktoba. Halafu Sosaiti ikakubali ombi langu la kuwa painia wa kawaida, nami nikaanza utumishi huu katika Novemba 1976. Katika Septemba  1977 shangwe yangu ilikamilika nilipopokea mgawo wa kuwa painia wa pekee pamoja na kundi huko Katako-Kombe.

Niliwezaje kutimiza jambo hili? Nilifanya kazi katika eneo lote nikiwa katika kiti-gurudumu changu kwa msaada wa mke wangu mpenzi na akina ndugu katika kundi. Nyakati fulani hata nilienda nje peke yangu kwa kutumia mikongojo. Nilianguka mara moja au mbili. Ndipo ningengojea tu, nikiwa hapo hapo chini bila kujongea, mpaka wakati ambapo mpita-njia angenisaidia kuinuka na kunirudishia mikongojo yangu. Sikuzote nilikumbuka hali ya kupiga moyo konde ya mitume na wanafunzi wa Yesu. (Matendo 14:21, 22; Waebrania 10:35-39) Kila wakati nilipoanguka, nilisali kwamba Yehova asiniache nivunjike moyo, bali anipe nguvu ya kuendelea kumtumikia. Sikuzote nilikumbuka ahadi ile nzuri sana iliyoandikwa katika unabii wa Isaya, kwamba “kilema ataruka-ruka kama kulungu.”—Isaya 35:6.

Kadiri nilivyozidi kuongeza utumishi wangu, ndivyo nilivyoweza zaidi kushinda vizuizi vyangu vya kimwili. Katika 1978 nilipata pendeleo la kuhudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme kule Lubumbashi, jambo ambalo lilihusisha kusafiri jumla ya kilometa 2,000 kwa lori, mashua, na gari-moshi. Kwa kweli, Yehova alifanya uwezo kamili uwe tele katika kisa changu. (Isaya 12:2; 40:29) Sasa naweza kutembea—kwa ugumu mkubwa—kufikia meta 100 bila msaada wa mikongojo. Mimi nasadiki kwamba Yehova alisikia sala yangu huko nyuma katika 1973 ya kunipa nguvu nimtumikie kwa kupiga moyo konde.

Mgawo Mpya

Katika 1984, baada ya miaka saba ya kuwa katika kundi la huko Katako-Kombe, nilipokea mgawo mpya nifanye kazi pamoja na kundi huko Lodja-Centre. Mwaka mmoja baadaye tulianzisha funzo jipya la kitabu kilometa 12 kutoka huko, na upesi tukaanzisha jingine kilometa 30 kutoka mahali hilo lilipo. Hili la pili lilitambuliwa upesi kuwa kikundi kilicho peke yake na katika 1988 likakubaliwa kuwa kundi, ambako wakati wa sasa natumikia nikiwa mzee.

Upainia umekuwa mzuri sana kwangu, kiroho na kimwili pia. Nikiwa nje katika utumishi, kwa kutumia mikongojo yangu, niliweza kutimiza yale mazoezi yaliyopendekezwa na madaktari. Sasa mimi ni mwenye nguvu kuliko wakati nilipoanza upainia, na tamaa yangu ni kuvumilia katika kazi hii mpaka mwisho. Nina hamu kuona jinsi Yehova atanisaidia ‘kuruka-ruka kama kulungu’ wakati ambapo haitakuwa lazima tena nivumilie yale maumivu makali ya ugonjwa huu.

Kwa moyo wangu wote, mimi nashukuru Baba yetu wa kimbingu, ambaye amenipa nguvu, moyo mkuu, na utumishi wa wakati wote. Sasa nina miaka 36, na baada ya miaka 11 katika kazi ya painia, natumaini kuendelea, hata kama kuna nini wakati ujao. Nimepiga moyo konde kutumia nguvu zote za uhai wangu katika kuheshimu na kusifu yule Mungu mkubwa Yehova.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki