Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 3/15 kur. 142-144
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Habari Zinazolingana
  • Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Hatua Muhimu kwa Wapendao Neno la Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 3/15 kur. 142-144

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

● Maoni ya mashahidi wa Yehova ni nini juu ya kuhudhuria arusi ya mtu wa ulimwengu wanayemfahamu au mtu wa ukoo?

Kwa habari ya watoto wanaofikiria kuhudhuria, uamuzi wa mwisho utafanywa na wazazi. Au sivyo hilo ni jambo la kuamuliwa na mtu mwenyewe, na kila Mkristo apaswa kuwa na nia ya kujichukulia daraka lake mwenyewe. Walakini, ziko kanuni za Maandiko na hali mbalimbali zinazopaswa kufikiriwa.

Huenda sherehe ya arusi ikafanywa katika kanisa ikiongozwa na kiongozi wa dini. Hiyo ingefanya sherehe hiyo isiwe ya kiserikali kabisa. Mkristo wa kweli hawezi kujiunga wala kushiriki katika sala zo zote au mambo ya kidini anayojua yanatofautiana na mafundisho ya Biblia, kulingana na dhamiri. Wala hapendezwi kuona anaweza kukaribia namna gani kufanya matendo ya kuasi imani bila kuruka mipaka. Yampasa atii amri ya Maandiko: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? . . . Au yeye aaminiye ana sehemu gani pamoja na yeye asiyeamini? . . . Kwa hiyo, Tokeni kati yao, mkatengwe nao, asema [Yehova], msiguse kitu kilicho kichafu.”​—2 Kor. 6:14-17.

Inafahamika kwamba mtu anayekaribishwa ahudhurie arusi ya watu wa ukoo wa kilimwengu na ya wengine anaowafahamu huenda nyakati nyingine akapatwa na tatizo kweli kweli. Kwa mfano, huenda mke Mkristo akawa amekaribishwa pamoja na mumewe asiyeamini. Huenda mume akadhani kwamba wote wawili wanapaswa kuhudhuria arusi. Lakini huenda mke akawa na wasiwasi juu ya kufanya hivyo. Huenda akawaza kwamba, akihudhuria arusi kanisani, hali zitamkaza moyoni na akilini hata afanye jambo baya. Kwa upande mwingine, huenda akakata maneno kwamba, aweza kwenda na mumewe akatazame tu, kwa sababu ya kumheshimu, lakini bila kuwa na nia ya kushiriki katika matendo yo yote ya kidini.

Bila ya kujali vile mke anavyoweza kuona jambo hilo, atafaidika akieleza mumewe maoni yake. Mume akiamua kwamba mkewe akienda naye, kulingana na maelezo ya mke, huenda kukatokea jambo la kumchukiza mume, aweza kuamua kwenda peke yake. Au, huenda bado akataka mkewe aende naye, akatazame akiwa kimya, na hapo mke atapaswa kuamua kama atakwenda au hatakwenda.

Jambo linalopaswa kufikiriwa ni matokeo ambayo kuhudhuria arusi katika kanisa kunaweza kuwa nayo juu ya waamini wenzetu. Je! huenda kufanya hivyo kukaumiza dhamiri za wengine? Je! huenda kujizuia kwao wasiabudu sanamu kukadhoofishwa na tendo hilo lako? Kanuni ya Biblia inayohusika ni hii: “Hakikisheni mambo yaliyo ya maana zaidi, ili msiwe na kosa na msiwe mkikwaza wengine mpaka siku ya Kristo.”​—Flp. 1:10, NW; tazama pia 1 Wakorintho 8:9-13.

Nyakati nyingine huenda mtu akakaribishwa arusini akawe mmoja wa wale watakaomtumikia bibi-arusi. Namna gani ikiwa hiyo inahitaji mtu ashiriki katika matendo fulani ya kidini? Kwa wazi mtu anayetaka kumpendeza Mungu hawezi kushiriki katika matendo hayo ya dini ya uongo; lazima atende kupatana na Neno lake. Lakini Mkristo aweza kueleza maoni yake na kuonyesha kwamba hataki kuharibu furaha ya siku ya arusi kwa kuleta aibu.

Katika mambo ya namna hiyo, lazima Wakristo wafikirie kwa uangalifu mambo yote yanayohusika. Katika hali fulani huenda wakaamua kwamba matatizo hayatatokea wakihudhuria wakatazame kwa kimya. Kwa upande mwingine, huenda hali zikafanya Mkristo awaze kwamba ni afadhali kutohudhuria arusi hizo za kilimwengu kuliko kuumiza dhamiri yake au za wengine. Vyo vyote iwavyo, yampasa Mkristo ahakikishe kwamba uamuzi wake hautamzuia kuendelea kuwa na dhamiri njema mbele za Mungu na wanadamu.

● Katika Biblia, Kutoka 4:11 yasema: “Ni nani afanyaye mtu kuwa bubu au kiziwi, au mwenye kuona, au kuwa kipofu? Si mimi, [Yehova]?” Je! hiyo maana yake ni kwamba Mungu ndiye hufanya watu wawe mabubu na vipofu nyakati zote?​—U.S.A.

Sivyo, kwa sababu hilo lisingepatana na utu mzima wa Mungu. Biblia yatuambia: “Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.” (Yak. 1:13) Sikuzote matendo yake huwa na kusudi. Yeye haletei mtu mabaya wakati wo wote bila sababu nzuri. Yeye ndiye mpaji wa “kila kutoa kuliko kwema, na kila kitolewacho kilicho kamili.” (Yak. 1:17) “Kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.”​—Kum. 32:4.

Kupatana na hilo, twaona kwamba Adamu na Hawa, wanadamu wawili wa kwanza, walipoteza ukamilifu wao kwa kupenda kwao wenyewe, na hivyo wakapoteza uwezo wa kuzaa watoto wakamilifu. (Ayubu 14:4) Wazao wao walipooa, kutokamilika zaidi na zaidi kulianza kuonekana kati ya wanadamu kutia na kasoro za kimwili kama vile upofu na uziwi. Kwa sababu Yehova Mungu ameacha hayo yatukie, angeweza kujitaja kama ‘mwenye kufanya’ mtu kuwa bubu, kiziwi na kipofu. (Linganisha Warumi 8:20, 21.) Tena,yeye anafahamu kabisa kasoro hizo na anajua zinaletwa na nini.

Vilevile, Yehova Mungu hakukinga watu na madhara yenye kuhuzunisha yanayoupata mwili kwa sababu ya kutokutii. Sheria ya Mungu isiyobadilika yasema hivi: “Cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.” (Gal. 6:7) Hivyo huenda watoto wanaozaliwa kutokana na zinaa ya maharimu (ya ndugu na dada, mama na mwana, baba na binti, n.k.) wakawa na kasoro; huenda wakawa vipofu, viziwi na kuwa na kasoro nyingine nyingine. Watu wanaofanya uasherati huenda wakapata ugonjwa wa kisonono au kaswende na kuwafanya vipofu, viziwi au hata wenda-wazimu. Ndivyo inavyoweza kuwa kwa watoto wazaliwao na mwanamke mwenye mmojawapo wa magonjwa hayo.

Yehova Mungu aweza kupofusha watu, kuwafanya viziwi na mabubu kwa halisi, ikiwa jambo hilo litapatana na kusudi na njia zake. Zakaria, baba ya Yohana Mbatizaji, ni mfano wa hilo. Wakati Zakaria alipotia shaka alipoambiwa angepata mwana kupitia kwa mkewe mzee Elizabeti, malaika Gabrieli alimwambia hivi: “Tazama! utakuwa bubu, usiweze kusema, mpaka siku ile yatakapotukia hayo, kwa sababu hukuyasadiki maneno yangu; nayo yatatimizwa kwa wakati wake.” (Luka 1:20) Halafu Zakaria akafanywa bubu kwa muda, asiweze kusema mpaka mwana wake alipotahiriwa akiwa wa siku nane.​—Tazama Matendo 13:8-11 pia.

Njia nyingine ambavyo Mungu ‘hufanya’ mtu bubu, kiziwi na kipofu ni ya kiroho. Watu wakichagua kuwa viziwi na vipofu wasisikie wala kuona ujumbe wake, yeye huwaruhusu wakae katika hali yao ya kutoamini. Ndivyo ilivyokuwa kwa habari ya Israeli wasioaminika wakati wa Isaya nabii. Isaya aliambiwa hivi: “Enenda, ukawaambie watu hawa, Fulizeni kusikia, lakini msifahamu; fulizeni kutazama, lakini msione. Uunoneshe moyo wa watu hawa, ukayatie uzito masikio yao, ukayafumbe macho yao; wasije wakaona kwa macho yao, na kusikia kwa masikio yao, na kufahamu kwa mioyo yao, na kurejea na kuponywa.”​—Isa. 6:9, 10.

Kwa kuwa Yehova Mungu alijua hali ya moyoni ya Waisraeli wasioaminika, alitangulia kujua kwamba wangeupinga ujumbe wake. Kadiri ambavyo Isaya alizidi kuwaeleza neno la Yehova, ndivyo walivyozidi kujigumisha wasilisikie. Hivyo kutabiri kwa Isaya kulionyesha wazi wao walikuwa vipofu na viziwi wa kiroho kwa kadiri gani. Kutabiri kwake kuliwafanya waonekane kama kwamba walikuwa wamefanywa viziwi na vipofu wa kiroho.

Kwa hiyo, kwa sababu ya yale ambayo Yehova Mungu amefanya na anayoweza kufanya, Maandiko yanamtaja kama ‘akifanya’ watu kuwa mabubu, viziwi na vipofu. Lakini si yeye mwenyewe anayeleta kasoro hizo za kimwili nyakati zote. Hasa kasoro hizo za kimwili zimetokea kwa sababu Mungu ameruhusu taifa la kibinadamu lenye dhambi litokee. Nyakati chache na kwa makusudi ya pekee Yehova Mungu amefanya watu wakawa vipofu na mabubu; amefanya upofu na uziwi wa kiroho uonekane wazi katika wale wasioamini neno lake na ujumbe wake. Kwa upande mwingine, amewapa pia wale wanaotafuta kufanya mapenzi yake macho na masikio ya kiroho, naye atakomboa wanadamu na kasoro zote za kimwili kupitia kwa ufalme wake utakaosimamiwa na Kristo.​—Isa. 61:1, 2; Ufu. 21:3, 4.

● Kwa sababu gani Biblia ya New World, Translation haionyeshi, katika dibaji, majina na elimu ya walioitafsiri?

Miaka iliyopita, Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania imechapa tafsiri nyingi mbalimbali za Biblia. Tulipofanya hivyo hatukupuza matakwa ya watafsiri. Kwa mfano, mwaka 1972 tulichapa The Bible in Living English kwa namna na mwundo uliotakiwa na mtafsiri wake.​—Tazama ukurasa wenye maelezo juu ya mwandikaji.

Septemba 3, 1949, halmashauri iitwayo New World Bible Translation Committee ilitutolea tafsiri iliyomalizwa ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hati hiyo, pamoja na tafsiri yao ya Maandiko ya Kiebrania iliyofuata, ikawa mali yetu kwa halali. Kwa habari hiyo, ukurasa 258 wa kitabu Jehovah’s Witnesses in the Divine Purpose wasema: “Ombi moja lililofanywa na halmashauri ya kutafsiri ni kwamba washiriki wake wasitajwe majina hata baada ya kufa kwao.” Tumefuata mapatano yetu tukaheshimu matakwa yao.

Lakini kwa sababu gani mapatano hayo yalifanywa? Watafsiri hao hawakuwa wakijitafutia umashuhuri; hawakutaka kujiletea sifa. Wakiwa na roho ya ‘kufanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu,’ walitaka msomaji aamini akilitegemea Neno la Mungu, si “sifa” zao za kilimwengu. (1 Kor. 10:31) Halmashauri nyingine za kutafsiri zimefuata maoni kama hayo. Jalada ya Reference Edition (1971) ya New American Standard Bible yasema: “Hatukutumia jina la mwanafunzi ye yote tuwe tukimwona au awe akisifiwa, kwa sababu twaamini Neno la Mungu lapaswa kujitetea kwa sifa zake lenyewe.”

Sifa za New World Translation zinasomwa kwa vyepesi. Chapa zake zenye maandishi makubwa zina maelezo mengi sana ya chini. Mengi yanaonyesha ni hati zipi za Biblia zilizotumiwa ili kuamua vile mambo fulani yatakavyotafsiriwa. Nayo maelezo hayo ya chini, pamoja na Utangulizi mrefu, yanampasha mwenye kujifunza habari zaidi juu ya hati zilizotegemewa, na kazi ya halmashauri ya kutafsiri, kuliko anazoweza kupashwa na tafsiri nyingi.

Tena, mwaka 1969 tulichapa The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures, na hiyo pia ni kazi ya New World Bible Translation Committee. Kitabu hicho kilichotafsiriwa kutoka Kigiriki kuingia katika Kiingereza champa mtu ye yote nafasi ya kuchunguza sana jitihada za halmashauri iliyotafsiri sehemu hiyo ya Biblia.

Huenda wengine wakabishia hilo wakisema kwamba hata vitabu vyenyewe vya Biblia vina majina ya walioviandika. Ni kweli kwamba vingi vimeonyesha majina ya walioviandika. Lakini, vitabu kadha vya Biblia havikuonyesha majina ya waandikaji. Tena, twaona kwamba hawataji sifa zao wala elimu waliyokuwa nayo. Walipokuwa wakitafsiri Neno la Mungu, New World Translation Committee waliona kwamba, ingawa tafsiri yao inashuhudia yenyewe kwamba walistahili, jambo la maana si kama walifika chuo kikuu au kama walipata elimu nyinginezo. Msomaji anapochunguza sana tafsiri yao, yampasa aelekeze fikira zake kwa Mbuni wa Biblia, Yehova Mungu, si kwa watafsiri.

Vilevile, twaona kwamba halmashauri ilikuwa na unyenyekevu kwa sababu imekubali katika maelezo yao ya chini kwamba ziko njia nyingine zinazoweza kutumiwa kutafsiri vifungu. Kwa kufahamu hivyo, sikuzote tumetambua na kutia watu moyo watumie tafsiri mbalimbali za Biblia.a Hivyo, ingawa mashahidi wa Yehova wanashukuru sana New World Translation Committee kwa kazi yao, wanatumia Biblia zo zote zinazopatikana katika lugha zao. Sisi tunatia watu wote moyo watumie taa ya Neno la Mungu kumulika njia ya uzima, wawe wanatumia Biblia ya New World Translation yenye usemi mwepesi kufahamika, wa kisasa, au wawe wanatumia nyingineyo.​—Zab. 119:105.

● Je! Yesu Kristo anajua wakati “dhiki kubwa” itakapoanza?

Huenda akawa anajua, lakini hatuwezi kusema hakika kwamba anajua.

Yesu alitabiri “dhiki kubwa” itakayofutilia mbali uovu tunaouona kutuzunguka. Kwa habari ya wakati wa uharibifu huu, Yesu alisema hivi: “Habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake.”​—Mt. 24:3, 21 36-42.

Kwa hiyo, wakati Yesu Kristo alipokuwa duniani kama mfalme aliyekusudiwa na Mungu, hakuijua tarehe iliyowekwa ya kuanza kwa “dhiki kubwa.” Alikufa akafufuliwa na kupewa uzima wa kimbinguni katika mkono wa kuume wa Mungu, akingojea kupewa mamlaka kamili ya kutawala na ‘kuponda’ mataifa vipande vipande. (Zab. 110:1; 2:6-9) Utimizo wa unabii wa Biblia waonyesha kwamba alipokea mamlaka hiyo mwaka wa 1914 W.K.; “kuwapo” kwake kulianza wakati huo. Hivyo, kizazi chetu ndicho kitakachopatwa na “dhiki kubwa” hiyo. (Mt. 24:34; Ufu. 11:15-18) Yesu ajua hilo pia, kama vile anavyojua tuko mbali kadiri gani katika historia ya mwanadamu tangu kuumbwa kwa Adamu na Hawa.

Sasa Yesu anafanya nini? Ufunuo 6:1-8 waonyesha kwamba mwaka wa 1914 W.K. alitoka “ili akishinda tena apate kushinda [“amalize ushindi wake,” NW].” Vita vya mwanadamu, upungufu wa chakula na magonjwa ya kipuku yanahakikisha kwamba huu ndio wakati anapoelekea kumaliza ushindi wake.

Yesu ataongoza majeshi ya kimbinguni katika “dhiki kubwa.” Sasa tumekwisha ingia ndani kabisa katika kipindi kinachojulikana kama wakati wa mwisho, kwa hiyo pengine Mungu amekwisha julisha Yesu maarifa yote ya kutumiwa katika pigano na mpango wa majeshi yake. Lakini ikiwa Yesu hajajua bado “siku ile na saa ile” ya ‘kumaliza ushindi wake,’ karibuni ataijua.

[Maelezo ya Chini]

a Tazama Watchtower, 1950, uk. 315.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki