Historia ya Mashahidi wa Yehova katika Nyakati za Kisasa
—Ujeremani (Inaendelea)
KWA sababu ya kutendewa hivyo ndugu zetu walihitaji imani yenye nguvu, imani yenye kutiwa nguvu na funzo la uangalifu la Neno la Mungu. Helmut Knöller aliona vile kukosa kujifunza kunavyoweza kuwa hatari na kumwacha mtu bila kuwa tayari kwa majaribu hayo. Acheni yeye asimulie aliyoyaona mwenyewe:
“Siku zangu za kwanza kukaa Dachau zilikuwa zenye magumu sana. Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 20, mimi ndimi niliyekuwa mchanga zaidi kuliko wafungwa waliofika karibuni. Nilipewa mgawo wa kufanya kazi pamoja na kikundi fulani cha pekee kilichopaswa kufanya kazi hata Jumapili. Mwangalizi wangu alinionea sana. Mimi ndimi niliyefanya kazi zilizo ngumu zaidi, na isitoshe, mimi sikuwa nimezizoea. Nilikuwa nikizimia-zimia nami nilipofanya hivyo kila mara nilikuwa naamshwa kwa kutiwa katika orofa ya chini ambapo maji yalikuwa yakinifika viunoni nayo yalikuwa yakimwagwa kichwani pangu.
“Wakanifanya kuwa hoi. Hii iliendelea kila siku hata nikawa karibu ya kukata tamaa, nikijua kwamba ingeendelea hivyo kwa juma nyingi hata miezi. . . . Lakini magumu yakawa makubwa sana hata mwishowe nikawaendea viongozi wa kambi nikatia sahihi tangazo lenye kuonyesha kwamba sikuwa na uhusiano tena na Wanafunzi wa Biblia wa Mataifa Yote. Kutia kwangu sahihi kulisababishwa hasa na kutojifunza kwangu vya kutosha nilipokuwa nyumbani. Wazazi wangu wenyewe hawakuwa wakijifunza sana na sisi watoto tulifundishwa nao juujuu tu. . . . Walikuwa wameniambia kwamba tungeweza kutia sahihi tangazo kama hilo kwa maana kwanza hakuna lililosemwa juu ya mashahidi wa Yehova ndani yake, bali Wanafunzi wa Biblia tu ndio waliotajwa, na, pili, haikuwa vibaya kudanganya adui ikiwa hiyo ingefanya tufunguliwe ili tuweze kumtumikia Yehova vizuri zaidi huko nje.” Baadaye alipokuwa katika Sachsenhausen ndipo ndugu waliokomaa walipomsaidia afahamu maana ya ukamilifu wa Kikristo na kumjenga imani yake.
Jambo jingine lililojaribu akina dada linatajwa na Auguste Schneider wa Bad Kreuznach:
“Siku moja mfungwa mmoja alinijia akaniambia: ‘Bi. Schneider, mimi nitaondoka hapa!’ (Alikuwa mwanamke.) Nikamwuliza atakwenda wapi naye kanijibu hivi: ‘Wanaume wamekuwa wengi sana hapa hata wafungwa wanatayarishiwa mahali pa kufanyia umalaya. Sisi tumeulizwa, na karibu wanawake 20 au 30 hivi wamejitolea. Tutapewa mavazi mazuri na kurembeshwa!’ Nikamwuliza jambo hilo litafanyiwa wapi, naye akajibu, ‘Katika kambi ya wanaume.’
“Ni vigumu kueleza yaliyotendeka huko. Lakini siku moja kiongozi wa askari wa SS aliniambia hivi: ‘Bi. Schneider, pengine umesikia yanayotendeka katika kambi ya wanaume. Nilitaka tu kukuambia kwamba hakuna hata mmoja wa ‘mashahidi wa Yehova ameshiriki!’”
Ravensbrück ikajulikana pote kuwa ndiyo kambi mbaya zaidi kuliko kambi zote za mateso za wanawake.
MIGAWANYIKO YAONGEZA MAGUMU
Kwa sababu ya kuwa mbali na akina ndugu walio nje, wale waliokuwa kambini waliona hamu nyingi ya chakula cha kiroho. Waliofika karibuni walihojiwa na akina ndugu wajue mambo yaliyochapwa katika Mnara wa Mlinzi. Nyakati nyingine walipashwa habari za kweli, mara nyingine hazikuwa za kweli. Walikuwako pia ndugu waliojaribu kutumia Biblia kuonyesha tarehe ambapo wangefunguliwa, na ingawa sababu zenyewe zilikuwa dhaifu, wengine walishikilia tumaini hilo la bure.
Wakati huo ndugu aliyekuwa na kumbukumbu zuri sana alifungwa Buchenwald. Mara ya kwanza uwezo wake wa kukumbuka na kushiriki mambo aliyokuwa amejifunza pamoja na wengine ulitia akina ndugu moyo. Lakini baada ya muda fulani akawa sanamu ya kuabudiwa, “bingwa wa Buchenwald,” nayo maneno yake, hata maoni yake ya kipekee, yalionwa kuwa ndiyo yenye uamuzi wa mwisho. Kutoka Desemba wa 1937 mpaka 1940 alitoa hotuba kila jioni, akatoa jumla ya karibu hotuba elfu moja, na nyingi kati yazo ziliandikwa kwa mwandiko wa shorthand ili ziweze kutolewa nakala nyingi kwa mimiografu. Ingawa walikuwako ndugu wengi wazee kambini waliokuwa na uwezo wa kutoa hotuba, ndugu huyu ndiye aliyefanya hivyo peke yake. Wo wote wasiokubaliana naye kabisa walitajwa kuwa “adui za Ufalme” na “jamaa ya Akani,” nao walipaswa waepukwe na “waaminifu.” Karibu ndugu 400 walifuata mpango huu kwa kutotaka sana.
Waliobandikwa jina hilo la “adui” walikuwa pia ndugu waliokuwa wamekuwa na nia ya kuhatirisha maisha zao waendeleze faida za Ufalme kama walivyoweza. Wao pia walikuwa wamefungwa kambini kwa sababu ya kujitahidi kwao kuhakikisha ukamilifu wao, hata mpaka kufa. Ni kweli kwamba wengine wao hawakuwa wakitumia kabisa kanuni za Biblia. Lakini walipojaribu kuonana na waliokuwa na madaraka ili nao pia waweze kufaidika na chakula cha kiroho kilichopatikana katika Buchenwald, wenye madaraka hawa waliona kwamba kuzungumza nao kungekuwa kujishushia cheo.
Wilhelm Bathen wa Dinslaken, ambaye hata sasa anamtumikia Yehova, anasimulia namna yeye mwenyewe alivyohusika na jambo hili: “Nilipojua hata mimi nilikuwa nimetengwa na ushirika nilitikisika kiroho nikahuzunika sana hata nikajiuliza ingewezekanaje. . . . Mara nyingi nilipiga magoti nikasali kwa Yehova kwamba anipe ishara kama kweli nimetengwa na ushirika. Nikajiuliza kama mimi ndimi nilikuwa wa kulaumiwa kwa sababu ya hali hiyo na kama yeye pia alikuwa amenitenga na ushirika. Nilikuwa na Biblia nami nilikuwa nikiisoma katika mwangaza mdogo hata nilifarijika sana nilipowaza kwamba jambo hili lilikuwa limenipata kunijaribu, ama sivyo ningekuwa nimekwisha haribiwa, kwa maana kutengwa na ndugu hivyo kulileta maumivu makali sana.”
Hivyo kwa sababu ya kutokamilika kwa kibinadamu na kwa sababu ya watu kujifikiria kuwa wa maana sana migawanyiko ilitokea kati ya watu wa Mungu, na kutokeza majaribu makali sana kwa wengine.
UGUMU WA NJAA
Baada ya vita ya ulimwengu ya pili kuanza chakula kilichopatikana kilipelekwa kwa majeshi. Vyakula katika kambi za mateso vilikuwa vya namna ya muhogo ambao kwa kawaida ulitumiwa kulisha wanyama. Vilipikwa kwa ukosefu wa upendo hata wafungwa wakasikika-sikika wakisema kwamba hata nguruwe wangalikataa kula vyakula hivyo. Lakini jambo la maana halikuwa kupata chakula chenye kuamsha hamu ya kula, la maana lilikuwa kuokoka. Wengi walikufa njaa. “Jaribu langu kubwa zaidi lilikuwa njaa,” aandika Ndugu Kurt Hedel, na kueleza kwa kusema hivi: “Urefu wangu ni karibu futi 6 na inchi 2 na kwa kawaida ratili zangu ni 230. Lakini katika masika ya miaka ya 1939 na 1940 ratili zangu zilikuwa 90 tu, pengine hata chini ya hapo. Nilikuwa gofu la mtu. Ingawa nilikuwa mkubwa nilipewa chakula kilicholingana. na walichopewa waliokuwa wadogo kuliko mimi. Nikawa nafinya tumbo kwa ngumi zangu nizuie maumivu hata ndugu mmoja aliyekomaa akanishauri nisali kwa Yehova juu ya ugumu wangu na kumwomba anisaidie nivumilie maumivu hayo. Karibuni nikajua namna sala inavyosaidia katika hali kama hiyo.” Ndugu mwingine akumbuka kwamba alikuwa akitia mchanga kinywani mwake aweze kupambana na maumivu ya njaa.
Ushirika wa kidugu ulikuwa wenye kufariji sana katika hali kama hizo. Lilikuwa jambo la kuvutia sana kuona akina ndugu ambao walikuwa karibu ya kufa wakiwapa wale waliokuwa na shida zaidi yao vipande vidogo vya mkate. Mara nyingi yalikuwa ni makombo waliyoficha chini ya mito ya wale ambao hawakupewa chakula na waliokuwa wamelazimishwa kusimama nje uani wakiwa uchi katika baridi kali sana. Lilikuwa jambo la kuburudisha namna gani kwa wale waliokaribia kuvunjwa na adui kusikia maneno ya kutia moyo ya ndugu aliyekomaa yakitoka kinywani mwake kama mafuta yenye kutiririka kuingia katika kidonda na kuwatia nguvu mpya wakiwa katika hali iliyoelekea kutovumilika! Nayo sala ya umoja ilisaidia kweli kweli! Wakati majumba ya majeshi yalipofungwa jioni kukawa kimya kabisa katika vyumba vya kulala, mara kwa mara sala za umoja zilitolewa kwa Yehova zikionyesha magumu yaliyokuwako. Magumu haya yaliwahusu wao wote au ndugu mmoja mmoja. Wakati wo wote Yehova alipobadili mambo yakawa mazuri, walikuwa wakitoa sala ya umoja ya kumshukuru kesho yake. Baada ya kutoka katika hali ambayo mtu asingaliweza kutoka kwa nguvu zake mwenyewe, akina ndugu walifahamu tena kwamba ‘hatuko peke yetu wakati wo wote.’
YALIYOWAPATA WALE WALIOKUBALI KUFANYA WALIVYOAGIZWA
Inafaa kuangaliwa kwamba askari wa SS waliotumia njia mbaya zaidi kufanya mtu atie sahihi katika tangazo, waliwageukia waliotia na kuwataabisha zaidi ya walivyokuwa wamewafanyia kabla hawajatia sahihi. Karl Kirscht anahakikisha jambo hili: “Mashahidi wa Yehova ndio waliofanyiwa hila kupita watu wengine katika kambi za mateso. Ilidhaniwa kwamba kwa kuwafanyia hivyo wangeweza kuwafanya watie sahihi katika tangazo. Tuliombwa-ombwa tufanye hivyo. Wengine walitia sahihi, lakini mara nyingi walikuwa wakingoja karibu mwaka mmoja kabla hawajafunguliwa. Wakati huo walikuwa wakitukanwa-tukanwa hadharani na askari wa SS kuwa ni wanafiki na waoga na kulazimishwa kufanya ‘matembezi ya heshima’ wakizunguka ndugu zao kabla hawajaruhusiwa kuondoka kambini.”
Wilhelm Roger anakumbuka kwamba ndugu mmoja alitia sahihi katika tangazo wakati mke wake na binti yake walipokuja kumtembelea, lakini hakuambia akina ndugu amefanya hivyo. “Juma kadha baadaye aliambiwa ajitayarishe kufunguliwa. (Watu kama hao kwa ujumla walipaswa kusimama langoni mpaka waitwe majina.) Ndugu huyu alisimama langoni mchana kutwa na hata jioni hiyo akawa amesimama hapo bado, kwa hiyo ikamlazimu kuwarudia akina ndugu katika majumba ya askari. Majina yalipokwisha kuitwa na mkuu aliyeitwa Knittler aliyeogopwa sana, ndugu huyu alitumwa akalete kiti cha miguu mitatu katika majumba ya askari halafu akalazimishwa kusimama juu yake uani akiwa mbele ya ndugu walioingia kijeshi. Ndipo Knittler akaelekeza fikira juu ya ndugu huyo na kutuambia hivi akitutazama kwa ukali: ‘Mtazameni mwoga wenu; ametia sahihi bila kumwambia ye yote kati yenu!’ Kwa kweli askari wa SS wangalipenda sote tutie sahihi. Lakini mtu fulani alipotia sahihi waliacha kutupa sisi heshima waliyotupa kwa siri.”
Dada Dietrichkeit akumbuka dada wawili waliotia sahihi katika tangazo. Waliporudi wakamwambia Dada Dietrichkeit wametia sahihi kwa sababu waliogopa kufa njaa. Hawakuficha kwamba waliulizwa hivi na askari wa SS: “Kwa kuwa sasa mmemkana Mungu wenu Yehova, mtatumikia Mungu yupi?” Dada hao wawili wakafunguliwa upesi, lakini Warusi walipoishambulia nchi wote wawili walikamatwa tena kwa sababu fulani wakapelekwa gerezani na Warusi na kufa wakiwa huko kwa sababu ya njaa. Katika kisa kingine dada aliyetia sahihi alinajisiwa na Warusi katika siku za mwisho za vita kisha wakamwua.
Hesabu kubwa ya ndugu waliotia sahihi katika tangazo waliandikwa jeshini wakapelekwa kwenye vikosi vya mbele ambako wengi wao walipotezea maisha zao.
Ingawa kuna uhakikisho wa kutosha kwamba ndugu hao waliotia sahihi walijitoa chini ya ulinzi wa Yehova kwa kufanya hivyo, wengi hawakuwa “wasaliti.” Wengi waliagiza sahihi zao zifutwe kabla hawajafunguliwa, baada ya ‘ndugu waliokomaa kuwasaidia waone walilokuwa wamefanya. Walipotubu wakamwomba Yehova awape nafasi nyingine ya kuhakikisha uaminifu wao, wengi wao wakawa wahubiri wa kundi na baadaye wakawa mapainia, waangalizi, hata waangalizi wenye kusafiri, wakiendeleza faida za ufalme wa Yehova kwa kuweka mfano mwema, baada ya serikali ya Hitler kuanguka. Wengi walifarijiwa na yaliyompata Petro, ambaye alimkana Bwana wake, lakini akarudishwa katika upendeleo wake.—Mt. 26:69-75; Yohana 21:15-19.
USALITI
Ijapokuwa wengine walipoteza hali yao ya kiroho kwa muda kwa sababu ya hila zilizotumiwa au kwa sababu ya udhaifu wa kibinadamu, wengine walipata kuwa wasaliti wakaletea ndugu zao taabu nyingi.
Julius Riffel asema kwamba katikati ya mwaka wa 1937 na 1938 “Ndugu Hans Miiller wa Dresden alikuja katika Betheli ya Bern akajaribu kuonana na ndugu wa Ujeremani, akidai kusudi lake lilikuwa ‘kuanza upya kazi ya siri katika Ujeremani baada ya ndugu wengi sana kukamatwa.’
“Upesi mimi nikasema nina nia ya kushirikiana naye, na ndugu kadha pia wakafanya hivyo. Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba, hatukujua wakati huo kwamba huyu ‘Ndugu’ Müller alikuwa akishirikiana na Gestapo (polisi) katika Ujeremani. Bila kujua hivyo tukafanya mipango katika Bern tukaanza kazi yetu. Mimi nilipaswa nichukue kazi aliyokuwa akifanya Baden Württemberg. Katika Februari 1938 nilivuka mpaka nikaingia Ujeremani nikajaribu kutengeneza utendaji kwa kuonana na ndugu waliokuwa wangali huru. Juma mbili baadaye nikakamatwa. . . . Gestapo walijua habari zote juu ya utendaji wote kwa kuambiwa na yule ndugu wa uongo aliyesaidia kuanza upya kazi ya siri. ‘Ndugu’ huyo alifanya jambo lilo hilo katika Netherlands na Czechoslovakia vile vile.”
MAMBO YAZIDI KUSONGA
Ingawa adui walizidi kuweka mapengo kati ya watu wa Mungu na kuua wengi kati ya wale waliokuwa huru, sikuzote walikuwako wenye kuona uhitaji wa kuwapa ndugu chakula cha kiroho. Walihatirisha maisha zao kwa kufanya hivi. Ndugu Ludwig Cyranek alianzisha upya ugawaji wa Mnara wa Mlinzi kati ya akina ndugu wakati Müller alipokuwa akiendesha kazi yake mbaya katika Dresden. Alifanya hivyo mpaka alipofungwa na kuhukumiwa kifungo cha miaka miwili. Halafu mara tu alipotoka kifungoni akaanza kufanya kazi tena.
Dada wengi walichukua kwa furaha nafasi zilizoachwa wazi na ndugu waliokamatwa, ingawa walijua kwamba wangeweza kupoteza maisha zao wakikamatwa, kulingana na sheria kali zaidi za wakati wa vita. Kwa mfano, kati ya wale waliotumiwa kugawa Mnara wa Mlinzi alikuwako Dada Neuffert katika Holzgerlingen, Dada Pfisterer katika Stuttgart na Dada Franke katika Mainz. Ndugu Cyranek aliandikia dada hawa barua zenye habari zisizoweza kuleta madhara, nao akina dada wakazipiga pasi ili waweze kusoma habari ya siri aliyokuwa ameandika chini yake kwa maji ya malimau, akiwaambia watakakopeleka Mnara wa Mlinzi na hesabu watakayopeleka.
WAAMINIFU MPAKA KUFA
Mauaji mengi yaliyofanywa wakati wa Utawala wa Hitler yanakumbukwa sana katika mateso yaliyotokea. Ndugu na dada wasiopungua 203 walikatwa vichwa au wakapigwa risasi, kulingana na ripoti zisizokamilika. Hesabu hiyo haitii ndani wale waliokufa njaa, wakauawa na magonjwa au kwa sababu ya kutendwa vibaya.
Kwa habari ya ndugu aliyehukumiwa kufa, Ndugu Bär anasema hivi: “Wafungwa wote na wakuu wa gereza pia walishangazwa naye. Alikuwa mtengeneza kufuli naye alifanya kazi ya kutengeneza vilivyoharibika katika gereza zima. Alifanya kazi yake ya kila siku bila kuonyesha dalili ya masikitiko wala huzuni; badala yake, aliimba nyimbo za kumsifu Yehova alipokuwa akiendelea na kazi yake nyingi.” Siku moja karibu saa sita ya mchana alitolewa dukani, akauawa jioni hiyo.
—Kutoka 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses.