Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Biblia inasema: “Jifanyieni rafiki kwa mali ya udhalimu.” (Luka 16:9) Je! hii maana yake ni kwamba, maadam pesa au mali nyingine zinatumiwa kwa njia nzuri au kwa kuwafaidi wengine, si jambo la maana kwamba vitu hivyo vya kimwili vimepatikana kwa udanganyifu, kwa udhalimu?—U.S.A.
Maneno yaliyoko juu ya Yesu Kristo hayamaanishi kwamba Yehova Mungu hajali namna watu wanavyojipatia mali. Luka 16:9 hasemi, ‘Jifanyieni mali kwa njia za udanganyifu kisha mzitumie mali hizi kwa njia inayofaa kusudi mjifanyie rafiki.’ Si njia ya kuzipata, bali ni mali zinazosemwa kuwa ‘za udhalimu.’ Kwa sababu gani? Tofauti na mali za kiroho au tamaa ya mali za kiroho, kuwa na mali za kimwili au kuzitamani kunaweza, na mara nyingi kunaelekeza kwenye matendo ya uasi.
Alipokuwa akisema “jifanyieni rafiki,” Yesu Kristo hakuwa akizungumza juu ya kujipatia rafiki kati ya wanadamu. Aliongeza kwamba rafiki ambao aliwataja wangemkaribisha mtu katika “makao ya milele” “mali ya udhalimu” ikishindwa. Mali zinashindwa kuwasaidia wanadamu wote wakati wa kufa, na wanadamu wanaokufa hawawezi kumkaribisha ye yote katika “makao ya milele.” Lakini Mungu asiyekufa, Yehova, na Mwanawe asiyekufa, Bwana Yesu Kristo, wanaweza kuwakaribisha wengine katika “makao ya milele.” Yesu Kristo aliwahakikishia wanafunzi wake, akisema: “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali.”—Yohana 14:2.
Watakaoruhusiwa kuingia katika “makao ya milele” ya Yehova Mungu na Mwanawe ni wale wanaoyatimiza matakwa yake peke yao. Akasema Yesu: “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.” (Mt. 7:21) Mapenzi ya Mungu kwa wanadamu yanatia na kuendesha kwao maisha ya uaminifu na ya haki. Katika Neno lake twaambiwa kwamba “wenye pupa” wala “wadhalimu” hawataurithi ufalme wake. (1 Kor. 6:9, 10, NW) Vile vile twasoma: “Mwibaji asiibe tena; bali afadhali afanye juhudi, akitenda kazi iliyo nzuri kwa mikono yake mwenyewe, apate kuwa na kitu cha kumgawia mhitaji.” (Efe. 4:28) Kwa hiyo hakuna anayeendelea kujipatia mali kwa udanganyifu atakayekuwa rafiki ya Yehova Mungu na ya Mwanawe wala hatakaribishwa katika “makao ya milele.”
Uaminifu unatakiwa si kwa wale watakaotawala na Kristo katika ufalme wa kimbinguni peke yao lakini vile vile na kwa wale watakaokuwa raia zake waaminifu. Raia hao waaminifu wanafananishwa katika Maandiko kama waliovikwa “mavazi meupe,” yaani, wakiwa wanaoonekana safi na wanaokubalika mbele za Yehova Mungu. Kwa kuwa ni pendeleo lao kumtolea Mungu utumishi mtakatifu katika hekalu lake, lazima wayatimize matakwa ya kuwa mgeni katika hekalu hilo. (Ufu. 7:13-15) Akilijibu ulizo juu ya nani atakayekuwa mgeni katika mahali patakatifu pa Yehova, mtunga Zaburi aliyeongozwa na roho ya Mungu alitangaza: “Ni mtu aendaye kwa ukamilifu, na kutenda haki. Asemaye kweli kwa moyo wake. . . . Hakutwaa rushwa amwangamize asiye na hatia.”—Zab. 15:l-5.
Kwa hiyo jambo lililotiliwa mkazo na Yesu katika Luka 16:9 linaonekana kuwa uhitaji wa mtu kutumia mali za kimwili sawasawa, kwa hekima. Yeye anayetamani kibali cha kimungu amepaswa atumie mambo ya kimwili yaliyopatikana kwa uaminifu, si kwa makusudi ya kichoyo, bali, kwa kuiendeleza ibada safi na kwa kuwapa msaada wanadamu wenzake wenye shida.