Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w82 2/1 kur. 20-23
  • Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KUKOSA TUMAINI KABISA
  • MWANZO WA TUMAINI
  • FURAHA KATIKA UTUMISHI WA KIKRISTO
  • BARAKA UJAPOKUWA UPINZANI
  • FURAHA NILIYOIPATA KARIBUNI YAWA WAZI KWA WENGINE
  • VITA HAVIKUNINYANG’ANYA FURAHA
  • MATUNDA YA KUSTAHIMILI
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
  • Yehova Amenipa Nguvu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Nashukuru kwa Ajili ya Utegemezo wa Yehova Usioshindwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Uchaguzi Wangu Kati ya Baba Wawili
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
w82 2/1 kur. 20-23

Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha

Kama inavyosimuliwa na Estefan Kalajian

TULIKUWA tunaishi katika nyakati zenye magumu katika Beirut, Lebanon, wakati wa vita ya ulimwengu ya pili. Jamaa yetu ya watu saba ilikuwa ikiishi ndani ya kichumba kidogo na ilikuwa na jikoni na maliwato (bafu) ndogo sana. Mimi ndimi niliyekuwa mvulana mkubwa zaidi, na nilikuwa na dada mkubwa wangu na mchanga wangu, pamoja na ndugu wawili wachanga wangu. Wazazi wetu na babu na nyanya zetu walikuwa Waarmenia waliokuwa wametoroka Uturuki.

Baba alikuwa akifanya kazi kwa bidii akiwa mshona-nguo ili atupe riziki. Mahali pa kunipeleka nikafanye kazi, kama ambavyo wazazi wengi walivyofanyia watoto wao, mimi nilipelekwa shuleni. Lakini baada ya kumaliza miaka miwili peke yake, nikapatwa na maradhi ya baridi yabisi. Miguu yangu haikuweza kuinua mwili wangu.

Mjomba wangu, ambaye wakati huo alikuwa akiishi Haifa, Israeli, akasikia juu ya hali yangu naye akauliza nipelekwe kwake nipewe matibabu. Baada ya mwezi mmoja nilipata afya, bila shaka hali ya hewa ya Haifa ilishiriki kunipa nafuu haraka. Walakini miaka kadha baadaye maradhi hayo yalinipata tena, yakaambukia hasa shingo na fundo la uti wa mgongo wangu. Nikarudi Haifa na kwa mara nyingine nikapona.

Hata hivyo, ugonjwa huo ukaendelea kurudi na kuwa mbaya zaidi. Baba yetu mpendwa, ambaye peke yake ndiye aliyekuwa mwenye kutupa riziki, akafa mwaka 1951. Nilikuwa mwenye umri wa miaka 16 na nikabaki nikiwa na mama yangu na dada mkubwa wangu. Watoto wale wachanga zaidi walipelekwa kwenye makao ya kutunza watoto wasio na wazazi. Upesi baadaye nikawa mgonjwa tena. Mama na dada yangu walifanya yote waliyoweza wanitafutie ponyo, wakitumia zaidi ya nusu ya mshahara wao ukiunganishwa pamoja ili kunitunza.

Katika mwaka 1953 niliingia katika hospitali ambayo ndiyo ingekuwa ya mwisho kuiingia nikitembea. Walijaribu namna zote za maponyo juu yangu, hata wakajaribu namna mpya za dawa, walakini yote ilikuwa kazi bure. Baada ya kukaa siku 26 katika hospitali hiyo, madaktari walisema kwamba miguu na mgongo wangu ulikuwa umepooza kwa daima. Kwa kweli, walimwambia mama yangu kwamba ningeishi miezi michache tu​—hiyo ilikuwa miaka zaidi ya 28 iliyopita!

KUKOSA TUMAINI KABISA

Nilirudi nyumbani nikangojee nife. Ingawa rafiki zangu, watu wa ukoo na jirani walijua juu ya hali yangu, ni wachache tu waliokuja kunitembelea. Ilionekana kama kwamba kila mtu alikuwa ananiona sifai kitu. Sana-sana rafiki wa umri wangu waliniacha.

Kwa upande mwingine, watu fulani wenye umri mkubwa zaidi walikuja ‘kunifariji.’ Waliniambia kwamba Mungu alinipenda kweli kweli na kwa hiyo alikuwa akiijaribu imani yangu. Hayo yalifanya nihisi (nisikie) vibaya zaidi. Mimi niliwajibu hivi: “Laiti Mungu asingalinipenda! Kama angenichukia pengine ningekuwa bado mwenye afya na mwenye kutembea.”

Mwaka mmoja ukapita, nami sikufa. Kwanza niliweza kutegemezwa nikiwa kitini, miguu yangu ikiwa imenyoshwa mbele yangu isiweze kujikunja. Ningeweza kutumia mikono yangu na kusogeza kichwa changu kidogo. Walakini baada ya muda, maradhi hayo yaliponiingilia sana, polepole mikono yangu ikaharibika kabisa na nikawa siwezi kusogeza kichwa changu upande huu na huu. Kwa miaka 19 iliyopita nimekuwa kitandani.

Maisha yalikuwa hayavumiliki. Nikaamua kujiua, na niliweka wembe ukiwa umefichwa kitandani mwangu kwa kusudi hilo. Walakini sikupata kamwe ujasiri wa kuutumia. Miaka ikapita polepole, na ikihuzunisha.

MWANZO WA TUMAINI

Katika Novemba 1960 wanawake wawili walinitembelea na wakasema juu ya Biblia. Muda mfupi nilirudi hospitali kwa miezi sita kwa matibabu. Katika Aprili 1961 mmoja wa wanawake hao akiwa na mwenzi tofauti alinitembelea. Kisha nikatambua kwamba walikuwa Mashahidi wa Yehova. Kutaka kujua kwangu kuliamshwa. Nilitaka kuyajua maoni yao juu ya dini mbalimbali.

Nilipokuwa nikikua nilikuwa nimekutana na dini za namna zote. Wazazi wangu walikuwa wa Orthodoksi ya Armenia, nilikuwa nimeishi kwa miaka 10 kati ya Wakatoliki wa Maroni na nilikuwa nimetumia likizo za wakati wa kiangazi na Waprotestanti. Nilikuwa hata nimepewa mtaala kwa njia ya barua wa Seventh-day Adventist, nikapewa shahada nao. Hata hivyo, ujapokuwa msingi huo, mimi sikujua jina la Mungu au namna ya kumwabudu.

Niliwauliza Mashahidi hao wanitembelee tena. Walinitembela na funzo la Biblia lilianzishwa katika kijitabu “Habari Njema Hizi za Ufalme.” Baada ya mafunzo matatu au manne peke yake nilikuwa nimejifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova na kwamba tunaishi katika siku za mwisho za hii taratibu ya mambo. Vilevile nikajifunza juu ya taratibu mpya ya Yehova na taraja la kuishi milele katika afya kamili! Jambo hilo lilivuta fikira zangu kweli kweli nami nikaanza kujifunza kwa tamaa nyingi.

Mashahidi hao waliniambia nitazamie mateso, pengine kutoka kwa watu wa nyumbani mwangu. Sisi sote tulikuwa tukiishi pamoja kwa mara nyingine katika kichumba kile kidogo. Hata hivyo, niliamua kwamba kama jamaa yangu ingenipinga, ingalikuwa afadhali niishi katika makao ya kutunzia wagonjwa (sanatorio) kuliko kuacha kweli za Biblia ambazo zilikuwa zimekuwa zenye thamani sana kwangu. Mlango wenye kuelekeza kwenye wakati ujao wenye furaha ulikuwa umefunguka nami nisingeruhusu mtu ye yote aufunge.

Furaha na kuthamini kwangu Yehova na watu wake kuliongezeka wakati niliporudishwa hospitali kwa miezi mingine sita, wakati huu ikiwa ni maili 25 (kilometre 40) nje ya Beirut. Je! rafiki zangu wapya wangeniacha? Hata kidogo! Shahidi mmoja na mkewe walisafiri kwa ukawaida kuja kujifunza nami.

Niliporudi nyumbani kutoka hospitali hiyo, Mashahidi wengi zaidi na zaidi, walipojua juu ya hali yangu, walikuwa wakipitia na kunitembelea, si wale tu wenye kuzungumza lugha ya Kiarmenia, bali pia wenye kuzungumza Kilebanoni. Kila mmoja alikuwa na neno la kufariji kweli kweli. Katika Septemba 8, 1962, kina ndugu walinisafirisha kwenye ufuo uliokuwa karibu, nami nilibatizwa katika bahari kuonyesha wakf wangu kwa Yehova Mungu.

FURAHA KATIKA UTUMISHI WA KIKRISTO

Kwa kuwa singeweza kuhudhuria mikutano ya kundi, Mashahidi hao walikuwa wakiniambia mambo yaliyokuwa yamezungumzwa. Walakini nilitaka kushiriki kikamilifu zaidi. Nilimwuliza ndugu yangu aninunulie tepu rekoda (kikamata sauti) naye akaninunulia. Baada ya hilo niliweza “kuhudhuria” mikutano yote na hata kutoa hotuba katika Shule ya Kitheokrasi kupitia sauti zilizonaswa (zilizokamatwa) kwenye tepu.

Walakini ningewezaje kushiriki katika utendaji wa kuhubiri? Nikiwa nimelazwa kitandani muda wote kufikia wakati huu, watu wa nyumbani mwangu walikuwa “eneo” linalofaa. Mahali pa kunitesa, mmoja baada ya mwingine walizikubali kweli za Biblia nilizowaambia​—kwanza, dada mchanga wangu, kisha ndugu mchanga wangu kabisa, halafu mama yangu na, mwishowe, dada yangu aliyeolewa. Yule ndugu yangu mwingine peke yake ndiye si Shahidi, ingawa mke wake ni Shahidi. Na mke wake, kwa upande wake, amewasaidia baadhi ya watu wake wa ukoo wawe Mashahidi, kutia ndugu yake ambaye sasa ni mzee Mkristo! Kwa hiyo eneo langu la kwanza lilikuwa na matokeo, na hiyo ikaniletea furaha nyingi sana.

Eneo jingine lilikuwa kati ya watu wachache wasio Mashahidi ambao wangali walikuwa wakinitembelea. Walakini nilihisi (niliona) kwamba lazima pawepo njia nyingine ya kutoa ushuhuda mkubwa zaidi. Kwa hiyo nikajipatia kitabu chenye namba za simu, na ndani yacho nikapata majina na anwani za watu wenye kuzungumza Kiarmenia ambao ningeweza kuwapa ujumbe wa Ufalme kupitia barua. Vilevile nilipeleka barua kwenye anwani za biashara na viwanda ambavyo nilihisi ingekuwa vigumu kwa Mashahidi wengine kufikia katika kuhubiri kwao. Nilitiwa moyo nishiriki katika utendaji wa kuhubiri wakati wote, au kazi ya upainia, kama inavyoitwa. Tangu wakati huo nimeweza kushiriki katika upainia msaidizi, mara tatu kwa mwaka kwa wastani.

BARAKA UJAPOKUWA UPINZANI

Magazeti ya kwetu ya Kiarmenia yalinisingizia mimi na jamaa yangu, kwa kudanganya yakasema kwamba mimi nilikuwa kiongozi wa Mashahidi Waarmenia na kwamba tulikuwa tukifanya mikutano ya kisiri ya kufanya mapinduzi. Vilevile, mjomba wangu, aliyekuwa jirani yetu, alitupinga vikali sana. Kwa hiyo tukaamua kutoka nyumba yetu ya chumba kimoja isiyolipiwa tukakodishe nyumba kubwa zaidi katika eneo jingine. Ingawa nyumba hiyo mpya ilikuwa yenye kugharimu sana na ikaleta matatizo ya kifedha, ilipata kuwa baraka kwetu sote.

Sasa tuna makao ya kuishi yenye starehe zaidi, na pia tuna mikutano ya kundi ya kawaida katika nyumba yetu. Nami naweza kushiriki kikamilifu zaidi katika utendaji wa kitheokrasi, na kuangalia madaraka yangu nikiwa mzee wa Kikristo. Ninatoa hotuba za watu wote, mimi mwangalizi wa Shule ya Kitheokrasi, ninaongoza funzo la kitabu mojawapo la kundi, na mwaka huu (1981) mimi ndimi mwangalizi msimamizi. Kwa hiyo upinzani umetokeza furaha na baraka tu.

Kwa kadiri sifa yangu mbaya ilivyoenea katika ujamii wote wa Waarmenia, viongozi wengi wa kidini wa dini mbalimbali walikuja kunitembelea ili “waninyoshe.” Nia na matendo yao yalinivuta tu karibu na watu wa Yehova. Ingawa mimi nilijibu maulizo yao yenye ushindani kwa utulivu, wao walikuwa wakikasirika na kupiga kelele, na kusema maoni yao hata karibu kufikia hatua ya kukufuru. Niliweza kuona tofauti tu kati yao na Mashahidi wanyenyekevu walioniletea kweli za Biblia.

FURAHA NILIYOIPATA KARIBUNI YAWA WAZI KWA WENGINE

Furaha yangu inakuwa ushuhuda kwa wengine, kutia madaktari ambao wamenitibu wakati wa miaka yote hiyo. Katika mwaka 1967 niliingia hospitali kwa mara nyingine kwa siku 12 ili nipewe matibabu, wakati huu ukiwa ni ugonjwa mwingine, usiohusiana na ule wa kwanza. Daktari wangu alikuwa mwenye urafiki sana naye aliona kwamba sikuzote nilikuwa mwenye furaha na mwenye maoni mazuri ujapokuwa udhaifu wangu. Akanieleza juu ya mgonjwa mwingine wake, mwanamume mwenye umri wa miaka 21 mwenye umizo la fundo la uti wa mgongo lililotokana na msiba wa motokaa. Ingawa alikuwa akitunzwa vizuri na kuangaliwa na wazazi wenye utajiri, alikuwa amevurugika akili sana na mwenye kudai mambo sana hata kwamba wazazi wake walikuwa wamechoshwa naye. Aliwavuruga sana wauguzi na watumishi.

“Lakini wewe hulalamiki kamwe,” ndivyo daktari huyo alivyosema. “Wauguzi wananiambia kwamba wewe hufinyi kengele yako ili utumikiwe na kwamba unaomba msaada wakati tu wanapoingia chumbani mwako. Hata uso wako unaonekana tofauti sana na wake.” Ndipo nilipomwambia daktari huyo juu ya sababu ya tofauti hiyo nami nikamweleza juu ya tumaini la kuishi milele katika dunia iliyo paradiso.

Siku moja katika Agosti 1975 Shahidi mmoja alileta mgeni mmoja aje kuniona. Kama kawaida, nilizungumza naye juu ya Ufalme na namna utakavyotatua matatizo yetu yote. Baada ya wakati fulani alisema hivi: “Nilikuwa nakuja kumwona mtu mgonjwa. Mimi ndiye niliyepaswa kumchangamsha. Walakini wewe ndiwe umenichangamsha!” Sikujua hata kidogo kwamba ndiye aliyekuwa mwandikaji na mhariri wa gazeti la kwetu. Juma iyo hiyo aliandika makala ndefu juu ya imani na ndani yake akatia kisa changu.

VITA HAVIKUNINYANG’ANYA FURAHA

Wakati wa vita ya wenyewe kwa wenyewe ya Walebanoni, iliyoanza mwaka 1975, tulielekeana na matatizo mapya. Nyumba yetu ya orofani ndiyo ya pili kutoka juu katika jengo refu sana. Raia waliozoezwa kijeshi wa mahali hapo walitwaa makao ya jeshi yaliyo karibu na nyumba yetu ya orofani, na kwa hiyo tulikuwa katika eneo ambalo risasi zilikuwa zikitupianwa mfululizo. Risasi nyingi zilianguka juu ya paa la jengo letu, walakini hakuna risasi moja lililoingia kupitia dari letu.

Wakati wa mfululizo wa mtupo wa risasi Wasiria katika vuli ya 1978 jirani zetu wote walikimbilia sehemu salama zaidi. Sisi tulibaki mahali tulipokuwa, jamaa yangu ikakataa kuniacha kwa kuwa nisingeweza kuhamishwa. Sisi sote tulihisi ulinzi wa Yehova wakati wa siku hizo chache zenye kuogopesha sana. Hata mpwa wangu mdogo wa kiume alizunguka-zunguka katika nyumba akirudia andiko la mwaka letu: “Mimi nipo pamoja nawe,” asema Yehova, “ili nikuokoe.” (Yer. 1:19) Alionekana kama kwamba anajituliza​—hakika alitutuliza sisi wenye umri mkubwa zaidi.

Ilionekana kama kwamba kweli kweli ulikuwa mwujiza kwa kuwa hakuna ye yote wetu aliyeumizwa. Risasi tatu kubwa zilianguka juu ya paa lililokuwa juu ya kitanda changu, mishindo kutoka kwa milipuko yazo ilivunja mamia ya madirisha katika eneo hilo. Mizinga inayoweza kutoboa kuta kadha wa kadha za saruji ilianguka juu ya paa lakini haikupenya ndani na kwa hiyo kukawa uharibifu mdogo tu. Upendo wa kunihangaikia wa jamaa yangu na Yehova kuwa karibu vilikuwa ni chanzo cha furaha hata katika siku hizo mbaya sana.

MATUNDA YA KUSTAHIMILI

Katika miaka 19 nikiwa Shahidi, nimeweza kuwasaidia watu 16 wawe watumishi waliojiweka wakf wa Yehova. Na kuna kadha ambao sasa ninajifunza nao wanaotazamia kubatizwa. Kati ya wale tayari wamekwisha kubatizwa wanne wanatumikia kama watumishi wa huduma kundini. Wanne kati yao ni wanafunzi wa chuo kikuu au wamekwisha kufuzu (kumaliza kisomo).

Mmoja (mwanamke) kati ya waliokuwa mafunzo yangu ya Biblia ni mwandishi wa habari za magazetini, mwandikaji wa vitabu na hapo mbele alikuwa profesa wa chuo kikuu na kwa miaka mingi amefanya kazi katika Wizara ya Habari. Akiwa huko wakati wote anakutana na wakuu wa kiserikali, kutia waziri mkuu. Kuthamini kwake kweli kulikuwa kwingi sana hata kwamba mara moja aliondoa mkutano mmoja aliokuwa nao pamoja na waziri mkuu na watu wengine wenye elimu ili nipate nafasi kwa ajili ya badiliko la ghafula katika orodha yangu ya mafunzo ya Biblia. Yeye pamoja na mwanafunzi mmoja wangu wa Biblia, ambaye hapo kwanza ndiye aliyesema naye juu ya ufalme wa Mungu, walibatizwa siku ile ile.

Wakati mwingi ninaongoza mafunzo ya Biblia kama saba kila mwezi licha ya kuangalia utendaji mwingine wangu wa kitheokrasi. Yote hayo yanasisimua hata kwamba sijisikii mgonjwa. Kiroho nimeponywa, nami najua kwamba karibuni nitaponywa kimwili pia. Nina uhakika kamili na ahadi ya Yehova kupitia nabii wake kwamba siku moja ‘nitaruka-ruka kama kulungu.’​—Isa. 35:6.

Kwa watu wote walioshuka moyo napendekeza watii maneno ya Yesu: “Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha. Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu; kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu.” (Mt. 11:28, 29) Kwangu, maneno hayo yamekuwa kweli, na kukosa kwangu tumaini kabisa kumekuwa furaha tupu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki