Mafunzo Juu ya Maandiko Yenye Pumzi ya Mungu na Habari ya Msingi Yayo
Funzo Namba 6—Maandishi-awali ya Kigiriki ya Kikristo ya Maandiko Matakatifu
Kunakiliwa kwa maandishi-awali ya Maandiko ya Kigiriki; upokezaji wayo katika Kigiriki na lugha nyinginezo mpaka leo hii; kutegemeka kwa maandishi-awali ya kisasa.
1. Programu ya kielimu ya Kikristo ilianzaje?
WAKRISTO wa mapema walikuwa waelimishaji na watangazaji wa ‘neno la Yehova’ lililoandikwa ulimwenguni pote. Walichukua kwa uzito maneno ya Yesu kabla tu hajapaa: “Nyinyi mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu nyinyi, na nyinyi mtakuwa mashahidi wangu mimi katika Samaria na kwenye sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Isa. 40:8; Mdo. 1:8, NW) Kama alivyokuwa ametabiri Yesu, wanafunzi 120 wa kwanza walipokea roho takatifu, pamoja na kani yayo yenye kutia nguvu. Hiyo ilikuwa mnamo siku ya Pentekoste ya 33 W.K. Siku iyo hiyo, Petro aliongoza programu mpya ya kielimu kwa kutoa ushahidi kamili, tokeo likawa kwamba wengi wakakubali kwa moyo ujumbe huo na karibu 3,000 zaidi wakaongezwa kwenye kundi la Kikristo lililoanzishwa karibuni.—Mdo. 2:14-42.
2. Ni habari njema gani ambayo sasa ilitangazwa, na kazi hiyo ya kutoa ushahidi ilikuwa wonyesho wa nini?
2 Kwa kuchochewa kwenye tendo kupita kikundi chochote kinginecho katika historia yote, wanafunzi hao wa Yesu Kristo walianzisha programu ya ufundishaji ambayo hatimaye ilifurika kwenye kila pembe ya ulimwengu uliojulikana wakati huo. (Kol. 1:23) Ndiyo, mashahidi hao waliojitoa wa Yehova walikuwa na shauku ya kutumia nyayo zao, wakitembea nyumba kwa nyumba, jiji kwa jiji, na nchi kwa nchi, wakijulisha rasmi “habari njema za mambo mema.” (Rum. 10:15, NW) Habari njema hizo zilieleza juu ya uandalizi wa dhabihu wa Kristo, tumaini la ufufuo, na Ufalme wa Mungu ulioahidiwa. (1 Kor. 15:1-3, 20-22, 50; Yak. 2:5) Ushahidi kama huo unaohusu mambo yasiyoonekana haukuwa umepata kamwe kutolewa ainabinadamu. Ukapata kuwa “wonyesho dhahiri wa mambo hakika ijapokuwa hayaonwi,” wonyesho wa imani, kwa wengi ambao sasa walikubali Yehova kuwa Bwana Mwenye Enzi Kuu wao kwa msingi wa dhabihu ya Yesu.—Ebr. 11:1, NW; Mdo. 4:24; 1 Tim. 1:14-17.
3. Ni kitambulisho gani walichokuwa nacho wahudumu Wakristo wa karne ya kwanza W.K.?
3 Wahudumu hao Wakristo, wanaume na wanawake, walikuwa wahudumu wa Mungu walioelimishwa. Wao wangeweza kusoma na kuandika. Walikuwa wameelimishwa katika Maandiko Matakatifu. Wao walikuwa watu wanaojua juu ya matukio ya ulimwengu. Walikuwa wamezoea kusafiri. Walikuwa kama nzige kwa kuwa hawakuruhusu kizuizi chochote kizuie mwendo wao wa mbele katika kueneza habari njema. (Mdo. 2:7-11, 41; Yoe. 2:7-11, 25) Katika karne hiyo ya kwanza ya Wakati wa Kawaida, walifanya kazi miongoni mwa watu ambao kwa njia nyingi walifanana sana na watu katika nyakati za ki-siku-hizi.
4. Chini ya upulizio wa na uongozi wa Yehova, ni uandishi gani uliofanywa katika siku za mapema za kundi la Kikristo?
4 Wakiwa wahubiri wa “neno la uzima” wenye maendeleo, Wakristo wa mapema walitumia vizuri hati-kunjo za Biblia zozote ambazo wangeweza kupata. (Flp. 2:15, 16; 2 Tim. 4:13) Wanne kati yao, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana, walipuliziwa na Yehova waandike “habari njema juu ya Yesu Kristo.” (Mk. 1:1, NW; Mt. 1:1) Baadhi yao, kama vile Petro, Paulo, Yohana, Yakobo, na Yuda, waliandika barua chini ya upulizio wa Mungu. (2 Pet. 3:15, 16) Wengine walikuwa wanakiliji wa mawasiliano hayo yaliyopuliziwa na Mungu, ambayo yalibadilishanwa kwa mafaa miongoni mwa makundi yenye kuongezeka. (Kol. 4:16) Zaidi ya hayo, “mitume na wazee walioko Yerusalemu” walifanya maamuzi ya kimafundisho chini ya mwelekezo wa roho ya Mungu, nayo yaliandikwa kwa ajili ya matumizi ya baadaye. Pia, baraza linaloongoza hilo lililokuwa mahali pamoja lilipeleka barua za maagizo kwa makundi yaliyokuwa sehemu za mbali. (Mdo. 5:29-32; 15:2, 6, 22-29; 16:4) Na kuhusu hilo, wao walilazimika kujifanyia utumishi wao wenyewe wa kupeleka barua.
5. (a) Kodeksi ni nini? (b) Wakristo wa mapema walitumia kodeksi kwa kadiri gani, na faida zayo zilikuwa nini?
5 Kwa kusudi la kuharakisha ugawanyaji wa Maandiko, na pia ili kuyatokeza kwa namna inayofaa kurejezea, Wakristo wa mapema upesi wakaanza kutumia hati ya namna ya kodeksi badala ya hati-kunjo. Kodeksi ina umbo linalofanana na kitabu cha kisasa, ina kurasa zinazoweza kugeuzwa kwa urahisi katika kutafuta mrejezo, badala ya kukunjua kwingi kulikotakwa kwa habari ya hati-kunjo. Zaidi ya hayo, umbo la kodeksi liliwezesha kuweka maandishi yanayokubaliwa pamoja kwenye jalada, ambapo kwa kawaida yale yaliyokuwa na umbo la hati-kunjo yalitunzwa katika makunjo tofauti-tofauti. Wakristo wa mapema walikuwa wa kwanza katika matumizi ya kodeksi. Hata yawezekana waliivumbua. Ingawa kodeksi ilitumiwa polepole na waandishi wasio Wakristo, mafunjo yaliyo mengi sana ya Kikristo ya karne ya pili na ya tatu yana umbo la kodeksi.a
6. (a) Kipindi cha Kigiriki cha maandishi yaliyo bora sana kilikuwa wakati gani, kilitia nini ndani, na Kigiriki cha Koine, au cha kawaida, kilisitawi wakati gani? (b) Ni jinsi gani na kwa kadiri gani Koine ikaja kutumiwa kijumla?
6 Matumizi ya Koine (Kigiriki cha Kawaida). Kile kiitwacho kipindi cha maandishi bora sana ya lugha ya Kigiriki kilianza tangu karne ya tisa K.W.K. mpaka karne ya nne K.W.K. Hicho kilikuwa kipindi cha lahaja za Kiati na Kioni. Ilikuwa katika wakati huo, na hasa katika karne ya tano na nne K.W.K., kwamba Wagiriki wengi walio wanamichezo ya kuigiza, watunga mashairi, wasemaji, wanahistoria, wanafalsafa, na wanasayansi walisitawi, kati yao Homer, Herodotus, Socrates, Plato, na wengine wakaja kujulikana sana. Kipindi cha kuanzia karibu na karne ya nne K.W.K. mpaka karibu karne ya sita W.K. kilikuwa muhula wa ile iitwayo Koine, au Kigiriki cha kawaida. Ukuzi wacho ulikuwa hasa kwa ajili ya shughuli kubwa za kijeshi za Aleksanda Mkuu, ambaye jeshi lake lilifanyizwa na askari kutoka sehemu zote za Ugiriki. Wao walisema lahaja tofauti-tofauti za Kigiriki, nao walipochangamana, lahaja moja, Koine, ilisitawi na ikaja kutumiwa kijumla. Ushindi wa Aleksanda juu ya Misri, na juu ya Asia kufikia kule mbali India, ulieneza Koine miongoni mwa watu wengi, hivi kwamba ikawa lugha ya kimataifa na ikaendelea hivyo kwa karne nyingi. Msamiati wa Kigiriki wa Septuagint ulikuwa Koine ya wakati huo ya Aleksandria, Misri, wakati wa karne ya tatu na ya pili K.W.K.
7. (a) Biblia yashuhudiaje matumizi ya Koine wakati wa Yesu na mitume wake? (b) Ni kwa nini Koine ilifaa sana kwa kuwasilisha Neno la Mungu?
7 Katika siku za Yesu na mitume wake, Koine ilikuwa lugha ya kimataifa ya milki ya Kirumi. Biblia yenyewe hushuhudia uhakika huo. Yesu alipogongomelewa juu ya mti, ilikuwa lazima maandishi juu ya kichwa chake yabandikwe si katika Kiebrania peke yake, kilichokuwa lugha ya Wayahudi, bali pia katika Kilatini, lugha rasmi ya bara, na katika Kigiriki, kilichonenwa kila mahali katika Yerusalemu karibu kama vile katika Rumi, Aleksandria, au Athene kwenyewe. (Yn. 19:19, 20; Mdo. 6:1) Matendo 9:29 huonyesha kwamba Paulo alihubiri habari njema katika Yerusalemu kwa Wayahudi walionena lugha ya Kigiriki. Kufikia wakati huo Koine ilikuwa ulimi wenye kutenda, ulio hai, uliositawishwa vizuri—lugha iliyojulikana na kufaa kusudi lililokwezwa la Yehova katika kuwasilisha zaidi Neno la kimungu.
MAANDISHI-AWALI YA KIGIRIKI NA KUPOKEZWA KWAYO
8. Ni kwa nini sasa twachunguza akiba ya hati za Andiko la Kigiriki?
8 Katika funzo lililotangulia, tulijifunza kwamba Yehova alihifadhi maji yake ya ukweli katika akiba ya hati zilizoandikwa—Maandiko ya Kiebrania yaliyopuliziwa na Mungu. Hata hivyo, vipi juu ya Maandiko yaliyopokezwa na mitume na wanafunzi wengine wa Yesu Kristo? Je! hayo yamehifadhiwa kwa ajili yetu kwa uangalifu kama huo? Uchunguzi wa akiba kubwa ya hati zilizohifadhiwa katika Kigiriki, na pia katika lugha nyingine, waonyesha ndivyo. Kama ilivyokwisha tolewa kielezi, sehemu hii ya vitabu vinavyokubalika vya Biblia ina jumla ya vitabu 27. Fikiria njia za upokezaji wa maandishi-awali ya vitabu hivi 27, zinazoonyesha jinsi maandishi-awali ya awali ya Kigiriki yamehifadhiwa kufikia wakati wetu wa kisasa.
9. (a) Maandiko ya Kikristo yaliandikwa katika lugha gani? (b) Twaona tofauti gani kwa Mathayo?
9 Akiba ya Hati za Kigiriki. Vile vitabu 27 vya Maandiko ya Kikristo yanayokubalika viliandikwa katika Kigiriki cha kawaida cha siku hiyo. Hata hivyo, kitabu cha Mathayo kwa wazi kiliandikwa kwanza katika Kiebrania cha Kibiblia, ili kutumikia watu wa Kiyahudi. Mtafsiri wa Biblia wa karne ya nne Jerome aeleza hilo, akisema kwamba baadaye kilitafsiriwa katika Kigiriki.b Mathayo mwenyewe yawezekana ndiye aliyefanya tafsiri hiyo—akiwa alikuwa amekuwa mfanya kazi wa serikali wa Rumi, mtoza ushuru, bila shaka yeye alijua Kiebrania, Kilatini, na Kigiriki.—Mk. 2:14-17.
10. Maandishi ya Biblia yametufikiaje sisi?
10 Wale waandikaji wengine wa Biblia Wakristo, Marko, Luka, Yohana, Paulo, Petro, Yakobo, na Yuda, wote waliandika hati zao katika Koine, lugha ya kawaida, iliyo hai ambayo Wakristo na watu wengine walio wengi wa karne ya kwanza walielewa. Ya mwisho ya hati za awali iliandikwa na Yohana karibu 98 W.K. Kwa kadiri ijulikanayo, hakuna yoyote ya hati hizo 27 za awali katika Koine imeokoka mpaka leo hii. Hata hivyo, kutokana na akiba hiyo ya awali, zimetiririka kwetu nakala za zile za awali, nakala za nakala, na familia za nakala, ili kufanyiza akiba kubwa ya hati za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
11. (a) Ni hazina gani ya nakala za hati inayopatikana leo? (b) Hizo zatofautianaje na vitabu vya maandishi yaliyo bora sana kwa habari ya wingi na umri?
11 Akiba ya Hati Zaidi ya 13,000. Hazina kubwa ya nakala za hati za vitabu vyote 27 vinavyokubalika yapatikana leo. Baadhi yazo zina visehemu vikubwa vya Andiko; nyingine ni vipande tu. Kwa kulingana na hesabu moja, kuna hati zaidi ya 5,000 katika Kigiriki cha awali. Kuongezea hizo, kuna hati zaidi ya 8,000 katika lugha nyingine mbalimbali—hati zote kwa jumla zinazidi 13,000 zikiwa pamoja. Zikiwa za tarehe ya kuanzia karne ya 2 W.K. mpaka karne ya 16 W.K., zote zasaidia katika kujua maandishi-awali ya kweli. Ya kale zaidi ya hati hizo nyingi ni kipande cha mafunjo ya Gospeli ya Yohana katika Maktaba ya John Rylands katika Manchester, Uingereza, inayojulikana kwa namba P52, ambayo ina tarehe ya nusu ya kwanza ya karne ya pili, yawezekana karibu 125 W.K.c Hivyo, nakala hiyo iliandikwa robo karne tu au hivyo baada ya ile ya awali. Tunapofikiria kwamba ili kupata kujua maandishi-awali ya watunzi walio wengi wa maandishi yaliyo bora sana, ni hati chache tu zilizopo, na ni mara chache hizi huwa za muda wa karne za yale maandishi ya awali, twaweza kuthamini jinsi kulivyo na uthibitisho tele wa kusaidia kujua maandishi-awali yenye amri ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
12. Hati za kwanza ziliandikwa juu ya nini?
12 Hati za Mafunjo. Kama vile nakala za mapema za Septuagint, hati za kwanza za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ziliandikwa penye mafunjo, nayo yaliendelea kutumiwa kwa hati za Biblia mpaka karibu na karne ya nne W.K. Waandikaji wa Biblia pia yaelekea walitumia mafunjo walipopeleka barua kwa makundi ya Kikristo.
13. Ni ugunduzi gani wenye maana wa mafunjo uliojulishwa umma katika mwaka 1931?
13 Hesabu kubwa za maandishi ya mafunjo zimepatikana katika mkoa wa Faiyūm, katika Misri. Katika mwisho-mwisho wa karne ya 19, hesabu fulani ya mafunjo ya Kibiblia ilipatikana. Ugunduzi mmoja wa hati wenye maana sana wa ki-siku-hizi ulijulishwa umma katika 1931. Ulikuwa wa sehemu 11 za kodeksi, zenye visehemu 8 vya vitabu tofauti-tofauti vya Maandiko Matakatifu ya Kiebrania yaliyopuliziwa na Mungu na vitabu 15 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, vyote vikiwa katika Kigiriki. Mafunjo hayo yana tarehe tofauti-tofauti za kuandikwa tangu karne ya pili mpaka karne ya nne ya Wakati wa Kawaida. Vingi vya visehemu vya Andiko la Kigiriki la Kikristo vya ugunduzi huo sasa vimo katika Mkusanyo wa Chester Beatty na vimeorodheshwa kuwa P45, P46, na P47, mfano “P” ukisimamia “Papyrus” (Funjo).
14, 15. (a) Ni zipi baadhi ya hati za mafunjo zenye kutokeza za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilizoorodheshwa katika jedwali katika ukurasa 313? (b) Onyesha jinsi New World Translation imetumia hati hizo. (c) Kodeksi za mafunjo za mapema zathibitisha nini?
14 Mafunjo ya mkusanyo mwingine wenye kutokeza yalitangazwa katika Geneva, Switzerland, kuanzia 1956 mpaka 1961. Yakiwa yanajulikana kuwa Mafunjo ya Bodmer, yanatia ndani maandishi-awali ya mapema ya Gospeli mbili (P66 na P75) ya tarehe ya kuanzia mapema karne ya tatu W.K. Jedwali inayotangulia funzo hili yaorodhesha baadhi ya mafunjo ya Biblia ya kale yenye kutokeza ya Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki ya Kikristo. Katika safu ya mwisho, kumetajwa vifungu katika New World Translation of the Holy Scriptures ambavyo hati hizo za mafunjo huunga mkono tafsiri iliyofanywa, na hilo laonyeshwa katika vielezi-chini vya mistari hiyo.
15 Magunduzi ya mafunjo hayo hutoa uthibitisho kwamba vitabu vinavyokubalika vya Biblia vilikamilishwa kwenye tarehe ya mapema sana. Miongoni mwa Mafunjo ya Chester Beatty, kodeksi mbili—moja ikitia katika jalada moja sehemu-sehemu za zile Gospeli nne na Matendo (P45) na nyingine ikitia katika majalada yayo 9 kati ya barua 14 za Paulo (P46)—huonyesha kwamba Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yaliyopuliziwa na Mungu yalikusanywa muda mfupi baada ya kifo cha mitume. Kwa kuwa ingelichukua wakati kwa kodeksi hizo kutawanywa sana na kufika Misri, ni wazi kwamba, kwa kuchelewa zaidi, Maandiko hayo yalikuwa yamekwisha kusanywa katika umbo layo ya kawaida kufikia karne ya pili. Kwa hiyo, kufikia mwisho wa karne ya pili, hakukuwako shaka kwamba vitabu vinavyokubalika vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo vilikuwa vimemalizwa, vikikamilisha vitabu vinavyokubalika vya Biblia nzima.
16. (a) Ni hati zipi za uncial za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zimeokoka mpaka leo hii? (b) Hati za uncial zimetumiwa kwa kadiri gani katika New World Translation, na kwa nini?
16 Hati za Mchapo na Ngozi. Kama tulivyojifunza katika funzo lililotangulia, mchapo wenye kudumu sana, ngozi ya hali ya juu ambayo kwa ujumla ilifanyizwa kwa ngozi ya ndama, ya mwana-kondoo, au ya mbuzi, ulianza kutumiwa badala ya mafunjo katika kuandika hati kuanzia karibu na karne ya nne W.K. na kuendelea. Hati fulani zenye maana sana za Biblia zilizopo leo zimeandikwa juu ya mchapo. Tayari tumekwisha zungumza juu ya hati za mchapo na ngozi za Maandiko ya Kiebrania. Jedwali iliyomo kwenye ukurasa 314 yaorodhesha baadhi ya hati za mchapo na ngozi zenye kutokeza za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na pia Maandiko ya Kiebrania. Zile zilizoorodheshwa za Maandiko ya Kigiriki ziliandikwa kwa ujumla kwa herufi kubwa na hurejezewa kuwa uncial. New Bible Dictionary huripoti hati za uncial 274 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, nazo ni za tarehe ya kuanzia karne ya nne W.K. mpaka karne ya kumi W.K. Kisha kuna hati 5,000 za mwandiko-mviringo, au minuscule, zilizofanyizwa kwa mwandiko wenye kushikamana.d Hizo, pia zikiwa penye mchapo, ziliandikwa wakati wa kipindi cha kuanzia karne ya tisa W.K. mpaka kuanzishwa kwa uchapaji. Kwa sababu ya tarehe yazo ya mapema na usahihi kwa ujumla, hati za uncial zilitumiwa sana na Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya New World katika kutafsiri kwa uangalifu kutoka maandishi-awali ya Kigiriki. Hilo laonyeshwa katika jedwali “Baadhi ya Hati Zenye Kutokeza za Mchapo na Ngozi.”
KIPINDI CHA UCHAMBUZI NA UCHUJAJI WA MAANDISHI-AWALI
17. (a) Ni matukio gani mawili yaliongoza kwenye uchunguzi ulioongezwa wa maandishi-awali ya Kigiriki ya Biblia? (b) Erasmo ajulikana kwa ajili ya kazi gani? (c) Maandishi-awali yaliyosahihishwa yaliyochapwa hufanyizwaje?
17 Maandishi-awali ya Erasmo. Katika karne zote nyingi za Enzi za Giza, wakati lugha ya Kilatini ilitawala na Ulaya ya Magharibi ikiwa chini ya utawala kamili wa Kanisa Roma Katoliki, usomi na elimu vilikuwa vimeshuka sana. Hata hivyo, ulipotukia uvumbuzi wa Ulaya wa uchapaji kwa mashine katika karne ya 15 na Mrekebisho wa dini wa mapema karne ya 16, uhuru zaidi ulikuwapo, na kulikuwako mtokezo mpya wa upendezi katika lugha ya Kigiriki. Ilikuwa wakati wa kuhuishwa huku kwa mapema kwa elimu kwamba msomi Mholanzi ajulikanaye sana, Desiderio Erasmo, akatokeza chapa yake ya kwanza ya maandishi-awali ya Kigiriki yaliyosahihishwa ya “Agano Jipya.” (Maandishi-awali hayo yaliyosahihishwa ambayo yamechapishwa yalitayarishwa kwa kulinganisha kwa uangalifu hati kadhaa na kutumia maneno ambayo kwa ujumla hukubaliwa kuwa ya awali, mara nyingi ikitia ndani, mpangilio ulio chini, maandishi juu ya kusomeka tofauti-tofuati katika hati fulani.) Hariri hiyo ya kwanza ilichapishwa katika Basel, Switzerland, katika 1516, mwaka mmoja kabla ya Mrekebisho wa Dini kuanza katika Ujerumani. Hariri ya kwanza ilikuwa na makosa mengi, lakini maandishi-awali yaliyosahihishwa yalitokezwa katika hariri zilizofuata katika 1519, 1522, 1527, na 1535. Erasmo alikuwa na hati chache tu za baadaye za maandishi-mviringo za kutumia kukusanya na kutayarisha maandishi-awali yake yaliyosahihishwa.
18. Maandishi-awali ya Erasmo yaliwezesha nini, na ni nani aliyeyatumia vizuri?
18 Maandishi-awali ya Erasmo ya Kigiriki yaliyochujwa yalikuja kuwa msingi wa tafsiri bora zaidi katika lugha kadhaa za Ulaya ya Magharibi. Hilo liliwezesha kutokezwa kwa tafsiri bora zaidi ya zile zilizokuwa zimekwisha tafsiriwa hapo awali kutokana na Vulgate ya Kilatini. Wa kwanza kutumia maandishi-awali ya Erasmo alikuwa ni Martin Lutheri wa Ujerumani, aliyekamilisha tafsiri yake ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kijerumani katika 1522. Akikabili mnyanyaso mwingi, William Tyndale wa Uingereza alifuatisha tafsiri yake ya Kiingereza kutokana na maandishi-awali ya Erasmo, akayakamilisha alipokuwa yungali uhamishoni katika kontinenti ya Ulaya katika 1525. Antonio Brucioli wa Italia alitafsiri maandishi-awali ya Erasmo katika Kiitalia katika 1530. Kuja kwa maandishi-awali ya Kigiriki ya Erasmo, kulifungua sasa kipindi cha uchambuzi wa maandishi-awali. Uchambuzi wa maandishi-awali ndiyo njia inayotumiwa ya kuandika na kurudisha mahali payo tena maandishi-awali ya Biblia.
19. Ni nini historia ya mgawanyo wa Biblia katika sura na mistari, na hilo limewezesha nini?
19 Mgawanyo katika Sura na Mistari. Robert Estienne, au Stefano, alikuwa maarufu kama mpiga chapa na mhariri katika karne ya 16 katika Paris. Akiwa mhariri, yeye aliona mafaa yenye kutumika ya kutumia mfumo wa sura na mistari kwa ajili ya mrejezo wa mara moja, na kwa hiyo akaanzisha mfumo huo katika Agano Jipya lake la Kigiriki-Kilatini katika 1551. Migawanyo ya mistari ilifanywa kwa mara ya kwanza kwa Maandiko ya Kiebrania na Wamasora, lakini Biblia ya Kifaransa ya Stefano ya 1553 ndiyo iliyoonyesha kwanza migawanyo ya sasa ya Biblia kamili. Hiyo ilifuatwa katika Biblia za lugha ya Kiingereza zilizofuata na ikawezesha kutokezwa kwa konkodansi za Biblia kama ile iliyoandikwa na Aleksanda Cruden katika 1737 na konkodansi mbili zenye habari zote za Tafsiri ya Biblia ya Authorized ya Kiingereza—ya Robert Young, iliyotangazwa mara ya kwanza katika Edinburgh katika 1873, na ya James Strong, iliyotangazwa katika New York 1894.
20. Textus Receptus ilikuwa nini, nayo ikaja kuwa msingi wa nini?
20 Textus Receptus. Vilevile Stefano alitokeza hariri kadhaa za “Agano Jipya” la Kigiriki. Hizo hasa zilitegemea maandishi-awali ya Erasmo, zikiwa na masahihisho yenye kulingana na Complutensian Polyglott ya 1522 na hati 15 za mwandiko-mviringo za baadaye za karne chache za awali. Hariri ya tatu ya Stephanus ya maandishi-awali ya Kigiriki katika 1550 ikaja kuwa Textus Receptus (Neno la Kilatini kwa “maandishi-awali yaliyopokewa”) ambayo ilitegemeza tafsiri nyinginezo za Kiingereza za karne ya 16 na King James Version ya 1611.
21. Ni maandishi-awali gani yaliyochujwa yametokezwa tangu karne ya 18, nayo yametumiwaje?
21 Maandishi-awali ya Kigiriki Yaliyochujwa. Baadaye, wasomi wa Kigiriki walitokeza maandishi-awali yaliyochujwa zaidi na zaidi. Yenye kutokeza yalikuwa yale yaliyotokezwa na J. J. Griesbach, ambaye aliweza kuchunguza mamia ya hati za Kigiriki zilizokuwa zimekuja kuwapo kuelekea mwishoni mwa karne ya 18. Hariri bora zaidi ya maandishi-awali kamili ya Kigiriki ya Griesbach ilitangazwa 1796-1806. Maandishi-awali yake yaliyosahihishwa yalikuwa ndiyo msingi wa tafsiri ya Kiingereza ya Sharpe katika 1840 na ndiyo maandishi-awali ya Kigiriki yaliyochapwa katika The Emphatic Diaglott, ambayo mara ya kwanza ilitangazwa ikiwa kamili katika 1864. Maandishi-awali mengine mazuri sana yalitokezwa na Konstantin von Tischendorf (1872) na Hermann von Soden (1910), hayo ya baadaye yakawa msingi wa tafsiri ya Kiingereza ya Moffatt ya 1913.
22. (a) Ni maandishi-awali gani ya Kigiriki yamekubaliwa na wengi? (b) Yametumiwa kuwa msingi wa tafsiri zipi za Kiingereza?
22 Maandishi-awali ya Westcott na Hort. Maandishi-awali yaliyosahihishwa ya Kigiriki ambayo yamekubaliwa na wengi ni yale yaliyotokezwa na wasomi wa Chuo Kikuu cha Cambridge B. F. Westcott na F. J. A. Hort, katika 1881. Miswada ya maandishi-awali ya Kigiriki ya Westcott na Hort ilishauriwa na Halmashauri ya Kusahihisha ya Uingereza, ambayo Westcott na Hort walikuwa washiriki wayo, kwa ajili ya sahihisho lao la “Agano Jipya” la 1881. Maandishi-awali hayo yaliyosahihishwa ndiyo yaliyotumiwa hasa katika kutafsiri Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo mpaka Kiingereza katika New World Translation. Maandishi-awali hayo pia ndiyo msingi wa tafsiri zifuatazo katika Kiingereza: The Emphasised Bible, American Standard Version, An American Translation (Smith-Goodspeed), na Revised Standard Version.e Tafsiri hiyo ya mwisho pia ilitumia maandishi-awali ya Nestle.
23. Ni maandishi-awali yapi mengine yaliyotumiwa kwa ajili ya New World Translation?
23 Maandishi-awali ya Kigiriki ya Nestle (chapa ya 18, 1948) yalitumiwa pia na Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya New World kwa kusudi la ulinganishi. Halmashauri hiyo pia ilirejezea ile ya wasomi wa Kiyesuiti Wakatoliki José M. Bover (1943) na Augustinus Merk (1948). Maandishi-awali ya United Bible Societies wa 1975 na maandishi-awali ya Nestle-Aland ya 1979 yalishauriwa ili kufanya vielezi-chini vya Hariri ya Mrejezo ya 1984 viwe vya kisasa.f
24. New World Translation imerejezea pia tafsiri zipi za kale? Baadhi ya vielelezo ni vipi?
24 Tafsiri za Kale Kutoka Kigiriki. Zaidi ya hati hizo za Kigiriki, leo kunapatikana hati nyingi za tafsiri za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika lugha nyinginezo ili kufanyia uchunguzi. Kuna hati (au vipande) zaidi ya 50 za tafsiri za Kilatini cha Kale na maelfu ya hati za Vulgate ya Kilatini ya Jerome. Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya New World ilirejezea hizo, na pia tafsiri ya Coptic, ya Armenia, na ya Syria.g
25. Tafsiri za lugha ya Kiebrania zilizorejezewa katika New World Translation ni zenye upendezi gani wa pekee?
25 Kuanzia angalau karne ya 14 na kuendelea, tafsiri za Maandiko ya Kigiriki mpaka lugha ya Kiebrania zimetokezwa. Hizo zapendeza kwa kuwa hesabu fulani yazo zimerudisha jina la kimungu katika Maandiko ya Kikristo. New World Translation hufanya marejezeo mengi kwenye tafsiri hizo za Kiebrania chini ya mfano “J” ukiwa na namba ndogo juu. Kwa habari ya kirefu, ona dibaji ya New World Translation of the Holy Scriptures—With References, kurasa 9-10, na appendix 1D, “Jina la Kimungu Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.”
TOFAUTI-TOFAUTI ZA MAANDISHI-AWALI NA MAANA ZAZO
26. Tofauti-tofuati za maandishi-awali na familia za hati zilitokeaje?
26 Kati ya zile hati zaidi ya 13,000 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, kuna tofauti-tofauti nyingi za maandishi-awali. Zile hati 5,000 katika lugha ya Kigiriki pekee zaonyesha tofauti nyingi kama hizo. Yaeleweka vizuri kwamba kila nakala iliyofanyizwa kutoka kwa hati za mapema ingekuwa na makosa ya uandishi yayo ya pekee. Wakati yoyote ya hati hizo za zamani ilipopelekwa kwenye eneo fulani ikatumiwe, makosa hayo yangerudiwa katika nakala katika eneo hilo na yangekuwa sehemu ya hati nyingine huko. Ni katika njia hiyo kwamba familia za hati zenye kufanana ziliongezeka. Kwa hiyo, je! maelfu ya makosa hayo ya uandishi hayapasi kutia wasiwasi? Je! hayaonyeshi ukosefu wa uaminifu katika upokezaji wa maandishi-awali? Hata kidogo!
27. Tuna uhakikisho gani juu ya uaminifu wa maandishi-awali ya Kigiriki?
27 F. J. A. Hort, aliyekuwa mtokezaji mwenzi wa maandishi-awali ya Westcott na Hort, aandika hivi: “Sehemu kubwa ya maneno ya Agano Jipya ni sahihi ijapokuwa taratibu zote za uchambuzi wa kuyachungua, kwa sababu hayana utofautiano-tofautiano, na yahitaji kunakiliwa tu. . . . Endapo tofauti ndogo-ndogo . . . zinawekwa kando, maneno ambayo kwa maoni yetu yangali yatilika shaka ni vigumu kukadiriwa yafikie zaidi ya sehemu moja ya elfu ya Agano Jipya.”h
28, 29. (a) Kadirio letu halisi la maandishi-awali ya Kigiriki yaliyochujwa ni nini? (b) Tuna taarifa gani yenye amri juu ya hilo?
28 Kadirio la Upokezaji wa Maandishi-awali. Kwa hiyo, basi, kadirio halisi la uaminifu na uasilia wa maandishi-awali ni nini, baada ya karne hizi nyingi za upokezaji? Si kwamba tu kuna maelfu ya hati za kulinganisha bali pia magunduzi ya hati za Biblia za kale zaidi wakati wa makumi machache ya miaka yaliyopita hurudisha maandishi-awali ya Kigiriki nyuma sana karibu na mwaka 125 W.K., makumi kadhaa ya miaka baada ya kifo cha mtume Yohana karibu 100 W.K. Uthibitisho huo wa hati hutoa uhakikisho wenye nguvu kwamba sasa tuna maandishi-awali ya Kigiriki yenye kutegemeka yaliyochujwa. Angalia kadirio ambalo aliyekuwa mkurugenzi na mtunza-maktaba ya Jumba la Vitu vya Ukumbusho la Uingereza, Sir Frederic Kenyon, huweka kuhusu hilo:
29 “Basi tofauti iliyopo kati ya tarehe za utungaji wa awali na ushuhuda wa mapema zaidi uliopo huwa ndogo sana hivi kwamba kwa kweli huwa si kitu, na msingi wa mwisho wa kuwa na shaka yoyote kwamba Maandiko yametufikia sisi kwa hakika kama yalivyoandikwa sasa umekwisha ondolewa. Uasilia na uaminifu wa ujumla wa vitabu vya Agano Jipya waweza kuonwa kuwa hatimaye umethibitishwa. Hata hivyo, uaminifu wa ujumla ni jambo moja, na uhakika kuhusu habari zote ndogo-ndogo ni jambo jingine.”i
30. Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba New World Translation yawapa wasomaji wayo ‘neno la Yehova’ jaminifu?
30 Kwa habari ya maoni hayo ya mwisho juu ya “uhakika kuhusu habari zote ndogo-ndogo,” nukuu katika fungu 27 la Dakt. Hort lazungumza juu ya hilo. Ni kazi ya wachujaji wa maandishi-awali kurekebisha hilo, nao wamefanya hivyo kwa kiwango kikubwa. Kwa sababu hiyo, maandishi-awali ya Kigiriki yaliyochujwa ya Westcott na Hort hukubaliwa kwa ujumla kuwa yenye ubora wa hali ya juu. Hivyo, sehemu ya Andiko la Kigiriki la Kikristo ya New World Translation, ikiwa imetegemezwa juu ya maandishi-awali hayo ya Kigiriki yaliyo bora sana, yaweza kuwapa wasomaji wayo ‘neno la Yehova’ jaminifu, maana limehifadhiwa kwa uzuri sana kwa ajili yetu katika akiba ya hati za Kigiriki.—1 Pet. 1:24, 25.
31. (a) Magunduzi ya ki-siku-hizi yameonyesha nini juu ya maandishi-awali ya Maandiko ya Kigiriki? (b) Chati kwenye ukurasa 309 yaonyeshaje chanzo kikuu cha sehemu ya Andiko la Kigiriki la Kikristo la New World Translation, na ni vipi baadhi ya vyanzo vya pili vilivyotumiwa?
31 Yenye upendezi zaidi ni maelezo ya Sir Frederic Kenyon katika kitabu chake Our Bible and the Ancient Manuscripts, 1962, kwenye ukurasa 249: “Ni lazima tuwe na uradhi kujua kwamba uasilia wa ujumla wa maandishi-awali ya Agano Jipya umeungwa mkono sana na magunduzi ya ki-siku-hizi ambayo yamepunguza kwa kadiri kubwa tofauti kati ya wasifu za awali na hati zetu za mapema zaidi zilizopo, na kwamba tofuti-tofauti za usomaji, zijapopendeza, hazibadili mafundisho ya msingi ya imani ya Kikristo.” Kama ilivyoonyeshwa katika ukurasa 309 katika chati, “Vyanzo vya Maandishi-awali ya Tafsiri ya New World—Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo,” hati zote zinazohusika zimetumiwa ili kutokeza maandishi-awali ya Kiingereza yaliyotafsiriwa kwa usahihi. Vielezi-chini vyenye thamani vyaunga mkono tafsiri hizo zote za uaminifu. Halmashauri ya Tafsiri ya Biblia ya New World ilitumia matokeo bora zaidi ya usomi wa Biblia yaliyositawishwa kwa muda wa karne nyingi katika kutokeza tafsiri yayo nzuri. Jinsi tunavyoweza kuwa na uhakika leo kwamba Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, tuliyo nayo sasa, kweli kweli yana “kiolezo cha maneno yenye afya” kama yalivyoandikwa na wanafunzi waliopuliziwa na Mungu wa Yesu Krito. Sisi na tuendelee kushikilia maneno hayo yenye thamani katika imani na katika upendo!—2 Tim. 1:13, NW.
32. Ni kwa nini nafasi tele imetumiwa hapa kuzungumza juu ya hati na maandishi-awali ya Maandiko Matakatifu, na tokeo lenye kuridhisha likawa ni nini?
32 Funzo hili pamoja na lile lililotangulia yameshughulikia mazungumzo ya hati na maandishi-awali ya Maandiko Matakatifu. Kwa nini jambo hilo limeshughulikiwa kindani hivyo? Kusudi limekuwa ni kuonyesha bila shaka yoyote kwamba maandishi-awali ya Maandiko ya Kiebrania na ya Kigiriki pia kwa ujumla ni yale yale kama maandishi-awali yenye uasilia, ya awali ambayo Yehova alipulizia wanaume waaminifu wa kale waandike. Maandishi hayo ya awali yalikuwa yamepuliziwa na Mungu. Wanakiliji, wajapokuwa stadi, hawakuwa wamepuliziwa na Mungu. (Zab. 45:1; 2 Pet. 1:20, 21; 3:16) Kwa hiyo, imekuwa lazima kupepeta akiba kubwa ya nakala za hati kwa kusudi la kutambulisha waziwazi na bila kosa lolote maji masafi ya ukweli kama yalivyomiminwa hapo awali kutoka Akiba Kubwa Zaidi, Yehova. Shukrani zote zamwendea Yehova kwa ajili ya zawadi nzuri sana ya Neno lake, Biblia iliyopuliziwa na Mungu, na ujumbe wa Ufalme wenye kuburudisha ambao hutiririka kutoka kurasa zayo!
[Maelezo ya Chini]
a Insight on the Scriptures, Buku 1, kurasa 354-5.
b Ona ukurasa 176, fungu 6.
c Insight on the Scriptures, Buku 1, ukurasa 323; New Bible Dictionary, hariri ya pili, 1986, J. D. Douglas, ukurasa 1187.
d New Bible Dictionary, hariri ya pili, ukurasa 1187.
e Ona chati “Baadhi ya Tafsiri za Biblia Zenye Kuongoza Katika Lugha Saba Kubwa,” katika ukurasa 322.
f The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures, 1985, kurasa 8-9.
g Ona vielezi-chini kwenye Luka 24:40; Yohana 5:4; Matendo 19:23; 27:37; na Ufunuo 3:16.
h The New Testament in the Original Greek, 1974, Buku 1, ukurasa 561.
i The Bible and Archaeology, 1940, kurasa 288-9.