Historia ya Mashahidi wa Yehova Katika Nyakati za Kisasa—
Ujeremani (Inaendelea)
LAKINI si kila mtu aliyekubaliana na namna habari njema zilivyokuwa zikihubiriwa. Hasa kati ya wengine wa ‘wazee’ waliochaguliwa kidemokrasi na makundi walikuwamo wale waliojitahidi zaidi kuizuia kazi badala ya kuiendeleza. Ikawa lazima kuwaonya akina ndugu wasibishane nao. Ilikuwa afadhali kuwaacha wafuate njia yao wenyewe na kutumia wakati ambao ungepotezwa kwa sababu yao katika mabishano yasiyofaa kitu katika huduma ya Ufalme. The Watch Tower lilieleza wazi kwamba kungekuwako kupepetwa, na kwa hiyo Wakristo walikuwa wameonywa kwa upole wajihadhari na wale walioleta migawanyiko na mabishano na kujitenga nao. Hii ilifanya iwe lazima kufanya mabadiliko fulani katika nchi za ujirani wakati wa mwaka wa 1919, nayo haya yaliwahusu akina ndugu na kazi katika Ujeremani. Kwa mfano, wakati wa mwaka huo Ndugu Lauper alianza kufanya kazi kulingana na alivyoona mambo mwenyewe. Kwa hiyo, aliombwa arudishe akiba yake ya vitabu na magazeti ya Watch Tower Society aliyokuwa amesimamia kwa miaka kadha.
Kuelekea mwisho wa mwaka wa 1919 akina ndugu walipashwa habari za ugumu mkubwa hata zaidi. Mapema Ndugu Russell alikuwa ameweka A. Freytag aangalie kazi katika Ufaransa na Ubelgiji miaka kadha iliyopita akiwa katika afisi ya Sosaiti ya Geneva. Mamlaka yake ilitia na kuchapa tafsiri ya Kifaransa ya Watch Tower la Kiingereza na pia Studies in the Scriptures. Walakini, alitumia mamlaka hii vibaya akaanza kuchapa vitabu vyake mwenyewe, kwa njia hiyo akileta mchafuko mwingi kati ya akina ndugu. Freytag aliondolewa katika cheo chake na afisi ya Sosaiti ikafungwa, afisi mpya ikafunguliwa katika Bern ikiongozwa na Ndugu E. Zaugg na usimamizi wote ukiwa chini ya Ndugu Binkele.
Kwa sasa, wenye kumwunga mkono Freytag walikuwa wameanza kufanya mikutano wakiwa wamejitenga na kufanya kazi yao kati ya akina ndugu Ujeremani, ambao wengine wao walipoteza maoni yao yafaayo sababu ya Freytag kulaumu na kusingizia Sosaiti na kuishtaki juu ya kueneza mafundisho ya uongo. Ndugu Binkele aliona ni lazima apinge mashtaka ya uongo ya Freytag na kujibu maulizo mengi yaliyotoka Ujeremani katika barua iliyogawiwa watu yenye kurasa nne katika Septemba wa mwaka wa 1920. Hata hivyo, mbegu za mashaka zilizokuwa zimepandwa na Freytag zilianza kuchipuka, na hesabu fulani ya wasio imara wakamfuata na kuanzisha makundi yao wenyewe. Kikundi hiki kingali kimo Ujeremani hata siku ya leo.
SHAMBA LILILO TAYARI KWA MAVUNO
Lo! Ujeremani ilikuwa imebadilika haraka namna gani katika miaka michache tu! Kabla ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza wachache walikuwa na nia ya kuzisikiliza habari njema za Ufalme. Lakini kaiser (mfalme), ambaye katika mwaka wa 1914 alikuwa ametangaza wakati ujao mtukufu kwa ushindi katika Ujeremani, sasa alikuwa amekimbilia uhamishoni katika Holland. Jeshi la Ujeremani lililotumwa likashinde Ufaransa lilikuwa limerudi makwao likiwa limeaibishwa. Mithali iliyokuwa mshipini mwao “Mungu yu pamoja nasi!” ikawa uongo. Askari waliorudi waliona ubatili wa vita, vita isiyoungwa mkono na Mungu kamwe, kama viongozi wa dini walivyokuwa wamejaribu kuwasihi mara nyingi.
Ndugu wengi ambao wangali hai wanahakikisha kwamba vita hii ya ubatili sana na isiyo na maana ndiyo iliyowafanya wafumbue macho na kuiona kweli. Wengi walikataa kuamini kwamba Mungu alikuwa amehusika katika uharibifu huu wa kipumbavu wa uhai wa kibinadamu; badala yake, waliwalaumu viongozi wa dini waliokuwa wamewaahidia waliopoteza uhai wao katika pigano kwamba wangepata thawabu ya kimbinguni, wakati wa ‘ibada zao za kidini zilizohusu vita.’ Wengine walipopata habari kwamba mume wao, baba yao au mwana wao alikuwa amekufa akitaka ‘kupata heshima vitani,’ walianza kushangaa kama kweli walikuwa mbinguni au pengine katika hell yenye moto kama ilivyohubiriwa na viongozi wa dini. Kwa hawa hotuba “Wafu Wako Wapi?” ilikuwa ya wakati wake. Akina ndugu waliweza kugawa vitabu kupita wakati mwingine wo wote uliotangulia. Dada wawili makolpota wanasemekana waliangusha kwa pamoja wastani ya vitabu 400 vya Studies in the Scriptures kila mwezi. Watumishi waaminifu wa Yehova walikuwa wakitumia vema nafasi zao kama walivyoweza. Baada ya muda mfupi makundi yenye afya yakachipuka mahali pengi.
Alhamisi, Mei 27, 1920, katika Berlin wasemaji saba walihutubia kati ya watu 8,000 na 9,000 wenye njaa ya kweli katika majumba saba katika sehemu mbalimbali za mji juu ya habari “Mwisho U Karibu! Halafu Nini?” Wengi walipendezwa hata watu 1,500 wakaomba watembelewe, na vitabu 2,500, pamoja na vitabu vingine, vikaangushwa.
Sasa ndipo sinema ya Photo-Drama ilipovuma. Mojawapo ya sinema zenye kuvutia zaidi ilionyeshwa katika Gustav-Siegle-Haus katika Stuttgart kwa watu elfu moja. Walipendezwa sana hata ndugu wakawaachia wenye kupendezwa viti. Sinema hiyo ilionyeshwa kwa pekee Jumapili kwa ajili yao kukiwa na pumziko fupi tu la kula chakula cha mchana, ijapokuwa programu yote kwa kawaida ilikuwa ikitolewa jioni nne.
Photo-Drama ilikubaliwa kwa kuthaminiwa sana katika Saxony, ngome ya mawazo ya ujamaa, ambako sasa makundi yalianza kuchipuka kama uyoga baada ya mvua ya utulivu. Kati ya haya lilikuwamo kundi la Waldenburg likiwa na zaidi ya watu mia moja wakikutana pamoja kwa kawaida wajifunze Neno la Mungu katika shamba kubwa, ambalo mwenyewe muda mfupi tu uliopita alikuwa amekuwa mshiriki wa baraza ya wasimamizi.
HATUA ZA MAANA ZINAKARIBIA KUFANYIZA TENGENEZO LA KITHEOKRASI
Ndugu Rutherford, aliyetaka kutembelea Ujeremani mwenyewe wakati huu lakini akashindwa kupata ruhusa ya kuingia, sasa alikaribisha ndugu 26 kutoka Ujeremani waende Basel, Switzerland, Novemba 4 na 5, 1920, wakazungumze njia za kuendesha kazi katika Ujeremani kwa matokeo mema zaidi. Halmashauri iliyokuwa imetumikia katika Ujeremani miaka mingi ilivunjwa. Ndugu Cunow, ambaye mpaka wakati huo alikuwa ameisimamia kazi miaka kadha, aliomba aondolewe katika cheo hiki na kutiwa katika kazi ya uhaji, kwa hiyo ikawa lazima kutafuta mwangalizi mpya. Paul Balzereit alichaguliwa awe mwangalizi wa Ujeremani na Ndugu Binkele akawekwa kama mwangalizi mkuu wa Central European Office.
SHUGHULI YA “MAMILIONI”
Kijitabu Millions Now Living Will Never Die cha Kijeremani, kilitangazwa kitatolewa Februari wa mwaka wa 1921, na shughuli ya kutoa hotuba iliyopaswa kuchukua miaka kadha ikapangwa rasmi Februari 15. Wasemaji bora waligawiwa hotuba na makundi yakawa yanaweza kuandikia Sosaiti ipange kuwe na wasemaji hao mahali ambako hawakupatikana wo wote.
Kwa njia hiyo mlango ulifunguliwa wa kutoa ushuhuda mwingi, ambao kifani chake wengi wa ndugu zetu hawakuwa wamepata kufikiri waweza kuwapo mwaka mmoja mapema. Ripoti ya kila mwaka ya Sosaiti ilisema hivi: “Hakujapata kuonyeshwa kupendezwa kwingi hivyo katika Ujeremani kama sasa. Makundi makubwa yanakuja na, ingawa upinzani unaongezeka, kweli inaenea.”
Ndivyo ilivyokuwa katika Constance. Dada Berta Maurer, ambaye amekuwa akimtumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 50, angali akumbuka namna hotuba ya watu wote “Ulimwengu Unakwisha—Mamilioni Yaliyo Hai Sasa Hayatakufa Kamwe!” ilivyotangazwa katika vipande vikubwa vya karatasi kisha ikatolewa katika jumba kuu zaidi la mji, jumba ambamo John Huss alihukumiwa kuteketezwa kwa moto mtini. Hotuba nyingine za kufuliza zilitolewa, na Mei 15, 1921, watu kumi na watano wakabatizwa—ukawa mwanzo wa kundi katika Constance.
Katika Dresden hotuba hiyo ilishangaza sana. Kundi lilikodi majumba makubwa matatu, lakini nyakati nyingine saa mbili kabla hotuba hazijatolewa, kazi ya kutangaza hotuba kwa kutumia motokaa ilikatazwa kwa sababu kundi kubwa sana lilikuwa limefanya magari yasiweze kupata nafasi ya kupita. Majumba yaliyosongamana na watu yasingeweza kuchukua watu zaidi. Wasemaji walikuwa na ugumu wa kupenya katika makundi ya watu kufika kwenye majumba. Ni baada tu ya kuahidiwa kwamba hotuba ingerudiwa kwa faida ya wenye kungoja kundi lilipokubali kufungua njia.
Ndugu Erich Eickedberg wa Remscheid alikuwa akigawa kijitabu Millions katika Solingen alipoona yafuatayo yenye kupendeza: Alijijulisha kwa mtu aliyekutana naye kwa kusema hivi: “Ninakuletea habari njema kwamba mamilioni walio hai sasa hawatakufa kamwe bali wataishi kwa amani na furaha milele juu ya dunia. Kijitabu hiki chahakikisha hili nacho ni pfennings kumi tu.” Mtu huyo alilikataa toleo lakini kivulana kilichokuwa kimesimama kando yake kikasema: “Baba, kwani usikinunue, kikasha ni pesa nyingi zaidi.”
Masimulizi haya ya Ujeremani yanaendelea katika toleo lifuatalo.—Kutoka 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.