Maswali Kutoka kwa Wasomaji
● Je! takwa lililoandikwa katika Kumbukumbu la Torati 23:2 linayahusuje matumaini ya watoto wa haramu ya kuwa watumishi waliokubaliwa wa Mungu?—U.S.A.
Amri iliyomo katika Kumbukumbu la Torati 23:2 ni sehemu ya sheria ya Musa. Inasema hivi: “Mwana wa haramu asiingie katika mkutano wa [Yehova]; hata kizazi cha kumi asiingie aliye wake katika mkutano wa [Yehova].”
Hii ilikuwa sheria yenye kusudi iliyozilinda haki za urithi za wana wa haramu na watoto wao. Pia ilizuia umalaya na kuvunjika kwa mpango wa jamaa. Bila shaka, sheria hii haikuonyesha hukumu ya milele juu ya watu hao. Kati ya wale watakaofufuliwa kutoka kwa wafu na kupewa nafasi ya kujifunza mapenzi ya kimungu katika taratibu mpya ya Mungu watakuwako watu waliokuwa wamezaliwa kama wana wa haramu.—Ufu. 20:13.
Leo Yehova Mungu hashughuliki na taifa moja tu la watu. Sheria ya Musa, pamoja na mpango wake wa kuzuia wana wa haramu wasiwe washiriki wa kundi la watu wake, haiwahusu Wakristo. (Kol. 2:13, 14) Kwa hiyo nafasi ya kuwa mmoja wa watumishi wa Mungu haikufungwa kwa ye yote. Kwa ufunuo wa kimungu mtume wa Kikristo Petro alijifunza kwamba ‘hakuna mtu anayepaswa kuitwa mchafu wala najisi’ kwa sababu ya taifa. (Matendo 10:28) Kwa hiyo, alipokuwa akiwahutubia watu wasio Wayahudi waukubali Ukristo, alisema hivi: “Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo; bali katika kila taifa mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Matendo 10:34, 35) Hii maana yake ni kwamba watu wote, hata watoto wa haramu, wanaweza kuwa watumishi waliokubaliwa wa Mungu, mradi wanaishi kupatana na mapenzi yake.