Je! 1 Yohana 5:7, 8 Inahakikisha Kuna Utatu?
KWA muda mrefu wanafunzi wa Biblia wametia shaka kama maneno fulani yanayopatikana katika 1 Yohana 5:7, 8 ni ya kweli. Lakini kwa kuwa yanapatikana katika Textus Receptus (“Maandiko Yaliyopokewa”), yanapatikana katika tafsiri ya King James, Douay na tafsiri nyinginezo. Walakini, ushuhuda ulipozidi kuhakikisha maneno hayo ni ya uongo, inaelekea wenye kuamini Utatu walikawia kuyaondoa katika tafsiri za Biblia.
Kwa mfano, mwanafunzi wa Biblia ambaye ni Mkatoliki mashuhuri wa Uingereza, Monsignor Knox, aliandika maelezo ya chini katika tafsiri yake (1944) akasema: “Mstari huu haupatikani katika hati yo yote nzuri ya Kigiriki. Lakini pengine tafsiri za Kirumi zilihifadhi andiko la kweli.” Na katika andiko lake halisi, tafsiri Confraternity ya Kikatoliki (1941) yasema hivi: “Kwa sababu wako watatu wanaotoa ushuhuda mbinguni: Baba, Neno, na Roho Mtakatifu; na hawa watatu ni mmoja. Na wako watatu wanaotoa ushuhuda duniani: Roho, na maji, na damu; na hawa watatu ni mmoja.” Katika maelezo ya chini, tafsiri hiyo inasema hivi: “Kulingana na ushuhuda wa hati nyingi, na kulingana na wanafunzi wengi mistari hiyo inapaswa kusema hivi: ‘Na wako watatu ambao wanatoa ushuhuda, Roho, na maji, na damu; na hivi vitatu ni kimoja.’ “Hata hivyo, maelezo ya chini yanaendelea kusema hivi: “Baraza ya Papa inajipatia haki ya kuamua vile andiko hili la sasa lilivyokuwa hapo mwanzo.”
A Catholic Commentary on Holy Scriptures (1953) kinajitanguliza jinsi Baba, Neno (Yesu) na Roho Mtakatifu wanavyotoa wote ushuhuda kwamba Kristo ni Mungu. Halafu, kinapoeleza maneno “na hawa watatu ni mmoja,” kitabu hicho kinasema kwamba “wana hali moja inayolingana.” Lakini, ndipo kinapotaja ukurasa mwingine (ambao pengine wasomaji wengi hawatataka kuutazama.) Katika ukurasa huo mtu anaona ikikubaliwa kwamba siku hizi kifungu hicho huchukuliwa kwa kawaida kama kosa lililoingizwa katika hati za tafsiri ziitwazo Old Latin, Vulgate na Greek. Kwa kuwa ndivyo, kuna faida gani ya kueleza ilivyokuwa?
Maelezo ya chini yanayopatikana katika The Jerusalem Bible (1966) yako tofauti, nayo hayana maneno yaliyoongezwa katika andiko halisi. Yanasema hivi: “Vulg[ate] mist. 7-8 yasema ifuatavyo ‘Wako mashahidi watatu mbinguni: Baba Neno na Roho, na hawa watatu ni mmoja; wako mashahidi watatu juu ya dunia: Roho maji na damu’. Maneno hayo ya kulala (yasiyopatikana katika hati yo yote ya zamani ya Kigiriki, au katika tafsiri yo yote ya kwanza, au katika hati iliyo nzuri zaidi ya tafsiri Vulg. yenyewe) huenda yakawa ni kosa lililoingizwa katika andiko hilo.”
Jambo la maana ni kwamba, maneno hayo ya uongo hayapatikani katika tafsiri ya karibuni zaidi ya Kikatoliki katika Kiingereza, yaani, The New American Bible. Lakini, je! yaliingiaje katika hati za Biblia? Inaelekea kwamba, mtu mmoja mwenye kunakili alikuwa na shauku ya kupita kiasi akayatia maneno hayo kwa makusudi ili aunge mkono fundisho la Utatu. Lakini, hakuna jambo lenye kuhakikisha fundisho hilo la uongo hapa wala mahali penginepo katika Maandiko Matakatifu.